27 Jul 2007

Asalam aleykum,

Katika makala iliyopita niliwapa kituko kimoja kuhusu memba 7 wa kabineti ya Bwana Gordon Brown ambao walikiri hadharani kuwa walishawahi kuvuta bangi wakati wa ujana wao.Maendeleo zaidi (“update”) kuhusu stori hiyo ni kwamba hadi sasa idadi hiyo imefikia mawaziri 10.Lakini wananchi wanaonekana hawajashtushwa sana na “confessions” (vitubio…naamini niko sahihi hapa,au kuna neno jingine linalowakilisha wingi wa kutubu?BAKITA msaada tafadhali) pengine kwa sababu wananchi mawaziri hao watahukumiwa na utendaji wao wa kazi na sio historia zao za kale.Joji Bushi,huyu raisi wa sasa wa Marekani alikuwa “mtu wa matingas” (mlevi) kabla hajamrejea Bwana,lakini ulevi wake wa zamani haukuwa kikwazo kwa yeye kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa ulimwenguni.Hata mie nadhani sio vema kumhukumu mtu kwa mambo alofanya zamani,alimradi anayofanya sasa yawe yanaridhisha.Wengi tunafahamu kwamba kuna wale waliosoma seminari na baadae kuingia kuutumikia umma,lakini si ajabu kukuta baadhi yao ni wala rushwa.Kwa maana hiyo,yayumkinika kusema kuwa bora kuwa mtu ambaye kwenye ujana wake alifanya mambo yasiyopendeza lakini sasa anafanya yale yanayotakiw,a kuliko yule ambaye CV yake ya ujana wake ni “supa” lakini kwa sasa anashiriki kuhujumu uchumi wa Taifa letu “changa” (nadhani neno “changa” sasa limeshapitwa na wakati maana taifa letu lina umri wa miaka 45,na naamini huko mtaani ukimwita mtu mwenye umri huo “mchanga” basi patakuwa hapakaliki hapo).

Kwa wale waliokuwa wanafuatilia stori ya Shambo,yule ng’ombe “mtakatifu” kwa Wahindu wa huko Skanda Valle,magharibi ya Wales,habari “latest” ni kwamba “ng’ombe-mungu” huyo amepelekwa mbele ya haki baada ya polisi 30 kuvamia hekalu lake na kumchukua kwa ajili ya kwenda kumchinja.Kwa wale ambao stori hii iliwapitia kando,ni kwamba Shambo alitakiwa kuuwawa baada ya kugundulika kuwa ana kifua kikuu (TB),na hivyo kuhatarisha afya za mifugo mingine katika eneo hilo.Lakini,Shambo si ng’ombe wa kawaida,bali ni “mungu” wa Wahindu,na waumini waliapa kuwa hawako tayari kuona “mungu” wao huyo akiuawa na binadamu.Baada ya mamlaka husika (DEFRA) kuwafahamisha waumini kuwa Shambo anapaswa kuuawa ili kuzuwia kuenea ugonjwa aliokuwa nao.Waumini walipinga uamuzi huo na hatimaye wakakata rufaa Mahakama Kuu ambapo amri ya kumuua “mungu” huyo ilitengeliwa.Lakini mamlaka husika zikaamua kukata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo iliamualiwa kuwa Shambo anastahili kuuawa.Zoezi la kumchukua “ng’ombe-mungu” huyo halikuwa jepesi kwani waumini walijitutumua kadri ya uwezo wao kuhakikisha kuwa Shambo hachukuliwi,na hapo ndipo ikabidi waletwe polisi kumaliza songombingo hiyo iliyochukua zaidi ya masaa 12,huku sakata zima kati ya waumini na DEFRA likiwa limedumu kwa wiki 12.Pengine kufanana kwa namba 12 katika matukio hayo kunaweza kuwa uhusiano na “umungu” wa ng’ombe huyo.

