Showing posts with label TISS. Show all posts
Showing posts with label TISS. Show all posts

27 Aug 2016

Tarehe 24 mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alimteua Dokta Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika kufuatia kustaafu kwa mkurugenzi aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.

Makala hii inajikita katika uchambuzi wa uteuzi huo kwa kuangalia changamoto na fursa zinazomkabili kiongozi huyo mkuu wa taasisi hiyo nyeti kabisa. Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Director of Risk Management alioshikilia Dokta Kipilimba huko nyuma alipokuwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.

Sote twafahamu jinsi Benki Kuu yetu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana ‘sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi.’ Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.

Kadhalika, huko mtandaoni kuna ‘tuhuma’ kadhaa kuhusu Dokta Kipilimba, lakini itakuwa sio kumtendea haki yeye, blogu hii na mie mwenyewe kujadili tuhuma ambazo hazina ushahidi wowote. Ni muhimu kutambua kuwa Tanzania yetu licha ya kuwa kisiwa cha amani pia ni kisiwa cha majungu, uzandiki, fitna, umbeya na uzushi.

Changamoto kubwa kwa Dokta Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Katika miaka ya hivi karibuni, taasisi hiyo muhimu kabisa imekuwa ikishutumiwa kuwa inachangia ustawi wa ufisadi, ujangili, biashara ya madawa ya kulevya, nk.

Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika matukio hayo ya kihalifu as such bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.

Ninaamini kuwa Dokta Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au mapungufu ya idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba “kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha mapungufu ya idara ya usalama wa taifa ya nchi husika, na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.”

Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya madawa ya kulevya, ujangili, rushwa, na ufisadi mwingine ni viashiria vya mapungufu ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama ‘kitengo cha usalama cha chama tawala CCM.’ Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.

Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna flani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa ‘Idara haina muda na makada wa chama tawala,’ na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.

Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala, na wakaishia kuonekana kama wahaini.

Changamoto nyingine kwa Dokta Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za ‘vigogo.’ Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ‘ndugu na jamaa hao wa vigogo’ haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6, HGCQ, nk wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.

Pia kuna tatizo la baadhi ya maafisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe ‘mtaani.’ Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.

Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao. Miongoni mwa maeneo hayo ni pamoja na ‘vituo muhimu’ na kwenye ofisi za balozi zetu nje ya nchi. Ikumbukwe kuwa unless afisa ametengeneza deep cover, uwepo wake kwa muda mrefu katika sehemu aliyokuwa ‘penetrated’ au kituo chake cha kazi kwingineko (mfano ubalozini) unaweza kupelekea ‘akaungua’ (burned).

Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa wa Tanzania yetu.

Kwa upande fursa kwa Dokta Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.

Dokta Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21, ambayo licha ya kutegemea HUMINT inaweza pia kutumia njia nyingine za kukusanya taarifa za kiusalama kwa kutumia teknolojia (GEOINT, MASINT, SIGINT, CYBINT, FININT na TECHINT kwa ujumla)

Na katika kwenda na teknolojia ya kisasa, basi pengine si vibaya iwapo Idara yetu ikafikiria haja ya uwepo wake kwenye mtandao, kwa kuwa na tovuti yake kamili na pia kufungua akaunti kwenye mitandao ya kijamii, hususan Twitter na Facebook. Hii sio tu inaweza kusaidia kutengeneza "human face" ya intel service bali pia yatoa fursa nzuri katika OSINT.

Fursa nyingine kwa Dokta Kipilimba ni matarajio ya sapoti ya kutosha kutoka kwa Rais Dokta Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka jana, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbe cha hali ya juu kabisa. Kama ‘sponsor’ na ‘consumer’ wa taarifa za kila siku usalama, inatarajiwa kuwa Dokta Magufuli atatekeleza ushauri wa Idara katika kukabiliana na matishio mbalimbali ya usalama wa taifa letu.

Dokta Kipilimba ana fursa ya kuleta mageuzi kwa Idara ya Usalama wa Taifa kwa kuangalia uwezekano wa kuwafikia watu walio nje ya taasisi hiyo, hasa pale uwezo wa Idara yetu unapokuwa limited. Nitoe mfano. Katika kupata taarifa mwafaka wa kudumu kuhusu, kwa mfano, mgogoro wa kisiasa huko Zanzibar, Idara inaweza ku-reach out wanazuoni wa historia ya taifa letu walipo ndani na nje ya nchi yetu.

Ikumbukwe kuwa sio rahisi kwa taasisi hiyo kuwa na maafisa au watoa habari katika kila eneo. Wenzetu wa nchi za Magharibi wamekuwa wakikabiliana na hali hiyo kwa kufanya kazi na ‘makandarasi’ (contractors), ambao of course, wamekidhi taratibu kama vile vetting.

Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na ‘subjects’ mbalimbali wanaolenga kulihujumu taifa letu.

Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dokta Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman, na kumkaribisha ‘uraiani.’

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI IDARA YETU YA USALAMA WA TAIFA




