Showing posts with label MAGAZETI. Show all posts
Showing posts with label MAGAZETI. Show all posts

10 Aug 2007


Further Updates: "Majibu" ya Mrisho na Tulizo Kilaga.USIKOSE KUSOMA COMMENTS MBALIMBALI MWISHO WA MAKALA HII NA KWENYE BLOGU YA MRISHO

Latest Updates: Baada ya "washtaki" kuwa judge,jury and prosecutor,hatimaye mtuhumiwa apewa nafasi ya kujieleza

Updates: Mashambulizi yaendelea

Updates: Kaazi kweli kweli

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti
Na Mwandishi Wetu
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi.

Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.

Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote.

Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.

Habari hizo ambazo chanzo chake ni mtandao, zilieleza kuwa wasichana hao ni Watanzania waliopiga picha wakiwa watupu kwa nia ya kutangaza biashara ya kuuza miili ambapo waliweka bayana mawasiliano yao.

Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania.

Mwandishi huyo alieleza katika makala yake hiyo kuwa, aliamua kuandika hivyo baada ya kuambiwa na rafiki yake anayeishi Marekani.

Akiongea na gazeti hili, Meneja Mkuu wa Kampuni inayochapa gazeti hilo, Abdallah Mrisho, alisema kuwa amesikitishwa na makala ya gazeti la Kulikoni ambayo haikufanyiwa utafiti wa kutosha.

"Habari iliyoandikwa na gazeti la Risasi ni ya kweli, hatujawahi kuandika wala haturuhusu wahariri wetu kuandika habari za uongo ndani ya magazeti yetu, ila Chahali ameropoka.

"Kimsingi mwandishi wa makala hayo, (Chahali) ameonyesha udhaifu mkubwa kwa kuandika habari bila kufanya utafiti na kufikia uamuzi wa kushambulia gazeti letu bila kuwa na uhakika na alichokiandika", alisema Mrisho.

Mrisho aliendelea kusema ana wasiwasi hata na shahada alizonazo Chahali, kwani mtu mwenye elimu kama yake hawezi kuandika habari za kuambiwa bila kufanyia utafiti, hivyo kuupotosha umma na anaweza kumponza mmiliki wa kampuni inayochapisha gazeti hilo, ambaye anaheshimika sana.

"Chahali hakupaswa kutoa shutuma nzito kama zile kwa maneno ambayo hakuyafanyia uchunguzi na kuchapa kwenye gazeti, kwani anaweza kumponza mmiliki wa kampuni hiyo tunayemuheshimu, anapaswa kuona aibu (shame on him)," alisema Mrisho.

Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.

Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana.

Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao.

"Chahali sio miongoni mwa wanafunzi wanaofanya vizuri sana chuoni," kilisema chanzo hicho.

Baadhi ya wanafunzi wanaosoma kozi moja na Chahali katika chuo hicho ni pamoja na Timofei Agarin, Gordon G. Davidson, Joyleve Elliat, Anna Gustavon, Jeremy Lamoreaux, Giseong lee, Yang Lia, Khristus Vassis, Lortraine Whitty na Anna Zawak.

Mrisho alimtahadharisha mhariri wa gazeti hilo kuwa asipokuwa makini na waandishi wanaoandika makala zao kwa chuki binafsi kama Chahali, wanaweza kujikuta kwenye matatizo makubwa.

Akiongea na mwandishi wetu kwa simu juzi, Mhariri Mtendaji wa magazeti ya This Day na Kulikoni, Evarist Mwitumba alisema kuwa hana habari kuhusu makala hayo.

"Nipigieni kesho asubuhi, kwa sasa niko barabarani naendesha gari na sijasoma gazeti lililoandika habari hiyo," alisema Mwitumba.


HAYA NI MAONI YA WATU MBALIMBALI KATIKA BLOGU YA IJUMAA/RISASI http://abdallahmrisho.blogspot.com KUHUSU MASHAMBULIZI DHIDI YANGU


mkandamizaji said...
Mrisho

Mimi sio mtaalam wa masuala ya mtandao, lakini hakuna mtandao ambao unavurugwa sana na watumiaji kama hi5.com. Kama hichi ndo chanzo chako pekee cha hiyo habari, nasikitika kuwa nitakuwa upande wa chahali kukusuta kuwa picha zile ni za Wamarekani na kuwa nyie mmedanganya watanzania.

Tupe mitandao yenye URL zinazoeleweka sio hi5.com. Mtu anaweza kuweka picha ya mtu yeyote kwenye hi5.com. Na kama nakumbuka kuhusu maelezo ya ile habari, ulisema kuwa kuna namba za simu, eno wanakopatikana hao wadada na mambo kama hayo. Lakini kwa hi5.com ambayo ni mtandao wa marafiki tu, bado hajani conivnce kuwa ulikuwa na source nzuri ya habari.

