2 Oct 2014

Bado ninakumbuka vizuri maongezi yangu ya mwaka 2005 na mtu mmoja jijini Dar, ambaye sio tu ni mwajiriwa katika taasisi moja nyeti lakini pia ana uelewa mkubwa wa masuala yanayojiri 'nyuma ya pazia' (yaani masuala mbalimbali mazito ambayo kamwe huwezi kuyasikia au kuyaona kwenye vyombo vya habari). Nikiwa huko nyumbani kwa likizo katika kipindi ambacho Tanzania yetu ilikuwa katika harakati za uchaguzi mkuu ambao hatimaye ulimwingiza madarakani Rasi Jakaya Kikwete, mwandamizi huyo alinieleza kwa undani kwanini aliamini JK angeshinda uchaguzi huo kwa ushindi wa kishindo.

Kadhalika, mtu huyo alibashiri kuwa Watanzania watajuta kumwingiza Kikwete Ikulu kwa kile alichokieleza kuwa "mtu huyu hayupo serious kiasi cha kumkabidhi dhamana ya kuongoza nchi hii yenye matatizo kibao." Alikwenda mbali zaidi na kunisimulia masuala kadhaa yaliyojiri katika utawala wa Rais Benjamin Mkapa (ambapo mie nilikuwa nje ya nchi kwa zaidi ya nusu ya awamu ya pili ya utawala wa Mkapa). Alieleza kuwa hali ilikuwa mbaya wakati huo, na laiti JK akiingia madarakani itakuwa mbaya zaidi.

Mtu huyo ameendelea kunijulisha mengi yanayojiri 'nyuma ya pazia,' na hivi karibuni aliniambia kuwa ana uhakika Watzanai wengi watapatwa na mshtuko mkubwa baada ya JK kuondoka madarakani hapo mwakani, pindi watakapopata fursa ya kufahamu jinsi nchi yao ilivyoendeshwa katika kipindi hiki cha miaka 10 (2005-2015). Alidai kwamba kinachofahamika kwa umma ni tone tu la maji kwenye bahari kwani kuna mlolongo wa 'madudu' yanayoendelea lakini nguvu iliyojengwa na mtandao wa JK 1995-2005 inafanya jitihada kubwa kuyadhibiti yasijulikane hadharani.

Lakini sidhani kama kuna Mtanzania anayehitaji kuwa na 'mjuzi wa mambo' kama  huyo jamaa yangu, kufahamu kwamba mwelekeo wa nchi yetu ni shaghalabaghala. Kwa wenye uelewa wa 'kusoma kati ya mistari' (reading between the lines) watabaini kuwa mengi ya yanayojiri huko nyumbani katika medani ya uongozi wa taifa letu ni matokeo ya ombwe kubwa la uongozi wa JK.

Wengi twakumbuka kauli ya Mbunge wa Ubungu kwa tiketi ya Chadema, Mheshimiwa John Mnyika, kuwa 'JK ni dhaifu.' Na kwa hakika watendaji wengi wa serikali ikiwa ni pamoja na mawaziri wake wanautumia vyema udhaifu huo wa bosi wao.

Hebu angalia mfano huu rahisi. Wakati lawama nyingi kuhusu sintofahamu ya hatma ya Katiba Mpya inaelekezwa kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katika, Samuel Sitta, mtu ambaye hawezi kukwepa lawama katika kuukoroga mchakato huo ni JK mwenyewe. Kana kwamba alilazimishwa kuteua Tume ya Kukusanya Maoni ya Katiba (Tume ya Warioba), JK pasi kujali athri za matendo yake alianzisha upizani wa waziwazi dhidi ya mapendekezo ya Tume hiyo ya Warioba. Mara kadhaa akiwa kama Mweneykiti wa Taifa wa CCM aliweka bayana upinzani wa chama tawala kwa mapendekezo ya Tume hiyo. Lakini yote tisa, kumi ni siku ya uzinduzi wa Bunge Maalum la Katiba ambapo badala ya kuwaunganisha Watanzania, hotuba yake ilipandikiza mbegu ambazo kwa hakika ndizo tunavyna matuonda yake sasa.

Ilipotokea baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo kuunda umoja wao wa UKAWA, na hatimaye kususia vikao vya bunge hilo, kauli za kujikanganya za JK hazikusaidia kuleta mwafaka, kwani mara aonekane anayetaka suluhu mara awatupie lawama UKAWA, mara awaombe viongozi wa dini wasaidie kuokoa mchakato huo, mara atumie ubabe kuzima hoja za UKAWA. Kwa kifupi, ukosefu wake wa msimamo wenye kulinda maslahi ya taifa ulitoa fursa kwa kila 'Dick, Toim na Harry' kujiropokea chochote kilichomuijia akilini.

Fast foward hadi hapa tulipo sasa, katika mazingira ya kawaida tu usingetegemea JK aende Marekani TENA kwa wiki mbili ilhali hatma ya Katiba mpya na Bunge Maalum la Katiba ni tata. Tumeshazungumza vya kutosha kuhusu jinsi JK anavyopenda kuzurura nje ya nchi, hususan ziara za Marekani. Kwa wanaofuatilia safari zake watafahamu kuwa alikuwa Marekani hivi majuzi tu kwa siku kibao, lakini hiyo haikumzuwia kwenda tena huko kwa wiki mbili kwa kisingizio cha kuhudhuria kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Je isingewezekana kwenda siku moja kabla ya siku yake ya kutoa hotuba na kisha kurejea nyumbani kushughulikia hatma ya Katiba mpya?

