14 Jan 2011


Kuna msemo wa kiswahili kuwa mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.Naomba niende moja kwa moja kwa kuhusisha msemo huu na mahusiano ya kibaradhuli kati ya vyombo vya dola na Serikali ya CCM chini ya utawala wa Jakaya Kikwete.Katika msemo wetu,Serikali inaweza kulinganishwa na baba,huku vyombo vya dola vikilinganishwa na mtoto. Na hapa sina nia ya kuonyesha undugu uliopo kati ya vyombo hivyo vya dola na CCM iliyozaa serikali tuliyonayo (hata kama ni kwa uchakachuaji).

Serikali ya Kikwete haina tatizo kuona vyombo vya dola vikikiuka maadili ya kazi yao alimradi kwa kufanya hivyo,yeye kama Rais,chama chake na maswahiba wake mafisadi wanaendelea kufakamia keki ya taifa pasipo usumbufu.

Kwa mfano,Kikwete na serikali yake haisumbuliwi na ukiukwaji wa hali ya juu wa haki za binadamu unaofanywa na jeshi la polisi.Na hapa sijagusia mauaji ya huko Arusha na haya ya hivi punde huko Mbarali,Mbeya.Hapa nazungumzia namna haki za msingi za Watanzania wa kawaida (wasio vigogo au mafisadi) zinavyofinyangwa na askari polisi kila kukicha.Madereva na makonda wa daladala ambao wanalazimika "kuziba pengo kati ya kipato halisi cha askari trafiki na mahitaji ya kawaida kwa siku/wiki/mwezi".

Sote tunajua ni rahisi zaidi kugema damu kwenye jiwe kuliko askari Trafiki kumpongeza "suka" (dereva).Sasa nini kinaendelea katika picha hiyo kati ya "maadui" hawa?
Rushwa kwa trafiki imekuwa ni sehemu ya sheria za usalama barabarani,na ndio maana kila kukicha ajali zinaendelea kugharimu maisha ya abiria wasio na hatia.Unategemea nini kama askari mla rushwa anaweza kuruhusu basi lenye injini ambayo hata kwenye trekta haifai?

Unapozungumzia amani na utulivu wa Tanzania,unaweza kuwa umeshahau nini kilichotokea mara ya mwisho ulipokutana na askari polisi wakiwa "kazini".Unless una undugu au ukaribu na kigogo au fisadi flani,ni dhahiri kuwa polisi wetu watatumia mbinu zote za medani kuhakikisha unawapa fedha.Ukibisha,utapigwa na kutumbukiziwa kete ya bangi kama sio cocaine feki.Askari hawa ambao wengi wao hawakujiunga na jeshi hilo kwa vile wanaipenda sana nchi yetu bali kwa sababu ya aidha ugumu wa ajira au wazazi kumwadhibu mtoto mtukutu kwa kumwingiza katika ajira ya polisi.

Hili kundi la pili ni la hatari zaidi kwa sababu linajumuisha watu wenye jeuri ya "baba ni flani" na wanajua hata "wakilikoroga" hakuna wa kuwaadhibu.Pia ni viumbe hatari zaidi kwa vile sababu ya wazazi wao kuwaunganishia ajira ndani ya jeshi hilo ni "kushindikana" kwao katika familia zao.Hawa ni binadamu ambao laiti uchunguzi wa kubaini ufanisi wa kiakili na uwezo wa mwajiriwa mtarajiwa ungefanyika (au ungefanyika bila kupindisha matokeo) wasingepatiwa ajira mahala popote pale.Unatarajia nini kutoka kwa binadamu ambaye kichwa chake kimegeuka ulingo wa vita kati ya ubongo na moshi wa bangi?


Lakini tukiweka kando matatizo binafsi ya askari polisi wetu,hebu fanya ziara kwenye makazi yao kisha jiulize mood watakayokuwa nayo kazini!Yayumkinika kusema kuwa miongoni mwa watumishi wa umma wanaoishi katika hali ya udhalilishaji mkubwa ni askari polisi.Sasa badala ya wao kuelekeza hasira zao kwa mwajiri wao,wanaelekea kuhamishia hasira hiyo kwa kila Mtanzania "wa kawaida".Njaa na dhiki zao zinakuwa kichocheo cha chuki yao dhidi ya walalahoi.Kwa upande mmoja,wamewageuza walalahoi hao kuwa shamba lao la kuchuma rushwa,na kwa upande mwingine wamewageuza sehemu za kutolea hasira zao za manyanyaso wanayovumilia kutoka serikalini.