Najua unaweza kuamua kutotundika hii comment, lakini ujumbe utakuwa umeupata.

Asante

August 9,:53 PM
================================================================
Anonymous said...
Nyote mnahitaji kuwa makini.Mbona hakuna cha ajabu katika hizo picha mnazozizungumzia?Bikini ni nguo za kawaida tu jamani..tuache ushamba na ushambenga watanzania.

August 10, 2007 1:02 AM
===================================================================
kichuguu said...
Nimeangalia picha zile pale Hi5, nina wasiwasi kuwa naweza kukubaliana na chahali kuwa wale ni pornstar wa kimarekani. mambo matatu yanawezekana:

(a)wasichana wa kitanzania wametumia picha za mastar hao.

(b) mastar wameamua kudanganya kuwa wako Tanzania.

(c) mastar hao ni watanzania.

Picha hizo hazikupigwa katika mazingira ya Tanzania. Baadaye nitakutafutia picha nyingine za yule anayejiita Melanie ndipo utakapogundua kuwa siyo za kutoka mazingira ya Tanzania.

August 10, 2007 6:40 AM
===================================================================
mzalendo said...
tumesikitishwa sana kuona vyanzo vyetu vya habari havina uhakika na habari zao. hiyo website iliyotolewa na gazeti la ijumaa inaonyesha moja kwa moja kuwa hao watu mmoja ni MGANDA na wote ni GAYS/ LESBIANS!
mbili ni kuwa hamkuhakikisha kama hizo picha ni za hao MNAOWAITA WAREMBO wa KIBONGO na MMEWASILIANA NAO. Mnauhakika gani kama ni picha za wabongo???? mpaka mkaamua kuandika gazetini?? ....au ndo mnafanya chochote kuuuza magazeti yenu?

August 10, 2007 7:59 AM
===================================================================
Anonymous said...
website mliyotupatia inahakikisha kuwa muandishi wa RISASI hana uhakika na alichokisema, kwa vile website hiyo inaonyesha kuwa wale ni GAYS/LESBIANS na pia HAILAZIMISHI kuwa zile picha ni za hao walioziweka na wala hamkutupa ushahidi kuwa mlihakikisha hao mlowapigia simu ndio wenye picha zile.

August 10, 2007 8:02 AM
====================================================================
Anonymous said...
na kwa vile hakuna uhuru wa kujielezea , na jua nilichokiandika hutokipublish

August 10, 2007 8:04 AM
===================================================================
Anonymous said...
nyote hapo juu nahisi mnamiss point, chahali aliamua kuwakandia wenzake bila kujua kama zile picha kweli zipo na wahusika wamejitambulisha kama wabongo, hivyo ishu sio kama ni wabongo au sio wabongo, ila ishu iliyopo hapa ni kwamba kwa nini Chahali amewakandia jamaa wa risasi na kudai wanaandika habari feki? kwa nini, wakati vitiu hivyo vipo? kama jamaa angefanya utafiti kidogo, angekuwa na ishu tofauti ya kuwabana.. hapa nawaunga mkono jamaa wa risasi..

August 10,:27 AM
===================================================================
Anonymous said...
Mimi naungana na Chalali kuwa magazeti hayo mara nyingi wanaandika habari za uongo ili watu wanunu e magazeti, utakuta mtu anaandika eti kapigiwa simu na mtu wanaandika habari kwenye gazeti je hii ni sawa??? unatunia uongo kupata pesa za watu???? I think tuungane watanzania tuanzishe kampeni za kutonunu magazeti ya udaku!!! Hongera chalali, najua unaweza usitoe hii lakini msg will be sent

August 10, 2007 1:10 PM
===================================================================
Anonymous said...
kwanza hii habari mbona imepindishwapindishwa jamani, kichwa cha habari cha muhusu Mengi, Ndani ya habari main content gazeti la Risasi.Mambo tofauti tofauti.

Simtetei Chalali...ila swala la kutofanya vizuri darasani linawahusu nini hasa, au linahusika vipi na habari yenyewe?...Huo ni mpindisho tosha na ni kupakana matope. Hatuelewi huyu jamaa anasoma katika mazingira gani, isitoshe level anayosoma Phd. haijadiliwi tena kama anafanya vizuri au vibaya darasani. Watanzania tuangalie cha kuandika.
Last point, magazeti ya udaku yapo hata Ulaya, ila cha muhimu ni kuandika mambo ambayo kweli yapo, au yametokea, si kubahatisha ili kuuzisha gazeti.

August 10, 2007 1:19 PM
===================================================================
mkereketwa said...
kama hiyo website ya porn iliyowekwa , chahali alikuwa na haki ya kupinga maelezo ya RISASI kwa vile hao watu hawapo TZ bali wanafanya kazi ya porn Marekani.
tusingefurahi kudanganywa na magazeti kwa kutofuatilia vyanzo vyao vya habari kikamilifu.
kosa la RISASI ni kutokufuatilia kikamilifu hao waliotowa namba zao na wapi wanapatikana kama ni sawa na hao walioweka picha za uchi kwenye Hi5. ushahidi mkubwa unaonyesha kuwa walitumia picha za hao watu tu kujipa umaarufu na kinachoshangaza ni kuona RISASI haikusema kuwa haikutuambia kuwa kuna uwezekano kuwa zile picha si zao.

