Showing posts with label Ufisadi Tanzania. Show all posts
Showing posts with label Ufisadi Tanzania. Show all posts

20 Jun 2017

Katika Tanzania yetu ya zama hizi ambapo takriban kila jambo linaanglaiwa kwa jicho la kisiasa, ni vigumu sio tu kusimamia ukweli bali pia kukwepa lawama kutoka kwa pande mbili kuu za siasa zetu: CCM au Upinzani.

Sie tusio na vyama, tukikosoa masuala yanayoigusa CCM/serikali, akina Humphrey Polepole wanakurupuka na kutuita majina ya ajabu ajabu. Tukikosoa Upinzani, tunaambiwa "nafasi za Ukuu wa Wilaya zimeshajaa." Good news is, kuna watu - hata kama ni wachache - waliopo CCM, Upinzani na wasio na vyama ambao wanatusikiliza. Na wanatusikiliza kwa vile wanafahamu hatuelemei upande wowote isipokuwa kwenye ukweli.

Baada ya angalizo hilo, tugeukia big news iliyosikika jana, ghafla, na kutukuta wengi wetu tusiamini macho/masikio yetu. Baada ya miaka nenda miaka rudi, hatimaye mfanyabiashara James Rugemalira na mwenzie Singasinga Harbinder Seth Singh walipandishwa kizimbani kwa tuhuma za kuhujumu uchumi.



Kwa tunaofahamu Rugemalira ameisumbua Tanzania yetu kiasi gani, na sambamba na 'usumbufu' wa huyu Singasinga, hatua hiyo tu ya kuwapindisha wawili hao kizimbani inastahili pongezi za kila Mtanzania. Na anayestahili pongezi hizo kwa wingi kabisa ni Rais John Magufuli.
Sawa, kuna watakaosema kuwa "lakini hiyo si ndio kazi ya Rais?" only if tukipuuzia ukweli kwamba Rugemalira alikuwa kama ameshindikana katika Awamu angalau mbili zilizopita, ya Mkapa na Kikwete, na ilikuwa kama huyu mtu kaachwa afanye apendacho katika kuihujumu nchi yetu.
Nimesoma angalizo la mwanasiasa wa Chadema na mwanasheria nguli, Tundu Lissu, akitahadharisha kuhusu Rugemalira na Singasinga, kwamba hao ni sehemu tu ya mtandao mkubwa wa ufisadi. Hata hivyo, japo angalizo hilo ni muhimu, haliondoi ukweli kwamba angalau JPM amethubutu, sio tu kuwapandisha Rugemalira na Singasinga kizimbani bali pia kuwalaza rumande.

Ni wazi kuwa vita hii ambayo Rais Magufuli ameivalia njuga sio rahisi. Sio tu kwa vile inahusisha watu wenye uwezo mkubwa kifedha bali pia kwa sababu pia inawagusa baadhi ya wanasiasa maarufu ndani ya chama chake cha CCM. 
Licha ya angalizo la Lissu, kuna baadhi ya wananchi wanaotoa tahadhari 'kushangilia mapema kabla ya dakika 90.' Hawa pia wana hoja ya msingi hasa kwa kuzingatia mfano kama wa kesi ya Balozi Mahalu. Hata hivyo, kuna haja ya kuwa na matumaini hasa ikizingatiwa kuwa JPM hafanyi anayofanya kwa shinikizo la mtu yeyote yule. Ni utashi wake tu. Angetaka kukaa kimya, kusingekuwa na maandamano ya kumshinikiza achukue hatua.

Kama ningekuwa na fursa ya kumshauri Rais Magufuli basi ningemwomba sana awekeze nguvu zaidi katika vita hii dhidi ya ufisadi ambayo kwa hakika inawaunganisha Watanzania wengi waliochoka kuona nchi yao ikigeuzwa shamba la bibi, badala ya 'uhasama na wanasiasa wa Upinzani.'

