23 Mar 2012


Mkapa, Wassira washitakiwe kwa kauli zao tata Arumeru Mashariki

Uskochi
Dk. Slaa, Nassari na Vincent Nyerere watangulie kortini
HUKO nyuma niliwahi kuandika makala ambayo ilijaribu kuangalia upande wa pili utawala wa Baba wa Taifa Mwalimu, Julius Nyerere. Katika makala hiyo ambayo baadhi ya wasomaji waliitafsiri visivyo kuwa ni kumkosea heshima Mwalimu, nilitanabaisha kuwa licha ya mazuri mengi ya Nyerere, kwa namna fulani alichangia kutufikisha katika mazingira hovyo ya sasa.
Kati ya mifano niliyotumia kuthibitisha hoja yangu ni baadhi ya viongozi walioaminiwa na Mwalimu wakati wa utawala wake lakini mara baada ya yeye kutoka madarakani na hatimaye kufariki waligeuka viumbe tofauti kabisa, huku baadhi wakijitahidi kubomoa kila msingi aliojenga Nyerere kwa manufaa ya Watanzania.
Nilitolea mfano wa mwanasiasa mkongwe na aliyekuwa rafiki wa karibu wa Mwalimu, Kingunge Ngombale Mwiru, ambaye mara kadhaa katika miaka ya hivi karibuni ameonekana kuwaunga mkono baadhi ya wanasiasa ambao ‘walikataliwa na Nyerere’ kutokana na wasifu wao usiopendeza.
Lakini pengine mfano hai na ‘mbichi’ kabisa ni wasifu wa Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, ambaye siku chache zilizopita alizungumza mambo ya ajabu wakati akizindua kampeni za CCM, katika uchaguzi mdogo Jimbo la Arumeru Mashariki.
Hata kabla ya kauli zake huko Arusha, Mkapa ameendelea kuonekana kama msaliti kwa Watanzania baada ya umma kufahamishwa mambo aliyokuwa akifanya ‘nyuma ya pazia’ wakati akiwa Ikulu.
Wakati Mkapa alikuwa akiwaaminisha Watanzania kuhusu umuhimu wa maadili bora na siasa za ukweli na uwazi, taarifa zilizopatikana baada ya kustaafu kwake ni tuhuma kwamba aliigeuza Ikulu kama kijiwe cha biashara.
Yayumkinika kuhisi kuwa laiti nchi yetu ingekuwa inazingatia utawala wa sheria, ni wazi muda huu Mkapa angekuwa matatizoni angalau kwa kuundiwa tume ya kuchunguza tuhuma kadhaa dhidi yake. Lakini kwa vile sheria zinazotawala Tanzania zipo katika makundi mawili - kwa vigogo na kwa walalahoi - Rais huyo mstaafu anaendelea kula pensheni yake nono kwa amani na utulivu, hasa baada ya Rais Jakaya Kikwete kuweka wazi msimamo wake kuwa mtangulizi wake huyo aachwe apumzike kwa amani.
Turejee Arumeru Mashariki. Katika uzinduzi huo wa kampeni za CCM, bila aibu na pasipo jitihada zozote za kutumia busara ya kumkumbusha kuwa pamoja na tuhuma za kuitumia vibaya Ikulu bado baadhi ya Watanzania wanamheshimu kama Rais wao mstaafu aliyewaongoza kwa miaka 10 mfululizo, Mkapa alizungumza maneno yaliyoshangaza wengi.
La kipuuzi zaidi ni kuingiza porojo za mtaani kwenye mambo ya msingi. Huku akitambua bayana kuwa uongozi ni haki ya kila Mtanzania bila kujali ametoka ukoo gani. Mkapa alitoa tuhuma nzito dhidi ya Mbunge wa Musoma Mjini (CHADEMA), Vincent Nyerere, kuwa hatoki katika ukoo wa Nyerere.
Ni kuzeeka vibaya au uthibitisho kuwa Nyerere alifanya kosa kubwa kumpigia debe apate urais mwaka 1995? Ukaribu wa Mkapa na Mwalimu hauwezi kuwa kigezo cha yeye kumfahamu kila mwana-ukoo wa Baba wa Taifa. Lakini hata kama angekuwa anafahamu kuwa Mbunge Vincent hatoki ukoo wa Nyerere, hilo linawasaidia vipi wapiga kura wa Arumeru?
Ni kwa nini Mkapa hajatoa ushirikiano kwa mamlaka husika iwapo alikuwa anafahamu kuwa Mbunge huyo wa Musoma Vijijini amedanganya kwa ‘kujipachika’ undugu na Baba wa Taifa?
Japo ninaamini kuwa sababu kubwa ya wapiga kura wa Jimbo la Musoma Mjini kumchagua Vincent ni imani yao katika uwezo wake kuwatumikia, lakini ukweli kwamba anatoka ukoo wa Nyerere unaweza kuwa ulimwongezea kura kadhaa (hasa kwa kuzingatia ‘siasa zetu za haiba ya mgombea’).
Kwa Rais mstaafu ‘kufahamu’ kuwa kuna mbunge anadanganya kuhusu wasifu wake lakini akakaa kimya hadi kwenye kampeni za uchaguzi ambapo Vincent ni mmoja wa waratibu wake kwa upande wa CHADEMA, inatueleza mengi kuhusu ubabaishaji wa Mkapa.
Lakini kubwa zaidi, kitendo cha mwenyekiti huyo mstaafu wa CCM kutokukifahamisha chama chake kuwa mgombea ubunge wa chama pinzani amedanganya kuhusu wasifu wake na hatimaye akafanikiwa kupata ubunge kinaweza kutafsiriwa kama usaliti dhidi ya chama alichokiongoza kwa mwongo mzima.
Sijui Mkapa alijisikiaje baada ya mmoja wa watoto wa Baba wa Taifa, Madaraka Nyerere kuwathibitishia Watanzania kuwa Vincent Nyerere anatoka ukoo wa Nyerere (kinyume cha uongo wa hadharani wa Mkapa).
Kilicho wazi ni kuwa upuuzi huo umeongeza sifa nyingine mbaya kwenye wasifu wake usiopendeza. Ni Mkapa pekee anayejua kwa nini alikurupuka kusema uongo hadharani lakini sote tunajua kuwa kitendo cha Rais mstaafu kusema uongo kwenye kadamnasi (tena pasipo hata haja ya kufanya hivyo) kimezidi kushusha hadhi ya kiongozi huyo.
