Showing posts with label MGAO WA UMEME. Show all posts
Showing posts with label MGAO WA UMEME. Show all posts

28 Jun 2011

Pichani ni jengo la "Tanesco ya Senegal",Senelec,lililoshambuliwa na waandamanaji wenye hasira kuhusu kukatika umeme mara kwa mara jijini Dakar.Akina sie tunashambulia kwa matusi,lawama,na manung'uniko huko Twitter na Facebook!!!

Sio siri kwamba upole wa Watanzania ni miongoni mwa sababu kuu za mabaya mengi yanayotokea huko nyumbani.Na kama kuna suala linalosikitisha kuhusu mwamko wa Watanzania kudai haki zao ni tatizo la mgao wa umeme sambamba na ubabaishaji wa hali ya juu wa serikali na Tanesco katika kushughulikia tatizo hilo.

Sasa hivi,mitandao ya jamii ya Twitter na Facebook imetawaliwa na malalamiko ya Watanzania wengi kuhusu mgao.Wengine wanaishiwa na uvumilivu na kuishia kuitukana Tanesco,kana kwamba matusi hayo yatarejesha umeme.Wengine wamekuwa wakipeana taarifa kuhusu maeneo ambayo "Tanesco wameshachukua umeme wao".Kwa kifupi,kinachosikika zaidi ni manung'uniko,lawama,vilio na hata matusi.Cha kusikitisha ni kwamba hakuna dalili yoyote kutafsiri malalamiko hayo into vitendo.

Sio kama nawasimanga ndugu zangu.I really feel you lakini ukweli mchungu ni kwamba kelele zenu haziwezi kumaliza tatizo hilo.Kinachohitajika ni kudai haki kwa nguvu.By "nguvu" simaanishi vurugu bali kuchukua hatua za makusudi kuhakikisha serikali na Tanesco wanawajibika.Mgao utaendelea milele iwapo Watanzania wataishia kulalamika tu.Hakuna miujiza katika kuleta mabadiliko.Either watu wajitoe muhanga kudai haki yao kama walipakodi au waendelee kuteswa na mgao.

Bahati nzuri,wenzetu nchini Senegal wanatuonyesha namna gani matatizo yanayoathiri nchi yanavyoshughulikiwa na umma.Nisieleze kwa maneno yangu bali naomba usome habari ifuatayo:

Associated Press

DAKAR,Senegal: Maelfu ya waandamanaji wameingia mitaani katika mji mkuu wa Senegal kupinga kukatika umeme mara kwa mara.Maandamano hayo ni tukio la tatu la vurugu nchini humo ndani ya wiki.

Wananchi wenye hasira walivamia ofisi za shirika la umeme la Senelec,jijini Dakar baada ya maandamano ya kupinga kukatika kwa umeme kwa muda mrefu.

Watu kadhaa walishambulia majengo ya serikali hapo jana.Wanadaia kuwa baadhi ya maeneo yamekuwa yakikosa umeme kwa masaa 24 au zaidi.

Kama ilivyo kawaida kwa vyombo vya dola barani Afrika,askari wa kikosi cha kutuliza ghasia walipambana na waandamanaji kwa kutumia maji na mabomu ya machozi.Msemaji wa polisi hakuweza kuthibitisha idadi ya waliojeruhiwa katika ghasia hizo.

Alhamisi iliyopita,vurugu kubwa ziliibuka kupinga mpango wa mabadiliko ya katiba ya nchi hiyo

Uchaguzi ni wenu Watanzania wenzangu.Mwendelee kulalama huku Serikali na Tanesco wakiendelea kuwasanifu (mgao wa umeme hauwagusi kwa vile aidha wana jenereta zinazojazwa mafuta na hela yako mlipakodi au maeneo wanayoishi hayakatwi umeme kutokana na unyeti wake) AU muige mfano wa wenzetu wa Senegal.Hakuna njia ya mkato katika kutatua matatizo sugu yanayosababishwa na watendaji wasiotimiza wajibu wao.It's now or never!