Kwa mfano, jana, kabla ya habari hiyo ya Rugemalira na Singasinga kufikishwa mahakamani na baadaye kutupwa rumande, zilizpatikana taarifa kuhusu serikali kupitia jeshi la polisi 'kuwabughudhi' wanasiasa kadhaa wa Chadema ikiwa ni pamoja na kuzuwia ziara ya Waziri Mkuu wa zamani na kiognozi wa ngazi za juu Chadema, Frederick Sumaye.
Katika kipindi hiki cha vita ngumu dhidi ya mafisadi na ufisadi, tunapaswa kuwa kitu kimoja. Si kwamba vyama vya upinzani viungane na CCM, bali angalau tofauti zisizo na msingi ziepukwe, na kubwa zaidi ni kupeuka uadui wa kisiasa.

Nihitimishe kwa pointi moja muhimu kwamba japo tuna historia isiyopendeza kuhusu mapambano dhidi ya ufisadi, na japo ni kweli kuwa wanasheria wa serikali hawana rekodi nzuri kwenye kesi kubwa za serikali, na vilevile japo ni kweli kuwa mara nyingi ukada umekuwa kikwazo kwa serikali kuchukua hatua stahili dhidi ya mafisadi, wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni kumuunga mkono Rais Magufuli kwani angalau ameonyesha dhamira ya kuchukua hatua stahili. 

Vilevile ni muhimu kutambua kuwa vita hii sio dhidi ya watu tu bali ni dhidi ya mfumo uliojengeka muda mrefu. Kwa maana hiyo, japo tunatamani kuona watuhumiwa wote wakikamatwa na kupandishwa kizimbani, ni muhimu tuwe na subira, hasa ikizingatiwa kuwa kukurupusha mambo kunaweza kutupelekea kupoteza kesi dhidi ya 'maadui' wetu ambao kwa uweo wao mkubwa wa kifedha, wataajiri wanasheria bora kabisa kuwatetea.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

26 May 2017



Juzi tumesikia ripoti kuhusu mchanga wenye madini unaosafirishwa nje ya Tanzania yetu (well, kuna jina la kitaalamu lakini sio la muhimu kulinganisha na athari kubwa za usafirishwaji wa mchanga huo).

Kwa baadhi ya wenzetu, taarifa hiyo imewashtua mno, na kuwapandisha hasira kubwa. Ndio Tanzania yetu hiyo, wengi wa raia wake hawana habari kuhusu yanayoisibu nchi yetu. Ukiwauliza watu, "hivi mustakabali wa Tanzania mwakani utakuwaje?" nina hakika watu kadhaa watajiumauma kutoa jibu la kueleweka.

Watanzania wengi aidha hawaelewi au wamesahau nchi yetu ilivyochukua mwelekeo mpya - na usiopendeza - baada ya kung'atuka kwa Baba wa Taifa, marehemu Mwalimu Julius Nyerere. Hatua ya kwanza kabisa ya kubadili mwelekeo ilikuwa kitu kinachofahamika kama Azimio la Zanzibar. Hili lilifanyika katika utawala wa Mzee Ruksa, Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi.

Kimsingi, Azimio la Zanzibar liliua Azimio la Arusha na kulizika mubashara. Ukitafuta nyaraka kuhusu Azimio hilo la Zanzibar hutozipata kirahisi kwa sababu lilifanyika katika mkusanyiko uliokuwa kama "mkutano haramu."

Mzee wetu Mwinyi hakuitwa Mzee Ruksa kama utani. Utawala wake ulitawaliwa na kile Waingereza wanaita 'laissez faire', labda kwa Kiswahili chepesi tuseme 'bora liende' au 'liwalo na liwe.' 

Lakini kumtendea haki 'Mzee Ruksa,' asili hasa ya ufisadi haikuanza katika utawala wake bali ilianza katika utawala uliomtangulia, wa Baba wa Taifa. 

Tofauti kati ya tawala hizo mbili ilikuwa bayana: Wakati baadhi ya waliomzunguka Baba wa Taifa walikuwa 'mafisadi wa chinichini' au 'waliokuwa wakisubiri atokea madarakani ili waanze kutafuna keki ya taifa,' katika utawala wa Rais Mwinyi, ilikuwa ni mwanzo wa 'kula kadri unavyoweza,' Waingereza wanaita 'open season.'

