Showing posts with label WAZIRI. Show all posts
Showing posts with label WAZIRI. Show all posts

13 Dec 2007

Makala ya wiki hii ndani ya gazeti la Mtanzania inaangalia namna mafisadi wa kigeni wanavyonufaika kutokana na uzembe wa baadhi ya Watanzania wenzetu tuliowakabidhi dhamana za uongozi.Lakini hata kama wawekezaji hao wangekuwa waadilifu hivi kweli ndoto ya "maisha bora kwa kila Mtanzania" itatimia wakati Waziri mwenye dhamana ya maendeleo ya sekta ya Maji (Waziri wa Maji) nae ni miongoni mwa wadaiwa sugu wa maji waliokatiwa huduma hiyo na DAWASCO?Makala nzima hii hapa chini

Waziri wa Maji anasubiri nini ofisini?

na evarist chahali, uskoch


Hadi muda huu haijaniingia akilini niliposoma habari kwamba aliyekuwa mwekezaji kwenye hoteli ya Millenium Tower “ameingia mitini” na kuacha deni kubwa la kodi ya jengo na bili nyingine.Kwa mujibu wa uongozi wa LAPF ambao ndio wamiliki wa jengo hilo,mwekezaji huyu alianza kuonyesha dalili za ubabaishaji muda mrefu kidogo kabla hajaamua kutoroka,lakini nachoshindwa kuelewa ni kwanini uongozi huo haukuchua hatua za tahadhari kuhakikisha kwamba wanalipwa kilicho chao kabla huyu jamaa hajaondoka kimyakimya.

Pengine ni vema nikitoa mfano halisi wa taratibu za upangaji zilivyo hapa Uingereza.Ukitembelea miji mikubwa kama London,Manchester,Birmingham na mingineyo,au hata kwenye mji mdogo kama Aberdeen (hapa ninapoishi) utakuta kuna jamaa wanaopata hifadhi ya makazi kwenye viambaza vya maduka na majengo mengine huko mjini kati.Hawa ni watu wasio na makazi,na japo wengine wameishia katika hali hiyo kutokana na uzembe wao,wapo wale ambao si rahisi kwao kupata makazi kutokana na ugumu katika utaratibu mzima wa kuingia mikataba ya makazi.Wamiliki wa majengo ya kupangisha wako makini mno kuhakikisha kwamba hawapangishi wababaishaji.

Na kwa wageni inakuwa suala zito zaidi kwani nyaraka kadhaa zinahitajika kabla mwenye jengo hajakukabidhi funguo la pango la kuishi.Mara nyingi taratibu za kupanga jengo huhusisha wanasheria ili pindi upande mmoja utakapokwenda kinyume na mkataba wa pango basi iwe rahisi kuhakikisha haki inapatikana.Hapa nawazungumzia wamiliki binafsi na sio makampuni yenye majengo ya kupangisha.

Pengine wamiliki wa nyumba za kupanga wanakuwa makini kwa vile wana uchungu na mali zao,lakini pengine ni kutokana na utaratibu mzuri wenye kumnufaisha mwenye nyumba na mpangaji.Lakini hata huko nyumbani kuna taratibu kama hizo japo zinatofautiana kwa kiwango flani.Inawezekana mwenye nyumba unayotaka kuhamia asijali sana kudadisi ulikotokea,lakini mara nyingi utaratibu unaofahamika ni kutanguliza malipo ya awali ambayo huweza kuwa sawa na kodi ya nusu mwaka au mwaka mzima.Na wengine hufikia hatua ya kuomba “kilemba” kana kwamba anayetaka kupanga anachumbia kwa mwenye nyumba,yote hiyo ni kwa mwenye mali yake kuhakikisha kuwa hatoishia kujilaumu baada ya kumruhusu mpangaji kuingia kwenye jengo lake.