1 Dec 2014

Kwanza niombe samahani kwa ku-update blogu hii kitambo. Nilitingwa na majukumu. Pili, makala hii chini ilichapishwa katika gazeti la RAIA MWEMA toleo la Jumatano Novemba 26, 2014, lakini kwa sbabau nisizofahamu tovuti ya gazeti hilo haikuwa up-dated hadi asubuhi hii. Licha ya kuwa na nakala halisi ya makala hii, nilionelea ni vema kusubiri 'edited version' ya makala hii pindi ikichapishwa kwenye tovuti ya RAIA MWEMA. Endelea kuisoma
KWANZA, nianze makala hii kwa kuomba samahani kwa ‘kutoonekana’ kwa takriban mwezi mzima sasa. Hali hiyo ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu. Ninapenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa wasomaji mbalimbali walionitumia barua-pepe kuulizia kuhusu ‘ukimya’ huo.
Wiki iliyopita, Rais wa Marekani, Barack Obama, aliandika historia kwa kuweka hadharani mpango kabambe kuhusu hatma ya takribani wakazi milioni 12 wanaoishi isivyo halali nchini humo.
Ujasiri wa Obama katika suala hilo unatokana na ukweli kwamba licha ya jitihada za muda mrefu, uhasama wa kisiasa kati ya vyama vikuu vya siasa nchini humo, Democrats na Republicans, ulikuwa kikwazo kikubwa katika kufikia mwafaka na ufumbuzi.
Wakati vyama vyote viwili vinaafikiana kuhusu uwepo wa wakazi hao wasio halali milioni 12, wahafidhina wa Republicans wamekuwa wapinzani wakubwa kuhusu ‘ufumbuzi rahisi’ wa kutoa msamaha (amnesty) kwa wahamiaji hao na kisha kuimarisha udhibiti katika mianya inayotumiwa na ‘wahamiaji haramu.’
Lakini suala hilo limekuwa mzigo mkubwa kwa Obama ambaye hata kabla hajaingia madarakani aliahidi kutafuta ufumbuzi hasa ikizingatiwa kwamba licha ya utajiri wa Marekani, hakuna uwezekano wa kuwatumia wahamiaji hao wote.
Kadhalika, mara kadhaa Obama alikuwa akieleza kwamba kulipuuza tatizo hilo hakutolifanya lipotee lenyewe, bali litazidi kuwa kubwa na gumu kulitatua.
Hatimaye Obama aliwatahadharisha Republicans kuwa atalazimika kutumia ‘Nguvu ya Kirais’ (Executive Order) ambayo haihitaji kuridhiwa na Bunge la nchi hiyo, iwapo wanasiasa wataendeleza malumbano pasipo kuja na ufumbuzi.
Hata hivyo, Republicans walitoa vitisho mbalimbali kwa Obama dhidi ya kutumia ‘executive order,’ huku baadhi wakitishia kumburuza mahakamani ili kumng’oa madarakani kwa madai ya ‘kukiuka katiba.’
Licha ya vitisho hivyo, na upinzani wa wengi wa wananchi wa kawaida (ambao kura za maoni zilionyesha wananchi wengi kutoafiki Rais kutumia ‘executive order’ katika suala hilo), hatimaye Obama aliweka hadharani mpango huo kabambe utakaowapatia ahueni ya kimakazi takriban wahamiaji milioni tano.
Matokeo ya uamuzi huo ni bayana: Republicans wamekasirishwa mno na hatua hiyo, huku chama cha Democrats ambacho kwa kiwango kikubwa kimekuwa mstari wa mbele kuwanusuru wahamiaji hao, kikinufaika kwa sapoti kutoka kundi muhimu katika siasa za chaguzi za Marekani, Walatino.
Kundi hili linatajwa kuwa muhimu mno kwa vyama vyote viwili, kwa Democrats kubaki madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2016, na Republicans kukamata Ikulu baada ya miaka 10 ya Obama. Kidemografia, idadi ya Walatino inaongezeka kwa kasi kuliko kundi lolote lile la ‘asili ya watu’ kwa maana ya Wamarekani Weupe na Wamarekani Weusi, na makundi mengine madogo.
Sasa ni wazi kuwa ili mgombea wa chama chochote kile afanikiwe kuingia Ikulu, ni lazima apate sapoti na kura za kutosha kutoka kwa Walatino.
Uamuzi huo wa Obama umekuwa kama mtego kwa Republicans. Laiti chama hicho kikiendeleza upinzani dhidi ya suala hilo, si tu kitajipunguzia umaarufu wake kwa Walatino na hivyo kuathiri nafasi yao katika uchaguzi mkuu ujao, lakini pia kitawatenga Wamarekani wasio Walatino lakini wanaotaka ‘wahamiaji haramu’ kupatiwa makazi ya kudumu nchi humo.
Lakini kwa upande mwingine, chama hicho kinatambua kuwa kwa kiasi kikubwa ‘Wamarekani hao wapya’ (kwa maana ya ‘wahamiaji haramu’ watakaopewa makazi ya kudumu) wataisapoti Democrats kama kulipa fadhila kwa kushughulikia tatizo lao.
Nitaendelea kuwaletea maendeleo ya suala hili katika makala zijazo hasa kwa vile uamuzi huo wa Obama ni kama umeanzisha ‘vita’ ya kisiasa kati yake binafsi (na chama chake) dhidi ya Republicans ambao mapema mwezi huu walifanikiwa kukamata uongozi wa mabunge yote mawili ya nchi hiyo, yaani Seneti na Congress.
Lengo hasa la kuzungumzia tukio hilo la nchini Marekani ni hali ilivyo huko nyumbani hivi sasa. Hadi wakati ninaandaa makala hii, ‘mshikemshike’ unaotokana na skandali ya ufisadi wa ESCROW sio tu unazidi kukua lakini pia unaleta dalili za uwezekano wa Rais Kikwete kulazimika kufanya mabadiliko kwenye Baraza lake la mawaziri kwa mara nyingine.
Kwa vile takribani kila Mtanzania anafahamu kinachoendelea kuhusu skandali hiyo ya ESCROW, sioni haja ya kuizungumzia kiundani. Hata hivyo, pasi haya, na huku nikitambua kuwa Rais wetu Jakaya Kikwete yupo katika matibabu nchini Marekani, ukweli unabaki kuwa yeye ndiye chanzo cha yote haya.
Nikirejea uamuzi wa Obama kutumia ‘nguvu ya kirais’ kupata ufumbuzi katika tatizo la ‘wahamiaji haramu,’ Kikwete alipaswa kuchukua hatua kama hiyo muda mrefu uliopita. Hapa ninamaanisha Rais kutumia nguvu alizopewa na Katiba kupambana na uhalifu.
Ninaandika hivyo kwa sababu Kikwete ana uelewa wa kutosha kuhusu ‘mgogoro wa IPTL’ ikizingatiwa kuwa huko nyuma alishawahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini. Lakini wakati miaka yake 10 ikielekea ukingoni, hakuna jitihada yoyote ya maana iliyofanywa nae kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.
Lakini hata tukiweka kando uzoefu wake katika suala hilo, utawala wake utakumbukwa zaidi kwa kuandamwa na mlolongo wa matukio ya ufisadi ambayo hatma yake imekuwa kuwashawishi mafisadi wengine ‘kujaribu bahati zao’.
Naam, kama Kikwete alidiriki ‘kukumbushia haki za binadamu’ za mafisadi wa EPA, na kuwapa deadline ya kurejesha mabilioni waliyoiba, kwanini mafisadi watarajiwa waogope kufanya uhalifu?
Yayumkinika kuhitimisha kwamba laiti idadi ya safari alizokwishafanya nchi za nje ingelingana na hatua dhidi ya ufisadi/ mafisadi, huenda leo hii tungekuwa tunazungumzia ‘mafanikio ya kihistoria ya uchumi wa Tanzania’.
Badala yake, tumekuwa tukiandamwa na vyombo vya habari vya kimataifa kuhusu taifa letu lilivyoukumbatia ufisadi kiasi cha kuruhusu ndege ya msafara wa Rais wa China kuondoka na vipusa, sambamba na taarifa mpya kuwa kuna mpango wa serikali kuwatimua wafugaji wa Kimasai katika makazi yao ili kukabidhi eneo hilo kwa familia ya kifalme ya mojawapo ya nchi za Kiarabu.
Sasa badala ya viongozi wetu kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa letu, wamekuwa ‘bize’ kupambana na vyombo vya habari vya kimataifa kukanusha tuhuma hizo. Hivi wazembe hawa hawaoni haya na kujiuliza “kwa kipi hasa cha kuvifanya vyombo vya habari vya kimataifa vituandame bila sababu?”
Kwa upande mwingine, skandali hii ya ESCROW ni uthibitisho mwingine kuwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa (TISS) imepoteza mwelekeo, haitimizi wajibu wake, na ni kama ipo likizo ya muda mrefu.
Hivi inawezekana vipi huyo ‘Singasinga’ anayetajwa kuwa mhusika mkuu katika skandali hiyo aliruhusiwa kuishi Tanzania huko rekodi yake ikionyesha bayana kuwa ni mtu hatari kwa usalama wa taifa letu?
Hii haikuhitaji hata operesheni maalum kwa Idara yetu ya Usalama wa Taifa kwani habari za mtu huyo zipo wazi kwenye mtandao. Hivi Idara hiyo imejaa uzembe kiasi cha kushindwa japo ku-Google taarifa za mtu huyo?
Lakini kama ambavyo lawama nyingi katika skandali hii zinaelekezwa kwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo na Katibu na Katibu Mkuu wake, Eliachim Maswi, sambamba na Mwanasheria Mkuu, Frederick Werema, huku Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akishutumiwa kwa kushindwa kusimamia vema watendaji walio chini yake, wenye kustahili kubeba lawama kubwa zaidi ni Rais Kikwete na idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Ninaandika makala hii kabla ya taarifa za uchunguzi za CAG na TAKUKURU kusomwa hadharani na ‘Kamati ya Zitto’ (PAC), kwahiyo ni vigumu kubashiri hatma ya suala hili. Hata hivyo, uzoefu wa skandali zilizopita, kuanzia Richmond, EPA, Mabilioni  yaliyofichwa Uswisi, Meremeta, Tangold, nk, si ajabu iwapo wahusika wakuu watalindwa na Watanzania kuachwa ‘wanang’aa macho tu.’
Muda mfupi uliopita, zimepatikana taarifa kwamba ripoti hiyo ya PAC imeonekana mitaani huku kurasa zenye majina ya wahusika zikiwa zimenyofolewa. Binafsi ninaamini huo ni ‘uhuni’ tu unaofanywa kuwachanganya Watanzania.
Lakini ukijumlisha na tukio linalodaiwa la kunyweshwa sumu Mbunge Nimrod Mkono, ni muhimu kutodharau nia, sababu na uwezo wa mafisadi kupambana na ukweli kuhusu skandali hii.
Nihitimishe makala hii kwa kumkumbusha Rais Kikwete- kwa mara nyingine - kuwa chini ya mwaka mmoja kutoka sasa atarejea ‘uraiani.’ Ni muhimu kwake kutumia miezi hii michache iliyobaki kurejea ahadi aliyotoa mara baada ya kuapishwa kuwa Rais wetu mwaka 2005 kuwa hatowaonea aibu mafisadi. Tungependa tumkumbuke kwa mema lakini sio rekodi ya kuliingiza taifa kwenye korongo refu la ufisadi.
Kwa ndugu zangu wa Idara ya Usalama wa Taifa, ninawasihi mtambue mzigo mkubwa mnaowabebesha Watanzania masikini kumudu gharama za operesheni zenu. Kwanini msijiskie aibu  kuwasaliti wanyonge hawa –wengi wakiwa ni ndugu, jamaa na marafiki zenu – kwa kutotimiza majukumu yenu ipasavyo?
TUSIPOZIBA UFA TUTAJENGA UKUTA

