Showing posts with label DAWASCO. Show all posts
Showing posts with label DAWASCO. Show all posts

23 Feb 2012


Tamko la Mbunge wa Ubungo kupitia Chadema,Mheshimiwa John Mnyika kuhusu tatizo za upatikanaji wa maji jijini Dares Salaam na ubabaishaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (Dawasco):


THURSDAY, FEBRUARY 23, 2012


DAWASCO imekiuka mikataba; hatua za haraka zinahitajika kuboresha upatikanaji wa maji DSM

Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO) imekiuka mikataba miwili muhimu inayoongoza kazi zake na kusababisha matatizo ya maji katika Jiji la Dar es Salaam ikiwemo maeneo mbalimbali ya Jimbo la Ubungo.


Imenibidi nitoe taarifa hii kwa umma kwa nilitumia taratibu za kawaida za kiofisi tarehe 14 Februari 2012 kuiandikia barua DAWASCO kuchukua hatua kuhusu tatizo la kutozingatiwa kwa ratiba ya mgawo wa maji katika Jiji la Dar es salaam hali ambayo imesababisha kero ya maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo la Ubungo.


Hata hivyo DAWASCO haikujibu barua husika kueleza hatua ambazo imechukua, hivyo natoa mwito wa wazi wa siku tatu kwa DAWASCO kufanya ukaguzi wa mtandao wa maji na kurekebisha kasoro zilizopo na kutoa taarifa kwa umma kuhusu matitizo ya maji yanayoendelea katika maeneo mengi ya Jiji la Dar es salaam ikiwemo katika Jimbo la Ubungo. 


Kazi ya mbunge kwa mujibu wa katiba ni kuwawakilisha wananchi, kutunga sheria na kuisimamia serikali hivyo nakusudia kuchukua hatua zaidi za kibunge dhidi ya DAWASCO iwapo haitazingatia masharti ya mikataba husika na kushughulikia matatizo ya maji yanayoendelea hivi sasa katika jiji la Dar es salaam ikiwemo katika Jimbo la Ubungo.


Ikumbukwe kuwa DAWASCO ni shirika la umma lililoundwa kwa tangazo la Serikali nambari 139 la tarehe 20 Mei 2005 kwa mujibu wa Sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1992.


Tarehe 1 Julai 2005 DAWASCO ilipewa mkataba wa ukodishaji (lease agreement) na DAWASA ambao unaitaka DAWASCO kuendesha miundombinu ya maji na kuhakikisha matengenezo ya mtandao wa maji katika jiji la Dar es salaam.


Aidha, katika kutekeleza mkataba huo DAWASCO inapaswa kuzingatia mkataba wa huduma kwa wateja (Client Service Charter) ambao unaitaka DAWASCO kushughulikia kwa muda maalum malalamiko ya wateja na kutoa taarifa kwa umma kila panapokuwa na matatizo ya maji.


Kwa mujibu wa mkataba wa huduma kwa wateja DAWASCO inapaswa kushughulia malalamiko ya wateja na kuyajibu ndani ya siku tano na iwapo matatizo yaliyopo yanahitaji hatua za kiufundi; DAWASCO inatakiwa kushughulikia matatizo hayo ndani ya siku 30.


Kuanzia mwishoni mwa mwezi Disemba 2011 mara baada ya maafa ya mafuriko katika Mkoa wa Dar es salaam mpaka leo tarehe 22 Februari 2012 nimepokea malalamiko mbalimbali toka kwa wananchi kuwa hali ya upatikanaji wa maji katika kata mbalimbali za Jimbo la Ubungo sio nzuri kama ilivyokuwa baada ya hatua ambazo tulichukua kwa nyakati mbalimbali kuanzia Januari 2011 mpaka Septemba 2011.


Itakumbukwa kwamba tarehe 5 mwezi Septemba 2011 nilifanya maandamano ya kwenda DAWASCO nikiwa na wawakilishi wa wananchi wa kata mbalimbali za Jimbo la Ubungo ambapo tulifanya mkutano na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASCO. 