Naamini kabisa kwamba laiti jengo la hoteli ya Millenium Tower lingekuwa mali ya mtu binafsi basi huyo mwekezaji tapeli asingeweza kutoroka kirahisi namna hiyo.Na kwanini watueleze sasa kuwa mpangaji wao kaingia mitini ilhali walishakuwa na matatizo naye kwa muda mrefu?Jibu jepesi kwangu ni kwamba hawana uchungu na fedha za waliowezesha jengo hilo kufikia hapo lilipo.Na hili ni tatizo kubwa sana katika hii inayoitwa mifuko ya jamii.Maamuzi ya mali zinazomilikiwa na mifuko hiyo yamebaki mikononi mwa watu wachache ambao pindi hasara ikitokea wanaishia kutoa sababu moja au nyingine na wala sio kuelezea namna gani hasara hiyo itakavyofidiwa

Natambua kwamba ni vigumu kuiwezesha demokrasia ichukue mkondo wake katika mfuko wa jamii wenye wanachama elfu kadhaa kama sio laki na kitu.Demokrasia nayozungumzia hapa ni ile ya maamuzi yanayofikiwa kwa makubalino ya wanachama wote.Hata hivyo,hiyo haitoi nafasi kwa wachache waliokabidhiwa dhamana ya kufanya maamuzi kwa niaba ya wanaowawakilisha wakafanya mambo kiholela kwa vile tu fedha zinazoteketea hazitoki mifukoni mwao.

Tumeshuhudia sehemu kadhaa zikibadilishwa majina kila mwaka baada ya wawekezaji wa awali kuondoka na kurusha mpira kwa wawekezaji wapya.Kubadili jina la biashara sio kosa kisheria kwani hata jina la mtu binafsi linawezwa kubadilishwa mahakamani.Tatizo hapa ni kwamba wawekezaji matapeli hutumia misamaha ya kodi na masharti mepesi wanayopatiwa wakati wanaingia mikataba na wakishachuma faida ya kutosha wanaondoka kistaarabu (kwa kutangaza kwamba wamekuwa wanapata hasara) au kibaradhuli (kwa kuingia mitini kama huyo mwekezaji wa zamani wa hoteli ya Millenium Tower).

Mwaka juzi nilialikwa kumtembelea rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani.Nilipofika ubalozi wa nchi hiyo jijini London kuomba viza,nilijionea mwenyewe namna gani wenzetu wanavyojithamini wao kwanza kabla ya wageni.Utaratibu wa kuingia hapo hauna tofauti na ule wa zamani katika ubalozi wa Uingereza hapo Dar ambapo waomba viza walikuwa wanalazimika kukesha usiku kucha kuwahi foleni ya kuonana na maofisa wa ubalozi huo.Japo sina hakika lakini nadhani utaratibu wa sasa wa kufanya maombi mtandaoni unaweza kuwa umepunguza tatizo hilo.Katika ubalozi huo wa Marekani hapo London,raia wa Marekani hawapatwi na usumbufu wa kukaa kwenye foleni ndefu au kupigwa na mvua au kibaridi (kulingana na majira ya mwaka) bali hupewa upendeleo maalumu.

Na hata kwenye maeneo ya kuangalia nyaraka za uraia na makazi kwenye viwanja vya ndege,wenzetu hujitahidi kuhakikisha kuwa raia wao hawapati usumbufu mkubwa kama ule tunaoupata wageni na wapita njia kama akina sie.Angalau pale uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere kuna kutenganishwa kati ya Watanzania,raia wa Afrika Mashariki na wengineo,lakini wengi mtakubaliana nami kuwa tuna kasumba ya kuwanyenyekea wageni kulko tunavyowanyenyekea Watanzania wenzetu.Wawekezaji feki wamekuwa wakiitumia vizuri fursa hiyo sambamba na ubabaishaji wa taratibu za mikataba kuhakikisha kwamba wanachuma vya kutosha na pale wanapovimbiwa wanaamua kuondoka bila matatizo.

Wageni hapa Uingereza wana uwezo wa kuomba viza ya makazi kwa kigezo cha biashara ndogondogo kwa wale wenye uwezo mdogo au biashara kubwa kwa wale wenye uwezo wa kutosha.Nizungumzie hilo kundi la kwanza ambalo kimsingi linatoa mwanya kwa wageni wengi zaidi kutokana na ukweli kwamba mtaji unaohitajika sio mkubwa sana.Kinachowakwamishwa wengi ni umakini katika utaratibu mzima ambao hautoi fursa hata chembe kwa wababaishaji.Mwingereza hawezi kukubali uje uwekeze nchini mwake kwenye sekta ya usafiri wa reli ilhali unategemea mabehewa na injini chakavu kutoka huko ulikotoka.

