Showing posts with label LAWRENCE MASHA. Show all posts
Showing posts with label LAWRENCE MASHA. Show all posts

17 Jan 2011


7 Jul 2010


Demokrasia katika jamii isiyojali utawala bora ni sawa na kufukia makaratasi ardhini kwa matarajio ya kuota mmea wenye matunda ya noti.Ni mithili ya kualika timu ya Taifa ya Brazil kwa mabilioni ya shilingi kisha mechi husika ituache na bili kubwa pasipo manufaa yoyote.Hebu tafakari.Mwezi Oktoba Watanzania kwa mamilioni yao watapiga kura kumchagua Rais na Wabunge.Japo shughuli hiyo ni ya siku moja tu,maandalizi yake yanagharimu mabilioni ya shilingi.Wenyewe wanasema ndio gharama ya demokrasia.Lakini baada ya uchaguzi,wengi-kama sio wote-wa tutakaowachagua watasahau kabisa kwanini tumewachagua,huku wakiwa bize kutafuta namna ya kufidia gharama walizotumia kuingia madarakani.

Zamani hizo tuliambiwa kuwa demokrasia ni pamoja na uwepo wa vyama vingi vya siasa.Takriban miongo miwili baadaye Watanzania wameshuhudia namna uwepo wa vyamahivyo vingi vya siasa ulivyoshindwa kulikwamua taifa letu kutoka kwenye lindi la umasikini.Sanasana umasikini umekuwa ukizidi kuongezeka huku wanasiasa wetu wakibadili kauli mbiu kila baada ya muhula (kwa mfano kutoka Ari Mpya,Kasi Mpya na Nguvu Mpya kuwa Ari Zaidi,Kasi Zaidi na Nguvu Zaidi).Tumeshuhudia pia mlolongo wa sera,mikakati,mpingo na vitu kama hivyo,from MKUKUTA to MKURABITA to KILIMO KWANZA.Na kwa mawazo mapya hatujambo,shughuli ipo kwenye utekelezaji.

Siku chache zilizopita nilitundika makala kuhusu utata wa kauli za Waziri wa Sheria na Katiba Mathias Chikawe na zile za Makamu Mwenyekiti wa CCM Pius Msekwa kuhusu suala la uanzishwaji Mahakama ya Kadhi.Wakati Waziri Chikawe aliahidi kuwa mahakama hizo zingeanza kazi mwakani,Msekwa alitamka bayana kuwa suala hilo haliwezekani.Hadi leo hakuna ufafanuzi uliotolewa kuhusu suala hilo ila kilicho bayana ni kuwa CCM imeamua kuachana nalo baada ya kuliingiza kwenye manifesto yake ya Uchaguzi mwaka 2005.Kwa vile sie ni mahiri zaidi wa kuhangaika na mambo kwa mtindo wa zimamoto tunasubiri liwake la kuwaka ndipo tuanze kuhangaika namna ya kudhibiti.Taasisi zenye majukumu ya kuwa proactive (yaani kuazuia majanga kabla hayajatokea) ziko busy zaidi na kuhakikisha CCM inarejea madarakani kwa ushindi wa kishindo badala ya kujishughulisha na jukumu lao la msingi la kulinda na kutetea ustawi wa taifa letu.Kwao,siasa (yaani CCM) ndio nchi na ndio kila kitu.

Majuzi umejitokeza utata mwingine wa kauli kati ya mawaziri wawili waandamizi kuhusu suala la uraia wa nchi mbili (dual citizenship).Na kichekesho ni kwamba tofauti na ule mgongano wa kauli kati ya Chikawe na Msekwa,safari hii mgongano wa kauli za mawaziri hao umejiri ndani ya jengo la Bunge katika kikao kinachoendela cha bajeti ya mwaka 2010/11.Awali,Waziri wa Mambo ya Ndani Lawrence Masha alilieleza Bunge Tukufu kuwa serikali imeamua kuwa huu sio wakati mwafaka kwa suala la uraia wa nchi mbili,na kwamba serikali anaangalia uwezekano wa kuanzisha ukaazi wa kudumu (permanent residency).Waziri Masha alieleza kuwa serikali inaandaa hoja kuhusu suala hilo la permanent recidency kwa minajili ya kuileta bungeni ijadiliwe. "Huu sio wakati mwafaka kuruhusu uraia wa nchi mbili,serikali inaangalia uwezekano wa kuanzisha ukaazi wa kudumu badala ya uraia wa nchi mbili", alisema Masha.

