Showing posts with label MAADILI. Show all posts
Showing posts with label MAADILI. Show all posts

20 Feb 2009




HAYA NDIO MAJIBU YA CCM.CHINI YA MAJIBU HAYO NI HABARI YENYE MATAMSHI YA DR KITINE.


CCM yamjibu Dk. Kitine

na Edward Kinabo

SIKU moja baada yaMkurugenzi mstaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa nchini, Dk. Hassy Kitine, kudai nchi inaendeshwa kienyeji na kukilalamikia Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuendelea kuwakumbatia wanachama wake wanaokabiliwa na kesi za ufisadi, chama hicho
kimesema hakiwezi kuwavua nyadhifa hizo, kwa sababu kesi zao bado ni tuhuma tu.

Sambamba na hilo, CCM imesema kauli ya Dk. Kitine kwamba nchi inaendeshwa kienyeji ni maoni yake binafsi, kwani hayana ukweli. Msimamo huo wa CCM ulitolewa jana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati, alipozungumza na Tanzania Daima, akijibu shutuma nzito zilizotolewa juzi na Dk. Kitine dhidi ya serikali.

“Sisi tunasema, yeye kama raia ana haki ya kutoa mawazo yake, na hiyo ndiyo demokrasia. Lakini si lazima kila anayetoa mawazo yake yawe sahihi. Mtu anaweza kujiuzulu nafasi yake kupisha uchunguzi ufanyike, hiyo haimaanishi kwamba hilo jambo amelifanya kweli.

“Uchunguzi unapofanyika kuna mambo mawili yanaweza kutokea, la kwanza huyo mtu anaweza kubainika alifanya hicho kitu na la pili anaweza kuonekana hana hatia.

“Hatuwezi kuwavua watu uanachama au nyadhifa zao ndani ya chama kwa sababu hiyo tu. Yeye aliyesema hivyo atutajie ni kiongozi gani wa serikali ambaye pia ni kiongozi wa chama, ameshathibitika kuwa hana maadili halafu kama chama tumeendelea kumwacha. Atuambie…..hakuna,” alisema Chiligati.

Alipoulizwa kwanini CCM isiwafukuze uanachama na kuwavua nyadhifa zao za kichama na ubunge, baadhi ya viongozi wake, ambao tayari serikali ya chama hicho ilisharidhika kwamba walikiuka maadili ya uongozi kwa kutumia vibaya madaraka yao, hata ikaamua kuwafungulia kesi, alisema: “Hatuwezi kuwachukulia hatua kwa sababu kesi zao bado ni tuhuma tu. Wakithibitika kama kweli walifanya hivyo, hatutawaacha,” alisema Chiligati.

Chiligati alipinga madai ya nchi kuongozwa kienyeji na kusisitiza kuwa kauli ya Dk. Kitine, haina ukweli wowote.

Alisema nchi inaongozwa vizuri kwa kufuata utawala wa sheria na mihimili yote ya dola, ikiwemo utawala, Bunge na Mahakama, inafanya kazi zake vizuri. Alibainisha kuwa kielelezo kuwa nchi haiongozwi kienyeji, ni amani na utulivu vilivyopo nchini, kwani kama nchi ingekuwa inaongozwa kienyeji kusingekalika.

“Kwa mfano, hilo alilosema nchi inaongozwa kienyeji, maana yake nini? Nchi kuongozwa kienyeji maana yake hakuna mfumo wa utawala kabisa, hakuna utawala wa sheria. Mahakama hazipo wala Bunge halipo…serikali haipo.

“Kungekuwa na hali hiyo, ingekuwa sawa na kusema nchi inaongozwa kienyeji. Lakini sisi hatujafikia hatua hiyo. Bunge lipo, Mahakama ipo, Serikali ipo. Utawala wa sheria. Nchi haiongozwi kienyeji, ndiyo maana kuna amani na
utulivu,” alisema Chiligati.

Mbali ya CCM kutoa kauli hiyo, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), aliunga mkono kauli ya Dk. Kitine.