Tatizo la kunyenyekea haliishii kwenye uwekezaji pekee bali hata kwa taasisi nyingine zinazopaswa kujiendesha kibiashara badala ya kutegemea ruzuku ya serikali.Niliposikia Dawasco ikitangaza kwamba itakata huduma ya maji “kwa vigogo” nilibaki najiuliza kama mamlaka hiyo ingeweza kutoa tishio la namna hiyo iwapo wadeni wake wangekuwa ni wale wa “uswahilini” (kama maji yangekuwa yanapatikana huko).Kama ilivyo kwa Tanesco (na pengine hata TTCL),malalamiko makubwa ya makampuni hayo ni kwamba huwa wanaingiliwa na vigogo kila wanapowabana wadaiwa sugu.Nisichoelewa ni hofu ya vigogo wa makampuni hayo kuchukua hatua madhubuti dhidi ya vigogo wanaowatisha hasa ikizingatiwa kuwa Mkurgenzi wa Dawasco au Tanesco anateuliwa na Rais,kwahiyo wakitishiwa na vigogo wengine wanaweza kabisa kukimbilia kwa Rais kumjulisha wanavyosumbuliwa na vigogo wadaiwa sugu.Japo najua itakuwa ni usumbufu usio na lazima kwa Mkuu wa nchi,lakini naamini kwamba iwapo makampuni yanayokwamishwa na vigogo ambao ni wadeni sugu yakiwajulisha vigogo hao kwamba yanawakatia huduma na “wakileta zao za kuleta” watawaripoti kwa Rais ni lazima watalipa madeni hayo.

Lakini pengine taarifa za hivi karibuni kuwa miongoni mwa wadaiwa wa DAWASCO ni pamoja na Waziri wa Maji zinaweza kutufanya tuionee huruma Mamlaka hiyo.Katika utetezi wake,Waziri huyo anadai kuwa hajawahi kupata huduma ya maji kwa miaka kadhaa,na amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara.Swali linakuja,je iwapo yeye kama waziri wa maji anatumiwa bili ilhali hapatiwi huduma ya maji alifanya jitihada gani kuhakikisha sio yeye tu bali Watanzania wengine hawakumbani na adha hiyo?Mbona alikuwa kimya siku zote hizi?Hivi karibuni,Mkuu wa polisi wa usalama barabarani huko Wales alilazimika kujiuzulu baada ya kunaswa na kamera zinazodhibiti mwendo kasi barabarani akiwa anaendesha gari yake zaidi ya kiwango kinachoruhisiwa kisheria.Kwa kuvunja sheria aliyopaswa kuisimamia,kamanda huyo alilazimika kujiuzulu.

Sitarajii waziri wa maji kujiuzulu kutokana na deni hilo,na wala sitarajii hilo kwa mawaziri na vigogo wengine wanaodaiwa kwa vile msamiati “KUJIUZULU” ulishafutika kwenye kamusi ya medani ya uongozi huko nyumbani.Ni udhaifu wa namna hii unaowapa jeuri wawekezaji feki kwani kabla ya kuingia mikataba huwa wanasema udhaifu wa hao waliopewa mamlaka ya kusaini mikataba ya uwekezaji.Kwa mtaji huu,ndoto ya maisha bora kwa kila Mtanzania ina safari ndefu sana kutimia.


27 Jul 2007

Asalam aleykum,

Katika makala iliyopita niliwapa kituko kimoja kuhusu memba 7 wa kabineti ya Bwana Gordon Brown ambao walikiri hadharani kuwa walishawahi kuvuta bangi wakati wa ujana wao.Maendeleo zaidi (“update”) kuhusu stori hiyo ni kwamba hadi sasa idadi hiyo imefikia mawaziri 10.Lakini wananchi wanaonekana hawajashtushwa sana na “confessions” (vitubio…naamini niko sahihi hapa,au kuna neno jingine linalowakilisha wingi wa kutubu?BAKITA msaada tafadhali) pengine kwa sababu wananchi mawaziri hao watahukumiwa na utendaji wao wa kazi na sio historia zao za kale.Joji Bushi,huyu raisi wa sasa wa Marekani alikuwa “mtu wa matingas” (mlevi) kabla hajamrejea Bwana,lakini ulevi wake wa zamani haukuwa kikwazo kwa yeye kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa ulimwenguni.Hata mie nadhani sio vema kumhukumu mtu kwa mambo alofanya zamani,alimradi anayofanya sasa yawe yanaridhisha.Wengi tunafahamu kwamba kuna wale waliosoma seminari na baadae kuingia kuutumikia umma,lakini si ajabu kukuta baadhi yao ni wala rushwa.Kwa maana hiyo,yayumkinika kusema kuwa bora kuwa mtu ambaye kwenye ujana wake alifanya mambo yasiyopendeza lakini sasa anafanya yale yanayotakiw,a kuliko yule ambaye CV yake ya ujana wake ni “supa” lakini kwa sasa anashiriki kuhujumu uchumi wa Taifa letu “changa” (nadhani neno “changa” sasa limeshapitwa na wakati maana taifa letu lina umri wa miaka 45,na naamini huko mtaani ukimwita mtu mwenye umri huo “mchanga” basi patakuwa hapakaliki hapo).

