17 Sept 2016

Nianze makala hii kwa kurejea salamu zangu za rambirambi kwa wafiwa na pole kwa majeruhi wa janga la tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba. 

Kadhalika, ningependa kuchukua fursa hii kuwapongeza wote waliojitokeza kuchangia kwa hali na mali kwa wahanga wa tukio hilo. Kipimo cha utu wetu ni katika nyakati ngumu kama hizi.

Pengine kabla ya kuingia kiundani zaidi katika mada ninayotaka kuongelea, nitoe mfano mmoja unaonihusu. Julai 8 mwaka jana, nilifiwa na baba yangu Mzee Philemon Chahali. Japo miaka saba kabla, yaani mwaka 2008, nilimpoteza mama yangu pia, lakini kuondokewa na mtu wa karibu, hususan mzazi, ni moja ya matukio magumu mno kukabiliana nayo maishani. Sikia tu watu wakilia kwa kufiwa na wazazi au ndugu wengine wa karibu, lakini in reality ni kitu kigumu mno 'kudili' nacho.

Sasa, katika mila zetu za Kiafrika, kipimo kikuu cha urafiki ni jinsi wenzetu wanavyoguswa na matukio makubwa maishani mwetu, pengine zaidi kwa yale ya majonzi kuliko ya furaha. Tunatarajia zaidi wenzetu kuwa karibu nasi kwenye misiba pengine kuliko kwenye harusi, birthday party au mahafali.

Wanasema "nikwepe kwenye sherehe yangu lakini usikose kuwepo kwenye msiba unaonihusu." Ni kwamba wakati wa furaha, hatuhitaji mtu wa kutuliwaza. Ni furaha, twafurahi wenyewe hata pale wenzetu wa karibu wasipokuwepo.Lakini kwenye majonzi twahitaji mno watu wa kutuliwaza. 

Kufupisha stori, nilipopatwa na msiba wa baba yangu mwaka jana nilikuwa nina-follow takriban watu 500 kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Japo haimaanishi kuwa mtu ambaye sim-'follow back' sio muhimu kwangu (nina-interact zaidi na watu ambao siwa-follow kuliko hao ninaowa-follow), hao takriban 500 niliokuwa ninawa-follow walikuwa na ukaribu wa aina flani nami.

Naam, katika dunia yetu ya sasa ambapo ni vigumu kuchora mstari unaotenganisha maisha yetu mtandaoni na maisha yetu halisi, kum-follow mtu ni sawa na kuanzisha nae urafiki. Na ni kwa mantiki hiyo, tunapowa-follow watu tunakuwa na matarajio flani kutoka kwao kama ilivyo kwa watu tunaofahamiana nao katika maisha yetu halisi nje ya mtandao.

Nifupishe stori, baada ya wiki kama mbili hivi za maombolezo ya kifo cha baba nilirejea mtandaoni, na kitu cha kwanza kilikuwa kupitia lundo la salamu za rambirambi kwa msiba huo. Na kwa hakika zilikuwa nyingi mno. Hata hivyo, baadhi ya watu niliokuwa ninawa-follow "walinikwepa." Na haikunichukua muda kuwa-unfollow kwa kigezo chepesi tu cha "nini thamani ya urafiki wetu kama mmeshindwa japo kunipa pole ya msiba?" Nika-unfollow takriban watu 400 kwa mkupuo.

Kama kum-unfollow mtu kwa vile "kakuangusha" ni jambo la busara au upuuzi, nadhani inategemea zaidi na jinsi mtu anavyothamini mahusiano, yawe ya mtandaoni au katika maisha yetu halisi.  

Lengo la makala hii sio kuelezea kuhusu tukio hilo linalonihusu bali nimelitumia tu kujenga msingi wa mada ninayoizungumzia leo, ambayo ni kile kinachoelezwa kama "ukimya wa Rais Dokta John Magufuli kuhusiana na tetemeko la ardhi huko Bukoba."

Katika makala yangu kwenye toleo la wiki hii la gazeti la Raia Mwema nimeongelea, pamoja na mambo mengine, uamuzi wa Rais Magufuli kuahirisha safari ya kwenda Zambia kuhudhuria kuapishwa kwa Rais Edgar Lungu. Japo niliwakosoa wasaidizi wa Rais kwa kutoa taarifa ya safari hiyo (kabla ya kutoa taarifa nyingine kuwa imeahirishwa na badala yake Rais angewakilishwa na Makamu wake) huku wakielewa bayana kuwa 'Rais angeonekana kituko' laiti angesafiri huku taifa likiwa kwenye maombolezo, nilipongeza uamuzi huo wa kuahirisha safari hiyo kwa mantiki ya kile  Waingereza wanasema 'the end justifies the means,' kwamba haikujalisha kama awali wasaidizi wa Rais 'walilikoroga,' cha muhimu ni kuwa Rais alionyesha kujali wananchi anaotuongoza, kwa kuahirisha safari hiyo.

