Showing posts with label JWTZ. Show all posts
Showing posts with label JWTZ. Show all posts

22 Aug 2011



Taarifa ifuatayo imetumwa na mwananchi aliyejitambulisha kama Msemakweli.Naiwasilisha kama ilivyo:
 Uvamizi wa wanajeshi dhidi ya wanakijiji Kimbiji ! Polisi kigamboni wamekua BUBU!hawajakubali kupokea malalamiko ya wanakijiji ! nani ? wa  kumfunga simba kengele? 
MALI NA MAKAZI YA WANAKIJIJI WAPATAO 200 Kimbiji zimeharibiwa.
 Uvamizi uliofanyika 16.08.2011 jumatano saa 4.00 hasubui wakazi kijiji cha Kimbiji,nje kidogo ya jiji la Dar,wamekuwa na mashaka ya maisha baada ya makazi na mazao yao kuharibiwavibaya na wanajeshi (JWTZ) ambao walivamia kijiji hiko na kuvunja vunja makazi ya raia..kinyume cha sheria. 
Hata hivyo baadhi ya wanakijiji walipereka taarifa katika vya  vituo vya polisi vya Kigamboni na mji mwema,havijakubali kupokea malalamiko ya wanachi walioharibiwa mali zao na kutishiwa usalama wao,hadi sasa inaonekana kuwa wanachi wa Kimbiji hawana wa kuwalinda wao na mali zao,kama inavyoeleza katiba ya nchi kuwa kila raia ana haki ya kupewa ulinzi wa maisha yake na mali zake! 
Katika Sakata hili la wanajeshi (JWTZ) kuvamia makazi ya raia na kuharibu mali za raiabado lina utata  wa nani ? kumfunga kengengele simba?

20 Feb 2011








Picha hizi za kutisha zinajieleza zenyewe.Hakuna maelezo yanayotosheleza kueleza kwa ufasaha kuhusu janga hili.Lakini kwa vile kamwe hatutoelezwa chanzo cha milipuko ya mabomu huko Gongo la Mboto,kama ambavyo hatukuelezwa chanzo cha milipuko iliyotokea mwaka juzi huko Mbagala,ni muhimu kwa kila Mtanzania kudai haki yake ya kikatiba ya usalama wa maisha yake.


Ni wazi kuwa wahusika wanapata jeuri ya kutangaza hadharani kuwa hawatajiuzulu kwa vile wanafahamu bayana kuwa aliyewateua kushika madaraka hayo ni mzembe,dhaifu na asiyejua kinachoendelea.Kwa lugha nyingine,YUPO YUPO TU.

Nilighadhibika sana niliposoma kauli ya Mkuu wa Usalama na Utambuzi wa JWTZ Brigedia Jenerali Paul Meela kuwa hakuna atakayejiuzulu kwa sababu uongozi jeshini sio nafasi za kisiasa.Haya ni matusi kwa Watanzania.Kwani Amatus Liyumba alipohukumiwa kwenda jela kwa ubadhirifu wa fedha za umma hapo Benki Kuu alikuwa mwanasiasa?

Kwa akili finyu ya Brigedia Meela,ni wanasiasa pekee wanaopaswa kuwajibika wanapoboronga.Lakini kwa vile kamanda huyo alikuwa anamwakilisha Mkuu wa Mwajeshi Jenerali Davis Mwamunyange,yayumkinika kuamini kuwa kauli hiyo pia ni msimamo wa mkuu huyo wa majeshi.

Tuliowahi kupitia mambo ya kijeshi tunafahamu kasumba ya jeuri na u-mungu mtu ilivyokomaa vichwani mwa viongozi jeshini.Hii inaimarishwa zaidi na utaratibu wa kawaida jeshini kwamba amri ina mwelekeo mmoja tu: kutoka juu kwenda chini,na haihojiwi.

Kwahiyo,wakati Kamanda Meela anaongea na waandishi wa habari,akilini mwake alikuwa kama anaongea na makuruta ambao ni dhambi kuu kwao kuhoji lolote lile.Na kwa vile Meela alikuwa anawakilisha mabosi wake,mtu pekee ambaye angeweza kumwadabisha ni Amiri Jeshi Mkuu,Rais Jakaya Kikwete.

Lakini takriban miezi mitano tangu baadhi ya Watanzania wenzetu watusaliti kwa kumrejesha Kikwete madarakani (tukiweka kando uchakachuaji wa Tume ya Uchaguzi),naamini kila Mtanzania anafahamu fika kuwa ombwe la uongozi wa taifa lililojiokeza wakati wa awamu ya kwanza ya utawala wa Kikwete,sio tu limezidi kukua bali pia limeifanya Tanzania kuishi kwa kutegemea kudra za Mwenyezi Mungu.Ni kama hatuna Rais wala serikali.