“Mzee Kitine ameongea jambo ambalo ninaliongea kila siku kwamba, kuna tatizo kubwa serikalini. Tuhuma za ufisadi zimeshamiri sana, watendaji hawachukui maamuzi, wanasiasa wenye nyadhifa serikalini wamejaza nafasi na hawako tayari kuwajibika. Tunahitaji muafaka wa kitaifa kwenye mambo mengi,” alisema Zitto. Alisema ili mambo yaende vizuri, Tanzania inahitaji kelele za wazee wastaafu kama Dk. Kitine, wasimamie kunena na kushauri na hata kukemea na wananchi wawapigie kura wabunge wengi wa upinzani ili Bunge liwe na meno.

Juzi, Dk. Kitine alisema taifa linakabiliwa na tatizo la uongozi, ambalo halijawahi kutokea katika historia ya nchi. Kada huyo wa siku nyingi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), aliyewahi kuwa mbunge wa Makete, mkoani Iringa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, chini ya uongozi wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa, alisema nchi imekuwa ikiendeshwa kienyeji, kwa sababu ya kuporomoka kwa maadili ya uongozi.

“Hali tuliyofikia si nzuri, tena niseme ni mbaya sana. Kuna kuporomoka kwa kiasi kikubwa kwa maadili ya uongozi. Na hii nawaambia, nchi haijawahi kuwa katika hali mbaya huko nyuma kama ilivyo sasa. Kwa hali tuliyofikia ni ngumu kurekebisha maadili ya uongozi."

“Tatizo kubwa ni viongozi kukosa integrity (uadilifu). Kwanza ni integrity ya viongozi wenyewe, pili ni commitment (wito), tatu ni nationalism (utaifa). Haya ndiyo yalikuwepo wakati wa Mwalimu,” alisema Dk. Kitine. Alisema baadhi viongozi wa serikali wamepoteza sifa kuu tatu za uongozi ambazo ni kuwa na uadilifu, wito na kuweka mbele
utaifa, sifa ambazo alisema ndizo zilikuwa nguzo ya uongozi wakati wa Serikali
ya Awamu ya Kwanza, chini ya Baba wa Taifa, hayati, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Alisema uteuzi mbaya wa viongozi hususan uteuzi wa mawaziri, umechangia
kupatikana kwa viongozi wasio waadilifu, wengi wao wakijihusisha na vitendo vya rushwa

CHANZO: Tanzania Daima



IFUATAYO NI HABARI ILIYOBEBA MATAMSHI YA DR KITINE.

MKURUGENZI Mkuu mstaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa, Dk. Hassy Kitine, amesema taifa linakabiliwa na tatizo kubwa la uongozi, ambalo halijawahi kutokea katika historia ya nchi.

Kitine ambaye aliiongoza idara hiyo nyeti kwa karibu miaka 30 zama za Serikali ya Awamu ya Kwanza na ya Pili, alisema ukosefu huo wa uongozi umesababisha nchi iongozwe kienyeji.

Kachero huyo namba moja kwa miaka mingi, ambaye alilazimika kujiuzulu wadhifa wa uwaziri wa nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora) wakati wa utawala wa Benjamin Mkapa, mwishoni mwa miaka ya 1990 kutokana na kuhusishwa na kashfa ya mkewe kufuja fedha za umma kiasi cha shilingi milioni 40, alirejea kutoa kilio chake cha miaka mingi cha kuporomoka kwa maadili ya uongozi nchini.

Kitine ambaye aliwahi pia kuwa Mbunge wa Makete kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), alitoa matamshi hayo mazito katika viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam jana, alipozungumza na waandishi wa vyombo kadhaa vya habari.

“Hali tuliyofikia si nzuri, tena niseme ni mbaya sana. Kuna kuporomoka kwa kiasi kikubwa kwa maadili ya uongozi.Na hii nawaambia, nchi haijawahi kuwa katika hali mbaya huko nyuma kama ilivyo sasa. Kwa hali tuliyofikia, ni vigumu kurekebisha maadili ya uongozi.

“Tatizo kubwa ni viongozi kukosa integrity (uadilifu). Kwanza ni integrity ya viongozi wenyewe, pili ni commitment (wito), tatu ni nationalism (utaifa). Haya ndiyo yalikuwepo wakati wa Mwalimu,” alisema Dk.Kitine.

