Showing posts with label Tegeta Escrow. Show all posts
Showing posts with label Tegeta Escrow. Show all posts

20 Jun 2017

Katika Tanzania yetu ya zama hizi ambapo takriban kila jambo linaanglaiwa kwa jicho la kisiasa, ni vigumu sio tu kusimamia ukweli bali pia kukwepa lawama kutoka kwa pande mbili kuu za siasa zetu: CCM au Upinzani.

Sie tusio na vyama, tukikosoa masuala yanayoigusa CCM/serikali, akina Humphrey Polepole wanakurupuka na kutuita majina ya ajabu ajabu. Tukikosoa Upinzani, tunaambiwa "nafasi za Ukuu wa Wilaya zimeshajaa." Good news is, kuna watu - hata kama ni wachache - waliopo CCM, Upinzani na wasio na vyama ambao wanatusikiliza. Na wanatusikiliza kwa vile wanafahamu hatuelemei upande wowote isipokuwa kwenye ukweli.

Baada ya angalizo hilo, tugeukia big news iliyosikika jana, ghafla, na kutukuta wengi wetu tusiamini macho/masikio yetu. Baada ya miaka nenda miaka rudi, hatimaye mfanyabiashara James Rugemalira na mwenzie Singasinga Harbinder Seth Singh walipandishwa kizimbani kwa tuhuma za kuhujumu uchumi.



Kwa tunaofahamu Rugemalira ameisumbua Tanzania yetu kiasi gani, na sambamba na 'usumbufu' wa huyu Singasinga, hatua hiyo tu ya kuwapindisha wawili hao kizimbani inastahili pongezi za kila Mtanzania. Na anayestahili pongezi hizo kwa wingi kabisa ni Rais John Magufuli.
Sawa, kuna watakaosema kuwa "lakini hiyo si ndio kazi ya Rais?" only if tukipuuzia ukweli kwamba Rugemalira alikuwa kama ameshindikana katika Awamu angalau mbili zilizopita, ya Mkapa na Kikwete, na ilikuwa kama huyu mtu kaachwa afanye apendacho katika kuihujumu nchi yetu.
Nimesoma angalizo la mwanasiasa wa Chadema na mwanasheria nguli, Tundu Lissu, akitahadharisha kuhusu Rugemalira na Singasinga, kwamba hao ni sehemu tu ya mtandao mkubwa wa ufisadi. Hata hivyo, japo angalizo hilo ni muhimu, haliondoi ukweli kwamba angalau JPM amethubutu, sio tu kuwapandisha Rugemalira na Singasinga kizimbani bali pia kuwalaza rumande.

Ni wazi kuwa vita hii ambayo Rais Magufuli ameivalia njuga sio rahisi. Sio tu kwa vile inahusisha watu wenye uwezo mkubwa kifedha bali pia kwa sababu pia inawagusa baadhi ya wanasiasa maarufu ndani ya chama chake cha CCM. 
Licha ya angalizo la Lissu, kuna baadhi ya wananchi wanaotoa tahadhari 'kushangilia mapema kabla ya dakika 90.' Hawa pia wana hoja ya msingi hasa kwa kuzingatia mfano kama wa kesi ya Balozi Mahalu. Hata hivyo, kuna haja ya kuwa na matumaini hasa ikizingatiwa kuwa JPM hafanyi anayofanya kwa shinikizo la mtu yeyote yule. Ni utashi wake tu. Angetaka kukaa kimya, kusingekuwa na maandamano ya kumshinikiza achukue hatua.

Kama ningekuwa na fursa ya kumshauri Rais Magufuli basi ningemwomba sana awekeze nguvu zaidi katika vita hii dhidi ya ufisadi ambayo kwa hakika inawaunganisha Watanzania wengi waliochoka kuona nchi yao ikigeuzwa shamba la bibi, badala ya 'uhasama na wanasiasa wa Upinzani.'