23 Jun 2011


Mgao wa Tanesco ukiwa kazini
Sio siri kwamba kinachowapa jeuri mafisadi kuwapalekesha Watanzania ni upole kupita kiasi walionao wanachi.Watu wanalipa kodi-kwenye mishahara kwa walioajiriwa,katika VAT kwenye manunuzi ya bidhaa mbalimbali,na utitiri mwingine wa kodi-lakini faida ya kodi hiyo inaonekana zaidi kwenye ukubwa wa vitambi vya viongozi wetu,thamani ya magari na mahekalu yao,na kuongezeka kwa idadi ya vimada na nyumba ndogo zao.

Sasa Tanesco wamekuja na kali kubwa kwa kutangaza mgao wa umeme usio na kikomo,masaa kumi kwa kila siku ya wiki.Ukienda huko Twitter utasikia "aah Tanesco wamechukua umeme wao".Wengine wanaishia kuitukana Tanesco kwa matusi ya "sehemu za siri za mama yake Tanesco".Hizi zote ni dalili za watu walioishiwa na mbinu zakudai haki zao.Hivi "kumtukana mama yake Tanesco" kutafupisha mgao wa umeme?

Imefika wakati Watanzania watambue kuwa mara nyingi HAKI HAITOLEWI KAMA ZAWADI BALI HUDAIWA...KWA NGUVU IKIBIDI.Hakuna uwezekano wa tatizo la mgao wa umeme kuisha kwa njia za kistaarabu.Utatuzi hauwezi kupatikana kwa vile sekta ya nishati,kama ilivyo ya madini ni kitega uchumi kikubwa kwa mafisadi wetu.Kukatika umeme kunawaingizia baadhi ya majambazi hao mamilioni ya shilingi kila siku.

Nina tatizo kubwa zaidi na Wtanzania wa tabaka la kati.Hawa ndio tunaokutana nao huko Twitter na Facebook...Kiingereza kiiingi huku nchi inateketea.Hawa ndio tunaowaona wakijirusha kwenye kumbi mbalimbali za "starehe".Kuna starehe gani kuwepo kwenye ukumbi unaobadilisha taa kutoka rangi moja kwenda nyingine (kwa kutumia jenereta) kisha kurudi nyumbani na kukumbana na kiza na joto kwa vile "Tanesco wamechukua umeme wao" na feni haiendeshwi kwa mafuta ya taa!

Kwanini nailamu middle class yetu?Ni kwa vile hiki ni kiungo muhimu kati ya tabaka tawala na tabaka la walalahoi.Hawa ndio wenzetu wenye shahada au stashahada katika fani moja au nyingine.Hawa ni watu wenye upeo na wanaweza kuihamasisha jamii kutambua na kudai haki zao.Wengi katika tabaka hili ni walalahoi wanaojaribu kuiga maisha ya wale wa tabaka la juu.

Uchaguzi ni wenu.Kujifanya mmezowea maumivu na mafisadi waendelee "kupeta" au kuweka kando "ubishoo na usistaduu" na kuungana na tabaka la walalahoi kuhamasisha mabadiliko katika nchi yetu.Akina sie tunatekeleza wajibu kwa namna kama inavyofanya makala hii.Sasa ni wajibu wa kila mmoja wetu kutimiza wajibu wake ili kuinusu nchi yetu.

Enewei,hebu soma stori husika hapa chini
Tanesco yatangaza mgawo wa saa 10 kwa siku nchi nzima
Wednesday, 22 June 2011 21:06

Waandishi Wetu
SHIRIKA la Umeme (Tanesco), limetangaza mgawo mkubwa wa umeme usio na kikomo, utakaokuwa kwa saa 10, siku saba kwa wiki nchi nzima.

Maafisa wa shirika hilo na Wizara ya Nishati na Madini wamesema mgawo huo umetokana na upungufu wa maji katika bwawa la Mtera na transfoma zake kuzalisha umeme mdogo kuliko mahitaji.Kwa mujibu wa tangazo la ratiba ya mgao huo lililotolewa na Tanesco jana, mgao huo utakuwa wa kati ya saa sita hadi 10 kwa siku ambapo maeneo yatabadilishana muda wa mgawo.

