Showing posts with label POLISI. Show all posts
Showing posts with label POLISI. Show all posts

24 Feb 2008

Hatimaye ukumbi wa majadiliano katika mtandao (web forums) wa Jambo Forums umerejea hewani baada ya kujitokeza matatizo kati ya baadhi ya wanachama wa Jambo na jeshi la Polisi.Habari zaidi soma hapa

9 Sept 2007

Asalam aleykum,

Joji W.Bush anafahamika kama rais wa taifa lenye nguvu zaidi ulimwenguni.Lakini Bush ni maarufu pia kwa “kuchapia” maneno.Juzijuzi alimshangaza Malkia Elizabeth alipomshukuru kwa ziara yake ya “mwaka 1776”! kabla hajajikosoa yeye mwenyewe baada ya kugundua kwamba ameboronga.Wiki iliyopita alirudia tena “mchemsho wake” huko Australia.Kwanza alimshukuru John Howard,waziri mkuu wa Australia,pamoja na nchi yake kwa mchango wa jeshi la “Austria” huko Iraki (ni kweli majina ya nchi mbili hizo yanachanganya lakini si vigumu kubaini kwamba moja iko bara la Ulaya na nyingine iko Oceania).Na hakuishia hapo.Alianza hotuba yake moja kwa kumshukuru Howard kwa ukarimu wake na kuwa mwenyeji mzuri wa kikao cha OPEC (ilhali ukweli ni kwamba Australia ilikuwa mwenyeji wa kikao cha APEC).Lakini “machale” yalimcheza na kurekebisha haraka “blunder” hiyo.OPEC ni “Organization of Petroleum Exporting Countries” (ambapo Australia haijawahi kuwa mwanachama) wakati APEC ni kifupi cha “Asia Pacific Economic Co-operation”.Ukidhani ngoma iliishia hapo basi umekosea kwani Bush alijikuta akijiumauma kwenye kutamka jina la kikundi kimoja cha kigaidi cha Jemmiah Islamia.Na katika hotuba yake hiyo alimwacha kiongozi mmoja kutoka ukanda wa Pacific akitabasamu baada ya “kulichapia” jina lake.Huyo ndio Joji Bush!!!

Tukiwa bado kwenye anga hizo,majuzi Osama bin Laden alitoa hotuba yake ya “kuadhimisha” mashambulizi ya kigaidi ya September 11,2001 huko Marekani ambapo takriban watu 3000 walipoteza maisha.Katika hotuba hiyo Osama alikuwa akiongea kama mwanasiasa flani ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka Wamarekani kujiunga na Uislam,alizungumzia pia “upinzani” wa baadhi ya wanasiasa wa Marekani katika suala la “global warming” na kugusia baadhi ya matatizo ya ndani ya uchumi wa nchi hiyo.Ikumbukwe kwamba Osama hajawahi kusikika hewani tangu mwaka 2004,na kujitokeza kwake kumezua maswali zaidi kuliko majibu.Nilikuwa naangalia kipindi cha “Late Edition” cha Wolf Blitzer wa CNN ambapo alimdadisi msaidizi mmoja wa White House kwamba je haoni kwamba kwa miaka sita tangu Osama na Al-Qaeda yake wafanye mashambulizi yao huko Marekani bado gaidi huyo sio tu kuwa yuko hai bali pia anajaribu ku-“influence” siasa za Marekani (mfano kwa kuwahubiria kuhusu “madhambi” ya viongozi wao).Wapo wanaodhani kwamba “kosa” la msingi katika msako dhidi ya Osama na kuiteketeza Al-Qaeda lilikuwa katika kuelekeza nguvu nyingi dhidi ya Saddam Hussein (ambaye madai kwamba anashirikiana na Al-Qaeda yalikuja kubainika kuwa sio sahihi) badala ya kukazania kwenye jitihada dhidi ya “adui halisi” Osama na wafuasi wake.Taarifa kutoka huko Afghanistan hazitoi picha nzuri kwani inaelekea kwamba washirika wakuu wa Al-Qaeda,kikundi cha Taliban,wamekuwa wakijiimarisha vizuri na huenda wakawa na nguvu kama walizokuwa nao kabla ya uvamizi dhidi ya Afghanistan uliiongozwa na Marekani.Na moja ya mambo yanayowaumiza vichwa watengeneza sera wa nchi mbalimbali ni hofu ya uwezekano wa Osama,Al-Qaeda,Taliban na vikundi vingine vya kigaidi kupata silaha za maangamizi ya halaiki (kwa mfano za kikemikali au kibaiolojia).Hofu hiyo inachochewa zaidi na ukweli kwamba mbio (kama zile za zama za Vita Baridi ) za kutengeneza na kuongeza uzalishaji wa silaha za nyukilia zimekuwa zikiongezeka kwa kasi.