Kwa mfano, jana, kabla ya habari hiyo ya Rugemalira na Singasinga kufikishwa mahakamani na baadaye kutupwa rumande, zilizpatikana taarifa kuhusu serikali kupitia jeshi la polisi 'kuwabughudhi' wanasiasa kadhaa wa Chadema ikiwa ni pamoja na kuzuwia ziara ya Waziri Mkuu wa zamani na kiognozi wa ngazi za juu Chadema, Frederick Sumaye.
Katika kipindi hiki cha vita ngumu dhidi ya mafisadi na ufisadi, tunapaswa kuwa kitu kimoja. Si kwamba vyama vya upinzani viungane na CCM, bali angalau tofauti zisizo na msingi ziepukwe, na kubwa zaidi ni kupeuka uadui wa kisiasa.

Nihitimishe kwa pointi moja muhimu kwamba japo tuna historia isiyopendeza kuhusu mapambano dhidi ya ufisadi, na japo ni kweli kuwa wanasheria wa serikali hawana rekodi nzuri kwenye kesi kubwa za serikali, na vilevile japo ni kweli kuwa mara nyingi ukada umekuwa kikwazo kwa serikali kuchukua hatua stahili dhidi ya mafisadi, wito wangu kwa Watanzania wenzangu ni kumuunga mkono Rais Magufuli kwani angalau ameonyesha dhamira ya kuchukua hatua stahili. 

Vilevile ni muhimu kutambua kuwa vita hii sio dhidi ya watu tu bali ni dhidi ya mfumo uliojengeka muda mrefu. Kwa maana hiyo, japo tunatamani kuona watuhumiwa wote wakikamatwa na kupandishwa kizimbani, ni muhimu tuwe na subira, hasa ikizingatiwa kuwa kukurupusha mambo kunaweza kutupelekea kupoteza kesi dhidi ya 'maadui' wetu ambao kwa uweo wao mkubwa wa kifedha, wataajiri wanasheria bora kabisa kuwatetea.

MUNGU IBARIKI TANZANIA

29 Jan 2015

Enzi hizo: Rais Kikwete akiwa na James Rugemalira

RAIS Jakaya Kikwete anapaswa kuwajibika binafsi katika kashfa ya ukwapuaji wa mabilioni ya shilingi katika Akaunti ya Tegeta Escrow. Saed Kubenea anaandika…(endelea)

Mjumbe wa Kamati Kuu (CC) ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Mabere Marando amesema, Rais Kikwete, ndiye aliyeruhusu kiasi cha Sh. 321 bilioni kuchotwa katika mazingira yaliyosheheni udanganyifu.

“Fedha zile zimechukuliwa kwa maelekezo ya Rais Kikwete ili kumuwezesha chama chake kufanikishe kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka huu,” ameeleza Marando.

Hata hivyo, Marando anasema, “Tumeambiwa na watu waliokaribu na chama hicho, kuwa ni sehemu ndogo sana ya fedha iliyoibwa zilizofikishwa CCM. Nyingi ya fedha hizo zimechukuliwa na familia ya rais mwenyewe.”

Taarifa zinasema, familia ya Rais Kikwete imepata zaidi ya Sh. 9 bilioni, kutoka katika mgawo wa fedha zilizohifadhiwa katika akaunti ya Escrow.


“Kikwete anajua kila kitu. Yule singasinga – Harbinder Singh Sethi – alitokea Ikulu. Mpango wa uchotaji wa fedha za umma ulipangwa Ikulu na ulitekelezwa kwa maelekezo ya rais,” ameeleza.


Taarifa zinasema, anayejiita na kuitwa na serikali kuwa ni “mmiliki mpya wa IPTL/PAP,” Harbinder Singh Sethi, alichotewa fedha hizo baada ya kufikishwa Ikulu na baadaye akakutanishwa na gavana wa BoT, Prof. Benno Ndullu; na kutoka hapo alikwenda kukwapua mabilioni hayo ya shilingi hata bila kumfahamisha James Rugemalira – mbia mwenzake.

Sakata la ukwapuaji wa fedha katika akaunti ya Escrow ndilo lililomtupa nje ya ofisi, aliyekuwa waziri wa nishati, Prof. Sospeter Muhongo.