Na taasisi muhimu kwa ustawi wa taifa kama Idara ya Usalama wa Taifa ziko katika usingizi mzito unaosababishwa zaidi na marupurupu makubwa licha ya utendaji kazi duni na wa chini ya kiwango.Sijui kama watu hawa wanasumbuliwa na mwenendo wa nchi yetu,kwani ingekuwa hivyo tusingeshuhudia mazingaombwe ya kuruhusu mtu kama Edward Lowassa kuwa Mwenyekiti wa kamati nyeti ya bunge ya Ulinzi na Usalama,leave alone ishu kama za Dowans,EPA,nk.

Na kwa kuonyesha watu wa Usalama wamegubikwa na usingizi,wameshindwa hata kumshauri bosi wao Kikwete kuwa safari yake kwenda Mauritania kusaka ufumbuzi wa mgogoro huko Ivory Coast,sio mwafaka wakati huu wa majonzi makubwa kwa Watanzania.Kikwete na washauri wake wanajifanya hawajui kuwa janga la Gongo la Mboto linawagusa zaidi Watanzania kuliko matatizo ya wa-Ivory Coast.Ni rahisi kwa baadhi ya watu kuhisi kuwa Kikwete anakwepa majukumu na kuamua kwenda kuzurura huko ng'ambo.

Tukirejea kauli za wanajeshi wetu,Brigedia Jenerali Meela anasema taarifa za milipuko iliyopita ni kwa matumizi ya jeshi.Kwani JWTZ limegeuka jeshi la mtu binafsi?Sote tunafahamu kuwa hilo ni Jeshi la Wananchi wa Tanzania.Sasa iweje madudu wanayofanya na yanayopelekea kuwaathiri wananchi wasio na hatia yaishie kuchungiuzwa na wao wenyewe kisha findings nazo zibaki kuwa siri yao?

Jibu la maswali haya na mengineyo mengi ni rahisi:Rais tuliyenae ni dhaifu na asiye na uwezo wa kuwawajibisha hata wale aliowateua yeye mwenyewe.Sasa kwa wanaotegemea Kikwete anaweza kudili na maharamia kama wa Dowans (ambao hakuwateua,na sanasana wanamdai fadhila) watakuwa wana jibu la msingi kuhusu kusuasua kwake kuwashughulikia mafisadi.

Picha kwa hisani ya Rev Masanilo wa Jamii Forums

16 Feb 2011




Habari kutoka Dar es Salaam zinaeleza kuwa milipuko kadhaa imetokea maeneo ya Gongo la Mboto.Hata hivyo habari nyingine zinadai kuwa milipuka hiyo imetokea maeneo ya Kisarawe

Bado hakuna taarifa rasmi kuhusu eneo na chanzo cha milipuko hiyo japokuwa habari zilizopo zinadai milipuko hiyo imetokea kwenye kambi ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).

Mtandao wa Jamii Forums umemnukuu Mnadhimu Mkuu wa JWTZ Brigedia Jenerali Abdulrahman Shimbo akisema "Hali ni mbaya Kikosi namba tano maghala yamelipuka ni hatari, watu wahame, maghala yako karibu karibu sana, tunaomba wananchi wahame sasa hivi, tunajitahidi kuzuia moto unaotokana na hilo unaweza kwenda mbali sana hadi Kilomota kumi, wananchi walioko karibu na maghala ya kikosi Gongo la Mboto wasogee mbali sasa hivi."

Hadi sasa hakuna taarifa kamili kuhusu idadi ya majeruhi japokuwa picha zilizotumwa na baadhi ya watumiaji wa huduma ya mtandaoni ya Twitter zinaonyesha majeruhi wakiwa katika hali mbaya



Tukio hili la kusikitisha linatokea wakati Serikali ikiwa haijaweka hadharani ripoti ya vyanzo vya milipuko iliyotokea kwenye Kambi ya JWTZ Mbagala mwezi Aprili na Mei mwaka juzi.

Wakati huo,aliyekuwa Waziri wa Ulinzi Dokta Hussein Mwinyi aliahidi kuwa angewajibika iwapo ingebainika amezembea.Lakini simulizi hizo ziliishia hapo baada ya vile Serikali kupitia Wizara inayoongozwa na Mwinyi kuamua kuiweka ripoti hiyo 'kapuni'

Wakati tovuti hii inaendelea kukusanya habari za uhakika kuhusiana na milipuko hiyo ni muhimu kwa Watanzania kudai haki zao za msingi za usalama wa maisha yao na mali zao.Haiyumkiniki kuona 'intelijensia' ya vyombo vya dola ikiwa na 'ufanisi mkubwa' katika kukandamiza haki za kikatiba za wananchi lakini ikishindwa kuepusha majanga kama haya.