Lakini kana kwamba  kasoro hiyo ya Mkapa kujifanya mwana-ukoo wa Nyerere na kumkana hadharani Vincent Nyerere, haitoshi kutueleza yeye ni binadamu wa aina gani, baadhi ya ahadi alizotoa kwa wapiga kura wa Arumeru Mashariki zinazua swali gumu, ilikuwaje yeye binafsi alifanikiwa kuwa Rais wetu kwa awamu mbili mfululizo.
Katika uzinduzi huo wa kampeni za chama tawala, Mkapa aliwaeleza wananchi kuwa amepokea taarifa za kuwapo kwa migogoro mikubwa ya ardhi inayosababishwa na baadhi ya wawekezaji kuhodhi maeneo makubwa na kusema atalifikisha kwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete na kumshauri achukue hatua kwa kuwawajibisha watendaji wa Serikali ambao wameshindwa kuwajibika na kuchukua hatua kwa wawekezaji waliokiuka masharti.
Hivi kweli Mkapa ameshasahau alikuwa Rais wetu kwa miaka 10 mfululizo na utawala wake ulifungua milango kwa kila mgeni kuja kuwekeza hata pale uwekezaji huo ulimaanisha uporaji wa rasilimali za nchi yetu?
Kama amesahau hilo lililojiri miaka michache tu iliyopita, kwa nini basi ajifanye kukumbuka kila kilichomhusu Baba wa Taifa kwa vile tu alikuwa msaidizi wake miaka mingi iliyopita?
Ni kwa vile tu CCM yenyewe inaendeshwa kimzaha ndio maana hadi sasa hakuna kiongozi yeyote wa chama hicho aliyediriki kumkemea Mkapa asimfarakanishe Kikwete na wananchi kwa ahadi za kumshauri Rais ashughulikie makosa yaliyofanywa na mtangulizi wake.
Na ni kwa sababu tu Kikwete ana huruma sana kwa viongozi wenye makosa ya wazi, ndio maana anaweza kuruhusu Mkapa ajipe wadhifa wa “mshauri” wa Rais katika kuwashughulikia wawekezaji feki waliokaribishwa wakati wa utawala wake. Vinginevyo, Kikwete asingeruhusu mtu aliyeshindwa kujishauri mwenyewe kuongoza nchi kwa maslahi ya umma atamke kuwa atambebesha Rais wa sasa mzigo wa kusafisha ‘uozo’ aliotenda.
Na kama CCM imekumbwa na virusi vinavyowafanya baadhi ya viongozi wake kuingilia mambo ya koo na familia za wanasiasa wa upinzani, mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Steven Wassira ameiga mfano wa Mkapa na kudai kuwa mgombea ubunge wa CHADEMA, Joshua Nassari hafai kuwa mbunge wa jimbo hilo kwa kuwa ni kijana mkorofi na mara kwa mara, baba yake mzazi amekuwa akimsihi kuachana na ukorofi tangu wakati akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Maneno haya yanatamkwa na mtu ambaye licha ya kuwa na wadhifa mkubwa ndani ya CCM pia ni waziri katika Ofisi ya Rais. Lakini tutegemee nini kwa mwanasiasa ambaye pengine ni maarufu zaidi kwa picha iliyosambaa mtandaoni akiwa kauchapa usingizi bungeni kuliko busara kutoka kinywani mwake!
Kama alimudu kusinzia wakati kikao cha Bunge kikiendelea, basi yayumkinika kuhisi hata huo wadhifa aliojipachika kuwa msemaji wa familia ya Nassari ni sehemu tu ya ndoto zake usingizini.
Lakini wito wa safu hii kwa familia ya Nassari ni huu, bila kujali matokeo ya uchaguzi wa Arumeru Mashariki ni muhimu kumfungulia Wassira kesi ya madai, awathibitishie Watanzania tuhuma alizotoa dhidi ya mgombea huyo. Ushauri kama huo unaelekezwa pia kwa Vincent Nyerere kwani kufanya hivyo kutatoa fundisho muhimu dhidi ya wanasiasa waropokaji.
Na kama tuhuma zake dhidi ya Nassari hazitoshi (na tayari baba wa mgombea huyo amezikanusha hadharani), Wassira amekaririwa akiendeleza matamshi yake tata kwa kudai kuwa Vincent Nyerere hawezi kutoka ukoo wa Nyerere eti kwa vile haiungi mkono CCM.
Huu ni uvivu wa kufikiri, kwa sababu hakuna sheria inayomlazimisha Mtanzania kufuata itikadi inayofuatwa na ndugu zake.
Kadhalika, Wassira ameendeleza kauli tata kwa kudai Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibroad Slaa alifanya ufisadi wa fedha za ziara ya Baba Mtakatifu John Paul wa Pili, alipozuru Tanzania mwaka 1990.
Japo Dk. Slaa hana tabia ya kufungua kesi za madai dhidi ya ‘wazushi’ wake, safari hii anapaswa kuangalia upya msimamo wake huo kwani njia pekee ya kuwafundisha ushirikiano kati ya ubongo na mdomo kwa watu aina ya Wassira ni kuwaburuza mahakamani.
Nimalizie kwa kutoa wito kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais Kikwete kuwakumbusha wana-CCM wenzake kama Mkapa, Wassira na wengineo kuwa kampeni za uchaguzi Arumeru Mashariki ni za kupata mwakilishi bora bungeni na sio referendum (kura ya maoni) kuhusu ukoo wa Nyerere, familia ya Nassari au ziara ya Baba Mtakatifu mwaka 1990.
Na wito wangu kwa wana-Arumeru Mashariki ni huu, kiongozi yeyote anayeweza kuwadanganya hadharani hatosita kuwahujumu faraghani. Njia pekee ya kuwaadhibu wanasiasa kama Mkapa na Wassira ambao wanawafanya ninyi wapiga kura kuwa watu msiojua mnachotaka bali ni masuala kuhusu ukoo na familia ya fulani ni kumnyima kura mgombea wanayempigia kampeni.
Pengine kushindwa kwa mgombea wao kutawafanya wanasiasa hao kuwa makini kabla hawajaropoka chochote kile hadharani.



