13 Jan 2012


Waziri Magufuli ashughulikiwe

Kejeli ya kupiga mbizi
BAADA ya makala yangu katika toleo lililopita la gazeti hili ambapo nilijaribu kutabiri kuhusu masuala mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa mwaka huu 2012, nimepokea maoni kadhaa, hususan kuhusu utabiri huo kugusia masuala machache tu.
Kama nilivyobainisha katika makala hiyo, kugusia kila nyanja ya maisha kungehitaji makala zaidi ya moja. Na kutokana na ufinyu wa muda na nafasi, nilidhani ni vema kugusia maeneo machache tu ya muhimu.
Lengo la makala hii si kuendeleza utabiri huo bali ni mwendelezo wa mjadala kuhusu masuala muhimu kwa ustawi wa taifa letu.
Miongoni mwa matukio yanayoweza kutafsiriwa kama mwanzo mbaya wa mwaka huu ni sakata lililotokana na tangazo la Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, kuhusu nyongeza ya nauli katika kivuko cha Kigamboni.
Kilichozua sokomoko kubwa si ongezeko hilo bali kauli ya kihuni ya Waziri Magufuli kwamba “wasiomudu ongezeko la nauli hiyo wapige mbizi.”
Inasikitisha kuona mmoja wa watendaji wachache kabisa wa Serikali ambao wanaonekana kujali maslahi ya umma na taifa kwa ujumla, anaingia kwenye kundi la watendaji wengi ambao kauli zao zinaweza kabisa kutuaminisha kuwa ushirikiano kati ya ubongo wao na midomo yao ni haba kama sio sifuri kabisa.
Hivi Magufuli angepungukiwa na nini kama angetumia kauli za kistaarabu tu kwamba japo anasikia vilio vya watumiaji wa kivuko hicho kuhusu ongezeko hilo la nauli, kuna kila sababu ya uamuzi huo kubaki kama ulivyo.
Hakukuwa na haja ya kutumia lugha ya kebehi na dharau. Lakini kama lugha hiyo ya kihuni haitoshi, Waziri huyo msomi ameendeleza ubabe wake sio tu kwa kueleza kuwa hatojiuzulu wala kuomba msamaha, bali pia kuwashushia lawama nzito wabunge wa majimbo ya Jiji la Dar es Salaam.
Pengine ni muhimu kujiuliza Waziri Magufuli amepata wapi jeuri hii. Jibu rahisi ni kwamba huhitaji kuwa mchambuzi wa siasa za nchi yetu kubaini kuwa chanzo kikubwa cha jeuri na utendaji mbovu wa watendaji wengi wa serikali yetu ni kiongozi aliyewateua. Hapa ninamaanisha Rais Jakaya Kikwete.
Mwanzoni mwa mwaka 2006, muda mfupi baada ya kuingia madarakani kwa mara ya kwanza, Rais Kikwete alitoa hadhari kwamba tabasamu lake lisitafsiriwe vibaya.
Huku akiweka wazi kuwa anawafahamu wala rushwa kwa majina, Kikwete alitoadeadline kwa wala rushwa hao kujirekebisha vinginevyo wangemtaka ubaya. Kadhalika aliwaonya watendaji wanaozembea majukumu yao akisisitiza kuwa asingekuwa na huruma nao.
Miaka sita baadaye ni wazi kuwa ‘mkwara’ huo wa Kikwete ulikuwa ni kama sehemu ya kutimiza majukumu yake ya kusema chochote. Sio tu kwamba hakuna mla rushwa aliyezingatia deadline hiyo bali pia baadhi ya watendaji wake wamepata ujasiri kutokana na upole wa kupindukia wa ‘bosi’ wao ambaye yayumkinika kuhitimisha kuwa ni mwoga wa kutumia ipasavyo mamlaka yake aliyopewa na Katiba kuchukua hatua stahili dhidi watendaji wabovu.