Akizungumza kwa kujiamini kama ilivyo kawaida yake, Kitine alisema viongozi wengi wa serikali wamepoteza sifa kuu tatu za uongozi ambazo ni kuwa na uadilifu, wito na kuweka mbele utaifa, sifa ambazo alisema ndizo zilikuwa nguzo ya uongozi wakati wa Serikali ya Awamu ya Kwanza, chini ya Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

“That was possible (hilo liliwezekana) chini ya Mwalimu. Kama alikuwa akifanya kosa, basi kosa hilo lilikuwa likitokea tu wakati akifanya jambo kwa ajili ya kuwasaidia Watanzania. "

“Philosophy (falsafa) ya Mwalimu, ilikuwa kwanza Mungu, pili Tanzania, halafu yeye binafsi. Kila kiongozi anayetofautiana na Mwalimu tu hulifikisha taifa hili kubaya, if you differ with him, utaishia kubaya,” alisema Dk. Kitine akionyesha hali ya masikitiko.

Alisema uteuzi mbaya wa viongozi, hususan ule wa mawaziri, umechangia kwa kiasi kikubwa kupatikana kwa viongozi wasio
waadilifu, wengi wao wakijihusisha na vitendo vya rushwa. “Haiwezekani viongozi wakateuliwa kwa misingi ya mitandao …sijui, kwa msingi wa politics of division (siasa za makundi) ndani ya chama. Haiwezekani nchi ikaendeshwa kienyeji. Integrity should be number one (uadilifu unapaswa kuwa kitu cha kwanza kuzingatiwa). "

“Mtu anajiuzulu, anafukuzwa uwaziri kwa sababu ya kashfa, kwa sababu ya kukosa maadili, halafu anabakia kuwa mbunge na mjumbe wa kamati kuu ya chama, nini hii? Hii haifai. Waziri akikosa uadilifu anatakiwa aondolewe mara moja nyadhifa nyingine zote alizobakiwa nazo. Nadhani hii itasaidia,” alisema Dk. Kitine pasipo kutaja jina la kiongozi yeyote.

Kitine ambaye wakati wote wa mazungumzo yake alisema alikuwa anataka kujadili masuala muhimu na si watu, alieleza namna asivyo na imani na hatua zinazochukuliwa na serikali katika kukabiliana na tatizo la rushwa kubwa. Kwa mujibu wa kachero, mwanasiasa na mwanazuoni huyo, hatua hizo ambazo zinahusisha baadhi ya watu wenye majina makubwa kufikishwa mahakamani, zimechukuliwa kwa ajili tu ya maandalizi ya uchaguzi ujao.

“Nilikuwa kiongozi wa kwanza kuzungumzia rushwa kubwa miaka 10 iliyopita. Nilisema ndiyo inayovuruga uchumi kuliko hata rushwa ya
nesi, hakimu, polisi,.… hakuna hata mkubwa mmoja aliyekamatwa. Ilinigharimu sana, na mimi nilipata adhabu ya kuzuiliwa kikao kwa miezi miwili, kama huyu nani huyu, Zitto (Kabwe). Wakati huo ilikuwa ndani ya CCM".

“Mimi nadhani hatua hizi zinazochukuliwa hazilengi kukomesha tatizo la rushwa, ni siasa tu za uchaguzi,” alisema Dk. Kitine.

Alipoulizwa nini kifanyike ili kukabiliana na tatizo hilo la uongozi mbaya, pamoja na mambo mengine, alielekeza changamoto zake kwa Idara ya Usalama wa Taifa.

“Usalama wa Taifa should be completely clean (unapaswa kuwa safi kabisa). Idara hii inatakiwa kuwa, juu ya mambo ya rushwa, iwe safi kabisa. Usalama wa Taifa ndiyo unayoteua viongozi, ndiyo inayoshirikiana na rais kwa kumshauri katika kuteua mawaziri. Sasa kama Usalama wa Taifa ukiwa mchafu ndio tunapata viongozi wala
rushwa. Nafikiri vigezo vinavyotumika kuteua viongozi pia vina matatizo,” alisema Dk. Kitine.