Hata hivyo, tangazo hilo la Tanesco limekuja wakati maeneo mengi nchini yakiwa na mgawo wa muda mrefu na ambao unachukua muda wa saa zaidi ya zilizotangazwa jana na shirika hilo hali iliyosababisha malalamiko kwa wananchi.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo mgawo huo utakuwa wa kila siku kuanzia Jumatatu hadi Jumapili ambapo baadhi ya maeneo yatakosa umeme mchana na mengine yatakosa usiku.Tanesco ilisema katika baadhi ya maeneo umeme utakatika kuanzia saa 2.00 asubuhi hadi saa 12.00 jioni, wakati maeneo mengine yatakosa umeme kuanzia saa 12.00 jioni hadi saa 5.00 usiku.

Akizungumza katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jana, Mhandisi Mkuu wa Tanesco, Juliana Pallangyo alisema mgawo huo unatokana na kupungua kwa kina cha maji katika bwawa la Mtera.

Alisema mahitaji ya umeme ni megawati 850 wakati uzalishaji ni megawati 600 hali inayochangia upungufu wa umeme.

“Mahitaji yaliyopo ni makubwa wakati umeme unaozalishwa ni mdogo, tunashindwa kumudu mahitaji ya watu wote kwa wakati mmoja na ndiyo maana tunakuwa na mgawo,” alisema Pallangyo.Aliongeza kuwa licha ya matatizo hayo shirika hilo lina malengo ya kusambaza umeme vijijini ambako bado hakujafikiwa na umeme.

Katibu adai mgawo utakuwa historia

Akizungumzia kuhusu mgawo huo, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo alisema mgawo huo unaweza kuwa historia katika miaka miwili ijayo na kwamba hali ya sasa inatokana na upungufu wa maji katika bwawa la Mtera ambalo linaweza kufungwa kwa sababu hiyo.

Katika hatua nyingine, Jairo alisema Serikali ya China itatoa mkopo wa dola za Marekani 778 milioni sawa na Sh1,167,000 bilioni, kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya kufunga bomba kubwa la kusafirisha gesi kutoka mkoani Mtwara hadi Dar es Salaam, itakayosaidia kuongeza uzalishaji wa umeme nchini.

Alisema hatua hiyo itafanyika endapo Serikali ya Tanzania itafikia makubaliano na Serikali ya China katika mazungumzo baina yao yanayotarajia kuyafanya wiki ijayo.Iwapo mpango huo utafanikiwa kampuni ya China Petrolium Company ndiyo itakayozalisha umeme.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Jairo alisema, kiasi hicho cha fedha ni kulingana na upembuzi yakinifu uliofanywa na kwamba gesi itakayozalishwa itasaidia kupunguza tatizo la umeme na uharibifu wa mazingira nchini.

Alisema bomba linalozalisha gesi kwa sasa kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam ni dogo likiwa na ukubwa inchi 30 hivyo uzalishaji wake pia ni mdogo.“Sisi kama wizara tunajitahidi kuweka mipango ya muda mfupi ya kukabiliana na tatizo la umeme lililopo nchini kwa hiyo Serikali ya China itatupa fedha hizo kama mkopo kwa ajili ya kuzalisha gesi hiyo,”alisema Jairo

CHANZO: Mwananchi

24 Dec 2010


Majuzi,msomaji mmoja wa blogu hii alinitumia maoni ambapo pamoja na mambo mengine aliashiria kuwa nina chuki dhidi ya Rais Jakaya Kikwete.Msomaji huyo aliyejitambulisha kuwa mkazi wa hapa Glasgow alidai (namnukuu) "...I know you hate JK because whatever happens to him you have a negative view, even a tyre puncture...",yaani kwa Kiswahili,"najua unamchukia JK kwa vile chochote kinachotokea kwake wewe una mtizamo hasi,hata pancha ya tairi".Hii ndio mitizamo ya Watanzania wenzetu ambao licha ya kubahatika kuwa nje ya nchi,hususan nchi zilizoendelea kama hapa Uingereza,bado wana mitizamo mgando ambayo kwa kiasi kikubwa imechangia kutufanya hata miaka 49 baada ya uhuru kutamani mkoloni arejee.