Hata hivyo, kama ambavyo baada ya matanga ya msiba wa baba mwaka jana nilikerwa na ukimya wa 'baadhi ya watu niliokuwa ninawa-follow Twitter,' ndivyo ambavyo baadhi ya Watanzania wameanza kuguswa na kile wanachotafsiri kama ukimya wa Rais Magufuli kuhusiana na janga la tetemeko la ardhi huko Bukoba. 

Naomba sana nieleweke vizuri katika maelezo haya ya mfano hayamaanishi kwa namna yoyote ile kulinganisha msiba wa baba yangu na janga kubwa la kitaifa lililotokana na tetemeko la ardhi huko Bukoba. Na wala siwalingishi waliokuwa followers wangu huko Twitter na wananchi wanaohoji kuhusu 'ukimya wa Rais Magufuli.' Nimetumia 'case yangu' kwa minajili ya mfano tu.

Katika kumtendea haki Rais Magufuli, ukweli ni kwamba hajakuwa kimya 'kihivyo.' Mara baada ya kupata taarifa ya janga hilo, Rais alitoa salamu zake za rambirambi kama inavyoonekana pichani chini



Lakini binafsi ninawaelewa vema wanaohoji 'ukimya' wa Rais wetu kuhusu janga hilo. Kwamba Dkt Magufuli sio tu ni Rais wetu bali pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, na pengine anatarajiwa kusikika kwa 'maneno ya mdomo' (na sio tamko tu la maandishi) akizungumzia suala hilo. Na pengine wanaohoji 'ukimya' wake walitarajia angekwenda eneo la tukio (hasa ikizingatiwa kuwa yeye ni 'mwenyeji' wa maeneo yaliyokumbwa na janga hilo). Hata hivyo, binafsi ninaamini kuwa Rais atazuru huko hivi karibuni tu.

Kadhalika, kwa vile Rais ndiye mkuu halisi wa serikali, taasisi yenye jukumu la usalama wa wananchi, basi huenda wanaohoji 'ukimya wake' wanatarajia yeye kuongoza jitihada za serikali kuwapatia confidence wahanga wa tetemeko hilo.

Na vilevile, licha ya ukweli kwamba kuna kundi flani ambalo limejiapiza kumkosoa Dokta Magufuli kwa kila atakalofanya, wanaohoji 'ukimya' wake sio tu wanaruhusiwa na Katiba kufanya hivyo bali pia wanaweza kuwa wanamsaidia Rais wetu ili kuepusha lawama za mapungufu ya kiuongozi wakati wa majanga.

Nihitimishe makala hii kwa kushauri kuwa pengine itakuwa vema iwapo Rais atafanya ziara huko Bukoba mapema zaidi au hata kuongea na taifa kwa njia ya hotuba, sio kwa minajili ya kuwajibu wanaohoji ukimya wake bali kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake kama 'baba' wa taifa letu katika nyakati kama hizi.

Naomba pia kutoa angalizo hususan kwa makada wanaoweza kujaribu kupotosha lengo la makala hii kuwa ni kumlaumu Rais (japo sio kosa kikatiba kufanya hivyo) au kumfundisha kazi (pia sio uhaini wala jinai kumshauri Rais). Dokta Magufuli ametuomba mara kadhaa kuwa tumsaidie, na moja ya njia za kumsaidia ni kumfikishia ujumbe kama huu (nimesikia watu wakihoji kuhusu 'ukimya' wake kuhusu tetemeko la Bukoba nami namjulisha kuhusu hilo). Kama tunampenda kweli Rais wetu basi na tusiwe wagumu  kumshauri au hata kumkosoa pale inapostahili.

UPDATE: Apparently, wanaohoji 'ukimya' wa Rais kuhusu tetemeko la ardhi huko Bukoba wamepata 'hoja mpya,' kwamba walitarajia asubuhi hii angeungana na wakazi wa jiji la Dar es Salaam kwenye matembezi ya hiari ya kuchangia wahanga wa tetemeko hilo, lakini badala yake mgeni rasmi amekuwa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi. 