Kada huyo wa CCM ambaye kitaaluma ni mchumi na mwanasheria, akizungumzia hali ya uchumi nchini, alisema kwa kiasi kikubwa uchumi umeshikiliwa na wageni kuliko wazawa, na kuelezea kusikitishwa kwake juu ya kuwepo kwa pengo kubwa kati ya matajiri na maskini.

Akitoa mfano alisema, miongoni mwa mambo yanayoonyesha kuparaganyika kwa mambo ni kukithiri kwa idadi ya ombaomba mitaani. “Mwalimu asingeruhusu watu hawa waombeombe barabarani. Kazi za Watanzania ni udereva teksi, daladala, mabasi, kazi ya uboi ndani ya nyumba na kazi ya kufagia barabarani. Hizi ndizo kazi za Watanzania na hawa ndio wenye mali."

“Uchumi huu wa Watanzania si wa kwao. Watanzania ambao ni matajiri hawazidi hata watano. Hakuna sera bora za kusaidia kutumia
maliasili zetu ili zitupe fedha ya kujenga shule, madaraja, hospitali…..”
alisema Dk. Kitine. Akizungumzia utendaji wa kazi wa Bunge katika kusimamia utendaji wa serikali, Kitine alisema kazi inayofanywa na taasisi hiyo hivi sasa ni kubwa kuliko ilivyopata kuwa wakati wowote huko nyuma.

Hata hivyo katika kuusifia utendaji wa kazi wa Bunge, aliupongeza mchango mkubwa na muhimu wa wabunge wa upinzani katika kuiimarisha taasisi hiyo muhimu. “Ni Bunge zuri kuliko lilivyowahi kuwa huko nyuma. Linaonyesha kila dalili za uhuru. Upinzani unafanya kazi nzuri. Bunge liko wazi zaidi na wabunge wanatoa michango mingi yakinifu, yenye manufaa kwa taifa. Likiendelea hivi tutafika mahali pazuri,” alisema
.

CHANZO :Tanzania Daima



WELL SAID!

18 Nov 2007

Soma makala nyingine mbili hapa

Asalam aleykum,

Moja ya mambo nayopendelea kufanya pindi muda unaporuhusu ni kuangalia runinga.Lakini naweza kusema kwa kujiamini kabisa kwamba mahaba yangu kwa runinga yamekuwa ni sawa na mithili ya kuingia darasani kwani ni nadra kwangu kupitisha siku nzima pasipo kujifunza kitu kipya kwenye runinga.Hiyo haimaanishi kwamba kila kipindi nachoangalia kina jambo jipya au la maana,bali najitahidi kuwa makini katika uchaguzi wa kile nachoangalia.Halafu nimejenga desturi ya kuangalia runinga huku laptop yangu ikiwa pembeni.Hiyo huwa inanirahisishia kufanya “reference” ya kitu nachokiona kwenye runinga lakini pengine hakijafafanuliwa vizuri.Inapotokea hivyo basi huwa naingiza neno husika kwenye mtambo wa kusaka habari kwenye mtandao ujulikanao kama “Google” au nakimbilia kwenye tovuti nyingine maarufu kwa maelezo ya watu na vitu ijulikanayo kama “Wikipedia”.

Kitu kimoja nilichojifunza kuhusu vipindi vya televisheni hapa Uingereza ni namna mashindano ya kupata watazamaji yalivyo juu.Kutokana na mashindano hayo,vituo vya televisheni hujitahidi kuja na ubunifu wa kila namna,wa maana na wa kipuuzi.Na miongoni mwa ubunifu huo ni hivi vipindi vinavyojulikana kama “reality tv” ambavyo kwa tafsiri isiyo rasmi ni vipindi vinavyoonyesha maisha katika uhalisi wake.Sintoingia kwa undani sana kuelezea maana ya vipindi vya namna hiyo kwani nilishawahi kuviongelea katika makala yangu moja huko nyuma.Ila kwa kukumbushia tu,katika makala hiyo nilizungumzia mbinde iliyojitokeza kwenye kipindi cha “celebrity big brother”,yaani “Big Brother” kama hiyo aloshinda Richard lakini wahusika wake wanakuwa “watu wenye majina” (celebrities).Hiyo ni “version” (aina) tofauti ya “Big Brother” ya kawaida ambayo kwa mwaka huu iliweka historia ya kupata mshindi Mweusi,Brian,Mwingereza mwenye asili ya Nigeria.Katika “Celebrity Big Brother” iliyopita kulizuka migogoro wa ubaguzi wa rangi dhidi ya stta wa filamu za Kihindi,Shilpa Shetty,ambapo washiriki watatu wakiongozwa na mshindi wa zamani wa “Big Brother” (ya kawaida) Jade Goody,walitoa matamshi kadhaa yaliyoashiria ubaguzi wa rangi.Zilipigwa kelele nyingi sana na nusura mashindano hayo yavunjike kabla ya muda wake,lakini yalifanikiwa kumalizika salama ambapo Shilpa aliibuka mshindi.Sokomoko hilo lilifika hadi bungeni na wakati flani Gordon Brown (Waziri Mkuu wa sasa) akiwa ziarani nchini India alilazimika “kuwaomba radhi” Wahindi kwamba yaliyomkuta Shilpa katika jumba la “Big Brother” sio taswira halisi ya jamii ya Waingereza.