Laiti Kikwete angekuwa ‘mkali japo kidogo’ kwa watendaji wake basi ni wazi Magufuli angefikiri mara mbili kabla ya kuwabwatukia watumiaji wa kivuko cha Kigamboni.
Ikumbukwe kuwa moja ya turufu muhimu kwa Kikwete wakati anagombea nafasi ya urais mwaka 2005 ilikuwa ni hoja kuwa ni ‘mtoto wa mjini’ na ni ‘mtu wa watu.’
Japo si lazima kila kiongozi awe ‘mtoto wa mjini’ lakini sifa hiyo inaweza kuwa ya msaada mkubwa kwa kiongozi kwani inamwezesha kuelewa mambo mbalimbali hata pasipo kutegemea taarifa mbalimbali anazoletewa na wasaidizi wake.
Naomba kusisitiza kuwa neno ‘mtoto wa mjini’ hapa limetumika kwa maana chanya likiashiria mtu anayelielewa Jiji la Dar es Salaam kwa marefu na mapana.
Kwa maana hiyo inatarajiwa kuwa Kikwete anafahamu fika kuwa kauli ya waziri wake Magufuli sio tu ni mithili ya matusi kwa wakazi wa Dar es Salaam wanaokitegemea kivuko cha Kigamboni kwa maisha yao, bali pia inatia mawaa kwa utawala wake.
Hivi ni vigumu kiasi gani kwa Rais Kikwete kumwita Magufuli na kumfahamisha kuwa lugha aliyotumia si nzuri, na anapaswa kuwaomba msamaha aliowatukana?
Hivi Rais hafahamu kuwa ukimya wake katika suala hili unaweza kutafsiriwa kama kumuunga mkono waziri wake au yeye kuwa na mtizamo kama wa Magufuli kuwa wasiomudu nauli hiyo wapige mbizi?
Japo Kikwete hakumtuma Magufuli kutoa kauli hiyo chafu lakini kwa vile ni yeye aliyemteua kushika wadhifa huo, na kwa vile kama ‘mtu wa watu’ anaelewa kuwa kauli ya waziri wake si nzuri, kwa nini basi ‘asijikongoje’ na kumsaidia mtendaji wake na kuisadia Serikali yake isionekane ina watendaji wanaopuuza vilio vya wananchi?
Kama nilivyoandika katika makala yangu kwenye toleo lililopita kuwa mwaka huu 2012 utaendelea kuwa wa machungu kwa Watanzania kwa vile moja ya kasoro za Rais wetu ni kusita kuchukua hatua za haraka pale mambo yanapokwenda mrama, hususan chanzo kinapokuwa mmoja wa watendaji wake.
Ukweli mchungu ni kwamba kama kauli ya kebehi ya Magufuli itaachwa kama ilivyo inaweza kuzalisha kasumba kwa viongozi wengine kuwatukana wananchi pasipo hofu ya kukemewa na aliyewapa nyadhifa husika.
Kwa upande mwingine siafikiani kabisa na sababu alizotoa Waziri Magufuli kuhusu ongezeko hilo la nauli. Kigezo kuwa nauli za awali ni pungufu kulinganisha na nauli katika vivuko vingine ni ya kipuuzi kwa sababu hata kama kiwango cha nauli katika kivuko kilichopo mkoani ingekuwa Sh. 500 lakini kinatumiwa na watu 200 kwa siku, kivuko cha Kigamboni kinatumiwa na watu wengi zaidi kiasi kwamba hata kiwango cha nauli cha Sh. 200 kwa watu 5,000 kwa siku kingezalisha fedha zaidi.