Kwa wale waliokuwa wanafuatilia stori ya Shambo,yule ng’ombe “mtakatifu” kwa Wahindu wa huko Skanda Valle,magharibi ya Wales,habari “latest” ni kwamba “ng’ombe-mungu” huyo amepelekwa mbele ya haki baada ya polisi 30 kuvamia hekalu lake na kumchukua kwa ajili ya kwenda kumchinja.Kwa wale ambao stori hii iliwapitia kando,ni kwamba Shambo alitakiwa kuuwawa baada ya kugundulika kuwa ana kifua kikuu (TB),na hivyo kuhatarisha afya za mifugo mingine katika eneo hilo.Lakini,Shambo si ng’ombe wa kawaida,bali ni “mungu” wa Wahindu,na waumini waliapa kuwa hawako tayari kuona “mungu” wao huyo akiuawa na binadamu.Baada ya mamlaka husika (DEFRA) kuwafahamisha waumini kuwa Shambo anapaswa kuuawa ili kuzuwia kuenea ugonjwa aliokuwa nao.Waumini walipinga uamuzi huo na hatimaye wakakata rufaa Mahakama Kuu ambapo amri ya kumuua “mungu” huyo ilitengeliwa.Lakini mamlaka husika zikaamua kukata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo iliamualiwa kuwa Shambo anastahili kuuawa.Zoezi la kumchukua “ng’ombe-mungu” huyo halikuwa jepesi kwani waumini walijitutumua kadri ya uwezo wao kuhakikisha kuwa Shambo hachukuliwi,na hapo ndipo ikabidi waletwe polisi kumaliza songombingo hiyo iliyochukua zaidi ya masaa 12,huku sakata zima kati ya waumini na DEFRA likiwa limedumu kwa wiki 12.Pengine kufanana kwa namba 12 katika matukio hayo kunaweza kuwa uhusiano na “umungu” wa ng’ombe huyo.

Tukiachana na “safari ya mwisho” ya ngombe-mungu Shambo,tuelekeze macho yetu huko nyumbani.Hebu ngoja kidogo.Kuna nchi inaitwa Guam.Je unaweza ku-guess iko wapi?Enewei,nilikuwa nachemsha kidogo ubongo wako.Nchi hiyo ni “koloni” la Marekani (well,iko chini ya mamlaka ya Marekani) na kwa mujibu wa sensa ya karibuni Guam ina wakazi 173,456.Bila kuingia kwa undani kuhusu jiographia,siasa na porojo nyingie kuhusu ka-nchi hako ambako ni kisiwa,ngoja nikudokezee kuhusu timu yake ya taifa.Hebu angalia matokeo ya mechi zake za hivi karibuni.Ilifungwa 10-0 na China,ikafungwa 15-1 na Hong Kong,na ikalambwa 9-0 na Korea ya Kusini.Kwa sasa inashilia nafasi ya 199 kwenye listi ya FIFA ya ubora wa soka duniani.Nafasi hiyo ndio ya mwisho kabisa,lakini habari njema kwa nchi hiyo ni kwamba haiko pekee kwenye nafasi hiyo kwani Djibouti, East Timor, Belize, the US Virgin Islands, Montserrat, American Samoa, Sao Tome e Príncipe na Aruba pia zinashikilia kwa pamoja nafasi hiyo ya 199.Wahenga walisema kilio cha wengi ni harusi.Kocha wa timu hiyo anawalaumu zaidi wachezaji wake kwa tabia yao ya kuendekeza pati,kujichanganya na magelifrendi wao (au wake zao) na kuthamini zaidi mambo ya binafsi kuliko majukumu yao ya soka.Pia wachezaji wa timu hiyo wanashutumiwa kwa kuzembea mazoezi,na hata wanapofika mazoezini wengi wao huwa wamechoka kutokana na “kujirusha” (sio kujirusha kimazoezi bali “kiaina”).Kiungo wa timu hiyo,Alan Jamison,ameeleza kuwa mara kwa mara akiwa usingizini amekuwa akisumbiliwa na ndoto moja:anaota kuwa amefunga goli (la mpirani…) na uwanja unalipuka kwa mayowe.Kwa bahati mbaya kila asubuhi anapoamka anagundua kuwa timu yake haijapata na haitarajii kupata ushindi hivi karibuni.

