Showing posts with label Mihadarati. Show all posts
Showing posts with label Mihadarati. Show all posts

28 Aug 2013


Majaji wanaowalinda wauza 'unga' wabainika

* Gazeti hili sasa limeamua kuwataja kwa majina
* Mahakimu nao wanawaachia mapapa kienyeji
* Kigogo ofisi ya DPP, Mahakama Temeke, Kinondoni balaa


Na Waandishi Wetu, Dar na Zanzibar
Mahakama kupitia baadhi ya majaji na mahakimu wasio waadilifu imebainika kuwa kikwazo kikubwa katika vita dhidi ya dawa za kulevya nchini, uchunguzi wa JAMHURI umebaini.
Pamoja na Mahakama, Ofisi ya Mwendesha Mashitaka wa Serikali (DPP), nayo imelaumiwa kwa kufuta kesi katika mazingira ambayo hata mtu ambaye hakusoma sheria, anaweza kuyatilia shaka. 
Wakati vyombo hivi vikikwamisha vita hii, lawama zimekuwa zikielekezwa kwa polisi na vyombo vingine vya usalama, ambavyo watendaji kazi wake wanafanya kazi usiku na mchana. 
Juhudi zote zinazofanywa na vyombo vya ulinzi na usalama zinagonga mwamba mahakamani kwa msaada wa ofisi hiyo ya DPP.
Wakati kesi nyingine zikifutwa, nyingine hazisikilizwi, kiasi cha kusababisha zirundikane mahakamani tangu mwaka 2005. Kesi chache zinazohusu watuhumiwa wakubwa wa kuuza ‘unga’ zinamalizwa haraka kwa utaratibu wa ofisi ya DPP kuwasilisha nia ya kutoendelea na mashtaka mahakamani (nolle prosequi) au wasimamizi hao wa utoaji haki kutoa hukumu zinazoacha wengi vinywa wazi na kuwakatisha tamaa polisi.
Katika hali ya kushangaza, majaji na mahakimu wamekuwa wakikiuka wazi Sheria ya Kuzuia Dawa za Kulevya Na, 9 ya Mwaka 1995 inayozuia mtu yeyote aliyekamatwa na dawa zenye thamani kuanzia Sh milioni 10 asipewe dhamana, lakini hilo halizingatiwi. JAMHURI haikubahatika kufahamu bayana nini kinawapofusha majaji na mahakimu wakati ‘mapapa’ wanapofikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuuza unga, lakini ni wazi kuwa kuna mtandao mkubwa wa kulindwa kwa watuhumiwa hao wenye ukwasi mkubwa.
Wakati polisi wanafanya kazi ya hatari usiku muda wote, wakipambana na wauaji, wahongaji na watu wanaouza dawa za kulevya, kesi za mapapa zinamalizwa kienyeji mahakamani.
Moja ya kesi inayotia shaka ni Na. 47 ya Mwaka 2011. Kesi hii ilifunguliwa dhidi ya watuhumiwa Fredy William Chonde, Kambi Zuberi Seif; ambao ni Watanzania na Abdulghan Peer Bux na Shaaban Malik ambao ni raia wa Pakistani.