Makazi ya polisi Msimbazi

Serikali ya Kikwete na CCM yake haina cha kupoteza (at least kwa sasa) kwani malalamiko ya askari polisi kuhusu maslahi duni yanapunguzwa na "ruhusa" waliyopewa kuchuma kipato kwa walalahoi,sambamba na kuhalalishiwa viumbe wa kumalizia hasira za askari hao.


 
Kilichonifanya niandike makala hii ni tamko la Jeshi la Polisi kuhusu mauaji waliyofanya huko Arusha.Ukiangalia juu juu,unaweza kudhani wanajitetea tu.Lakini ukiingia kwa undani zaidi utabaini kauli hiyo ni dalili za wazi za kiburi kinachoanza kujitokeza kutoka kwa "mtoto aliyekosa malezi bora".

Kwanini nasema hivyo?Kwanza Rais Kikwete alitoa kauli ya kizushi kwa mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania na kudai kuwa "MAUAJI YA ARUSHA NI BAHATI MBAYA".Nilishalizungumzia hilo kwa mapana zaidi HAPA .Jumatatu iliyopita,Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,Bernard Membe alijaribu kutuliza hasira za Watanzania kwa kukiri bayana kuwa Jeshi la Polisi lilikiuka maadili ya kazi yao, lilipokuwa likikabiliana na raia waliokuwa wakiandamana kupinga suala la uteuzi wa meya wa Arusha.

Lakini katika kile blogu hii inatafsiri kuwa JEURI,KICHWA NGUMU na UBABE,jana jeshi hilo lilitoa tamko ambalo haihitaji elimu yoyote kufahamu kuwa ni jibu lao kwa Membe.Katika tamko hilo la kihuni,jeshi hilo sio tu linahalalisha ukatili na uonevu uliopelekea vifo vya mashujaa wawili na majeruhi luluki,pia linafanya mzaha mbaya kwa kudai ni viongozi wa Chadema waliosababisha vurugu na mauaji (kana kwamba viongozi hao ndio waliofumua risasi zilizoua na kujeruhi).

Haihitaji kuumiza kichwa kujiuliza tamko hilo la jeshi la polisi limetolewa na nani.Forget about yule mbabaishaji aliyesimama mbele ya waandishi wa habari kusoma tamko hilo.Huyu alikuwa anatimiza agizo la bosi wake,yaani Inspekta Jenerali wa Polisi, Said Mwema.Ni Mwema ambaye haafikiani na kauli ya Membe kuwa jeshi hilo lilikiuka maadili.Na kwa vile Mwema ni "mungu wa polisi" basi msimamo wake automatically unakuwa msimamo wa jeshi hilo.Na Mwema ni "mungu-mtu" kweli hasa baada ya kujipachika jukumu la kutoa uhai wa binadamu (kama ilivyotokea huko Arusha na sasa huko Mbarali).

Lakini je Mwema anapata wapi jeuri hiyo ya kupingana na kauli ya Membe,ambaye katika uhusiano wa kimataifa,ni kama mwakilishi mkuu wa Rais katika mahusiano kati ya Tanzania na mataifa mengine duniani?Jibu jepesi lipo katika uhusiano wa karibu uliopo kati ya Mwema na aliyemteua,yaani Rais Kikwete.Mwema anaweza kusema lolote lile lakini Kikwete hawezi kumfukuza kazi.Na sio kwa sababu Kikwete ni dhaifu na mgumu wa kufukuza kazi watendaji wazembe,bali ni huo uhusiano wa karibu kati ya wawili hao.

Sijui kicheko hicho kinahusiana na usalama wa raia au mengineyo

Je inawezekana Kikwete anatuchezea shere kwa kumwelekeza Membe aseme hili kisha kumwambia swahiba wake Mwema aseme tofauti?Nahoji hivyo kwa vile sidhani kama kauli za Membe na Mwema hazina baraka za Kikwete.Ikumbukwe pia kuwa Kikwete na Membe ni "washkaji" mno,huku ikielezwa kuwa Membe alimsaidia sana Kikwete kukubalika ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa wakati wa kinyang'anyiro cha uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.

Ushkaji

All in all,Kikwete na Serikali yake ya CCM wanapaswa kutambua kuwa wanacheza mchezo hatari sana ambao unaweza kupelekea balaa kubwa huko mbeleni.Of course,wengi wetu tunafahamu kuwa kuna ombwe kubwa la uongozi linalosababishwa na uwezo duni wa Kikwete katika medani ya uongozi,lakini pengine ni vema akajiweka kando badala ya kuitumbukiza nchi yetu kwenye mtaro wa kupotea kwa amani.

