14 Oct 2016


HISTORIA FUPI YA MWALIMU NYERERE
MPAKA MAUTI YALIPOMFIKA

Tarehe ya kuzaliwa 13 Aprili 1922
Mahali pa kuzaliwa Butiama
Tarehe ya kifo 14 Oktoba 1999
Rais wa Tanzania
Alingia ofisini 1964
Aliondoka ofisini 1985
Alitanguliwa na (alikuwa rais wa kwanza)
Alifuatwa na Ali Hassan Mwinyi
Dini Mkristo Mkatoliki
Elimu yake Chuo Kikuu cha Edinburgh - Uskoti Digrii
anazoshika M.A. ya historia na uchumi
Kazi mwalimu, mwanasiasa Mengine Nyerere alikuwa
mwenyekiti wa chama cha TANU na baadaye wa CCM.
Mara nyingi aliitwa "Mwalimu Nyerere".
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa rais wa
kwanza wa Tanzania. Alizaliwa Butiama, mkoani Mara
pembezoni mwa Ziwa Nyanza tarehe 13 Aprili, 1922.
Alifariki dunia 14 Oktoba, 1999. Aliiongoza Tanzania toka
mwaka 1961 hadi mwaka 1985.
Yeye ni mwasisi wa itikadi ya ujamaa na kujitegemea.
Kabla ya kuingia kwenye siasa alikuwa ni mwalimu. Kazi
hii ndiyo ilimpatia jina ambalo lilimkaa maisha yake yote la
"Mwalimu." Mwalimu Nyerere ni kati ya viongozi wachache
wa Afrika ambao wameacha madaraka kwa hiyari baada
ya kutawala kwa muda mrefu. Alipostaafu urais mwaka
1985 alirudi kijijini kwake Butiama ambako aliendesha
shughuli za kilimo. Aliendelea kuwa na athari kubwa
katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.
Maisha Ya Mwalimu
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alizaliwa mwaka 1922
( katika kijiji cha Butiama, wilaya ya Musoma, mkoa wa
Mara, Tanzania (wakati ule: Tanganyika). Alikuwa
mojawapo kati watoto 26 wa Nyerere Burito, chifu wa
kabila la Wazanaki. Alipokuwa mtoto Nyerere alichunga
mifugo ya babake; katika umri wa miaka 12 aliingia shule
akitembea kilomita 30 hadi Musoma. Baada ya kumaliza
shule ya msingi aliendelea kusoma shule ya wamisionari
Wakatoliki huko Tabora. Katika umri wa miaka 20
alibatizwa akawa mkristo Mkatoliki hadi mwisho wa
maisha yake.
Mapadre wakaona akili yake wakamsaidia kusoma ualimu
huko Makerere, Kampala, Uganda kuanzia 1943 - 1945.
Makerere akaanzisha tawi la Umoja wa wanafunzi
Watanganyika pia amejihusisha na tawi la Tanganyika
African Association (TAA). Baada ya kumaliza masomo ya
ualimu alirudi Tabora akifundisha shule ya St.Mary´s.
Mwaka 1949 alipata skolashipu ya kwenda kusoma
kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh huko Uskoti /Uingereza
akasoma M.A. ya historia na uchumi(alikuwa mtanzania
wa kwanza kusoma katika chuo kikuu cha Uingereza na
mtanzania wa pili kupata shahada ya elimu ya juu nje ya
Tanzania).
Aliporejea Tanganyika kutoka masomoni, Nyerere
alifundisha Historia, Kingereza na Kiswahili katika shule ya
St. Francis iliyo karibu na Dar es Salaam. Mwaka 1953
alichaguliwa kuwa raisi wa chama cha Tanganyika African
Association (TAA), chama ambacho alikisaidia kukijenga
alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Makerere.
Mwaka 1954 alikibadilisha chama cha TAA kwenda katika
chama cha Tanganyika African National Union (TANU)
ambacho kilikuwa cha kisiasa zaidi kuliko TAA. Ndani ya
mwaka mmoja chama cha TANU kilikuwa tayari chama cha
siasa kinachoongoza Tanganyika.
Uwezo wa mwl. Nyerere uliwashitua uongozi wa kikoloni
na kumlazimisha Nyerere kuchagua kati ya siasa na kazi
ya ualimu. Nyerere alisikika akisema kuwa alikuwa
mwalimu kwa kuchagua na mwanasiasa kwa bahati
mbaya. Alijiuzuru ualimu na kuzunguka nchini Tanganyika
kuzungumza na watu wa kawaida na machifu ili kuleta
muungano katika mapigano ya uhuru. Pia alizungumza
kwa niaba ya TANU katika Trusteeship council na Fourth
committee ya Umoja wa Mataifa (UN) huko New York.
Uwezo wake wa kimaongezi na kuunganisha watu
ulimwezesha kufanikisha Tanganyika kupata uhuru bila
umwagaji wa damu. Ushirikiano mzuri aliouonyesha
aliyekuwa gavana wa wakati huo bwana Richard Turnbull
ulisaidia pia kuharakisha upatikanaji wa uhuru. Nyerere
aliingia katika bunge la kikoloni mwaka 1958 na
kuchaguliwa kuwa waziri mkuu mwaka 1960. Mwaka 1961
Tanganyika ilipata uhuru wake na tarehe 9/12/1961
Nyerere alichaguliwa kuwa waziri mkuu wa Tanganyika
huru na mwaka mmoja baadae Nyerere alikuwa raisi wa
kwanza wa jamhuri ya Tanganyika. Nyerere alikuwa kiungo
muhimu katika muungano wa Tanganyika na Zanzibar
kutengeneza Tanzania baada ya mapinduzi ya Zanzibar
mwaka 1964 yaliyomtoa madarakani sultani wa Zanzibar
Jamshid bin Abdullah.
Sifa zake
Bado anakumbukwa na watanzania hasa wa hali ya chini
kutokana na sera zake za kujali utu na ubinadamu.Pia
ataendelea kukumbukwa na waafrika kote barani hasa kwa
mchango wake mkubwa wakati wa harakati za kupigania
uhuru katika nchi mbali mbali barani Afrika.
Ni mmoja wa viongozi wachache wanaokumbukwa kwa
kutojilimbikizia mali pamoja na kutawala kwa miaka zaidi
ya 24.
Mwishoni mwa maisha yake Nyerere aliishi kama mkulima
wa kawaida kijijini kwake Butiama. Alipatwa na kansa ya
damu (leukemia) na kufariki Uingereza wakati wa kutibiwa
katika mji wa London tarehe 14 Oktoba, 1999. Alizikwa
mahali pa kuzaliwa kwake, kijiji cha Butiama.
Machapisho ya mwl.Julius K. Nyerere.
• Freedom and Socialism.Mkusanyiko wa maandiko na
hotuba, 1965-1967 (1968)
• Freedom & Development, Uhuru Na Maendeleo (1974)
• Ujamaa - Essays on Socialism' (1977)
• Crusade for Liberation (1979)