Hawa walikamatwa eneo la Mbezi Beach, Dar es Salaam wakiwa na kilo 175 za heroin, ambako kesi dhidi yao ilifunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini humo. Wakati kesi inaendelea Kisutu, mawakili wa vigogo hawa walikwenda Mahakama Kuu wakafungua shauri la kuomba wapewe dhamana chini ya Jaji Pendo Msuya, wakitambua kuwa sheria inazuia.
Bila kuchukua jalada wala kuwasiliana na Mahakama ya Kisutu, huku Jaji Msuya akijua fika kuwa kilo 175 ambazo thamani yake ni zaidi ya Sh bilioni tano, na watuhumiwa hawapaswi kupewa dhamana; yeye kwa mamlaka aliyonayo kama Jaji aliamua kuwapa dhamana watuhumiwa hawa. Baada ya kupata dhamana, Wapakistani walirejeshewa pasipoti zao na wakakimbia nchi. Hawajakamatwa hadi leo.
“Cha kusikitisha kesi iliendelea bila kujua kuwa watuhumiwa wamekwishapewa dhamana na hadi Aprili 8, mwaka huu 2013 kesi hiyo ilitajwa… baadaye Mahakama ikapewa taarifa kuwa watuhumiwa walishapewa dhamana na Mahakama Kuu ndiyo maana hawaonekani mahakamani. Tulishangaa sana,” kilisema chanzo chetu kutoka Mahakama ya Kisutu.
Kesi nyingine iliyomalizwa kienyeji ni ya Mwinyi Rashid Mkoko. Vyanzo vya JAMHURI vinaonesha kuwa huyu na familia karibu yote wanatuhumiwa kufanya biashara ya dawa za kulevya. Ndugu zake waliokamatwa kwa nyakati tofauti na baba yao, ambako mmoja alidhulumiana, na ‘mzigo’ na wauza unga, hali iliyofanya wamuue kwa kumpiga risasi.
Katika familia hii, Rashid Ismail Mkoko ndiye aliyeuawa na wauza unga wenzake eneo la Ilala, Dar es Salaam. Huyu alipata kukamatwa kuhusiana na dawa za kulevya, ila pia kwa kosa la mauaji. Shuhuda wa tukio la Rashid Ismail Mkoko anasimulia kama ifuatavyo:“Huyu ndiye wa kesi ile ambayo kijana aliyemtuma mzigo Pakistan pipi zilipasukia tumboni akafia gesti kule Tabata, Dar es Salaam. Mmoja wa ndugu wa kijana huyu aliyefariki, alimpigia simu akamwambia ‘si unajua alikuwa na mzigo wako ndiyo umemuua? Sasa mbona umetususa? Hata maji ya kunywa hutupatii msibani?’
“Mkoko akamwambia nitakuja jioni. Na kweli jioni iliyofuata akampigia simu kuwa anakwenda hapo nyumbani msibani. Alipofika akampigia simu, akamwambia njoo tuonane. Huyu ndugu wa kijana aliyefariki akatoka nje, akaenda kwenye gari kuonana na Mkoko.“Alipofika Mkoko akamuuliza ndiye wewe uliyenipigia simu jana, yule ndugu wa marehemu akajibu ‘ndiyo’, basi Mkoko alichofanya akatoa bastola akampiga risasi ya usoni yule kijana…akafariki papo hapo, Mkoko akaondoka.