Kikwete anaendesha nchi katika namna ileile anavyoendesha CCM ambapo hana hata nguvu ya kuwakemea wasema-ovyo wa Chama hicho wanaoongozwa na Yusuph Makamba,Tambwe Hizza na mropokaji brand new Mary Chatanda.Sijui anahofia akiwakemea watamgeuka na kutoboa siri ambazo hataki umma ufahamu!Yaleyale ya akina Rostam na Lowassa.Hawa wanamjua Kikwete in and out,na Kikwete anatambua kuwa akiwatibua tu,amekwisha.Yaani kwa kifupi,uongozi wa Kikwete ni kama umewekwa rehani vile.



Sijui kesho au keshokutwa watakurupuka na lipi jipya kuhusu mauaji ya binadamu wasio na hatia.Midomo inawaruhusu kusema lolote lile,na vyombo vya habari vya KURIPOTI BILA KUCHAMBUA vitajibidiisha kurusha habari hizo.Lakini,wakati wanaendelea kubwatuka,ni muhimu wakaitafakari kwa makini kauli ya Paroko wa Parokia ya Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi, Padre Henry Mushi aliyetanabaisha kuwa damu ya vijana waliouawa kwa kupigwa risasi na Polisi Jijini Arusha, itawaandama polisi waliouhusika katika maisha yao yote.

Namnukuu
"...polisi waliohusika na mauaji hayo, hawawezi kujitetea kuwa walitumwa kwani wao sio mashine kiasi cha kuua raia bila kutafakari...Tendo la kumwaga damu lililotokea Arusha ni baya na yeyote aliyefanya kitendo hicho damu hiyo itamsumbua kama ilivyomsumbua Kaini…Huyo aliyefanya hivyo naye atafuata njia hiyo hiyo...wewe ni binadamu sio mashine kwa hiyo hata kama utasema ulitumwa kufyatua risasi lakini, wewe unayepiga risasi ndiye utakayeulizwa mbele za Mungu kwa kushindwa kutafakari...polisi aliyefanya kitendo hicho asifikiri atajificha mbele ya uso wa Mungu"


“Huyo aliyefanya kitendo hicho hatujui yuko wapi lakini afahamu yuko chini ya Mwanga wa Mungu na njia pekee ya kuepuka hasira ya Mungu ni kutubu dhambi hiyo vinginevyo damu aliyoimwaga itaendelea kumsumbua,”

Padre Mushi alitoa kauli hiyo kijijini Makiidi wilayani Rombo wakati wa ibada maalumu ya mazishi ya mmoja wa wafuasi wa Chadema aliyeuawa katika tukio hilo, Dennis Shirima.



Pichani ni Jeshi La Polisi Tanzania likiwa KAZINI.Hii ilikuwa huko Arusha ambapo WALIUA,na sasa WAMEUA TENA huko Mbeya.

Brandy Nelson, Mbeya na Ramadhan Semtawa

POLISI nchini wameendelea kutumia risasi za moto dhidi ya raia na jana wanadaiwa kuwauwa watu wawili kwa kuwapiga risasi katika vurugu zilizotokea katika wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.

Habari kutoka Mbarali zinasema polisi walitumia mabomu ya kutoa machozi na risasi za moto kuzima vurugu ambazo chanzo chake ni mabishano baina ya raia na polisi hao.

Vurugu hizo zilizotokea jana majira ya saa nane mchana zinadaiwa kusababishwa na baadhi ya wakazi wa kata ya Ubaruku kuzuia kuingia katika eneo lao lori lenye uzito wa zaidi ya tani kumi.

Baadhi ya walioshuhudia tukio hilo walisema hatua ya wananchi kuzuia kwa lori hilo inatokana na kuwepo kwa amri ya serikali wilayani Mbarali itayokataza magari yenye uzito mkubwa wa zaidi ya tani kumi kuingia katika kata ya Ubaruku.

Mmoja wa mashuhuda hao alisema lori hilo lilipokuwa likijaribu kuingie katika eneo hilo wananchi walianza kulizuia huku wakimhoji dereva wake sababu za kuvunja amri iliyopo.

“……walipokuwa wakiendelea kuhojiana na dereva, polisi walifika hapo na hapo wananchi wakaanza kuwauliza polisi sababu za kuruhusu gari kuingie katika eneo lao wakati serikali imeishakataza..,” alisema shuhuda huyo na kuongeza:

“ ni kama polisi na wananchi walishindwa kuelewana lugha hapo tukaanza kusikia mabomu ya machozi na risasi…”.