9 Aug 2012




Picha zote mbili zinamwonyesha Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki Samwel Sitta alipotembelea maonyesho ya kilimo ya Nane Nane mkoani Morogoro.Katika picha zote,Waziri Sitta ameambatana na mlinzi (BODIGADI) kutoka Idara ya Usalama wa Taifa.Ninakumbuka,uamuzi wa kumpatia Sitta ulinzi ulifanywa na Serikali wakati waziri huyo alipokuwa Spika wa bunge lililopita,na alidai anatishiwa maisha.Je matishio hayo bado yanaendelea?Ikumbukwe,gharama za kutoa ulinzi kwa kiongozi ni kubwa sana,na kimsingi,kiprotokali,Sitta hastahili kuwa na bodyguard....unless tumembiwe kuwa tishio dhidi ya maisha yake bado lipo hai 



Picha kwa hisani ya AudifaceJackson Blog


19 Jul 2012


Wanafunzi wa Sekondari ya Wavulana Tabora wakiwa katika mafunzo ya kivita katika mapori ya Uchama,wilayani Nzega.Picha kwa hisani ya Tabora School Facebook Group

Naikumbuka Tabora Boys,Najivunia Uzalendo Wangu
NIANZE makala hii kwa kurejea barua-pepe niliyotumiwa na mmoja wa wasomaji wa gazeti hili. Msomaji huyo ambaye kwa bahati mbaya au makusudi hakuambatanisha jina lake alieleza kuwa aliguswa sana na makala yangu katika toleo lililopita iliyobeba kichwa cha habari “Ni Vigumu Kuiamini Serikali kwa Dkt Ulimboka.”
Na kuguswa kwa msomaji huyo ni kwa namna mbili; kwa upande mmoja alidai amevutiwa sana na changamoto niliyoitoa kwa Idara ya Usalama wa Taifa, ambayo kwa maelezo yake, anaiona kama taasisi pekee anayoitumainia kuiokoa Tanzania yetu inayoelekea kusikoeleweka.
Lakini kwa upande mwingine, msomaji huyo alionyesha wasiwasi wake kuhusu anachokiona kama uwezekano wa walioudhiwa na makala hiyo (na nyinginezo zinazowazungumzia) kutafuta namna ya kuninyamazisha.
Msomaji huyo aliniusia kuwa japo anatambua kuwa pengine ninachoandika kuhusu yasiyopendeza huko nyumbani kinatokana na uchungu tu kwa taifa langu lakini akanikumbusha yaliyowahi kutokea huko nyuma kwa wengi waliojaribu kukemea maovu katika jamii yetu.
Akanikumbusha kuhusu kiongozi aliyemuita ‘mtoto wa kweli wa Tanzania’ yaani aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Sokoine, ambaye kwa mujibu wa msomaji huyo, anaamini alifupishiwa maisha kutokana na kuingilia maslahi ya mafisadi wa zama hizo.
Kadhalika, aligusia kilichomkumba mmoja wa waandishi bora kabisa wa habari za uchunguzi Marehemu Stan Katabalo. Akadai, kilichompeleka kuzimu mwandishi huyo hakina tofauti na shambulio la kinyama la kumwagiwa tindikali mwandishi mwingine, Said Kubenea.
Pia akaniusia kuwa (namnukuu) “Kama kosa la Dk. (Steven) Ulimboka lilikuwa kutimiza tu wajibu wake kama kiongozi wa jumuiya ya madaktari na matokeo yake ametishia kutekwa na kuteswa, vipi wewe unayediriki kuikosoa taasisi nyeti kama Idara ya Usalama wa Taifa?”
Katika kuhitimisha, msomaji huyo aliniusia kwamba kwa maneno haya (namnukuu), “Kwa vile wewe upo huko Ulaya ambapo shida zake si kama huku kwetu, basi mie ninakushauri usijitafutie matatizo. Hii nchi yetu mtuachie sie wenyewe tuliokwishazoea mgawo wa umeme usioisha licha ya ahadi za kila kukicha, rasilimali zetu kutoroshwa kana kwamba tumezichoka, na mabilioni yetu kuletwa huko Ulaya kwenu kwenye akaunti za mafisadi huku wakituacha tunataabika na uchumi unaozidi kudidimia.”
Kwa hakika nimeguswa mno na barua-pepe hiyo ya msomaji huyu. Japo hakutaja jina lake lakini ninamshukuru kwa yote aliyoandika. Na kikubwa zaidi, angalau anatambua kwa nini 'ninajiingiza matatizoni' kwa kuzungumzia yale ambayo katika mazingira ya kawaida hayapaswi kuzungumzwa.
Ni kweli, nina uchungu na nchi yangu, na kama hilo ni ‘kosa’ litakaloweza kunigharimu huko mbeleni, basi na iwe hivyo. Naomba niweke rekodi vizuri: ninaposema nina uchungu kwa nchi yangu simaanishi kuwa mie ndiye mwenye uchungu (au mapenzi zaidi) kwa nchi yangu zaidi ya watu wengine. Hapana. Ninaamini huo ni wajibu wa asili wa kila Mtanzania mzalendo.
Lakini pengine ni vema nikieleza kwa nini ninaguswa sana na mwenendo wa mambo huko nyumbani, ukiachilia mbali Utanzania wangu. Pengine ni baadhi ya mazingira niliyopitia hadi kufika hapa nilipo. Kwa mfano, mwaka 1990 nilichaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora (Tabora Boys High School). Shule hii yenye historia ya kipekee kwa nchi yetu imetoa mchango mkubwa sana wa ‘kuzalisha’ viongozi wa nchi yetu.
Wakati ninajiunga na shule hiyo ilikuwa na mchepuo wa kijeshi. Kama kuna faida kubwa niliyoipata kwa kuwa mwanafunzi hapo ni hiyo ‘bahati’ ya kuwa ‘nusu-mwanafunzi, nusu-mwanajeshi.’
Bahati nyingine niliyoipata nikiwa mwanafunzi shuleni hapo ni kuchaguliwa kuwa kiranja mkuu. Kwa vile shule ilikuwa ni ya mchepuo wa kijeshi, wadhifa wa kiranja mkuu ulikuwa ukijulikana kama Kamanda Mkuu wa Wanafunzi (kwa kimombo Students’ Chief Commander). Hadi leo, baadhi ya wanafunzi niliokuwa ninasoma nao wanaendelea kuniita ‘Chief.’