“Polisi walimkamata wakamfikisha mahakamani. Mahakama ikamwachia kwa mizengwe. Ila Mungu si Athumani, ikatokea naye akadhulumu wauza unga wenzake huko Ilala, nao wakamuwinda wakampiga risasi akafa mwaka juzi.
“Huyu alikuwa muuza dawa za kulevya mkubwa. Mdogo wake Mwinyi Rashid Mkoko, naye anauza dawa. Tulimkamata na heroin gramu 250 zenye thamani ya Sh milioni 11, ikafunguliwa kesi Temeke Na. PI 26 chini ya Hakimu Mkwawa, lakini ajabu wakati kesi inaendelea kutajwa Temeke hadi leo, huyu Mwinyi Mahakama Kuu imekwishamwachia huru bila vielelezo vyovyote,” kilisema chanzo chetu kutoka mahakamani.Uchunguzi wa JAMHURI umeonesha kuwa awali mawakili wa Mwinyi waliwasilisha ombi la dhamana kwa Jaji Munisi, ambaye aliwaelekeza mawakili wa Serikali kuwa badala ya kumshtaki Mwinyi kwa kukutwa na dawa za kulevya, waiondoe kesi mahakamani na kuifungua upya kama kesi ya kusafirisha dawa za kulevya. Kwa kawaida tuhuma za aina hiyo huwa hazina dhamana.Mawakili walivyopata mwanya huo, wanajua jinsi walivyozungumza na wanasheria wa Serikali. Kesi hiyo badala ya kuiondoa kama alivyoelekeza Jaji Munisi wakaihamishia kwa Jaji Dk. Fauz Twalib, ambaye katika hukumu yake ya Julai 30, 2012 alikiri kuwa mbele yake halikufikishwa jalada la kesi hiyo na wala hakuwa na mamlaka ya kuisikiliza kwani yeye si hakimu, ila akasema kwa kuwa Mahakama ya Temeke haina mamlaka ya kusikiliza kezi za dawa za kulevya kama cocaine, basi akatoa fursa ya kumsikiliza mtuhumiwa.“Kwa kasi ya aina yake, siku hiyo hiyo ya Julai 30, 2012 baada ya Jaji Dk. Fauz kutoa hukumu hiyo ya ajabu, mawakili wa Serikali ambao ni upande wa mashitaka wakawasilisha nolle chini ya Section 91 ya CPA (Sheria ya Mwenendo wa Mashitaka), hivyo Mwanasheria wa Serikali Mpembo kwa niaba ya DPP akawasilisha hati hiyo, na Jaji Fauz akaifuta kesi dhidi ya Mwinyi.“Kisichoeleweka na kufahamika ni nini kilitokea na nini kiliendelea siku hiyo hiyo kutoa hukumu, na siku hiyo hiyo Mpembo akawasilisha nolle na kesi ikafutwa siku hiyo hiyo. Hapa kuna maswali mengi. Mwinyi amekimbilia Zanzibar. Yupo anaponda raha, kesi bado ipo Temeke na hakuna kinachoendelea,” kimesema chanzo chetu.Baba yao Mwinyi na Rashid, naye kwa nyakati tofauti anadaiwa kukamatwa na polisi akituhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya. Mtoto wake mwingine, Abubakar Mkoko, yeye alitolewa dawa za kulevya tumboni, lakini Mahakama ikampiga faini ya Sh milioni 1 na kumwachia huru.Kesi nyingine inayowakosesha usingizi polisi ni ile ya Dhoulkefly Awadh Abdallah Na. 238 ya Mwaka 2010. Kesi hii ilimhusisha Abdallah na mkewe Asha Seif Kiluvya. Asha ndiye aliyekamatwa na dawa za kulevya. Hata hivyo, katika mazingira ya kutatanisha, ofisi ya DPP ilipeleka nolle prosequi mahakamani Asha akaachiwa huru, na sasa anashitakiwa Abdallah ambaye hakukutwa na kitu chochote.Kioja kinginge kilifanywa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kinondoni anayetajwa kwa jina la Msongo. Kesi hii ilianza mwaka 2005 na kumalizika mwaka 2008. Mshitakiwa alikuwa Yusufu Hassan Yossye, mkazi wa Kinondoni A, Mtaa wa Togo, aliyekutwa na gramu 1,244 za heroin ambazo alikamatwa nazo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam. Aliwekwa chini ya ulinzi kwa lengo la kumfanya atoe ‘pipi’ kwa njia ya haja kubwa. Katika hukumu ambayo inatia shaka Hakimu Msongo aliandika hivi:“Katika ushahidi wote uliotolewa, hakuna ubishi kuwa ni kweli amekutwa na dawa za kulevya. Pia ushahidi unaonesha kuwa mshitakiwa alitoa madawa hayo kwa njia ya haja kubwa. Hata hivyo, upande wa mashitaka umeshindwa kueleza ni dalili zipi zilipelekea (zilisababisha) kushukiwa kuwa mshitakiwa ana madawa ya kulevya. Na pia hawakushirikishwa watu au wataalamu wa afya ya binadamu.