August 10, 2007 2:45 PM


PIA NIMEONA MAONI HAYA HUKO JAMBO FORUMS

Vyanzo vya Habari vya Magezeti Mengine
Mimi ni msomaji sana wa blogu ya Abdallah Mirosho ya http://www.abdallahmrisho.blogspot.com. Blogu hii hunipatia udaku safi sana kutoka mitaa mbali mbali ya Dar es Salaam. Habari niliyonukuu hapa ilinishtua sana kwamba badala ya wao kukubali kuwa magaxeti yao ni ya udaku, wakaamua kumtukna mwandishi aliyewasema kuwa habari waluyokuwa wameandika haikuwa sahihi.

Quote:

Mtanzania huyu kumponza Mengi

Ni mropokaji, anayeandika bila kufanya utafiti

Na Mwandishi Wetu

Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Aberdeen, Scotland, Evarist Chahali huenda akamponza Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, ambaye pia ni mmiliki wa gazeti la Kulikoni, kufuatia habari potofu aliyoiandika kwenye gazeti hilo dhidi ya gazeti la Risasi......Kwa mujibu wa habari hiyo, mwandishi huyo ambaye ni Mtanzania anayedai kuchukua kozi ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika chuo hicho, aliandika makala ya kuyashutumu magazeti ya Udaku kuwa yanaandika habari feki na kutolea mfano gazeti la Risasi.Katika makala yake ya Jumatano Agosti 8, mwaka huu, Chahali alidai kuwa habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Risasi ambalo ni dada la hili, zilizoambatana na picha hazikuwa na ukweli wowote......Chahali alitolea mfano wa habari iliyochapwa kwenye gazeti hilo la Julai 18-20 iliyokuwa na kichwa cha habari 'Warembo wa TZ wapiga picha za X tupu'.....Hata hivyo, Chahali alidai kuwa habari hiyo ni ya uongo (feki), kwani picha zilizotumika ni za nyota wa sinema za ngono (porn star) wa Marekani na si Watanzania................Kuthibitisha kuwa habari iliyoandikwa ni ya kweli, wahariri wa gazeti la Risasi wamelazimika kutaja anuani ya tovuti ambako wasichana hao wanapatikana, ili umma kwa ujumla uelewe nani mkweli kati ya Chahali na gazeti la Risasi, ingawa haikuwa kusudio lao kufanya hivyo.Anuani hiyo ni http://swallowmyjuice.hi5.com ambako picha zilizotumika, mahali wanakoishi na utambulisho wa wasichana hao vinapatikana....Aidha, kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari cha kuaminika kilichoko ndani ya chuo cha Aberdeen, Chahali ni miongoni mwa wanafunzi wasiofanya vizuri sana katika masomo yao...."

Nilipoangalia picha zilizosemekana za watanzania pale http://swallowmyjuice.hi5.com, nilikuta mwanadada mmja anayejiita Melanie ambaye kwa bahati mbaya ninadhani namfahamau vizuri na picha hiyo imepigwa zaidi ya miaka saba iliyopita. Mwanadada yule alikuwa mmoja wa ma-hooker wazuri sana pale South Beach Miami na nadhani kuwa alikuwa damu mchanganyiko mwasia na mwafrika. Nimeweza kupata baadhi ya picha zake nyingine kwenye websites chafu kama hii hapa. (ONYO: PICHA HIZO NI CHAFU SANA USIZIFUNGUE MBELE YA WATOTO NA WATU WA HESHIMA.)


Swali, je mwandishi wa Risasi kweli alifanya haki kumtolea matusi ya kashfa mwandishi wa Kulikoni kuhusu uhalali wa picha zile kama kweli zilikuwa za akina dada wa kitanzania?
__________________
Kichuguuu: Nyumba inayohifadhi mchwa na nguchiro kwa pamoja bila mkwaruzo