Yah,huwezi kuwalaumu wanaotama mkoloni arejee japo mie si mmoja wao.Hivi tunawezaje kuelezea namna Watanzania wanavypelekeshwa kama watoto wadogo tena yatima siku chache tu baada ya Kikwete na CCM yake kupita huku na kule kuahidi neema,only for madudu and more madudu kuibuka kila kukicha?Unajua,angalau mkoloni alipotupelekesha alikuwa na excuse (japo isiyokubalika) kwamba yeye hakuwa Mtanganyika,na hakuwa na uchungu na nchi yetu.Na kwa wanaokumbuka vizuri somo la historia wanafahamu bayana kuwa ujio wa mkoloni ulikuwa kwa minajili ya kuendeleza nchi zao za asili,yaani kukwapua raslimali zetu kwa ajili ya viwanda vyao,kupata masoko ya bidhaa zao na eneo la makazi kwa nguvukazi ya ziada katika nchi hizo za wakoloni.Sasa ondoa neno mkoloni kisha weka neno FISADI,na yayumkinika kuhitimisha kuwa angalau mkoloni alikuwa na ajenda ya maendeleo huko kwao japo at our expense.Mafisadi nao wana ajenda za maendeleo pia,ila ni katika kutunisha akaunti zao kwenye mabenki ya hukohuko kwa wakoloni,kuongeza idadi ya nyumba ndogo zao (isomeke ufuska au uzinzi),kuongeza idadi ya mahekalu yao na magari ya kifahari,na sasa ajenda mpya ya kuimarisha himaya zao kwa kutumbukiza kila mwanafamilia na ndugu wa karibu kwenye siasa ili pindi baba akiondoka madarakani basi mwana amrithi kuzuia uwezekano wa baba mtu kukaliwa kooni kwa madudu aliyofanya akiwa madarakani.

Nimelazimika kuandika makala hii sio kwa minajili ya kumjibu huyo msomaji wangu wa hapa Glasgow bali ni baada ya kusoma toleo la mtandaoni la gazeti la Mwananchi ambapo kuna habari kuwa Tanesco wametangaza tena mgao wa umeme nchi nzima.Hivi sio majuzi tu shirika hilo lilitangaza mwisho wa mgao wa umeme?Tuwe wakweli,hivi uhuni huu wa Tanesco,ambao mie natafsiri kuwa ni uhuni wa serikali iliyopo madarakani,utaendelea hadi lini?So far,hakuna taarifa za wazi kuhusu athari za mgao wa umeme lakini haihitaji sayansi ya roketi au dissertation ya quantum physics kumaizi kwamba mgao huo una madhara makubwa mno kwa uchumi wa taifa na kwa maisha ya walalahoi kwa ujumla (vigogo licha ya kunufaika na ufisadi unaowawezesha kuuza jenereta kila mgao unapotangazwa lakini pia hawaathiriki kwa vile majumbani na maofisini kwao kuna jenereta zinazoendeshwa na fedha za kodi za walalahoi).