Ukiachia Mataifa “yenye ruhusa” ya kumiliki nguvu za nyuklia (kwa mfano Marekani na Israel) mataifa mengine yaliyolazimisha “haki hiyo” (kwa mfano Pakistan na India) yanaendeleza kasi ya uzalishaji huku nchi kama Iran ikilazimisha kwa nguvu kujiunga na “klabu hiyo ya nyuklia.” Wajuzi wa mambo wanabashiri kwamba kuna uwezekano mkubwa wa nchi kama Misri na Saudi Arabia nazo kujikuta zinalazimika kuingia kwenye harakati hizo (inaaminika kuwa Saudi Arabia iko mbioni kununua silaha za nyuklia iwapo tishio inaloliona kutoka Iran halitadhibitiwa).Lakini hofu hiyo inaongezeka pia kutokana na taarifa zinazodai kwamba Russia imekuwa ikizidisha uzalishaji wa silaha hizo,na kutokana na mazingira ya kihistoria na sababu za kiuchumi,nchi hiyo inaweza kuuza teknolojia na silaha za nyuklia kwa “mikono isiyostahili” (wrong hands).Je kuna uwezekano kwa nchi kama Iran,China au Russia kuuza uwezo wa kinyuklia kwa kikundi kama Al-Qaeda?Jibu langu ni hapana.Kwanini?Kwa vile naamini nchi hizo zina busara ya kutosha ya kutofanya kosa la aina hiyo ambalo pia linaweza kuwagharimu hata wao.Je kuna uwezekano wa vita vya kinyuklia kati ya taifa moja na jingine?Sidhani kama uwezekano huo ni mkubwa sana japo upo kwa mbali.Je kuna uwezekano wa shambulizi la kikemikali au kibaiolojia litakalofanywa na kikundi cha kigaidi?Jibu la kutisha ni kwamba uwezekano huo upo kwani malengo ya mashambulizi yanayofanywa na vikundi hivyo yamekuwa ni kusababisha vifo vingi,na silaha gani ni bora zaidi katika kuleta madhara ya juu kabisa zaidi ya silaha hizo.Na inajulikana kwamba vikundi vya kigaidi vimekuwa vikihangaika sana kupata teknolojia na silaha za aina hiyo.Hiyo ndio dunia tunayoishi sasa.

Tuangalie mambo yalivyo huko nyumbani.Habari zinazovuma kwa sasa ni madai ya rushwa kwenye mchakato kuelekea kwenye uchaguzi ndani ya CCM.Naamini kuwa wanaofuatilia makala zangu wanafahamu bayana msimamo wangu dhidi ya rushwa na wala rushwa.Lakini niseme bayana kwamba madai ya rushwa kwenye uchaguzi huo hayanishangazi hata kidogo.Nadhani tatizo liko kwenye mkanganyiko wa suala zima la matumizi ya fedha katika harakati za kisiasa.Sidhani kama niko peke yangu katika kuamini kwamba nchi yetu inaimba wimbo wa Ujamaa ilhali staili ya kucheza wimbo huo ni ya Ubepari.Na ukiangalia kwa mfano namna mbio za kuelekea Ikulu ya Marekani hapo mwakani utabaini kwamba matumizi ya fedha ni makubwa sana.Tofauti yao na sisi ni kwamba kuna utaratibu maalumu uliowekwa katika namna gani mtu anaweza kuchangisha fedha,kutoa misaada au zawadi au hata namna ya kutoa fedha kwa ajili ya kujiimarisha kisiasa.Mantiki nyepesi ni hii: ukiwa unahitaji nafasi flani basi yayumkinika kusema kwamba utatumia kila nyenzo uliyonayo kuhakikisha unapata nafasi hiyo.Kinachodhibiti matumizi mabaya ya nyenzo hiyo ni sheria zinazotekelezeka na kufuatiliwa kwa makini.Wanachofanya watoa rushwa katika mchakato huo wa uchaguzi wa CCM ni kutumia “nyenzo” (fedha) walizonazo.Wanaofanya hivyo wanajua bayana kwamba kutumia uwezo sio kosa alimradi kama wanazingatia sheria zinazotawala zoezi zima.Lakini hawajali sana kuhusu kuvunja sheria kwa vile kwa namna flani mazingira yanawapa nafasi ya kufanya hivyo.Rushwa ni kama mmea,unastawi pale tu kwenye ardhi yenye rutuba.Inahitajika busara ya namna flani kuelewa nachomaanisha hapa vinginevyo unaweza kunishangaa kwa kudhani natetea matumizi ya rushwa kwenye jamii yetu.

