17 Jan 2007

KULIKONI UGHAIBUNI


Asalam aleykum,

Nadhani pilika za Krismasi zimekwisha salama.Sasa tunausubiria mwaka mpya ambao tutauanza Jumatatu ijayo.Makala yangu ya leo inaambatana na salamu zangu za mwaka mpya lakini kwa mtazamo wangu binafsi.Kwanza naomba niseme mie naweza kuitwa mhafidhina linapokuja suala la sikukuu.Jinsi navyoziadhimisha baadhi ya sikukuu inaweza kabisa kuonekana kama ni dharau kwa siku hizo.Hapana,sio dharau bali kwa mtizamo wangu nadhani ndio namna sahihi ya kuziadhimisha siku hizo.Ni hivi,kweli ni sahihi kwa mtu kusherehekea siku yake ya kuzaliwa na pengine kutumia kipato chake cha ngama kuangusha bonge la pati kwa kutimiza miaka kadhaa.Lakini mashamsham hayo yatakuwa na maana gani iwapo huyo mwenye kushereheka hana hata wazo moja kuhusu kinachomsubiri katika mwaka unaofuatia?Yaani mtu alipotimiza miaka 25 alijipangia malengo flani na bethdei ilofatia akajipangia malengo mengine,lakini hadi anasherehekea kutimiza miaka 30 bado anaendelea kujipangia malengo tu bila kutekeleza.Katika hali hiyo binafsi sioni umuhimu wa kusherehekea kubadilika kwa namba ya umri ilhali hakuna la maana lililofikiwa.

Katika mtizamo huohuo huwa najikuta nawashangaa wale jamaa zangu ambao akili zinawaruka kila unapofika mwaka mpya.Sawa,kumaliza mwaka ni jambo kubwa lakini ukweli unabaki kwamba kinachobadilika ni namba tu kwenye kalenda na kama mtu hajapanga karata zake vizuri basi mwaka mpya hauwezi kuja na jipya lolote.Kupiga madebe na kuwanyima watu usingizi inapotimu saa sita usiku sambamba na kuchoma matairi (huu ni uchafuzi wa mazingira tu) ni mambo ambayo yanaweza kuwa sehemu ya furaha za kumaliza mwaka mmoja na kuingia mwaka mwingine lakini pasipo kupangilia mambo vizuri hayo makelele na moshi wa matairi haviwezi kubadilisha kitu.Kwa hawa wenzetu huku,mwaka mpya huwa unaambatana na kitu wanachokiita “new year resolution(s)” yaani lengo au malengo kwa mwaka ujao.Sambamba na hilo ni kupitia kwa makini nini kilikwenda mrama katika mwaka uliopita na nini kifanyike katika mwaka ujao.

Katika miaka ya hivi karibuni mie nimekuwa nikiukaribisha mwaka mpya kwa namna mbili.Kwanza huwa nafuatilia kwenye runinga jinsi gani mwaka mpya unavyowasili katika miji mbalimbali duniani.Kwa hapa Uingereza mara nyingi runinga “hugawanywa” sehemu nne na kuonyesha “laivu jinsi gani unavyokaribishwa katika “miji mikuu” ya “mataifa” yanayounda Uingereza,yaani London (England),Cardiff (Wales),Edinburgh (Scotland) na Belfast (Ireland ya Kaskazini).Baada ya hapo runinga zinaelekezwa kamera zao kwenye miji mingine ya hapa na sehemu nyingine duniani.Baada ya kumaliza kuangalia jinsi miji inavyokaribisha mwaka mpya huwa nahamia kwenye hatua ya pili,nayo ni kufanya sala.Huwa namshukuru Mungu kwa yote alonijaalia mwaka ulopita na kumwombea anijalie tena kwa mwaka ujao.

Hivi tunaonaje kama mwaka mpya ukiadhimishwa kwa kufanya sala na dua dhidi ya wezi,majambazi,matapeli na wala rushwa wanaofanya maisha yetu kila mwaka kuwa magumu zaidi ya miaka ilotangulia?Hii inaweza kuleta mabadiliko flani hasa ikizingatiwa kuwa wahalifu hao (yes,hata wala rushwa ni wahalifu) huwa tunajichanganya nao katika sherehe kama hizo.Nitamke bayana kwamba kila siku chuki yangu inazidi kukua dhidi ya watu ambao hawana uchungu na maisha ya wenzao.Sio kama napandikiza mbegu za chuki bali sote tunahitaji maisha bora,na sote tunatambua kuwa maisha bora sio zawadi ya wateule wachache.Kwa mantiki hiyo,katika sala zangu za mwaka mpya nitawajumuisha hawa majambazi wanaotafuna nchi yetu bila chembe ya huruma.Sintawajumuisha kuwaombea mema bali sanasana kwa kuzingatia maadili ya kidini ntawaombea wapate moyo wa huruma dhidi ya hao wanaowatesa.Katika dini nayofuata mie tunaambiwa kuwa tuwapende maadui zetu.Hiyo kidogo huwa inakuwa ngumu linapokuja suala la watu kama wala rushwa.Kadri tunavyozidi kuwapenda ndio kadri wanavyoneemesha vitambi vyao,wanavyozidi kuongeza nyumba ndogo na wanavyozidisha dharau kwa watu walewale wanaowaibia.Najua zipo dini ambazo mtu akifanya makosa anaombewa dua ya laana,na nadhani katika mazingira tuliyonayo wahalifu kama wala rushwa wanastahili dua za laana.Niite jina lolote unaloona linafaa lakini naamini kuwa hawa majambazi wa haki na raha zetu hawastahili kuingia mwaka mpya wakiwa na akili hizohizo za kuendeleza maovu yao dhidi yetu.