Kwamba labda Baba wa Taifa alifahamu watu hao au walikuwa mahiri kuficha tabia zao, sina jibu la hakika. Lakini huhitaji kuwa mchambuzi mahiri wa siasa kubaini kwamba mara baada ya Nyerere kung'atuka na hatimaye kufariki, ghafla watu walewale waliokuwa wakiimba kuhusu Ujamaa na kulaani Ubepari wakageuka matajiri wa kupindukia, mabepari. Ninachofahamu ni kwamba kulikuwa na idadi kubwa tu ya wanasiasa waliomhadaa Baba wa Taifa kuwa ni waumini wa Ujamaa lakini walimudu kuhifadhi fedha huku nje wakisubiri 'Nyerere aondoke.' 

Kwahiyo, Awamu ya Pili ya Mzee Ruksa ni kama iliyotoa ruksa kwa walafi waliokuwa wakimendea keki ya taifa, lakini walishindwa kuitafuna wakati wa utawala wa Nyerere. Kwa kifupi, utawala wa Mzee Ruksa ulitoa rasmi ruksa kulifisadi taifa letu, hasa kupitia Azimio la Zanzibar. 

Ni muhimu kukumbuka Utawala wa Mzee Ruksa ulikuwa wa Chama Cha Mapenduzi, CCM.

Kuingia kwa Rais Benjamin Mkapa mwaka 1995 kuliingiza zama mpya kuhusiana na ufisadi. Miaka 10 ya Mzee wa Uwazi na Ukweli ilitawaliwa na Watanzania kuhadaiwa kuwa ufumbuzi wa matatizo yao upo mikononi mwa wawekezaji, ilhali wengi wa hao walioitwa wawekezaji walikuwa in fact majambazi waliokuwa wakiwinda raslimali zetu. 

Miaka 10 ya Mkapa ilileta matumaini ya kitakwimu, tukiambiwa kuwa sijui GDP, sijui Pato la Taifa, sijui vipimo gnai vya kiuchumi, kuwa vyote vilionyesha uchumi wa Tanzania ukifanya vizuri. Kama kuna kitu kinanichukiza mno kuhusu hizi takwimu za uchumi ni kuwaangalia watu kama bidhaa au namba na sio binadamu. Haiingii akilini kusema uchumi unakua ilhali watu wanazidi kuwa masikini. Uchumi unakua kimazingaombwe?

Tofauti kati ya utawala wa Mwinyi na Mkapa ni ya wazi: nimeshaeleza kuwa katika zama za Mwinyi ilikuwa 'ruksa' kufanya lolote lile. Zama za Mkapa zilituaminisha kuwa kila kitu kinafanyika kwa uwazi na ukweli, na kwenye uwazi na ukweli hakupaswi kuwa na ufisadi. 

Yaliyojiri katika utawala wa Mwinyi yalikuwa yakionekana mubashara. Hiki kilikuwa kipindi cha mtu tu kuamua kuwa tajiri kwa njia halali au zisizo halali, maana ilikuwa ruksa. Lakini katika zama za 'uwazi na ukweli,' watu pekee walioonekana kuwa na ruksa ya kufanya wapendayo ni wawekezaji.Mkapa aliwathamini wawekezaji kuliko Watanzania wenzake.

Lakini ni baada ya Mkapa kutoka madarakani ndio tukafahamu kilichokuwa kikijiri 'behind the scene.' Kumbe wakati anatuhubiria kuhusu uwazi na ukweli, yeye akaigeuza Ikulu kuwa soko la Kariakoo, akawa anafanya biashara. 

Na Mkapa, mwanafunzi mtiifu wa Mwalimu Nyerere, ni mfano sahihi wa watu ambao Nyerere aliwaamini sana lakini alipoondoka nao wakapuuza misingi aliyoijenga Mwalimu. 

Zama za Mkapa ndio haswa zilizowavutia wawekezaji kujazana nchini mwetu. Wengi wao walikuja na brifukesi tupu, wakaondoka na mamilioni ya dola. Baadhi ya wawekezaji hao, walipoona bado wanahitaji kuchuma wasichopanda, walibadili majina na kuongezewa likizo ya kulipa kodi.

Ni muhimu kukumbuka kuwa Mkapa alikuwa Rais kwa tiketi ya CCM.

Baada ya Mkapa akaingia Kikwete. Ili kuorodhesha madudu yote yaliyofanywa katika utawala wa Kikwete inahitaji kitabu kizima. Wakati mwingine unaweza kupatwa na kizunguzungu kuona sasa Watanzania wengi wanamlilia JK, mwanasiasa ambaye hakuwa makini kabisa kuhusu mustakabali wa Tanzania yetu.