CHANZO: Jamii Forums


13 Oct 2016

NIANZE makala hii kwa kueleza masikitiko yangu kutokana na tukio lililoripotiwa wiki iliyopita ambapo walimu wanafunzi kadhaa walionekana katika video wakimwadhibu mwanafunzi katika namna isiyofaa na isiyokubalika kabisa. Laiti mtu akiiona video husika bila ya maelezo anaweza kudhani mwanafunzi aliyekuwa akipigwa na walimu hao wanafunzi alikuwa mwizi.
Pamoja na kukerwa mno na kitendo hicho, sikushangazwa na suala zima la vurugu (violence) dhidi ya mwanafunzi husika. Sikushangazwa kwa sababu jamii yetu imekuwa ikisherehesha vurugu. Ni mara ngapi tumeshuhudia polisi wetu wakitumia nguvu nyingi zaidi hata pale ambapo busara tu ingetosha? Ni watumishi wa nyumbani wangapi ambapo tulichokishuhudia kwenye video husika ndio maisha yao ya kila siku, kwa maana ya unyanyasaji wanaofanyiwa na waajiri wao na hawana sehemu ya kukimbilia?
Na je, ni watoto wangapi – hususan watoto wa kambo – ambao kila siku ya maisha yao ni zaidi ya unyanyasaji aliofanyiwa mwanafunzi wa kwenye video husika? Je, ni Watanzania wenzetu wangapi ambao ulemavu wao wa ngozi yaani ualbino umekuwa chanzo cha wao kuwindwa, kukatwa viungo na kuuawa? Na wazee wetu wangapi wameuawa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa vile tu wana macho mekundu (imani fyongo kuwa ni dalili ya ushirikina)?
Na kuhusu vurugu shuleni, kama hilo tukio la walimu hao wanafunzi, sheria za nchi zimehalalisha vurugu kwa kuendelea kuruhusu adhabu za kikoloni kama hiyo ya viboko. Tatizo letu ni kuamini zaidi katika adhabu badala ya kukarabati tabia. Angalia magereza zetu zilivyojaa vibaka na wezi wa kuku badala ya kuwapa kifungo cha nje na kuweka mkazo katika kuwageuza kuwa raia wema.
Tukio hilo sio tu liifumbue macho serikali kuhusu umuhimu wa mitandao ya kijamii katika kutuhabarisha yale ambayo pengine vyombo vyetu vya habari vya asili visingeweza kuripoti (na hili ni angalizo kwa Rais Dk John Magufuli kuhusu matamanio yake kuona malaika wakishuka na kuifunga mitandao ya kijamii) bali pia liiamshe kuhusu suala la viboko shuleni. Adhabu ya viboko imepitwa na wakati, ni kandamizi, ni mwendelezo wa vurugu dhidi ya watoto na si ya kistaarabu.
Baada ya kuzungumzia suala hilo la kipigo cha walimu hao kwa mwanafunzi, nigusie mada ya wiki hii ambayo pia inahusu elimu. Mwishoni mwa mwezi uliopita, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipiga marufuku wanafunzi kwenda shuleni pekupeku au na nguo zilizochanika.
Alitoa maagizo hayo katika ziara yake mjini Kibiti, Pwani wakati akizungumza na wananchi wa eneo hilo kwenye mkutano wa hadhara. Waziri Mkuu alisema;  “Zile fedha mlizokuwa mnatumia kulipa ada na michango sasa zitumieni kununua sare na chakula cha watoto wenu, ni marufuku mtoto kwenda shule huku akipekua au akiwa amevaa sare zilizochanika,”
Hivi kweli Majaliwa anadhani wazazi wa watoto wanaokwenda shuleni wakiwa pekupeku au na nguo zilizochanika wanafanya hivyo kama ‘fasheni’ ya suti za waheshimiwa wetu? Hivi kweli Majaliwa hajui kuwa ni umasikini wa kupindukia unaosababisha baadhi ya Watanzania wenzetu kutomudu uwezo wa kuwanunulia watoto wao viatu na sare nzuri?
Moja ya masuala yaliyonikera sana katika miaka 10 ya Awamu ya Nne ni pale viongozi wakuu wa serikali, Rais na Waziri Mkuu wake, wakieleza bayana kuwa hawajui kwa nini Tanzania ni masikini. Lakini angalau wao, licha ya kutoelewa chanzo cha umasikini wetu, hawakuja na amri ya kushangaza kama hiyo ya Majaliwa.
Pamoja na heshima kubwa niliyonayo kwa Waziri Mkuu wetu, ninaomba kutofautiana naye kuhusu amri hiyo. Anachopaswa kufanya ni kutilia mkazo sera zitakazoziwezesha familia masikini sio tu kumudu fedha za kuwanunulia watoto wao sare na viatu, bali angalau kuwa na uhakika wa mlo ujao.
Ni hivi, Waziri Mkuu, kimsingi amri yako ina- criminalise umasikini, kwamba ni kosa kisheria kwa mzazi kuwa masikini kiasi cha kushindwa kumnunulia mwanaye sare bora za shule.
Amri hiyo ya Waziri Mkuu inaonesha jinsi baadhi ya viongozi wetu walivyo mbali na wananchi wanaowaongoza kiasi cha kutoelewa shida wanazokabiliana nazo katika maisha yao.
Nihitimishe makala hii kwa kumsihi Majaliwa atafakari upya kuhusu amri yake hiyo na kwa vile ninaamini anawajali Watanzania wote, wenye kujimudu kimaisha na masikini wasiomudu kununua sare bora za shule kwa watoto wao, atatengua amri hiyo.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