Kufuatia mkutano huo DAWASCO ilichukua hatua mbalimbali ambazo ziliboresha mgawo wa maji katika maeneo kadhaa ya Jimbo la Ubungo kabla ya ratiba ya mgawo kuvurugika kufuatia mafuriko yaliyokumba mkoa wa Dar es salaam.


Hata hivyo, baada ya mafuriko hayo DAWASCO haikuchukua hatua zinazostahili kwa wakati na kuachia kurejea tena kwa mtandao haramu wa biashara ya maji wenye kuhujumu wananchi hususan wa kipato cha chini katika Jiji la Dar es salaam ikiwemo katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Ubungo.


Hivyo, bodi ya wakurugenzi ya DAWASCO chini ya uenyekiti wa Mhandisi Suleiman Said Suleiman na Mtendaji Mkuu wa kampuni Jackson Midala wanapaswa kurekebisha kwa haraka mfumo mzima wa ufuatiliaji wa DAWASCO kuwezesha ukaguzi wa ufanisi wa mtandao mzima wa maji.


Katika kipindi hiki cha matatizo makubwa ya maji katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam ikiwemo katika kata mbalimbali za Jimbo la Ubungo DAWASCO iache kuwatumia wafanyakazi wanaohusika na ukaguzi kufanya kazi tofauti za kusoma mita na kugawa Ankara badala yake wafanyakazi tajwa wafanye ufuatiliaji wa dharura wa ufanisi wa mtandao mzima wa maji katika maeneo mbalimbali.


Baadhi ya maeneo ambayo yanapaswa kutembelewa ni kata za Makuburi, Kimara, Saranga, Mbezi Luis, Msigani, Kwembe, Goba, Kibamba, Sinza, Makurumla, Mabibo, Manzese, Ubungo na Mburahati. 


Kwa upande mwingine, kwa kuwa mkataba wa huduma kwa wateja unatoa haki kwa wateja wa DAWASCO lakini pia unaeleza wajibu; natoa mwito kwa wananchi katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam kutimiza wajibu wa kuwaelekeza wakaguzi husika mitaa yenye matatizo katika mtandao wa maji ili hatua ziweze kuchukuliwa.


Mkataba huo unawataka wateja wa DAWASCO kutoa taarifa kuhusu uharibifu wa miundombinu, wizi wa maji na kuhusu matatizo ya maji hivyo wananchi watoe taarifa husika na kufuatilia wakaguzi kufika maeneo yao kwa kupiga nambari ya bure 0225500240 au 0762979627 za DAWASCO makao makuu.


Pia, wananchi wanaweza kuwasilisha kero za maji kwa ofisi ya DAWASCO zilizo katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam na kupitia nambari zifuatazo: Temeke +255 775016184, Ilala +255 775048556, Magomeni +255 775016179, Boko/Tegeta +255 775048553, Tabata +255 775016181, Kawe +255 775016185, Kinondoni +255 775016180 na Kimara +255 775048554. 


Wananchi watumie pia nafasi hii kuwasilisha kwa DAWASCO maelezo na vielelezo kuhusu maeneo ambayo hakuna miundombinu ya maji kabisa au miundombinu iliyopo haijawahi kutoa maji kwa kipindi kirefu kwa ajili ya kutaka hatua za ziada. 


Matatizo ya maji katika maeneo mengi ya jiji la Dar es salaam ikiwemo katika Jimbo la Ubungo yamedumu kwa miaka mingi, wananchi wametupa wajibu wa kuwawakilisha kuisimamia serikali na mamlaka zake kupunguza kero husika kwa haraka hivyo wananchi watarajie vitendo zaidi vya kushinikiza uwajibikaji kwenye sekta ya maji katika kipindi cha karibuni.