Nimeizungumzia timu ya taifa ya Guam ili kutengeneza mazingira mazuri ya kuitupia madongo timu yetu ya iliyokwenda kutuaibisha huko Aljeria.Kulikuwa na umuhimu gani wa kuingia gharama ya kuwapeleka watalii hao kama walikuwa hawajajiaanda kwa mashindano?Enewei,mie najua kwanini walipelekwa hivyohivyo:POSHO.Posho ya safari.Linapokuja suala la posho ya safari usishangae chama cha mchezo wa bao au drafti (kwa mfano) kumpeleka mchezaji kipofu.Wanajua kabisa kuwa kipofu hawezi kucheza drafti au bao lakini hilo haliwasumbui viongozi hao kwani tayari watakuwa wamejipatia visenti vya kupeleka kwenye nyumba ndogo zao (utafiti usio rasmi umeonyesha kuwa asilimia kubwa ya fedha inayopatikana kwa rushwa au ubadhirifu inaishia kwenye nyumba ndogo).Viongozi walichagua wanamichezo wazembe wanastahili lawama nyingi zaidi kuliko wazembe hao waliokwenda kututia aibu huko Aljeria (ukiachia huyo mmoja aliyeambulia medali ya fedha).Nawalaumu zaidi viongozi hao kwa vile hawana cha kujitetea kwa kuchagua wanamichezo wasio na uwezo wa kutuletea ushindi.Angalau timu ya taifa ya Guam inaweza kujitetea kwani kijinchi chenyewe kina watu wachache zaidi ya wilaya ya Kinondoni.Tanzania ina watu zaidi ya milioni 30,na miongoni mwao ni wanamichezo wenye vipaji ambavyo aidha vinapuuzwa,haviendelezwi au vinaminywa na viongozi walafi wa madaraka na fedha lakini hawana hata chembe ya mawazo endelevu ya ushindi kwenye michezo.Kwenye nchi za kidikteta viongozi kama hawa wanaporejea kutoka mashindanoni wanapokelewa na karandinga kuelekea Segerea.

Majuzi tumesikia EWURA ikidai kwamba waziri Meghji kadanganya kuhusu uwezo wa mamlaka hiyo kuwabana wafanyabiashara wa mafuta.Sijui nani anasema ukweli kwani sijaona sheria iliyoanzisha mamlaka hiyo ila ni dhahiri kuwa kuna kitu hakiko sawia.Kuna umuhimu gani wa kuwa na mamlaka isiyo na uwezo wa kisheria katika kutekeleza majukumu yake?Au kwa mfano sahihi,kuna umuhimu gani wa kufuga mbwa mwenye mapengo na ambaye akisikia kelele za “mwizi,mwizi” anakwenda kujificha?Inanikumbusha mchapo mmoja nilowahi kusimuliwa huko Tanga kuwa baba mwenye nyumba mmoja alipoamshwa na mkewe na wanawe kuwa wamesikia watu wanavunja dirisha akaanza kulia na kuwaacha watoto hawajui la kufanya.Tukiachana na mifano hiyo,swali la muhimu ni kuwa hivi huku kurushiana mpira kunamsaidia vipi mwananchi wa kawaida?Nilishapendekeza huko nyuma kwamba njia nyepesi ya kudhibiti bei ya mafuta ni “kuchimba mkwara wa nguvu” kwamba atakayezidisha bei stahili ya mafuta atafutiwa leseni.La muhimu hapa sio kwamba amri hiyo itolewe na Meghji au EWURA,bali itekelezwe.Hakuna mfanyabiashara aliye tayari kufutiwa leseni na kwa hakika watatekeleza amri hiyo.