12 Oct 2016

Moja ya kazi ambayo inapendwa na kutamaniwa na watu wengi mno DUNIANI ni Uafisa Usalama wa Taifa, kwa jina jingine USHUSHUSHU.

Kuipenda au kuitamani fani hiyo kunachangiwa na ukweli kwamba, kwa upande mmoja ni eneo ambalo limekuwa maarufu mno kwenye filamu, na kwa hakika watu wengi wanapenda filamu za kishushushu.Ni nani asiyependa filamu za James Bond? Au series kama 24 na Homeland zinazohusu fani ya ushushushu?

Lakini licha ya filamu, kuna lundo la vitabu vya riwaya za kuhusu matukio halisi (non- fiction) au ya kutunga (fiction), na vingi ya vitabu hivyo ni 'vitamu' ukivisoma. Na sote twafahamu kuwa moja ya vitabu vilivyokuwa na bado vina umaarufu mkubwa mno nchini Tanzania ni vya Willy Gamba, shushushu mhusika katika vitabu vya Marehemu Eristablus Musiba.

Binafsi nilitamani kuwa shushushu nilipokuwa mtoto mdogo tu. Marehemu baba alikuwa na tabia ya kutusimulia kuhusu vitabu alivyosoma. Na kitabu cha kwanza hakikuwa cha kishushushu, bali story tu, kilichoandikwa na James Hadley Chase, "Come Easy Go Easy."

Baadaye alitusimulia kuhusu kitabu kimoja na James Bond, japo sikikumbuki jina. Kwa mara ya kwanza ndio nikafahamu kuwa kuwa watu wanaitwa 'ma-spy' na wanafanya kazi hiyo ya ushushushu. Fast forward miaka kadhaa baadaye, nikakutana na vitabu vya Willy Gamba, kuanzia "Njama," "Kikomo," "Kikosi cha Kisasi" na kadhalika.Kwa kweli kusoma vitabu hivyo vilikuwa kama kuangalia filamu. Tangu wakati huo nikatamani kuwa Willy Gamba.

Anyway, japo ushushushu kama tunavyoufahamu ni kwa ajili ya masuala ya usalama wa taifa, mbinu zinazotumiwa na mashushushu kusaka habari zinatumika katika maeneo mengine pia. Eneo linalotumia mbinu zinazoshibihiana zaidi na ushushushu ni uandishi wa habari.

Lakini eneo ambalo linanufaika na mbinu mbalimbali za kishushushu ni maisha yetu ya kila siku. Kwamba kuna mbinu mbalimbali za kishushushu ambazo zinaweza kumsaidia mtu wa kuwaida kufanikisha azma kama vile pale inapotokea mwenza mmoja kuhisi kuwa mwenzio anamsaliti au kupima uaminifu wa mwenza wako, kufahamu yanayoendelea 'behind the scene' katika masuala mbalimbali ya kimaisha,nk.

Je unahisi kuwa girlfirend/ boyfriend wako anaku-cheat? Je wahisi kuwa mumeo/mke 'anachepuka? Je unahisi kuwa binti yenu ameanza 'michezo michafu'? Je unahisi kuwa mtoto wenu wa kiume kaanza kujihusisha na makundi yasiyofaa? Je mshirika wako wa kibiashara ana ajenda ya siri dhidi yako? 

Ili uweze kupata majibu ya uhakika au yanayokaribiana na uhakika inabidi uwe shushushu, sio kwa ajili ya usalama wa taifa bali kwa ajili yako wewe mwenyewe au na mwenza wako au familia yako, nk.

Anza safari ya kujifunza ushushushu kwa kununua kitabu changu kuhusu taaluma ya Uafisa Usalama wa Taifa, kitabu pekee katika historia ya Tanzania, kinachoeleza kwa undani kuhusu taaluma hiyo. Ukifuatilia 'comments' za waliokwishasoma kitabu hicho utabaini kuwa wengi wamejifunza kutumia mbinu za kishushushu katika maisha yao binafsi.

Kwa wakazi wa Dar, unaweza kununua kitabu hicho na kuletewa hadi nyumbani, kazini, sehemu ya biashara, shuleni/chuoni, au hata kijiweni au pub.