Alisema hatua ya polisi iliwafanya wananchi kutawanyika na wengine kuanza kuyavamia magari yaliyokuwa kwenye kituo cha mafuta likiwemo gari lililosababisha mvutano huo.

Katika tafrani hiyo magari mawili yaliyokuwa kwenye kituo cha mafuta yalichomwa moto. Magari hayo yanasadikiwa kuwa ni mali ya ndugu wa mwekezaji katika shamba la mpunga la Mbarali.

Mkuu wa Wilaya ya Mbarali, Kanali Cosmas Kayombo alipohojiwa alikiri kupata taarifa hizo lakini akadai kwamba yuko mbali na tukio hilo na amedai kuwa amewasiliana na mbunge jimbo la Mbarali Dickson Kulufi afike eneo la Tukio.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Mbeya Advocate Nyombi alipohojiwa alisema kuwa analifuatilia tukio na mpaka tunakwenda mitamboni tayari gari nne mbili zikiwa zimebeba askari wa kutuliza ghasia (FFU), moja ikiwa imebeba polisi waliovalia kiraia huku wakiongozwa na king`ora kikipiga kelele zikiwa zinaelekea eneo la tukio.

CHANZO: Mwananchi


Katika moja ya maeneo machache ambayo Watanzania tumepiga hatua ya kuridhisha ni fani ya kublogu.Ni vigumu kufahamu idadi kamili ya mabloga wa-na blogu za- Kitanzania (ndani na nje ya nchi) lakini haihitaji sensa kutambua kuwa idadi ni ya kuridhisha.Iwapo idadi hiyo inaendana na matarajio ya wasomaji,hilo ni suala jingine.

Kwa haraka haraka,ni rahisi pia kutambua blogu za picha (zinazoambatana na habari) ndizo zinazotamba zaidi.Pengine ni kwa vile,kama wasemavyo, "PICHA MOJA INAWEZA KUWAKILISHA MANENO ELFU MOJA".Lakini inawezekana pia kuwa wasomaji wetu wengi wako bize,na hawana muda wa kusoma makala ndefu kwenye blogu kama hii.Kadhalika,na hili nalitamka kwa uangalifu mkubwa,huenda kuna kundi dogo la wenzetu ambao kwa mtizamo wao,kusoma ni mithili ya self-inflicted third degree torture.

Blogu hii ina umri wa miaka mitano kasoro miezi mitatu (ilizaliwa mwezi April 2006).Ukiangalia idadi ya wasomaji wanaoitembelea (visitors),unaweza kudhani imeanzishwa miezi michache tu iliyopita.Kuna blogu kadhaa zenye visitors milioni kadhaa,na baadhi yao zina umri haba kulinganisha na wa blogu hii.

Unaweza kudhani inakatisha tamaa.Hapana.Binafsi,naamini nina kundi dogo la wasomaji "tunaoelewana".Yaani namaanisha wasomaji ambao kwa kiasi kikubwa wanaafikiana na dhima kuu ya blogu hii: harakati za haki kwa jamii na mapambano dhidi ya uhujumu uchumi,ukiukwaji haki za binadamu na utawala bora.Haimaanishi kuwa wasomaji hao wanaoiamini blogu hii wanaafikiana na kila nachoandika.Hapana.Kuna nyakati tunatofautiana kimtazamo,na wengi wao huwa huru kunikosoa au kutoa mawazo tofauti na yangu.Of course,kuna nyakati,baadhi ya wasomaji huamua kutumia lugha isiyofaa kuwasilisha ujumbe/mtizamo wao.Hizo ni changamoto katika maisha kwani ukiona kila kitu kinakwenda sawia basi huenda kuna walakini mahala flani.

Of course,ingependeza kuona blogu hii nayo ina visitors milioni 5 au zaidi.Lakini what if kati ya hao,ni asilimia ndogo tu wanaochukulia kwa makini ujumbe uliomo bloguni hapa?Kwangu,idadi ya visitors hainusumbui kwa vile naamini nina kundi dogo la wasomaji makini ambao wanaichukulia blogu hii kama kiwanja chao cha mazoezi kwa ajili ya mapambano ya kusaka uhuru wa pili wa Tanzania,sambamba na kuhabarishana kinachojiri kwenye korido za watawala wetu.