Mwisho,tumeambiwa na Profesa Maghembe kuwa wizara yake ina baadhi ya watendaji ambao kwa jina jepesi tunaweza kuwaita mafisadi.Hao ni pamoja na wale wanaoshiriki kwenye biashara ilopigwa marufuku ya kusafirisha magogo nje.Waziri anastahili pongezi kwa kuweka bayana uozo huo.Lakini unategemea nini kwenye wizara ambayo Severe alipewa uhamisho na akagoma kuhama na hadi leo bado anapeta?Prof Maghembe anasema amepeleka majina ya wahusika kwenye “ngazi za juu” kwa vile yeye hana uwezo kisheria kuwawajibisha.Pengine tunachopaswa kufahamu ni kuwa lini majina hayo yamewasilishwa huko ngazi za juu,na kwanini mafisadi hao bado wanaendelea kuuza maliasili zetu.Sintoshangaa kusikia mmoja wao akiitisha press conference kama ile ya gavana wetu na “kutupa somo la uzalendo.”Kwa vile mafisadi hawa wanajulikana,kuendelea kuwaacha madarakani ni sawa na kuwapa nafasi ya kufuja kwa kasi zaidi (kwa vile wanaelewa kuwa maamuzi kutoka “ngazi za juu” yanaweza kuwahamisha kutoka kwenye ulaji) na kuharibu ushahidi dhidi ya tuhuma zinazowakabili.Sheria ichukue mkondo wake ili kuzuia virusi vya ufisadi kusambaa zaidi (wanaoona mafisadi hao wanazidi kupeta wanashawishika kuiga ufisadi wao).

Nimalizie kwa kumpongeza Waziri Mwapachu kwa kuhitimisha bethidei yake kwa kuwatembelea watumishi wa Wizara yake huko Dodoma.Ni mfano wa kuigwa.Pia hoja yake ya kuwa na “data bank” ya simu ni nzuri (japo ufanisi wake ni mgumu) na inaweza kuigwa kwenye maeneo mengine kwa mfano kuanzisha daftari la kudumu la wala rushwa.

Alamsiki


13 Jul 2007

Asalam aleykum,

Baada ya matukio ya hivi karibuni yaliyotuweka matumbo moto kufuatiwa mahayawani flani kuamua kuendesha kampeni yao ya kishetani ya kutaka kulipua mabomu huko London na hapo Glasgow (Waskotishi bado hawaamini kuwa ugaidi umeingia kwenye ardhi yao) sio wazo baya kuanza makala hii kwa habari “nyepesi nyepesi.” Gazeti la Daily Mail la hapa liliripoti hivi karibuni kuhusu matokeo ya utafiti yaliyoonyesha kuwa wanaume wenye aibu wana nafasi kubwa ya kupata magonjwa ya moyo kuliko wale wasio na aibu!Hizi tafiti nyingine…we acha tu.Kwa mujibu wa gazeti hilo,utafiti huo ulifanyika kwa kipindi cha miaka 30 uliwahusisha maelfu ya wanaume ambapo watafiti kutoka chuo kikuu cha Northwestern cha Chicago,Marekani walipokuwa wanafanya ufuatiliaji wa wawaliowahoji kwenye utafiti huo walibaini kuwa asilimia 60 kati yao (waliohojiwa) walikuwa wameshafariki,huku chanzo kikuu cha vifo kikiwa “heart attack” (nadhani kwa Kiswahili sahihi ni msongo wa moyo).Mambo hayo!

Na ukisikia duniani kuna mambo usidhani ni utani.Mzembe mmoja amekamatwa huko New Hampshire (Manchester) baada ya kushindikana kwa jaribio lake la kutaka kufanya uporaji benki huku akiwa amejivika matawi ya miti kama “camouflage” (kificho) yake.Jamaa huyo,James Coldwell,aliingia kwenye tawi la benki ya ushirika ya Citizens,huku akiwa amejivika majani na kuwatisha wahudumu wa benki hiyo kabla ya kufanikiwa kuondoka na kitita cha fedha,lakini alinaswa na polisi muda mfupi baadaye kwani triki yake ya “uninja wa majani” haikumsaidia kwa vile majani hayo hayakufunika sura yake,na wanausalama waliweza kuitambua vizuri kwenye CCTV.