Wakati Masha akisema hivyo,Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Bernard Membe alilieleza Bunge hilohilo kuwa serikali imeridhia suala la uraia wa nchi mbili na kwamba Wizara yake iko kwenye mchakato wa kuwasilisha suala hilo kwenye kikao cha Barza la Mawaziri.Pia Membe alieleza kuwa anafanya mawasiliano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ili kupata baraka zao kutokana na suala hilo kuwa la Muungano.Akihitimisha hoja ya bajeti ya wizara hiyo, kwa mwaka wa fedha 2010/2011, Waziri Membe alisema siyo dhambi, Watanzania kutafuta riziki nje ya nchi na ni haki yao kubaki na uraia wa Tanzania.Alisema wakati umefika kwa Watanzania, kupatiwa haki yao ya msingi kwani licha ya kuwa ni manufaa kwao pia ni manufaa kwa nchi kutokana na fursa ya kuongeza pato la taifa.

Kadhalika,inadaiwa kuwa Waziri Membe aliwaeleza Watanzania waliohudhuria mkutano wa Diaspora jijini London hivi karibuni kwamba suala hilo limeshajadiliwa na baraza la mawaziri na linasubiri kuwasilishwa bungeni ili upitishwe au kupingwa na wabunge.Mimi sikuhudhuria Mkutano huo wa Diaspora kwa vile niliamini ungenipotezea muda wangu tu kwa sababu viongozi wetu ni mahiri sana katika kuahidi mambo mazuri kwenye hadhara,na hujifanya wasikivu sana lakini utekelezaji ni zero,sifuri,zilch!

Ni dhahiri kwamba mmoja kati ya mawaziri hawa anadanganya.Wakati sina la kusema kuhusu kauli ya Waziri Masha,kauli za Waziri Membe huko Bungeni na London zinaleta utata unaoweza kuyumkinisha kuwa kuna urongo wa namna flani.Je kauli ipi ni sahihi kati ya hiyo alotoa London kuwa suala hilo limeshajadiliwa na Baraza la Mawaziri na hiyo ya bungeni kuwa suala hilo bado liko wizarani huku likifanyiwa mchakato wa kulipeleka kwenye Baraza la Mawaziri?

Unajua kwanini mmoja wao anadanganya?Sababu ni kadhaa,lakini kwa ufupi,moja,ni kwa vile mdanganyifu huyo anafahamu bayana kuwa wabunge wanaoelezwa suala hilo wapo bize zaidi kufikiri namna watakavyorudi bungeni baada ya uchaguzi (sambamba na kuwazia posho zao nono za vikao vya bunge) kuliko kumkalia kooni waziri aeleze kinagaubaga.Ndio maana mwanzoni mwa makala hii nilibainisha uselessness ya demokrasia yetu.Tunapoteza mabilioni ya shilingi (sambamba na muda wetu kusikiliza porojo za "mkituchagua tufafanya hiki na kile") kuwachagua watu wa kutuwakilisha bungeni lakini wakishafika huko wanakuwa bize zaidi na maslahi yao binafsi.

Pili,anayedanganya kati ya mawaziri hao anafahamu kuwa aliyemteua hatamwajibisha.Kama kuna mtu alimudu kumzuga Rais kwa kuchomekea ishu kadhaa kwenye muswada wa sheria za gharama za uchaguzi na kisha akasalimika,kwanini basi mdanganyifu huyo katika suala hili la uraia mbili awe na hofu?

