Showing posts with label MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA UMMA. Show all posts
Showing posts with label MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA UMMA. Show all posts

11 Feb 2012

Rais Kikwete na Lundo la Mawaziri Wanaounda Kabineti yake ya wababaishaji

Bunge letu linalosheheni walafu mia tatu na ushee ambao licha ya kutugharimu mamilioni kila mmoja wanataka fedha zaidi
Na hii ndiyo hali halisi ya umasikini wetu duniani

29 Jun 2011


Serikali yafanya kufuru
• Yatumia milioni 50/- kumlipia Waziri Hoteli

na Martin Malera Dar na Dauson Kaijage, Dodoma

SERIKALI inatumia zaidi ya sh milioni 50 kwa mwezi kwa ajili ya kugharimia malazi na chakula kwa ajili ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha, anayeishi katika Hoteli ya New Afrika tangu alipoteuliwa, Tanzania Daima Jumatano, limebaini.

Taarifa ya Waziri Nahodha kuishi hotelini, ziliibuliwa bungeni wiki iliyopita wakati wa kipindi cha maswali na majibu kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Ingawa taarifa ya bungeni hazikuwa za kina, uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini Nahodha ambaye amepata kuwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), amekuwa akiishi hotelini hapo tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo Novemba mwaka jana.

Habari kutoka ndani ya hoteli hiyo yenye hadhi ya Nyota Nne zilisema waziri huyo amepangishiwa vyumba vitatu ndani ya hoteli hiyo.

Inaelezwa kwamba amepanga kwenye moja ya vyumba maalumu kwa vigogo, (Executive); chumba ambacho kina sehemu mbili, ikiwemo ya kulala na ya kumpumzikia.

Kwa mujibu wa habari hizo, chumba hicho kinalipiwa dola 300 kwa siku, sawa na sh 480,000.

Vyanzo vyetu vya habari vilitonya kuwa chumba cha pili kinatumika kwa ajili ya walinzi na wasaidizi wake na cha tatu ni kwa ajili ya wageni muhimu wanaomtembelea hotoleni hapo hasa familia yake ambayo iko Zanzibar.

Habari hizo zinasema vyumba hivyo vinagharimu dola 220 kila kimoja kwa siku.

“Kwa maana hiyo, serikali kwa siku inalipa dola 740, sawa na sh 1,124,800 kwa ajili malazi tu ya Waziri Nahodha.

“Kwa hiyo ukifanya hesabu kwa mwezi serikali inalipa sh milioni 33.7 kwa ajili ya malazi tu ya Waziri mmoja na hadi sasa ana miezi saba hotelini,” kilisema chanzo chetu cha habari.

Kwa mujibu wa habari hizo, gharama hizo ni mbali ya chakula na huduma zingine hotelini ambazo kwa mwezi ni zaidi ya sh milioni 20, hivyo kufikia kiasi cha sh milioni 50 kwa mwezi.

Sababu kubwa ambayo inadaiwa na serikali kumfanya waziri huyo aishi hotelini ni uhaba wa nyumba za mawaziri.

Inadaiwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani aliyepita, Laurence Masha, alikuwa akiishi nyumbani kwake katika kipindi chote alichoshika nafasi hiyo na wala siyo kwenye nyumba ya serikali.

“Kwa hiyo Nahodha alipoteuliwa kushika wadhifa huo, serikali ikajikuta haina nyumba kwa ajili ya Waziri wa Mambo ya Ndani na hicho ndicho chanzo cha Waziri Nahodha kulala hotelini,” kilisema chanzo chetu cha habari.

Mbali ya Nahodha, kuna mawaziri wengine wanne wanaoishi hotelini kutokana na uhaba wa nyumba za serikali.

Uchunguzi zaidi unasema kuwa sababu kubwa ya Waziri Nahodha na wenzake kukosa nyumba, ni serikali kuwaacha baadhi ya mawaziri waliotemwa kuendelea kuishi kwenye nyumba za serikali.

“Kuna waziri alifariki; mjane wake bado anaishi kwenye nyumba za serikali, wapo mawaziri waliotemwa, wameomba wabaki kwa muda kwenye nyumba za serikali, ili wajipange. Hawa wote wameziba nafasi za mawaziri wa sasa,” alisema mmoja wa maofisa wa Wizara ya Ujenzi.

Habari zaidi kutoka ndani ya Wizara ya Ujenzi zimedokeza kuwa Nahodha ilishapata nyumba ya kuishi, lakini alikataa kwa madai kuwa haina ulinzi na samani za ndani.

Mtoa habari huyo alisema mvutano uliopo sasa ni kuwa kiongozi huyo anataka apewe stahiki hizo kama Waziri Kiongozi mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) wakati Wizara ya Ujenzi ikipinga jambo hilo kwamba anapaswa kugharimiwa sawa na mawaziri wengine.

