18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI

Asalam aleykum.

Hapa Uingereza kuna chama cha siasa kinachoitwa British National Party au kwa kifupi BNP.Hiki ni chama kinachofuata siasa za mrengo wa kulia kabisa,far right kwa “lugha ya mama.”Siasa za namna hiyo ndio zilizokuwa zinahusudiwa na Manazi chini ya Hitler na Mafashisti chini ya Mussolini.Hawa jamaa wa BNP ni wabaguzi waliokithiri.Majuzi wakati wa uchaguzi mdogo huko England mmoja wa watu muhimu katika BNP,Dokta Phill Edwards (jina lake halisi ni Stuart Russell) alizua mjadala mkubwa kuhusu siasa za chama hicho pale alipotoa matamshi ya kuchefua dhidi ya watu weusi.Alirekodiwa kwa siri na kituo cha televisheni cha Sky akisema kuwa watu weusi wana IQ (uwezo wa akili) ndogo,na watoto weusi wakikua sanasana wataishia kukaba watu (vibaka au majambazi).Aliendelea kusema,hapa namnukuu “suala hapa sio kama tunawachukia watu weusi bali ni kama wao ni tishio kwa amani,utulivu na utamaduni wa jamii ya Kiingereza…watoto weusi wakikua watanyonya uchumi wetu na kujaza magereza yetu na pengine kukukaba…huko Afrika kusini mwa jangwa la Sahara hakuna ustaarabu wowote,na hakuna maendeleo ya sayansi…”Kwa kweli ilikuwa inauma kuangalia upuuzi huo kwenye runinga,lakini ni hali tunayoishi nayo hapa kila siku.

Miongoni mwa mambo “halali” yanayowapa nguvu wabaguzi hawa ni vitendo vya baadhi ya wageni na hasa weusi kujihusisha na uhalifu au mambo mengine yasiyofaa katika jamii.Kwa wao,samaki mmoja akioza basi wote wameoza,yaani mtu mmoja mweusi akihusika kwenye uhalifu basi watu wote weusi ni wahalifu.Na kwa BNP sio weusi tu wanaolengwa.Chama hicho kilipata “pumzi” ya kutosha kupinga sera za uhamiaji na ujio wa wageni hapa Uingereza baada ya matukio ya kujilipua mabomu kwa kujitoa mhanga mjini London mwezi Julai mwaka jana. “Vita” ya BNP dhidi ya wageni ikapamba moto na sasa walengwa wakuu wakawa watu wenye asili Asia (hasa Wapakistani).Watatu kati ya waliojilipua mabomu ya muhanga walikuwa Waingereza wenye asili ya Pakistani,na kwa chama hicho cha kibaguzi hiyo ilikuwa sababu tosha ya kuwajumuisha watu wenye asili ya Pakistani na Asia kwa ujumla,na wageni wengine kuwa ni tishio kwa maisha ya Taifa hili.

Huko nyubani moja ya mambo ambayo Watanzania tunajivunia sana ni jinsi “tunavyojichanganya” bila kujali kabila,dini au jinsia.Nikisema “kujichanganya” namaanisha ushirikiano,upendo na maelewano,na sio kukosa msimamo kama maana halisi ya neno ilivyo.Niliwahi kusikia stori flani siku za nyuma inayohusu timu moja ya soka kutoka nchi flani ya jirani.Wachezaji wa timu hiyo walipokuwa wanafanya mazoezi walikuwa wanavuta umati mkubwa wa wakazi wa mji wa Arusha,ambako kulikuwa na michuano ya kimataifa.Kilichokuwa kinawashangaza wachezaji hao ni jinsi watazamaji walivyokuwa “wanajichanganya” kana kwamba ni watu wa kabila moja.Nchi wanayotoka wachezaji,kama zilivyo nchi kadhaa za Afrika,inasifika sana kwa ukabila.Inasemekana katika nchi hiyo ni nadra watu wanaotoka makabila tofauti kuwa marafiki wa dhati.Sasa walipoona baadhi ya watazamaji “wanagongeana sigara” na kutia stori kana kwamba wanaishi nyumba moja,ilikuwa ni jambo la kushangaza sana kwao.Huenda waliondoka Arusha wakiwa na fundisho flani.
Rafiki yangu mmoja,Profesa Tunde Zack-Williams,aliwahi kuniambia kwamba napaswa kujivuna kuwa Mwafrika kutoka Tanzania.Alinieleza kwamba kwa uzoefu wake mwenyewe kama mwanataaluma na Mwafrika,Watanzania ni watu waliojaliwa na “karama” ya mshikamano,upendo na umoja,na wanawaheshimu sana wageni bila kujali wanatoka wapi.Profesa huyo ni mzaliwa wa Sierra Leone,nchi ambayo imeathiriwa sana vita vya wenyewe,na amekuwa akiwasaidia sana kitaaluma vijana wa Kiafrika.Rafiki yangu mwingine anayetoka Sudan aliniambia kwamba alishangaa sana alipofika Tanzania kwa mara ya kwanza,kwa sababu licha ya nchi yetu kuwa na makabila zaidi ya 120 hakuona dalili zozote za watu kubaguana kwa misingi ya kikabila.

Hata hivyo,katika siku za hivi karibuni kumeanza kujitokeza dalili za baadhi ya watu kuchoshwa na “ujiko” huo tulionao ndani na nje ya Afrika.Binafsi,nafanya utafiti unaohusu masuala ya dini na siasa.Sintoongelea sana utafiti huo kwa vile bado “uko jikoni” lakini miongoni mwa matokeo yake ya awali ni dalili kuwa kuna watu au vikundi flani vya jamii vinavyotumia dini kujenga mpasuko katika jamii kwa manufaa yao binafsi.

Kibaya zaidi ni dalili kwamba baadhi ya Watanzania ambao tuna haki ya kuwaita “wageni” wanapoanza kujiingiza kwenye kuleta chokochoko kwenye jamii yetu iliyozowea amani.Siku zote tumekuwa tukiheshimiana na kupendana bila kujali kuwa flani alizaliwa Ifakara au New Delhi.Lakini kama BNP inavyopata “nguvu halali ya kusema ovyo” pindi wageni “wanapoharibu” inaweza kufika mahali Watanzania wazawa wakaanza kujenga chuki dhidi ya wale ambao licha ya “ugeni” wao wanachochea mpasuko katika nchi yetu.Na si “wageni” tu bali hata wale wanaotumia nafasi zao za juu katika jamii kutukoroga.Waasisi wa Taifa letu walifanya kazi kubwa sana kutufikisha hapa tulipo,na nawausia Watanzania wenzangu tusifumbe macho pale wale tulikowakaribisha kwa upendo (na maswahiba zao) wanapoanza kutuletea dharau na chokochoko kwenye nchi yetu.

Alamsiki

0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.