Mara baada ya uchaguzi
mkuu wa mwaka juzi nilipata ujumbe kutoka kwa watu kadhaa wakinieleza kuwa kwa
namna moja au nyingine niliwasaidia kufanya maamuzi ya kumpigia kura aliyekuwa
mgombea wa CCM, John Magufuli.
Unajua, moja ya makosa
makubwa waliofanya wana-UKAWA kwenye kampeni za uchaguzi huo ni kutojihangaisha
kulifikia kundi muhimu la wapigakura nchini Tanzania: wananchi wasiofungamana
na chama chochote.
Ili kulielewa vema
kundi hili, inabidi kuangalia idadi ya wanachama wa CCM na UKAWA (kwa
kuzingatia uchaguzi wa mwaka 2015). Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa CCM ina
wanachama milioni 8. Makadirio ya idadi ya wanachama wa UKAWA ni angalau
milioni 5. Kwahiyo makadirio
ya jumla ya wapigakura wenye kufungamana na vyama vya siasa ni takriban milioni
13. Tanzania ina watu zaidi ya milioni 50, tukitoa hao milioni 13 tunabakiwa na
watu milioni 37. Tukienda kwenye idadi ya waliojiandikisha kupiga kura walikuwa
milioni 23 hivi. Kwahiyo, kimahesabu, takriban watu milioni 10 (milioni 23
waliojiandikisha kutoa milioni 13 wenye ufuasi wa vyama vya siasa) walikuwa
wapigakura wasiojihusisha na chama chochote.
Tofauti na UKAWA ambayo viongozi na wanachama wake walielemea zaidi
kuhamasishana wao kwa wao, wenzao wa CCM waliwalenga hao takriban milioni 10
wasiofungamana na chama chochote.
Na kimsingi, mie japo sikuwa mpigakura, nilikuwa katika kundi la watu wasio
na vyama. Mara ya mwisho kuwa mwanachama wa chama cha siasa ilikuwa mwaka 2005,
na takriban miaka 15 baadae, sheria ilinizuwia kuwa mwanachama wa chama
chochote cha siasa.
Mwaka 2006 nilianza kufuatilia skandali ya Richmond iliyokuwa ikimhusisha
aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa. Naweza kwa uhakika kuwa
nilikuwa bloga pekee niliyevalia njua suala hilo, sambamba na kuliandikia
makala mbalimbali katika magazeti ya ‘Kulikoni’ na baadaye ‘Mtanzania’ na
hatimaye Raia Mwema. Ufuatiliaji huo ulinigharimu mno lakini hilo si la muhimu
kwa sasa.
Kutokana na bughudha niliyopata kuanzia mwaka 2006 na kuendelea, haikuwa
ajabu kwa mie kuunga mkono harakati za Chadema kupambana na ufisadi. Na mwaka
2010 nilishiriki kikamilifu kumnadi mgombea urais wa Chadema, Dkt Wilbrord
Slaa. Hata baada ya uchaguzi huo, niliendelea kuunga mkono sera hiyo ya ufisadi
ya Chadema. Hata hivyo, sikuwahi kuwa mwanachama wa chama hicho.
Mwanzoni mwa mwaka 2015 nilikuwa miongoni mwa watu waliopiga kelele kwenye
mitandao ya kijamii kuwataka UKAWA watangaze mgombea wao wa kiti cha urais
mapema hasa ikizingatiwa kuwa CCM walikuwa na safari ndefu ya ‘kung’oana macho’
kugombea kuteuliwa na chama chao kuwania urais. Hata hivyo, kelele hizo
hazikuzaa matunda, na utetezi mkubwa ulikuwa “UKAWA inajibidiisha kushughulikia
daftari la wapigakura sambamba na kuhamasisha wapigakura watarajiwa kujiandikisha.”
Hatimaye tulikuja kufahamu kuwa mbinu hiyo ya “kununua muda” ililenga
kumwandalia nafasi Bwana Lowassa endapo asingepitishwa huko CCM. Muungano wa vyama
makini vinne vya upinzani unasubiri ‘kapi’ kutoka chama tawala!
Kufupisha stori, mara baada ya UKAWA kumtangaza Lowassa kuwa mgombea wao,
kwa sie wengine ilikuwa haiwezekani tena kuunga mkono umoja huo uliojumuisha
vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Kwa vile wagombea wakuu katika uchaguzi huo walikuwa Lowassa na Magufuli,
ilikuwa vigumu kumpinga Lowassa bila kumsapoti Magufuli. Kwahiyo japo awali
nilijaribu kuepuka kumnadi mgombea wa CCM, Magufuli, mazingira yaliyokuwepo –
pamoja na mkataba wa kutoa huduma ya usadi (consultancy) – ilipelekea
nami nianze kumnadi Magufuli. Haukuwa uamuzi rahisi hasa kwa kuzingatia
serikali ya CCM ilivyonitenda kuanzia mwaka 2006 nilipoanza kufuatilia skandali
ya Richmond.