Kadhalika, hakuna uthibitisho wowote kuonyesha kuwa ongezeko hilo la viwango vya nauli kwa kivuko cha Kigamboni litaongeza mapato zaidi kwa Serikali kwani busara nyepesi tu inabainisha kuwa, kama mafisadi walimudu kuiba kidogo kilichopatikana kutokana na nauli ya awali, itakuwa rahisi zaidi kwao kuiba mapato yanayotarajiwa kupatikana kutokana na viwango vipya.
Kwa lugha nyingine, kama walikuwa wanaiba kila Sh. 50 katika nauli, sasa wataweza kuiba hata shilingi 100 katika kila nauli.
Tatizo la msingi linalokabili vyanzo vya mapato ya Serikali halijawahi kuwa katika viwango vidogo vya nauli au kodi bali usimamizi wa matumizi ya mapato hayo.
Yayumkinika kubashiri kuwa laiti mapato yanayopatikana kutokana na vivuko vyetu yangesimamiwa na kutumiwa vizuri, basi ndoto za ujenzi wa madaraja kwenye vivuko hivyo zingekuwa zimekwishatimia.
Nirejee kwa Rais Kikwete. Ninaamini anahesabu siku zilizosalia kabla muda wake wa kuwa madarakani haujafikia mwisho hapo mwaka 2015. Kwa hakika bado ana nafasi nzuri ya kuwafanya Watanzania wasahau (ambao kimsingi ni wepesi wa kusahau mabaya) upungufu wote unaoendelea kuufanya utawala wake kuwa dhaifu zaidi ya tawala zilizotangulia.
Lakini hata tukiweka suala hilo la kuwaachia wananchi kumbukumbu nzuri, Kikwete anaweza kuuthibitishia umma kuwa alipotoa hadhari kwamba tabasamu lake lisieleweke vibaya alikuwa serious na sasa ameamua kutafsiri hadhari hiyo kwa vitendo.
Anaweza kuanza na Magufuli; kama kumwambia ana kwa ana kutakinzana na huruma yake kwa watendaji wake basi anaweza kumfikishia ujumbe kupitia kwa makamu wake au waziri mkuu.
Amueleze kuwa ujumbe mzuri unaweza kusababisha matatizo makubwa kama hautowasilishwa kwa lugha ya kistaarabu.
Kwa upande mwingine, Rais Kikwete anaweza kujipatia umaarufu mkubwa iwapo atamwacha Magufuli na jeuri yake lakini akitumia mamlaka yake kama mkuu wa nchi na kubatilisha uamuzi wa waziri huyo kwa kurejesha nauli ya awali.
Na pengine baada ya kufanya hivyo, anaweza 'kufunga bao la kisigino’ kwa kutangaza kuwa uamuzi wa wabunge kujiongezea posho hauendani na hali halisi ya uchumi wetu na Serikali yake haina fedha za kumudu mahitaji yao ya kifahari.
Sababu ya kuchukua uamuzi wa aina hiyo anazo, na mamlaka aliyonayo yanampa uwezo wa kufanya hivyo. Kinachohitajika ni nia tu ya kufanya hivyo.
Laiti akizingatia ushauri huu na kufanya hivyo, sio tu Watanzania wengi watarejesha imani kuwa ‘Kikwete ni mtu wa watu’ bali hata wale waliosema yeye ni chaguo la Mungu wanaweza kupata ujasiri wa kurejea kauli hiyo (kwa vile kiongozi ambaye ni chaguo la Mungu hawezi kulea mafisadi, viongozi wazembe na hao wenye kauli za kebehi kama ya Magufuli).