Taarifa zinasema, Prof. Muhongo, ni miongoni mwa wanaotajwa kunufaika na fedha za Escrow zilizopitia benki ya Stanbic. Mwingine ambaye jina lake lilitajwa bungeni na mmoja wa wabunge wa upinzani, ni Albert Marwa.

Marando anasema, “Pamoja na kujiuzulu kwa Prof. Muhongo, bado haitoshi bila kuhojiwa au kuwajibishwa kwa gavana Ndullu, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, Katibu Mkuu wizara ya Fedha, Dk. Servacius Likwalile na maofisa wa ikulu na hata rais mwenyewe ambaye ndiye aliyeruhusu fedha hizo kutolewa.”

Akiongea kwa kujiamini, Marando anasema, “Wizi huu ulianzia Ikulu na umefanyika kwa baraka za Ikulu na mbele ya macho ya rais. Umewashirikisha baadhi ya maofisa wake na hata familia yake.”

Dk. Likwalile ndiye aliyewasilisha kwa gavana wa BoT kwa ajili ya utekelezaji, maagizo ya Rais Kikwete kuwa fedha katika akaunti ya Escrow zilipwe kwa PAP.

Alikuwa akirejea maagizo kutoka kwa Rais Kikwete kwa kunukuu barua ya tarehe 13 Novemba 2013, ambayo ilisainiwa na Katibu wa Rais, Bw. Prosper Mbena.


24 Dec 2014

Awali,kupitia akaunti yake ya Twitter, Idhaa ya Kiswahili ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC Swahili) iliripoti ifuatavyo



Hata hivyo, baada ya kuzongwa na baadhi ya WANAHARAKATI huko Twitter walioonyesha kukerwa na hatua hiyo ya nchi wahisani, Mwenyekiti wa nchi wahisani, Balozi wa Finland nchini Tanzania Sinikka Antila (@SinikkaAntila) alifafanua kwa tweet ifuatayo 


Kwa lugha ya taifa, Balozi huyo anaeleza kwamba "vyombo vya habari havipo sahihi. Asilimia 15 ya msaada ulioahidiwa kwa bajeti ya mwaka 2014/15 ilitolewa kabla ya hotuba ya Rais (Kikwete)."

Hata hivyo, licha ya kauli hiyo ya Balozi Antila kutanabaisha kuwa BBC Swahili waliripoti ndivyo sivyo kuwa wafadhili wameamua kutofa fedha hizo baada ya kuridhishwa na hotuba ya Rais Kikwete, bado kuna swali gumu kuhusu suala hilo, nalo ni JE NCHI WAFADHILI ZILITUHADAA ZILIPODAI KUWA ZIMESITISHA MISAADA HADI HATUA ZITAKAPOCHUKULIWA KUHUSU SUALA LA ESCROW?

Swali hilo linatokana na kauli ya Balozi huyo wa Finland kuwa fedha hizo zilishatolewa hata kabla ya hotuba ya Rais Kikwete, ikimaanisha aidha nchi hizo wahisani zilikuwa zina hakika kuwa Rais Kikwete angechukua 'hatua hizo za kuwaridhisha wafadhili' au 'walituzuga tu' kuhusu kusitishwa misaada hiyo.

Kadhalika, kauli ya Balozi Antila haikanushi kuridhishwa kwa wafadhili na hotuba ya Rais Kikwete, ambayo Watanzania wengi wanaamini kuwa imewalinda mafisadi hasa ikizingatiwa mzigo mkubwa wanaoubeba kutokana na sakata la muda mrefu la IPTL. Kwa Rais Kikwete kushindwa kumaliza sakata hilo, na kuridhia kuwa pesa za Tegeta Escrow ni za IPTL/ PAP, ina maana Watanzania wataendelea kulipa mamilioni ya shilingi kila siku kwa huduma ya umeme ambayo kimsingi ni hewa.

Binafsi ninaguswa na uamuzi wa nchi wahisani kwa sababu kama mkazi wa Uingereza, ninalipa kodi mbalimbali, ambazo sehemu ya kodi hiyo ipo katika misaada inayotolewa na nchi hii kwa Tanzania. Wakati sina kipingamizi kwa nchi hizo kuisaidia Tanzania, siungi mkono kabisa kuendelea kutoa fedha zinazoishia kuwaneemesha mafisadi kwa kunenepesha akaunti zao, kuongeza idadi za mahekalu na magari yao ya thamani na kukuza idadi ya nyumba zao ndogo.