Mwisho ni habari mbili za kusikitisha zilizojiri mwishoni mwa wiki.Ya kwanza ni matokeo mabaya ya Taifa Stars.Katika hilo naweza kuwafariji Watanzania wenzangu kwamba hata hapa Scotland,ambapo wana kila nyenzo wanayohitaji,timu yao ya taifa imehangaika kweli kufika ilipo sasa.Mafanikio ya Taifa Stars hayawezi kupatikana “overnight.” Tujifunze kwa hawa wenzetu ambao kwao matokeo mabaya ni changamoto ya kujipanga vyema kwa ajili ya mashindano yajayo.Hilo linawezekana kama kutakuwa na subira,uvumilivu na mipango bora.Kutambua ugonjwa,kupata dawa ya ugonjwa huo na kuitumia dawa husika ni hatua tu ya kuelekea kupona,haimaanishi kuwa ugonjwa utaondoka dakika hiyohiyo.Inaweza kufikia wakati ikalazimu kubadili dawa.Tuwe na subira,tutafika.Habari ya pili ni vifo vya Watanzania wenzetu katika ajali huko Mbeya.Hivi maisha ya wenzetu yataendelea kupotea hadi lini?Mbunge Shabbiby aliongea bungeni kuhusu “usanii” unaofanywa na baadhi ya wamiliki wa mabasi ambapo wanapandikiza bodi mpya za mabasi hayo kwenye chasis za zamani au za malori.Simaanishi kuwa basi lililopata ajali ni miongoni mwa yaliyofanyiwa usanii huo lakini kinachosikitisha ni kwamba mamlaka husika bado hazijaanza kufanyia kazi ushauri wa Mbunge huyo.Lakini eneo jingine linalopaswa kurekebishwa kwa haraka ni sheria za usalama barabarani.Semina lukuki na maadhimisho ya kila mwaka ya wiki ya “nenda kwa usalama barabarani” hayawezi kuepusha ajali zinazopoteza maisha takriban kila wiki pasipo kuzisimamia kwa makini sheria zilizopo.Yule “mzalendo” aliyekuja na wazo la “spidi gavana” alikuwa na busara sana lakini sijui mkakati huo umefia wapi!!!Tukiendelea kuamini kuwa spidi gavana bora ni madereva na askari wa trafiki basi, “unfortunately”,habari za kuhudhunisha kuhusu ajali zitaendelea kutusumbua kwa muda mrefu.

Alamsiki

20 Jul 2007

Asalam aleykum,

Juzi nilipata barua-pepe kutoka kwa rafiki yangu mmoja aliyeko huko nyumbani.Huyu jamaa alikuwa akinilaumu “kirafiki” kwamba inaelekea nimeanza kuishiwa pointi za kuandika ndio maana takriban nusu ya makala yangu iliyopita ilikuwa ina habari “nyepesi nyepesi.”Sikukasirika kwani siku zote nathamini sana ushauri wenye lengo la kujenga au kuleta maendeleo.Nilimjibu kwamba nina pointi lukuki za kuandika,lakini kuna wakati inabidi “tupunguze kasi ya maisha” kwa kuangalia habari za vituko mbalimbali hususan vinavyojiri huku Ughaibuni.Pia nilimhakikishia kuwa “nyepesi nyepesi” hizo sio “fiksi” bali ni habari zinazohusu matukio ya kweli,ila tu yanachekesha kwa namna moja au nyingine.Kicheko ni afya.