Tatu,waziri anayedanganya kati ya hao wawili anafahamu udhaifu wa Watanzania katika kudai haki zao za msingi.Kiongozi anaweza kudanganya waziwazi kwenye umati wa watu lakini bado akaishia kupigiwa makofi na vigeregere.Ule wimbo wa "Ndio Mzee" wa Profesa Jay unawakilisha hali halisi ya namna Watanzania wengi wanavyoridhia kuzugwa na wanasiasa wababaishaji.Hebu angalia namna harakati za kuirejesha tena madarakani CCM zinavyopamba moto huko nyumbani.Kwa mgeni,anaweza kudhani labda chama hicho ni kipya na hakihusiki kabisa na kashfa za ufisadi,kubebana,kubomoa uchumi wetu na madudu mengine chungu mbovu yanayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi masikini kabisa duniani licha ya raslimali lukuki iliyojaaliwa kuwa nazo.Binafsi naamini kuwa unyonge huo wa Watanzania umechangiwa sana na siasa za chama kimoja ambapo kiongozi alikuwa mithili ya Mungu-mtu,hakosei,lazima ashangiliwe hata akiongea utumbo,sambamba na suala la kujikomba kwa viongozi kwa matarajio ya kujikwamua kwa namna moja au nyingine.

Na kwa vile vyama vya upinzani vimetuthibitishia kuwa uwezo wao katika kuing'oa CCM madrakani ni kama haupo,basi mazingaombwe kama hayo ya Chikawe na Msekwa,na haya ya sasa kati ya Masha na Membe yataendelea kuwepo kwa muda mrefu sana.Unaweza kuhisi kama nimekata tamaa vile kwa namna ninavyoandika.Hapana,ila safari yetu ni ndefu sana,na tatizo sio urefu tu bali ni kiza kilichotanda kwenye njia yetu ambayo imejaa mashimo kadhaa.Ni sawa na kipofu kumsaka paka mweusi kwenye chumba chenye giza ilhali paka huyo hayumo chumbani humo.

4 May 2009


WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha ameingiza serikali katika mgogoro mkubwa na wafadhili kutokana na madai ya matumizi mabaya ya madaraka, MwanaHALISI limeelezwa.

Masha anatuhumiwa kupendelea raia wa Ubelgiji, Brigitte de Floor, katika mgogoro kati yake na Wiebke Gaetje ambaye anatoka Ujerumani, jambo ambalo limeingiza serikali katika mgogoro wa kidiplomasia.

Brigitte de Floor na Wiebke Gaetje ni wajane wa Klaus Gaetje ambaye anatoka Ujerumani. Klaus Gaetje ambaye alikuwa mfanyabiashara mkoani Mwanza, alifariki dunia katika mazingira ya kutatanisha Julai 2004 huko Port Bell, nchini Uganda.

Waziri Masha anatuhumiwa na Wiebke Gaetje kuwa kikwazo katika upatikanaji wa urithi wa mume wake.

Gaetje anadai kuwa kampuni ya uwakili ya Masha, IMMMA Advocates, imehusika katika kushughulikia baadhi ya nyaraka ambazo zimesaidia “kupora mali” ya marehemu mume wake.

Miongoni mwa mali ambazo Masha anatuhumiwa kusaidia Brigitte de Floor kupora ni vivuko vitatu, viwanja vinne na “baadhi ya magari ya kampuni.”

Vivuko vinavyohusika ni Kamanga, mv Uzinza na mv Karumu. Vyote viko katika eneo la Kamanga.

Taarifa kutoka ubalozi wa Ujerumani nchini zinasema tayari serikali ya Ujerumani imelalamikia hatua hiyo ya waziri Masha ikiiita, “Matumizi mabaya ya madaraka.”

Naye Ofisa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa jijini Dar es Salaam, ambaye aliomba jina lake lisiwekwe wazi, alithibitisha kwamba “serikali ina taarifa hizo.”

Klaus Gaetje na Wiebke Gaetje walifunga ndoa tarehe 12 Oktoba 1979 nchini Ujerumani na kuzaa mtoto mmoja wa kiume, Mark Gaetje (28). Mtoto huyo na mama yake wanalalamikia Masha kushirikiana na Brigitte de Floor kutapanya mali yao.