Binafsi nadhani sio vema kulaumu bila kujua sababu. Na ukiniuliza kwanini Rais Magufuli hakushiriki matembezi hayo, jibu langu la haraka haraka laweza kuwa 'sababu za kiusalama.' Hilo ni kwa sie 'tunaoelewa,' lakini si kila mtu anaweza kuelewa hivyo, na hatuwezi kuwalaumu wakohoji.

15 Sept 2016


NIANZE makala hii kwa kutoa salamu za rambirambi na pole kutokana na vifo vilivyosababishwa na tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba. Hadi wakati ninaandika makala hii jumla ya watu 16 walikuwa wamepoteza maisha huku wengine zaidi ya 200 wakiwa wamejeruhiwa.
Jinsi janga hilo lilivyochukuliwa kwa kiasi kikubwa ‘kama tukio la kawaida’ huku baadhi ya wenzetu wakiendelea na tamasha la muziki wakati tunapaswa kuwa katika maombolezo ya kitaifa, imenifanya nijikute katika tafakuri kuhusu uhusiano kati yetu na nchi yetu.
Ukiacha ‘mbwembwe’ za hapa na pale, huku nyingi zikiwa za kinafiki, Watanzania wengi wanaielezea vibaya nchi yao. Si jambo la kushangaza kusikia mtu akidai ni bora kuzaliwa paka Ulaya kuliko kuzaliwa binadamu Tanzania. Kadhalika, siku hizi imezoeleka kusikia baadhi ya wenzetu wakidai bora nchi yetu ilipokuwa chini ya utawala wa mkoloni kuliko hali ilivyo sasa.
Na kwa akina sisi tulio nje ya nchi tukijaribu kuchangia japo kwa mawazo tu kuhusu mustakabali wa tafa letu, tunaishia kuambiwa tunajipendekeza…tunataka ukuu wa wilaya na vitu vya kukatisha tamaa kama hivyo.
Tofauti za kiitikadi zimechangia kuimarisha ‘chuki dhidi ya Tanzania,’ ambapo kwa upande mmoja, wengi wa wafuasi wa chama tawala CCM wamekuwa wakijaribu kujenga picha kuwa wafuasi wa vyama vya upinzani ‘sio Watanzania kamili,’ huku kwa upande mwingine, wafuasi wengi wa vyama vya upinzani wakijaribu kujenga picha ya Tanzania kama nchi mbaya kabisa duniani kutokana na utawala wa CCM.
Kuna kitu kinafahamika kama ‘national psyche’ au saikolojia ya taifa – kwa maana nyepesi, sisi kama Watanzania tunajionaje? Na sisi kama Watanzania tunalichukuliaje taifa letu?  Tukiweka kando ‘mabaya’ kama rushwa, ufisadi na umasikini wetu, je kuna lolote tunalojivunia kuhusu nchi yetu? Tunapoona yanayojiri nchi kama Burundi, Somalia na Sudan ya Kusini, tunatambua thamani ya tulichonacho ambacho baadhi ya wenzetu hawana?
Hii saikolojia ya taifa inaweza kuwa muhimu sana katika kuelezea kwanini uzalendo umekuwa ukiporomoka kwa kasi. Tunapowaona wenzetu wamejipaka rangi za bendera za nchi zao katika mechi za kimataifa au matukio muhimu yanayohusu mataifa yao sio suala la ushabiki tu bali mapenzi waliyonayo kwa nchi zao.
Kwa hapa Uingereza bendera yao ya ‘Union Jack’ inagusa na kuvuta hisia kali kwa Waingereza wengi kama ilivyo bendera ya Marekani, ‘Stars and Stripes.’ Lakini sio bendera tu, hata alama za kitaifa kama vile sanamu ya Kristo Mkombozi (Christ the Redeemer), jijini Rio, Brazil; Mnara wa Eiffel, Paris, Ufaransa; Mapiramidi ya Giza, Misri; Ukuta Mkuu wa China, Mnara wa Uhuru (Statue of Liberty), New York, Marekani, na ‘Jicho la London’ (London Eye) na Big Ben, jijini London, hapa Uingereza.