“Nyepesi” za wiki hii ni pamoja na taarifa kwamba “wanene” 7 ndani ya baraza jipya la mawaziri la Gordon Brown (mrithi wa Tony Blair) wamekiri katika nyakati tofauti kuwa walishawahi kutumia “widi” (kwa wale ambao lugha ya mtaani ni mgogoro, “widi” ni bangi au marijuana).Siku kadhaa zilizopita,kiongozi wa chama cha wahafidhina (Conservative Party) David Cameron naye alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupatikana nyeti kuwa alikuwa akivuta bangi katika siku za ujana wake.Cameron amekataa kuendelea na mjadala wa suala hilo akisema kuwa kila binadamu anaweza kufanya makosa hususan akiwa kijana.Alitaka wanaomshupalia wamhukumu kwa utendaji wake wa kazi wa sasa na sio mambo aliyofanya nyma.Kali zaidi ya zote ni pale Katibu wa Ofisi ya Mambo ya Ndani (Home Office-yaani ni sawa na Wizara ya Mambo ya Ndani huko nyumbani),Jacqui Smith,na waziri mmoja katika ofisi hiyo (hapa katibu wa wizara ni mkubwa kicheo kuliko waziri),Tony McNulty,walipotangaza hadharani kuwa nao walishawahi kuvuta bangi huko nyuma.Na “ushuhuda” huo umekuja wakati mwanamama huyo (Smith) akitangaza mpango wa serikali kuangalia upya uamuzi wa awali wa serikali ya Blair wa kushusha daraja (declassifying) la bangi.Habari kwamba viongozi hao wawili (ambao pamoja na majukumu mengine wana dhamana ya kudhibiti mihadarati) waliowahi kuwa wavuta bangi zimezua mjadala kama kweli wanapaswa kuendelea na nyadhifa zao.Pengine kinachowasaidia ni ukweli kwamba kuna wanasiasa wengine (wakiwamo mawaziri vivuli wa upinzani) ambao nao wameweka bayana kuwa walishawahi kuvuta bangi walipokuwa vijana.Uwazi na ukweli au vituko vya siasa?


Kuna habari nyingine ya majonzi lakini kwa namna flani inaweza inachekesha.Mwanamke aliyekuwa na uzito mkubwa kuliko wote hapa Uingereza,Nazima Hussein,amefariki na kuwaacha wanandugu wakiwa na wakati mgumu baada ya kubambikwa ushuru wa pauni 4,000 (zaidi ya shilingi milioni 8) kutoka kwa manispaa huko Southall,London.Ushuru huo ulitokana na gharama za kuuhudumia mwili wa marehemu ambao ulihitaji watumishi wa kikosi cha zima moto (firemen) 13 kuutoa mwili huo (uliokuwa na unene wa futi 3) kutoka katika flati aliyokuwa akaishi.Na walipoufikisha mochwari huko Uxbridge ilizuka kasheshe nyingine kwani hakuna toroli la kubebea maiti lililomtosha marehemu na pia mafriji yote ya kuhifadhia maiti hayakuweza kumudu ukubwa wa mwili wa marehemu huyo.Marehemu Nazima alifariki akiwa na uzito wa kilo 349 .Habari njema ni kwamba baada ya watu wa Manispaa “kusomeshwa” walikubali kupunguza gharama hadi pauni 3,000 (zaidi ya shilingi milioni 6).Ukiskia msiba mzito ndio huo.

Turejee nyumbani.Siku chache taifa limepewa changamoto ya kutosha kutoka kwa JK kuhusu suala la “kupima ngoma” (ukimwi).Na kwa mujibu wa taarifa za magazeti mbalimbali ya huko nyumbani watu kadhaa wameitikia wito wa Rais kwa kwenda kwenye vituo vya afya kupima ukimwi.Kwa mtizamo wangu,hamasa aliyotoa JK inaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwani kwa upande mmoja inaweza kuwasaidia wale waliokuwa hawajui kama wameathirika kuanza kuchukua tahadhari ambazo zitawasaidia kuishi maisha marefu zaidi.Pia kwa wale ambao vipimo vitaonyesha hawajaathirika wanaweza kuachana kabisa na matendo ya ngono zisizo salama,na hata kumrejea Mola wao.Kadhalika,kwa wale watakaokutwa wana virusi vya ukimwi na wakati huohuo wana familia zinazowategemea wanaweza kupata nafasi mwafaka ya kuandaa “future” za familia zao.Jingine ni kwamba kampeni hiyo inaweza kuwafumbua macho wale vichwa sugu na viwembe wanaopenda kujidanganya kuwa ukimwi ni ajali kazini,na eti ajali haina kinga.