Sokomoko la ubaguzi wa rangi katika kipindi hicho lilipelekea baadhi ya watu kuhoji umuhimu wa vipindi vya namna hiyo na faida yake kwa jamii.Lakini pia lilizua swali moja la msingi,je panapojitokeza vipindi vya kipuuzi namna hiyo wa kulaumiwa ni nani?Waandaaji au watazamaji?Kwamba kama waandaaji watakuwa makini basi ni dhahiri hakutakuwa na upuuzi katika vipindi wanavyoandaa.Lakini pia iwapo kipindi kitaonekana cha kipuuzi basi watazamaji wanaweza kukisusia hivyo kuwalazimisha waandaaji kukirekebisha au kukiondoa kabisa hewani.Ikumbukwe kwamba kwa nchi za Magharibi,vyombo vya habari vinahangaika sana kupata “ratings” nzuri,yaani idadi kubwa ya watazamaji au wasomaji.Wapo wanaodhani kuwa “ratings” zimekuwa zikichochea sana vyombo vya habari kukurupuka na habari zenye utata au za kusababisha mgongano kwani sote twafahamu kuwa “mbwa kung’ata mtu sio habari lakini mtu kung’ata mbwa ni zaidi ya habari”.Yaani kwa kifupi,utata “unalipa sana” kwenye habari.

Nije kwenye “Big Brother” ya akina Richard.Binafsi sikuwa nafuatilia kwa karibu japo ilipokuwa inaelekea ukiongoni nilijikuta natamani Mtanzania mwenzetu Richard ashinde.Lakini tukiwa wakweli na waadilifu,tunaweza kweli kujibu kwa uhakika nini cha msingi tulichojifunza kutokana na mashindano hayo?Hivi kuna lolote la maana la kujifunza pale mshiriki mmoja anapolewa chakari na kuishia kufanya tendo la ndoa huku anafahamu bayana kuwa kamera zinarekodi tukio hilo laivu?Naamini kuna wenzangu wengi tu ambao “Big Brother” kwao ina umuhimu mdogo kuliko hata vichekesho vya kikundi cha “Ze Comedy” ambavyo kwa kiasi flani vinafikisha ujumbe muhimu katika namna ya kuvunja mbavu.Sina tatizo na ushindi wa Richard,ila tatizo langu ni mantiki nzima ya “Big Brother”.

