20 Jun 2017

Katika Tanzania yetu ya zama hizi ambapo takriban kila jambo linaanglaiwa kwa jicho la kisiasa, ni vigumu sio tu kusimamia ukweli bali pia kukwepa lawama kutoka kwa pande mbili kuu za siasa zetu: CCM au Upinzani.

Sie tusio na vyama, tukikosoa masuala yanayoigusa CCM/serikali, akina Humphrey Polepole wanakurupuka na kutuita majina ya ajabu ajabu. Tukikosoa Upinzani, tunaambiwa "nafasi za Ukuu wa Wilaya zimeshajaa." Good news is, kuna watu - hata kama ni wachache - waliopo CCM, Upinzani na wasio na vyama ambao wanatusikiliza. Na wanatusikiliza kwa vile wanafahamu hatuelemei upande wowote isipokuwa kwenye ukweli.

Baada ya angalizo hilo, tugeukia big news iliyosikika jana, ghafla, na kutukuta wengi wetu tusiamini macho/masikio yetu. Baada ya miaka nenda miaka rudi, hatimaye mfanyabiashara James Rugemalira na mwenzie Singasinga Harbinder Seth Singh walipandishwa kizimbani kwa tuhuma za kuhujumu uchumi.



Kwa tunaofahamu Rugemalira ameisumbua Tanzania yetu kiasi gani, na sambamba na 'usumbufu' wa huyu Singasinga, hatua hiyo tu ya kuwapindisha wawili hao kizimbani inastahili pongezi za kila Mtanzania. Na anayestahili pongezi hizo kwa wingi kabisa ni Rais John Magufuli.
Sawa, kuna watakaosema kuwa "lakini hiyo si ndio kazi ya Rais?" only if tukipuuzia ukweli kwamba Rugemalira alikuwa kama ameshindikana katika Awamu angalau mbili zilizopita, ya Mkapa na Kikwete, na ilikuwa kama huyu mtu kaachwa afanye apendacho katika kuihujumu nchi yetu.
Nimesoma angalizo la mwanasiasa wa Chadema na mwanasheria nguli, Tundu Lissu, akitahadharisha kuhusu Rugemalira na Singasinga, kwamba hao ni sehemu tu ya mtandao mkubwa wa ufisadi. Hata hivyo, japo angalizo hilo ni muhimu, haliondoi ukweli kwamba angalau JPM amethubutu, sio tu kuwapandisha Rugemalira na Singasinga kizimbani bali pia kuwalaza rumande.

Ni wazi kuwa vita hii ambayo Rais Magufuli ameivalia njuga sio rahisi. Sio tu kwa vile inahusisha watu wenye uwezo mkubwa kifedha bali pia kwa sababu pia inawagusa baadhi ya wanasiasa maarufu ndani ya chama chake cha CCM. 
Licha ya angalizo la Lissu, kuna baadhi ya wananchi wanaotoa tahadhari 'kushangilia mapema kabla ya dakika 90.' Hawa pia wana hoja ya msingi hasa kwa kuzingatia mfano kama wa kesi ya Balozi Mahalu. Hata hivyo, kuna haja ya kuwa na matumaini hasa ikizingatiwa kuwa JPM hafanyi anayofanya kwa shinikizo la mtu yeyote yule. Ni utashi wake tu. Angetaka kukaa kimya, kusingekuwa na maandamano ya kumshinikiza achukue hatua.

Kama ningekuwa na fursa ya kumshauri Rais Magufuli basi ningemwomba sana awekeze nguvu zaidi katika vita hii dhidi ya ufisadi ambayo kwa hakika inawaunganisha Watanzania wengi waliochoka kuona nchi yao ikigeuzwa shamba la bibi, badala ya 'uhasama na wanasiasa wa Upinzani.'

Kwa mfano, jana, kabla ya habari hiyo ya Rugemalira na Singasinga kufikishwa mahakamani na baadaye kutupwa rumande, zilizpatikana taarifa kuhusu serikali kupitia jeshi la polisi 'kuwabughudhi' wanasiasa kadhaa wa Chadema ikiwa ni pamoja na kuzuwia ziara ya Waziri Mkuu wa zamani na kiognozi wa ngazi za juu Chadema, Frederick Sumaye.
Katika kipindi hiki cha vita ngumu dhidi ya mafisadi na ufisadi, tunapaswa kuwa kitu kimoja. Si kwamba vyama vya upinzani viungane na CCM, bali angalau tofauti zisizo na msingi ziepukwe, na kubwa zaidi ni kupeuka uadui wa kisiasa.

Nihitimishe kwa pointi moja muhimu kwamba japo tuna historia isiyopendeza kuhusu mapambano dhidi ya ufisadi, na japo ni kweli kuwa wanasheria wa serikali hawana rekodi nzuri kwenye kesi kubwa za serikali, na vilevile japo ni kweli kuwa mara nyingi ukada umekuwa kikwazo kwa serikali kuchukua hatua stahili dhidi ya mafisadi, wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni kumuunga mkono Rais Magufuli kwani angalau ameonyesha dhamira ya kuchukua hatua stahili. 

Vilevile ni muhimu kutambua kuwa vita hii sio dhidi ya watu tu bali ni dhidi ya mfumo uliojengeka muda mrefu. Kwa maana hiyo, japo tunatamani kuona watuhumiwa wote wakikamatwa na kupandishwa kizimbani, ni muhimu tuwe na subira, hasa ikizingatiwa kuwa kukurupusha mambo kunaweza kutupelekea kupoteza kesi dhidi ya 'maadui' wetu ambao kwa uweo wao mkubwa wa kifedha, wataajiri wanasheria bora kabisa kuwatetea.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

1 comment:

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.