Waziri wa Afya amelielezea Bunge kuwa kuna mpango wa kuwapima ukimwi wale wote wanaofika hospitali kwa matibabu.Wazo hilo ni zuri sana lakini linahitaji tahadhari ya namna flani.Wapo wanaosema kuwa ukimwi ni sawa na maradhi mengine yasiyo na tiba kama kansa au kisukari.Hapana,ukimwi ni tofauti sana hasa kwenye namna jamii yetu inavyowaangalia walioathirika na ukimwi (unyanyapaa).Nadhani wapo watakaokubaliana nami kwamba baadhi ya watumishi wa taasisi za afya wana tabia ya kukiuka maadili ya taaluma yao kwa kutoa siri kuhusu afya za wagonjwa.Naamini baadhi ya wasomaji wameshawahi kunong’onezwa na dokta au nesi flani kuwa “yule nanihii anao (ukimwi).” Sasa kama Wizara ya Afya itatekeleza dhamira yake ya kutaka watu wote wanaofika hospitali wapime ukimwi inapaswa pia kuboresha mambo kadhaa ikiwa pamoja na kuhakikisha kuna washauri nasaha wa kutosha watakaoweza kuwasaidia hao watakaobainika kuwa “wanao.” Naamini pia kuwa kuna sheria inayowabana watumishi wa afya kutoa “siri” ya ugonjwa wa mtu,na katika mpango huu wa Wizara ni muhimu sheria hiyo ikaimarishwa zaidi kwani bila kufanya hivyo si ajabu watu wanaweza kukwepa kwenda hospitali sio kwa kuhofia kupimwa na kukutwa wanao bali kwa kuwaogopa hao wauguzi wasioweza kuhifadhi siri za wagonjwa.Pia Wizara inapaswa kuweka bayana iwapo mpango huo wa kumpima kila mgonjwa utakuwa ni suala la hiari au la lazima.Kwa hapa,wagonjwa wanahamasishwa kupima ukimwi lakini hawalazimishwi.Pasipo kuweka misingi mizuri,nia nzuri ya Wizara ya Afya inaweza kuleta mkorogano usio wa lazima,maana si ajabu tukasikia flani kanyimwa nafasi ya kuonana na daktari kwa vile tu kukataa kupima ukimwi.Ifahamike kuwa suala la kupima au kutopima ni haki ya mtu binafsi.

Pia nimesoma habari iliyonisikitisha husu kilio cha Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwamba imekuwa ikipata ushirikiano hafifu kutoka kwa waajiri katika suala la kuhakiki vyeti vya taaluma za waajiriwa.Unajua utandawazi umeleta mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na fursa ya mtu kujipatia taaluma bila kutia mguu chuoni.Vipo vyuo kadhaa duniani vinavyotoa kozi kwa njia ya mtandao,lakini tatizo ambalo limekuwa likizisumbua hata nchi za Magharibi ni lile la baadhi ya vyuo vya kitapeli ambavyo vinaweza kukupatia cheti cha Udaktari wa Falsafa kwa wiki moja.Ukiona mfumuko wa madokta (sio wale wa hospitali) usikimbilie kufikira kuwa pengine siku hizi PhD zimekuwa rahisi.Ukweli ni kwamba PhD feki zimetapakaa sana kutokana na vyuo feki (japo vingine vimeandikishwa kisheria) ambavyo wanachojali wao ni fedha tu ya huyo anayehitaji PhD ya chapchap.Inatuuma sana sie wengine ambao tunazeekea maktaba kutafuta huo udokta “wa kwelikweli” huku wenzetu “wanasomea baa au kwenye nyumba ndogo zao” na wanaamka asubuhi na “hangover” wakiwa madaktari wa falsafa.Nadhani falsafa pekee waliyonayo “vilaza” hawa ni kuhusu waganga gani wa kienyeji wanasaidia mtu kula rushwa na aendelee kuonekana mwadilifu au namna ya kutogonganisha magari kati ya mama watoto na nyumba ndogo.

Ukweli mchungu ni kwamba TCU ina wakati mgumu kufanikiwa katika azma yake hiyo njema,kwani wengi wetu tunajua kuwa baadhi ya waajiri nao wana elimu za kutilia mashaka.Pia nadhani kuna mapungufu ya kisheria kuhusu matumizi ya vyeti feki,kwani nakumbuka jeshi la polisi halikuchukua hatua yoyote lilipobaini kuwa mbunge mmoja hakuwa mkweli kuhusu elimu yake ya sekondari.Sasa kama ufeki wa vyeti vya sekondari “sio big deal” kwa polisi je hao wenye PhD feki wataweza kuguswa?Enewei,tuna vita kadhaa tunazopenda zianze dakika hii:dhidi ya wala rushwa,majambazi,wabadhirifu,wauza unga,nk.Pengine siku moja itatangazwa vita ya kitaifa dhidi ya vyeti na taaluma feki.Yote yanawezekana.

Alamsiki


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.