Sisi licha ya vivutio lukuki tulivyonavyo, mpaka leo ‘tunasuasua’ kuwa na utambulisho wa taifa letu. Kama ni Mlima Kilimanjaro, basi huo unafahamika zaidi kuwa upo Kenya kuliko Tanzania, na kama ni madini ya Tanzanite ambayo yanapatikana nchi kwetu pekee, ni India na Kenya ndizo zinazoongoza kwa mauzo ya madini hayo. Mchakato wa kusaka vazi la taifa umejifia kifo cha asili. Hii inatosha kueleza sie ni watu wa aina gani.
Lakini kinachokera zaidi ni kuona taifa limekumbwa na janga la tetemeko la ardhi lililotokea Jumamosi iliyopita huko Bukoba, na kusababisha vifo 16 na majeruhi zaidi ya 200 (hadi wakati ninaandika makala hii) lakini tukio hilo linaonekana kuwagusa zaidi watu walio nje ya Tanzania kuliko sisi Watanzania wenyewe.
Hivi inaingia akilini kweli kuona tamasha la burudani la Fiesta likifanyika Jumapili huko Singida katika kipindi cha majonzi ambapo Watanzania walikuwa wakiendelea kupata habari za kusikitisha (zaidi kupitia vyombo vya habari vya kimataifa) za kuongezeka idadi ya vifo na majeruhi? Katika hili lawama zinapaswa kwenda kwa waandaaji wa tamasha hilo, wasanii walioshiriki na wahudhuriaji. Hawa wote ni Watanzania na walipaswa ‘kuwa na mshipa wa aibu’ kuwafahamisha kuwa maombolezo ni muhimu zaidi ya burudani
Jumapili hiyo tena kulijitokeza mkanganyiko ambapo awali taarifa iliyotolewa na Ikulu ilieleza kuwa Rais Dk John Magufuli angesafiri kwenda Zambia kwenye sherehe ya kuapishwa Rais mteule wa nchi hiyo Edgard Lungu. Hivi kweli kabla ya kutolewa taarifa hiyo, wahusika walikuwa hawafahamu kuhusu kilichojiri huko Bukoba kiasi cha ‘kuamini’ kuwa Rais angeweza tu kusafiri?
Japo baadaye iliripotiwa kuwa Rais hatosafiri na badala yake atawakilishwa na Makamu wa Rais Samia Suluhu, baadhi yetu tulibaki na ‘sintofahamu’ kuhusu kilichopelekea mkanganyiko huo.
Hadi wakati ninaandika makala hii, mtandao wa kijamii wa Jamii Forums, blogu kadhaa za Tanzania na vyombo vya habari vya kimataifa ndio vimekuwa vikitoa ripoti za takriban kila saa kuhusu tukio hilo, ilhali vyombo vingi vya habari ‘vikiburudika na mapumziko ya mwisho wa wiki.’
Kitaifa, hakuna tamko la maombolezo ya kitaifa wala bendera kupepea nusu mlingoti. Tumezowea sana majanga, kama vile ajali mfululizo zinazogharimu maisha ya Watanzania lukuki, kiasi kwamba hatujali ‘kihivyo’ kilichotokea huko Bukoba?
Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa Rais Magufuli kuangalia uwezekano wa kufanyika mjadala wa kitaifa kuhusu uhusiano wetu na Tanzania yetu, kushuka kwa kasi kwa uzalendo, na saikolojia ya taifa letu kwa ujumla. Kadhalika, ninamwomba Mungu awapumzishe mahali pema peponi Watanzania wenzetu waliouawa na tetemeko hilo la ardhi, sambamba na kumwomba awajalie ustahimilivu wafiwa, na uponyaji wa haraka kwa majeruhi wa janga hilo la kitaifa.
Baruapepe: [email protected] Blogu:www.chahali.com Twitter: @chahali  

