27 Aug 2007

Asalam aleykum,


Kuna habari flani nimeiona gazetini imeniacha nakenua meno kwa kicheko.Kwa mujibu wa gazeti moja la Daily Mail la hapa Uingereza eti inadaiwa kwamba wanawake warefu “wanawazimia sana” wanaume wafupi.Kilichopelekea madai hayo ni maswali wanayojiuliza wafuatiliaji wa mambo ya watu (wambeya?) eti kwanini mwanamitindo wa kimataifa Sophia Dahl “amekolea” kwa mwanamuziki “andunje” wa midundo ya jazz,Jamie Callum.Gazeti hilo linadai kwamba wanaume wafupi huwa wanafanya jitihada sana kuhakikisha kuwa wanafidia “pengo” la urefu wao kwa kujituma kwenye maeneo mengine.Hoja nyingine ya kuchekesha ni ile inayodai kuwa watu wafupi ni “vipotabo” kwa wanawake warefu,na hata wakialikwa kwenye nyumba za watu warefu basi ni rahisi kwa “masoti chesisi” hao kufiti kwenye makochi pasipo kulalamika kuwa miguu inauma iwapo kochi lenyewe ni la kujibana.Sijui habari hiyo inawahusu wanaume wafupi wa nchi za Magharibi pekee au dunia nzima lakini lililo wazi ni kwamba suala la mwanamke kumzimia mwanaume au mwanaume kumzimia mwanamke ni la mtu binafsi,na ufupi,urefu,wembamba au unene sio kigezo muhimu sana japo sote tunafahamu kwamba wengi wetu tuna “mapendezeo” yetu.


Wiki iliyopita nilipata nafasi ya kushuhudia mchezo wa kirafiki wa soka kati ya timu ya taifa ya Scotland dhidi ya ile ya Afrika Kusini (Bafana Bafana),mechi iliyofanyika kwenye uwanja wa Pittodrie hapa Aberdeen.Ilipendeza kuona Waafrika wachache wanaoishi hapa wakiwa wametinga jezi za Bafana kuonyesha sapoti yao kwa timu hiyo.Japo mechi hiyo iliisha kwa Scotland kuibuka na ushindi kiduchu wa bao moja kwa bila, “sie” tuliofungwa (Waafrika wote siku hiyo tuligeuka kuwa Wasauzi) tulifarijika kuiona timu ya “nyumbani” ikitandaza kabumbu la kuvutia.Unajua mara nyingi hawa watu weupe wanakupa heshima pale utapowaonyesha una uwezo sawa nao au pengine zaidi yao.

Na wikiendi nilipata fursa ya kuangalia (kwenye runinga) michuano ya kimataifa ya riadha kutoka huko Osaka,Japan.Kama kawaida,Waethiopia na Wakenya wametesa vilivyo.Nimesoma kwenye magazeti yahuko nyumbani kuwa nasi tunawakilishwa na wanariadha kadhaa.Sijui tutaambulia chochote au itaendelea kuwa hadithi ile ile ya kuwa wasindikizaji wa kudumu.Lakini naamini kwamba kama Wakenya na Waethiopia wanaweza kutawala kwenye anga hizo,basi nasi pia tunaweza kabisa kufanya vizuri.Ni lini tutapata akina Filbert Bayi na Suleiman Nyambui wengine?Upeo wangu mdogo wa Jiografia unanishawishi kuamini kwamba hali ya hewa ya mkoa kama Arusha unatupatia mazingira mazuri ya kuzalisha wanariadha ya viwango vya kimataifa.Na ushahidi upo kwa kuangalia “perfomance” ya baadhi ya mashujaa wetu wa miaka ya nyuma.Penye nia pana njia,na kama tutawekeza vya kutosha basi kwa hakika tutaweza kurejesha historia ambayo kwa sasa imeshaanza kusahaulika.

Kuna dalili za mafanikio huko mbele ya safari kwenye soka letu. “Uchawi wa Kibrazil” wa Maximo na mwenzie Tinoco unaelekea kuzaa matunda.Ukichanganya na sapoti ya kutosha kutoka kwa JK mwenyewe basi si ajabu nasi tukajikuta tunaingia kwenye ramani ya soka ulimwenguni.Kinachonipa shaka ni matatizo ya uongozi kwenye vilabu vyetu vya soka.Maana kila kukicha utasikia wanachama Simba wanataka kupindua uongozi,au wenzao wa Yanga wanamkalia kooni kiongozi flani,au mara usikie kocha flani kabwaga manyanga kwa vile hajalipwa stahili zake,na vioja vingine visivyo na mwisho.Katika makala yangu iliyopita niliwausia viongozi wa Simba kutumia vizuri mkataba walioingia na kampuni moja kupromoti “chata” ya Adidas.Hee!haujapita muda mrefu nasikia baadhi ya wanachama wanapania kuung’oa uongozi ulio madarakani.Na hapohapo nasikia kocha Twalib Hilal anasema anarejea umangani kwa vile hajakamilishiwa malipo yake.Kiongozi mmoja anang’aka jukumu la kumlipa kocha huyo kwa kudai kwamba aliletwa na Friends of Simba.Ok,tuseme kuwa mapenzi ya Friends of Simba kwa klabu yao yaliwasukuma kumtafuta kocha mwenye uwezo wa kuipeleka mbali klabu ya Simba,na wakamsomesha Twalib hadi akakubali kusamehe mshahara mnono huko Umangani.Sasa,viongozi hawakupaswa kubweteka na kuliacha jukumu la mshahara kwa Frienda of Simba pekee.Kwanza,msaada uliotolewa na kikundi hicho unaweza kutafsiriwa kama msaada kwa uongozi kwani sote tunajua “politiki” za Simba na Yanga:matokeo yakiwa mabaya basi uhai wa viongozi kuwa madarakani unakuwa unaning’inia kwenye utando wa buibui.

