12 Jul 2009


Kizitto Noya na Habel Chidawali, Dodoma

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Shamsa Mwangunga, amekiri kukithiri wizi wa nyara za serikali hasa pembe za ndovu na kueleza kuwa sio rahisi kudhibiti vitendo hivyo kwa kuwa vinafanywa na mtandao wa watu wenye fedha nyingi.

Mwangunga alisema hayo bungeni jana alipokuwa akihitimisha mjadala wa bajeti ya wizara yake mjini na kufafanua wizi wa makontena mawili ya pembe za ndovu yaliyokamatwa Machi, mwaka huu nchini Vietnam.

“Kukithiri kwa wizi huo kumetokana na Wizara ya Maliasili na Utalii kutohusishwa na ukaguzi wa mizigo bandarini na soko kubwa la nyara hizo liko katika nchi za Asia. Mtandao wa watu wenye fedha nyingi ndio unaendesha biashara hiyo kwa kushirikiana na maafisa wa bandari,” alisema Mwangunga.

“Ninasema maafisa wa bandari wanahusika kwa sababu bandarini ndiko kwenye lango la kupitisha nyara hizo na maafisa wake ni miongoni mwa watuhumiwa katika matukio hayo.”

Mwangunga alikuwa akijibu hoja ya mbunge wa Same Mashariki Anne Kilango Malecela ambaye juzi alitishia kutoa hoja binafsi kutaka iundwe Kamati teule ya Bunge kuchunguza wizi wa makontena hayo yaliyokamatwa Machi 25, mwaka huu nchini Vietnam.

Mbunge huyo alitaka kamati hiyo ichunguze jinsi makontena hayo yalivyopita kwenye bandari za hapa nchini baada ya kukaguliwa na mamlaka husika na kufika Vietnam bila kujulikana kuwa yalibeba pembe za ndovu.

"Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie kuhusu jambo ambalo kwa kweli limenisikitisha sana ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii ambao ni wizi wa nyara; wizi wa pembe za ndovu. Wizi huu Mheshimiwa Spika, unafanyika kama vile nchi yetu hakuna ulinzi," alilaumu Kilango na kuongeza:

"Nimefanya utafiti nina faili zima; Mheshimiwa Spika nilikwenda kufanya utafiti, baada ya kusoma kwenye magazeti kuhusu makontena mawili yaliyokamatwa Vietnam, nikaona nisiishie hapo niende ndani mpaka nipate faili zima.

"Nasikitika sana. Nilikwenda kuhoji; nikaelezwa; nikapewa na faili; nikasoma kontena zile mbili zilipitia bandari yetu kama kawaida".

Kilango aliomba atumie kanuni ya 117 ya Bunge kuwasilisha hoja binafsi kutaka iundwe kamati teule kwa ajili ya kuchunguza jambo hilo.

Hata hivyo, jana Spika wa Bunge Samuel Sitta ambaye juzi aliahidi kufanyia kazi suala hilo, alitupa hoja hiyo baada ya Kilango kushindwa kuwasilisha kusudio lake hilo kwa maandishi kwa wakati.

”Kulikuwa na hoja ya kuundwa kamati teule jana, lakini niseme kwamba, hoja hiyo sijaipata hapa kwa maandishi, nimwombe Katibu aendelee na shughuli za leo,” alisema Sitta muda mfupi kabla ya bunge kukaa kama kamati.

Kabla ya Sitta kusema hivyo, aliingia bungeni akikimbia akiwa ameshika bahasha ya kaki ambayo ilisemekana kuwa ilikuwa na hoja yake hiyo kimaandishi ambayo alitarajia kuiwasilisha.

”Naona kuna kitu kinataka kunifikia sijui kama ndio hiyo hoja, ah, lakini kwa mujibu wa kanuni za Bunge siwezi kuipokea hoja hiyo na kusema kweli itakuwa ndiyo basi, sitaipokea tena hivyo tunaendelea waheshimiwa,” alisema Sitta.

Akizungumza na gazeti hili katika viwanja vya Bunge jana, Kilango alisema alichelewesha kupeleka hoja yake baada ya awali kushauriwa na Spika kuwa suala hilo liachwe liendelee kushughulikiwa na Polisi wa Interpol chini ya makubaliano ya Lusaka (Lusaka Agreement).

”Mimi hoja nilishaandaa, lakini Spika alinishauri kuwa kwa vile suala hilo linashughulikiwa na Interpol, tuache kwanza.

Lakini hii haina maana kwamba, hoja imekufa. Nitaiibua tena wakati wowote baada ya interpol kumaliza kazi yake,” alisema.

Awali akizungumzia wizi huo Mwangunga alisema ulitokea Machi 25 mwaka huu na tayari watu tisa wamekamatwa na kuhojiwa.

”Kati yao, watu wanne wamefunguliwa kesi mahakamani mkoani Tanga,” alisema Mwangunga na kutaja majina ya watuhumiwa hao.

Alisema mbali na tukio hilo, kontena lingine lilikamatwa Machi Mosi, mwaka huu katika Bandari ya Manila Ufilipino ambako pembe za ndovu zenye uzito wa tani tano lilikamatwa.

Siku nne baadaye maafisa Forodha wa Vietnam walikamata kontena lingine namba ESU 1174 lililokuwa na tani 6.2 za pembe za ndovu.

Hata hivyo, Mwangunga alishindwa kusema pembe hizo za ndovu zilitoka wapi kama alivyotakiwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe.

Kabwe alitaka waziri huyo aeleze endapo shehena hiyo ni ndovu wanaoendelea kuuawa au zimekwapuliwa kutoka kwenye ghala la serikali.

”Siwezi kusema kuwa zilitoka wapi kwani katika ghala za serikali hakuna wizi uliotokea na namna zilivyopangwa na kama ingechukuliwa hata moja ni rahisi sana kujua, hivyo inawezekana zilitoka katika maeneo yetu au hata nchi jirani waliamua kusafirisha kwa kupitia bandari zetu kutokana na udhaifu uliopo katika bandari za hapa nchini,” alisema Mwangunga.

CHANZO: Mwananchi

INA MAANA WIZARA INGEWEZA KUWADHIBITI MAFISADI HAO LAITI MTANDAO WAO UNGEKUWA NA FEDHA KIDOGO AU HOHEHAHE?HII WIZARA IMEKUWA KICHAKA CHA MAFISADI MIAKA NENDA MIAKA RUDI.BY THE WAY,KAMA MAFISADI WANAWEZA KUTUIBIA BENKI KUU (THRU EPA,etc) AMBAPO KUNA ULINZI WA HALI YA JUU,TUTEGEMEE NINI HUKO MBUNGANI?TUTAJUA MENGI PINDI IKIFANYIKA "SENSA" YA RASLIMALI ZETU HUKO MBUGANI.HOPEFULLY,BY THEN MAFISADI HAWA HAWATAKUWA WAMEKOMBA KILA KITU!


<

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.