Kwenye mafundisho ya Kikristo,ndani ya Agano la Kale kulikuwa na sheria tunazoweza kuziita “za kisasi” (laws of retaliation) kwa mfano “jicho kwa jicho” na “jino kwa jino”.Kwenye Agano Jipya kuna sheria tunazoweza kuziita za “mapatano” (laws of reconciliation) na humo ndio tunaambiwa mtu akikupiga kofi shavu la kushoto basi mgeuzie na la kulia.Tunasisistizwa kuwapenda maadui zetu.Ila nadhani kwa watu kama wala rushwa,sheria zinazowafaa ni zile za kisasi kwa sababu kimsingi rushwa ni kama ugonjwa wa kubwia unga,kadri mtu wanavyozidi kuiba ndio kadri anavyozidi kubobea,anakuwa “teja la rushwa”.Kibaya zaidi ni kwamba rushwa inazaa rushwa zaidi.Yaani kwa mfano mtu anapoingia ofisini akiwa na roho safi anaweza kujikuta anashawishika kuingia kwenye “madili” haramu pale anapobaini kuwa katika ofisi hiyo watu hawaishi kwa kutegemea mishahara.Halafu jamii yetu nayo kuna wakati inalea mawazo ambayo kimsingi yanawashawishi watu kuwa wezi zaidi.Yaani kwa mfano mhasibu wa sehemu “yenye ulaji” akiwa anaishi maisha ya kawaida utawaskia watu wanamsema pembeni kuwa “ahh huyu jamaa anaishi kama mesenja wakati ndio anashughulikia hela za kampuni?”Na si ajabu kuona wala rushwa wakisifiwa mtaani kwamba “usifanye mchezo bwana,flani ana hekalu si la mchezo kule sehemu flani.”

Najua wala rushwa watakuwa wamenuna sana kwa salamu nazowapatia kwa mwaka mpya,na pengine baada ya kusoma “paragrafu” chache za mwanzo kwenye makala hii wameashaamua kulitupa gazeti hili.Enewei,ujumbe umefika,mwenye kuchukia achukie lakini ukweli ushasemwa.Katika lugha nyepesi,majambazi hawa wanaombwa kusherehekea mwaka mpya kwa kupata moyo wa huruma.Wakati wananenepesha matumbo yao wajaribu pia kufikiria vile “vitambi” vya utapiamlo vinavyowakabili watoto wetu lukuki huko mitaani.Wakumbuke pia kuwa fedha wanazowahonga mahawara zao zinaweza kuwa ni ada wanayolipia vifo vyao kwa ukimwi au magonjwa ya zinaa (wanapaswa kufahamu kuwa huko kwenye nyumba ndogo huwa wanaitwa “darling” lakini wakiondoka tu majina yao yanagezwa kuwa “mabuzi” au “ATM”…zamani walikuwa wanaitwa “wageni kutoka Vingunguti”).Unajua nachofanya hapa ni kuwapandisha hasira kwa matarajio kwamba wanaweza kubadilika.Naanzisha “moral crusade” (mapambano ya kiroho) dhidi ya wahalifu na walengwa wangu wakubwa ni wala rushwa.

Enewei,baada ya salamu hizo kwa wahalifu basi sina budi kuwatakia heri na Baraka ya mwaka mpya wasomaji wapendwa wa gazeti hili na wale waumini wa safu hii.Pia salamu zangu nazielekeza kwa raia wema wote bila kusahau wale ambao wakati tunalala usiku wao wako bize kuhakikisha kuwa angalau tunaamka salama.Mungu awazidishie baraka kwa jitihada zao na awaongezee moyo wa ujasiri.Hapa nimtakie mwaka mpya mwema jemedari wetu Kikwete nikiamini kuwa Mwenyezi Mungu atamzidishia kila la heri katika azma yake ya kuleta Maisha Bora kwa Kila Mtanzania.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.