5 Jan 2012



2012, mwaka wa chuki za kisiasa, kiuchumi

CCM, Upinzani ishara si njema
Nchi tajiri kuiyumbisha Tanzania
NIANZE makala hii ya kwanza kwa mwaka huu kwa kupigia mstari pointi mbili za msingi. Kwanza, kama nilivyokwishawahi kubainisha huko nyuma, katika kujiingiza kwenye fani ya uandishi magazetini, niliwahi kuwa na safu ya “unajimu wa kisanii” katika baadhi ya “magazeti pendwa” (jina la kistaarabu la magazeti ya udaku).
Ninauita unajimu wa kisanii kwa vile haukubeba ukweli wowote bali lengo lilikuwa kuburudisha tu. Kwa mfano, katika moja ya safu zangu nilibashiri yafuatayo:
Wiki hii itatawaliwa na mkosi utakaokuletea neema. Mwanao atagongwa na gari la ubalozi wa nchi moja tajiri. Usipaniki kwa vile mwanao atapona. Na hapo ndipo neema itakapokuangukia. Licha ya kugharamia matibabu ya mwanao, ubalozi huo utampatia viza ya kwenda kuishi katika nchi hiyo ya ahadi. Angalizo: usimkataze mwanao kucheza barabarani.”
Ni “upuuzi” wa aina hii ndio uliowasukuma rafiki zangu waliokuwa kwenye medani ya uandishi wa habari kunishauri kujikuta kwenye uandishi wa makala za “mambo ya msingi”, hoja yao kubwa ikiwa kama ninamudu kuandika “nyota za kisanii” na kuburudisha jamii, basi inawezekana nikaandika makala za masuala muhimu za kuelimisha, kukosoa na kuhabarisha.
Ushauri huo ndiyo kiini cha “kifo cha safu za unajimu za Ustaadh Bonge (jina nililojipachika kuendana na suala zima la ‘unajimu’ huo).”
Nimegusia suala la utabiri kwa vile makala hii inalenga kubashiri masuala na matukio mbalimbali katika mwaka huu mpya. Tofauti na unajimu wa Ustaadh  Bonge kwenye “magazeti pendwa” ya SanifuKasheshe na Komesha, utabiri huu ni makini na unazingatia mwenendo wa mambo katika mwaka uliopita, sambamba na ufahamu wangu wa kitaaluma na binafsi.
Pointi ya pili inawahusu watu wawili maarufu kwenye medani ya siasa za Marekani. Wa kwanza ni Profesa Larry Sabato, mwanasayansi ya siasa (political scientist), mchambuzi wa siasa na Mkurugenzi wa Kituo cha Siasa katika Chuo Kikuu cha Virginia.
Sabato ni maarufu kwa utabiri wake katika chaguzi kuu nchini Marekani. Tovuti yake ya Sabato’s Crystal Ball huchambua duru za siasa za nchi hiyo na kutabiri matokeo ya uchaguzi wa wawakilishi, maseneta na urais. Kinachosababisha msomi huyo na tovuti yake kuwa muhimu ni usahihi mkubwa wa utabiri husika.
Mtu mwingine ni Paul Begala, gwiji la mikakati ya siasa (political strategist) na mshauri wa zamani wa aliyekuwa Rais wa Marekani, Bill Clinton. Pamoja na mshiriki wake wa karibu James Carville, Begala ambaye pia ni Profesa wa utafiti (research professor) katika sera za umma (public policy) katika Chuo Kikuu cha Georgetown, waliwezesha ushindi wa Rais Clinton katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1992, sambamba na kumwezeshea ushindi wa maseneta kadhaa.
Nimewataja Sabato na Begala kwa sababu, kwanza, hao ni role models (mifano ya kuigwa) kwa upande wangu, na pili, wote ni mahiri katika utabiri wa siasa za Marekani, hususan kwenye chaguzi.
Sasa tuangalie utabiri wangu wa mwaka 2012, hususan kwenye medani ya siasa (za kimataifa na huko nyumbani-Tanzania) na maeneo mengine muhimu.
