14 Sept 2008



Rais Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kutambua kuwa njia pekee itakayowakwamua kiuchumi na kuwaletea maisha bora ni kujishughulisha na shughuli mbalimbali za maendeleo na si kukaa tu vijiweni na kulalamika. 
Kauli hiyo aliitoa jana wakati akijibu malalamiko ya wananchi wa kijiji cha Nyumba ya Mungu, kilichopo katika kata ya Lang`ata, tarafa Msitu wa Tembo, wilayani Simanjiro, ikiwa ni siku yake ya kwanza ya ziara yake ya kikazi mkoani Manyara. 

Wananchi hao waliokuwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali, walimweleza Rais Kikwete kuwa bado wanashindwa kuishi maisha bora kama walivyokuwa wametarajia na badala yake wanakabiliwa na matatizo sugu ya kupata huduma bora ya afya na mitaji ya biashara na ukosefu wa ajira. 

Rais Kikwete alielezwa hayo na wananchi wa kijiji cha Lemkuna, muda mfupi kabla ya kuzindua bonde la umwagiliaji la kijiji hicho, ambapo pia walilalamikia bei kubwa ya pembejeo za kilimo na umbali wa upatikanaji wake, hasa mbolea. 

Akizungumza mara baada ya kuwasikiliza wananchi hao, Rais Kikwete, aliwaeleza kuwa wanapaswa kujiajiri wenyewe kupitia utaratibu wa kupata mikopo na kujiunga kwenye vikundi vya kuweka na kukopa (SACCOS) ili waweze kuanzisha miradi ya maendeleo. 

``Jamani msitarajie maisha bora kama yatadondoka kutoka juu, utaratibu uliopo ni wa mikopo tuliyoianzisha ili muweze kufanya shughuli za maendeleo, awamu ya kwanza imekwishapita wengine wamepata wengine hawajapata ila tutaendelea kuhakikisha kuwa mikopo zaidi inatatolewa ili wale ambao hawajapata waweze kupata`` alisema. SOURCE:ippmedia.com

Kauli hiyo inashabihiana na hii iliyotolewa na Waziri Mkuu wa zamani,Edward Lowassa

2007-05-10 15:55:28 
Na Radio One Habari

Waziri Mkuu, Mheshimiwa Edward Lowassa amesema maisha bora kwa kila Mtanzania hayawezi kuja kwa kukaa vijiweni na kunywa kahawa bali kwa kufanyakazi kwa bidii na hasa kuendeleza kilimo. 

Amefafanua kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanayosemwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ni matokeo ya kazi na hayaji kwa kukaa vijiweni kutwa nzima kunywa Kahawa na kutaka wananchi wa Pwani wafanye kazi kwa bidii kujiletea maendeleo. 

Akihutubia mkutano wa hadhara kijijini Maneromango Wilayani Kisarawe Mkoani Pwani Waziri Mkuu amesema watu wa mkoa huo lazima wabadili pato la mwaka la kila mtu ili liwe kubwa kama katika mikoa mingine. 

Aidha ameagiza mashambapori yaliyopo Kisarawe na wilaya nyingine Mkoani Pwani yaorodheshwe, yapelekwe Wizara ya Ardhi ili hatimaye yafikishwe kwa Rais yatwaliwe na kuwagawia vijana wafanye kazi za kilimo. 
Waziri Mkuu anakamilisha ziara yake ya siku sita ya Mkoa wa Pwani leo kwa kutembelea Wilaya ya Bagamoyo. 
SOURCE: Radio One


0 comments:

Post a Comment

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.