Enewei,kisa cha kuandika post hii ni mfadhaiko nilioupata siku chache zilizopita pale nilipotuma post (niliyoichapisha hapa) kwa bloga mwenzangu wa picha-habari.Kuna nyakati huwa naona umuhimu wa kufikisha ujumbe wangu kwa wasomaji wengi zaidi,hususan wale wapenda picha lakini sio habari.Na kwa kutambua kuwa blogu ya rafiki yangu huyo inatembelewa na wasomaji wengi kuliko hii,na pia kwa vile alishatoa wazo la kumtumia angalau makala moja kwa wiki,nikaona hakuna ubaya wa kumtumia post hiyo.

Cha kusikitisha,sio tu hakuichapisha bali amekuwa akikwepa hata meseji nazomtumia (sio kumkumbushia kuhusu post husika bali mawasiliano yetu ya kawaida tu).Nafahamu kuwa baadhi ya "waswahili" wanapata wakati mgumu sana kuwa wawazi na wakweli kusema "samahani,hii haiendani na hadhi ya blogu yangu".Mhusika anadhani kukaa kimya kutapelekea mie kusahau ombi langu kwake,na ishu itamalizika kienyeji.

Najua kwanini bloga huyo aliogopa kuchapisha post niliyomtumia.Anaogopa mamlaka.Lakini uoga wa nini wakati kilichoandikwa si mawazo yake?Binafsi,kuna nyakati huwa natumiwa habari au matangazo mbalimbali,na ninachofanya ni kuyatundika sambamba na kubainisha chanzo au mtumaji.

Ushirikiano ni muhimu kwa mabloga hasa kwa vile yawezekana mwenzangu hana nilichonacho,nae anacho kile ambacho mie sina.Wingi wa idadi ya visitors isiwafanye  baadhi ya "mabloga wenye majina makubwa" (kama huyu rafiki yangu nayemzungumzia hapa) wajisahau kuwa sisi kama wanadamu ni wanyama tunaohitaji sana ushirikiano (social animals).Na sio lazima ushirikiano huo uwe kwenye kublogu pekee bali mambo mbalimbali yanayotugusa binafsi au jamii kwa ujumla.

Enewei,simlaumu ndugu yangu huyo kwa vile kama ilivyo katika blogu hii,yeye pia ana haki yake ya kikatiba kutochapisha kitu anachoona hakiendani na maudhui ya blogu yake.Lakini,japo pia ni haki yake ya kikatiba,kufanya dharau si jambo la kiungwana.Kunifahamisha kuwa "aah ndugu yangu ile kitu naona inaweza kuniletea matatizo..." sio kauli ngumu,hasa ikitolewa kwa njia ya meseji.

Well,wakati tunaanza mwaka mpya ni vema kufanya inventory ya kuangalia watu walio na umuhimu kwako na wale ambao wanaongeza tu idadi.Namshukuru ndugu yangu huyu kwa kunirahisishia zoezi hilo.



13 Jan 2011

Baadhi ya Makamanda wa ngazi za juu wa Jeshi la Polisi Makao Makuu, wakiangalia sehemu ya video iliyokuwa ikionesha jinsi Polisi walivyokuwa wakituliza ghasia huko Arusha.


Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi nchini, Kamanda Paul Chagonja akizungumza na Waandishi wa habari katika Makao makuu ya Jeshi hilo leo



TAARIFA YA JESHI LA POLISI


MSIBA WA MASHUJAA WALIOUAWA KWA AMRI YA DIKTETA JAKAYA KIKWETE

 











































































SARAFINA THE FUNERAL SONG



PICHA NA VIDEO KWA HISANI KUBWA YA MTANDAO NAMBARI WANI Jamii Forums.KWA HABARI KAMILI SOMA HAPA.

11 Jan 2011



Pengine wakati uongozi wa Chadema mkoani Pwani ulipochukua uamuzi wa kuahirisha mkutano wao wa hadhara-baada ya "intelijensia yao kubainisha kuwa jeshi la polisi lilikuwa na njama za kuzusha zahma kama ile ya Arusha-hawakufahamu kuwa actually wanavumbua mbinu inayoweza kuwatwanga misumari wadhalimu pale inapouma zaidi (hitting where it hurts most).

Ofkozi,yayumkinika kuamini kuwa Chadema mkoani Pwani waliingia gharama kuandaa mkutano huo,na kuuahirisha kumewatia hasara.Lakini ni dhahiri kuwa upande uliopata hasara kubwa ni Serikali iliyoamua kutuma rundo la askari kwenda "kutoa kipigo" kwa wananchi wasio na hatia,lakini target ikayeyuka.