Ufadhili usiozingatia maslahi ya nchi fadhiliwa sio tu ni upuuzi bali pia ni ku-abuse fedha za walipakodi katika nchi wafadhili.

5 Dec 2014

Waingereza wana msemo ambao unatafsirika kwa Kiswahili kama "chuki ya pamoja ni mwanzo wa urafiki mkubwa." Kimahesabu kama A hapatani na B, na A anamchukia C kama ambavyo B anamchukia pia C, basi chuki ya A na B kwa C yaweza kuwa mwanzo wa wawili hao A na B kuwa marafiki wenye lengo la kumwangamiza C.

Binafsi, naomba kukiri kuwa kwa muda sasa nimekuwa siafikiani na mitizamo na mwenendo wa mwanasiasa mahiri wa upinzani, Zitto Kabwe. Siwezi kusema nina chuki dhidi yake bali mie sio miongoni mwa supporters wake.Pamoja na sababu nyingine, kubwa ni kile ninachokitafsiri kama mwanasiasa huyo kutanguliza mbele maslahi yake binafsi badala ya chama chake yaani Chadema. Kwa mtizamo wangu, mgogoro uliopelekea hatua ya Chadema kumvua madaraka Zitto ni matokeo ya 'imani potofu' kuwa kuna mwanasiasa anayeweza kuwa maarufu kuliko chama chake, Si kwamba haiwezekani kabisa kwa hilo kutokea lakini si kwa hatua waliyofikia Chadema hivi sasa.

Lakini lengo la makala hii si kumjadili Zitto wala ugomvi kati yake na Chadema. Ila nimegusia suala hilo kwa sababu nililazimika 'kurejesha urafiki' na mwanasiasa huyo, angalau kinadharia, wakati akifanya jitihada kubwa binafsi na kama mwenyekiti wa PAC kushughulikia ufisadi wa Tegeta Escrow. Kwa kutumia mfano huo hapo juu wa chuki za A kwa C na za B kwa C, na A ni Zitto, na B ni mie, huko C wakiwa mafisadi wa Escrow, basi 'urafiki' usingeepukika.

Hakuna Mtanzania atakayeshindwa kumpongeza Zitto na Kafulila pamoja na PAC kwa ujumla walivyofanya kazi kubwa na nzuri katika kushughulikia skandali hiyo. Nina imani hata wahusika wa ufisadi huo wa Escrow wanamkubali kwa jinsi alivyowakalia kooni...ALMOST.

Hata hivyo, mara baada ya kumalizika kwa 'timbwili' hilo la Escrow bungeni, nilitumiwa meseji na 'mjuzi mmoja wa mambo ya huko nyumbani' ambaye alidai kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na PAC, kuna 'mchezo mchafu' uliofanyika katika kufikia mwafaka miongoni mwa wajumbe, hususan wale wa kutoka CCM. Alidai kuwa kilichowezesha mwafaka huo kufikiwa ni pamoja na 'kumnusuru' Rais Jakaya Kikwete, ambaye kama Mbunge Tundu Lissu alivyobainisha bungeni, anatajwa kuhusika katika skandali hiyo. Kimsingi, hoja ya Lissu, ambaye pia aliilaumu Idara ya Usalama wa Taifa kwa kutowajibika ipasavyo katika mlolongo wa skandali mbalimbali zinazougubika utawala wa Rais Kikwet, iliuawa kimyakimya licha ya umuhimu wake mkubwa.

Hata hivyo, kwa uelewa wangu, jaribio lolote la kumhusisha Rais Kikwete na skandali hiyo hata kama ushahidi upo lingepelekea mparaganyiko mkubwa katika kamati hiyo ya Zitto. Na kama tulivyoshuhudia 'makada' wa CCM huko bungeni walivyopigana kufa na kupona hadi Waziri Mkuu Mizengo Pinda akanusuriwa, kwa hakika ishu ya Kikwete kuhusishwa na Escrow ingepelekea bunge hilo kuvunjika pasi kufikia hitimisho.