Hatuwezi kuilaumu Tanesco pekee kuhusiana na uhuni huu kwani ni siri ya wazi kuwa shirika hilo na sekta ya nishati kwa ujumla vimegeuzwa kitegauchumi kizuri kwa mafisadi.Majuzi tu tumesikia majambazi wa Richmond wakijiandaa kurejeshewa fedha walizotuibia ambapo watalipwa fidia ya mabilioni kwa mgongo wa binamu zao wa Dowans.Hatuwezi kumwepusha Kikwete na CCM yake na ufisadi huu kwa vile licha ya madudu hayo kushika hatamu wakati wa utawala wake,sasa tunafahamu kuwa amekuwa akiwakingia kifua mafisadi wasichukuliwe hatua za kisheria (thanks to nyaraka za siri za kidiplomasia zilizovujishwa na mtandao wa WikiLeaks).Kwa wale ambao hawajabahatika kusoma habari hizo,kuna nyaraka kutoka ubalozi wa Marekani hapo Dar zilizobeba maongezi kati ya bosi wa Takukuru Edward Hoseah na afisa ubalozi wa Marekani ambapo Hoseah alinukuliwa akieleza bayana kwamba Kikwete alishinikiza baadhi ya mafisadi wasichukuliwe hatua.Japo bosi huyo wa Takukuru amejaribu kuruka kimanga na kukana tuhuma hizo,kila mwenye akili timamu anafahamu kuwa ufisadi unashamiri Tanzania kwa vile Kikwete ameshindwa kuwachukulia hatua mafisadi papa licha ya madaraka lukuki aliyorundikiwa na Katiba.

Baadhi yetu tuliwaasa Watanzania wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita majuzi kwamba kuirejesha tena madarakani serikali ya Kikwete ni sawa na kumwaga chumvi kwenye kidonda kibichi,na matokeo yake ndio haya.Wakati tunaelekea mwezi wa pili tangu Kikwete atangazwe mshindi,hakuna lolote la maana lililokwishafanyika kuashiria kuwa kiongozi huyo ana ajenda mpya tofauti na zile zilizotawala miaka mitano iliyopita,kubwa ikiwa na kushamiri kwa ufisadi na uimarishaji himaya za mafisadi huko nyumbani.

Sawa,makosa yameshafanyika kwa kumrejesha Kikwete na CCM yake madarakani lakini hiyo isiwe sababu ya kuendelea kunung'unika kimoyomoyo huku nchi yetu ikizidi kuteketea.Umefika wakati Watanzania wasikubali kupelekeshwa namna hii.Kwanini Kikwete asibanwe kuhusu tatizo la umeme licha ya ahadi zake za mara kwa mara kuwa tatizo hilo lingekuwa historia?Au alimaanisha kuwa tatizo hilo litaendelea kuwa la kihistoria?

Nimesikia taarifa za mpango wa Chadema kuandaa maandamano ya nchi nzima kupinga kuongezwa bei ya umeme.Yaani licha ya mgao wa kila kukicha bado Tanesco wanataka kuongeza bei?Yayumkinika kuhisi kuwa wazo hilo la ongezeko la bei ya umeme ni la kifisadi lenye lengo la kupata fedha za kuwafidia mafisadi wa Richmond/Dowans.Ni muhimu kwa kila Mtanzania mzalendo kuunga mkono mpango huo wa maandamano ya amani ili kufikisha ujumbe kwa Kikwete na serikali yake kuwa Watanzania wamechoka kupelekeshwa.Hata hivyo,kama maandamano ya kuwapongeza wabunge wa upinzani yalizuiliwa na polisi,sidhani kama serikali itaridhia maandamano hayo ya kupinga ongezeko la bei ya umeme.

Mwisho,tuna choices mbili tu:kuchukua hatua sasa kabla hatujafika mahala ambapo hata tukichukua hatua itakuwa sawa na kutwanga maji kwenye gunia,au tusubiri kusoma rambirambi kuhusu nchi yetu hapo 2015.

4 Oct 2009


HATIMAYE Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) limetangaza mgawo wa umeme nchi nzima kutokana na upungufu wa maji kwenye vituo vya kuzalisha umeme vya Kihansi na Pangani.

Hatua hiyo ya TANESCO imekuja miezi michache tu baada ya Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Dk. Idris Rashid, kuonya kuwa taifa litaingia gizani iwapo mitambo ya Kampuni ya Dowans yenye uwezo wa kuzalisha megawati 100 haitanunuliwa.

TANESCO ilikuwa na mpango wa kununua mitambo ya Dowans ambayo ilirithi mkataba kutoka Kampuni ya kuzalisha umeme wa dharura ya Richmond iliyobainika kutokuwa na uwezo wa kuzalisha nishati hiyo...ENDELEA

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.