Ni hivi, kuna mengi hayawekwi wazi kuhusu yaliyojiri kati ya 2005 na 2015, na siku yakiwekwa hadharani itakuwa balaa. Bwana Magufuli aliposema 'tusifukue makaburi' alitumia busara tu ili kuepusha aibu ambayo kimsingi isingekuwa kuhusu utawala wa JK tu bali mwendelezo wa CCM kuwa janga kwa taifa letu.

Kutoka EPA hadi Kagoda hadi Richmond hadi Escrow, utawala wa JK ulitawaliwa na skandali mfululizo. Pengine JK hakuwa mwanasiasa mwenye mapungufu lakini kosa lake kubwa lilikuwa maandalizi yake kuwania urais from 1995 to 2005, ambapo alikusanya sapoti ya kila kundi, ikiwa ni pamoja na mafisadi. lipopata urais, JK alikuwa na deni kubwa kwa watu hawa, na hii ilipeleka awaruhusu kutafuna keki ya taifa kama asante yake kwao.

Sihitaji kukumbusha kuwa JK alikuwa Rais kwa tiketi ya CCM.

Magufuli pia ni Rais kwa tiketi ya CCM, lakini wakati tunapongeza jitihada zake binafsi ni muhimu kutambua kuwa chama chake kina mchango mkubwa katika matatizo mengi yanayotukabili leo, ikiwa ni pamoja na hilo la utoroshaji wa mchanga wa dhahabu.

Lakini Magufuli hawezi kukwepa lawama kwa uamuzi wake kumteua Profesa Sospeter Muhongo kuwa Waziri wa Nishati na Madini, nafasi aliyolazimika kujiuzulu katika utawala wa JK kutokana na kashfa ya Escrow. Hivi Magufuli alikuwa anategemea miujiza kutoka kwa Prof Muhongo? 

Kwa waliosoma kitabu changu cha 'Dokta John Magufuli: Sa fari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake' watakumbuka nilichoandika ukurasa wa 74 kuhusu uamuzi wa Magufuli kumteua Profesa Muhongo. 



Niliandika


Hata hivyo, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Angalau Magufuli amejitahidi kufanya jitihada binafsi kukabiliana na majambazi wanaobaka uchumi wetu. Ile tu kuchukua hatua inapaswa kupongezwa hasa ikizingatiwa kuwa watangulizi wake watatu -Mwinyi,Mkapa na JK - waliishia kutupatia matumaini hewa huku ufisadi ukizidi kushamiri.

Jana nilimwangalia Katibu Mwenezi wa CCM Humphrey Poplepole akitoa maneno mazito kuhusiana na suala la mchanga wa dhahabu. Nikaandika tweet kwamba Bwana Polepole anaongea kana kwamba CCM haihusiki na kuwezesha ujambazi uliopelekea mchanga wa madini kusafirisha. Akaleta uzushi kuwa sijui mie nipo ughaibuni, sijui sina uhalali. Baadhi ya watu wakamshutumu kuwa ni mbaguzi (kuwa ughaibuni  hakuninyimi uhuru wa kuzungumzia mustakabali wa taifa letu) lakini mie siamini kabisa kuwa huyu Polepole ni mbaguzi. Ni siasa tu.

Mwisho, makala hii haitokamilika ipasavyo bila kuwatupia neno ndugu zangu wa kitengo. Hebu fanyeni kuona aibu japo kidogo. Hivi inawezekanaje taifa kuibiwa zaidi ya shilingi trilioni moja ilhali ninyi mkifaidi mishahara minono na posho nzuri inayotakana na jasho la Watanzania masikini lakini mnawaangusha kiasi hicho? Tatizo la kitengo ni vipaumbele fyongo, kuandama watu wasiohusika badala ya kukwekeza nguvu dhidi ya wahalifu halisi/matishi halisi kwa usalama wa taifa letu.

