3 May 2011


Mtoto wa Rais Kikwete aukana ubilionea

na Betty Kangonga

MJUMBE wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UVCCM), Ridhiwan Kikwete, amekanusha tuhuma zilizoelekezwa kwake juu ya kumiliki mali na mabilioni ya fedha.

Ridhiwan alikanusha madai hayo baada ya nyakati tofauti Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa na Mchungaji Christopher Mtikila kutoa madai kuwa Ridhiwan pamoja na kumaliza shule miaka michache iliyopita, hivi sasa ni tajiri bilionea.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam na waandishi wa habari, Ridhiwan, alisema habari hizo si za kweli bali za kizushi na kwamba zimejaa uongo unaolenga kumchafua yeye pamoja na baba yake Rais Jakaya Kikwete huku wakipandikiza chuki kwa umma.

Ridhiwan alisema kwa sasa anamiliki shamba la hekari moja na nusu, gari aina ya Toyota Cami na akaunti tatu tofauti zilizo katika benki ya NBC, Stanbic na CRDB.

Alipoulizwa mbona anaonekana akitembelea magari ya kifahari, mtoto huyo wa Rais alisema: “Hapa mjini unaweza kumuona mtu amevaa suti ukadhani ya kwake kumbe ameazima. Mimi nina marafiki wengi, huwa wananiazima magari yao nitembelee, juzijuzi hapa nilikuwa na benzi ya rafiki yangu….jamani miundombinu ya mjini si mnaijua?”

Alisema kutokana na kuwaheshimu wazee hao na umri walionao ni bora watumie busara na kujitokeza ili watoe ushahidi juu ya hayo waliyoyasema na hatua zaidi zichukuliwe.

Aliongeza kuwa iwapo itadhihirika kuwa habari walizozieleza ni za uongo basi atakuwa tayari kuwasamehe; lakini alidai leo atawafikishia barua wazee hao ambapo ndani ya wiki mbili amewataka wathibitishe taarifa hizo walizozitoa juu yake.

“Kama haitoshi narudia tena niliwaahidi ushirikiano na endapo watataka ili kuthibitisha yote hayo waliyosema na hata yale wanayoyasikia, wakithibitisha habari walizopewa ni za uongo basi wasisite kuueleza umma,” alisema Ridhiwan.

Ridhiwan alienda mbali zaidi na kudai kuwa si mara ya kwanza kwa Dk. Slaa kuongopewa, akidai kuwa wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka jana, watu wasiopungua 50 walikutana katika mji wa Mwanza kwenye Hoteli ya La Cairo ili kuhujumu uchaguzi.

“Mchungaji Mtikila ambaye yeye amewahi kukiri wazi kuwa alishawahi kuongopewa hivyo, imani yangu kwamba atakapojiridhisha juu ya maroli, maghorofa na hiyo kampuni ya kutengeneza barabara atatumia busara ili hatua za kisheria zifuatwe,” alisema.

Aliwataka wazee hao kutokuwa makanjanja wa kutengeneza habari katika njia ya kutafuta sifa za kisiasa na kuonekana wanajua kuongea.

Ridhiwan alieleza kutokana na kutokuwa na kinga ya aina yoyote na kutambua nchi inaendeshwa katika misingi ya utawala bora ambao unaheshimu haki za binadamu, yuko tayari kutoa ushirikiano kwa vyombo mbalimbali ili ukweli uwekwe wazi.

Mwishoni mwa wiki iliyopita mchungaji Mtikila alimtuhumu Rais Jakaya Kikwete kuitumia Ikulu kumtajirisha mwanawe, ambaye anaaminika kuwa tajiri bilionea.


3 comments:

  1. kwa mfumo tulio nao wa ubepari-uchwara sio dhambi wala kosa mtu kuwa bilionea (ninashangaa kwa nini Mhe Dkt Ridhiwani Kikwete anaonyesha kana kwamba ni dhambi kuwa bilionea!!!), bali sisi tuncahotaka kukiona ni kwamba huo ubilionea ujulikane chanzo chake - kama ni halali na iwapo kodi halali inalipwa!!!! Kwa mfano, Bill Gates wa Marekani ni bilionea lakini kila dola anayopata katika biashara yake iko kwenye rekodi na kodi halali inakatwa kwa mujibu wa sheria.

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.