17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-39:

Asalam aleykum,

Leo ni siku ya UKIMWI duniani.Ni siku ambayo kwa wengi ni ya majonzi kwa vile ni kumbukumbu ya wapendwa wao ambao wamepoteza maisha kutokana na gonjwa hili ambalo hadi sasa halina tiba.Pia ni siku ngumu kwa mamilioni ya wenzetu ambao wameambukizwa na virusi vya ugonjwa huo hasa kwa vile ni mwaka mwingine unakamilika pasipo dalili kwamba lini zahma hii itaondoka katika uso wa dunia.Kadhalika siku hii inawagusa pia wale ambao wanauguza wazazi,watoto,rafiki na jamaa zao huku wakipigana na kutokata tamaa hasa kwa vile kumkatia tama mgonjwa ni sawa na kumwombea dua afariki,na katika mila zote hiyo ni sawa na kufuru.

Wanasayansi katika kila kona ya sayari hii wanahangaika usiku na mchana kutafuta ufumbuzi wa ugonjwa huu.Kwa upande mwingine,wanaharakati wa UKIMWI nao wanahangaika na jitihada za kuukumbusha umma kuwa ugonjwa huu bado upo na unateketeza watu kila kukicha.Wanaharakati hao pia wanaendelea kuweka msukumo kwa jamii kufahamu kuwa waathirika wa UKIMWI ni watu kama sisi,wanahitaji upendo na sapoti ili kuweza kuendelea kuishi kwa matumaini.Sambamba na hilo ni harakati zao za kudhibiti unyanyapaa ambao kwa kiasi kikubwa ni jambo linalowafanya waathirika wajione kama watu wa kutoka sayari nyingine.

Takwimu zilizopo kuhusu ugonjwa huo huko nyumbani sio za kufurahisha.Naomba niziweke bayana hapa,kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linashughulikia Ukimwi (UNAIDS) katika ripoti yake ya mwaka huu ambayo kimsingi inaelezea hali ilivyokuwa mwaka jana.Watu wazima na watoto wanaoishi na virusi vya ugonjwa huo ni kati ya 1,300,000-1,600,000 (wastani 1,400,000),ambapo wanawake ni kati ya 640,000-780,000 (wastani 710,000), watoto 43,000-210,000 (wastani 110,000), huku vifo vya watu wazima na watoto vikiwa ni kati ya 110,000-180,000 na idadi ya yatima ni kati ya 910,000-1,200,000 (wastani 1,100,000).Binafsi nina “allergy” na hisabati (na ndio maana ndoto zangu za kuwa daktari-wa hospitali-zilimomonyoka baada ya kuambulia F nzuri tu kwenye Fizikia na D ya kubabaisha kwenye hisabati kwenye “pepa” za kidato cha nne).Kwa mantiki hiyo naomba mnisamehe kwa kuepuka kuchambua takwimu hizo,ila naamini zinajieleza zenyewe.Hata hivyo,pamoja na “umaimuna” wangu kwenye hisabati nafahamu kwamba takwimu huzingatia makadirio,na kwa namna flani hazitoi picha kamili kabisa bali picha ya jumla.

Na kuna jambo moja la kuzingatia kuhusu hizi takwimu “za kimataifa.” Nalo ni namna takwimu hizo zinavyokusanywa.Yayumkinika kusema kwamba ni rahisi kupata takwimu sahihi zaidi za UKIMWI kwa nchi kama Uingereza ambapo watu wana tabia ya kufanya uchunguzi wa afya zao angalau mara moja kila mwaka.Lakini sote tunatambua kuwa kwa huko nyumbani utaratibu huo ni kama anasa flani,yaani wengi hupima afya zao pale tu wanapojiskia vibaya,au pale akinamama wanapokuwa wajawazito,au pengine pale mtu anapopata ajali au kulazwa,na kwa nadra pale zinapojitokeza safari za kwenda nje ya nchi.Hapa simlaumu mtu bali najaribu tu kuonyesha namna ambavyo takwimu za magonjwa zinavyoweza kuwa rahisi au ngumu kuzikusanya ukilinganisha nchi kama Uingereza na Tanzania.Inamaanisha kuwa ni vigumu kwa namna flani kutambua afya za kwa wale wenye “miili ya chuma” ambao hawajakanyaga hospitali kwa miaka kadhaa.