Hata hivyo, kwa vile lawama hazijengi, ni matumaini yangu makubwa kuwa suala hilo la mchanga wa dhahabu litatufungua mcho kama taifa na kukabiliana na ujambazi wa aina hii. Sina uhakika sana kuhusu mbinu mwafaka, lakini pengine kwa kuanzia, CCM hata kama inaona aibu kuwaomba radhi Watanzania kwa kuwa kichaka cha ufisadi, hali iliyowezesha ujambazi wa mchanga huo wenye madini, basi angalau imuunge mkono mwenyekiti wao, si kwa porojo za kina Polepole bali kwa vitendo halisi. Wingi wa wabunge wa chama hicho tawala uwe na faida kwa wananchi na taifa na sio mhuri wa kupitisha kila kitu kama ilivyokuwa kwa miswada iliyopeleka sheria za madini zinazowapa fursa wawekezaji wasio waaminifu kutorosha kila wanachotaka ilhali sie tukizidi kuwa masikini.

Mungu ibariki Tanzania

1 Dec 2014

Kwanza niombe samahani kwa ku-update blogu hii kitambo. Nilitingwa na majukumu. Pili, makala hii chini ilichapishwa katika gazeti la RAIA MWEMA toleo la Jumatano Novemba 26, 2014, lakini kwa sbabau nisizofahamu tovuti ya gazeti hilo haikuwa up-dated hadi asubuhi hii. Licha ya kuwa na nakala halisi ya makala hii, nilionelea ni vema kusubiri 'edited version' ya makala hii pindi ikichapishwa kwenye tovuti ya RAIA MWEMA. Endelea kuisoma
KWANZA, nianze makala hii kwa kuomba samahani kwa ‘kutoonekana’ kwa takriban mwezi mzima sasa. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Ninapenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa wasomaji mbalimbali walionitumia barua-pepe kuulizia kuhusu ‘ukimya’ huo.
Wiki iliyopita, Rais wa Marekani, Barack Obama, aliandika historia kwa kuweka hadharani mpango kabambe kuhusu hatma ya takribani wakazi milioni 12 wanaoishi isivyo halali nchini humo.
Ujasiri wa Obama katika suala hilo unatokana na ukweli kwamba licha ya jitihada za muda mrefu, uhasama wa kisiasa kati ya vyama vikuu vya siasa nchini humo, Democrats na Republicans, ulikuwa kikwazo kikubwa katika kufikia mwafaka na ufumbuzi.
Wakati vyama vyote viwili vinaafikiana kuhusu uwepo wa wakazi hao wasio halali milioni 12, wahafidhina wa Republicans wamekuwa wapinzani wakubwa kuhusu ‘ufumbuzi rahisi’ wa kutoa msamaha (amnesty) kwa wahamiaji hao na kisha kuimarisha udhibiti katika mianya inayotumiwa na ‘wahamiaji haramu.’
Lakini suala hilo limekuwa mzigo mkubwa kwa Obama ambaye hata kabla hajaingia madarakani aliahidi kutafuta ufumbuzi hasa ikizingatiwa kwamba licha ya utajiri wa Marekani, hakuna uwezekano wa kuwatumia wahamiaji hao wote.
Kadhalika, mara kadhaa Obama alikuwa akieleza kwamba kulipuuza tatizo hilo hakutolifanya lipotee lenyewe, bali litazidi kuwa kubwa na gumu kulitatua.
Hatimaye Obama aliwatahadharisha Republicans kuwa atalazimika kutumia ‘Nguvu ya Kirais’ (Executive Order) ambayo haihitaji kuridhiwa na Bunge la nchi hiyo, iwapo wanasiasa wataendeleza malumbano pasipo kuja na ufumbuzi.
Hata hivyo, Republicans walitoa vitisho mbalimbali kwa Obama dhidi ya kutumia ‘executive order,’ huku baadhi wakitishia kumburuza mahakamani ili kumng’oa madarakani kwa madai ya ‘kukiuka katiba.’
Licha ya vitisho hivyo, na upinzani wa wengi wa wananchi wa kawaida (ambao kura za maoni zilionyesha wananchi wengi kutoafiki Rais kutumia ‘executive order’ katika suala hilo), hatimaye Obama aliweka hadharani mpango huo kabambe utakaowapatia ahueni ya kimakazi takriban wahamiaji milioni tano.