“Upande wa mashitaka katika ushahidi wao umeonesha walipishana kutoa idadi [ya pipi alizotoa kwa haja kubwa]. Kutokana na hilo, ushahidi hautoshelezi na mshitakiwa namwachia chini ya Kifungu cha 235 cha CPA (Kanuni ya Mwenendo wa Mashitaka) katika mashitaka yote mawili.” Hukumu hii ilitolewa na Hakimu Msongo Mei 2, 2008. Yossye alikuwa akishitakiwa kwa kukutwa na dawa; na pia kwa kuwaambia polisi uongo kuwa hakuwa na dawa, lakini baadaye akazitoa kwa njia ya haja kubwa.Katika Mahakama ya Kisutu, mwanamke mwingine aliyetambuliwa kwa jina la Pilly, alikamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akiwa na zawadi ya kinyago ambacho ndani yake kilikutwa na dawa za kulevya, lakini Mahakama ya Kisutu wakati inatoa taarifa ilimwachia huru Pilly kwa maelezo kuwa wakati polisi wanamkamata, hakuwapo mwanamke, hivyo ni kosa mhalifu mwanamke kukamatwa na polisi mwanaume. Akaachiwa huru!
Kesi nyingine ni ya Kwaku Sarfo, raia wa Ghana, alikamatwa Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere mnamo Novemba 14, 2010. Thamani ya dawa ilikuwa Sh milioni 390. Kesi ilipelekwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Samora kwa Hakimu Mkazi Luago.“Tulishangaa, kwamba kwanza Mahakama hii haina mamlaka ya kusikiliza kesi hii, lakini pia baada ya kupita siku 60; bila mamlaka kisheria, Hakimu Luago akaifuta. Hakimu huyu ni kero. Amehamishiwa Lindi akagoma kwenda. Hatujui anapewa jeuri na nani. Tungeomba Rais Kikwete na mhimili wa Mahakama waingilie kati suala hili vinginevyo nchi inateketea,” kimesema chanzo chetu.Uchunguzi umebaini kuwa kati ya kesi 423 zilizofikishwa Mahakama Kuu kati ya mwaka 2005 na 2013 hadi leo kesi iliyokwisha ni moja tu ya Shaaban Mintanga, ambayo nayo imeisha kutokana na mashahidi muhimu kufariki dunia kabla kesi haijasikilizwa. Kati ya mashahidi waliofariki dunia ni Mkemia Mkuu, Dk. Ernest Mashimba, aliyefariki Septemba 2010.
Kamanda wa Kikosi Maalumu cha Kuzuia Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa, alikiri matukio hayo kuwapo na akasema: “Mimi mamlaka yangu ni kukamata, na kuwafikisha mahakamani. Sasa huko kama mmekuta hali iko hivyo, ambayo ni kweli kimsingi inasikitisha na kukatisha tamaa, inabidi muwaulize huko mahakamani au kwa DPP wao ndiyo waeleze nini kinatokea.”
JAMHURI haikufanikiwa kuzungumza na Msajili wa Mahakama Kuu kwani mara zote kila mwandishi wetu alipofika aliambiwa yuko kwenye vikao kwa wiki nzima, na hata alipoacha ujumbe wa maandishi haukujibiwa.
Baada ya juhudi za kumpata Msajili wa Mahakama Kuu kugonga mwamba, JAMHURI iliwasiliana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu wa Bunge), William Lukuvi, ambaye Kamisheni ya Dawa za Kulevya iko chini yake. Yeye alisema ni kweli tatizo hilo lipo, na kwamba kuna mengi zaidi ya hayo.
“Mimi nasema sheria zinapaswa kubadilishwa, na Serikali tayari imeanza mchakato. Mtu akipatikana na pipi za dawa za kulevya zikatolewa tumboni mwake, nataka sheria irahisishwe na kuwezesha ashitakiwe na kufungwa maisha ndani ya siku saba.
“Hali ilivyo sasa ambapo unapaswa kuhifadhi ushahidi kwa miaka hadi 10 ukiendesha kesi moja, ushahidi unapoteza ubora. Wakati mwingine mtuhumiwa anashindwa kesi anatozwa faini ya Sh 500,000. Hatuwezi kupambana na dawa za kulevya tukashinda vita hii kwa utaratibu huo.
“Sasa Serikali imejipanga, ipo kwenye mchakato wa kuanzisha mahakama maalum ya kudhibiti dawa za kulevya na kwa kweli katika hili tunataka mchakato uwe mfupi kadiri inavyowezekana. Ndani ya muda mfupi kadiri inavyowezekana tupitishe sheria hii ili sheria iwe kali itoe adhabu itakayowazuia wengine kufanya biashara hii,” alisema Lukuvi.
Hivi karibuni, Tanzania imeanza kuzungukwa na sura ya kuwa Taifa la wauza dawa za kulevya baada ya Watanzania wengi kukamatwa ndani na nje ya nchi wakiwa na dawa hizo. Taarifa za uhakika zilizoifikia JAMHURI zinasema Rais Jakaya Kikwete ametoa maelekezo ya dhati kuhakikisha linafanyika jambo kubwa litakalowezesha kukamata mtandao wa wauza dawa za kulevya na kumaliza tatizo hili nchini.
Kwa mwezi mmoja sasa, JAMHURI imekuwa ikichapisha orodha ya wauza unga ‘dagaa’ na ‘mapapa’ hapa nchini, ambako hadi sasa gazeti hili limekwishatangaza