2 Aug 2007

Asalam aleykum,

Wanasema kuwa siasa inahitaji kuwa na mvuto (appeal).Lakini mvuto wa mwanamama Myra Bushell,mshindi wa uchaguzi mdogo wa kanseli kwa tiketi ya chama cha Liberal Democrats cha hapa Uingereza,ni zaidi ya mvuto wa kawaida unaohitajika kwenye siasa.Myra aligombea na kushinda nafasi ya uwakilishi kwenye kanseli ya Bideford huko Devon,huku akiwa ni mcheza-uchi/nusu uchi kwenye vilabu (stripper) na mwendesha huduma ya ngono-kwa-simu (phone-sex-line) ambayo anachaji pauni 1.50 kwa dakika (takriban shilingi 3500 za huko nyumbani).Yeye anajitetea kuwa hayo ni maisha yake binafsi nje ya siasa,lakini tayari wajumbe watatu wa kanseli hiyo wameshajiuzulu kupinga vitendo vya mwanasiasa huyo ambaye pia ana tovuti yake ya huduma za ngono.Myra anajitetea kwamba wakati anautumikia umma kama mwanasiasa,anapaswa pia kumudu gharama za maisha,na ndio maana amekuwa akijihusisha na shughuli hizo “nyeti.” Habari njema kwake ni kwamba katibu (clerk) wa kanseli hiyo,George McMauchlan,ametamka bayana kuwa Myra hajavunja sheria yoyote ya maadili ya kazi ya ujumbe wa kanseli kwa vile “shughuli zake binafsi nje ya siasa” haziathiri utendaji wake wa kazi.Kaazi kweli kweli!!


Tukiachana na habari hizo za mwanasiasa “stripper”, kwa takriban wiki nzima iliyopita,medani za sera za nje za Marekani ilikuwa imetawaliwa na habari kwamba taifa hilo lilikuwa linajiandaa kutekeleza mpango wa kuziuzia silaha baadhi ya nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati.Wanufaika wakubwa wa mpango huo ni pamoja na Saudi Arabia,Misri,na kama ilivyo ada,Israel.Hata hivyo,mpango huo umezaa mvutano wa namna flani kwenye duru za siasa za ndani za Marekani kwani wapo wanaodhani kwamba hoja ya serikali ya Bush kuwa inaziuzia silaha nchi kama Saudi Arabia na Misri ili,pamoja na mambo mengine,kudhibiti kujitanua kijeshi kwa Iran,inaweza kupingana na ukweli kuwa rafiki wa leo anaweza kuwa adui wa kesho,na silaha unazompatia leo kujilinda zinaweza kutumika kesho kukudhuru.Na mpango huu umekuja wakati wachambuzi wa siasa za kimataifa wanaoona kuna kuyumba kwenye urafiki wa muda mrefu kati ya Marekani na Saudi Arabia.Hivi karibuni,Saudi iliweka bayana mtizamo wake kuhusu vita ya Irak kwa kusema kuwa uvamizi wa Marekani nchini Irak unachochea machafuko na suluhisho pekee ni kwa majeshi ya kigeni kuondoka nchini Irak.Pia kumekuwepo shutuma za hapa na pale kwamba Saudi Arabia inavisapoti vikundi vya madhehebu ya Sunni nchini Irak ili kuvikabili vikundi vya madhehebu ya Shia ambavyo inadaiwa vinapata sapoti ya Iran.Kitakwimu na kujiografia,Saudi ni taifa la ki-Sunni wakati Iran ni la ki-Shia,na mahusiano kati ya nchi hizo mbili sio mazuri.Saudi kwa upande wake inahofia sana kukua kwa nguvu za kijeshi za Iran,hasa kwa vile hadi sasa,ukitoa Israel,Saudi ni taifa lenye nguvu kubwa katika eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati.

Wakati mwingine ni vigumu kuzielewa sera za nje za Marekani kwani kwa jinsi flani ilipaswa kujifunza kutokana na maamuzi yake ya zamani ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakiiumiza kichwa katika kipindi hiki tulichonacho,kwa mfano msaada wake wa silaha kwa Irak wakati Saddam alipokuwa rafiki wa nchi hiyo,na misaada yake kwa mujahidina wa Afghanistan wakati wa vita dhidi ya Muungano wa nchi za Kisovieti (USSR).Tawala za nchi nyingi za Kiarabu na Ghuba sio za kidemokrasia (kwa vipimo vya nchi za magharibi),na miongoni mwa sababu zinazodaiwa kuchangia kuibuka kwa siasa za msimamo mkali wa kidini katika nchi hizo kushindwa kwa tawala hizo kuleta mabadiliko ya manufaa ya kisiasa,kiuchumi na kijamii.Lakini katika kukoroga zaidi mambo,baadhi ya tawala hizo zimekuwa zikuvikumbatia na kuvifadhili vikundi vyenye msimamo mkali wa kidini ili tawala hizo ziendelee kuwa madarakani.Kwa uchambuzi mwepesi,yayumkinika kusema kuwa hatma ya tawala hizo kwa muda mrefu sio ya kuaminika sana,na Marekani inaweza kujutia huko mbeleni kwa kuzilinda tawala hizo kwa misaada ya kijeshi.