Matokeo ya uamuzi huo ni bayana: Republicans wamekasirishwa mno na hatua hiyo, huku chama cha Democrats ambacho kwa kiwango kikubwa kimekuwa mstari wa mbele kuwanusuru wahamiaji hao, kikinufaika kwa sapoti kutoka kundi muhimu katika siasa za chaguzi za Marekani, Walatino.
Kundi hili linatajwa kuwa muhimu mno kwa vyama vyote viwili, kwa Democrats kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2016, na Republicans kukamata Ikulu baada ya miaka 10 ya Obama. Kidemografia, idadi ya Walatino inaongezeka kwa kasi kuliko kundi lolote lile la ‘asili ya watu’ kwa maana ya Wamarekani Weupe na Wamarekani Weusi, na makundi mengine madogo.
Sasa ni wazi kuwa ili mgombea wa chama chochote kile afanikiwe kuingia Ikulu, ni lazima apate sapoti na kura za kutosha kutoka kwa Walatino.
Uamuzi huo wa Obama umekuwa kama mtego kwa Republicans. Laiti chama hicho kikiendeleza upinzani dhidi ya suala hilo, si tu kitajipunguzia umaarufu wake kwa Walatino na hivyo kuathiri nafasi yao katika uchaguzi mkuu ujao, lakini pia kitawatenga Wamarekani wasio Walatino lakini wanaotaka ‘wahamiaji haramu’ kupatiwa makazi ya kudumu nchi humo.
Lakini kwa upande mwingine, chama hicho kinatambua kuwa kwa kiasi kikubwa ‘Wamarekani hao wapya’ (kwa maana ya ‘wahamiaji haramu’ watakaopewa makazi ya kudumu) wataisapoti Democrats kama kulipa fadhila kwa kushughulikia tatizo lao.
Nitaendelea kuwaletea maendeleo ya suala hili katika makala zijazo hasa kwa vile uamuzi huo wa Obama ni kama umeanzisha ‘vita’ ya kisiasa kati yake binafsi (na chama chake) dhidi ya Republicans ambao mapema mwezi huu walifanikiwa kukamata uongozi wa mabunge yote mawili ya nchi hiyo, yaani Seneti na Congress.
Lengo hasa la kuzungumzia tukio hilo la nchini Marekani ni hali ilivyo huko nyumbani hivi sasa. Hadi wakati ninaandaa makala hii, ‘mshikemshike’ unaotokana na skandali ya ufisadi wa ESCROW sio tu unazidi kukua lakini pia unaleta dalili za uwezekano wa Rais Kikwete kulazimika kufanya mabadiliko kwenye Baraza lake la mawaziri kwa mara nyingine.
Kwa vile takribani kila Mtanzania anafahamu kinachoendelea kuhusu skandali hiyo ya ESCROW, sioni haja ya kuizungumzia kiundani. Hata hivyo, pasi haya, na huku nikitambua kuwa Rais wetu Jakaya Kikwete yupo katika matibabu nchini Marekani, ukweli unabaki kuwa yeye ndiye chanzo cha yote haya.
Nikirejea uamuzi wa Obama kutumia ‘nguvu ya kirais’ kupata ufumbuzi katika tatizo la ‘wahamiaji haramu,’ Kikwete alipaswa kuchukua hatua kama hiyo muda mrefu uliopita. Hapa ninamaanisha Rais kutumia nguvu alizopewa na Katiba kupambana na uhalifu.
Ninaandika hivyo kwa sababu Kikwete ana uelewa wa kutosha kuhusu ‘mgogoro wa IPTL’ ikizingatiwa kuwa huko nyuma alishawahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini. Lakini wakati miaka yake 10 ikielekea ukingoni, hakuna jitihada yoyote ya maana iliyofanywa nae kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.
Lakini hata tukiweka kando uzoefu wake katika suala hilo, utawala wake utakumbukwa zaidi kwa kuandamwa na mlolongo wa matukio ya ufisadi ambayo hatma yake imekuwa kuwashawishi mafisadi wengine ‘kujaribu bahati zao’.
Naam, kama Kikwete alidiriki ‘kukumbushia haki za binadamu’ za mafisadi wa EPA, na kuwapa deadline ya kurejesha mabilioni waliyoiba, kwanini mafisadi watarajiwa waogope kufanya uhalifu?
Yayumkinika kuhitimisha kwamba laiti idadi ya safari alizokwishafanya nchi za nje ingelingana na hatua dhidi ya ufisadi/ mafisadi, huenda leo hii tungekuwa tunazungumzia ‘mafanikio ya kihistoria ya uchumi wa Tanzania’.