Lakini what if mkakati huo wa 'kumnusuru Rais Kikwete' unabeba mengi zaidi ya tunavyodhani? 


Kwa kifupi, tume-settle for less. Na Waingereza wana msemo unaotahadharisha kuhusu ku-settle for less, ambapo wanasema 'pindi ukikubali kupokea pungufu ya unachostahilki basi hatimaye utaishia kupokea pungufu zaidi ya kile ulichostahili awali.' Japo ni mapema kuhitimisha kwamba 'tumeingizwa mkenge,' lakini ukimya wa Rais Kikwete katika kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu Escrow umeanza kuzua wasiwasi.

Na 'kigugugmizi' kinachomkabili Rais Kikwete kina sababu kadhaa za wazi. Kwa mfano, kumtimua Mwanasheria Mkuu Jaji Werema kunaweza kupelekea kuzuka kwa skandali nyingine iwapo Jaji huyo ataamua 'mmemwaga mboga, na mie namwaga ugali' kwa maana anajua mengi yaliyojiri na yanayojiri katika utawala wa Rais Kikwete. Japo si kwamba haiwezekani kumtimua na kisha kumfunga mdomo, lakini historia ya wanasheria wakuu huko nyuma inapaswa kutukumbusha jinsi 'wanavyobebwa' kwa minajili ya 'kutotengeneza uadui na mtu anayejua siri nyingi.'

Kwa upande wmingine, ni muhimu kukumbuka kuwa kimsingi Rais Kikwete ndo aliyemleta Profesa Muhongo katika frontline politics. Hawa ni marafiki wa karibu. Na hadi sasa Muhongo ameendeleza jeuri yake ya kisomi na kusisitiza kuwa fedha za Escrow si za umma. Msimamo huo pia washikiliwa na Waziri Mkuu Pinda. Je kuna anayefahamu msimamo wa Rais Kikwete? Maelezo yanaonyesha kuwa yeye aliridhia malipo ya Escrow kufanyika. Je amebadili mawazo na kutambua kuwa hilo lilikuwa kosa?

Lakini wakati tayari tunafahamu majina mengi ya walionufaika na mgao wa Escrow kupitia Benki ya Mkombozi, inadaiwa kuwa mgao mkubwa zaidi uliopitia Benki ya Stanbic ulihusisha vigogo kadhaa lakini hadi muda huu hakuna jina hata moja lililowekwa hadharani. So far, gazeti la Raia Mwema limeripoti kuwa mke wa kigogo momja mwandamizi huko Ikulu alikatiwa shilingi bilioni 5. Sasa huhitaji kujua hesabati vizuri kubashiri kwamba kama mke wa kigogo alikatiwa mbilioni tano, mumewe alipewa kiasi gani? 

Hayo yote tisa, kumi ni kauli niliyokumbana nayo muda mfupi uliopita, na ambayo kwa hakika ndio iliyonisukuma kuandika makala hii. Kauli hiyo ni ya Jaji Mkuu Chande ambayo kimsingi inaharibu mwenendo wa kesi yoyote itakayofunguliwa dhidi ya wahusika wa ufisadi wa Escrow. Nimeinukuu kwa picha hapa chini.


Je Jaji Mkuu alikuwa anatoa tu tahadhari au alikuwa akifikisha ujumbe mahsusi kwamba hata tukiwapeleka mahakamani wahusika wa Escrow, utetezi wao upo bayana...kwamba walishahukumiwa bungeni. Na kama Jaji Mkuu 'hakutumwa' basi kwa hakika amewapatiwa washtakiwa-watarajiwa ushauri mzuri wa bure kisheria kuhusu jinsi ya kupambana na kesi yoyote watakayofunguliwa kuhusisna na suala hilo: wajitetee kuwa walishahukumiwa na bunge, na mawakili waoa waweza kutumia kauli hiyo ya Jaji Mkuu kama supporting evidence.