Mbinu hii inaweza kuwa na ufanisi mkubwa.Kutangaza maandamano au mkutano mkubwa,kisha kama kawaida Serikali inaingia gharama za kuandaa operesheni ya kwenda kuangamiza watakaohudhuria maandamano/mkutano husika,lakini hatimaye nguvu ya tembo kukanyaga sisimizi inaishia kukanyaga hewa tupu.

Ili mpango huu ufanikiwe kunahitajika intelijensia bora zaidi ya vyombo vyetu vya usalama vilivyosheheni vihiyo wa taaluma ya usalama.Intelijensia inayohitajika ni ya kuhakikisha ujumbe kuwa kutakuwa na maandamano au mkutano umefika kwa wakandamizaji hao wa haki za binadamu.Ujumbe ukifika,raslimali na nguvu kazi ya kukandamiza jamii itaandaliwa chapchap,only for them kuishia kukandamiza hewa (uwanja au ukumbi mtupu).

Good news is,viongozi wengi-kama sio wote- wa vyombo vyetu vya usalama ni vihiyo wa taaluma ya usalama.Kwao,usalama ni kwa vigogo na mafisadi tu ilhali kinachowezesha wanausalama hao kulipwa mishahara na marupurupu lukuki ni fedha zinazotokana na kodi za walalahoi (vigogo na mafisadi wakilipa kodi ni kwa hisani tu,si lazima kwa vile hakuna sheria dhidi yao).Ukihiyo wa viongozi hao ni muhimu katika mkakati huu kwani,kama ilivyothibitika katika intelijensia yao ya kiwendawazimu kabla ya mauaji ya Arusha,wakishaskia kuna maandamano au mkutano basi badala ya kufanya analysis makini ya kiusalama za kuwawezesha kubashiri matishio la usalama na namna ya kuyadhibiti,wao wanakimbilia kuamrisha askari polisi wajiandae kwa vita huku magari ya mapambano na yale yenye maji ya upupu yakijazwa mafuta tayari kwa "vita".

Sasa kama kila baada ya wiki mbili wanyanyasaji hawa wanaingia mkenge na kujitwisha gharama za kudhibiti maandamano au mikutano hewa,ni dhahiri kuwa sio tu itavunja morali wa polisi wanaomtumikia kafiri ili mkono uende kinywani bali pia itaikamua serikali ambayo imeshatumia mabilioni kuchakachua uchaguzi uliopita,let alone gharama za kumudu lifestyles za kifahari za watawala wetu.

Wito wa blogu hii kwa Chadema ni simple: moto mlioanzisha haupaswi kuzimika mpaka kieleweke.Kwa upande mmoja,kuuzima moto huo kutamaanisha kusalimu amri kwa utawala wa kidikteta wa Kikwete.Na kwa upande mwingine,kuzima moto huo kutamaanisha uhai wa wazalendo waliouawa na polisi umepotea bure.Sio tu kwamba vuguvugu lililoanzishwa likiendelea kwa muda mrefu litapelekea Serikali kuishiwa nguvu ya kupiga na kuua kila kunapokuwa na mkutano au maandamano bali pia linaweza kuwafanya polisi wanaotumwa kuua Watanzania wenzao kupatwa na akili ya kutambua kuwa wanatumika vibaya kukandamiza raia wasio na hatia.Unaweza kudhani polisi hawa katili hawawezi kupatwa na roho ya kibinadamu.Hilo linawezekana,na dalili kuwa mwenye nguvu anaweza kutalikiwa na mnyonge kukumbatiwa inaonekana katika uamuzi wa diwani wa CCM huko Arusha aliyeamua kukitosa chama hicho tawala na kujiunga na Chadema.Uthibitisho mwingine ni kitendo cha Naibu Meya wa Arusha aliyeamua kubwaga manyanga kwa vile hayuko tayari kuwasaliti Watanzania wenzie.Trust me,vuguvugu hili likiendelea tunaweza kusikia stori kwamba polisi kadhaa wameamua kubwaga silaha kukwepa kwenda kuwaadhibu Watanzania wenzao wasio na hatia.