Jumuiya ya Ulaya (EU) nayo ilijikuta kwenye wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa filamu fupi kwa ajili ya promosheni ya kuhamasisha Jumuiya hiyo ambapo wahusika kwenye filamu hiyo ya sekunde 44 yenye jina “Let’s Come Together” walikuwa wakifanya “ngono nyepesi” (soft porn).Wapinzani wa wazo la Muungano wa nchi za Ulaya waliishambulia EU kwa kupoteza fedha za walipa kodi kwa kutengeneza filamu hiyo waliyoiona kuwa ni mwendelezo wa ubabaishaji wa Jumuiya hiyo.Nilipomtumia rafiki yangu flani habari hiyo kutoka gazetini alitania kwa kusema labda na sie tunahitaji “kampeni chafu” kama hiyo ya EU “kuuza” wazo la Muungano wa Afrika Mashariki ambao unaelekea kuwakera wadau wengi.

Nae mwanamama Amy Beth Ballamura amaepigwa marufuku kutia mguu kwenye pwani yoyote ya Uingereza baada ya kufanya majaribio zaidi ya 50 ya kujiua kwa kurusha baharini.Miongoni mwa sababu zilizopelekea kuchukuliwa kwa hatua ya kumdibiti mwanamama huyo ni pamoja na kuzitia huduma ya uokoji (emergency services) gharama ya zaidi ya pauni milioni 1 (zaidi ya shilingi bilioni mbili za huko nyumbani) kila wanapoitwa kwenda kumuokoa.Lakini pamoja na “tamaa” yake ya kujitoa roho,askari mmoja aliambulia tuzo ya ushujaa mwaka 2003 baada ya kusikia kelele za kuomba msaada kutoka baharini na kuamua kujitosa majini kufuata kelele hizo,ambapo alifanikiwa kumuokoa mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 44.Cha kushangaza ni kwamba kama kweli alikuwa na nia ya kujitoa uhai sasa hizo kelele za kuomba msaada zilikuwa za nini?

Enewei,baada ya "nyepesi nyepesi" hizo (zote ni habari za kweli na wala sio kuwa “nawapiga fiksi” wasomaji wangu wapendwa) sasa tuangalie mambo ya muhimu zaidi huko nyumbani.Kwanza niseme siafikiani na hoja za Waziri wa Sheria Mama Nagu kwamba Bunge halipaswi kufanya kazi ya kupitia mikataba kabla ya kutiwa saini ili libaki na uhalali wake wa kuiwajibisha Serikali kwa mujibu wa dhamana ya mgawanyo wa mamlaka, kuchunguzana na kuwajibishana.Siafikiani naye kwa sababu hoja za baadhi ya wabunge kuwa mikataba hiyo ifikishwe kwao kabla ya kusainiwa zilizingatia ukweli kwamba kuna mapungufu makubwa yanayoendelea katika suala zima la kusaini mikataba mbalimbali.Mantiki nyepesi (simple logic) inaweza kutueleza kwamba maslahi ya nchi ni muhimu zaidi ya huo mgawanyiko wa madaraka.Hivi kwa mfano wazo la mikataba kuletwa bungeni lingekubaliwa,halafu nchi inufaike kwa kuingia mikataba yenye maslahi kwa Taifa,tatizo linakuwa wapi?Hivi kipi bora,kulinda mgawanyiko wa madaraka huku mikataba ya ajabu ajabu ikiendelea kuwepo au “kupindisha sheria” kwa kuileta mikataba hiyo bungeni kabla haijasainiwa halafu nchi ikanufaika nayo?