Maduka ya vitabu jijini Dar na mikoani yanayouza kitabu hicho ni kama ifuatavyo


KARIBUNI SANA



7 Oct 2016


NIMEKUWA mfuatiliaji mkubwa wa habari na eneo moja ninalolipa umuhimu mkubwa ni habari za teknolojia.
Ufuatiliaji huo wa habari za teknolojia umenifanya niwe na wasiwasi, kwa upande mmoja na matumaini kwa upande mwingine. Wasiwasi wangu mkubwa ni hatma ya Bara la Afrika ambalo kwa kiasi kikubwa linaichukulia teknolojia kama anasa ilhali wenzetu hususan nchi zilizoendelea wanachukulia teknolojia kama sehemu ya mahitaji muhimu kwa binadamu kama ilivyo chakula, makazi na mavazi.
Matumaini yangu katika teknolojia yanatokana na ukweli kwamba licha ya kutelekezwa kwa kiwango kikubwa, matumizi japo kidogo ya teknolojia katika sehemu mbalimbali za dunia inayoendelea, kwa mfano huko nyumbani Tanzania, yanaleta mabadiliko makubwa. Angalia jinsi mfumo wa kusafirisha fedha wa m-pesa unavyofanya kazi, ‘apps’ kama Whatsapp zinavyowezesha watu mbalimbali kuepuka gharama kubwa za simu na ujumbe wa maneno, barua-pepe zinavyotuwezesha kuwasiliana papo kwa papo bila kwenda posta kutuma au kupokea barua na maendeleo mengine mbalimbali.
Nimebahatika kushuhudia zama kabla ya ujio wa intaneti na mitandao ya kijamii, televisheni, simu za mkononi na takriban kila aina ya teknolojia ya kisasa inayoifanya dunia kuwa kama kijiji. Kadhalika, nilikuwa miongoni mwa Watanzania wa awali kukumbatia teknolojia mpya (nilikuwa miongoni mwa Watanzania wa kwanza kabisa kufungua blogu Aprili 2006).
Jumamosi iliyopita niliweza kuangalia mechi ya watani wa jadi, Simba na Yanga, kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook. Hii ilinikumbusha miaka kadhaa huko nyuma ambapo tegemeo pekee la kusikia matangazo ya mpira lilikuwa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) ambayo wakati mwingine iliwalazimu wasikilizaji kupanda juu ya miti ili kudaka vema mawimbi ya radio.
Lakini pengine lililo kubwa zaidi kuhusu teknolojia ni jinsi uchaguzi mkuu wa mwaka jana ulivyoandika historia ya kuwa wa kwanza kabisa ‘kujenga ndoa’ kati ya teknolojia na siasa. Tulishuhudia jinsi mitandao ya kijamii, hususan Facebook na Twitter, ‘apps’ kama Whatsapp na Instagram, na majukwaa ya uchapishaji kama vile blogu na ‘webforums’ (kama Jamii Forums) zilivyotumika kwa ufanisi mkubwa katika kampeni za urais, ubunge na udiwani.
Na kwa hakika, ushindi wa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Rais wa sasa Dk. John Magufuli, ulichangiwa na kampeni zilizofanyika kwenye mitandao ya kijamii, apps na webforums. Kama kuna Rais wa Tanzania anayepaswa kuthamini mno mchango wa teknolojia kwenye siasa basi ni Magufuli.
Hata hivyo, katika mazingira ya kushangaza kabisa, Dk. Magufuli alisikika akieleza kuwa anatamani malaika washuke na kusimamisha mitandao ya kijamii kwa mwaka moja na itaporudi hewani (baada ya mwaka huo mmoja) ishuhudie maendeleo yaliyofikiwa.
Watetezi wa rais wanadai kuwa kauli hiyo ni ya utani tu, lakini nikiwa miongoni mwa watu walioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni Magufuli nikiwa maili kadhaa kutoka huko nyumbani lakini nikawezeshwa kufanya hivyo kwa kutumia maendeleo ya teknolojia kama vile matumizi ya mitandao ya kijamii na blogu, nilisikitishwa na kauli hiyo ya Magufuli.
Ni kweli kwamba baadhi ya wenzetu wamekuwa wakiyatumia vibaya maendeleo ya teknolojia, kwa kujenga chuki miongoni mwa Watanzania, upinzani dhidi ya kila kitu hata chenye manufaa kwa taifa, kugeuza mitandao ya kijamii kuwa uwanja wa matusi, na kadhalika.
Hata hivyo, wanaotumia vibaya teknolojia ni wachache kulinganisha na sisi tunaoitumia kwa nia nzuri. Hivi kama kosa la wachache linafanya wote kuwa wabaya, je itakuwa sahihi kudai kuwa malaika washuke na kuifunga serikali kwa muda fulani kwa vile ilikuwa na watumishi hewa zaidi ya 10,000 na watumishi kadhaa wasio hewa lakini ni majipu?
Na hata kama kuna haja ya kuifunga mitandao hiyo, Dk. Magufuli hahitaji malaika bali sheria dhidi ya makosa ya mitandao ya kijamii (Cyber Crime Act 2015) iliyokwishawatia hatiani watu 10 kwa tuhuma za “kumtukana rais kwenye Facebook au Whatsapp?”
Wito wangu kwa Rais Magufuli ni kwamba awe mstahimilivu. Kazi anayofanya ni nzuri na inawapendeza Watanzania wengi. Sasa kuna haja gani asumbuliwe na hizo kelele za hapa na pale ilhali anayofanya ni makubwa zaidi ya kelele hizo?
Kadhalika, kwa vile tu rais wetu hapendezwi na kitu fulani haimaanishi kitu hicho sio halali kikatiba. Kama ambavyo wengi wetu tunatumia uhuru na haki yetu kikatiba kumpongeza Magufuli, katiba yetu inatoa haki na uhuru pia kwa wenzetu kumkosoa rais wetu alimradi wasitumie lugha isiyokubalika kisheria.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