Badala yake, tumekuwa tukiandamwa na vyombo vya habari vya kimataifa kuhusu taifa letu lilivyoukumbatia ufisadi kiasi cha kuruhusu ndege ya msafara wa Rais wa China kuondoka na vipusa, sambamba na taarifa mpya kuwa kuna mpango wa serikali kuwatimua wafugaji wa Kimasai katika makazi yao ili kukabidhi eneo hilo kwa familia ya kifalme ya mojawapo ya nchi za Kiarabu.
Sasa badala ya viongozi wetu kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa letu, wamekuwa ‘bize’ kupambana na vyombo vya habari vya kimataifa kukanusha tuhuma hizo. Hivi wazembe hawa hawaoni haya na kujiuliza “kwa kipi hasa cha kuvifanya vyombo vya habari vya kimataifa vituandame bila sababu?”
Kwa upande mwingine, skandali hii ya ESCROW ni uthibitisho mwingine kuwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa (TISS) imepoteza mwelekeo, haitimizi wajibu wake, na ni kama ipo likizo ya muda mrefu.
Hivi inawezekana vipi huyo ‘Singasinga’ anayetajwa kuwa mhusika mkuu katika skandali hiyo aliruhusiwa kuishi Tanzania huko rekodi yake ikionyesha bayana kuwa ni mtu hatari kwa usalama wa taifa letu?
Hii haikuhitaji hata operesheni maalum kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani habari za mtu huyo zipo wazi kwenye mtandao. Hivi Idara hiyo imejaa uzembe kiasi cha kushindwa japo ku-Google taarifa za mtu huyo?
Lakini kama ambavyo lawama nyingi katika skandali hii zinaelekezwa kwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu na Katibu Mkuu wake, Eliachim Maswi, sambamba na Mwanasheria Mkuu, Frederick Werema, huku Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akishutumiwa kwa kushindwa kusimamia vema watendaji walio chini yake, wenye kustahili kubeba lawama kubwa zaidi ni Rais Kikwete na idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Ninaandika makala hii kabla ya taarifa za uchunguzi za CAG na TAKUKURU kusomwa hadharani na ‘Kamati ya Zitto’ (PAC), kwahiyo ni vigumu kubashiri hatma ya suala hili. Hata hivyo, uzoefu wa skandali zilizopita, kuanzia Richmond, EPA, Mabilioni  yaliyofichwa Uswisi, Meremeta, Tangold, nk, si ajabu iwapo wahusika wakuu watalindwa na Watanzania kuachwa ‘wanang’aa macho tu.’
Muda mfupi uliopita, zimepatikana taarifa kwamba ripoti hiyo ya PAC imeonekana mitaani huku kurasa zenye majina ya wahusika zikiwa zimenyofolewa. Binafsi ninaamini huo ni ‘uhuni’ tu unaofanywa kuwachanganya Watanzania.
Lakini ukijumlisha na tukio linalodaiwa la kunyweshwa sumu Mbunge Nimrod Mkono, ni muhimu kutodharau nia, sababu na uwezo wa mafisadi kupambana na ukweli kuhusu skandali hii.
Nihitimishe makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete- kwa mara nyingine - kuwa chini ya mwaka mmoja kutoka sasa atarejea ‘uraiani.’ Ni muhimu kwake kutumia miezi hii michache iliyobaki kurejea ahadi aliyotoa mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wetu mwaka 2005 kuwa hatowaonea aibu mafisadi. Tungependa tumkumbuke kwa mema lakini sio rekodi ya kuliingiza taifa kwenye korongo refu la ufisadi.
Kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ninawasihi mtambue mzigo mkubwa mnaowabebesha Watanzania masikini kumudu gharama za operesheni zenu. Kwanini msijiskie aibu  kuwasaliti wanyonge hawa –wengi wakiwa ni ndugu, jamaa na marafiki zenu – kwa kutotimiza majukumu yenu ipasavyo?
TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.