Na taarifa zaidi kutoka Irak zinaeleza kuwa “picha haziivi” kati ya mkuu wa majeshi ya Marekani nchini humo,Jenerali David Petraeus,na Waziri Mkuu wa Irak,Nour al-Maliki.Inasemekana kuwa Maliki alishamuomba Rais Bush amwondoe Jenerali huyo msomi mwenye shahada ya kwanza katika sayansi (Bachelor of Science),shahada ya uzamili katika Utawala wa Umma (M.A in Public Administration) na shahada ya uzamifu kwenye siasa za kimataifa (PhD in International Relations) na alishakuwa (assistant) Professor kwenye US Military Academy. “Bifu” (kupingana) kati ya Maliki na Jen Petraeus kunatokana na baadhi ya maamuzi yanayopingana kati ya watu hao muhimu kwa mafanikio au kutofanikiwa kwenye sera ya Bush kuhusu Irak.Inaelezwa kuwa Maliki haafikiani na mpango majeshi ya Marekani unaoelekea kuasisiwa na Jen Petraeus wa kuvipatia silaha vikundi vya madhehebu ya Sunni ili vipambane na wapiganaji wa Al-Qaeda nchini humo.Maliki ambaye ni muumini wa madhehebu ya Shia anaelekea kuhofia kuwa silaha hizo zinaweza kutumika dhidi ya vikundi vya madhehebu ya Shia,au kwa mtizamo wa muda mrefu,kuchangia vita vya wenyewe kwa wenyewe pindi majeshi ya Marekani yatakapoondoka (kama kuna kuondoka kweli).

Baada ya mjadala wa siasa za kimataifa,hebu tegeukie mambo mengine ya huko nyumbani.Nitahadharishe kuwa naamini baadhi ya ntakayoandika hapa yatawaudhi watu flani lakini kuudhika kwao kutakuwa na maana moja tu kwangu:kwamba ujumbe umefika na wabadilike badala ya kununa.Binafsi,nadiriki kusema kuwa mzazi makini hawezi kumrushusu binti yake kuingia kwenye mambo ya u-Miss.Kwanini?Kwa sababu inaelekea wengi wa mabinti wanaotafuta u-miss huwa aidha wanarubunika kuwa wenye tabia mbovu baada ya kupata majina au pengine fani nzima ya u-miss ni kichocheo cha umalaya (samahani kwa maneno makali).Yaani kila kukicha utaskia sijui Miss nanihii katembea na mume wa mtu,au Wema Sepetu kapigwa picha za utupu,au Faraja Kotta kalibwaga buzi lake lililoiba fedha wapi sijui,na vituo vingine mia kidogo.Kuna kasoro kwenye fani ya u-miss lakini jamii inaelekea imelifumbia macho suala hilo.Lundenga,Chipungahelo na wadau wengine wa fani ya u-miss wana jukumu la kuithibitishia jamii kuwa tatizo haliko kwenye fani hiyo bali ni kwa baadhi tu ya washiriki.Na kama tatizo ni washiriki basi watuambie bayana inakuwaje wanaweza kupenya katika ngazi mbalimbali hadi kifikia levo ta taifa na kuanza kutuonyesha madudu yao.Rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari aliwahi kunidokeza kuwa fani hiyo imetawaliwa sana na viongozi,wadhamini na mapromota walafi wa kula uroda ambao wanarahisishiwa kazi na mabinti wenye tamaa ya umaarufu wa chapchap,ambao kwao sio ishu kuvua “makufuli” yao ili wakwae u-miss.Ujumbe wangu kwenu ni simpo:msipokuwa makini mtaondoka kwa kilo mbili,na kwa vile mnathamini sana umaarufu,basi kudhoofika kwa afya zenu kutatawala sana kurasa hizohizo zinazoripoti kila siku namna mnavyoibemenda Amri ya Sita kama hamna akili nzuri.Mkikasirika shauri yenu lakini mmezidi kufanya mambo ya aibu.

Halafu kuna mambo mawili yamenisikitisha sana.La kwanza ni hii tabia ya ubabe inayoelekea kumkolea msanii TID.Binafsi,nazipenda sana kazi za kijana huyu,na mwanzoni nilikuwa namtofautisha na wasanii wengine wa bongo kwa vile amewahi kukaa ugahibuni kwa muda wa kutosha na amekuwa akipata mialiko ya nje mara kwa mara.Lakini pengine kwa kutotambua kuwa taswira (image) ya msanii ni muhimu katika kumuweka au kumporomosha kwenye chati,ameendelea kushika vichwa vya habari kwa matukio yasiyopendeza.Wimbo wake naoupenda sana unaitwa “chagua moja”,nami ujumbe wangu kwake ni mfupi:chagua moja kati ya kujiporomosha wewe mwenyewe kwa matendo yasiyofaa au jirekebishe tabia zako ili uendelee kubaki kuwa “Top In Dar.” Usikasirike,ni somo jepesi tu hilo.