Lakini kama nilivyosema awali kuwa “mtu akimng’ata mbwa inakuwa zaidi ya habari”.Pengine laiti “Big Brother” ikiondoa “manjonjo” ya ngono za hadharani na uchafu mwingine inaweza kupoteza umaarufu na si ajabu ikafutiliwa mbali baada ya muda mfupi.Nadhani vimbwanga vinavofanyika kwenye jumba hilo vinachangia sana kuongeza umaarufu wa kipindi hicho.Kwa bahati mbaya,vimbwanga hivyo havina umuhimu wowote,sio kwa washiriki pekee bali hata kwa watazamaji.Pia nadhani ngono ndani ya jumba la “Big Brother” inaweza kufunua unafiki wa namna flani wa wenye majukumu ya kulinda maadili ya jamii yetu.Nilisoma mahala flani habari kwamba video ya wimbo “Simama Tucheze” wa Q-Chief imepigwa stop kuonyeshwa katika vituo vya runinga kwa vile imejaa vitendo vya ngono.Japo siungi mkono video zenye kuonyesha vitendo vya ngono lakini kinachonifanya niwatolee mimacho “askari wetu wa maadili” ni namna wanavyoweza kufumbia macho matendo ya ngono kwenye jumba la “Big Brother” lakini wanadiriki kumkalia kooni Q-Chief.Na si hapo tu,kama msomaji mpendwa utakuwa msikilizaji wa vipindi vya miziki (hususan vile vya mchana) nadhani utakuwa umeshasikia baadhi ya tungo za muziki wa kufokafoka (hasa wa Marekani) ambazo “hazijachujwa” na hivyo kujumuisha maneno yasiyofaa katika maadili ya jamii yetu.Kwa kawaida na kwa kuzingatia ujumbe uliomo,nyimbo za kufokafoka hutolewa katika “versions” mbalimbali lakini nazozungumzia hapa ni “radio version” (ambapo “maneno machafu” huwa yamefutwa,yamehaririwa-edited-au yameminywa) na “dirty version” (ambapo kila neno linasikika bila kujali “makali” yake).Inawezekana watangazaji wanaopiga “dirty versions” radioni huwa hawajui kinachoongelewa katika nyimbo hizo au wanajua lakini hawajali kwa vile “askari wa maadili” hawana muda wa kufuatilia.

Kabla ya kuandika makala hii nilisoma Sera ya Taifa ya Utamaduni ambayo inaharamisha waziwazi burudani zinazoendana kinyume na maadili ya jamii yetu.Lakini nadhani ufuatiliaji ni mdogo kwani hata video za baadhi ya nyimbo za wakongomani (Wazaire) ni “chafu” mno kuzionyesha kwenye runinga.Na kama unadhani hiyo ni ndogo basi nenda kajionee “ubunifu” wa bendi zetu katika suala zima la unenguaji.Amin nakuambia,namna baadhi ya wanenguaji wanavyocheza ni mithili ya kuangalia filamu ya “X”.Ukilogwa kwenda na mama mkwe kwenye shughuli kama hizo basi unaweza kujikuta unamtaka radhi kwa namna wanenguaji “wanavyojituma”.

“Askari wa maadili” wanakabiliwa na changamoto nyingine kubwa ya kudhibiti watazamaji wenye umri mdogo kwenye shughuli “za watu wazima”.Kwa hapa Uingereza,ili kijana aweze kuingia kwenye ukumbi wa disko ni lazima awe na kitambulisho kinachoonyesha kuwa umri wake unamruhusu kuingia humo.Na hilo ni hata kwenye kununua pombe na sigara.Sheria iko wazi na inasomeka kwenye kila duka kwamba ili mteja anayeonekana kuwa na umri mdogo aweze kuuziwa bidhaa anapaswa kuthibitisha umri wake.Lakini kwa huko nyumbani ni suala la kawaida kumwona mtoto mdogo kabisa akiwa na “michupa kadhaa ya bia” akielekea grosari au baa kwenda kununua bia.Hivi lile zoezi la kuanzisha vitambulisho vya taifa limefikia wapi?Je vitambulisho hivyo vitaonyesha umri wa mwenye kitambulisho?Nadhani mpango huo utakapokamilika basi inaweza kuwa rahisi kwa “askari wa maadili” kuanza kudhibiti watoto na vijana wenye umri mdogo wasiruhusiwe kuingia sehemu zinazoweza “kuwazibua akili” au kuwabana kununua bidhaa kama bia au sigara.

Pengine kabla sijamalizia makala hii utakuwa unajiuliza tangu lini jeshi la polisi limekuwa na kitengo cha “askari wa maadili”.Well, “askari wa maadili” ni pamoja na mamlaka zinahusika na kuhakikisha maadili ya jamii hayavunjwi,kuupuuzwa au kupindwa.Wahusika wengine ni wazazi,kaka,dada,mabaunsa wanaoruhusu watu kuingia disko,wauza maduka na baa,bila kusahau mimi na wewe.

Alamsiki




Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.