hadharani majina ya wauza unga 504 katika matoleo manne yaliyotangulia.
CHANZO: Jarida la Jamuhuri

Woman caught with Dhs3 million of drugs blames husband for...

Mwanamke wa Kitanzania aliyekamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dubai akiwa na madawa ya kulevya yenye thamani ya Dirham milioni tatu (takriban shilingi bilioni 1.3 za Kitanzania) amedai kuwa alifanywa 'punda' na mumewe.

Mwanamke huyo ambaye hata hivyo hajatajwa jina alikamatwa na kilo 3 za 'unga' (cocaine) akitokea nchini Brazil, ambapo alipita transit Dubai, kwa madhumuni ya kuja Tanzania.

Kwa mujibu wa Polisi wa Dubai, mwanamama huyo alieleza kuwa alitibuana na mumewe, na mumewe akaamua kumpeleka Brazil kwa mapumziko, na wakati anarejea kutoka huko alikabidhiwa suitcase ambayo baadaye iligundulika kuwa ina madawa hayo ya kulevya.

Polisi hao wanasema kilichopeleka mwanamke huyo kushtukiwa na hali yake ya kutia mashaka wakati akiwa airport hapo.

Kesi yake imewasilishwa kwa waendesha mashtaka kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria

iMETAFSIRIWA KUTOKA TOVUTI YA 7 Days in Dubai



29 Jul 2013

Ukisoma habari hii utabaini kwanini biashara ya madawa ya kulevya inazidi kushamiri. Ni kwamba, wauza unga wanafahamika,sio kwa polisi tu bali hata kwa Rais Jakaya Kikwete, na hakuna uthibitisho mzuri kama huu uliomo katika habari hii. 

Zingatia tarehe ya habari hii,18 SEPTEMBA 2006, les than mwaka mmoja tangu JK aingie madarakani.Sasa kama alikabidhiwa majina tangu wakati huo na hakuchua hatua, hivi waliotajwa katika orodha hiyo wamesha-multiply mara ngapi?

Vigogo dawa za kulevya watajwa

Written by Mwananchi 
Monday, 18 September 2006

*Majina yao yapelekwa kwa Rais Kikwete
*Ni orodha ndefu ya majina ya watu 58
*Wamo wafanyabishara, wanasiasa, viongozi wa dini
*Mbinu wanazotumia nazo zaanikwa hadharani

WITO wa Rais Jakaya Kikwete wa kutaka wananchi wajitokeze kutaja majina ya wahalifu nchini, umepata mwitikio mpya, safari hii watu kadhaa wakijitokeza kutaja majina ya vigogo wanaoongoza kwa biashara ya dawa za kulevya nchini.

Majina hayo yako katika barua iliyoandikwa na wananchi 15 kwenda kwa Rais Kikwete, ambamo wanadai kwamba walikuwa wakitumiwa na vigogo hao kufanya biashara
hiyo, lakini sasa wameamua kuachana nayo. Barua hiyo iliandikwa Septemba 8, mwaka huu na wahusika wanadai wamekwisha kuiwasilisha Ikulu.

Kwa mujibu wa barua hiyo, majina 58 yameorodheshwa yakiwa katika makundi matatu makubwa, la kwanza likiwa ni waagizaji wakubwa wa dawa hizo; la pili ni
wafadhili ambao majina yao hutumika kusafirisha dawa hizo; na la tatu ni wauzaji walioko Dar es Salaam, Tanga, Mwanza, Mbeya na Zanzibar.

Katika orodha ya waandishi wa barua hiyo wanaodai kusukumwa na uzalendo na uchungu kwa nchi yao, yamo majina ya wafanyabiashara maarufu nchini na wanasiasa,
wakuu wa taasisi nyeti, baadhi ya viongozi wa dini na maafisa wa juu serikalini.

Kundi la kwanza lina majina 12, miongoni mwao ni wafanyabiashara maarufu katika miji ya Dar es Salaam, Morogoro, Zanzibar, Arusha na Bagamoyo na baadhi ya
 viongozi wa dini wa madhehebu fulani.

Kundi hili linadaiwa kuwa linaingiza dawa za kulevya kwa njia mbalimbali zikiwamo, kutumia mipira ya kondomu, majokofu, vifaa vya hospitali, meli na
 marobota ya mitumba.

Katika kundi la pili kuna watu 19, miongoni mwao wamo wanasiasa wakubwa nchini wakiongoza kundi hili, kutoka taasisi ya fedha nchini na wafanyabiashara maarufu wa
Dar es Salaam na Zanzibar.

Kundi la tatu lina majina 27, ambao si ya watu wenye majina makubwa, lakini ndio wanaotumika kusambaza mitaani kwa watumiaji wa dawa za kulevya.
 

Mbali ya kushiriki katika kusambaza dawa za kulevya, kundi hili pia lina baadhi ya majina ya watu waliotajwa kushiriki katika kuingiza silaha nzito
 zinazotumika kwa ajili ya ujambazi kutoka nchi jirani.