Jingine lililonikera ni gazeti la RISASI ambalo katika toleo lake la Julai18-20 lilikuwa na habari kwamba “Warembo TZ wapiga picha za X tupu…zasambazwa mitaani,baadhi yao ni washiriki wa kusaka mataji ya u-miss.” Kinachosikitisha sio kama iwapo habari hiyo ni ya kweli au ya kubuni bali ni picha zilizotumika kwenye habari hiyo.Rafiki yangu mmoja aliyeko Marekani amenifahamisha kuwa wasichana walioko kwenye picha hizo ni wacheza filamu za ngono (porn stars) wa Marekani na wala sio Watanzania.Kwa kuthibitisha alichokuwa anasema,alinipatia tovuti ambazo zina picha za Wamarekani hao weusi.Kama picha zilizotumiwa na RISASI ni feki basi yayumkinika kusema kuwa hata habari yenyewe ni feki.Hivi ni uzembe wa mhariri kucheki ukweli wa habari husika au ndio kuwafanya Watanzania wajinga kwa kuwapa habari “sensational” ambazo hazina ukweli?Nyie ni watu wazima ambao mmeshatengeneza faida ya kutosha kwa kuandika udaku lukuki wa kweli,sasa tamaa ya nini hadi mfikie hatua ya kunyofoa mapicha kwenye mtandao na kuzusha habari?Shame on you!

Alamsiki

18 Jun 2006

KULIKONI UGHAIBUNI:

Habari za huko nyumbani

Mojawapo ya tofauti kubwa kati ya jamii ya hawa wenzetu na huko nyumbani ni namna uhuru wa kujieleza (freedom of expression) unavyothaminiwa.Of course,uhuru huo unaambatana na wajibu,kwa sababu kama wanataaluma wa kanuni za maisha wanavyosema,uhuru bila wajibu ni sawa na kukaribisha vurugu.Kadhalika,uhuru huo sio wa asilimia 100 (absolute),kwa vile hakuna kitu kama hicho duniani.Lakini ukilinganisha na huko nyumbani,yayumkinika kusema kwamba hawa wenzetu wana uhuru mkubwa zaidi wa kujieleza.Sambamba na hilo ni uhuru wa taasisi zinazopaswa kuujulisha umma nini kinaendelea katika jamii yao na hata nje ya jamii hiyo.Hapa nalenga zaidi kwenye taasisi za habari:hususan magazeti na vituo vya radio na runinga.

Kuna magazeti hapa ambayo ni mithili ya hayo yanayoitwa “ya udaku” huko nyumbani.Magazeti kama The Sun,News of the World,Daily Mirror,nk yamebobea sana katika kuibua skandali mbalimbali hapa Uingereza.Inapotokea kwamba habari flani imepotoshwa basi hao walioguswa na habari hiyo wataamua aidha kukanusha au kukimbilia mahakamani kudai fidia.Wakati mwingine watajwa kwenye habari hizo hulazimika kukiri makosa yao hadharani.Kwa mfano,juzijuzi iliripotiwa kuna Naibu Waziri Mkuu John Prescott alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na katibu muhtasi wake Tracey Temple.Katika sekeseke hilo ambalo bado halijatulia ilimzalimu Bwana Prescott kukiri kuwa yaliyosemwa na magazeti ni kweli.

Nakumbuka mwanataaluma mmoja huko nyumbani aliwahi kuvitaka vyombo vya habari kuwa na ujasiri wa kutaja majina ya watuhumiwa bila kuwa na hofu ya kuburuzwa mahakamani,iwapo vyombo hivyo vina uhakika na walinachoripoti.Hebu chukulia mfano wa habari kama hii: “kiongozi wa chama kimoja cha siasa kinachoanzia na herufi C anadaiwa kuwa na uhusianowa kimapenzi na mtangazaji flani ambaye jina lake linaanzia na herufi D…”Hivi habari kama hiyo si ni sawa na chemsha bongo kwa msomaji?Hali ilikuwa mbaya sana miaka ya nyuma kwa sababu ilikuwa ni vigumu mno kujua ni mtuhumiwa gani hasa anazungumziwa katika stori husika.Hata hivyo,kuna dalili kwamba mambo huenda yakabadilika hasa baada ya ujio wa magazeti jasiri ambayo yako tayari kwa lolote.Ukweli ni kwamba kama ushahidi upo wa kutosha hakuna haja ya kuficha jina la mhusika (labda ithibitike kuwa kumtaja kutaathiri uchunguzi,au kwa sababu za kimaadili).

Siyalaumu magazeti yanayoshindwa kutaja majina ya wahusika katika skendo flani japokuwa nayapa changamoto kufanya hivyo.Siyalaumu kwa sababu sio kosa lao,sio uoga,bali ni mazingira yaliyopo.Siasa za nchi yetu baada ya uhuru hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990 zilikuwa zimegubikwa na usiri mkubwa.Kutaja madhambi ya kiongozi ilikuwa dhambi,na hapa tunazungumzia kuanzia ngazi ya mtaa hadi taifa.Usiri sio mbaya kama unatumiwa kwa manufaa ya wengi,lakini kwa bahati mbaya baadhi ya watu walikuwa wanautumia kuficha maovu yao.Waliofilisi mashirika ya umma walinufaika sana na siasa za usiri.Viongozi hawakuwa tayari kusikia kauli nyingine zaidi ya sifa,na kuwakosoa ilikuwa ni kujichimbia kaburi.Kwa hiyo,hali tuliyonayo sasa ni matokeo ya miongo kadhaa ya kuishi katika siasa za kusifia na si kukosoa.