11 Sept 2016

Tanzania yetu ipo katika msiba mkubwa (hata kama dalili za msiba hazionekane) kufuatia tetemeko la ardhi lililotokea jana alasiri kwenye eneo la ukanda wa Ziwa Viktoria, ambapo kwa mujibu wa taarifa, tetemeko hilo limepeleka vifo 13 hadi sasa na majeruhi takriban 200.



Tetemeko hilo la ardhi lilikuwa na ukubwa (magnitude) wa kati ya 5.7 na 5.9 (taarifa bado zinakanganya) lilitikisa pia baadhi ya maeneo yanayozunguka Ziwa Victoria nchini Uganda na pia baadhi ya maeneo nchini Rwanda na kidogo nchini Kenya.

Picha ziliowekwa kwenye mitandao ya kijamii zimeonyesha uharibifu mkubwa katika mji wa Bukoba wenye wakazi takriban 70,000, sambamba na vifo na majeruhi.

"Tukio hili limesababisha maafa makubwa... kwa sasa hali imetulia..." alisema Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Deodatus Kinawila. "

Vipimo vya Idara ya Jiologia ya Marekani vinaonyesha kuwa tetemeko hilo la ardhi la kina cha kilomita 10 lilitokea saa 9.27 alasiri kwa saa za Afrika Mashariki.
Map showing Tanzania and Bukoba, where earthquake hit in September 2016
Bonde la Ufa la Afrika Mashariki linapita katika 'mstari wenye kasoro kijiolojia' (geologocal fault line), moja ya vyanzo vya matetemeko ya radhi duniani, lakini matukio ya matetemeko ya ardhi yamekuwa ni ya nadra.
Julai mwaka 2007, tetemeko la ardhi la 'magnitude' sita lilitokea Arusha, mkoa uliopo mashariki mwa Bukoba.

Kijiolojia, Bonde la Ufa la Afrika Mashariki linapita katika eneo kulikotokea tetemeko hilo la ardhi. Kwa kifupi, chanzo cha tetemeko hilo ni kutokana na tabaka la miamba katika eneo husika kuwa fukuto jingi la joto na kusigana kwa miamba, hali ambayo hupelekea miamba kukatika, na hiyo hupelekea ardhi itikisike.

Kwa maelezo ya kina kuhusu chanzo cha matetemeko ya ardhi, BONYEZA HAPA 

MIMI BINAFSI NINATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA FAMILIA ZA MAREHEMU 13 WALIOFARIKI KUTOKANA NA TETEMEKO HILO, NA POLE KWA MAREJURHI TAKRIBAN 200. POLENI SANA WAFIWA NA NINAWAOMBEA MAJERUHI UPONYAJI WA HARAKA.