Kufupisha maelezo, mchepuo huo wa kijeshi sio tu ulitupatia wanafunzi ukakamavu na nidhamu ya hali ya juu bali pia ulitujaza uzalendo kwa nchi yetu kwa kiwango kikubwa. Huku tukiwa na sare zetu za ‘kijeshi’ (zilikuwa kombati za khaki kama za jeshi la mgambo), maafande wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) waliokuwa wakiendesha ‘kitengo cha jeshi’ shuleni hapo walitupatia mwamko wa hali ya juu kuhusu kuitumikia na kuilinda nchi yetu.
Kabla ya kuanza masomo tulipewa kile kilichoitwa “karibu shuleni” iliyojumuisha kwata za kijeshi na hatua nyingine wanazopitia ‘makuruta’ wanapoingia kambini kwa mara ya kwanza. Ilipofika mwisho wa mwaka, wanafunzi wa kidato cha tatu na cha tano tulipelekwa msituni kwa mafunzo ya vita kwa vitendo.
Baada ya kutoka hapo nilijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa ambapo kwa wakati huo ilikuwa ni lazima (kwa mujibu wa sheria). Kwa bahati nzuri, muda mfupi tu baada ya kujiunga na JKT nilichaguliwa kuingia kwenye kundi lililotarajiwa kutoa marubani na mainjinia wa ndege za jeshi.
Tukapelekwa kambi ya JWTZ Kunduchi (RTS). Tulipofika hapo, tukapewa jina la ‘wazalendo,’ yaani watu tuliojitolea kwa ajili ya nchi yetu. Well, sikufanikiwa kuwa rubani au injinia lakini ‘tuzo’ hiyo ya kuitwa mzalendo ilikuwa shani kubwa kwa kila mmoja wetu.
Miaka machache baadaye nilijiunga na taasisi moja ambayo sio tu ili kujiunga ilipaswa kuwa na uzalendo wa hali ya juu lakini pia ilinijaza ‘dozi zaidi’ za kuipenda na kuitumikia nchi yangu kwa nguvu zote.
Kama ilivyo kwa taaluma kama ualimu ambapo pindi ukiwa mwalimu unabaki kuwa na maadili ya kiualimu hadi uzeeni, mafunzo na uzoefu wa kazi niliopata kutoka katika taasisi hiyo unanifanya niendelee kuwa na wajibu ule ule: kutimukia nchi yangu kwa nguvu zote.
Sipendi kuandika makala inayonizungumzia mie, kwani lengo la safu hii ni kuzungumzia masuala muhimu yanayohusu nchi yetu. Lakini Nimelazimika kuandika haya ili kuondoa dhana potofu kuwa labda nina chuki na taasisi fulani au ‘kwa mujibu wa wahusika’ ninafanya uchochezi.
Kuna suala moja la msingi ambalo walafi wanaotafuna rasilimali zetu na mafisadi kwa ujumla wanajitahidi kulipuuza. Tanzania ni yetu sote, na kwa namna moja au nyingine sote ni kitu kimoja. Sasa fisadi anapokwapua fedha zilizopaswa kuleta maendeleo kwa nchi yetu anapaswa kutambua kuwa katika mlolongo wa wahanga wa ufisadi huo ni mtu au watu wanaohusiana naye.
Ni muhimu tufike mahala turuhusu maoni yanayokinzana na matendo au mtizamo wetu. Mara kadhaa tumeshuhudia wazalendo wanaojaribu kuwakumbusha watawala wetu wajibu wao wakiishia kuitwa majina mabaya na wengine kuhujumiwa. Mifano ni mingi lakini si vibaya kupigia mstari kauli za mtu kama Mzee Hans Kitine, Mkurugenzi wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa, ambaye mara kadhaa amekuwa mstari wa mbele kujaribu kushauri kuhusu mwenendo wa CCM, serikali na taifa kwa ujumla. Lakini kila anayefuatilia vema matukio ya huko nyumbani, mzee huyo aliyelitumikia taifa kwa uadilifu (akiwa Mkurugenzi wa TISS, kabla ya kuingia kwenye siasa) ni mmoja wa wahanga wa fitna dhidi yake. Kosa lake kubwa ni kukemea maovu na kushauri njia mwafaka za kulinusuru taifa letu.
Sawa, kama alivyoandika msomaji aliyenitumia barua-pepe, sisi wengine tupo mbali na nyumbani, na ni kweli kuwa hatuguswi moja kwa moja na adha mbalimbali zinazoendelea huko. Lakini, uwepo wetu huku nje sio tu hautupunguzii Utanzania wetu bali pia ifahamike kuwa baadhi yetu tuna ndugu, jamaa na marafiki ambao ni wahanga wa kila siku wa mwenendo mbovu wa mambo huko nyumbani. Haihitaji busara kumaizi kuwa huwezi kuwa na raha ughaibuni huku watu wako wa karibu huko nyumbani ‘wanapigika.’
Kwa wanaodhani kuwa dawa na kudhibiti ‘kelele kama zetu’ ni ‘kutushughulikia sisi wapiga kelele’ ni vema wakatambua kuwa huwezi kuua wazo sahihi. Kama ambavyo vifo vya akina Katabalo havijazuia uzalendo wa kuwasemea walalahoi wasio na wasemaji (rejea timua-timua huko bungeni kwa baadhi ya wabunge wanaowasilisha vilio vya wapiga kura wao) ndivyo ambavyo baadhi yetu tutaendelea kukemea maovu yanayotishia kuipeleka Tanzania yetu kwenye korongo lenye kina kirefu.
Nimalizie makala hii kwa fundisho hili la historia: japo wabaguzi wa rangi walimuua Martin Luther King, Jr (mpigania haki za Weusi huko Marekani) lakini leo taifa hilo lina Rais Mweusi (Barack Obama). Na japo makaburu waliweza kumfunga Nelson Mandela kwa miaka kadhaa, leo hii Afrika Kusini ipo chini ya utawala wa weusi walio wengi.
Kutekwa na mateso kama vilivyomkumba Dk. Ulimboka, na matukio ya kihuni kwa watu kama Kubenea, na ‘sumu’ inayomwagwa kwa wazalendo kama Mzee Kitine, kamwe haviwezi kutuzui sisi wenye uchungu na nchi yetu kuendelea kukemea maovu na kudai kile Waingereza wanaita ‘value for money’ yaani ubora unaotokana na fedha (ya mlipakodi wa Tanzania).
Na kwa msomaji aliyenisihi niwe makini, licha ya kumshukuru ningependa kumhakikishia kuwa sijakurupuka katika harakati hizi za kuwasemea walalahoi. Mwanafalsafa wa Kichina wa sanaa ya vita (Art of War) Sun Tzu anaasa; “If you know the enemy and know yourself you need not fear the results of a hundred battles.”
Mungu Ibariki Tanzania (na umwangamizie kila fisadi na yule anayemlinda).