19 Mar 2012



WIKI YA MADAI YA MAJI

Mwito wa kushiriki wiki ya madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii:
Nimerejea toka Afrika Kusini nilipokuwa kikazi na kukuta Wizara ya Maji imezindua maadhimisho ya Wiki ya Maji kuanzia tarehe 16 Machi na kilele kitakuwa Siku ya Kimataifa ya Maji tarehe 22 Machi 2012.

Ujumbe wa mwaka huu ni “Maji na Usalama wa Chakula”, hata hivyo tunahimizwa kuadhimisha ujumbe mpya bila kuelezwa matokeo ya ujumbe wa mwaka mmoja uliopita wa “Maji kwa ajili ya Miji: Kukabiliana na changamoto mbalimbali mijini”.

Kazi ya wabunge na bunge kwa mujibu wa katiba ibara ya 63 ni kuwawakilisha wananchi na kuisimamia serikali na mamlaka zake katika kuwezesha maendeleo kwa kutumia rasilimali za umma na za wadau wengine.

Kwa nafasi hiyo natoa mwito kwa wananchi wa Jimbo la Ubungo na wa Jiji la Dar es salaam kwa ujumla kwamba badala ya kuadhimisha sherehe za maji bila ya maji kila mmoja ashiriki kwa namna mbalimbali katika Wiki ya Madai ya Maji.

Kila mmoja anaweza kushiriki kwenye wiki hii ya madai ya maji kwa njia mbalimbali, njia mojawapo ambayo natoa mwito kwa wananchi wa Jimbo la Ubungo kuitumia ni kushiriki madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii kwa kuandika barua pepe kwa bodi ya Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) kuitaka ifanye kazi ipasavyo ya kuharakisha upatikanaji wa maji kwa mujibu wa sheria, kanuni, mipango na mikataba.

Waandikie wajumbe wa bodi ya DAWASA madai ambayo unataka wayafanyie kazi katika eneo lako na nakala ya barua pepe hiyo kuituma kwa[email protected] kwa ajili za hatua zaidi za kibunge za uwakilishi na usimamizi.

Bodi ya DAWASA ni kama ifuatavyo: Mwenyekiti Dr. Hawa E. Sinare([email protected]), Makamu Mwenyekiti-Alhaj Said H. El-Maamry[email protected], wajumbe: Bw. Laston Msongole ([email protected]),Bi. Mary Mbowe ([email protected]) , Bi. Christine Kilindu([email protected]), Bw. Daniel Machemba ([email protected],[email protected]), Alhaj Bakari Kingobi ([email protected]), . Mary G. Musira([email protected]), B. Florence S. Yamat ([email protected]), Mh. Amina N. Mkilagi (Mb), Mhandisi. Archard Mutalemwa-Afisa Mtendaji Mkuu ([email protected]).