1 Sept 2016

WIKI iliyopita, Rais Dk. John Magufuli alimteua Dk. Modestus Kipilimba kuwa Mkurugenzi Mkuu (DGIS) wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS). Uteuzi huo umefanyika baada ya kustaafu kwa mkurugenzi mkuu aliyemaliza muda wake, Othman Rashid.
Kwa mtizamo wangu, kama kuna kitu ambacho kinaweza kuzua maswali kuhusu uteuzi huo basi ni wadhifa wa Mkurugenzi wa Majanga (Director of Risk Management) alioshikilia Dk. Kipilimba akiwa mtumishi wa Benki Kuu ya Tanzania.
Tunafahamu Benki Kuu imekuwa ikiandamwa na matukio mfululizo ya ufisadi, kuanzia EPA hadi Tegeta Escrow. Kwa wadhifa wake katika taasisi hiyo, kuna uwezekano wa bosi huyo mpya wa mashushushu kuonekana sehemu ya mfumo ulioshindwa kudhibiti ufisadi. Hata hivyo, utetezi unaweza kuwa huenda yeye alitekeleza majukumu yake vema lakini walio juu yake hawakuchukua hatua stahili.
Changamoto kubwa kwa Dk. Kipilimba ni pamoja na kurejesha hadhi na heshima ya Idara ya Usalama wa Taifa. Wanaoilaumu taasisi hiyo hawamaanishi kuwa watumishi wake wanahusika katika baadhi ya matukio ya kihalifu bali kushindwa kwa Idara hiyo kukabiliana na kushamiri kwa matendo hayo ya kihalifu, ambayo kimsingi ni matishio kwa usalama wa taifa, na kazi kuu ya Idara hiyo ni kukabiliana na matishio kwa usalama wa taifa la Tanzania.
Ninaamini kuwa Dk. Kipilimba anafahamu kanuni muhimu kuhusu ufanisi au upungufu wa idara ya usalama wa taifa popote pale duniani, kwamba kushamiri kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa lolote lile ni kiashiria cha upungufu katika idara ya usalama wa taifa ya nchi husika na kudhibitiwa kwa vitendo vinavyotishia usalama wa taifa popote pale duniani ni kiashiria cha uimara wa idara ya usalama wa taifa ya nchi husika.
Kwahiyo, kwa kuzingatia kanuni hiyo, kushamiri kwa biashara ya dawa ya kulevya, ujangili, rushwa na ufisadi mwingine ni viashiria vya kasoro ya Idara yetu ya Usalama wa Taifa.
Changamoto nyingine kwa Dk. Kipilimba ni tuhuma za mara kwa mara dhidi taasisi hiyo muhimu kabisa kuwa katika utendaji kazi wake imegeuka kuwa kama kitengo cha usalama cha chama tawala CCM. Idara hiyo imekuwa ikituhumiwa kuwa kwa kiasi kikubwa imeweka kando taaluma ya ushushushu (tradecraft) na kutekeleza majukumu yake kisiasa.
Madhara ya muda mfupi ya kasoro hiyo ni taasisi hiyo kujenga uhasama na vyama vya upinzani na kwa namna fulani kupoteza heshima na uhalali wake. Lakini la kuogofya zaidi ni madhara ya muda mrefu, ambapo watu wanaoweza kuwa ni matishio kwa usalama wa taifa letu wanaweza kutumia ‘urafiki’ unaodaiwa kuwepo kati ya Idara ya Usalama wa Taifa na CCM, wakitambua bayana kuwa Idara haina muda na makada wa chama tawala na hatimaye kufanikiwa kutimiza azma zao ovu.
Baadhi ya watumishi wa zamani wa taasisi hiyo walijikuta matatizoni kwa vile tu walitekeleza majukumu yao dhidi ya wanasiasa wa chama tawala na wakaishia kuonekana kama wahaini.
Changamoto nyingine kwa Dk. Kipilimba ni tuhuma zinazoikabili taasisi hiyo kuhusu mfumo wa ajira ambapo inadaiwa kuwa zimekuwa zikitolewa kwa upendeleo kwa ndugu na jamaa za vigogo. Tatizo kubwa hapa ni kwamba utiifu wa ndugu na jamaa hao wa vigogo haupo kwa taifa bali kwa vigogo hao waliowaingiza Idarani. Pengine sio vibaya kufikiria ‘utaratibu wa wazi’ katika ‘recruitment’ kama inavyofanywa na wenzetu wa CIA, NSA, MI5, MI6 au HGCQ wanaotangaza nafasi za ajira kwenye vyombo vya habari.
Pia kuna tatizo la baadhi ya maofisa usalama wa taifa ‘kujiumbua’ kwa makusudi kwa sababu wanazojua wao wenyewe, kubwa ikiwa kutaka sifa tu, au waogopwe mtaani. Hii inaathiri sana ufanisi wa maafisa wa aina hiyo kwani ni vigumu kutekeleza majukumu yao ipasavyo pasi usiri.
Sambamba na hilo ni kasumba ya muda mrefu ambapo baadhi ya maafisa wa Idara hiyo waliopo kwenye vitengo mbalimbali kuwepo huko kwa muda mrefu mno kiasi cha kuathiri utendaji wao.
Changamoto nyingine kubwa ni uwepo wa majasusi kibao nchini mwetu, hususan kutoka nchi moja jirani, huku wengi wa majasusi hao wakiwa wameajiriwa katika taasisi za umma na binafsi. Hili ni tishio kubwa kwa usalama wa taifa letu. Licha ya hilo, kiintelijensia, kila ‘nchi rafiki’ ni ‘adui yetu’ muda huu tulionao au siku zijazo.
Kwa upande wa fursa kwa Dk. Kipilimba, licha ya kuwa ‘mwenyeji’ katika taasisi hiyo muhimu, wasifu wake kitaaluma unamweka katika nafasi nzuri sana kukabiliana na changamoto za karne ya 21 ambayo imetawaliwa zaidi na teknolojia ya kisasa.
Dk. Kipilimba ni msomi aliyebobea kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) na yayumkinika kuamini kuwa anaweza kutumia usomi wake kuibadilisha Idara ya Usalama wa Taifa kwenda na wakati, kufanya kazi kama taasisi ya kishushushu ya karne ya 21.
Fursa nyingine kwa Dk. Kipilimba ni matarajio ya kuungwa mkono vya kutosha kutoka kwa Rais Magufuli ambaye kama alivyoahidi wakati wa kampeni za kuwania urais, mapambano dhidi ya ufisadi yamepewa kipaumbele cha hali ya juu kabisa.
Sambamba na hilo ni Idara hiyo kuangalia uwezekano wa kutumia hazina kubwa tu ya maafisa wake wa zamani, hususan wastaafu. Ikumbukwe kuwa wengi wao ni watu wanaowindwa na makundi au taasisi mbalimbali zinazolenga kulihujumu taifa letu.
Nimalizie makala hii kwa kutoa pongezi za dhati kwa Dk. Kipilimba na Naibu wake (DDGIS) Robert Msalika, sambamba na kumtakia mapumziko mema Mkurugenzi mstaafu Othman na kumkaribisha uraiani.
Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.