16 Jul 2012



KWA mara nyingine, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetoa tuhuma nzito dhidi ya Idara ya Usalama wa Taifa (TISS), safari hii ikidaiwa kuwa baadhi ya viongozi wa taasisi hiyo nyeti wana mpango wa kuwaua baadhi ya viongozi wa CHADEMA.

Itakumbukwa kuwa wakati wa mchakato wa Uchaguzi Mkuu uliopita, CHADEMA kiliituhumu Idara hiyo kuwa ilikuwa inakihujumu chama hicho, tuhuma ambazo zilifanya Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TISS, Jack Zoka (pichani juu) , kuzikanusha vikali.

Tuhuma hizi za CHADEMA zimekuja siku chache baada ya tukio la kusikitisha na la kinyama lililomkuta kiongozi wa jumuiya ya madaktari Dk. Steven Ulimboka ambaye alitekwa na hatimaye kuteswa na watu 'wasiojulikana.'

Katika tukio la Dk. Ulimboka, Serikali imejikuta ikinyooshewa vidole kuwa inahusika, hali iliyomfanya Rais Jakaya Kikwete kulizungumzia suala hilo katika hotuba yake kwa Taifa hivi karibuni.

Lakini takriban kila anayefuatilia kwa ukaribu suala hilo anaweza kuungana nami kutanabahisha ya kuwa japo hotuba ya Rais Kikwete imesaidia kwa namna fulani kuonyesha kuwa Serikali yake imeguswa (kwa maana ya kusikitishwa) na tukio hilo, kwa kiwango kikubwa haijasaidia kuondoa fikra kuwa kuna mkono wa Serikali.

Binafsi, nimelichambua kwa kirefu tukio hilo la kutekwa na kuteswa kwa Dk. Ulimboka katika mfululizo wa makala zangu za sauti (podcasts). Makala husika yenye kichwa cha habari “Nani aliyemteka na kumtesa Dk. Ulimboka?”

Kwa kifupi, katika makala hiyo nimezungumzia dhana tatu kuhusiana na tukio la Dk. Ulimboka. Ya kwanza ni hiyo inayogusa hisia za wengi kuwa Serikali inahusika na tukio hilo. Katika makala hiyo, nimeungana kimtizamo na kauli ya Rais Kikwete kuwa “Serikali imteke na kumtesa Dk. Ulimboka ili iweje.”

Kadhalika, nimeeleza kuwa japo kuna nyakati Serikali kwa kutumia vyombo vya dola inaweza kutumia vitisho na hata nguvu ikibidi ili kuzima upinzani dhidi yake, katika mazingira ya kawaida ni vigumu kuamini kuwa Serikali ya Rais Kikwete ingekuwa tayari kujiingiza matatizoni kwa kumteka na kumtesa kiongozi wa madaktari ili tu iwatishe madaktari wanaogoma.