Tuungane pamoja kutaka serikali kuu na serikali za mitaa zitumie wiki hiyo kutoa maelezo kwa umma kuhusu hatua iliyofikiwa katika kutekeleza miradi ya maji na pia kuharakisha uzinduzi wa miradi ilicheleweshwa.

Njia hii ya kuunganisha nguvu ya umma kwa kutumia TEHAMA (SMS, facebook, twitter, email na njia nyingine) tuliitumia tarehe 1 Disemba 2011 wakati wa kuhamasisha umma kushiriki mkutano wa wadau uliotishwa na EWURA kuhusu ombi la TANESCO kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa 155% (zaidi ya mara tatu ya bei iliyokuwepo).

Hatimaye umeme ulipandishwa lakini si kwa kiwango hicho cha awali bali kwa wastani wa 40% kwa kuzingatia pia viwango vya utumiaji. (Suala la Umeme nimeanza kuchukua hatua zingine kama Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kutokana na matatizo yanayoendelea kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Dharura wa umeme na nitatoa kauli kuhusu mgawo wa umeme unaoendelea kinyemela).

Izingatiwe kuwa nilipanga kwenye wiki hii ya madai ya maji kuunganisha nguvu ya umma kwa kuwaongoza wananchi kukutana na serikali na mamlaka nyingine zinazohusika hata hivyo itabidi kutumia njia mbadala za kuwasilisha madai.

Hii ni kwa sababu kuanzia kesho tarehe 19 Machi 2012 nitakuwa mfululizo mahakamani kwenye kesi ya uchaguzi wa Jimbo la Ubungo wa mwaka 2010. Hivyo, wakati kesi hiyo ikiendelea nitaendelea kutumia njia nyingine za kibunge kuchukua hatua kuhusu masuala ya maji lakini natoa mwito kwa wananchi nanyi kwa upande wenu kila mmoja kuchukua hatua zinazowezekana katika wiki hii ya madai ya ya maji. Umoja ni Nguvu.
Maadhimisho ya Wiki ya Maji bila ya Maji
Upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es salaam miaka michache baada mwaka 1961 ulikuwa zaidi ya asilimia 68; hivi sasa miaka 50 baada ya uhuru tumerudi nyuma na upatikanaji kuwa wastani asilimia 55 tu tena kwa mgawo.

Uchakavu na wa miundombinu kutokana na mabomba kutokarabatiwa ipasavyo pamoja na uharibifu katika mitandao ya maji wa kujiunganishia kinyemela na kiholela umesababisha ongezeko kubwa la upotevu wa maji mpaka kufikia kati ya asilimia 40 hadi 45.

Hali ni mbaya zaidi kuhusu uondoaji wa maji taka ambapo ni asilimia 18 tu ya makazi ndiyo yaliyounganishwa katika mtandao wa maji taka na hivyo kuleta uchafuzi wa mazingira hususani katika maeneo yasiyopimwa. Hata katika maeneo yaliyopimwa kama Sinza mitandao ya maji taka haijakarabatiwa na kupanuliwa kwa wakati kwa kuzingatia ongezeko la watu suala ambalo lisipochuliwa kwa uzito unaostahili madhara yatatokea katika siku za usoni.

Katika muktadha huo hakuna sababu ya kusherekea wiki ya maji bila maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam kwa ujumla hivyo Wizara ya Maji na mamlaka nyingine husika zitumie wiki hii kutoa majibu ya msingi kwa wananchi kuhusu namna ambavyo wataongeza kasi ya kushughulikia kero ya maji.
Itakumbukwa kwamba akihutubia Bunge mwezi Juni mwaka 2010 wakati wa kuwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maji ya mwaka wa fedha 2010/11 Waziri Mark Mwandosya aliahidi kwamba usanifu wa bwawa la Kidunda linatarajiwa kutoa mchango mkubwa wa utatuzi wa kero ya maji kwa wananchi wa Ubungo lingekamilika mwezi Septemba mwaka huo wa 2010; lakini mwezi Machi 2011 Waziri Mwandosya kauli tofauti kuwa upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bwawa hilo utakamilika mwezi Juni mwaka 2011 na ujenzi mwaka 2013.
Kwa sababu hiyo, ni muhimu kuendelea kuwasilisha madai ili taratibu zote za msingi zikakamilishwa mwaka huu wa 2012 kwa haraka; hivyo pamoja na kutenga bilioni sita kwenye bajeti ya mwaka 2011/2012 kwa ajili ya ulipaji fidia iongeze fedha kwa ajili ya ujenzi kuanza. Maamuzi haya yafanyike pia kuhusu kuharakisha upanuzi wa Bomba la Ruvu Chini na ujenzi wa bomba jipya toka Ruvu Juu kama Serikali ilivyoahidi bungeni wakati wa kujibu swali langu la msingi tarehe 13 Aprili 2011.
Aidha, DAWASA ambayo ndiyo mamlaka yenye dhamana ya mtandao wa maji katika jiji la Dar es salaam ieleze ni lini maeneo ya pembezoni yenye mtandao wa mabomba maarufu kama mabomba ya wachina hususani ya Kimara Bonyokwa, King’ong’o, Mbezi kwa Msuguri, Malambamawili yataanza kutoa maji.