Nitagusia maeneo machache yenye umuhimu zaidi kwa vile ni vigumu kuzungumzia kila eneo la maisha katika makala moja.
Siasa za kimataifa
Tukianza na siasa za kimataifa, mwaka huu unatarajiwa kutawaliwa zaidi na kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu nchini Marekani, Rais Barack Obama atakuwa anajaribu kupata ridhaa ya kuongoza taifa hilo kubwa duniani kwa muhula wa pili.
Obama, Mmarekani mweusi wa kwanza kuwa rais wa nchi hiyo anatarajiwa kukumbana na upinzani mkali kutoka kwa mgombea wa chama cha Republican (ambaye hajafahamika hadi sasa).
Kwa kuzingatia uchambuzi wa watu mbalimbali na kwa kadiri ninavyofuatilia siasa za Marekani, dau (bet) langu ni ushindi “kiduchu” kwa Obama dhidi ya Mitt Romney, mgombea ninayetabiri atapitishwa na Republican (iwapo upepo wa kisiasa hautabadilika).
Turufu kubwa kwa Obama ni kupendwa (likeability) kwake dhidi ya mgombea mwingine yeyote. Hata hivyo, busara za siasa zinatanabaisha kwamba, mwanasiasa anayependwa lakini hamudu kazi yake vyema anaweza kung’olewa madarakani.
Lakini ili Obama ashinde inategemea sana mwenendo wa uchumi wa nchi hiyo ambao kwa sasa ni mbaya (japo si kosa la moja kwa moja kwa Rais huyo).
Obama aliingia madarakani huku Marekani ikiwa kwenye hali mbaya ya kiuchumi, na kwa namna fulani kuna mtizamo kuwa ingehitajika miujiza kwa yeye kuboresha uchumi huo katika kipindi cha miaka minne aliyokuwa madarakani.
Turufu nyingine kwa Obama ni kile kinachoweza kuiangamiza CCM mwaka 2015, yaani kukosekana kwa mwafaka wa jumla katika kumuunga mkono mgombea urais kwa tiketi ya Republican.
Hadi sasa, hakuna mwanasiasa miongoni mwa waliokwishajitokeza kuwania nafasi hiyo anayeonekana kuungwa mkono vya kutosha ndani na nje ya chama.
Na kwa vile urais si suala la majaribio, Obama anaweza kuwa salama zaidi kwa kigezo cha “jini likujualo” nikimaanisha angalau Wamarekani wanafahamu ubora na udhaifu wake kuliko kubahatisha kwa mgombea wasiyemjua kwa namna hiyo.
Naomba kusisitiza kuwa lolote linawezekana katika siasa. Iwapo hali ya uchumi wa Marekani itazidi kudhoofika, basi nafasi ya Obama kurejea Ikulu ya nchi hiyo itazidi kuwa finyu.
Ikumbukwe kuwa tofauti na huko nyumbani, wenzetu huku Magharibi hawapendi mambo ya ‘bora liende’ ni kwamba kama mtu ameshindwa kazi basi awajibishwe.
Kwa ufupi, utabiri mwingine kwenye duru za kimataifa ni uwezekano wa Marekani kuishambulia kijeshi Iran (hasa ikizingatiwa kuwa kufanya hivyo kutampa Obama nafasi nzuri ya kushinda uchaguzi utakaofanyika Novemba, mwaka huu).
Shambulizi hilo linaweza pia kuijumuisha Israel ambayo inaitazama Iran kama tishio kwa ustawi wake.
Jingine ni uwezekano wa kuanguka kwa utawala wa Rais Bashir al-Asad wa Syria, sambamba na uwezekano wa machafuko makubwa zaidi ya kidini Nigeria.
Hali ya uchumi wa dunia itaendelea kuwa fyongo huku nchi masikini kama Tanzania zikiguswa na domino effect (zahama) ya kinachojiri katika nchi wafadhili.
Ndani ya CCM
Kwa huko nyumbani (Tanzanaia), ninatabiri kuwa siasa zetu zitatawaliwa zaidi na kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa chama tawala, CCM.