Kama alivyoandika mwanahabari mahiri Ansbert Ngurumo katika safu yake ya "Maswali Magumu" katika toleo la juzi la gazeti la Tanzania Daima,uamuzi wa Rais Kikwete na IGP wake Said Mwema kukandamiza wananchi kwa kipigo na risasi kitasaidia kuchochea hamasa kwa Watanzania wengi zaidi,na-kama alivyobainisha mwanahabari mwingine mkongwe Padri Privatus Karugendo- polisi hawana uwezo wala raslimali za kupiga risasi kila Mtanzania.Tupo wengi kuliko wao,na pia kama sera ya chinja chinja itaendelea basi mwishowe polisi hao watajikuta wanaua wazazi wao kama sio memba wengine wa familia zao.

Naanza kuhisi joto la ukombozi wa pili ikijongea kwa kasi.Na kichocheo cha joto hilo si kingine bali damu za wazalendo na mashujaa zilizomwagwa na askari waliotumwa na Kikwete kudhibiti raia wema huku mafisadi wakipewa hifadhi na fidia (rejea mabilioni kwa Dowans).


10 Jan 2011



Tanzania tuna tatizo kubwa.Hakuna haja ya kunyoosheana vidole as to nani amechangia tatizo hilo bali cha muhimu na haraka ni namna tutakavyoweza kutatua tatizo hili.Nisimung'unye maneno: tatizo kubwa linaloikabili ni kuwa na Rais ambaye takriban miaka sita tangu aingie Ikulu haelewi wajibu wake.

Hivi msomaji mpendwa wa blogu hii utamuelezeaje Jakaya Kikwete,Rais wetu,baada ya kumsikia akijitetea kwa mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania kuwa "unyama wa hali ya juu uliofanywa na polisi huko Arusha,na kusababisha vifo vya Watanzania wasio hatia,ni BAHATI MBAYA"!!!

Yani Kikwete aliishiwa kabisa na cha kudanganya mpaka akakurupuka na excuse dhaifu kiasi hiki!Bahati mbaya kwa maana gani?Bahati mbaya IGP Said Mwema kutengua dakika za majeruhi ruhusa ya maandamano iliyotolewa na RPC wa Arusha?Bahati mbaya polisi kuachana na jukumu la kusindikiza maandamano ya amani na badala yake kuanza kuwaadhibu wananchi wasio na hatia ambao "kosa" lao lilikuwa kutumia haki yao ya kikatiba kuandamana kwa amani?Bahati mbaya kupuuza miito kutoka kada mbalimbali juu ya umuhimu wa kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa umeya wa Arusha?Au bahati mbaya kwa risasi kutoka kwenye mitutu ya bunduki na hatimaye kutoa uhai wa Watanzania wasio na hatia?

Au Kikwete alikuwa anamaanisha kwamba unyama wa polisi wake dhidi ya wafuasi wa CUF walipoandamana,au vitendo vya udhalilishaji vya polisi hao dhidi ya wastaafu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki,au unyanyasaji uliozoeleka dhidi wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kila wanapoandamana,ni BAHATI NZURI kwa vile hakuna aliyeuawa?

Nashindwa hata kuhisi mabalozi walipatwa na mawazo gani walipomsikia mkuu wa nchi anatoa kauli ya ajabu kiasi hicho.Nahisi kuna waliomhurumia kwa kijibebesha jukumu asiloweza.Hii inanikumbusha wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 (ambazo zilinikuta nikiwa huko nyumbani kwa miezi kadhaa).Kuna baadhi ya wajuzi wa siasa za Tanzania waliniambia kuwa Kikwete anaweza kushinda urais kwa vile ana timu ambayo iko tayari kufanya lolote kuhakikisha anapata ushindi LAKINI urais wake utakuwa kituko.Na kituko amekuwa.

Kuna watakaosema wa kulaumiwa ni washauri wake.Lakini hao watakuwa wamesahau kuwa alipoanguka Mwanza alitanabaisha kuwa huwa anapuuza ushauri wa washauri wake (ambapo tulielezwa walimshauri apumzike kabla ya kukumbwa na zahma hiyo).Sasa inawezekana kabisa kuwa hata kabla ya kuongea na mabalozi hao,washauri wake walimshauri kitu sensible cha kuongea lakini akapuuza.Au pengine waliona hakuna haja ya kumshauri mtu ambaye ni "haambiliki".