Kama hatua za dharura, DAWASA iharakishe kukamilisha uchimbaji wa visima virefu nane vyenye kuweza kuhudumia kwa ujumla wakazi zaidi ya elfu thelathini wa Kimara Mavurunza, Bonyokwa, Kilungule na King’ong’o kama ilivyoahidiwa na Rais Jakaya Kikwete mwezi Mei mwaka 2010.

Visima hivi ni suluhisho la dharura wakati tukiendelea kufuatilia suluhisho la kudumu linalopaswa kuhusisha pamoja na mambo mengine kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mikataba, kudhibiti ufisadi unaofanywa katika mtandao ikiwemo kukabiliana na upotevu wa maji unaondelea na kupanua miundombinu.

DAWASA ieleze pia mpango ilionao wa kumalizia maeneo ambayo hayakufikiwa na mtandao wa mabomba ya maji hususani ya pembezoni ya Saranga, Makoka, Msakuzi, Kibamba, Kwembe, Msakuzi, Goba, Mpiji Magohe, Makabe, Msumi, Kilungule nk.

Kwanini madai ya sasa ya maji yaelekezwe DAWASA kwa niaba ya Serikali?
Ni muhimu ikazingatiwa kuwa kwa mujibu wa katiba ibara ya 8 mamlaka na madaraka yote ni ya umma, serikali na vyombo vyake vinafanya kazi kwa niaba; hivyo wiki hii ya madai ya maji iwezeshe kuongeza msukumo katika kazi za kuboresha upatikanaji wa maji kwa njia mbalimbali.

Njia mojawapo ni pamoja na kuwasilisha madai ya mamlaka husika na kutaka majibu kuhusu kazi ambazo zinafanyika na katika wiki hii ya madai ya maji, pamoja na kuwa wahusika wa masuala ya maji ni wengi kwenye sekta ya umma na sekta binafsi; ni muhimu nguvu zielekezwe kwa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA).

Hii ni kwa sababu kwa mujibu wa Sheria ya DAWASA (Dar es salaam Water and Sewerage Authority Act no.20 of 2001) kifungu cha 22 DAWASA ndio chombo kikuu cha utekelezaji wa mipango na sera za serikali kuhusiana na maji, ugavi wa maji, huduma za maji taka na uhifadhi wa maji katika Jimbo la Ubungo na Jiji la Dar es salaam kwa ujumla.

Tarehe 1 Julai 2005 DAWASA ilitoa mkataba wa ukodishaji (lease agreement) kwa DAWASCO ambao unaitaka DAWASCO kuendesha miundombinu ya maji na kuhakikisha matengenezo ya mtandao wa maji katika jiji la Dar es salaam.

Hata hivyo, uhusiano wa DAWASA na DAWASCO ni kama wa mwenye duka na muuza duka; ambao kunaweza kuwa na matatizo ya muuza duka lakini lakini panaweza kuwa na matatizo ya uhaba wa bidhaa na duka lenyewe ambayo kimsingi yanamhusu mwenye duka.

Hivyo, katika wiki hii ya madai ya maji nguvu zielekezwe kwenye kuisimamia DAWASA ambayo kwa mujibu wa kifungu cha 33 cha sheria tajwa inatumia kodi za wananchi wote ikiwemo ambao hawapati huduma ya maji toka kwao na pia tozo za wateja wanaopata maji kwa mgawo, hivyo DAWASA inawajibika kuhakikisha huduma zinapatikana kwa kuzingatia sheria, kanuni, mikataba na mipango.

Bodi ya DAWASA inapaswa kwa kuzingatia mamlaka yake kwa mujibu wa kifungu cha 10 cha Sheria tajwa na majukumu mengine ya DAWASA kwa kurejea vifungu vya 6, 7 na 8 vya sheria husika kuhakikisha huduma ya maji safi na maji taka inapatikana kwa wananchi.

Mtakumbuka kwamba Machi Mosi 2012 niliungana na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) katika kata saba Jimboni Ubungo kwenye kazi za kuboresha upatikanaji wa maji.

Tarehe 2 Machi 2012 nilifanya mkutano na wanahabari na kutaka hatua za ziada kuchukuliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) na Wizara ya Maji.

Nashukuru kwa hatua ambazo zimeanza kuchukuliwa na DAWASCO na EWURA katika masuala kadhaa; hata hivyo sijaridhika na namna ambavyo DAWASA na Wizara ya Maji wanavyoshughulikia masuala ya maji katika maeneo mengi; hivyo wiki ya madai ya maji kupitia mitandao ya kijamii itumike kuongeza msukumo wa umma kabla ya kuchukua hatua zaidi za kibunge katika Mkutano wa Saba wa Bunge unaotarajiwa kuanza tarehe 10 Aprili 2012.