Ushiriki wangu kwenye
kampeni haukuwa rahisi. Katika maisha yangu yote sikuwahi kutukanwa kiasi
nilichotukanwa katika kampeni za uchaguzi huo. Jitihada zangu za kuwaelewesha
watu kwanini nimelazimika kumuunga mkono Magufuli hazikusaidia kitu. Pengine
kibaya zaidi ni kwamba wakati wa kuelekea uchaguzi huo nilifiwa na baba yangu,
marehemu Mzee Philemon Chahali. Baadhi ya watu bila utu walitumia msiba huo
kuingiza uhasama wa kisiasa.
Pamoja na mvua ya matusi ya kila aina, niliendelea na jukumu la kumnadi
Bwana Magufuli. Nadhani mchango wangu mkubwa zaidi ulikuwa kwa wapigakura
waliokuwa hawajafungama na chama chochote. Na nilifahamu kuhusu hilo baada ya
uchaguzi ambapo baadhi yao walinieleza bayana kuwa ushawishi wangu kwao
ulipelekea kufanya uamuzi wa kumpigia kura mgombea huyo wa CCM.
Lakini tukiweka kando ‘sababu zangu binafsi,’ Magufuli alionekana kama
mgombea bora zaidi ya mpinzani wake Lowassa. Pamoja na sababu nyingine, wakati
Magufuli alikuwa ‘mgombea wa CCM kutoka CCM,’ Lowassa alikuwa mgombea wa UKAWA
kutoka CCM.
Hatimaye uchaguzi ukafanyika na Magufuli akaibuka mshindi. Kama kuna kitu
kilichonipa matumaini sana kuhusu urais wa Magufuli ni hotuba yake aliyoitoa
wakati wa uzinduzi wa bunge la Jamhuri ya Muungano. Katika hotuba hiyo,
Magufuli alionyesha kuwa mtu anayezielewa vema shida za Watanzania hususan
janga la rushwa na ufisadi, na akaapa kushughulikia kwa nguvu zake zote. Na
alipoomba Watanzania wamwombee katika vita hiyo ngumu, naamini hata miongoni
mwa wale ambao hawakumpigia kura waliitikia wito huo wa kumfanyia maombi.
Kisha zikaja ziara ya kushtukiza na taratibu tukaanza kuingiwa na matumaini
mapya ya “mrithi halisi wa Nyerere/Sokoine.” Na dunia pia ikaungana nasi
kusherehekea kiongozi huyo adimu, na ikaibuka alama ya reli #WhatWouldMagufuli
Do iliyotamba kila kona ya dunia. Na haikupita wiki bila kushuhudia “tumbua
majipu.”
Kwa kufurahishwa na kuridhishwa na utendaji wake, mie ‘nikajipinda’ na
kuandika kitabu cha tathmini ya urais wa Magufuli, siku 55 tu baada ya yeye
kuapishwa kuwa Rais wa tano wa Tanzania. Watu kadhaa walinikosoa kwamba haikuwa
sahihi kwangu kufanya tathmini hiyo mapema kiasi hicho.
Kwa wakati huo niliona
walionikosoa kuhusu suala hilo kama watu wenye chuki binafsi dhidi ya ‘mkombozi’
Magufuli.
Dalili ya kwanza kwamba huenda kuna walakini katika utawala wa Magufuli ni
pale alipotangaza baraza lake la mawaziri ambalo ilituchukua wiki kadhaa
kulisubiri. Lilipotangazwa, sio tu lilikuwa kubwa kuliko ahadi yake kuwa
angeunda serikali ndogo tu ili kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali,
bali pia lilijumuisha baadhi ya sura ‘zenye utata.’ Miongoni mwa sura hizo ni
Profesa Muhongo, ambaye alilazimika kujiuzulu katika serikali ya Awamu ya Nne
kutokana na kuhusishwa na skandali ya Tegeta Escrow.
Kuna tuliouona uteuzi wa mtu kama Nape Nnauye kuwa ni wa kisiasa zaidi,
huku sura kama Simbachawene, Lukuvi na Profesa Maghembe zikijenga ishara kuwa
huenda mambo hayajabadilika kama tulivyotarajia.
