Showing posts with label NGUZA VIKING. Show all posts
Showing posts with label NGUZA VIKING. Show all posts

31 Jul 2013

WARAKA MZITO WA PAPII KOCHA KWA JK

Na Mwandishi Wetu
ULE waraka wa mwanamuziki aliyefungwa gerezani kifungo cha maisha sambamba na baba yake mzazi, Nguza Viking ‘Babu Seya’, Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ umeibua mjadala tena huku Naibu Waziri wa Mali Asili na Utalii, Lazaro Nyalandu akiombwa na kukubali kuufikisha kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete.
Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ (kushoto) akiwa na baba yake Nguza Viking ‘Babu Seya’.
MIAKA 10 GEREZANI
Hivi karibuni wasanii hao walitimiza miaka kumi tangu walipofungwa katika Gereza la Ukonga, Dar mwaka 2003 hivyo kusababisha waraka huo aliouandika Papii Kocha Februari mwaka 2010 kusababisha mjadala upya.
Kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter, Julai 21, mwaka huu waraka huo ulikuwa gumzo kubwa juu ya ombi la Papii Kocha kwa Rais Kikwete kuwa amhurumie atoke gerezani kwa kuwa bado ni kijana mdogo huku nyuma yake watu wakituhumiana bila ushahidi.
Waraka alioandika Papii Kocha kwa Mhe rais Kikwete.
OMBI KWA WAZIRI NYALANDU
Mwandishi Mtanzania aishie Uskochi, Evarist Chahali aliutundika waraka huo katika ukurasa wake wa Twitter na kusababisha msigano wa kimawazo.
Chahali aliusindikiza waraka huo na maneno akimuomba Waziri Nyalandu kwa kuwa ni mmoja wa ‘memba’ wake mtandaoni aufikishe kwa Rais Kikwete kwa kuwa ulimlenga yeye moja kwa zote.
Alimwandikia Waziri Nyalandu: “Nina imani sana kwako, mheshimiwa waziri na kwa vile Rais Kikwete yupo katika swaumu, natumaini kilio hicho kitasikilizwa.”
Kukawa mchana, kukawa usiku, siku hiyo ikaisha.
Waziri Nyalandu.
WAZIRI NYALANDU AKUBALI
Kesho yake, yaani Julai 22, mwaka huu, Waziri Nyalandu alimjibu Chahali kwa kumwandikia: “Chahali copy that (nimepokea), asante kaka.”

SEHEMU YA MANENO YA KUCHOMA YA WARAKA WA PAPII KOCHA
Baada ya salamu kwa mkuu huyo wa nchi, Papii Kocha aliyekuwa nyota wa Bendi ya FM Academia ‘Wazee wa Ngwasuma’ aliandika: “Naanguka na kushika miguu yako mitukufu mheshimiwa rais.
“Nakuomba msaada (msamaha) kwako mheshimiwa rais kwa njia hii ya maandishi kusudi niweze kuondolewa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani, niliyohukumiwa na mahakama tajwa hapo juu (Kisutu).
“Mhe. Rais mimi nimefungwa nikiwa bado kijana mwenye umri mdogo. Mpaka sasa natambua wazi hatima pamoja na dhamana ya maisha yangu ipo katika mikono yako mitukufu Mhe. Rais.
“Naomba huruma yako mheshimiwa Rais maana mimi ni mtoto wako ninayehitaji huruma yako wewe mzazi.
“Natumaini kauli yako ya mwisho ndiyo itakayoleta pumzi ya uhai nafsini mwangu.
“Nakutakia kazi njema, afya njema na maisha marefu. Mungu akubariki.”
Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
WAKIKUBALIWA WATAREJEA URAIANI?
Baada ya Waziri Nyalandu kukubali kuupeleka waraka huo ikulu na habari hiyo ikasambaa mitandaoni, baadhi ya watoa maoni walikwenda mbele zaidi wakidai huenda ombi lake litakubaliwa na kumfanya Papii Kocha na baba yake kurudi kula bata uraiani.
Wanamuziki hao walifungwa gerezani kwa tuhuma za kunajisi watoto 10 wa Shule ya Msingi Mashujaa, Sinza jijini Dar.
Mbali na kuachiwa kwa baadhi ya watoto wa familia ya Babu Seya waliokuwa wakitumikia kifungo cha maisha, Papii na baba yake bado wanaendelea kutumikia kifungo hicho hadi sasa.