John Mnyika (Mb)
Jimbo la Ubungo
18/03/2012

MTEMBELEE MHESHIMIWA MNYIKA KWENYE TOVUTI YAKE INAYOPATIKANA HAPA

18 Mar 2012


Nimetumiwa hii nami naiwasilisha kama ilivyo:




Ndugu Blogger, 
Husika na Kichwa cha Habari hapo juu, kwa masikitiko makubwa chanzo chetu cha ripoti kimepokea Habari ya kwamba kuna mchakato unafanyika wa kuweka usiku wa Bloggers Tanzania Lakini cha kushangaza sana usiku huo utakuwa ni usiku wa ubaguzi pia kwa maana watakao alikwa ni Bloggers wakubwa tuu wa Tanzania sasa tujiulize kwa umakini sana, Kwanza ni wakina nani hao ambao ndio wanazania kuwa ni bloggers wakubwa Tanzania, Pili tujiulize hao wanaojiita kuwa ni Mabloga wakubwa na maarufu tanzania wamechukua kigezo gani? 

Tufike mahali kwamba nyie mnao jiita bloggers wakubwa hapa nchini msiwadharau na kuwatenga hao mabloga wadogo, inasikitisha sana badala ya kuwasaidia nyie mnawakandamiza. kama mpo juu mpo juu tuu hakuna wa kuwashusha chini basi wasaidieni na hao mabloga wadogo wadogo.

Na mwisho kwa niaba ya Timu nzima inayo endelea kufuatilia kwa umakini mchakato mzima wa umoja wa bloggers Tanzania na kufuatilia kwa ukaribu na umakini vikao vya Siri na vya chini vinavyo endelea kwa ajili ya huo usiku wa bloggers, tunapenda kusema kwamba kama mpo hapa ni bora muwashirikishe na wengine email ndio hizi hizi za bloggers. Tusiwe na roho ya kwanini sote ni watanzania.

Imetolewa na 

Ripota wenu




It's like you were gone yesterday.I just can't believe that you're gone.On this day,I'd be calling you and daddy to say how much I love you,mamma.But you're not there.The only comfort I have is the strong belief that you're resting in peace.And though you're not with us on this Mother's Day,you remain the best thing God could give any son.Rest in peace,mamma.You'll always be missed and remembered!Oh! My mama, happy mother’s day
You are the greatest mother I have ever had
You are my mother today
You will be my mother tomorrow
You are always my mother
You will forever be my mother

Thank you my mother for bringing me into this world
Thank you my mother for taking care of me in your womb
Thank you my mother caring for me as a toddler
Thank you my mother for feeding me since I was a baby
Thank you my mother for all the clothes you bought for me
Thank you my mother for teaching me good manners at home

Thank you my mother for sending me to school
Thank you my mother for supervising my homework
Thank you my mother for ensuring I eat before going to school
Thank you my mother for all the regular pocket money
Thank you my mother for liking my friends
Thank you my mother for all the everyday advices

My mother always remind me that fingers are not equal
As I grow up, I have seen the correlation of this analogy
To many human beings, neighbors, societies and nationalities
Oh! My mama, thank you for your words of wisdom
My mother taught me many things that I have never read in books
Thank you my mother for all your guiding philosophies

Oh! My mama, I sincerely wish everyday could be Mother’s Day
One day in a year is not enough to thank my wonderful mother
Oh! My mama, I will forever be your child
Oh! My mama, you will eternally be my mother
Thank you my mother for being my best friend
Thank you my mother for being my trusted adviser
I honestly wish you HAPPY MOTHER’S DAY!
.Rest in Eternal Peace,mamma!

15 Mar 2012


Baada ya kulainika…Madaktari wamevuna au ‘wameliwa’?