Nimebainisha hivyo kwa vile ninaamini kuwa Serikali inafahamu fika kuwa kumnyamazisha Dk. Ulimboka hakuwezi kuwanyamazisha madaktari wote nchini.

Dhana ya pili ni ile ya hujuma dhidi ya Serikali. Kimsingi dhana hiyo inabashiri kuwa pengine kuna ‘watu wenye nguvu na jeuri ya fedha’ ambao wamefanya unyama huo dhidi ya Dk. Ulimboka kwa minajili ya 'kuikoroga' Serikali. Takriban kila anayefuatilia mwenendo wa siasa ndani ya chama tawala CCM atakuwa anafahamu kuwa kuna mtifuano mkubwa (japo usiosikika sana waziwazi) unaoendelea ndani ya chama hicho, hususan kuhusiana na kinyang’anyiro cha urais mwaka 2015.

Kwamba kuna mafisadi wanaoweza kumwaga fedha aidha kwa ‘majasusi binafsi’ au ‘majasusi rasmi’ ni jambo linalowezekana. Kinachonifanya niipe uzito mdogo dhana hii ni uchambuzi wa hasara na faida za tendo husika (cost and benefit analysis).

Hivi, kama mafisadi wakimteka na kumtesa Dk. Ulimboka, kisha Serikali ya Kikwete ikaandamwa, mafisadi hao watanufaikaje (zaidi ya kufurahia kuona Serikali inabebeshwa lawama isizostahili)?

Dhana ya tatu, na ambayo binafsi ninaipa uzito mkubwa, ni uwepo wa kile kinachofahamika katika lugha ya Kiingereza kama ‘rogue elements of the state apparatus’ (yaani ‘watendaji katika taasisi za dola ambao wanatenda kazi zao kinyume na taratibu na sheria,’ kwa tafsiri isiyo rasmi).

Dhana hii ya mwisho inaweza kushabihiana na ya pili kwa maana ya hicho nilichoita ‘majasusi rasmi,’ yaani watumishi wa vyombo vya dola ambao wanatumia ujuzi wao kutekeleza matakwa, si ya mwajiri wao, bali ya mafisadi waliowapa fedha kwa ‘kazi maalumu.’

Katika makala hiyo ya sauti nimeeleza kuwa ni wazi vyombo vya dola vilikuwa vikimfuatilia Dk. Ulimboka na waratibu wengine wa mgomo wa madaktari. Hilo si la kuhoji kwani ni utaratibu ‘wa kawaida’ kwa wana usalama. Iwe ni taasisi ya mashushushu wa ndani wa Marekani (FBI), au wenzao wa Uingereza (MI5), au TISS huko nyumbani, kila mtu au kikundi kinachotazamwa kama tishio kiusalama hufuatiliwa kwa karibu.

Sasa basi, kwa kuzingatia dhana hiyo ya ‘rogue elements,’ inawezekana watendaji waliokabidhiwa jukumu hilo waliamua kutumia njia za ‘liwalo na liwe’ (hapana, si kama ile ya tamko la Waziri Mkuu Mizengo Pinda) baada ya ‘njia za kistaarabu’ kumlazimisha Dk. Ulimboka awaeleze ‘nani anayewachochea madaktari kugoma’ kutozaa matunda.

Yaani baada ya diplomasia kushindwa, wakaamua kutumia mateso ya hali ya juu (kwa lugha ya kisheria ‘third degree torture’ na kitaalamu ‘fifth degree torture’).

Kwa nini ninashawishika kuamini kuhusu rogue elements? Tumeshuhudia matukio kadhaa huko nyuma. Naamini wengi wa wasomaji mtakuwa bado mnakumbuka tukio la mwandishi wa habari mahiri na mhariri  wa gazeti la Mwanahalisi, Said Kubenea, kumwagiwa tindikali usoni. Kibaya zaidi katika tukio hilo, mmoja wa wahusika alitajwa kuwa ni mwajiriwa wa TISS.

Sijui kesi hiyo iliishaje lakini la msingi hapa ni kuwa iliacha doa la aina fulani kwa taasisi hiyo hasa kwa vile haikuwahi kumkana afisa huyo (kwa maana ya kusema hakutumwa kiofisi bali alikuwa ‘rogue officer’ tu).
Itakumbukwa pia kuwa Waziri wa Uchukuzi Dk. Harrison Mwakyembe aliwahi kueleza kuwa Idara ya Usalama wa Taifa ilikuwa na mpango wa kumuua. Kama ilivyokuwa kwa tukio la Kubenea lililomhusisha mtu aliyatajwa kuwa ni Afisa Usalama wa Taifa, Idara hiyo haikuwahi kukanusha tuhuma hizo.

Tukirejea kwenye tuhuma za CHADEMA dhidi ya TISS, binafsi nashawishika kuamini kuwa kama kuna ukweli katika tuhuma hizo basi itakuwa ni zilezile ‘rogue elements’ ambazo ninaamini zipo ndani ya taasisi hiyo nyeti.

Najua hili halitowapendeza wahusika, lakini kuna hisia kwamba ukiweka kando taasisi hiyo kuendeshwa kama kitengo cha usalama cha CCM moja ya sababu nyingine kubwa ya matatizo yanayoikabili taasisi hiyo ni ajira zilizotolewa pasipo kuzingatia ‘wito’ na ‘kipaji’ cha kuwa Afisa Usalama.

Popote duniani, maafisa usalama wanapaswa kuwa ‘watu zaidi ya watu wa kawaida’ kwa maana ya kuwa na upeo na uwezo wa hali ya juu katika takriban kila nyanja ya akili zao:  na huo ndio msingi wa neno INTELLIGENCE kwa kimombo.

Sasa tunaporuhusu watoto zetu, ndugu au jamaa zetu kuingizwa kwenye taasisi nyeti kama hiyo kwa vile tu ‘kuna maslahi manono’ tunaiweka rehani nchi yetu.

Naomba niwe mkweli. Madudu mengi yanayoendelea katika Tanzania yetu kwa sasa yanachangiwa na ubabaishaji unaoendelea ndani ya idara hiyo muhimu kwa ustawi na maendeleo ya taifa lolote lile duniani. Wao wanafahamu kanuni hii: uimara au kuyumba kwa nchi ni kielelezo cha uimara au udhaifu wa Idara ya Usalama ya nchi husika.