Ufukwe wa Pwani ya Bahari ya Hindi eneo la Muhoro wilayani Rufiji inaelezwa kuwa linatumika kuingizia silaha hizo kutoka nchi jirani pamoja na dawa za
 kulevya chini ya ufadhili wa mmoja wa wanasiasa nchini.

Uwanja wa ndege wa Mwalimu J.K. Nyerere unatajwa kuwa unatumiwa na watu hawa kuingiza dawa hizo nchini kutokea nchi za nje, huku baadhi ya maafisa wa polisi
 watatu wakitajwa kuwa ndio wanaotoa ulinzi kwa watu wanaopitisha dawa hizo.

Nyumba ya afisa wa juu mstaafu katika idara nyeti iliyopo jijini Dar es Salaam inatajwa kuwa inatumika katika kuhifadhi vijana wanaoingiza dawa za kulevya
 nchini, huku nyumba ya mfanyabiashara mmoja iliyopo Mikocheni jijini Dar es Salaam ikitajwa kuwa ndiyo inayotumika kama kituo cha kutolea pipi tumboni kwa vijana wanaotumika kuingiza dawa hizo kutoka nje ya nchi.

Vile vile, katika kundi hili mwanamke mmoja anayefanya kazi katika taasisi moja ya fedha anatajwa kuwa anashiriki katika kuhujumu uchumi wa nchi kwa
 kusafirisha kwenda nje fedha nyingi za kigeni akitumiwa na mfanyabiashara mmoja maarufu wa dawa za kulevya nchini.

Mipaka ya Tunduma mkoani Mbeya, Horohoro mkoani Kilimanjaro na Namanga mkoani Arusha, nayo imetajwa kuwa inatumika kupitisha dawa za kulevya kwa kutumia
 mabasi na magari mengine. Kuna kampuni mbili za mabasi nchini zinazotajwa kuongoza kutumika katika usafirishaji.

Barua hiyo ya kurasa 10, pia inamtaja mwanamke mmoja ambaye anatumika kupitisha dawa za kulevya uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere kuwa ni sugu; aliwahi
 kuhukumiwa kifungo cha miaka 35 jela kwa kosa la kupatikana na dawa za kulevya, lakini hivi sasa yupo mitaani kifungo chake akitumikia mtu mwingine.

Alipoulizwa kutoa ufafanuzi wa suala hilo, Waziri wa Nchi ofisi ya Rais (Utawala Bora), Philip Marmo, alisema hajapata barua hiyo na kwamba atalizungumzia
 baada ya kuipata.

Naye Waziri wa Usalama wa Raia, Bakari Mwapachu, alisema hana taarifa za kuwako kwa barua hiyo. Hata hivyo, alisema kuna tume ya dawa za kulevya iliyopo
 chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo inayoshughulikia zaidi suala hilo.

Alisema Jeshi la Polisi linafanya kazi za kukamata watu wanaojihusisha na dawa hizo na kwamba mikakati mingine ya kupambana na watumiaji inafanywa na tume
 hiyo.

Mwanzoni mwa mwaka huu, Rais Kikwete aliagiza Jeshi la Polisi liongezewe uwezo wa kupambana na uhalifu, ikiwa ni pamoja na kuwahamisha vituo vya kazi askari
 waliokaa kituo kimoja kwa muda mrefu.

Pia alilitaka Jeshi hilo lijisafishwe lenyewe kutokana na madai kwamba polisi wanahusika na baadhi ya matukio ya uhalifu nchini.
 

Rais alitoa wito kwa wananchi wenye taarifa zozote za uhalifu, na wanaojua waliko majambazi wazipeleke taarifa hizo kwake kama wanaogopa kuzipeleka polisi.
 

Katika kuitikia wito huo, wananchi kadhaa waliandika barua iliyooroshesha majina ya polisi 20, wakiwamo baadhi ya makamanda wa polisi wa mikoa na kuikabidhi kwa Waziri wa Usalama wa Rais, Bakari Mwapachu.

Tangu wakati huo, mabadiliko makubwa yameshuhudiwa yakifanywa kwenye jeshi hilo, hata hivyo hii ni mara ya kwanza kwa watu kujitolea kuandika barua yenye
 majina na maelezo ya kina kama hii kuhusu biashara ya kulevya na kuipeleka kwa Rais.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.