Upatikanaji wa taarifa sahihi unakuwa mgumu hasa kutokana na vyombo 'rasmi' vya habari nchini Tanzania kutowajibika ipasavyo kuwajulisha wananchi kinachoendelea.Tovuti zote za magazeti 'makubwa' hazina breaking news hadi wakati naweka habari hii.

(Video kwa hisani ya Dedichjr na Picha kwa hisani ya Jamii Forums)

30 Apr 2009

Wingu la moshi jijini Dar kufuatia mlipuko wa mabomu maeneo ya Mbagala.Picha kwa hisani ya MICHUZI
Na Mussa Juma, Arusha

WIZARA ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, imeunda Tume ya Wataalam wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), kuchunguza chanzo cha kulipuka silaha za aina mbali mbali katika ghala la kambi ya jeshi iliyopo eneo la Mbagala, jijini Dar es salaam.

Naibu Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Emanuel Nchimbi alitangaza uamuzi huo jana, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Hoteli ya Ngurdoto, jijini Arusha.

Nchimbi alisema Baraza hilo, litafanya kazi ya kuchunguza chanzo cha ajali hiyo na athari zote ambazo zimetokana na mlipuko huo.

Alisema vilivyokuwepo katika ghala hilo ni mabomu na risasi za aina mbali mbali na silaha nyingine ndogo.

Naibu Waziri huyo, alitoa wito kwa wakazi wote wanaoishi jirani na kambi hiyo kutookota kitu chochote cha chuma na wanapokiona watoe taarifa katika kambi ya JWTZ iliyokaribu nao.

"Endapo wataona au kutilia shaka aina yoyote ya chuma , watoe taarifa haraka katika kambi ya jeshi iliyo karibu nao au katika timu ya wataalam wa jeshi hilo ambayo imeanza uchunguzi," alisema Nchimbi.

Hata hivyo, kwa niaba ya Amiri Jeshi Mkuu, Rais Jakaya Kikwete na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi, alitoa pole kwa wote walioathirika na tukio hilo.

"Amiri jeshi mkuu anawapa pole wananchi wote wa Dar es Salaam na Pwani kwa usumbufu ambao wameupata kutokana na tukio hilo," alisema Nchimbi.

Alifahamisha bado chanzo cha ajali hakijajulikana na pia kutokana na sababu za kiusalama haitakuwa rahisi kutangaza athari za kijeshi zilizopatikana kutokana na tukio hilo.
CHANZO: Mwananchi
HIZI TUME HADI LINI?ILE YA AJALI YA CHENGE HAIJATOA TAARIFA YAKE JAPO TUKIO LENYEWE LILIHUSISHA WATU WANNE TU!JE TUKIO KUBWA KAMA HILI TAARIFA SI ITAKUWA MWAKA 2050!?
HIYO WIZARA YA NCHIMBI INA REKODI ISIYOPENDEZA KUHUSIANA NA TUME.HIVI IMESHATUAMBIA MATOKEO YA TUME ILIYOUNDWA KUCHUNGUZA AJALI YA HELIKOPTA YA JWTZ?
LAITI TUNGEKUWA NA UTAMADUNI WA KUWAJIBIKA,BASI MUDA HUU NCHIMBI NA WAZIRI WAKE DR MWINYI WANGEKUWA WAMESHAJIUZULU.LAKINI KWA VILE UWAJIBIKAJI NI MSAMIATI UNAOELEKEA KUTOLETA MAAN KWETU,BASI TUTARAJIE TUME MOJA BAADA YA NYINGINE...NA KWA VILE WATANZANIA WANAONGOZA KWA REKODI YA USAHAULIFU,AT THE END OF THE DAY WAHUSIKA WATAISHIA "KUUCHUNA" TU.

5 Dec 2008


Picha (for illustrative purpose only) kwa hisani ya MWANAKIJIJI.

MAPIGANO ya koo katika wilaya ya Tarime mkoani Mara, yameingia katika sura mpya baada ya kubainika watu wanaodaiwa kuwa askari wastaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kutumia silaha, sare za Jeshi hilo na mbinu mbalimbali ili kuhakikisha koo wanazotoka zinashinda. 