Chanzo hicho kimedokeza kuwa kilimtaarifa Waziri Shamsi kuwa kama anataka samani za nyumba awasiliane na Wizara ya Mambo ya Ndani anayoiongoza ili kuangalia uwezekano wa kupata vitu anavyovitaka.

Chanzo kingine cha Tanzania Daima Jumatano, kimedokeza kuwa Shamsi, anaweza kupewa huduma hizo kama angeendelea kuwapo Zanzibar na si bara ambako hivi sasa ameteuliwa kuwa waziri.

Kilibainisha kuwa SMZ, haina utaratibu wa kuwapangia nyumba na kuwapa huduma mbalimbali ikiwemo ulinzi na wahudumu wa ndani viongozi wake wanaoishi nje ya Zanzibar.

Kiliongeza kuwa Shamsi, anapata huduma za hadhi ya Waziri Kiongozi kila anapokuwapo visiwani humo lakini anapotoka nje ya mipaka hiyo kwa maana ya kuwa Tanzania Bara, anagharimiwa sawa na mawaziri wengine.

Alipoulizwa na gazeti hili sababu za Waziri Nahodha kuendelea kuishi hotelini na gharama ambazo serikali inazipata, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodluck Ol- Medeye, alisema wizara yake haihusiki na utoaji wa makazi ya viongozi na watendaji wa serikali, bali inahusika kwa Watanzania wote.

“Suala hili sio la wizara yetu, hatuhusiki kabisa na makazi ya mawaziri wala viongozi wengine wa serikali, tunahusika na makazi ya Watanzania wote,” alisema Naibu Waziri huyo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, alipoulizwa kuhusiana na suala la makazi la Waziri Nahodha na wengine, alisema hajui chochote kwani yuko mjini Dodoma kuhudhuria vikao vya Bunge la Bajeti.

“Mimi sijui chochote, muulizeni Katibu Mkuu ambaye yuko jijini Dar es Salaam, atawapa ufafanuzi,” alisema kwa kifupi Dk. Mwakyembe.

Sakata la Waziri Nahodha kuishi hotelini, liliibuliwa kwa mara ya kwanza wiki iliyopita wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu na Mbunge wa Chambani, Salim Hemed Khamis (CUF).

Mbubge huyo alitoa taarifa zilizomshtua Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, na wabunge wengine kuwa Waziri Nahodha, anaishi hotelini.

Kabla ya kutoa kauli hiyo, mbunge huyo alihoji dhamira ya serikali katika kupunguza matumizi.

Alisema serikali inakusudia kusitisha ununuzi na matumizi ya mashangingi, kuacha kuagiza fenicha kutoka nje na kupunguza posho kama moja ya njia ya kupunguza gharama za matumizi kwa serikali.

Alisema pamoja na dhamira hiyo ya kubana matumizi, serikali imewaacha baadhi ya mawaziri wake waishi hotelini na hivyo kuongeza gharama za matumizi.

“Kuna mawaziri wanaishi hotelini tangu walipoteuliwa hadi sasa, serikali haioni kama hali hiyo ni kikwazo kwa mafanikio ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano tulioupitisha hivi karibuni bungenin?” alihoji mbunge huyo.

Akijibu swali hilo, Waziri Mkuu Pinda kwanza alionekana kushangazwa na taarifa hiyo na baadaye alimtaka ataje majina ya mawaziri anaowajua wanaishi hotelini hadi sasa tangu walipoteuliwa.

“Naomba Mheshimiwa Mbunge nitajie majina ya mawaziri unaowajua kwamba wanaishi hotelini,” alisema Pinda.

Mbunge huyo ambaye alikuwa akisubiri majibu ya Waziri Mkuu kwa hamu, akataja jina la Waziri Nahodha kwamba ni mmoja wa mawaziri wanaoishi hotelini.

Huku akiwa haamini na kumwangalia Waziri Nahodha, Pinda alijibu kwa kifupi tu: “Basi nimesikia.”


5 May 2009


Ikulu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mhasibu Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Makamu wa Rais, Polisi, Msajili wa Vyama vya Siasa na Sekretarieti ya Maadili ni kati ya ofisi ambazo, mahesabu yake yalionekana kuwa na mapungufu na kutofuata kanuni za fedha au kufanya malipo yenye nyaraka pungufu.
Mapungufu hayo yamo kwenye ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu Serikali (CAG) kwa mwaka 2007/08 iliyowasilishwa bungeni wiki iliyopita.