Imetolewa tarehe 22 Februari 2011 na:


John Mnyika (Mb) 

13 Dec 2007

Makala ya wiki hii ndani ya gazeti la Mtanzania inaangalia namna mafisadi wa kigeni wanavyonufaika kutokana na uzembe wa baadhi ya Watanzania wenzetu tuliowakabidhi dhamana za uongozi.Lakini hata kama wawekezaji hao wangekuwa waadilifu hivi kweli ndoto ya "maisha bora kwa kila Mtanzania" itatimia wakati Waziri mwenye dhamana ya maendeleo ya sekta ya Maji (Waziri wa Maji) nae ni miongoni mwa wadaiwa sugu wa maji waliokatiwa huduma hiyo na DAWASCO?Makala nzima hii hapa chini

Waziri wa Maji anasubiri nini ofisini?

na evarist chahali, uskoch


Hadi muda huu haijaniingia akilini niliposoma habari kwamba aliyekuwa mwekezaji kwenye hoteli ya Millenium Tower “ameingia mitini” na kuacha deni kubwa la kodi ya jengo na bili nyingine.Kwa mujibu wa uongozi wa LAPF ambao ndio wamiliki wa jengo hilo,mwekezaji huyu alianza kuonyesha dalili za ubabaishaji muda mrefu kidogo kabla hajaamua kutoroka,lakini nachoshindwa kuelewa ni kwanini uongozi huo haukuchua hatua za tahadhari kuhakikisha kwamba wanalipwa kilicho chao kabla huyu jamaa hajaondoka kimyakimya.

Pengine ni vema nikitoa mfano halisi wa taratibu za upangaji zilivyo hapa Uingereza.Ukitembelea miji mikubwa kama London,Manchester,Birmingham na mingineyo,au hata kwenye mji mdogo kama Aberdeen (hapa ninapoishi) utakuta kuna jamaa wanaopata hifadhi ya makazi kwenye viambaza vya maduka na majengo mengine huko mjini kati.Hawa ni watu wasio na makazi,na japo wengine wameishia katika hali hiyo kutokana na uzembe wao,wapo wale ambao si rahisi kwao kupata makazi kutokana na ugumu katika utaratibu mzima wa kuingia mikataba ya makazi.Wamiliki wa majengo ya kupangisha wako makini mno kuhakikisha kwamba hawapangishi wababaishaji.

Na kwa wageni inakuwa suala zito zaidi kwani nyaraka kadhaa zinahitajika kabla mwenye jengo hajakukabidhi funguo la pango la kuishi.Mara nyingi taratibu za kupanga jengo huhusisha wanasheria ili pindi upande mmoja utakapokwenda kinyume na mkataba wa pango basi iwe rahisi kuhakikisha haki inapatikana.Hapa nawazungumzia wamiliki binafsi na sio makampuni yenye majengo ya kupangisha.

Pengine wamiliki wa nyumba za kupanga wanakuwa makini kwa vile wana uchungu na mali zao,lakini pengine ni kutokana na utaratibu mzuri wenye kumnufaisha mwenye nyumba na mpangaji.Lakini hata huko nyumbani kuna taratibu kama hizo japo zinatofautiana kwa kiwango flani.Inawezekana mwenye nyumba unayotaka kuhamia asijali sana kudadisi ulikotokea,lakini mara nyingi utaratibu unaofahamika ni kutanguliza malipo ya awali ambayo huweza kuwa sawa na kodi ya nusu mwaka au mwaka mzima.Na wengine hufikia hatua ya kuomba “kilemba” kana kwamba anayetaka kupanga anachumbia kwa mwenye nyumba,yote hiyo ni kwa mwenye mali yake kuhakikisha kuwa hatoishia kujilaumu baada ya kumruhusu mpangaji kuingia kwenye jengo lake.

