17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI-41

Asalam aleykum,

Leo nawaletea habari mbalimbali zilizotawala kwenye anga hizi.Kwanza nianze na uzinduzi wa matangazo kwa lugha ya kiingereza ya kituo cha televisheni cha Aljaazera.Japo huduma hiyo imeanza hivi majuzi tu lakini tayari imeonekana kuwavutia watu wengi wanaofuatilia habari za kimataifa.Miongoni mwa “hobi” zangu ni kuangalia runinga na vipindi navyopendelea zaidi ni vya habari.Na nilikuwa na kiu kubwa ya kujua kitachotokea baada ya kupata habari kwamba Aljaazera wataanzisha huduma ya matangazo kwa lugha ya kiingereza.Wenyewe wanasema kwamba George W Bush au Osama bin Laden wote ni watu muhimu na ulimwengu una kiu ya kusikia wanayosema.Ikumbukwe kwamba kituo hiki kimekuwa mwiba mchungu kwa Marekani katika kinachoitwa vita dhidi ya ugaidi hasa kwa vile kimeonekana kuwa kama kipaza sauti cha watu au vikundi ambavyo pengine “waamuzi wa sera za dunia” wasingependa kuona watu kama Osama bin Laden wanapewa uwanja wa kutoa kauli zao.Lakini baada ya takriban wiki mbili za kufuatilia matangazo ya Aljaazera English nashawishika kusema kwamba kituo hicho kinaweza kabisa kuwa bora zaidi katika fani ya habari za kimataifa.Na inaelekea walijiandaa vilivyo kabla ya kuanza huduma hiyo.Katika timu yao ya habari wana “vichwa” maarufu kama vile Sir David Frost,ambaye “goli” lake la kwanza lilikuwa kum-bana Tony Blair katika mahojiano hadi Blair akajikuta anakiri kuwa uvamizi dhidi ya Irak umekwenda harijojo.Pia wana gwiji la mahojiano Riz Khan ambaye wengi mtakumbuka katika enzi zake akiwa CCN.Pamoja na hao ni Mike Hanna aliyekuwa CNN na Ragi Omari,mtangazaji aliyewafanya watazamaji wa runinga hasa wale wa BBC waione vita ya Irak kama inatokea “live” ndani ya nyumba zao.Niliangalia kipindi kimoja kuhusu mauaji ya halaiki yaliyotokea huko Rwanda na kwa hakika nilipata picha kwamba Aljaazera wamedhamiria kwa dhati kutuletea habari kwa namna ambayo mtazamaji unaridhika.

Kingine ni mauaji yanayoelekea kuendelea ya makahaba katika mji wa Ipswich,hapa Uingereza.Hadi wakati naandaa makala hii tayari makahaba watano wameshauawa na haijafahamika muuaji ni nani.Matukio haya yanaanza kulinganishwa na yale yaliyotokea miaka ya 1880 yaliyomhusisha mtu aliyeitwa Jack the Ripper ambaye kama huyu wa Ipwich,walengwa wake wakubwa walikuwa makahaba.Tofauti kati ya mauaji hayo ya zamani na haya ya sasa ni kwamba wakati maiti za wahanga wa Jack the Ripper zilikutwa zikiwa zimecharangwa vibaya vibaya,maiti tano zilizopatikana hadi sasa zimekutwa zikiwa hazijachrangwa japo zote zimekutwa zikiwa uchi.Vyombo vya usalama vinaendela kumsaka muuaji na haijulikani lini atakamatwa na iwapo mauaji yataendelea au la.Polisi wameshawatahadharisha makahaba kwamba kuwa wanapokwenda kwenye mawindo yao wafahamu kuwa wanahatarisha maisha yao.Lakini kahaba mmoja aliyehojiwa kwenye runinga alinukuliwa akisema kuwa japo wao wanatambua hatari inayowakabili hawana jinsi nyingine hasa kwa vile nao wanahitaji fedha hasa kwa msimu huu wa sikukuu ya Krismasi.