Tukiachana na “safari ya mwisho” ya ngombe-mungu Shambo,tuelekeze macho yetu huko nyumbani.Hebu ngoja kidogo.Kuna nchi inaitwa Guam.Je unaweza ku-guess iko wapi?Enewei,nilikuwa nachemsha kidogo ubongo wako.Nchi hiyo ni “koloni” la Marekani (well,iko chini ya mamlaka ya Marekani) na kwa mujibu wa sensa ya karibuni Guam ina wakazi 173,456.Bila kuingia kwa undani kuhusu jiographia,siasa na porojo nyingie kuhusu ka-nchi hako ambako ni kisiwa,ngoja nikudokezee kuhusu timu yake ya taifa.Hebu angalia matokeo ya mechi zake za hivi karibuni.Ilifungwa 10-0 na China,ikafungwa 15-1 na Hong Kong,na ikalambwa 9-0 na Korea ya Kusini.Kwa sasa inashilia nafasi ya 199 kwenye listi ya FIFA ya ubora wa soka duniani.Nafasi hiyo ndio ya mwisho kabisa,lakini habari njema kwa nchi hiyo ni kwamba haiko pekee kwenye nafasi hiyo kwani Djibouti, East Timor, Belize, the US Virgin Islands, Montserrat, American Samoa, Sao Tome e Príncipe na Aruba pia zinashikilia kwa pamoja nafasi hiyo ya 199.Wahenga walisema kilio cha wengi ni harusi.Kocha wa timu hiyo anawalaumu zaidi wachezaji wake kwa tabia yao ya kuendekeza pati,kujichanganya na magelifrendi wao (au wake zao) na kuthamini zaidi mambo ya binafsi kuliko majukumu yao ya soka.Pia wachezaji wa timu hiyo wanashutumiwa kwa kuzembea mazoezi,na hata wanapofika mazoezini wengi wao huwa wamechoka kutokana na “kujirusha” (sio kujirusha kimazoezi bali “kiaina”).Kiungo wa timu hiyo,Alan Jamison,ameeleza kuwa mara kwa mara akiwa usingizini amekuwa akisumbiliwa na ndoto moja:anaota kuwa amefunga goli (la mpirani…) na uwanja unalipuka kwa mayowe.Kwa bahati mbaya kila asubuhi anapoamka anagundua kuwa timu yake haijapata na haitarajii kupata ushindi hivi karibuni.

Nimeizungumzia timu ya taifa ya Guam ili kutengeneza mazingira mazuri ya kuitupia madongo timu yetu ya iliyokwenda kutuaibisha huko Aljeria.Kulikuwa na umuhimu gani wa kuingia gharama ya kuwapeleka watalii hao kama walikuwa hawajajiaanda kwa mashindano?Enewei,mie najua kwanini walipelekwa hivyohivyo:POSHO.Posho ya safari.Linapokuja suala la posho ya safari usishangae chama cha mchezo wa bao au drafti (kwa mfano) kumpeleka mchezaji kipofu.Wanajua kabisa kuwa kipofu hawezi kucheza drafti au bao lakini hilo haliwasumbui viongozi hao kwani tayari watakuwa wamejipatia visenti vya kupeleka kwenye nyumba ndogo zao (utafiti usio rasmi umeonyesha kuwa asilimia kubwa ya fedha inayopatikana kwa rushwa au ubadhirifu inaishia kwenye nyumba ndogo).Viongozi walichagua wanamichezo wazembe wanastahili lawama nyingi zaidi kuliko wazembe hao waliokwenda kututia aibu huko Aljeria (ukiachia huyo mmoja aliyeambulia medali ya fedha).Nawalaumu zaidi viongozi hao kwa vile hawana cha kujitetea kwa kuchagua wanamichezo wasio na uwezo wa kutuletea ushindi.Angalau timu ya taifa ya Guam inaweza kujitetea kwani kijinchi chenyewe kina watu wachache zaidi ya wilaya ya Kinondoni.Tanzania ina watu zaidi ya milioni 30,na miongoni mwao ni wanamichezo wenye vipaji ambavyo aidha vinapuuzwa,haviendelezwi au vinaminywa na viongozi walafi wa madaraka na fedha lakini hawana hata chembe ya mawazo endelevu ya ushindi kwenye michezo.Kwenye nchi za kidikteta viongozi kama hawa wanaporejea kutoka mashindanoni wanapokelewa na karandinga kuelekea Segerea.