Kisha kukafanyika uteuzi wa mabalozi ambao ulionekana bayana kama kutumia
nafasi hizo nyeti kuwaondoa watu flani kwenye nyadhifa zao huko CCM. Baadhi
yetu tukaanza kujiuliza, “hivi hatujayashuhudia haya huko nyuma?” Lakini
tukaendelea kuwa na matumaini.
Dalili ya kwanza kabisa kuwa pamoja na mazuri yake yaliyowavutia Watanzania
wengi na kona mbalimbali duniani, Bwana Magufuli ana mapungufu yake ni pale
serikali yake kupitia ‘shujaa wa sasa’ Nape Nnauye ilipozuwia haki ya mamilioni
ya Watanzania kusikiliza matangazo ya moja kwa moja ya Bunge. Niwe mkweli,
wanaomwona Nape shujaa huwa siwaelewi kabisa. Ningemwona shujaa laiti angetumia
ukongwe wake ndani ya CCM kumweleza bosi wake Magufuli kuwa wazo la kuzuwia
matangazo ya bunge live ni fyongo, na laiti Magufuli angemomea basi angejiuzulu
kishujaa badala ya kusubiri kufukuzwauwaziri kwa kupambana na ‘kimeo kingine
cha Magufuli’ yaani Daudi Albert Bashite.
Baadaye likaja zuwio dhidi ya mikutano na maandamano ya vyama ya siasa.
Awali baadhi yetu tulijipa matumaini kwamba “ah huu ni muda wa kuchapa kazi.
Hayo maandamano na mikutano ni ya nini muda huu?” Kwahiyo kwa wakati huo
ili-make sense.
Mara tukakumbwa na janga la tetemeko la ardhi huko Kagera. Ikategemewa Rais
angekwenda kuwafariji wahanga hasa ikizingatiwa kuwa anatoka Kanda ya Ziwa.
Hakwenda hadi baadaye. Na alipokwenda akatoa hotuba isiyopendeza kuisikiliza.
Maneno kama “serikali haikuleta tetemeko la ardhi” sio ya busara hata kidogo.
Pia akaongopa kwa kudai hakuna serikali duniani inayotoa misaada kwa wahanga wa
majanga ya asili. Sijui muda huu anajisikiaje akiona kwenye runinga jinsi
serikali ya Marekani inavyowahudumia wahanga wa vimbunga.
Baadaye kukusikika taarifa mbalimbali za tishio la uhaba wa chakula, lakini
badala ya kuwafariji wananchi, Magufuli akawaropokea kwamba serikali yake
haitotoa chakula kwa vile serikali haina shamba.
Na wakati mmoja alipita sijui Nzega au Urambo, mwananchi mmoja akamwambia “njaa
Mheshimiwa.” Hilo jibu alilotoa utadhani ugomvi. Pamoja na majibu mengine ya
ngebe akasema “njaa, kwani mnataka niingie jikoni kuwapikia?” Ovyo kabisa.
Likatokea tukio la maaskari polisi wanane kuuawa huko Kibiti lakini Amiri
Jeshi Mkuu akaenda kufungua mabweni chuo kikuu cha Dar es Salaama badala ya
kwenda kuaga miili ya askari hao.
Pia kulijitokeza tukio la ‘kupotea’ kwa kada wa Chadema Ben Saanane ambaye
hadi ‘kupotea’ kwake alikuwa akihoji kwa nguvu kubwa kuhusu PhD ya Magufuli.
Baadhi tulimsihi awe makini (kwa sababu dalili zilishaanza kujionyesha kuwa
Magufuli ni mtu wa aina gani) lakini bahati mbaya hakusikia ushauri wetu. Hadi
leo haijulikani nini kimemsibu kijana huyo japo Chadema nao hawawezi kukwepa
lawama katika poor handling ya suala hilo. Kumekuwa na kauli zinazokinzana
kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho kama ile ya mwenyekiti Mbowe kuwa
Ben alitekwa huku Mbunge wa chama hicho Saeid Kubenea akidai kuwa kada huyo
anaonekana vijiweni. Kwanini chama hicho hakijawabana
viongozi hao kufafanua kauli zao, only God knows!
Lakini kama kuna tukio lililompotezea heshima kubwa Bwana Magufuli ni lile
la Mkuu wa Mkoa Paul Makonda kuvamia stesheni ya redio na runinga cha
Clouds akiwa na askari wenye silaha.
Siku chache baadaye huku baadhi ya watu wakitarajia angemtimua Makonda,
Magufuli akatufanya sote mabwege kwa kumtetea Makonda huku akidai yeye
hapangiwi kazi, yeye ndo Rais, na kumwita Makonda mchapakazi. Yaani Mkuu wa
Mkoa amevamia kituo cha habari, kitendo ambacho ni kosa la jinai, halafu Rais
anamsifu kuwa ni mchapakazi?