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni miongoni mwa maeneo ambayo yameathiriwa sana na kutokuwepo uhuru wa kutoa mawazo sambamba na uoga wa kuadhibiwa unapoongea kinyume na matakwa ya wakubwa.Nilikuwa sijazaliwa wakati mataifa haya yanaungana,na sijafanya utafiti wa kutosha iwapo Muungano huo ulifanywa kwa ridhaa ya wadau (wananchi) au yalikuwa ni maamuzi tu ya viongozi.Miaka nenda miaka rudi watu wamekuwa wakiongea “chini ya uvungu” kwamba Muungano huu una matatizo mengi tu japokuwa yanaweza kutatuliwa pale penye nia.Baadhi ya viongozi wamekuwa wanakwepa kuzungumzia matatizo yaliyopo kwa madai ya “kukwepa jinamizi la Muungano.”

Hivi karibuni kumekuwa na harakati za kisheria na kisiasa kuhusu Muungano.Kundi la Wazanzibari limefungua kesi kuhusu Muungano,Mchungaji Mtikila nae anaonekana kuukalia kooni Muungano,na viongozi wa serikali kutoka Bara walikutana na wale wa viswani kujadiliana kuhusu suala la Muungano.Juu ya hayo serikali ya awamu ya nne ina waziri anaeshughulikia suala la Muungano.Hata hivyo,kauli za Waziri Kiongozi wa Zanzibar Samsi Vuai Nahodha kuwa suala la mafuta ni la kisiwa hicho pekee,sio kitu cha kukiacha kipite hivihivi tu.Scotland,sehemu ya muungano unaounda United Kingdom (Uingereza) ina utajiri mkubwa wa mafuta.Lakini japokuwa kumekuwa na kelele za hapa na pale kuhusu muungano huo,utajiri wa mafuta haujawahi kuipa kiburi Scotland ifikirie kujitoa katika muungano huo au itumie mapato yote ya mafuta peke yake.Sasa kelele zimeanza hata kabla hayo mafuta hayajapatikana huko Zanzibar,je yakipatikana si ndio itakuwa mshikeshike!

Mimi nadhani suala la Muungano linazungumzika.Ikibidi kufanya kura ya maoni kujua matakwa ya sasa ya wananchi kuhusu Muungano,basi na ifanyike bila kuogopa matokeo yake.Siasa za kuogopana na kubembelezana zimepitwa na wakati,na iwapo itathibitika kuwa upande mmoja wa Muungano hauridhiki na muundo au kuwepo kwake,basi jitihada za dhati zifanyike kupata ufumbuzi.Tukiendelea na siasa za usiri na kujidanganya kwamba kila kitu kinakwenda vizuri,si ajabu siku moja Muungano huu ukavunjikia mahakamani.Hiyo itakuwa aibu sana hasa kwa wale wanaodai kukwepa “jinamizi la kuvunjikiwa na Muungano.”Inatokea huko Serbia-Montenegro,inaweza pia kutokea huko nyumbani iwapo wanasiasa wetu hawatafanya jitihada za makusudi.

Alamsiki

KULIKONI UGHAIBUNI:

Mambo?

Siku chache zilizopita nilibahatika kuwa na maongezi na babu mmoja wa Kiskotishi ambaye kwa maelezo yake mwenyewe yeye ni “mkazi wa dunia nzima” (global citizen).Babu huyo anadai kuwa dunia ingekuwa mahala bora sana kama kusingekuwa na mipaka na sheria kali za uhamiaji.Na katika kutimiza azma yake ya kuwa mkazi wa dunia nzima anadai ametembelea takribani nchi 10 katika kila bara.Sijui kama alikuwa anasema ukweli au “ananifunga kamba” tu.Katika maongezi yetu hayo aligusia jambo flani ambalo liliniingia sana na ambalo ndio mada yangu ya wiki hii:UZALENDO.