Anyway, pengine ni mapema mno kuhukumu lakini kama ambavyo Mzee Warioba alivyoonyesha mapungufu ya taarifa ya PAC na maazimio ya bunge kuhusu skandali ya Escrow, sintomshangaa mtu yeyote atakayeanza kupatwa na wasiwasi kuwa tumeingizwa mkenge...TENA.


Sijui msomaji mepndwa unaonaje. 





1 Dec 2014

Kwanza niombe samahani kwa ku-update blogu hii kitambo. Nilitingwa na majukumu. Pili, makala hii chini ilichapishwa katika gazeti la RAIA MWEMA toleo la Jumatano Novemba 26, 2014, lakini kwa sbabau nisizofahamu tovuti ya gazeti hilo haikuwa up-dated hadi asubuhi hii. Licha ya kuwa na nakala halisi ya makala hii, nilionelea ni vema kusubiri 'edited version' ya makala hii pindi ikichapishwa kwenye tovuti ya RAIA MWEMA. Endelea kuisoma
KWANZA, nianze makala hii kwa kuomba samahani kwa ‘kutoonekana’ kwa takriban mwezi mzima sasa. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Ninapenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa wasomaji mbalimbali walionitumia barua-pepe kuulizia kuhusu ‘ukimya’ huo.
Wiki iliyopita, Rais wa Marekani, Barack Obama, aliandika historia kwa kuweka hadharani mpango kabambe kuhusu hatma ya takribani wakazi milioni 12 wanaoishi isivyo halali nchini humo.
Ujasiri wa Obama katika suala hilo unatokana na ukweli kwamba licha ya jitihada za muda mrefu, uhasama wa kisiasa kati ya vyama vikuu vya siasa nchini humo, Democrats na Republicans, ulikuwa kikwazo kikubwa katika kufikia mwafaka na ufumbuzi.
Wakati vyama vyote viwili vinaafikiana kuhusu uwepo wa wakazi hao wasio halali milioni 12, wahafidhina wa Republicans wamekuwa wapinzani wakubwa kuhusu ‘ufumbuzi rahisi’ wa kutoa msamaha (amnesty) kwa wahamiaji hao na kisha kuimarisha udhibiti katika mianya inayotumiwa na ‘wahamiaji haramu.’
Lakini suala hilo limekuwa mzigo mkubwa kwa Obama ambaye hata kabla hajaingia madarakani aliahidi kutafuta ufumbuzi hasa ikizingatiwa kwamba licha ya utajiri wa Marekani, hakuna uwezekano wa kuwatumia wahamiaji hao wote.
Kadhalika, mara kadhaa Obama alikuwa akieleza kwamba kulipuuza tatizo hilo hakutolifanya lipotee lenyewe, bali litazidi kuwa kubwa na gumu kulitatua.
Hatimaye Obama aliwatahadharisha Republicans kuwa atalazimika kutumia ‘Nguvu ya Kirais’ (Executive Order) ambayo haihitaji kuridhiwa na Bunge la nchi hiyo, iwapo wanasiasa wataendeleza malumbano pasipo kuja na ufumbuzi.
Hata hivyo, Republicans walitoa vitisho mbalimbali kwa Obama dhidi ya kutumia ‘executive order,’ huku baadhi wakitishia kumburuza mahakamani ili kumng’oa madarakani kwa madai ya ‘kukiuka katiba.’
Licha ya vitisho hivyo, na upinzani wa wengi wa wananchi wa kawaida (ambao kura za maoni zilionyesha wananchi wengi kutoafiki Rais kutumia ‘executive order’ katika suala hilo), hatimaye Obama aliweka hadharani mpango huo kabambe utakaowapatia ahueni ya kimakazi takriban wahamiaji milioni tano.
Matokeo ya uamuzi huo ni bayana: Republicans wamekasirishwa mno na hatua hiyo, huku chama cha Democrats ambacho kwa kiwango kikubwa kimekuwa mstari wa mbele kuwanusuru wahamiaji hao, kikinufaika kwa sapoti kutoka kundi muhimu katika siasa za chaguzi za Marekani, Walatino.