30 Sept 2016

TANZANIA ina matatizo kadhaa, lakini tatizo ambalo sikuwahi kulitambua awali ni hili linalozidi kupanuka la chuki ya baadhi ya Watanzania wenzetu dhidi ya nchi yetu.
Naam, hakuna neno stahili zaidi ya chuki, pale unapokutana na Mtanzania anafurahi kusikia kuwa majirani zetu wa Malawi wameanza chokochoko kuhusu mpaka kati yetu na nchi hiyo.
Au unakutana na mtu anayefurahia taarifa za kuyumba kwa uchumi wetu, anakenua meno yote 32 huku akidai eti “si mliichagua CCM, mnaisoma namba sasa.”
Lakini kama kuna kitu kimenikera zaidi ni hizi kebehi za watu hao dhidi ya jitihada zilizofanywa na Serikali ya Rais Dk John Magufuli kununua ndege mbili kama mkakati wa kulifufua shirika letu la ndege.
Wenye chuki hao wanaendelea kukosoa kila kitu kuhusu ndege hizo, kuanzia yule twiga kwenye nembo (baadhi wanadai eti huyo twiga anaonekana kama ameteguka miguu), rangi ya ndege na kila kitu kuhusu ndege hizo.
Wanataka serikali ingenunua ndege kubwa zaidi, wengine wanataja kabisa aina ya ndege waliyotaka, wengi wao wakitamani ndege kubwa zinazotengenezwa na kampuni za Boeing au Airbus.
Ni watu hawa hawa ambao laiti serikali ingetumia fedha nyingi zaidi kununua ndege kubwa zaidi wangeishia kuilaumu kuwwa ndege sio muhimu zaidi ya mahitaji mengine mbalimbali muhimu kwa taifa letu.
Jitihada za kuwaelimisha kuwa ndege hizo mbili za aina ya Bombardier zina ufanisi zaidi kwa maana ya bei yake na gharama za uendeshaji zinagonga ukuta kwa sababu watu hawa hawataki kusikia habari yoyote njema kuhusu Tanzania.
Wataalamu wa usafiri wa anga wanaeleza kuwa ndege hizo zilizonunuliwa na serikali zinatumia mafuta kidogo zaidi kulinganisha na ndege nyingine, lakini wenye chuki hao hawataki kabisa kusikia maelezo hayo ya kitaalamu.
Na kwa kuonyesha kuwa watu hawa wana chuki kali dhidi ya nchi yao, hawataki kabisa kuzungumzia habari nyingine njema ya ujio wa mabehewa kwa ajili ya kuboresha huduma za usafiri wa Reli ya Kati.
Hawazungumzii sio kwa sababu hawafahamu kuhusu habari hiyo njema bali wameishiwa na hoja za kuwawezesha kukosoa kuhusu mabehewa hayo.
Sote tunatambua kuwa kwa miaka kadhaa nchi yetu ilikuwa ‘shamba la bibi’ kwa genge la mafisadi. Kuibadili hali hiyo sio kitu cha siku moja. Na Rais Magufuli ameshatukumbusha mara kadhaa kwamba itachukua muda kabla mambo hayajanyooka, akatuomba tumsaidie.
Lakini tatizo la wenzetu hao na chuki yao sio ununuzi wa ndege hizo, zingekuwa kubwa wangelalamika na sasa sio kubwa sana wanalalamika. Tatizo la wenzetu hao ni chuki dhidi ya nchi yetu. Wanatamani sana kuiona nchi ikiwa kwenye wakati mgumu ili wapate fursa ya kutuambia “mnaisoma namba.”
Kibaya zaidi kuhusu wenzetu hawa ni kwamba sasa wamefika mahala kuwa hoja za kuikosoa serikali pale inapostahili ni haki yao pekee. Nilishuhudia hali hiyo ya kuchukiza mwishoni mwa wiki iliyopita, ambapo niliweka bandiko kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook nikieleza upungufu ya Muswada wa Huduma za Habari (Media Services Bill) ambao licha ya kupingwa na wadau wengi, upo katika mchakato wa kuwa sheria kamili.
Badala ya kujadili mada husika, wenye hatimiliki ya kuikosoa serikali ‘wakanikalia kooni’ wakinituhumu kuwa nilimpigia kampeni Dk. Magufuli na sasa baada ya kukosa nilichotarajia ndio najifanya kumkosoa. Kimsingi wala sikumkosoa rais bali serikali kwa ujumla hasa ikizingatiwa kuwa mchakato wa muswada huo ulianza wakati wa Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete.
Na kabla ya hapo, nilitoa pongezi zangu za dhati kwa aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa, kutokana na ziara yake mkoani Kagera kuhusu janga la tetemeko la ardhi. Lakini watu wenye hatimiliki ya kumpongeza Lowassa wakanijia juu wakidai kuwa ni unafiki kumpongeza sasa wakati sikumuunga mkono kipindi cha kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka jana.
Wengi wao wanaishi kama tupo katika kipindi cha kampeni za uchaguzi huo. Kwao ni kama rais halali hajapatikana. Pengine kwa vile walijiaminisha mno kuhusu mgombea wao, basi hawataki kabisa kukubali ukweli ambao upo kinyume cha matarajio yao.
Nihitimishe makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa hatuna nchi nyingine zaidi ya Tanzania na ni wazi tusipoipenda wenyewe, tusitarajie wasio Watanzania kuipenda. Mafanikio ya nchi yetu ni yetu sote na kukwama kwake kunatuathiri sote. Tuweke mbele maslahi ya nchi yetu badala ya maslahi binafsi au ya kiitikadi.
Mungu ibariki Tanzania

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

28 Sept 2016

Pengine umeshasikia taarifa kuwa akaunti zaidi ya milioni 500 za Yahoo zimedukuliwa (hacked). Yawezekana kabisa kuwa akaunti yako ni miongoni mwa hizo milioni 500 (nusu bilioni). Makala hii inakuelekeza hatua za kuchukua.

Kama una muda wa kutosha basi nenda kwenye tovuti HII kisha fuata maelekezo ya kufahamu iwapo akaunti yako ipo salama au la. Ushauri wangu ni kwamba usipoteze muda wako kuhakikisha kama akaunti yako imedukuliwa au la bali nenda moja kwa moja kwenye akaunti yako na kubadili password.

Lakini sio kubadili password ya Yahoo pekee. Yawezekana umejisajili Facebook au Instagram au Twitter kwa kutumia akaunti ya Yahoo. Basi pengine sio vibaya ukabadili passowrds na huko pia, hasa kwa wale wanaotumia passowrd moja kwa akaunti zote.