Kwa mujibu wa babu huyo,enzi zao wakiwa vijana suala la uzalendo lilikuwa likitiliwa mkazo sana.Alidai kuwa japo kwa sasa hali ni tofauti kidogo lakini bado nchi nyingi za magharibi zinatilia mkazo sana suala hilo.Alieleza kwamba akiwa kijana babu yake alikuwa akimwambia kuwa mazingira mazuri watakayoyaweka wakati huo yatakuja kuvinufaisha zaidi vizazi vijavyo.Baba yake pia alikuwa akimweleza hivyo hivyo.Na yeye alipokuwa mtu mzima alikuwa akiwaeleza wanae hivyohivyo.Na sasa anasema amekuwa akitoa changamoto ya aina hiyohiyo kwa wajukuu wake.Furaha aliyonayo ni kwamba utabiri wa babu na baba yake umetimia.Maendeleo yaliyopo hivi sasa yamechangiwa na msingi mzuri uliojengwa karne kadhaa zilizopita.Na kilichowasukuma hao waliotengeneza misingi hiyo si kingine zaidi ya uchungu wao kwa taifa lao na vizazi vijavyo.

Huko nyumbani kuna tatizo kuhusiana na suala la uzalendo.Wapo wapuuzi fulani ambao wanaendesha mambo utadhani hakuna kesho au labda Tanzania haitakuwepo miaka 50 ijayo.Na hawa ndio baadhi yao waliripotiwa kutishia maisha ya waandishi wa KULIKONI na THIS DAY kwa sababu magazeti hayo yameapa “kula nao sahani moja” (kuwaweka hadharani).Hawa ni watu ambao hawana uchungu si kwa nchi yao tu bali hata kwa wajukuu zao.Ukweli ni kwamba mtu anayekula fedha iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi wa shule hana upeo wa kufikiria kwamba kwa kufanya hivyo huenda wajukuu wa mtoto wake wa mwisho watakaopaswa kwenda shule miaka 20 ijayo wanaweza kukosa nafasi hiyo kwa upuuzi uliofanyika mwaka 2006.Kuna watu wanafanya mchezo na maisha ya Watanzania wenzao kwa kutumia fedha za wenzao bila hata kuwashirikisha hao waliowekeza.Jamani,hata sheria za kawaida mtaani si kwamba bwana au bibi harusi mtarajiwa hawezi kutumia michango ya harusi yake mwenyewe pasipo kuwajulisha wanakamati?Sembuse hao ambao wamekabidhiwa fedha ambazo baadae wanapaswa kuzirejesha kwa wahusika!Nadhani mnaniapata hapo.

Wabadhirifu wa mali za umma na wala rushwa ni sawa na majambazi tu.Ni majambazi ambao silaha yao kubwa ni dhamana walizokabidhiwa kuwatumikia wananchi.Majambazi hawa wanachoiba sio fedha tu bali hata haki za Watanzania wenzao.Na kama walivyo majambazi wengine,hawa wakishahisi kuwa wanafahamika hukimbilia kutumia silaha kuu mbili:rushwa na vitisho.Kama gazeti linachimba maovu yanayofanywa na watu flani wasio na uchungu na nchi yao,basi waandishi wa gazeti hilo watafuatwa ili “wadakishwe kitu kidogo kuua soo.”Na itapoonekana kuwa gazeti hilo na waandishi wake wako ngangari katika kutetea maslahi ya Taifa na hivyo kukataa kuuza taaluma yao kwa kupokea rushwa basi hapo ndipo vitakapoanza vitisho.Sio huko nyumbani pekee ambako waandishi wa habari wanaovalia njuga kufichua maovu katika jamii wanakumbana na vitisho kutoka kwa wahusika.Mwaka 1996,Veronica Guerin, mwandishi wa habari wa kike huko Northern Ireland alipigwa risasi na kuuawa kutokana na makala za uchunguzi kuhusu biashara ya madawa ya kulevya nchini humo.Mwaka juzi,waandishi kadhaa wa magazeti ya Daily Record na Sunday Mail ya hapa Uingereza waliripoti kupokea vitisho kutokana na habari za uchunguzi walizokuwa wakiandika kuhusiana na magenge ya uhalifu.Kadhalika,mwaka jana waandishi wa habari wa magazeti kadhaa nchini Italia waliripoti kupokea vitisho baada ya kuripoti tuhuma za rushwa kuhusiana na klabu ya soka ya Genoa ya nchini humo.

Mifano hiyo michache inaonyesha ni jinsi gani watu waovu wanavyopenda kuendelea na maovu yao bila kubughudhiwa.Lakini haiwezekani watu wenye uchungu na nchi yetu wawaachie kufanya ufisadi wao wapendavyo.Naamini kila mzalendo anaelitakia mema Taifa letu atahakikisha kuwa wanahabari wanaosimama kidete kuwafichua wala rushwa na wabadhirifu hawabughudhiwi hata kidogo.Mjenga nchi ni mwananchi na mvunja nchi ni mwanachi pia.Tukiendelea kuwalea hawa majambazi wa mali na haki zetu basi tujue kuwa sio tu tunajitengezea “future” mbaya bali pia vizazi vijavyo vitatuhukumu kwa kuwaachia watu wachache wasio na uchungu na nchi yetu kutuharibia mambo.Tukiamua kwa nia moja tunaweza kuwadhibiti majambazi hao.

Alamsiki.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.