Tukiachana na mambo ya takwimu hebu tuangalie namna ambavyo jamii inaweza kupambana na janga hili.Ni ukweli mchungu lakini usiopingika kwamba ngono holela inachangia sana kuenea kwa UKIMWI.Katika hili,kila mtu ana ngao ya kujilinda.Kwa wenzetu mliojaliwa kuwa ndani ya ndoa ni suala la lazima na si hiari kuwa mnapaswa kuwa waadilifu kwa wenza wenu.Upo msemo mmoja wa “kizushi” kwamba kuwa ndani ya ndoa ni kama kuwa gerezani:walio ndani wanatamani uhuru uliopo nje na walio nje wana kiu ya kujua yanayotokea ndani.Mwanandoa,asikudanganye mtu.Katika zama hizi za UKIMWI kuwa ndani ya ndoa ni baraka na kama wanandoa wakizingatia maadili ya taasisi hiyo tukufu basi kupata ugonjwa huo kwao inaweza kuwa ni mkosi tu usiotarajiwa au kuepukika (kwa mfano pale kwa bahati mbaya mtu anapoambukizwa kwa kuchomwa sindano yenye virusi).Naamini kuwa hadi kufikia uamuzi wa kuoa au kuolewa basi wahusika wanakuwa “wamesharidhika” au “kutosheka” na pilikapilika za ubachela.Kwa mantiki hiyo,kutoka nje ya ndoa ni kujitafutia balaa tu.Kwa wale ambao imani zao zinawaruhusu kuwa na mke zaidi ya mmoja basi ni bora kuongeza mke mwingine kuliko kujaribu habari za nyumba ndogo.Ni hatari isiyo salama na ukiukwaa huko kwenye nyumba ndogo ujue unaleta balaa kwenye familia yako.

Halafu kuna haya mambo ambayo watoto wa mjini wanayaita “kumtega mtu.”Utamkuta binti ambaye anajua kabisa kuwa hata akivaa nguo ya heshima bado maumbile yake yanaweza kupeleka mbio mapigo ya moyo ya mwanaume rijali.Lakini kama hiyo haitoshi anatoka na kimini ambacho akiinama tu inakuwa hadithi nyingine.Au bonge la “mpasuo” ambao upepo ukivuma kidogo tu basi mambo yote yanakuwa hadharani.Jamani,sio kama mie ni mpinzani wa “fasheni” au kwenda na wakati lakini hayo mnayoyaona kwenye Isidingo yanaweza kuzusha balaa.Na ukienda huko kwenye kumbi za starehe ndio balaa kubwa zaidi.Sidhani kama itakuwa ni kosa nikitaja maeneo flani ambayo niliyashuhudia mwenyewe nilipokuwa huko nyumbani.Ule mduara pale kona za Morocco unataka mtu mwenye moyo,vinginevyo mtu anaweza kujilaumu kwanini alioa mapema.Viuno vinavyokatwa hapo ni zaidi ya ile ya uchezaji wa kawaida bali ni sawa na kumwaga radhi,yaani ni mambo yanayopaswa kufanywa kwenye faragha na si hadharani.Na ukienda kwenye mambo ya mipasho sehemu flani pale Magomeni ndio hatari ya balaa.Ukisikia wanasema mwanamke nyonga basi eh…kazi ipo!Na kama hujaskia “mugongo mugongo” maana yake nini basi waulize walioushuhudia wakwambie yanayotukia huko.Sawa,ni mambo ya starehe,au “kujirusha” kama wanavyosema wenyewe,lakini ukichanganya na bia mbili tatu kichwani,si ajabu mtu akajikuta anaamkia mtaa ambao haufahamu hata jina lake.

Kuna msemo kwamba kila mmoja wetu ni mwathirika wa UKIMWI.Usitake kurusha ngumi hapo kama majuzi umepima na kujikuta safi.Nachomaanisha ni kwamba takribani kila mmoja wetu ameshashiriki kuuguza au kumzika mwenzetu aliyekuwa na ugonjwa huo.Kama si baba basi ni mama,kama si dada basi ni kaka,kama si mke basi ni mume,jirani yako,mfanyakazi mwenzio au Mtanzania mwenzako.Tusichoke “kufungana breki” pale tunapoona mienendo ya wenzetu inawaweka wao au wenzao katika hatari ya kuambukizwa ugonjwa huo.Vita dhidi ya ugonjwa huu ni jukumu la kila mmoja wetu.Viongozi wa dini wana sehemu ya pekee kwa vile dini zote zinakemea zinaa.Tukumbuke kuwa kati ya takribani watu milioni 39.5 walio na UKIMWI duniani kote,milioni 4.3 waliambukizwa mwaka jana pekee.Hatujui mwaka huu ni wangapi.Mimi,wewe na yeye tunaweza kuleta tofauti kwa KUWAJIBIKA kama unavyotutaka ujumbe wa Siku ya Ukimwi mwaka huu.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.