Kwa sasa, Mark Gaetje anaishi Uholanzi na alitarajiwa kuwasili nchini juzi, Jumatatu saa nne usiku kwa ndege ya Shirika la Ndege la Uholanzi (KLM) ili kushughulikia suala hilo. Tayari mama wa Mark amewasili nchini.

Mgogoro huu uliomuingiza Masha katika kashifa nyingine, umetokana na hatua ya Brigitte de Floor, ambaye anajiita mjane wa Klaus Gaetje kudaiwa kugushi baadhi ya nyaraka ikiwamo cheti cha ndoa na wosia kwa lengo la kujimilikisha mali hizo.

Cheti cha ndoa kinachodaiwa kugushiwa ni Na. E 087887 kinachoonyesha kuwa kimetolewa 10 Oktoba 1999 wilayani Magu, mkoani Mwanza. Kimesainiwa na Msajili Msaidizi wa Ndoa, Anthony Jakonyango.

Hata hivyo, katika hati yake ya kiapo ya 5 Julai 2008 mbele ya kamishina wa viapo, Elias Kitwala, ambayo gazeti hili linayo nakala yake, Jakonyango anakana kufungisha ndoa hiyo; anasema cheti hicho ambacho waziri Masha anang’ng’ana nacho kimegushiwa.

Anasema, “Mimi nilihama Magu, 20 Mei 1999 kwenda Bukoba, mkoani Kagera. Hivyo kwa vyovyote vile, nisingeweza kufungisha ndoa Magu 10 Oktoba 1999.” Jakonyango anasema cheti cha ndoa anachodaiwa kusaini siyo halali.

MwanaHALISI limefahamishwa kwamba kwa msaada wa Masha, Brigitte de Floor amefanikiwa kumuondoa Mark na mama yake Wiebke Gaetje katika umiliki wa hisa za kampuni ya Kamanga Ferry Limited (KFL).

Katika nyaraka kadhaa ambazo ziko mikononi mwa MwanaHALISI, Masha amesaini, kama Katibu wa kampuni ya Kamanga Ferry Limited huku kampuni yake ya IMMMA Advocates ikithibitisha baadhi ya nyaraka ukiwamo wosia wa marehemu Klaus Gaetje.

Tayari wosia huo umelalamikiwa na mke wa kwanza wa Klaus Gaetje, Wiebke na mtoto wake Mark kwa hoja kwamba mke wa pili Brigitte de Floor amegushi.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Idara ya Uhamiaji, Brigitte de Floor aliingia nchini kama mtalii na amekuwa akiishi nchini bila kibali cha kufanya kazi, lakini kutokana na mahusiano yake na Masha, serikali imeshindwa kumchukulia hatua.

Taarifa zinasema tayari mipango inasukwa ili kumpatia mama huyo kibali cha kuishi nchini ili kuendeleza kile kinachodaiwa na Wiebke, “urafiki wa damu na waziri Masha.”

Anasema, “Ninajua ukaribu wa familia ya Masha na de Floor. Baba yake Masha amekuwa akipewa misaada na de Floor. Tayari ameipa familia hiyo viwanja vinne ambavyo ni mali ya mwanangu.”

Katika wosia huo, Brigitte de Floor ambaye anatambulishwa kama shahidi amesaini kila karatasi, wakati saini ya marehemu inaonekana katika karatasi moja tena ya mwisho.

Aidha, familia ya Masha inatuhumiwa kumilikishwa viwanja vinne vilivyopo Kamanga, na kwamba suala hilo tayari limewasilishwa Ofisi ya Rais, kwa Waziri Mkuu, Wizara ya Sheria na Katiba, Taasisi ya Kuzuia na Kupamban na Rushwa (TAKUKURU) na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP).

Wiebke Gaetje alitalikiana na mumewe, Klaus Gaetje, mwaka 1996 na baadaye Klaus alimwoa Brigitte de Floor, mtalaka mwenye watoto wa kike wawili ambao si wa Klaus Gaetje.

Hata hivyo, katika hali ambayo haijulikani chanzo chake, Masha ameridhia mali za Klaus Gaetje, zimilikiwe na watoto wa mke wake, jambo ambalo limelalamikiwa na mke wa kwanza Wiebke na mtoto wake Mark.