Pamoja na kubadili password yako ya Yahoo, unaweza kuongeza ngazi moja zaidi ya ulinzi kwa akaunti yako, kwa kutumia kitu kiitwacho two-step verification. Kitu hicho kinalazimisha kuwa kila unapo-log onto akaunti yako basi lazima uthibitishe kuwa wewe ndo mhusika. Maelezo ya jinsi ya kuwezesha two-step verification yapo HAPA

KAMA UTAKWAMA KATIKA HATUA YOYOTE BASI USISITE KUWASILIANA NAMI KWA MSAADA/MAELEKEZO. 





27 Sept 2016

Naomba anayefahamiana na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt Charles Kimei, amfikishie ujumbe huu kwa njia yoyote mwafaka.

Ndugu Dkt Kimei,

Nakuandikia barua hii ya wazi nikiwa na masikitiko makubwa kutokana na huduma zisizoridhisha za benki unayoiongoza. Nimekuwa mteja wa benki yenu kwa zaidi ya miaka kumi sasa, nikitumia huduma ya Tanzanite Account, maalum kwa ajili ya Watanzania wanaoishi nje ya nchi.

Tarehe 20/09/2016 nilitumiwa barua pepe ikieleza kuwa uboreshaji (upgrade) wa huduma za kibenki kwa kutumia intaneti ulikamilika tarehe 19/09/2016 na kuwa tayari kwa matumizi saa 12 jioni (kwa saa za Tanzania). Hata hivyo, kulijitokeza matatizo ya kiufundi, na licha ya kuomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza, alifahamisha kuwa wateja wangejulishwa pindi matatizo hayo yakitatuliwa 




Siku moja baadaye, tarehe 21/09/2016 nilitumia barua-pepe nyingine yenye maelezo ya jinsi ya kuingia kwenye akaunti yangu. Nilielezwa pia kuwa tarakimu za siri (one time key) za kuniwezsha kuingia kwenye akaunti yangu zimeshatumwa kwa SMS kwa namba yangu ya simu inayoishia na namba ***2957, na kama sijapata tarakimu hiyo ya siri basi niwasiliane na benki kwa barua-pepe [email protected].


Nilipoangalia SMS zangu sikuona ujumbe wowote kutoka Tanzania. Nikadhani kwamba labda SMS hiyo itakuja mara baada ya kufuata maelekezo ya kuingia kwenye akaunti yangu. Nikafanya hivo, hakuna SMS iliyotumwa kwangu. Baada ya hapo nikatuma barua pepe kwa anwani [email protected]. Hiyo ilikuwa tarehe 21/09/2016



Kuonyesha kuwa wahusika huko CRDB sio watu makini, katika jibu lao kwangu wakaniomba niwapatie namba yangu ya simu japo awali walieleza kuwa nitapata tarakimu ya siri kwa namba niliyosajili kwa benki hiyo. 


Sijawahi kuitaarifa CRDB kuwa nimebadili namba yangu ya simu, sasa ni kituko kusikia wakiniomba niwapatie namba yangu ya simu. Je walipoteza namba yangu niliyoisajili kwao? Sidhani, kwa sababu katika email ya awali walieleza kuwa tarakimu ya siri ingetumwa kwa namba yangu yenye kuishia namba ***2957. Kama wanayo, kwanini waombe tena niwatumie namba yangu? Je hii haitoshi kumpa hofu mteja kuhusu usalama wa habari (data) zake katika benki hiyo?


Sikujibiwa. Nikawaandikia tena na tena na tena, lakini sijajibiwa hadi wakati ninaandika makala hii














Baadaye nikasema labda nijaribu kuwasiliana na benki hiyo kupitia akaunti yao katika mtandao wa kijamii wa Twitter, lakini ilikuwa kazi bure kama sehemu ya maongezi yetu inavyoonyesha hapo chini. Pia nilijaribu kutumia huduma ya mwasiliano ya maongezi (chat service) kwenye tovuti ya benk hiyo lakini nilitumia zaidi ya masaa mawili bila kupata mtu wa kuongea nami. Pia nilijaribu kutumua SMS kwa namba ya huduma kwa wateja, sikujibiwa. Nikajaribu kutuma ujumbe kwa Whatsapp, pia sikujibiwa.



Nilichobaini baada ya kujaribu kuwasiliana na CRDB huko Twitter ni kwamba kuna wananchi kadhaa ambao pia hawaridhishi na huduma za benki hiyo. Kwa lugha nyingine, mie sio mwathirika pekee wa huduma za kiwango cha chini za benki hiyo.

Sasa naomba nilikabidhi suala hili kwako Dokta Kimei. Haikubaliki kabisa kwa mteja wenu kunyimwa huduma za kibenki katika intaneti (internet banking) kwa takriban wiki nzima sasa kwa sababu ya uzembe tu. 

Kwenu wasomaji wa makala hii, ninaomba kuwafahamisha kuwa kama kuna mtu yeyote amekumbana na huduma mbovu iwe kwa hawa jamaa wa CRDB au huduma yoyote ile - na ana ushahidi - basi naomba uwasiliane nami ili angalau tuwafikishie ujumbe wa husika hadharani namna hii, na pengine kuwaumbua kwa uzembe wao au huduma zao mbovu.  Kukalia kimya huduma mbovu ni sawa na kuridhika nazo. Huduma bora kwa mteja sio suala la fadhila bali haki na stahili ya mteja.