Naamini kabisa kwamba laiti jengo la hoteli ya Millenium Tower lingekuwa mali ya mtu binafsi basi huyo mwekezaji tapeli asingeweza kutoroka kirahisi namna hiyo.Na kwanini watueleze sasa kuwa mpangaji wao kaingia mitini ilhali walishakuwa na matatizo naye kwa muda mrefu?Jibu jepesi kwangu ni kwamba hawana uchungu na fedha za waliowezesha jengo hilo kufikia hapo lilipo.Na hili ni tatizo kubwa sana katika hii inayoitwa mifuko ya jamii.Maamuzi ya mali zinazomilikiwa na mifuko hiyo yamebaki mikononi mwa watu wachache ambao pindi hasara ikitokea wanaishia kutoa sababu moja au nyingine na wala sio kuelezea namna gani hasara hiyo itakavyofidiwa

Natambua kwamba ni vigumu kuiwezesha demokrasia ichukue mkondo wake katika mfuko wa jamii wenye wanachama elfu kadhaa kama sio laki na kitu.Demokrasia nayozungumzia hapa ni ile ya maamuzi yanayofikiwa kwa makubalino ya wanachama wote.Hata hivyo,hiyo haitoi nafasi kwa wachache waliokabidhiwa dhamana ya kufanya maamuzi kwa niaba ya wanaowawakilisha wakafanya mambo kiholela kwa vile tu fedha zinazoteketea hazitoki mifukoni mwao.

Tumeshuhudia sehemu kadhaa zikibadilishwa majina kila mwaka baada ya wawekezaji wa awali kuondoka na kurusha mpira kwa wawekezaji wapya.Kubadili jina la biashara sio kosa kisheria kwani hata jina la mtu binafsi linawezwa kubadilishwa mahakamani.Tatizo hapa ni kwamba wawekezaji matapeli hutumia misamaha ya kodi na masharti mepesi wanayopatiwa wakati wanaingia mikataba na wakishachuma faida ya kutosha wanaondoka kistaarabu (kwa kutangaza kwamba wamekuwa wanapata hasara) au kibaradhuli (kwa kuingia mitini kama huyo mwekezaji wa zamani wa hoteli ya Millenium Tower).

Mwaka juzi nilialikwa kumtembelea rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani.Nilipofika ubalozi wa nchi hiyo jijini London kuomba viza,nilijionea mwenyewe namna gani wenzetu wanavyojithamini wao kwanza kabla ya wageni.Utaratibu wa kuingia hapo hauna tofauti na ule wa zamani katika ubalozi wa Uingereza hapo Dar ambapo waomba viza walikuwa wanalazimika kukesha usiku kucha kuwahi foleni ya kuonana na maofisa wa ubalozi huo.Japo sina hakika lakini nadhani utaratibu wa sasa wa kufanya maombi mtandaoni unaweza kuwa umepunguza tatizo hilo.Katika ubalozi huo wa Marekani hapo London,raia wa Marekani hawapatwi na usumbufu wa kukaa kwenye foleni ndefu au kupigwa na mvua au kibaridi (kulingana na majira ya mwaka) bali hupewa upendeleo maalumu.

Na hata kwenye maeneo ya kuangalia nyaraka za uraia na makazi kwenye viwanja vya ndege,wenzetu hujitahidi kuhakikisha kuwa raia wao hawapati usumbufu mkubwa kama ule tunaoupata wageni na wapita njia kama akina sie.Angalau pale uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere kuna kutenganishwa kati ya Watanzania,raia wa Afrika Mashariki na wengineo,lakini wengi mtakubaliana nami kuwa tuna kasumba ya kuwanyenyekea wageni kulko tunavyowanyenyekea Watanzania wenzetu.Wawekezaji feki wamekuwa wakiitumia vizuri fursa hiyo sambamba na ubabaishaji wa taratibu za mikataba kuhakikisha kwamba wanachuma vya kutosha na pale wanapovimbiwa wanaamua kuondoka bila matatizo.

