20 Jan 2012


Dk Slaa: Kwa nini sikumsalimia JK 


Thursday, 19 January 2012 20:42
Fredy Azzah 
KATIBU Mkuu wa Chadema Dk Willibrod Slaa  amesema kuwa, hakuweza kusalimiana na Rais Jakaya Kikwete kutokana na Jiografia ya eneo la makaburini lilivyopangwa na watu wa usalama wa taifa pamoja na kamati ya mazishi kutomruhusu kufanya hivyo.

 
Hata hivyo Dk Slaa alisisitiza kuwa, kwa upande wake, kwenye msiba siyo sehemu ya kwenda kwa ajili ya kusalimiana na watu ama kurekebisha mambo yaliyoharibika bali ni sehemu ya kumwombea marehemu.

 “Siyo hulka ya Dk Slaa kutumia misiba kama sehemu ya kusalimiana, wala kutengeza mambo yaliyoharibika, mimi huwa naenda kwenye msiba kwa lengo moja tu la kumwombea marehemu, huwa simtazami hata mtu aliyekaa pembeni yangu,” alisema Dk Slaa alipozungumza kwa njia ya simu  jana.  

Alifafanua kuwa, katika eneo la makaburi kulikuwa na mabanda matano ambayo yalipangwa kwa ajili ya Askofu, Rais, Viongozi wa vyama vya siasa, mwili wa marehemu  na familia na banda jingine lilikuwa la watu wengine waliohudhuria mazishi hayo. 

“Sasa kutoka alipokuwa amekaa Rais mpaka kwenye banda nilipokuwa mimi, kulikuwa na umbali wa karibu  mita 20, sasa mlitaka nikimbie kumsalimia Rais nivunje protokali kisha nikamatwe na usalama wa taifa,” alisema Dk Slaa. Alisema alikuwa mtu wa kwanza kufika makaburini kwa lengo la kuangalia jinsi kaburi la mbunge wa chama chake lilivyochimbwa kisha akaonyeshwa sehemu ya kukaa na watu wa usalama wa taifa.

 Alisema kuwa, hata katika wakati wa kuaga mwili wa Marehemu Regia Mtema, katika ukumbi wa Karejee, kulikuwa na utaratibu kama huo ambapo ilitengwa sehemu ya kukaa Makamu wa Rais, Spika wa Bunge, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Makamu wake na yeye Dk Slaa akawekewa sehemu yake kama Katibu wa Chama alichokuwa akikitumika marehemu.

 “Mimi sipendi kuweka siasa kwenye mambo kama ya msiba, Dk Slaa siyo kichaa siyo kichaa aanze kukimbia kumsalimia Rais. Katika sehemu kama ile Rais huwa anakuja baada ya watu wote wakiwa wameshakaa, yeye ndiye hupita na kuanza kusalimia watu na hamjaona hata sehemu moja aliponyoosha mkono kunisalimia nikamkwepa,” alisema Dk Slaa:

 “Msiba siyo mahali pa kutengeza urafiki, au kutengeza mambo yaliyo haribika, pale ni ibada tu na kumuombea marehemu siyo sehemu ya kufanya siasa” alisisitiza Dk Slaa. Jana baadhi ya vyombo vya habari viliripoti kuwa, Dk Slaa alishindwa kusalimiana na Rais Jakaya Kikwete katika mazishi ya Regia Mtema yaliyofanyika kijijini kwao Ipangalala Morogoro juzi.Regia alifariki dunia Januari 14 kwa ajali ya gari iliyotokea katika eneo la Ruvu mkoani Pwani.  


CHANZO: Mwananchi

1 comment:

  1. Baadhi ya Magazeti huwa yanagombanisha viongozi wetu, hili liangaliwe pia. Wanapenda kuandika bila kuchunguza mambo!!!.

    ReplyDelete

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.