Sasa kama tuna maofisa usalama huko Benki Kuu (BoT) lakini bado ufisadi wa EPA ukafanikiwa, na kama TISS ipo kazini saa 24 lakini bado kuna majambazi wamemudu kutorosha mabilioni ya dola na kuzificha nchini Uswisi basi ni wazi Idara hiyo ni dhaifu.

Na kama tunakubaliana kuwa kuna udhaifu mkubwa katika taasisi hiyo, kwa nini basi CHADEMA wasiamini taarifa kuwa Idara hiyo ina mpango wa kuwadhuru? Sitaki kuamini kuwa, iwapo taarifa hizo ni kweli, basi ni za ki-Idara bali ninaendelea kuhisi kuwa ni matokeo ya kulea ‘rogue elements’ ndani ya chombo hicho muhimu.

Unajua, inapofika mahala Afisa Usalama wa Taifa anaona sifa kutangaza wadhifa wake baa ili vimwana watambue kuwa yeye ni shushushu, au kiongozi mwandamizi wa taasisi hiyo nyeti anapoweza kufanya ‘madudu’ hadi sisi tulio nje ya nchi tukafahamu, basi ni wazi kunahitajika kazi ya ziada kurekebisha mwenendo wa chombo hicho nyeti.

Ninatambua kuwa kuna watakaokerwa (na pengine kushauri hatua ‘mwafaka dhidi ya mtizamo wangu’) lakini ninaamini kuwa kila Afisa Usalama wa Taifa mzalendo na aliyekula kiapo cha utii kwa Taifa anakerwa kuona nchi yetu ikienda kwa mwendo wa bora liende huku rasilimali zetu zikiporwa kwa mtindo wa ‘bandika bandua.’

Pasipo mageuzi ya haraka ndani ya taasisi hiyo si tu itaendelea kutuhumiwa na CHADEMA lakini mwishowe walipa kodi wanaowezesha maslahi manono kwa wanausalama wetu watasema ‘imetosha.’
Watanzania wanaweza kufika mahala wakahoji umuhimu wa kuwa na taasisi ya ‘kufikirika’ ambayo licha ya kuogopwa na wengi (nikiamini bado kuna wanaoiogopa) inashindwa kudhibiti uharamia lukuki unaofanywa dhidi ya nchi yetu na Watanzania wenzetu kwa kutumia madaraka yao.

Nimalizie makala hii kwa kutoa tahadhari kwa Idara hiyo kwamba maswali magumu hayajibiwi kwa majibu mepesi. Mmoja wa viongozi wa ngazi za juu za taasisi hiyo amejibu tuhuma zilizotolewa na CHADEMA kwa namna ileile alivyojibu mwaka 2010 pale Idara hiyo ilipotuhumiwa kuihujumu CHADEMA kwenye kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu. Tatizo la kiongozi huyo, na pengine Idara hiyo kwa ujumla ni uzembe wa kusoma alama za nyakati.

Na kila mzalendo-awe ndani ya taasisi hiyo au mwananchi wa kawaida-anapaswa kupinga kwa nguvu zote dalili za kutaka kuigeuza nchi yetu kuwa ‘Mafia State’ (yaani dola ambayo kila Tom, Dick na Harry anaweza kuteka na kutesa au kupanga kuuwa wale  wanaopigania haki za wanyonge kama hao viongozi wa CHADEMA wanaodai kutishiwa kuuawa kwa ‘kosa la kuwakalia kooni wabaka uchumi wetu.’)

Biblia inasema mwenye haki ataanguka saba mara sabini lakini atasimama. Na kila mzalendo atakwazwa vya kutosha lakini, inshallah, Tanzania tunayoistahili itafikiwa.

MAKALA KAMILI INAPATIKANA HAPA http://raiamwema.co.tz/ni-vigumu-kuiamini-serikali-kwa-dk-ulimboka

26 Sept 2011


Wajuzi wa mambo wanadai kuwa moja ya mambo yanayopunguza ufanisi wa Idara yetu ya Usalama wa Taifa ni tabia iliyoota mizizi ambapo kila kigogo anataka kumpatia mwanae,mpwae,mtoto wa rafiki yake,nk katika ajira ya taasisi hiyo nyeti.Haina ubaya kutoa ajira iwapo mwajiriwa mtarajiwa atakuwa na sifa husika.Lakini uzoefu umeonyesha kuwa kanuni na taratibu zinabemendwa makusudi ili ajira hizo ziende kwa watu wa karibu wa vigogo hao.

Kibaya zaidi ni ukweli kwamba wengi wa watoto wa vigogo wanapopata ajira kwenye taasisi kama hii ambayo msingi wake mkubwa ni uzalendo wa mtumishi husika hujiona kama 'untouchables' flani,wanafanya mambo wapendavyo,usumbufu mtaani kwa zile 'unajua mimi ni nani/nafanya kazi wapi' huku bastola zikiachwa zionekane waziwazi kama Aden Rage.Wengi wa hawa vijana hawafahamu jukumu kubwa walilonalo kwenye kila sekunde ya uhai wa Mtanzania.Don't get me wrong kuwa ninajifanya kuelewa sana mambo haya lakini ukweli ni kwamba taaluma ya ushushushu ni uti wa mgongo wa uhai wa taifa lolote lile duniani.Idara ya Usalama ya nchi ikiyumba,nchi nayo inayumba.Watu wengi hawaelewi umuhimu wa chombo hiki kwa vile kimaadili kinapaswa kufanya kazi zake kwa siri,japo watoto wa vigogo wanaona usiri huo kama kero.

Anyway,nimekutana na tangazo la ajira za ushushusu katika 'Idara ya Usalama' (wa ndani-yaani ya kuzuia ujasusi) ya Uingereza-MI5 au kwa kirefu Military Inteligence,Section 5)-ambalo limewekwa kwenye gazeti la bure la kila siku la METRO.Utaratibu huu ambao sitarajii kuuona ukiigwa na taasisi nyingi za usalama duniani,achilia mbali yetu,unaweza kusaidia sana kufanya zoezi zima la kuajiri (recruitment process) kuwa ya huru,wazi na inayowekea mkazo uwezo,ujuzi na sifa za mwombaji kazi (based on merit(s)).

Hii ni mada nyeti kwahiyo naomba niishie hapa.Ukiwa na swali,usisite kuniuliza (majibu yatategemea swali limeulizwaje).