Ni kama kichekesho vile kwa sababu miezi michache iliyopita,uongozi huohuo wa Simba uliweka msimamo thabiti dhidi ya kundi la Friends of Simba wakidai kundi hilo linaihujumu klabu hiyo.Navyoelewa mimi ni kwamba kwa vile klabu hiyo inajiendesha “Kiswahili” ni lazima wawepo watu wa kuikwamua kifedha pale inapokwama,na kwa namna mambo yalivyo,kila wakati uchumi wa vilabu vyetu ni wa kusuasua kama suala la amani huko Somalia.Ufumbuzi wa matatizo sio Mapinduzi,kwani yameshafanyika mengi tu na hakuna lolote la msingi lililopatikana.Wala kukimbilia mahakamani sio ufumbuzi wa matatizo.Na kuwa na mahusiano mazuri na vipoba hakuwezi kuwa ufumbuzi wa kudumu wa matatizo ya klabu kama Simba.Ufumbuzi pekee ni kwa vilabu hivyo kujiendesha kibiashara.Soka ni zaidi ya burudani kwani ikiendeshwa kisasa inaweza kuwa chanzo kizuri cha mapato.Unaposikia Manchester United,Chelsea au Liverpool zinavutia wawekezaji kutoka nje ya Uingereza sio kwamba matajiri hao ni wakereketwa sana wa soka (ingekuwa ni ukereketwa basi wangenunua vilabu katika nchi zao) bali wanajua bayana kwamba soka ni biashara yenye faida.

Twanga Pepeta wako ziarani hapa Uingereza,na wametapisha kumbi walizotembelea.Hivi kwa mfano Simba au Yanga wangefanya ziara sehemu mbalimbali duniani wasingeweza kujichumia mapato mkubwa pengine zaidi ya hayo wanayopata Twanga?Na kwa kufanya ziara nje ya nchi vilabu vyetu vingeweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja:kutengeneza mapato ya kutosha na kuitangaza vipaji vya wanasoka wao,ambao wakipata timu huku nje inamaanisha mapato zaidi kwa vilabu hivyo.Najua wapo wanaoniona kama nimechanganyikiwa kwa kutoa mawazo kama haya.Siwalaumu kwani kwa jinsi wanavyofahamu ubabaishaji uliokithiri kwenye vilabu vyetu,hata ziara za mikoani zinahitaji mitulinga ili ziwe na mafanikio.

Mwisho,ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza marais wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuzingatia maoni ya wananchi wao kuhusu suala la kuharakisha Muungano wa nchi hizo.Mimi ni muumini wa hekima ya umoja,yaani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.Lakini umoja kati ya watu wenye “backgrounds” zinazotofautiana unaweza usizae matokeo yanayokusudiwa.Nilisoma sehemu flani ambapo DCI Manumba aliweka bayana kuwa kuongezeka kwa wimbi la ujambazi huko nyumbani kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wanaoingiza nchini pasipo kufuata taratibu za uhamiaji.Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya amani iliyopo Tanzania ni kivutio kizuri kwa “watu wa shari” kutoka nchi jirani.Unadhani hali itakuwaje pindi “washari” hao watakuwa wanaweza kuingia Tanzania kirahisi kama vile mtu anavyotoka Ilala kwenda Temeke hapo Muungano huo utakapokuwa umekamilika.Lakini hoja hiyo ya uhalifu ni ndogo tu ukilinganisha na ukweli kwamba tuna mambo yetu kadhaa ya muhimu tunayopaswa kuyashughulikia kwanza kabla ya kufikiria kujitanua.Na miongoni mwa mambo hayo muhimu ni suala la Muungano kati ya “Tanganyika” na Zanzibar.Halafu kuna hii “lulu” yetu ya amani na utulivu.Najua kila mtu ana tafsiri yake ya neno “amani na utulivu” lakini naamini sote tunakubaliana kuwa hatuwezi kulinganisha nchi yetu na mbinde za Wahutu na Watutsi huko Rwanda na Burundi au tatizo la ukabila huko Kenya (bila kusahau Mungiki).Na yayumkinika kusema kuwa “uwekezaji” wa wenzetu hapo nyumbani ni mkubwa zaidi ya wetu huko kwao.Mazingira yaliyoiua jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki bado yapo,na ni vema yakarekebishwa kabla ya kufikiria wazo la Muungano mpya.

Alamsiki






0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.