Brigitte de Floor anadaiwa kuhamisha fedha nyingi na kuzipeleka kwenye akaunti zake zilizoko nje ya nchi, jambo ambalo vyombo vya dola na taasisi nyingine za serikali zimearifiwa, lakini bado kimya kimetanda.

Imefahamika kuwa de Floor alitumia kampuni ya KFL kujipatia mkopo kutoka Benki ya CRDB na fedha hizo alizihamishia kwenye akaunti yake iliyopo Ubeligiji.

Klaus na Wiebke waliishi Kamanga kuanzia mwaka 1974 hadi 1994 na mtoto wao, Mark Gaetje, alilelewa kwenye eneo hilo la Ziwa Viktoria na hivyo kuusiwa na baba yake kuwa mrithi wa mali zote.

Kamanga ndipo makao makuu ya Kamanga Ferry Limited yenye vivuko vitatu vinavyofanya safari zake katika eneo hilo la ziwa Viktoria.

Baada ya kifo cha Klaus Gaetje Julai 2004, Brugitte de Floor aliamuru mwili wake uchomwe moto na kuzikwa Kamanga, tendo lililofanyika haraka na bila kushirikisha familia ya marehemu wala kuufanyia mwili uchunguzi.

“Baada ya hapo de Floor alighushi wosia wa pili wa Klaus kwa kusaidiwa na mwanasheria wake,” anasema mmoja wa watu walio karibu na Wiebke.

Tangu hapo de Floor amekuwa anadai kuwa alipewa mamlaka ya kufanya mambo yote ya KFL kwa niaba ya Mark na ametumia fursa hiyo kuwafukuza wafanyakazi wengi wa zamani na kuajiri wageni kutoka nje ya nchi.

Kutokana na hali hiyo, Mark Gaetje alilazimika kuandika barua, Oktoba mwaka jana, kwa Ofisa Uhamiaji wa Mkoa wa Mwanza, kulalamikia hatua ya mama yake huyo wa kambo kughushi cheti cha ndoa ili kufaidi huduma za uhamiaji nchini.

Lakini pia 11 Februari mwaka huu, Mark aliandika barua kwenda kwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), akilalamikia mambo manne, likiwamo la kampuni kukosa mkurugenzi baada ya aliyekuwapo kufukuzwa.

“Tangu kifo cha baba yangu sijawahi kuhudhuria kikao chochote cha bodi wala kupewa taarifa yoyote na de Floor…Isitoshe, sijawahi kupewa fedha zozote kama mkurugenzi na wala sijapokea habari kuwa de Floor ametumia kibali changu kufanya mambo kwa niaba yangu. Nakanusha kuwa sijampa ruhusa yoyote,” anasema.

Anaeleza kuwa kama kuna mabadiliko yoyote katika KFL, “Uongozi, anwani au vingine ambavyo vinaathiri kampuni na ambavyo vinadaiwa kufanyika nikiwa mshiriki kati ya mwaka 2004 na sasa, visichukuliwe umuhimu kwa kuwa vitaathiri kampuni ambayo mimi ni mkurugenzi wake,” anasema Mark.

Akizungumza kwa njia ya simu juzi Jumatatu na MwanaHALISI, Wiebke amesema tayari ubalozi wa nchi yake nchini umeomba hati ya kifo cha mumewe Klaus kutoka Uganda, kutokana na utata mkubwa uliogubika kifo chake.

Hii ni mara ya tatu mwaka huu waziri Masha kutuhumiwa kutenda kinyume cha utawala bora.

Januari alituhumiwa kuingilia mchakato wa zabuni ya vitambulisho vya taifa na Februari akatuhumiwa kufanya upendeleo kwa Mwingereza Douglas Hume Claxton kwa kufuta amri ya Mkurugenzi wa Uhamiaji ya kumfukuza nchini.


CHANZO: Mwanahalisi.

5 Feb 2009

Habari HII ni kwa mujibu wa toleo la wiki hii la jarida la Raia Mwema.Bingirika nalo kwa habari za uhakika sambamba na makala zilizokwenda shule.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.