6 Jul 2011

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalam wa Taifa Rashid Othman (wa tatu kushoto,mwenye shati la kitenge)
Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TISS, Jack Zoka

Wabunge walipua Usalama wa Taifa  
Tuesday, 05 July 2011 21:00

Ramadhan Semtawa, Dar
WABUNGE watatu jana waliishambulia Idara ya Usalama wa Taifa (TISS), bungeni baada ya kueleza kuwa imeshindwa kuzuia uhujumu uchumi na badala yake imejikita kwenye siasa za kukipendelea chama tawala, CCM na kuukandamiza upinzani.

Tuhuma hizo zinakuja wakati tayari nchi imetikiswa na matukio kadhaa ya ufisadi ikiwamo wizi wa zaidi ya Sh133 bilioni katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ununuzi wa rada ya kijeshi na ufisadi unaodaiwa kufanywa katika kampuni za Meremeta, Tangold na Deep Green Finance.

Kwa nyakati tofauti wakichangia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (Utumishi, Utawala Bora na Uratibu na Mahusiano ya Jamii), wabunge hao waliirushia makombora idara hiyo na kupendekeza ikajifunze nje jinsi ya kufanya kazi zake.

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, ndiye alikuwa mwiba zaidi baada ya kuweka bayana kwamba idara hiyo imeshindwa kusaidiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuzuia rushwa kubwa zinazohujumu uchumi wa nchi.

Mchungaji Msigwa ambaye alizungumza kwa hisia kali, alisema idara hiyo imegeuka chombo cha kulinda maslahi ya kisiasa hasa ya CCM na kukandamiza upinzani huku ikiacha uchumi wa nchi ukiendelea kuhujumiwa.

Kwa mujibu wa Msigwa, endapo Idara ya Usalama wa Taifa, ingetumia nguvu nyingi kuzuia uhujumu uchumi kama inavyotumia kukandamiza upinzani kwa kujihusisha kwenye siasa, nchi ingeweza kupiga hatua kubwa.

Alitaka watendaji wake kwenda kujifunza majukumu yao nje ya nchi badala ya kuendelea kujihusisha na siasa kama wanavyofanya sasa.Mchungaji Msigwa alisema nchi inakabiliwa na maadui ndani na nje hivyo ni vema idara ikajikita katika kuwashughulikia hao kuliko kujiingiza zaidi kwenye siasa na kugeuka idara ya usalama ya CCM.


Takukuru na rushwa
Akizungumzia Takukuru na mapambano dhidi ya rushwa kubwa, Mchungaji Msigwa alimtaka Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Dk Edward Hoseah, kuendeleza mapambano na kama wakubwa wakimwekea kiwingu katika utendaji wake, bora aachie ngazi.

Msigwa alifafanua kwamba, hata katika nchi za Kenya na Uganda, wakuu wa taasisi za kupambana na rushwa walipoona mambo ni magumu kutokana na wakubwa kuwadhibiti, waliamua kuachia nyadhifa zao.

Mnyika naye ashambulia usalama
Mbunge wa Ubungo John Mnyika, naye alitumia mjadala huo kuipa somo TISS akiitaka iachane na siasa za kukandamiza upinzani bali ijikite katika kulinda maslahi ya taifa.

Katibu huyo wa wabunge wote wa Chadema bungeni, alisema kazi kubwa za idara hiyo isiwe kujiingiza kwenye siasa kwa kukandamiza upinzani bali kuangalia mustakabali mzuri wa nchi.

Mnyaa: Idara imejikita Bara
Mbunge wa Mkanyageni (CUF), Habib Mnyaa, alisema awali Usalama wa Taifa ulikuwa ukijitegemea kwa upande wa Zanzibar na iliyokuwa Tanganyika ambayo kwa sasa inaitambulika kwa mwavuli wa Tanzania Bara.

Hata hivyo, alisema baada ya idara hiyo kuunganishwa miaka ya 1980, idara hiyo inaonekana kujikita zaidi Bara huku Zanzibar ikikosa hata ofisi kubwa ya maana kwa ajili ya operesheni.

Maji Marefu aikingia kifua
Hata hivyo, mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM), Stephen Ngonyani maarufu kama Profesa Majimarefu, alipinga hoja za wabunge wenzake hao, akisema hawaitendei haki kwani imekuwa ikifanya kazi kubwa kulinda usalama wa taifa.

Kwa mujibu wa Ngonyani, wakosoaji hao wa TISS wanapaswa kuwa mashuhuda kwa kwenda nchi jirani na nyingine za Afrika, ambako usalama wa taifa ni mbaya, huku zikikabiliwa na vitisho vikubwa vya mauaji na vurugu.

Akisisitiza alitoa mfano wa nchi moja (hakuitaja) ambako aliwahi kuingizwa ndani kulala wakati wa mchana kutokana na hali mbaya ya usalama katika taifa na kusisisiza, "ninyi mnaoisema Idara ya Usalama wa Taifa hebu acheni kauli zenu hizo."

"Nendeni nchi jirani au kwingine mkaangalie, mimi niliwahi kuingizwa ndani mchana kwenda kulala kutokana na hali mbaya ya usalama. Hapa kwetu Idara inafanya kazi kubwa, nchi imetulia," alizidi kuikingia kifua na kuwararua wakosoaji.

Katika kuonyesha jinsi idara hiyo inavyofanya kazi kwa ufanisi, Ngonyani alitaka Serikali kuongezea mishahara watumishi wa TISS na kuongeza, "hawa vijana tunashinda nao hapa hadi saa 4:00 usiku wanaangalia usalama halafu tunawasema hawafanyi kazi!"

"Tena nasema waongezewe mishara, vijana wanafanya kazi nzuri na kubwa ya kulinda nchi. Tunapaswa kuwapa nguvu siyo kuwalaumu siyo sahihi hata kidogo," alisisitiza Ngonyani.

Katika miaka ya karibuni hasa baada ya kuongezeka vuguvugu la vyama vingi vya siasa, TISS imekuwa ikikokosolewa na baadhi ya watu kutokana na kuacha baadhi ya misingi yake ya kulinda maslahi ya taifa ikiwamo uchumi, kama ilivyokuwa ikifanya wakati wa Awamu ya Kwanza chini ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Mwaka jana baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu, idara hiyo pia ilijikuta katika tuhuma za kile kilichoelezwa na Chadema kwamba, ilitumikia kuchakachua matokeo ya kura za urais, hali iliyomlazimu Naibu Mkirugenzi Mkuu Jack Zoka, kujitokeza hadharani na kufanya mkutano na waandishi wa habari kuondoa hali tete na giza lililokuwa limegubika nchi. Zoka alikanusha tuhuma hizo kwamba Idara ilihusika katika kuchakachukua matokeo ya urais.

CHANZO: Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.