24 Jul 2013


WAKATI taifa likiwa katika maombolezo ya vifo vya mashujaa wetu saba waliouawa huko Darfur, Sudan, wakitumikia kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini humo, Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilifanya tukio linalostahili pongezi nyingi, japo huenda ni wananchi wachache tu wenye taarifa nalo.
Jumapili iliyopita jeshi hilo lilianza kutumia rasmi mtandao wa kijamii wa twitter likitumia ‘handle’ @jw_tz. Hatua hiyo ni ya kimaendeleo na inaonyesha kuwa jeshi letu limedhamiria kwenda na kukumbatia teknolojia ya kisasa ya mawasiliano.
Mtandao wa twitter na pengine mitandao ya jamii kwa ujumla, bado ni suala geni kwa Watanzania wengi. Na licha ya ugeni huo, ukweli kwamba umiliki na upatikanaji wa huduma ya kompyuta bado ni ‘anasa’ wanayomudu watu wachache unafanya matumizi ya twitter (na mitandao mingine ya kijamii) kutokuwa suala muhimu au maarufu kwa jamii yetu.
Hata hivyo, mitandao ya kijamii hivi sasa imekuwa sehemu muhimu ya mawasiliano; huku ikibadili kwa kiasi kikubwa upatikanaji na kupashana habari. Wakati kwa muda mrefu mawasiliano kati ya mtu na mtu yamekuwa yakitegemea aidha neno la mdomo (kwa maana ya watu kukutana au kwa njia ya barua) au magazeti na redio, na kwa kiasi fulani runinga, mitandao ya jamii na teknolojia ya mawasiliano kwa ujumla imetokea kuwa njia ya haraka ya mawasiliano katika jamii.
Ukitaka kupata mfano wa umuhimu wa teknolojia hiyo ya mawasiliano, ni jinsi ziara ya kihistoria ya Rais wa Marekani Barack Obama huko nyumbani Tanzania, hivi karibuni, ilivyoripotiwa in real time (kadri matukio yalivyokuwa yakitokea) badala ya kusubiri gazeti la kesho au ripoti za redioni au kwenye runinga.
Kadhalika, kwa kutumia mtandao wa twitter, wananchi wamekuwa wakiendesha kampeni mbalimbali, na ya hivi karibuni kabisa ni ile inayohamasisha kupinga kodi ya sim card ambapo inatumia hashtag #NoSIMcardTax.
Iwapo Serikali itasikiliza kilio cha wananchi na kusitisha au kufuta kodi hiyo, basi kampeni hiyo ya mtandaoni (hususan huko twitter) itastahili pongezi kubwa.
Pamoja na pongezi zangu kwa hatua hiyo ya JWTZ kujiunga na mtandao wa twitter, bado taasisi hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa; hususan kutumia ipasavyo mtandao huo kama nafasi kwa jeshi hilo kuupasha umma habari stahili.
Kwa mfano, juzi Rais Jakaya Kikwete aliwaongoza Watanzania kutoa heshima zao za mwisho kwa miili ya wanajeshi wetu waliouawa Darfur, na katika mazingira mwafaka, tungetegemea akaunti ya twitter ya JWTZ ingetulea tukio hilo ‘live’ lakini haikuwa hivyo. Siwalaumu kwa vile pengine ni ugeni tu katika matumizi ya teknolojia hiyo.
Licha ya ujio huo wa JWTZ huko twitter, mtandao huo wa kijamii unatumiwa pia na baadhi ya viongozi wetu wa serikali na wanasiasa, japo idadi yao ni ndogo. Rais Kikwete ni miongoni mwa viongozi hao; huku akiweka historia ya kuwa mmoja wa marais wachache wa Afrika wanaotumia mitandao ya kijamii.
Miongoni mwa mawaziri wachache wanaotumia mtandao wa twitter ni Mheshimiwa Lazaro Nyalandu (@LazaroNyalandu), Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii. Uwepo wake katika mtandao huo umenisaidia kumfahamu katika namna ambayo pengine Watanzania wengi hawaifahamu.
Nyalandu amekuwa mfano bora wa jinsi inavyostahili na inavyowezekana kuweka maslahi ya nchi mbele ya maslahi ya kiitikadi. Lilipotokea tukio la milipuko ya mabomu jijini Arusha, Waziri Nyalandu alishiriki kikamilifu kuufahamisha umma kuhusu hatua mbalimbali zilizokuwa zikifanyika kuwasaidia majeruhi.
Na japo Nyalandu ni Mbunge wa CCM, kamwe hajawahi ku-tweet mambo ya kiitikadi, na badala yake tweets zake zimekuwa zikihusu masuala ya Tanzania na Watanzania, badala ya masuala ya CCM.