Pia nimesoma kwenye gazeti moja la huko nyumbani kwamba lile tishio la wafugaji huko wilayani Kilombero limerejea tena.Nitamke bayana kuwa hili linanihusu binafsi kwa vile mie ni “mwana wa pakaya” naetokea mitaa ya huko.Hawa wafugaji ni wakorofi,watovu wa nidhamu na wavunja sheria wakubwa.Maagizo kadhaa yameshatolewa kuwataka waheshimu sheria za nchi lakini wameamua kuweka pamba masikio.Mamlaka husika zinapaswa kuliangalia suala hili kwa makini zaidi kwani wanachofanya wafugaji hao sio tu kinahatarisha amani (mifugo yao inakula mazao ya wakulima,na hilo pekee linatosha kuzusha ugomvi) lakini pia hawawatakii mema wakulima kwani kwa kuswaga mifugo yao kwenye mashamba wanamaanisha kuwa wanataka wakulima hao wakose chakula na hela wanazojipatia kwa kuuza akiba ya mavuno yao.Hili ni bomu la wakati (time bomb) kwani japo hakuna bondia wa Kindamba (kama yupo basi samahani kwani sijamsikia) lakini hiyo haimaanishi kuwa mtu atakaeswaga mifugo yake kwenye mashamba ataachwa afanye anavyotaka.Hapo itakuwa kuchukua sheria mkononi,na japo mie ni mpinzani mkubwa wa kuchukua sheria mkononi,natambua dhahiri kuwa mtu “anapoletewa za kuleta” anaweza kabisa kuiweka sheria kando,hususan pale haki yake inapopuuzwa kwa makusudi.Kwa vile mkoa wa Morogoro umebahatika kuwa na RC ambaye ni “mjeshi” mstaafu basi hapana shaka Brigedia Jenerali Kalembo huyo atatumia “mbinu za medani” kuwadhibiti wafugaji hao wenye uhaba wa nidhamu.

Kikao cha Bunge kinaelekea ukingoni na miongoni mwa hoja nilizovutiwa nazo ni ile ya Mheshimiwa Shabiby (wa Gairo) kuhusu ujanja unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi makubwa ya abiria.Alieleza kuwa mengi ya mabasi yanayotumika sasa yamefanyiwa “usanii” kwa kuweka mabodi mapya kwenye “chasis” na injini za malori au za kale.Kuna jina moja tu linalowafaa “wasanii” hawa nalo ni “WAUAJI.” Wanathamini sana kukwepa gharama za kununua mabasi mapya lakini hawajali hata chembe madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na vitendo vyao vya “kuunda mabasi feki.” Kwa upande mwingine tuseme bila kuonekana aibu kwamba mabasi ya namna hiyo yanafahamika hata bila kuwa na ujuzi wa umakanika kwani ulifika pale stendi ya mabasi Ubungo unaweza kukutana na basi ambalo linaonekana dhahiri kuwa bodi yake “imepachikwa” sehemu isiyostahili.Trafiki yeyote aliyehitimu mafunzo yake vyema na mwenye uchungu na maisha ya Watanzania wenzie hawezi kuliruhusu basi “lililovimba mbavuni utadhani lina ujauzito” liendelee na safari,na mabasi ya namna hiyo yako mengi tu.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kuwa wanavunja sheria na kuhatarisha maisha ya abiria wao lakini hawajali kwa vile hakuna aliyechukuliwa sheria hadi leo.Si ajabu tukisikia kuwa baadhi ya mabasi hayo yanatumia injini za matrekta au hata za mashine za kusaga….(nashindwa kumalizia,nimekabwa na kicheko japo jambo hili sio la kuchekesha hata chembe.)

Mwisho,wakati Gavana wetu keshatamka bayana kuwa hatojiuzulu (utadhani alijichagua mwenyewe kwenye posti hiyo),sie wapenzi wa Simba tunajipoza kwa kusherehekea ubingwa wetu ambao kidogo umetibuliwa na hizi habari za viongozi kugombea mapato ya mechi huko Morogoro.Wito kwa watani wetu wa jadi Yanga ni huu:Micho akirudi (kama kweli atarudi) ashauriwe kukutana na Twalib Hilal apewe darasa kuwa ukocha sio sawa na ukatibu mwenezi wa klabu: ukocha ni vitendo vingi maneno machache lakini Mserbia Micho kila siku “anachonga” kuhusu hili au lile lakini matunda ya kazi yake kwenye dimba ni haba.Enewei,asilaumiwe sana kwani alishawahi kusema kuwa wachezaji wake hawafundishiki,na katika mechi ya juzi anaweza kuongeza sababu kuwa “lile tumbo la kuendesha” limechangia kukosa ushindi.

Alamsiki






Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.