Wageni hapa Uingereza wana uwezo wa kuomba viza ya makazi kwa kigezo cha biashara ndogondogo kwa wale wenye uwezo mdogo au biashara kubwa kwa wale wenye uwezo wa kutosha.Nizungumzie hilo kundi la kwanza ambalo kimsingi linatoa mwanya kwa wageni wengi zaidi kutokana na ukweli kwamba mtaji unaohitajika sio mkubwa sana.Kinachowakwamishwa wengi ni umakini katika utaratibu mzima ambao hautoi fursa hata chembe kwa wababaishaji.Mwingereza hawezi kukubali uje uwekeze nchini mwake kwenye sekta ya usafiri wa reli ilhali unategemea mabehewa na injini chakavu kutoka huko ulikotoka.

Tatizo la kunyenyekea haliishii kwenye uwekezaji pekee bali hata kwa taasisi nyingine zinazopaswa kujiendesha kibiashara badala ya kutegemea ruzuku ya serikali.Niliposikia Dawasco ikitangaza kwamba itakata huduma ya maji “kwa vigogo” nilibaki najiuliza kama mamlaka hiyo ingeweza kutoa tishio la namna hiyo iwapo wadeni wake wangekuwa ni wale wa “uswahilini” (kama maji yangekuwa yanapatikana huko).Kama ilivyo kwa Tanesco (na pengine hata TTCL),malalamiko makubwa ya makampuni hayo ni kwamba huwa wanaingiliwa na vigogo kila wanapowabana wadaiwa sugu.Nisichoelewa ni hofu ya vigogo wa makampuni hayo kuchukua hatua madhubuti dhidi ya vigogo wanaowatisha hasa ikizingatiwa kuwa Mkurgenzi wa Dawasco au Tanesco anateuliwa na Rais,kwahiyo wakitishiwa na vigogo wengine wanaweza kabisa kukimbilia kwa Rais kumjulisha wanavyosumbuliwa na vigogo wadaiwa sugu.Japo najua itakuwa ni usumbufu usio na lazima kwa Mkuu wa nchi,lakini naamini kwamba iwapo makampuni yanayokwamishwa na vigogo ambao ni wadeni sugu yakiwajulisha vigogo hao kwamba yanawakatia huduma na “wakileta zao za kuleta” watawaripoti kwa Rais ni lazima watalipa madeni hayo.

Lakini pengine taarifa za hivi karibuni kuwa miongoni mwa wadaiwa wa DAWASCO ni pamoja na Waziri wa Maji zinaweza kutufanya tuionee huruma Mamlaka hiyo.Katika utetezi wake,Waziri huyo anadai kuwa hajawahi kupata huduma ya maji kwa miaka kadhaa,na amekuwa akinunua maji kutoka kwa wafanyabiashara.Swali linakuja,je iwapo yeye kama waziri wa maji anatumiwa bili ilhali hapatiwi huduma ya maji alifanya jitihada gani kuhakikisha sio yeye tu bali Watanzania wengine hawakumbani na adha hiyo?Mbona alikuwa kimya siku zote hizi?Hivi karibuni,Mkuu wa polisi wa usalama barabarani huko Wales alilazimika kujiuzulu baada ya kunaswa na kamera zinazodhibiti mwendo kasi barabarani akiwa anaendesha gari yake zaidi ya kiwango kinachoruhisiwa kisheria.Kwa kuvunja sheria aliyopaswa kuisimamia,kamanda huyo alilazimika kujiuzulu.

Sitarajii waziri wa maji kujiuzulu kutokana na deni hilo,na wala sitarajii hilo kwa mawaziri na vigogo wengine wanaodaiwa kwa vile msamiati “KUJIUZULU” ulishafutika kwenye kamusi ya medani ya uongozi huko nyumbani.Ni udhaifu wa namna hii unaowapa jeuri wawekezaji feki kwani kabla ya kuingia mikataba huwa wanasema udhaifu wa hao waliopewa mamlaka ya kusaini mikataba ya uwekezaji.Kwa mtaji huu,ndoto ya maisha bora kwa kila Mtanzania ina safari ndefu sana kutimia.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.