Jingine lililotawala kwenye televisheni zetu ni kifo cha shushushu wa zamani wa shirika la ujasusi la Rusia (KGB),Alexander Litvinenko.Jasusi huyo aliyepewa hifadhi ya kisiasa na serikali ya Uingereza alifariki baada ya kuwekewa sumu iitwayo “Polonium-210” ambapo inadhaniwa iliwekwa kwenye chakula au kinywaji siku alipokutana na mtoa habari wake Mario Scalamella kutoka Italia kwenye mgahawa wa sushi jijini London.Baada ya kufahamika kuwa aliuawa kwa sumu hiyo,mamlaka za afya za Uingereza zikatoa wito kwa watu wote wanaohisi kuwa walikuwa kwenye mgahawa huo waende kupima afya zao kujua kama nao wamedhurika au la.Hadi sasa tayari watu kadhaa wameshapimwa na kugundulika kuwa wamedhurika na sumu hiyo japo ni kwa kiwango kidogo ambacho pengine hakiwezi kuua.Hadi sasa chembechembe za sumu hiyo zimeshakutwa kwenye baadhi ya ndege zinazofanya safari kati ya Urusi na Uingereza,na pia zimepatikana huko Italia anakotoka Scaramella na Humburg huko Ujerumani.Mke wa Litvinenko nae amepimwa na kukutwa amedhuriaka na sumu hiyo.Vilevile,baadhi polisi wa upelelezi waliokuwa wakichunguza kifo hicho nao wamepimwa na kukutwa wameathirika.

Maafisa wa Scotland Yard wamekuwa jijini Moscow kuendeleza uchunguzi wao na hivi punde shirika la polisi la kimataifa (Interpol) nalo limeingilia kati uchunguzi huo.Majuzi,Balozi wa Uingereza nchini Urusi alilalamika kuwa amekuwa akibughudhiwa na kikundi cha vijana wenye mrengo mkali wa kitaifa kiitwacho Nashi,na amehusisha suala la Litvinenko na kukua kwa kadhia hiyo.Hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo lakini tayari bodigadi wa zamani wa KGB Andrei Lugoyov,ambaye alikutana na Litvinenko siku aliyoanza kujisikia vibaya na hatimaye kulazwa na kufariki,amekuwa akidhaniwa kuwa anaweza kuwa na ufunguo wa kutatua kitendawili hiki ambacho sasa kimechukua taswira ya kimataifa.

Litvinenko alikuwa mpinzani mkali wa siasa za Rais Putin wa Urusi na inasemekana Scaramela alikutana nae kumpatia orodha ya watu wanaotakiwa kuuawa (hit list) ambapo inadaiwa jina lake (shushushu huyo ) lilikuwamo kwenye orodha hiyo.Juzi kituo cha televisheni cha CCN kilieleza jinsi gani vikundi vya mauaji vilivyotapakaa nchini Urusi na kuyaweka hatarini maisha ya wale wanaokosoa sera za serikali hiyo.Hata hivyo,kuna hisia pia kwamba inawezekana kifo cha shushushu huyo wa zamani ni kazi ya maswahiba zake wa zamani ndani ya KGB ambao pengine hawakupendezwa na mwenendo wake,hasa mahusiano yake na vikundi vya upinzani huko Chechnya.Kadhalika zipo hisia kuwa kifo hicho kinaweza kuwa kimeandaliwa na wapinzani wa Rais Putin ambao wanaotaka kumchafulia rekodi yake wakati nchi hiyo inajiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao.Maswali ni mengi kuliko majibu,na kwenye maswali magumu sio busara kutoa majibu rahisi.

Mwisho,nimesoma kwenye magazeti ya huko nyumbani kuhusu mchezo wa kutupiana lawama (blame game) unaoendela kati ya TANESCO na Kampuni ya Richmond ambao ulianza baada ya Richmond kuishutumu TANESCO kuwa inakwamisha jitihada za Richmond kuingiza megawati zake kwenye gridi ya Taifa kwa vile “TANESCO waliipatia kampeni hiyo gesi chafu.”Wakati nawaachia wataalamu wa fizikia kutueleza nini kazi ya “filter” kwenye mtambo mpya,wito wangu kwa Richmond na TANESCO ni kwamba blame game hiyo haiwasaidii Watanzania kuondokana na adha ya mgao wa umeme.Jamani,hivi kama megawati 22 zinachukua muda wote huu,je hizo 80 ambazo hata mitambo yake haijawasili zitachukua muda gani?Hapa nilipo siathiriwi moja kwa moja (directly) na mgao huo na pengine naweza kuonekana kama kimbelembele flani lakini ikumbukwe kuwa nami ni Mtanzania,wazazi wangu,ndugu,marafiki na jamaa zangu na walipa kodi wenzangu wanaathiriwa mno na sakata hili la umeme.Kadhalika,uchumi wetu ambao tunahangaika kuuboresha nao unakwamishwa sana.Tupatieni zawadi ya miaka 45 ya uhuru kwa kusitisha hii tamthiliya isiyoisha na kutuletea umeme.Naamini mkiamua kwa dhati kutafsiri falsafa ya kasi mpya,ari mpya na nguvu mpya kwa vitendo,ni dhahiri tatizo hili litakwisha kabisa.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.