Majuzi tumesikia EWURA ikidai kwamba waziri Meghji kadanganya kuhusu uwezo wa mamlaka hiyo kuwabana wafanyabiashara wa mafuta.Sijui nani anasema ukweli kwani sijaona sheria iliyoanzisha mamlaka hiyo ila ni dhahiri kuwa kuna kitu hakiko sawia.Kuna umuhimu gani wa kuwa na mamlaka isiyo na uwezo wa kisheria katika kutekeleza majukumu yake?Au kwa mfano sahihi,kuna umuhimu gani wa kufuga mbwa mwenye mapengo na ambaye akisikia kelele za “mwizi,mwizi” anakwenda kujificha?Inanikumbusha mchapo mmoja nilowahi kusimuliwa huko Tanga kuwa baba mwenye nyumba mmoja alipoamshwa na mkewe na wanawe kuwa wamesikia watu wanavunja dirisha akaanza kulia na kuwaacha watoto hawajui la kufanya.Tukiachana na mifano hiyo,swali la muhimu ni kuwa hivi huku kurushiana mpira kunamsaidia vipi mwananchi wa kawaida?Nilishapendekeza huko nyuma kwamba njia nyepesi ya kudhibiti bei ya mafuta ni “kuchimba mkwara wa nguvu” kwamba atakayezidisha bei stahili ya mafuta atafutiwa leseni.La muhimu hapa sio kwamba amri hiyo itolewe na Meghji au EWURA,bali itekelezwe.Hakuna mfanyabiashara aliye tayari kufutiwa leseni na kwa hakika watatekeleza amri hiyo.

Mwisho,tumeambiwa na Profesa Maghembe kuwa wizara yake ina baadhi ya watendaji ambao kwa jina jepesi tunaweza kuwaita mafisadi.Hao ni pamoja na wale wanaoshiriki kwenye biashara ilopigwa marufuku ya kusafirisha magogo nje.Waziri anastahili pongezi kwa kuweka bayana uozo huo.Lakini unategemea nini kwenye wizara ambayo Severe alipewa uhamisho na akagoma kuhama na hadi leo bado anapeta?Prof Maghembe anasema amepeleka majina ya wahusika kwenye “ngazi za juu” kwa vile yeye hana uwezo kisheria kuwawajibisha.Pengine tunachopaswa kufahamu ni kuwa lini majina hayo yamewasilishwa huko ngazi za juu,na kwanini mafisadi hao bado wanaendelea kuuza maliasili zetu.Sintoshangaa kusikia mmoja wao akiitisha press conference kama ile ya gavana wetu na “kutupa somo la uzalendo.”Kwa vile mafisadi hawa wanajulikana,kuendelea kuwaacha madarakani ni sawa na kuwapa nafasi ya kufuja kwa kasi zaidi (kwa vile wanaelewa kuwa maamuzi kutoka “ngazi za juu” yanaweza kuwahamisha kutoka kwenye ulaji) na kuharibu ushahidi dhidi ya tuhuma zinazowakabili.Sheria ichukue mkondo wake ili kuzuia virusi vya ufisadi kusambaa zaidi (wanaoona mafisadi hao wanazidi kupeta wanashawishika kuiga ufisadi wao).

Nimalizie kwa kumpongeza Waziri Mwapachu kwa kuhitimisha bethidei yake kwa kuwatembelea watumishi wa Wizara yake huko Dodoma.Ni mfano wa kuigwa.Pia hoja yake ya kuwa na “data bank” ya simu ni nzuri (japo ufanisi wake ni mgumu) na inaweza kuigwa kwenye maeneo mengine kwa mfano kuanzisha daftari la kudumu la wala rushwa.

Alamsiki


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.