Kituko ni kwamba wakati akiwa ziarani Marekani, alifanya 'safari ndani ya safari' na kuja hapa Uingereza, kabla ya kurejea tena Marekani. Kwa hakika ni vigumu kubashiri maisha ya Rais wetu huyu atakapostaafu mwakani kwani ni wazi kuwa moja ya vitu atakavyovi-miss sana ni hizo safari mfululizo za nje ya nchi. Japo kuwa Rais mstaafu hakutomzuwia kusafiri mfululizo, lakini angalau kwa wakati huo 'hatokuwa na jeuri' ya kuambatana na lundo la watu kwenye misafara yake. Na hatuwezi kujua, huenda Rais ajaye akadhibiti safari za viongozi au viongozi wastaafu nje ya nchi pasipo sababu za msingi.

Ombwe la uongozi wa JK, ukichanganya na mchango wake katika kuukoroga mchakato wa Katiba mpya, ndio moja ya fursa zilizotumiwa kikamilifu na Sitta katika kufanikisha uhuni wa kisiasa/ mzaha wa kidemokrasia unaoendelea huko Dodoma. Kwa lugha nyingine, kiburi, ubishi, nyodo, na kila kisichopendeza kutoka kwa Sitta na uendeshaji wake wa Bunge Maalum la Katiba ni dalili tu za ugonjwa, ilhali chanzo cha ugonjwa huo ni ombwe hilo linalouandama utawala wa JK.

Hivi tuwe wakweli. Laiti JK angemkalisha Sitta kitako kama Waziri wake na ' kumpa darasa la kiutu-uzima' Mwenyekiti huyo wa BMK angeendeleza kufanya madudu tunayoshuhudia? Ni suala jepesi tu la bosi kukaa chini na anayemwongoza, kisha kumwambia bayana kuwa , "No, Mr Sitta, this is wrong." Na hata kama kuna watakaodhani huo ni sawa na udikteta, basi na bora iwe hivyo kwani udikteta kwa maslahi ya umma ni suala linalokubalika.Uzoefu unaonyesha kuwa kumpa mtu uhuru usio na mipaka unaweza kuufanya uhuru huo kuleta madhara yasiyokusudiwa. Rais asipokuwa na uwezo wa kumkaripia Waziri wake, au hata kumshauri tu abadili mwelekeo basi ana ,udhaifu mkubwa.

Twafahamu kuwa JK aliafikiana na Kituo cha Demokrasia kuhusu njia mwafaka za kukamilisha mchakato wa Katiba mpya kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kuliendesha zoezi hilo taratibu badala ya kuliharakisha kama Sitta anavyofanya sasa. Kwa makusudi kabisa, Sitta akaamua kupuuza ushauri wa JK, na kuendesha BMK atakavyo. Si vigumu kufahamu kuwa kilichompa jeuri Sitta ni ufahamu mzuri kwamba bosi wake, yaani JK, ni dhaifu asiyeweza kumwajibisha kwa kiburi hicho. Na muda wa kumshughulikia Sitta ataupata wapi ilhali yupo bize na safari zake za kuzunguka dunia?

Uongozi katika zama hizi za JK umekuwa kama mzaha flani, mchezo wa kuingiza usiopendeza, yaani a bad comedy, Hebu angalia picha hizi hapa chini kupata uthibitisho wa ninachoandika





Pichani juu ni vimemo vya Sitta akilazimisha matakwa yake.

Lakini tukiangalia kwa upana zaidi kuhusu ombwe lililosababishwa na udhaifu wa JK, tunakutana na kituko hiki hapa chini. Kimsingi, moja ya kumbukumbu za muda mrefu kuhusu utawala wa JK itabaki kuwa kuibuka kwa wanasiasa/viongozi ambao pengine sifa pekee waliyonayo katika uanasiasa/ uongozi wao ni vituko, kashfa, mazingaombwe, na mambo mengine yasiyopendeza. Kama nilivyotanabaisha hapo awali, ombwe hilo liletoa fursa kwa kila Dick, Tom na Harry kufanya atakavyo. Hebu angalia kioja hiki


Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa Watanzania wenzangu kukazani katika dua/sala ili JK amalize muda wake kwa amani, maana mustakabali wa taifa letu upo hatarini. Ni muhimu kufahamu kuwa amani na utulivu tuliyonayo yahitaji vitendo vya wapuuzi wachache tu kabla haijatokomea. Na uzoefu waonyesha kuwa amani ikipotea ni ngumu sana kuirejesha. Na kubwa tunalohitaji ni kukoma mara moja kwa vitendo vya watawala wetu kuwaona Watanzania kama 'hamnazo' kama tunavyoshuhudia katika BMK huko Dodoma.

Tumtegemee Mungu katika hili, sambamba na jitihada zetu wenyewe kukabiliana na tabia inayozidi kukota mizizi ya kugeuza uongozi kuwa uhuni flani.

MUNGU IBARIKI TANZANIA 


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.