Japo kila mmoja wetu angetamani kuona uozo, ubabaishaji na ufisadi uliotawala mwaka 2011 unapungua kama si kufutika kabisa, kwa bahati mbaya (au kwa makusudi) dalili zinaashiria kuwa wanasiasa wetu wakiwamo wa CCM, wapo madarakani kwa ajili ya maslahi yao, na hakuna njia mwafaka ya kudumisha nafasi zao zaidi ya kuwa na nyadhifa ndani ya chama.
Kwa hiyo, tutarajie kuona wanasiasa wa CCM wakipigana vikumbo kuhakikisha wao au wagombea wanaowaunga mkono wanashinda katika uchaguzi huo.
Ikumbukwe kuwa uchaguzi huo una umuhimu wa kipekee kwa wanasiasa wanaotamani urais kupitia CCM katika Uchaguzi Mkuu, 2015 kwa vile hiyo ni nafasi mwafaka kwao kutengeneza “timu ya ushindi.”
Wakati Uchaguzi Mkuu wa CCM usingepaswa kuwaathiri wananchi wengine wasioshabikia chama hicho, mfumo mbaya wa kiuongozi ambao, Serikali kuanzia ngazi ya taifa hadi wilaya inaendeshwa zaidi kisiasa (wakuu wa mikoa na wilaya kuteuliwa kutokana na ukada wa CCM, sambamba na wao kutumia muda mwingi kwenye shughuli za chama, bila kusahau malengo yao binafsi ya kisiasa), harakati za kusaka uongozi ndani ya chama tawala zinatarajiwa kuwaathiri Watanzania wote.
Viongozi wengi wa Serikali katika ngazi zote wanatarajiwa kutumia muda mwingi kujihusisha na uchaguzi huo kuliko kutekeleza majukumu yao kwa umma.
Kambi ya Upinzani
Kwa upande wa siasa za upinzani, kuna uwezekano mkubwa wa “vita ya wenyewe kwa wenyewe” na dalili ni dhahiri ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) na NCCR-Mageuzi, hasa baada ya vyama hivyo kumaliza mwaka 2011 kwa kutishiana na kufukuzana.
Wakati vita vya panzi vinapaswa kuwa sherehe kwa kunguru (kwa maana ya migogoro ndani ya CUF na NCCR kuwanufaisha CCM na CHADEMA), kuna uwezekano, CCM kunufaika zaidi kuliko CHADEMA.
Kimsingi, mwanasiasa wa upinzani akihamia CCM hawezi kukiyumbisha chama hicho katika namna ya akina John Shibuda alivyogeuka “maumivu” kwa CHADEMA.
Ili wasikumbwe na vurugu kama zinazoendelea kwa wenzao, CHADEMA wajiepushe kudaka kila “korokoro la kisiasa” linalowajia baada ya kufukuzwa au kunyimwa nafasi katika chama kingine.
Hali ya uchumi
Nimalizie kwa kutabiri hali ya uchumi na maisha kwa ujumla. Kwa kusikiliza hotuba ya mwisho wa mwaka ya Rais Jakaya Kikwete, ni dhahiri mwaka huu utaendelea kuwa mchungu kwa walalahoi.
Katika hotuba hiyo ya kisiasa, Kikwete hakujihangaisha kuwapa matumaini Watanzania kuwa anaelewa hali yao ngumu ya maisha (na akatoa takwimu za kukua kwa uchumi), akikwepa kuzungumzia wimbi la ufisadi.
Japokuwa aligusia tatizo la uhalifu ambalo anadai limepungua, lakini inaelekea kwake ufisadi si uhalifu na ndiyo maana aliwahi kutetea haki za binadamu za mafisadi.
Haihitaji upeo wa akina Sabato au Begala kubashiri kuwa tutaendelea kushuhudia mafisadi wakigeuza nchi yetu kuendelea kuwa shamba la bibi, huku Rais akiendeleza huruma kwa watuhumiwa wa ufisadi (na alihitimisha mwaka 2011 kwa picha yenye tabasamu akiwa na Katibu Mkuu (mstaafu) Philemon Luhanjo, ambaye dalili zinaashiria ameruhusiwa kustaafu kwa heshima - kama ilivyokuwa kwa aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Johnson Mwanyika, licha ya kudaiwa kuhusika kwenye tuhuma za ufisadi). Kila la heri kwa mwaka huu mpya 2012.