Kundi hili linatajwa kuwa muhimu mno kwa vyama vyote viwili, kwa Democrats kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2016, na Republicans kukamata Ikulu baada ya miaka 10 ya Obama. Kidemografia, idadi ya Walatino inaongezeka kwa kasi kuliko kundi lolote lile la ‘asili ya watu’ kwa maana ya Wamarekani Weupe na Wamarekani Weusi, na makundi mengine madogo.
Sasa ni wazi kuwa ili mgombea wa chama chochote kile afanikiwe kuingia Ikulu, ni lazima apate sapoti na kura za kutosha kutoka kwa Walatino.
Uamuzi huo wa Obama umekuwa kama mtego kwa Republicans. Laiti chama hicho kikiendeleza upinzani dhidi ya suala hilo, si tu kitajipunguzia umaarufu wake kwa Walatino na hivyo kuathiri nafasi yao katika uchaguzi mkuu ujao, lakini pia kitawatenga Wamarekani wasio Walatino lakini wanaotaka ‘wahamiaji haramu’ kupatiwa makazi ya kudumu nchi humo.
Lakini kwa upande mwingine, chama hicho kinatambua kuwa kwa kiasi kikubwa ‘Wamarekani hao wapya’ (kwa maana ya ‘wahamiaji haramu’ watakaopewa makazi ya kudumu) wataisapoti Democrats kama kulipa fadhila kwa kushughulikia tatizo lao.
Nitaendelea kuwaletea maendeleo ya suala hili katika makala zijazo hasa kwa vile uamuzi huo wa Obama ni kama umeanzisha ‘vita’ ya kisiasa kati yake binafsi (na chama chake) dhidi ya Republicans ambao mapema mwezi huu walifanikiwa kukamata uongozi wa mabunge yote mawili ya nchi hiyo, yaani Seneti na Congress.
Lengo hasa la kuzungumzia tukio hilo la nchini Marekani ni hali ilivyo huko nyumbani hivi sasa. Hadi wakati ninaandaa makala hii, ‘mshikemshike’ unaotokana na skandali ya ufisadi wa ESCROW sio tu unazidi kukua lakini pia unaleta dalili za uwezekano wa Rais Kikwete kulazimika kufanya mabadiliko kwenye Baraza lake la mawaziri kwa mara nyingine.
Kwa vile takribani kila Mtanzania anafahamu kinachoendelea kuhusu skandali hiyo ya ESCROW, sioni haja ya kuizungumzia kiundani. Hata hivyo, pasi haya, na huku nikitambua kuwa Rais wetu Jakaya Kikwete yupo katika matibabu nchini Marekani, ukweli unabaki kuwa yeye ndiye chanzo cha yote haya.
Nikirejea uamuzi wa Obama kutumia ‘nguvu ya kirais’ kupata ufumbuzi katika tatizo la ‘wahamiaji haramu,’ Kikwete alipaswa kuchukua hatua kama hiyo muda mrefu uliopita. Hapa ninamaanisha Rais kutumia nguvu alizopewa na Katiba kupambana na uhalifu.
Ninaandika hivyo kwa sababu Kikwete ana uelewa wa kutosha kuhusu ‘mgogoro wa IPTL’ ikizingatiwa kuwa huko nyuma alishawahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini. Lakini wakati miaka yake 10 ikielekea ukingoni, hakuna jitihada yoyote ya maana iliyofanywa nae kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.
Lakini hata tukiweka kando uzoefu wake katika suala hilo, utawala wake utakumbukwa zaidi kwa kuandamwa na mlolongo wa matukio ya ufisadi ambayo hatma yake imekuwa kuwashawishi mafisadi wengine ‘kujaribu bahati zao’.
Naam, kama Kikwete alidiriki ‘kukumbushia haki za binadamu’ za mafisadi wa EPA, na kuwapa deadline ya kurejesha mabilioni waliyoiba, kwanini mafisadi watarajiwa waogope kufanya uhalifu?
Yayumkinika kuhitimisha kwamba laiti idadi ya safari alizokwishafanya nchi za nje ingelingana na hatua dhidi ya ufisadi/ mafisadi, huenda leo hii tungekuwa tunazungumzia ‘mafanikio ya kihistoria ya uchumi wa Tanzania’.
