17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-40

Asalam aleykum,

Kesho nchi yetu inatimiza miaka 45 tangu ipate uhuru.Kwangu,itakuwa ni zaidi ya sherehe ya uhuru.Kesho ni siku yangu ya kuzaliwa.Natimiza miaka 35.Natanguliza asante zangu kwa wale wote watakaonipa “hepi bethdei ” na kwa wenye husda “watalijua jiji.”Kwa namna flani ni kama nimebahatika “kushea” siku moja ya kuzaliwa na nchi yangu.Siku maalumu kama hiyo hutumika kuangalia wapi umetoka,wapi ulipo na wapi unaelekea.Kadhalika,wakati unasherehekea bethdei ni vema kuangalia malengo ulojiwekea wakati wa bethdei zilizopita,na kama umefanikiwa kuyatimiza au la.Kwa lugha nyingine,huo ni wakati mwafaka wa kuangalia mafanikio na kutokufanikiwa.

Kwa upande wangu,niliwahi kujiwekea malengo flani siku za nyuma.Kubwa zaidi ilikuwa suala la elimu.Ngoja nikupe mchapo mmoja wa “mwaka 47”.Nilipokuwa shule ya sekondari kule Ifakara,mwalimu wangu mmoja alizowea kuniita “Dokta” Chahali.Sasa unajua kitu kikiwa kinaendela kila siku unatokea kukizowea.Na ndivyo ilivyokuwa kwangu.Taratibu nikajikuta natamani huo u-Dokta usiwe jambo la utani bali kiwe kitu cha kweli.Mungu si Athumani,panapo majaliwa ndani ya kipindi hiki cha miaka 35 (yaani kabla ya bethdei ijayo) ndoto yangu hiyo ya utotoni itatimia.Nikiangalia nyuma natambua kuwa Mungu amenibariki kwa kuniwezesha kuruka vihunzi kadhaa nilivyokutana navyo hadi kufikia hapa nilipo.Lakini siku zote kuna mambo makuu matatu ndio ambayo naamini yamenifikisha hapa nilipo.La kwanza ni imani kwa Mungu.Japo mahudhurio yangu kwenye nyumba za ibada sio mazuri,lakini imani yangu ya kidini ni kubwa sana.Na pengine ni kubwa zaidi ya wale ambao mahudhurio yao kanisani ni ya daraja la kwanza.Enewei,siko hapa kuhukumu mtu,hasa kwa vile Maandiko Matakatifu yanatamka bayana kwamba “ukihukumu nawe utahukumiwa.”Kwa namna flani huwa najiskia kama sijamtendea haki Mola wangu.Hapo ngoja nikupe mchapo mwingine.Nilipomaliza elimu ya msingi huko Ifakara,nilichaguliwa kujiunga na seminari ya Kasita iliyopo Mahenge.Tulichaguliwa watu wane kati ya vijana kama 30 hivi.Naskia wenzangu wameshakuwa mapadre wazoefu hivi sasa.Mie nikaamua kujiunga na sekondari ya serikali baada ya kufaulu (matokeo ya kujiunga seminari yalitangulia yale ya mtihani wa Taifa wa darasa la saba).Nikiri kwamba uamuzi wangu ulikuwa kinyume na matakwa ya wazazi wangu.Labda nachoweza kujitetea ni kwamba huenda sikuwa na “wito” (kitu kinachomsukuma mtu kuwa padre,bruda au sista).Hata hivyo,mdogo wangu anayenifuatia alifanikiwa kutimiza wito huo ambapo sasa ni mtawa.Na licha ya kutobahatika kufaulu mtihani wa darasa la saba,Kanisa limemsomesha na sasa yuko mwaka wa pili pale chuo kikuu cha Mzumbe.Angalau Sista Chahali ameniondolea ile dhambi yangu ya kukwepa upadre.

Kitu cha pili ambacho naamini kimeniongoza vema ni “Miungu wangu wa hapa duniani.”Hapa nawazungumzia wazazi wangu.Hawa wamekuwa ni watu muhimu kabisa katika maisha yangu.Japo niliwavunja moyo kwa kutojiunga na seminari wameendelea kunisapoti katika kila nilalofanya.Kizuri zaidi ni kwamba wao ni watu walioshika sana ibada.Na kila mara napoongea nao hunifanyia maombi na kunitakia baraka.Na kesho natapoongea nao watarejea tendo wanalonifanyia kila mwaka siku ya bethdei yangu:kuniimbia kwa sauti ya kwaya ule wimbo wa “hepi bethdei tu yu.”Kwenye mafundisho ya dini nayoamini mie tunaambiwa “wapende baba na mama upate heri na maisha marefu duniani.”Nami naamini kuwa upendo wangu na heshima kwao imekuwa chachu ya kunifikisha hapa nilipo.