2 Jan 2012

Magufuli achafua hali ya hewa Dar Send to a friend
Sunday, 01 January 2012 22:20

Waziri wa ujenzi Dk John Magufuli

BAADA YA KUWAAMBIA WAKAZI KIGAMBONI WAKISHINDWA KULIPA NAULI MPYA ZA VIVUKO WAPIGE MBIZI

Ramadhan Semtawa
WAZIRI wa Ujenzi, Dk John Magufuli amechafua hali ya hewa na kuingia kwenye mgogoro na wakazi wa Kigamboni, Dar es Salaam baada ya kuwaeleza kuwa ni lazima walipe nauli mpya za vivuko vya Mv Kigamboni na Alina na kama watashindwa, wapige mbizi baharini kuvuka.

Kauli hiyo ya Dk Magufuli imekuja siku mbili baada ya wizara hiyo kutangaza viwango vipya vya nauli mnamo Desemba 29, mwaka jana ambavyo vimepanda kwa asilimia 100 na vilianza kutumika jana Januari Mosi nchi nzima.

Baada ya kutangazwa kwa viwango hivyo vipya vya nauli, wakazi wengi wa Kigamboni walipinga kutokana na kile wanachosema hawakushirikishwa na ndipo jana asubuhi, Dk Magufuli alipoamua kufanya ziara ya ghafla katika vivuko hivyo na kusisitiza kwamba viwango hivyo lazima vilipwe.

Katika ziara hiyo, vyanzo vya kuaminika vilisema Dk  Magufuli alipofika eneo hilo la Kivukoni, alitoa msimamo huo na ndipo wananchi waliokuwa wakimsikiliza walipoanza kumzomea na kukatisha hotuba yake mara kwa mara.

Vyanzo hivyo viliongeza kwamba, kitendo hicho cha zomeazomea, kilimkera Dk Magufuli ambaye pamoja na mambo mengine, alisisitiza nauli hizo lazima zilipwe na mtu asiyetaka ni vyema akapiga mbizi kwa kuogelea kutoka Kigamboni hadi ng'ambo ya pili au apite Kongowe kuingia katika katikati ya jiji.

Msemaji: Waziri amechukizwa
Akizungumzia tukio hilo, Msemaji Mkuu wa wizara hiyo, Martin Ntemo alisema Waziri Magufuli hakufurahishwa na kitendo cha baadhi ya watu kumzomea wakati alipokuwa akizungumza... “Amechukizwa na baadhi ya watu kuzomea wakati alipokuwa akizungumza. Alichokuwa akisisitiza ni kwamba nauli mpya lazima ilipwe lakini wapo waliokuwa hawataki kuelewa wakawa wanapinga.”

Alisema kuna watu walikuwa wamepangwa kufanya mgomo kupinga nauli mpya kitendo ambacho pia kilimkera waziri alipokuwa kwenye ziara hiyo.


Magufuli na waandishi

Baada ya kuzomewa Kigamboni, Dk Magufuli alifanya mkutano na waandishi wa habari na kusisitiza kwamba, “Kuanzia Januari, Mosi, mwaka huu Wizara ya Ujenzi kupitia Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa), imeongeza viwango vya nauli katika vivuko vyote vya Serikali nchini.”

Alisema kwa muda wa miaka 14 iliyopita Kivuko cha Kigamboni kimekuwa kikitoza nauli ya Sh100 kwa mtu mmoja, wakati vivuko vingine vyote nchini, vimepandisha nauli zaidi ya mara mbili tangu mwaka 1997 kuendana na gharama za uendeshaji.

“'Kwa mfano, Kivuko cha Pangani ambako umbali wa uvushaji hauzidi ule wa Magogoni kilikuwa kinatoza Sh 200 na hali ya uchumi kwa wananchi ni ya chini kuliko Dar es Salaam. Kivuko cha Kilombero kilikuwa kikitoza Sh200 ikilinganishwa na Sh100 zilizokuwa zikitozwa hapa Magogoni.” 

Dk Magufuli alitaja sababu zilizochangia kupandisha nauli hizo kwamba ni pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi serikalini kwa zaidi ya asilimia 100, ongezeko alilosema la zaidi ya asilimia 400 la bei ya mafuta ya dizeli na mafuta ya kulainishia mitambo ambayo hutumika kuendeshea vivuko hivyo. 
Alitaja sababu nyingine kwamba ni pamoja na: “Ongezeko la bei za vipuri na kodi zake linalowiana na kushuka kwa thamani ya shilingi na ongezeko la bei kwa jumla.”

Alisema upandishaji wa nauli hizo ulifanywa kwa kuzingatia taratibu za kisheria na hatimaye kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali toleo Na. 367 la Novemba 4, mwaka jana kwa mujibu wa sheria za uendeshaji wa vivuko vya Serikali.