UPDATE: Hatimaye tatizo langu limetatuliwa kwa jithada kubwa za Msimamizi wa Huduma za benki kwa intaneti, Bi Sarah Nzowa. Ninamshukuru kwa msaada mkubwa alionipatia

23 Sept 2016

NIANZE makala hii kwa kurudia salamu zangu za rambirambi kwa vifo vya Watanzania wenzetu 17 na pole kwa majeruhi 440 kutokana na tetemeko la ardhi maeneo ya Ukanda wa Ziwa, hususan mkoani Kagera.
Pia ningependa kutumia fursa hii kumshukuru Diwani William Rutta wa Kata ya Ishozi, wilayani Missenyi, mkoani Kagera, kwa kutumia muda wake kipindi hiki kigumu kunitumia barua pepe kuhusu janga hilo la tetemeko la ardhi lililoharibu nyumba 2,063 huku 14,081 zikiwa katika hali hatarishi, 9,471 zikiwa zimepata uharibifu mdogo na wananchi 126,315 wakihitaji misaada mbalimbali.
Licha ya pongezi zake kwa makala yangu katika gazeti hili toleo la wiki iliyopita, Diwani huyo alielezea masikitiko yake kuona vyombo vya habari vikiitaja Wilaya ya Bukoba tu kuhusu tetemeko hilo ilhali waathirika wengi wapo wilayani Missenyi.
Kadhalika Diwani huyo alitoa wito kuwa tofauti zetu za kisiasa zisituondolee uzalendo na kutoa wito kwa watu na taasisi mbalimbali kuendelea kutoa michango ya hali na mali kwa waathirika wa tetemeko hilo, sambamba na kuhakikisha michango iliyokwishatolewa inawafikia walengwa.
Baada ya shukrani hizo, nigusie kuhusu mijadala ya chinichini inayoendelea, angalau katika mitandao ya kijamii ya Watanzania kuhusu kinachoelezwa kuwa ni ukimya wa Rais Dk. John Magufuli katika janga hilo la tetemeko la ardhi.
Katika kumtendea haki Rais Magufuli, ukweli ni kwamba hajawa kimya kama inavyoelezwa. Mara baada ya kupata taarifa ya janga hilo, rais alitoa salamu zake za rambirambi siku hiyo ya tukio kupitia taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa.
Lakini binafsi ninawaelewa vema wanaohoji 'ukimya' wa Rais wetu kuhusu janga hilo. Kwamba Dk Magufuli sio tu ni Rais wetu bali pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama na pengine anatarajiwa kusikika kwa 'maneno ya mdomo' (na sio tamko tu la maandishi) akizungumzia suala hilo. Na pengine wanaohoji 'ukimya' wake walitarajia angekwenda eneo la tukio (hasa ikizingatiwa kuwa yeye ni 'mwenyeji' wa maeneo yaliyokumbwa na janga hilo). Hata hivyo, binafsi ninataraji kuwa rais atazuru huko hivi karibuni tu.
Kadhalika, kwa vile rais ndiye mkuu halisi wa serikali, taasisi yenye jukumu la usalama wa wananchi, basi huenda wanaohoji ukimya wake wanatarajia yeye kuongoza jitihada za serikali kuwapatia uhakika waathirika wa tetemeko hilo, sio tu kwa kuongoza jitihada za michango ya kuwasaidia wahusika bali pia kuonekana katika eneo la tukio.
Na vile vile, licha ya ukweli kwamba kuna kundi fulani ambalo limejiapiza kumkosoa Dk. Magufuli kwa kila atakalofanya, wanaohoji ukimya wake sio tu wanaruhusiwa na Katiba kufanya hivyo bali pia wanaweza kuwa wanamsaidia rais wetu ili kuepusha uwezekano wa lawama za upungufu wa kiuongozi katika nyakati za majanga.
Licha ya wanachokitafsiri kuwa ni ukimya wa rais, wanaozungumzia suala hilo pia wameonesha kuguswa na Rais Magufuli na watangulizi wake wawili, yaani marais wastaafu Jakaya Kikwete na Benjamin Mkapa kutojitokeza kwenye matembezi ya hiari yaliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kuwachangia waathirika wa tetemeko hilo la ardhi. Matembezi hayo yaliongozwa na Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambaye kiumri ni mkubwa zaidi ya Dk Magufuli, Kikwete na Mkapa.
Binafsi nadhani pengine isingekuwa mwafaka kiusalama kwa rais aliyepo madarakani na watangulizi wake watatu kushiriki matembezi hayo kwa pamoja, japo ingewezekana baadhi yao au wote kumpokea mwenzao aliyeongoza matembezi hayo. Hata hivyo, sidhani kama suala hili ni muhimu zaidi ya ukweli kuwa matembezi hayo yaliyowezesha kupatikana zaidi ya shilingi bilioni moja zikiwa ni michango na ahadi.
Kama nilivyotanabaisha awali, kuna wenzetu ambao ni kama wamejiapiza kumkosoa Magufuli kwa lolote atakalofanya, hata liwe zuri kiasi gani. Kana kwamba hilo sio tatizo, kuna wenzetu wengine ambao kwa mtazamo wao, mtu yeyote anayemkosoa rais hata kama ni kwa sababu halali basi mtu huyo ni adui wa taifa. Makundi haya mawili yanafanya mijadala ya kitaifa kuwa migumu.
Nimalizie kwa kutoa pongezi kwa wote waliochangia na wanaochangia misaada kwa waathirika wa tetemeko hilo, hususan marais Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda na Uhuru Kenyatta wa Kenya, mabalozi wa nchi mbalimbali nchini Tanzania, taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa, washiriki katika matembezi ya kuwachangia waathirika wa tetemeko, pamoja na wanaofanya michango ya kiroho kwa njia ya sala au dua.
Mungu ibariki Tanzania

18 Sept 2016


Majuzi nilikutana na tweet ya rafiki yangu Profesa Kitila Mkumbo ambayo kidogo ilinitatiza. Mwanataaluma huyo ambaye ni pamoja na majukumu yake ya uhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni mshauri wa kitaalamu (consultant) wa taasisi ya Twaweza ambayo majuzi ilichapisha utafiti wake kuhusu masuala mbalimbali yanayoihusu Tanzania.


Tweet ya Profesa Kitila iliyonigusa ni hii hapa chini




Tafsiri ya Kiswahili ni kwamba "tafiti za Twaweza zinawahoji Watanzania, sio tabaka la Watanzania wasomi pekee waliosheheni kwenye mitandao ya kijamii. Katika Tanzania, mitandao ya kijamii hairandani na dunia halisi."