Kingine kinachopendeza kuhusu Naibu Waziri huyo ni usikivu kwa hoja mbalimbali zinazowasilishwa kwake kupitia mtandao huo. Kama ilivyo kwa Naibu Waziri mwingine, Januari Makamba (@JMakamba), Nyalandu huwasiliana na wananchi waliopo twitter kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, kiasi yaweza kuwa vigumu kudhani ni mtu mwenye dhamana kubwa serikalini.
Ni kwa sababu hiyo, kupitia mtandao wa twitter Jumapili iliyopita nilimtumia ombi Waziri Nyalandu kumsihi awasilishe kilio cha msanii Johnson Nguza (Papii Kocha) ambaye, pamoja na baba yake Nguza Viking na kaka zake wawili, wanatumikia kifungo kirefu jela kwa kosa la kubaka.
Mwishoni wa wiki, blog mbalimbali zilichapisha barua iliyoandikwa na msanii huyo (Papii Kocha) kwenda kwa Rais Kikwete akiomba msamaha kwa yeye na familia yake, na kumwomba Rais awatoe gerezani.
Nina sababu mbili za msingi za kuguswa na suala la ‘Babu Seya’ na wanae ambao wamekuwa gerezani kwa takriban miaka 10 sasa. Kwanza, japo kuna msemo maarufu kwenye kila jela kuwa ‘kila mfungwa hana hatia’ (yaani amefungwa kwa kuonewa), tangu Nguza na wanae walipokamatwa na hatimaye kufungwa nimebaki na hisia kuwa sheria ilipindishwa dhidi yao.
Mengi yameshasemwa huko mitaani kwamba kesi hiyo ilisababishwa na visasi binafsi dhidi ya msanii huyo na wanae. Ikumbukwe kuwa katika nchi zetu masikini kuna ‘haki za aina mbili,’ kwa wanyonge ambao wanaweza kwenda jela kwa kusingiziwa tu, na kwa vigogo ambao ni kama wana kinga ya kudumu ya kisheria.
Sababu ya pili ya kumwomba Waziri Nyalandu amfikishie Rais Kikwete ujumbe wa Papii Kocha ni ya kibinadamu zaidi. Tuweke kando hisia kuwa kifungo cha Nguza na wanae ni sheria kufuata mkondo au kupindishwa.
Kama binadamu, na hasa katika Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhan, unajiskiaje ukisoma barua ya kutoa majonzi kutoka kwa kijana mfungwa anayezeekea jela akiomba msamaha kuhusu hukumu ambayo tangu mwanzo wafungwa hao wamekuwa wakidai ni ya uonevu tu dhidi yao?
Ndio, huko jela ‘kila mfungwa hana hatia’ (yaani wafungwa wengi hudai wamefungwa kwa kuonewa hata kama walikamatwa red-handed wakifanya makosa).Lakini katika mazingira ya kawaida, ni wafungwa wangapi waliopo jela kwa takriban miaka 10 na wanaendelea kusisitiza kuwa walifungwa kwa uonevu na wanaomba hukumu dhidi yao ziangaliwe upya au wasamehewe?
Laiti ukisoma barua hiyo ya Papii Kocha (na amekuwa akiandika barua kama hiyo mara kadhaa) usipolengwa na machozi basi utakuwa na ‘moyo mgumu’ kweli.
Lakini hata tukiweka kando huruma ambayo baadhi yetu tunayo kwa Nguza na wanae, katika ubinadamu tu, msanii huyo na wanae wameshatumikia adhabu ndefu (bila kujali walitenda kosa au la), na adhabu waliyokwishapata inatosha kutoa fundisho kwao na kwa jamii kwa ujumla. Hivi sisi kama jamii tutaathirika vipi iwapo Nguza na wanawe wakisamehewa?
Kama nilivyotarajia, ‘mtu wa watu’ Naibu Waziri Nyalandu alinijibu juzi akisema kwa tweet (namnukuu) “copy that...” akimaanisha amesikia ombi langu na atalifanyia kazi.
Licha ya imani yangu kwa Nyalandu, nina imani pia kuwa Rais Kikwete atasikiliza ujumbe huo kutoka kwa mteuliwa wake. Vilevile ukweli kuwa huu ni Mwezi Mtukufu, na nina hakika Rais amefunga pia, roho ya huruma itamsukuma kusikiliza kilio cha mara kwa mara kutoka kwa Papii Kocha, kaka zake na baba yao.
Mwisho, ninaomba kila Mtanzania mwenye kuamini katika kuwasamehe waliotukosea (ikiwa ni pamoja na wanaotajwa kuwa wahanga wa makosa yaliyofanywa na ‘Babu Seya na wanawe) atajumuika nami kuwaombea msamaha wasanii hao.
Maandiko Matakatifu katika Surat Al I’mran 155 ya Kurani Tukufu na Marko 11:25 ya Biblia Takatifu ni baadhi za aya lukuki zinazotusisitiza kuhusu msamaha.



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.