Kitu cha tatu ni kazi au masomo.Nimeshawahi kufanya kazi hapa na pale kabla ya kuja huku kwa masomo.Kwa hakika nathamini sana ajira hasa ikizingatiwa kuwa kwa nchi zatu za dunia ya tatu ajira ni suala la bahati zaidi kuliko taaluma aliyonayo mtu.Na ukiwa unatoka familia masikini basi kazi yako ndio inakuwa kila kitu.Na hata kama unatoka ukoo “unaojiweza” basi ni sharti uelewe kuwa ajira yako ndiyo inakufanya uitwe flani hivi leo.Na kwa sasa niko masomoni basi shule ndio kila kitu kwangu.Naithamini,nainyenyekea na kuipenda.Namshukuru Mungu kwamba sijawahi kukutana na kitu kinachoitwa kufeli katika muda wote huu wa miaka 35 tangu nizaliwe lakini pamoja na Baraka za Mungu,mie mwenyewe nimekuwa “Joni Kisomo” flani linapokuja suala la kitabu.Kwa wasiojua,Joni Kisomo ni mtu mpenda shule,na kinyume chake ni “kilaza” kwa lugha za pale Mlimani.

Kwa hiyo,wakati kesho natimiza miaka 35,mwongozo wangu umekuwa ni Mungu,wazazi na kazi/shule.Kwa “mwana-bethdei mwenzangu” Tanzania,naamini nae ana yake mengi ya kusema kuhusu miaka 45 yake tangu “azaliwe.”Sawa,kuna matatizo kadhaa katika nchi yetu hivi sasa lakini matatizo hayo hayapaswi kufunika mafanikio ya muhimu yaliyofikiwa katika kipindi chote hiki.Ukiangalia hali ilivyo kwa majirani zetu utafahamu bayana kuwa sie tuna bahati sana.Na hapa naizungumzia AMANI. “Ofkoz” wanafalsafa wa masuala ya amani na migogoro wanadai kuwa amani sio tu ukosefu wa vurugu,mikwaruzano au songombingo,lakini katika hali halisi kama unaweza kutembea kutoka Boko hadi Kigilagila bila kuhofia kukwatwa na sime basi hiyo ni amani.Ukitaka kujua nini maana ya amani basi angalia kinachotokea Iraki,Afghanistan,Somalia,Sudan na kwingineko halafu utajua kuwa wanachozunguzia wanafalsafa wa amani ni vitu vya kitaaluma zaidi kuliko vya hali halisi ya mtaani.Na siku zote,wenye busara zao hutenganisha matamshi ya kitaaluma na uhalisia uliopo tunakoishi.Jamani, yote tunaweza kuyafanyia mzaha lakini sio amani.Hiyo ni lulu ambayo wenzetu wengine wanakesha wakiomba iwarejee lakini hawaipati.Amani ni kama hadhi.Inachukua miaka lukuki kuijenga lakini inaweza kuporomoka katika muda mfupi tu.Kwa mantiki hiyo,mamlaka husika zinapaswa “kuwakomalia” wale wote wanaotaka kuichezea amani yetu.

Wakati Tanzania anatimiza miaka 45 ya kuzaliwa kwake,sina budi kumtaja Rais Jakaya.Inawezekana kabisa kuwa sherehe hizi za uhuru zikawakuta watu flani wakiwa wamenuna,wamekata tamaa wana hasira “kibwena” (nyingi).Mimi naamini kuwa Tanzania imempata mrithi wa Mwalimu,naye si mwingine bali ni Jakaya.Sura inaeleza mengi,na ukiangalia sura ya Jakaya utagundua kuwa sio tu “hendsam” flani bali ni mtu mwenye imani flani katika anayofanya.Tangu wakati wa kampeni alionyesha kuwa anafahamu matatizo ya Watanzania na ana nia ya kuwakomboa.Naomba tuelewe kwamba kazi hiyo sio nyepesi,na katika kutekeleza azma hiyo kuna uwezekano wa baadhi ya watu kuhisi kwamba huko mbele kuna giza.Wanafalsafa wa maisha wanasema “kujua tatizo ndio hatua ya kwanza ya kulitatua.”JK amebainisha bayana kuwa anajua matatizo ya Bongo, na sio kuyajua tu bali amedhamiria kuyaondoa.Ninaposikiliza kauli zake naendelea kuamini kuwa ipo siku kauli yake ya “Maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana” itatimia.Na kinachomrahisishia JK kutimiza azma yake ni ukweli kwamba Taifa hili linalotimiza miaka 45 hapo kesho liko naye katika jitihada zake za kuliboresha.Kama Ustaadh wangu mmoja aitwaye Nzowa alivyokuwa akinichagiza kwa nukuu kutoka katika Kuran Tukufu kwamba “Innalahu Maswabirina” (sijui inaandikwa hivyo,lakini inamaanisha kuwa kila mwenye subra yuko na mwenyezi Mungu) naamini subira inahitajika ili kufikia “maisha abora kwa kila Mtanzania,”

Hepi bethdei Tanzania.
Kwa makala zilizopita,tembelea http://chahali.blogspot.com na http://chahali.livejournal.com

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.