HATIMAYE Rais Jakaya Kikwete amefanikiwa kuleta suluhisho katika mgogoro kati ya Serikali yake na madaktari waliopania kugoma wakidai maslahi bora na mazingira mazuri ya kazi. Kadhalika watoa tiba hao walikuwa wakiitaka Serikali iwawajibishe Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda na Naibu wake, Dk. Lucy Nkya.
Kwa upande mmoja, hatua hiyo ya Rais na madaktari ilikuwa habari njema kwa wanyonge wasio na uwezo wa kwenda India au kwingineko nje ya nchi kutibiwa.
Lakini kwa upande mwingine, habari kwamba madaktari wamesalimu amri baada ya kukutana na Rais, Ikulu, zimepokewa kwa hasira na baadhi ya wananchi ambao waliuona mgomo huo kama adhabu sahihi kwa Serikali yao ambayo kwa kiasi kikubwa inazembea kujali maslahi yao.
Binafsi, japo niliipokea taarifa hiyo ya kumalizwa mgomo kwa furaha, nafsini ninaona kama tatizo hilo limeahirishwa kwa muda tu. Wakati madaktari wanaonekana kuwa na imani kuwa Rais Kikwete atatekeleza ahadi alizowapa (pasipo kutuambia kwa nini wana imani hiyo), rekodi isiyopendeza ya Kikwete na Serikali yake katika utekelezaji wa ahadi ingepaswa kuwafahamisha madaktari hao kuzichukulia ahadi hizo za Rais kwa hadhari.
Kama nilivyowahi kuandika mara kadhaa huko nyuma, tatizo la uongozi wa nchi yetu halijawahi kuwa kwenye kutoa ahadi nzuri na zenye kutia matumaini. Viongozi wetu ni wepesi mno kuahidi mambo yaliyo ndani ya uwezo wao na hata miujiza.
Laiti madaktari wangekuwa makini, wangejiuliza kwa nini ahadi zisizoisha kuhusu utatuzi wa tatizo la mgawo wa umeme zinaendelea kuwa ahadi tu huku mgawo ukigeuka kuwa kama stahili katika maisha ya kila siku ya Mtanzania.
Kama kumbukumbu yangu iko vizuri, nadhani ahadi ya mwisho ya Kikwete kuhusu kupunguza makali ya mgawo wa umeme iliashiria tatizo hilo lingeanza kushughulikiwa Desemba, mwaka jana. Lakini ahadi kubwa zaidi ya Rais ilikuwa ile aliyotoa muda mfupi baada ya kuingia madarakani mara ya kwanza (mwaka 2005) ambayo iliishia kwa Watanzania ‘kuingizwa mkenge’ na kampuni feki ya Richmond.
Na kama Tanzania ni shamba la bibi ambapo kila mtu ana uhuru wa kuvuna asichopanda, kampuni hiyo hewa ‘ilizaa’ kampuni nyingine ya Dowans (katika mazingira yanayoleta maana ndotoni tu na si katika hali halisi). Japo inaleta uchungu mkubwa kuizungumzia Dowans na jinsi watendaji mbalimbali wa Serikali walivyosimama kidete kuitetea ilipwe japo haikutekeleza wajibu wake, sakata hilo linashabihiana na maisha ya kawaida ya Mtanzania kwenye ‘kona za uswahilini’ ambapo si jambo la ajabu kwa vibaka kukupora kisha kukupigia kelele za ‘mwizi….mwizi.’ Kinachofuatia hapo ni ‘maumivu mengine’ ya kipigo kutoka kwa wananchi walioamini hadaa za vibaka hao kuwa wewe uliyeporwa ndiye mwizi uliyewapora vibaka hao.
Waingereza wanasema the end justifies the means, yaani; ‘mwisho (wa jambo) huhalalisha njia (iliyotumika kufikia mwisho huo).’ Kwa mantiki hiyo, jitihada za Kikwete zilizofanikiwa kuwalainisha madaktari kutoendelea na mgomo zinahalalisha hatua hiyo.
Lakini suala la msingi hapa si uhalali wa hatua hiyo ya Kikwete na madaktari kuafikiana nae, au hata suala zima la mgomo. Na katika suala la mgomo ni vigumu kuona uhalali wa hatua ambayo kimsingi ingewaumiza wanyonge ambao hata pale huduma za afya zinapopatikana inawawia vigumu kumudu gharama za kupata huduma hizo.
Katika stadi za mantiki, ili jambo liwe halali ni lazima lionekane kuwa halali. Kwa mgomo huo, japo ilikuwa halali kwa madaktari kudai maslahi na mazingira bora ya kazi lakini uhalali wa njia waliyotumia kudai haki yao uliathiriwa na ukweli kwamba mgomo wao ulikuwa na madhara makubwa zaidi kwa wasiohusika (yaani wananchi wa kawaida ambao kimsingi hawahusiki na sababu za uduni wa maslahi na mazingira ya kazi ya madaktari hao).
Lakini hata tukiweka kando suala la uhalali, bado inanitatiza kuelewa madaktari wamepata nini katika mgomo wao wa kwanza na hatua yao ya majuzi kuamini ahadi za Kikwete.
Japo mgomo wa kwanza ulichangia Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu, Deo Mtasiwa kusimamishwa kazi, sitaki kuamini kuwa harakati hizo zilizogusa hisia na uhai wa kila Mtanzania zililenga tu kuona viongozi hao wawili wakisimamishwa (na si kufukuzwa) kazi.
Tangu mwanzo madaktari hao waliitaka Serikali kuchukua hatua dhidi ya Mponda, Nkya, Nyoni na Mutasiwa lakini hadi sasa inaonekana wazi kuwa Serikali haipo tayari kuwatoa rehani waziri na naibu wake.