Lakini tukiweka kando excuse hiyo ya kitoto iliyotolewa na mtu tuliyemkabidhi jukumu la kutuongoza Watanzania takriban milioni 50,ukweli kwamba Kikwete amediriki kujiumauma kwa mabalozi unapigia mstari ushauri niliotoa kwenye makala yangu iliyopita.Katika makala hiyo niliwashauri Watanzania wanaoishi katika nchi wafadhili wa Tanzania kuwasiliana na wabunge/wawakilishi wao na kuwafahamisha udikteta wa Kikwete,kisha kuwaomba wafikishe kilio cha Watanzania kwa serikali za wafadhili hao.Kikwete amelazimika kuokoteza excuses kwa vile anatambua bayana kuwa ni lazima awapoze wafadhili kwani mchango wa wafadhili hao ni muhimu sana kwa ustawi wa taifa letu.Ni muhimu zaidi kwa ustawi wa Kikwete na serikali yake inayosifika kwa matumizi ya anasa yanayozidi mapato.Wafadhili wakiamua kusitisha misaada,serikali itaanguka within months if not weeks.Lakini idea yangu ya kufikisha ujumbe kwa nchi wafadhili haikulenga kuwashawishi wasitishe misaada bali naamini wao wanaweza kumbana dikteta huyu aanze kuheshimu haki za binadamu.

Na kuthibitisha kuwa Kikwete alikuwa anawazuga mabalozi hao,gazeti la Tanzania Daima lina habari kuwa jeshi la polisi limezuia maandamano ya amani huko Songea yaliyoandaliwa na Chadema kupinga ufisadi katika sekta ya kilimo. Huu ni uthibitisho tosha kuwa unyanyasaji wa raia wasio na hatia na ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na polisi sio suala la BAHATI MBAYA kama anavyozuga Kikwete.Ni utekelezaji wa maagizo ya serikali iliyopo madarakani inayoongozwa na Kikwete huyohuyo.

Hivi Kikwete ameshindwa angalau kuwatosa Waziri wa Mambo ya Ndani Shamsi Vuai Nahodha,IGP Mwema na RPC wa Arusha kuwa "mbuzi wa kafara" ali mradi imsaidie kudanganya kuwa yeye hahusiki na maagizo yaliyopeleka polisi kuua.Hawezi kuwatosa kwa vile ni kiongozi anayeendekeza ushkaji.Sasa kama familia haiwezi kuongozwa kishkaji,nchi ikiongozwa kwa mtindo huo inakuwaje?

Na kuna kila dalili kuwa hivi sasa Kikwete anaongoza nchi na CCM yake kwa mtindo wa "bora liende".Hebu angalia jinsi ishu ya fidia kwa Dowans inavyoonyesha mparaganyiko kwenye kabineti ya Kikwete.Wakati Waziri William Ngeleja anatweta kuwakikishia mafisadi wa Dowans kuwa lazima walipwe kwa utapeli wao,Waziri Samuel Sitta anatangaza hadharani kuwa kuwalipa Dowans ni jambo la hatari.Uwajibikaji wa pamoja Kikwete's cabinet style!Huko CCM,Katibu wa chama hicho mkoani Arusha,Mary Chatanda anawawakia viongozi wa dini akiwataka wavue majoho yao wajiunge na siasa badala ya kukemea maovu (mpuuzi huyu anakosa adabu hata kwa Watumishi wa Mungu!).Kwa upande mwingine,Katibu Mkuu wa chama hicho,Yusuph Makamba,anadai kila mtu ana uhuru wa kutoa mawazo yake including viongozi wa dini.Na yote hayo yanatokea huku yakiweka kivuli kwenye tukio la kihistoria la diwani wa CCM kujiunga na Chadema.Tukio hili linapaswa kuchukuliwa kama ugonjwa nyemelezi kwa mwathirika wa ukimwi: linaashiria mwanzo wa mwisho wa CCM.

NIMALIZIE KWA KUKUMBUSHIA WITO WANGU KWA WATANZANIA WENZANGU WANAOISHI NCHI ZA WAFADHILI WA TANZANIA.KUWA MBALI NA NYUMBANI ISIWE SABABU KWETU KUSHINDWA KUSAIDIA UPATIKANAJI WA UHURU WA PILI WA TANZANIA (wa kwanza ulikuwa wa kumwondoa mkoloni,wa pili ni wa kuondoa udhalimu,ufisadi,ubabaishaji,unyanyasaji,ukiukwaji haki za binadamu,udikteta na kila baya unalofahamu).TUWASILIANE NA WABUNGE/WAWAKILISHI KATIKA MAENEO TUNAYOISHI NA KUWAOMBA WATUFIKISHIE KWA SERIKALI ZAO VILIO VYA WATANZANIA WENZETU WANAONYANYASIKA KWA KILA HALI CHINI YA UTAWALA WA KIKWETE NA CCM YAKE

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.