Badala yake, tumekuwa tukiandamwa na vyombo vya habari vya kimataifa kuhusu taifa letu lilivyoukumbatia ufisadi kiasi cha kuruhusu ndege ya msafara wa Rais wa China kuondoka na vipusa, sambamba na taarifa mpya kuwa kuna mpango wa serikali kuwatimua wafugaji wa Kimasai katika makazi yao ili kukabidhi eneo hilo kwa familia ya kifalme ya mojawapo ya nchi za Kiarabu.
Sasa badala ya viongozi wetu kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa letu, wamekuwa ‘bize’ kupambana na vyombo vya habari vya kimataifa kukanusha tuhuma hizo. Hivi wazembe hawa hawaoni haya na kujiuliza “kwa kipi hasa cha kuvifanya vyombo vya habari vya kimataifa vituandame bila sababu?”
Kwa upande mwingine, skandali hii ya ESCROW ni uthibitisho mwingine kuwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa (TISS) imepoteza mwelekeo, haitimizi wajibu wake, na ni kama ipo likizo ya muda mrefu.
Hivi inawezekana vipi huyo ‘Singasinga’ anayetajwa kuwa mhusika mkuu katika skandali hiyo aliruhusiwa kuishi Tanzania huko rekodi yake ikionyesha bayana kuwa ni mtu hatari kwa usalama wa taifa letu?
Hii haikuhitaji hata operesheni maalum kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani habari za mtu huyo zipo wazi kwenye mtandao. Hivi Idara hiyo imejaa uzembe kiasi cha kushindwa japo ku-Google taarifa za mtu huyo?
Lakini kama ambavyo lawama nyingi katika skandali hii zinaelekezwa kwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu na Katibu Mkuu wake, Eliachim Maswi, sambamba na Mwanasheria Mkuu, Frederick Werema, huku Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akishutumiwa kwa kushindwa kusimamia vema watendaji walio chini yake, wenye kustahili kubeba lawama kubwa zaidi ni Rais Kikwete na idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Ninaandika makala hii kabla ya taarifa za uchunguzi za CAG na TAKUKURU kusomwa hadharani na ‘Kamati ya Zitto’ (PAC), kwahiyo ni vigumu kubashiri hatma ya suala hili. Hata hivyo, uzoefu wa skandali zilizopita, kuanzia Richmond, EPA, Mabilioni  yaliyofichwa Uswisi, Meremeta, Tangold, nk, si ajabu iwapo wahusika wakuu watalindwa na Watanzania kuachwa ‘wanang’aa macho tu.’
Muda mfupi uliopita, zimepatikana taarifa kwamba ripoti hiyo ya PAC imeonekana mitaani huku kurasa zenye majina ya wahusika zikiwa zimenyofolewa. Binafsi ninaamini huo ni ‘uhuni’ tu unaofanywa kuwachanganya Watanzania.
Lakini ukijumlisha na tukio linalodaiwa la kunyweshwa sumu Mbunge Nimrod Mkono, ni muhimu kutodharau nia, sababu na uwezo wa mafisadi kupambana na ukweli kuhusu skandali hii.
Nihitimishe makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete- kwa mara nyingine - kuwa chini ya mwaka mmoja kutoka sasa atarejea ‘uraiani.’ Ni muhimu kwake kutumia miezi hii michache iliyobaki kurejea ahadi aliyotoa mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wetu mwaka 2005 kuwa hatowaonea aibu mafisadi. Tungependa tumkumbuke kwa mema lakini sio rekodi ya kuliingiza taifa kwenye korongo refu la ufisadi.
Kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ninawasihi mtambue mzigo mkubwa mnaowabebesha Watanzania masikini kumudu gharama za operesheni zenu. Kwanini msijiskie aibu  kuwasaliti wanyonge hawa –wengi wakiwa ni ndugu, jamaa na marafiki zenu – kwa kutotimiza majukumu yenu ipasavyo?
TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.