Kutokana na mapungufu hayo, ripoti ya CAG inaonyesha kwamba ofisi hizo, licha ya kupewa hati ya ukaguzi inayoridhisha, kila hati imeambatana na mambo ya msisitizo yenye kuzitaka ofisi hizo zisirudie makosa hayo.

Ripoti hiyo inafafanua: ``Kimsingi, aya inayohusu `Mambo ya Msisitizo` ni tahadhari kwa Afisa Masuuli na taarifa muhimu kwa watumiaji wa taarifa za fedha. Vivyo hivyo, kama udhaifu huo haujarekebishwa, unaweza kusababisha hati isiyoridhisha (kutolewa) kwa kaguzi zijazo.``

Ofisi nyingine zilizopewa hati yenye mambo ya msisitizo ni Magereza, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) (Ngome), Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Mahakama, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikino wa Kimataifa, Ofisi ya Rais na Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri, Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko na Wizara ya Ardhi na Makazi.

Zingine ni Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Wizara ya Fedha na Uchumi, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Tume ya Mipango, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Tume ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya, Tume ya Utumishi wa Umma na Tume ya Kudhibiti Ukimwi.

Vilevile zipo sekreterieti za mikoa kadhaa kama vile Arusha, Mara, Iringa, Kigoma, Pwani, Kilimanjaro, Mbeya, Singida, Morogoro, Shinyanga, Kagera, Dar es Salaam na Rukwa ambazo zilipata hati inayoridhisha yenye msisitizo.

Kuhusu Ikulu, kwa mfano, ripoti ya CAG inaonyesha katika mwaka wa fedha 2007/08 hakukuwa na mpango wa mwaka wa manunuzi, kinyume na kifungu cha 45 (a) hadi (e) cha Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004.

Pia mahesabu ya Ikuku yalikuwa na mambo yasiyosuluhishwa katika taarifa za benki, yanayofikia Sh. 2,710,000.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Ofisi ya Waziri Mkuu ilifanya malipo yenye nyaraka pungufu yanayofikia Sh. milioni 21.8 na malipo yaliyolipwa mara mbili yenye thamani ya sh. milioni 45.

Idara ya Mhasibu Mkuu imeelezwa kufanya malipo yanayofikia sh. milioni 570 kwa M/s Fifth Africa Population bila nyaraka ambatanifu, huku mishahara yenye thamani ya Sh. milioni 8.6 ikilipwa kwa watu walioondoka kwenye utumishi wa umma.

Kwa upande wa ofisi ya Makamu wa Rais, malipo ya madeni ya Sh milioni 89.2 yalifanyika kwenye bajeti ya mwaka huu bila idhini huku stakabadhi za kukiri malipo ya Sh. Milioni 8.9 zikishindwa kuwasilishwa ili kukaguliwa. Pia ofisi inalaumiwa na CAG kwa kufanya manunuzi ya Sh milioni 20.8 kutoka kwa M/s Colour Print (T) Ltd bila kufanya ushindani wa zabuni.

Kuhusu jeshi la polisi, ipo milolongo kadhaa ya makosa ya kihasibu, lakini moja wapo ni malipo ya Sh. milioni 74.1 kufanywa bila nyaraka sahihi na masurufu yasiyorejeshwa kufikia sh. milioni 131.

Ofisi zilizopewa hati yenye shaka ni pamoja na ya Bunge, Wizara za Kilimo, Chakula na Ushirika, Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Mambo ya Ndani, Jinsia na Maendeleo ya Watoto, Nishati na Madini, Maliasili na Utalii, Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Miundombinu.

Sekretareti za mikoa zilizopewa hati yenye shaka ni Dodoma, Lindi, Mtwara, Mwanza, Ruvuma, Tabora na Tanga. Pia kwenye kundi hilo imo Mahakama ya Ardhi.

Ufafanuzi wa ofisi ya CAG unaonyesha kwamba hati zenye shaka hutolewa pale kunapokuwa na udhaifu wenye uzito na unaoathiri taarifa za fedha lakini hausababishi taarifa hizo kukosa maana kabisa.

Taarifa inasema Bunge lilipewa hati yenye shaka kutokana na mlolongo wa makosa ya kanuni za fedha ikiwa ni pamoja na kulipa matibabu ya Sh. Milioni 102 nje ya nchi bila kuidhinishwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Ofisi zilizopewa hati isiyoridhisha, kwa mujibu wa ufafanuzi, udhaifu unaojitokeza unapotosha kabisa tarifa za hesabu ni pamoja na Wizara ya Kazi, Idara ya Uhamiaji na Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi.

Wizara hiyo katika ripoti hiyo inaonyesha kulikuwa na upotevu wa Sh. milioni 90.9 na taarifa za masurufu yasiyorejeshwa ilikuwa inatofutiana.

CHANZO: Nipashe



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.