Kutokana na kuguswa kwangu, nilimjibu Profesa Kitila kama ifuatavyo


Nikimaanisha "inasikitisha pale watu wa tabaka halisi la wasomi kama wewe Profesa mnaposhindwa kutambua ni jinsi gani mitandao ya kijamii imebadilisha jinsi tunavyowasiliana."


Na Profesa 'akajitetea' kuwa anaelezea tu 'hali halisi,' na sio kama hathamini mitandao ya kijamii


Niliamua kuahirisha mjadala huo hadi siku nyingine licha ya ukweli kuwa siafikiani na mtazamo wa Profesa Kitila kwamba hali halisi ni kuwa mitandao ya kijamii hairandani na dunia halisi. Sawa, kuna vitu vingi/watu wengi feki katika mitandao ya kijamii, matajiri mtandaoni ilhali masikini wa kutupwa katika maisha yao halisi, furaha mitandaoni lakini majonzi katika maisha halisi, na vitu kama hivyo.

Hata hivyo, miongoni mwa vitu chanya kuhusu mitandao ya jamii ni katika jinsi inavyorahisisha maisha yetu. Na katika hili sio kwa tabaka la wasomi pekee bali takriban kila mtu mwenye uwezo wa kutumia inteneti. 

Na kama kuna kundi ambalo bado linasuasua katika matumizi ya mitandao ya kijamii hukoTanzania basi ni hilo la wasomi. Wakati kwa huku nchi za Magharibi ni suala la kawaida kwa watu wa tabaka la juu kuwasiliana na wenzao wa tabaka hilo au hata wa tabaka la chini kwa meseji, iwe SMS au Whatsapp, kwetu sie 'vigogo' wengi bado wana 'fikra za mwaka 47' kwamba kumtumia mtu meseji ni kama 'mtu amefulia, hana uwezo wa kupiga simu.'

Enewei, lengo la makala hii sio kuelezea kuhusu mjadala huo mfupi kati yangu na Profesa Kitila bali kutoa darasa kuhusu namna ya kurekodi call ya whatsapp na jinsi ya ku-share na ku-save voicenote ya Whatsapp.

Kwanini darasa hili ni muhimu? Kwa sababu Whatsapp imekuwa mkombozi wetu mkubwa katika kukwepa gharama za mawasiliano hususan kwa sie tunaofanya mawasiliano ya kimataifa.

Na kwanini unaweza kuhitaji kurekodi Whatsapp call? Well, labda ni kwa sababu unahitaji kuisikia call hiyo baadaye, lakini pia pengine kuna mtu anakubighudhi na wahitaji kumrekodi kwa minajili ya kumchukulia hatua za kisheria.

KUREKODI WHATSAPP CALL

Katika mazingira ya kawaida, Whatsapp hurekodi calls zote na kuzihifadhi kwenye SD card katika folder liitwalo "Whatsapp calls."
Record WhatsApp Calls
Record WhatsApp Calls




Lakini uwepo wa faili hilo unategemea aina ya simu unayotumia, na iwapo simu yako ina SD card. Na kuna nyakati folder hiyo ipo lakini haina kitu ndani yake.

Kadhalika, inaelezwa kuwa hata kama kuna mafaili yenye calls kwenye folder hiyo, basi calls hizo zina sauti yako tu na sio zote, yaani yako na mtu unayeongea nae.

Kutatua tatizo hilo inabidi kutumia apps zinazorekodi calls. Type 'whatsapp call recorder' na utakutana na orodha ya apps kadhaa. Ushauri wangu ni kwamba jaribu apps mbalimbali kabla hujaamua ipi ni bora zaidi kwa mahitaji yako. 

Mie natumia Samsung Galaxy Note 4 (usipoteze fedha zako ku-upgrade to aidha Note 5 au Note 7 kwani Note bora kabisa ni Note 3 na Note 4, hizo nyingine ni mbwembwe tu. Nitaelezea kuhusu hilo katika makala nyingine) na app ninayotumia kwa kurekodi calls za Whatsapp ni All Call Recorder. 

Kuhusu ku-save au ku-share voice notes za Whatsapp, maelekezo ni rahisi tu. 

1. Highlight voicenote husika kisha click share
2. Share hiyo voice note kwa app inayoweza kuipeleka kwa computer yako. Mie natumia aidha 'Send Anywhere' au 'Pushbullet.'
3. Ukishafikisha kwa computer yako, hatua inayofuatia ni kwenda kwenye website hii www.online-covert.com kisha upload voice yako ambayo itakuwa kwenye mfumo wa faili la sauti wa .opus
4. Ili ku-upload, chagua sehemu iliyoandikwa 'Audio converter.' Kisha kwenye drop-down menu (pameandikwa 'select target format') chagua 'covert to mp3' kisha click 'go.'
5. Utapelekwa kwenye ukurasa mwingine ambapo unatakiwa kwenda palipoandikwa ' upload your audio you want to convert to mp3' kisha bonyeza 'choose your file' itakupeleka mahala ulipohifadhi voice note yako ya Whatsapp kwenye computer yako ikiwa katika mfumo wa faili la sauti wa .opus
6.Upload kisha nenda palipoandikwa 'convert file' katika tovuti hiyo ya www.online-covert.com
7. Ikishamaliza kubadili mfumo wa file la sauti kutoka .opus ya whatsapp voice note kwenda mp3, file husika litakuwa downloaded tayari kwa matumizi yako mengine

Ukitaka ku-save voice note ya Whatsapp, 
1. Highligh voice note husika
2. Chagua share pale juu ya whatsapp
3 Chagua app unayotaka kutumia ku-share
4. Peleka voice note hiyo kwenye app ya ku-save mafaili, zilizo maarufu zaidi ni Google Drive, Dropbox au One Drive. Chaguo ni lako.

Kama una swali au maoni au hata kukosoa basi usisite kunitumia kupitia sehemu ya 'comment.' Endelea kutembelea blogu hii kwa habari mbalimbali za teknolojia na nyinginezo. Karibuni sana 







Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.