Na hili liliwekwa bayana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyeweka wazi msimamo wa Serikali kuwa “kama kugoma basi (madaktari) tu lakini Serikali haiwezi kushinikizwa kuwafukuza kazi Waziri na Naibu wake kwa mgomo.”
Nimebainisha hapo juu kuwa binafsi nahisi suala hili limeahirishwa tu kwa sababu historia ina muhukumu Kikwete linapokuja suala la utekelezaji ahadi, hata zile anazotoa pasipo haja ya kuzitoa.
Hivi madaktari wamesahau ile kauli maarufu ya Kikwete kuwa; anawafahamu wala rushwa lakini anawapa muda tu wa kujirekebisha, na wasipofanya hivyo watagundua kuwa tabasamu lake halimaanishi huruma kwa wazembe na wababaishaji?
Au madaktari wameshasahau kioja alichotoa Rais Bandari ya Dar es Salaam, alipotamka kuwa anawafahamu kwa majina wanaofanya ufisadi bandarini hapo na angeyawasilisha kwa uongozi ili wachukuliwe hatua, lakini hakufanya hivyo hadi leo.
Waingereza wana busara moja isemayo; “The minute you settle for less than you deserve, you get even less than you settled for,” yaani-kwa tafsiri isiyo rasmi- unapokubali ‘yaishe’ licha ya upungufu, utaishia kupata pungufu zaidi ya kile ulichokubali.
Licha ya ukweli kuwa wao ndio waathirika wakubwa, wananchi wengi walikuwa upande wa madaktari kwa maana ya kuunga mkono hoja zao. Mtego waliojiingiza watoa tiba huo ni huu: wakikurupuka tena kutishia kugoma kwa madai kuwa Rais Kikwete aliwalaghai, wataishia kuonekana wababaishaji wasio na msimamo, na pengine wananchi wataamua kuwapuuza na kuwaona kama ‘kundi linalotaka kuweka rehani uhai wa wanyonge.’
Lakini hata tukiamua kuamini kuwa ahadi za Rais kwa madaktari hao ni za dhati, hizo fedha za kuwatimizia madai yao zitatoka wapi? Hapa sina maana kuwa hakuna njia za kupata fedha za kushughulikia madai hayo, bali ukweli ni kwamba Serikali ya Kikwete ina rekodi nzuri ya matumizi ya anasa yasiyoendana na hali mbaya ya uchumi wetu.
Sidhani kama kuna mtu yeyote (pamoja na madaktari) anayedhani Rais yupo tayari kupunguza safari zake za nje ya nchi ili kuokoa fedha japo kidogo kuanza kushughulikia matatizo ya madaktari hao. Na sitaki kabisa kuamini Serikali ya Kikwete iko radhi kuendesha kampeni za CCM huko Arumeru Mashariki kwa ‘kuuza sera’ pekee bila kumwaga fedha kwa wapiga kura (fedha ambazo zingeweza kuanza kutatua kero za madaktari hao).
Pengine gumu zaidi katika utekelezaji wa ahadi hiyo ya Rais kwa madaktari ni ukweli kuwa, pindi Serikali ikianza kutoa fedha za kutatua matatizo ya madaktari kuna uwezekano mkubwa wa watumishi wa kada nyingine kuanza shinikizo la kudai ‘watendewe haki kama madaktari.’
Kama nilivyobainisha katika makala yangu ya wiki iliyopita, kilio cha madaktari kuhusu maslahi na mazingira bora ya kazi ni kiwakilishi tu cha tatizo linalowakabili watumishi wengine wa umma na wananchi wengi kwa ujumla.
Ni wazi kuwa kama Serikali itaamua kupunguza matumizi ya anasa na kushughulikia madai ya madaktari hao, kuna uwezekano wa watumishi wengine wa umma kupata funzo kutoka katika mgomo wa madaktari kuwa ‘ukigoma utaitwa Ikulu, na Rais atatumia nguvu zake kutatua matatizo husika.’
Mwisho, inakera kuona Serikali iliyojaa mawaziri lukuki (ambao wanaongeza mzigo wa gharama za kuwahudumia) inashindwa kupata ufumbuzi wa kundi moja la watumishi wa umma hadi kulazimu Rais aingilie kati.
Tuna Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, mawaziri na manaibu wao kibao (huwezi kukumbuka majina yao wote pasipo kuwa na orodha yao mkononi), na mlolongo wa makatibu wakuu na wakurugenzi wa wizara lakini inabidi kumsubiri Rais ndipo ufumbuzi wa tatizo upatikane.
Anayestahili lawama kubwa si watendaji hao bali aliyewateua. Sote tunafahamu kuwa Rais hakuwahi kushikiwa mtutu wa bunduki ili ateue watendaji ambao sio tu ni wengi bali wengi wao ni kama bado wapo kwenye sherehe za kujipongeza kwa kuteuliwa kwao na Rais, huku baadhi yao wakiwa kama hawajui kwa nini Rais aliwateua.
Na kwa mazingira haya ya lundo la wasaidizi wasio na msaada wa maana kwa Rais, Serikali na umma kwa ujumla, sio tu tutaendelea kushuhudia madaktari, watumishi wengine na wananchi kwa ujumla wakiingia kwenye mgogoro na Serikali kudai uwajibikaji bali pia tutasikia sana vioja kama hivyo vya Naibu Waziri aliyeibiwa hotelini katika mazingira ya kutatanisha.
Utitiri wa viongozi wasio na cha kufanya unaweza kabisa kusababisha waishie kuwa vituko ili angalau majina yao yasikike na ijulikane kuwa wapo kazini.


Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.