Uswahiba wa Magufuli na Makonda umechangia mno ugumu wa kuchunguza tuhuma
kuwa mkuu huyo wa mkoa amefoji jina analotumia pamoja na cheti cha kuhitimu
kidato cha nne. Laiti Magufuli angekuwa mwajibikaji kama tunavyoamini basi
angeamuru uchunguzi kuhusu suala hilo.
Na kwa wanaofahamu yanayoendelea ‘nyuma ya pazia,’ inadaiwa kuwa vetting
aliyofanyiwa Bashite ilionyesha bayana mapungufu yanatajwa kumhusu yeye, na ‘Bwana
mkubwa’ akashauriwa kuchukua hatua stahili lakini hakufuata ushauri huo.
Hili la Bashite limeendelea kuwakera watu wengi sana, hasa ikizingatiwa
kuwa mtu huyo anatumia ipasavyo upendeleo anaopewa na Magufuli, na kufanya
dharau za wazi kama ile ya kupigiwa saluti na vingozi wa ngazi za juu wa jeshi
la polisi huku amevaa kapelo. Hiyo ni dharau ya hali ya juu kwa vyombo vyetu
vya dola.
Na Magufuli ataingia kwenye vitabu vya historia kwa serikali yake
kulifungia gazeti la kila wiki la Mwanahalisi kwa miaka mitatu, na siku 10
baadaye akalifungia gazeti jingine la kila wiki la Raia Mwema kwa siku 90.
Na kama kuna gazeti lilijitahidi mno 'kumnadi' Magufuli ni Raia Mwema. Nakumbuka makala nyingi katika gazeti hilo wakati wa kuelekea kwenye uchaguzi zilisheheni habari 'nzuri' kuhusu Magufuli.
Pengine si vibaya nikitumia fursa hii kueleza kuwa sababu hasa iliyonifanya niache uandishi wa makala katika gazeti hilo ni kwamba lilihojiwa na 'vijana wa Magufuli' kuhusu mie lakini wahusika hawakuona umuhimu wa kunieleza wala kuandika kuhusu habari hiyo.
Na kilichopelekea bwege huyo kudadisi kuhusu mie ni TWEET...Yes, just a tweet, a #FutureTweet to be precise.
Kanuni muhimu katika chombo cha habari ni kwamba unyanyasaji wa taasisi yoyote ile dhidi ya mwenzenu ni unyanyasaji dhidi yenu nyote. Gazeti hilo lilipaswa kunijulisha kuhusu kilichotokea au kukiandika kama habari gazetini. Lakini bahati nzuri mie mzoefu wa 'dark arts' nikafahamu mapema kilichokuwa kinaendelea.
Hata hivyo, kitendo cha gazeti hilo nilikiona kama usaliti, nikaamua kuachana nao. Hata hivyo, mie sina kinyong'o nao na ndio maana jana nililaani na kupiga kelele kuhusu hatua hiyo ya serikali.
Na kama kuna gazeti lilijitahidi mno 'kumnadi' Magufuli ni Raia Mwema. Nakumbuka makala nyingi katika gazeti hilo wakati wa kuelekea kwenye uchaguzi zilisheheni habari 'nzuri' kuhusu Magufuli.
Pengine si vibaya nikitumia fursa hii kueleza kuwa sababu hasa iliyonifanya niache uandishi wa makala katika gazeti hilo ni kwamba lilihojiwa na 'vijana wa Magufuli' kuhusu mie lakini wahusika hawakuona umuhimu wa kunieleza wala kuandika kuhusu habari hiyo.
Na kilichopelekea bwege huyo kudadisi kuhusu mie ni TWEET...Yes, just a tweet, a #FutureTweet to be precise.
Hata hivyo, kitendo cha gazeti hilo nilikiona kama usaliti, nikaamua kuachana nao. Hata hivyo, mie sina kinyong'o nao na ndio maana jana nililaani na kupiga kelele kuhusu hatua hiyo ya serikali.
Haya yanatokea wakati Tanzania bado ipo kwenye mshtuko kufuatia jaribio la
kumuua mwanasiasa ambaye amekuwa mpinzani mkubwa wa Magufuli, mbunge wa Chadema
Tundu Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria cha TLS. Chuki
inayopandikizwa dhidi ya wapinzani imepelekea takriban asilimia 99 ya viongozi
wa CCM kuogopa kwenda kumjulia hali Lissu huko Nairobi alikolazwa.