Baada ya kugundulika kwa matumizi hayo ya vifaa vya JWTZ, Polisi mkoa wa Mara imeanzisha operesheni kali na limewafanikiwa kukamata bunduki tatu, risasi 56 na sare mbalimbali za Jeshi, ambazo zimekuwa zikitumiwa na baadhi ya watu katika mapigano ya koo za Wairegi na Wanyabasi wilayani Tarime. 

Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara, Bw. Deusdedit Kato, alisema jana kuwa silaha hizo ndizo zilizotumika katika mapigano hayo juzi na kuua watu wawili kwa risasi. 

Alisema ingawa bado haijathibitishwa kuwa wamiliki wa silaha hizo kinyume cha sheria ni askari wastaafu wa JWTZ, lakini kuna ukweli huo kutokana na taarifa za awali na wamekuwa pia wakiendesha mafunzo kwa vijana hili kumudu mapambano hayo ya koo. 

Alisema katika operesheni hiyo inayoendeshwa na Polisi, limeweza kukamata bunduki mbili aina ya shotgun namba 979256 na 85084 na risasi 56 zinazomilikiwa kinyume cha sheria nyumbani kwa Bw. Samwel Range wa kijiji cha Magoto ambaye alikimbia kabla ya kukamatwa. 

Kamanda Kato alisema katika upekuzi huo, pia polisi walikamata sare za JWTZ kama vile half sack (2), kit bags (6), suruali za JWTZ (2), suruali za JKT (2) na shati aina ya kombati moja ya JWTZ ambazo zimekuwa zikitumiwa katika mapigano ya koo na matukio mengine ya uhalifu. 

Alisema katika upekuzi mwingine uliofanyika nyumbani kwa Bw. Samwel Magabe, askari hao wa Polisi walikamata bunduki nyingine aina ya shotgun 978862 CAR 151 ambayo pia inasadikiwa kutumika katika mapigano ya koo hizo mbili katika kata ya Nyamwaga. 


Kamanda Kato ambaye pia ni Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Mkoa (RCO) wa Mara, alisema pia viongozi wawili wa kijiji cha Magoto wamekatwa baada ya kudaiwa kuchochea mapigano hayo ya koo. 

Aliwataja viongozi hao kuwa ni Bw. Gabriel Matiku, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho na Bw. Charles Chacha, Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho na hivi sasa wanahojiwa na Polisi Tarime kabla ya kufikishwa mahakamani. 

“Vita hii ya koo katika wilaya ya Tarime, kwa kweli inatuumiza vichwa kwani baadhi ya viongozi pia wanahusika, sasa lazima tufanye uchunguzi na hatutashindwa kuwachukulia hatua viongozi wote wanaodaiwa kuwa wachochezi,” alisema Kamanda Kato. 

Katika mapigano hayo ambayo kwa sasa yameanza kudhibitiwa na polisi waliosambazwa katika vijiji vya Nyamwaga na Magoto, watu wawili waliuawa kwa kupigwa risasi na kutajwa kuwa ni Bw. Girasi Marwa na Bw. Samwel Chacha wote wakazi wa Nyamwaga kutoka koo ya Wairegi. 

Wilaya ya Tarime imekumbwa na vita vya koo kwa muda sasa na watu kadhaa kuuawa kwa mishale, kukatwa mapanga, kuchomwa moto na wengine kupigwa risasi, huku mali na nyumba zikiteketezwa kwa moto kwa kuhusisha koo za Wakira, Waanchari na Warechoka katika kata za Susuni na Sirari, wakati mapigano kama hayo pia yamekuwa yakiibuka katika kata ya Bumera kwa kuhusisha koo za Wahunyaga na Wamera. 

Chanzo kikuu cha mapigano hayo kimekuwa kikitajwa kuwa ni wizi wa mifugo, mipaka ya ardhi na kilimo cha bangi.

CHANZO:Majira

MAUAJI YA DHIDI YA ALBINO YAMESHINDWA KUDHIBITIWA,NA HAKUNA ANAEWAJIBIKA.MAPIGANO YA KOO HUKO TARIME YAMEKUWA YAKIENDELEA KWA MUDA MREFU SASA NA ENEO HILO LIMEGEUKA MITHILI YA ENEO LISILOTAWALIKA LA MPAKA KATI YA PAKISTAN NA AFGHANISTAN.AGAIN,HAKUNA ANAYEWAJIBIKA KUTOKANA NA MAPIGANO HAYO HUKO TARIME.NA KAMA KAWAIDA YETU,TUNASUBIRI MOTO UWE NJE YA UWEZO WA ZIMAMOTO NDIO TUANZE KUUZIMA KWA MIKONO. 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.