Lakini pengine kipimo halisi cha mambo kwenda kinyume na matarajio ya
baadhi yetu kuhusu Magufuli ni kwamba tangu aingie madarakani, zaidi ya
viongozi na wanachama 400 wa Chadema wamekamatwa na polisi. Imefika mahala,
wakuu wa wilaya wanakamata viongozi wa Chadema kila wanapojisikia. Na pengine
kibaya zaidi ni ukweli kwamba taratibu jamii inaanza kuzowea kuona viongozi na
wanachama wa upinzani – hususan Chadema – wakidhalilishwa na kukamatwa
kiholela.
Jambo jingine la kusikitisha kuhusu utawala wa Magufuli ni utitiri wa
sheria kandamizi kuhusu uhuru wa habari. Licha ya sheria ya makosa ya mtandao
ya mwaka 2015 ambayo ni kazi ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete, tayari kuna sheria
ya Huduma za Habari, ambayo ‘shujaa Nape’ alihusika kwa kiasi kikubwa, na sasa
kuna kinachoitwa ‘Kanuni za Maudhui ya Mitandao ya Kijamii,’ ambayo laiti zikipitishwa
zitakuwa balaa kubwa.
Na huku Chadema ikishuhudia viongozi na wanachama wake wakinyanyaswa ovyo
ovyo, kuna kila dalili kuwa mgogoro unaoendelea ndani ya chama cha CUF una
mkono wa serikali hasa kwa kuzingatia mwenendo wa ofisi ya Msajili wa Vyama vya
Siasa (taasisi ya serikali) kuibeba waziwazi kambi ya mwanachama aliyejiuzulu
kwa utashi wake Prof Lipumba, ambaye from nowhere alirudi chamani na kudai yeye
bado mwenyekiti.
Majuzi, Magufuli katumwagia siri kwamba kuna siku aliombwa ushauri na Spika
Ndugai kuhusu uteuzi wa wajumbe wa kamati ya bunge. Hiyo ina maana kuwa bunge
limewekwa mfukoni na mhimili wa serikali. Kadhalika, kauli za Jaji Mkuu ‘mpya’ baada ya jaribio la mauaji dhidi ya Tundu
Lissu zinajenga taswira ya mhimili wa mahakama nao kuwekwa mfukoni na mhimili
wa serikali.
Katika kuhitimisha makala hii ndefu ninarudia swali lililobeba kichwa cha
habari: nini kilichomsibu Magufuli hadi kubadilika kiasi hiki? Kauli yake kuwa
alisukumwa kuchukua fomu ya urais inazidi kuleta mkanganyiko kwamba labda
alikuwa anafahamu fika hana uwezo wa kuongoza taifa letu lakini akakubali tu
kutokana na shinikizo hilo, ambalo hata hivyo hatujui limetoka kwa watu gani.
Dalili kwamba ‘Magufuli atabadilika’ (kurejea kuwa yule tuliyemwona ni
mkombozi wetu) ni finyu. Kwa vile maamuzi yake mengi yanamtengenezea maadui
zaidi ya waliopo, kuna kila dalili kwamba atazidi kuwa mkali ili ‘kujilinda.’ Tutegemee
uhuru wa kujieleza/habari uendelee kubinywa zaidi kadri bwana mkubwa anavyozidi
kutukumbusha yeye ndio Rais, asiyeambiwa nini cha kufanya, anayejua siri
zote na nchi yetu, na vitu kama hivyo.
Nimalizie kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuhusu rai ya mara kwa mara
ya Rais Magufuli kuwataka Watanzania tumwombee. Na tufanye hivyo kwa bidii
kubwa ili Mwenyezi Mungu amwonyeshe njia sahihi ya kuliongoza taifa letu kwa
kuzingatia haki na usawa. Tumwombee aondokane na 'fear of the unknown,' apate muda wa kupumzika badala ya kukesha macho akihofia 'the unknown.' Aachane na chuki dhidi ya kila anayemkosoa hata kama kukosoa huko ni kwa nia njema. Tumwombee awe na busara ya kutokitumia 'kitengo' kama kampuni yake binafsi. Ajiulize, kwanini licha ya ulinzi wake wa 'kufa mtu' bado siri zinavuja? Jibu jepesi: ukiwafanya watu wazima tena wenye utaalamu nyeti kuwa kama watoto, inakuwa 'mwaga ugali nimwage mboga.' Na asije kukasirishwa na makala hii...
Ni wazi kuwa ndoto za kuikomboa Tanzania yetu
kiuchumi haziwezi kufanikiwa katika hali ya sasa ya siasa za vitisho,
kunyanyasa wapinzani, “watu wasiojulikana,” na vitu kama hivyo.
Mungu ibariki Tanzania
0 comments:
Post a Comment