“Sura 173 Kifungu cha 11(b), mwenye mamlaka ya kupanga nauli za vivuko vya Serikali ni Waziri mwenye dhamana na vivuko vya Serikali. Hata hivyo, kabla ya kufikia uamuzi huu, kumekuwa na jitihada za aina mbalimbali katika kuimarisha mapato ya vivuko. Machi, 2009, Wakala wa Ufundi na Umeme wakishirikiana na  
Jeshi la Polisi pamoja na Askari kutoka Kikosi cha Wanamaji waliendesha zoezi la kudhibiti mapato ya Kivuko.”

Alisema hilo liliwahi kufanywa na na Kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart mnamo Aprili 17 hadi 20, mwaka jana kwa makubaliano na Temesa. “Zoezi hilo liliendeshwa tena Septemba 16 hadi 20, 2010 na 
Wizara kwa ushirikiano na Jeshi la Polisi.”

Alisema Julai, 2011, Temesa iliamua kubadili wakata tiketi na kuajiri wengine akisisitiza kuwa Serikali imechukua hatua mbalimbali kupambana na matukio ya watumishi wasio waaminifu. Hatua nyingine ni ile ya Temesa  kuondoa askari wa kuajiriwa na badala yake kuingia mikataba na kampuni za ulinzi.

“Kwa sasa katika Kivuko cha Magogoni, Kampuni ya ulinzi ya Suma JKT ndiyo inayotumika kufanya kazi hiyo,” alisema.

Alisema juhudi hizo zimesaidia kuongeza mapato kwa siku kutoka Sh5.5 milioni mwaka 2009 hadi Sh9 milioni kwa sasa katika Kivuko cha Magogoni na kusisitiza kwamba wizara itaendeleza hatua hizi kwa lengo la kubana uvujaji wa mapato na matumizi yasiyo ya lazima kwa vivuko vyote. 

Magufuli alisema kwa utaratibu, watumiaji wote wa huduma za vivuko wanatakiwa walipie huduma hiyo na kuongeza: “Tunaomba utaratibu huu uzingatiwe isipokuwa kwa wanafunzi waliovaa sare za shule. Tunasisitiza watumiaji wa vivuko waheshimu sheria na taratibu zote za vivuko kwa ajili ya usalama wao na ufanisi wa huduma.”



Mbunge achukizwa

Kwa upande wake Mbunge wa Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile alikiri kusikia maneno ya Magufuli ambayo hayakuwafurahisha wapiga kura wake na kuahidi kuendelea kufuatilia kujua undani hasa wa kauli hizo. 

Dk Ndugulile alifafanua kwamba baada ya tangazo hilo la ongezeko la nauli, aliwasiliana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki na taarifa alizonazo ni kwamba nauli hizo zimesitishwa.

Alifafanua kwamba baada ya kuwasiliana na waziri mkuu, jibu alilopata jana saa 1: 00 usiku ni kwamba mpango huo wa kupandisha nauli umesitishwa hadi hapo itakapoamuliwa vinginevyo.

Dk Ndugulile alisema sababu zilizomfanya yeye na wananchi kupinga nyongeza hiyo ya nauli ni Serikali kushindwa kueleza wazi vigezo vilivyotumika na kushindwa kuwashirikisha wananchi wa maeneo husika. Alitoa mfano wa Bajaji ambao alisema ni usafiri wa wanyonge uliokuwa ukitozwa Sh300 lakini kwa viwango hivyo vipya, itavushwa kwa Sh1,300 huku baiskeli ya miguu mitatu inayotumiwa na wanyonge pia kuchukulia bidhaa kutoka Kariakoo ikiongezewa nauli kutoka Sh200 hadi Sh1,800 na gari ndogo sasa zinatakiwa kulipa Sh1,500 badala ya Sh800.

“Sasa angalia hivyo vigezo, utaona mwananchi wa kawaida amezidi kuumizwa. Leo hii tayari bei za bidhaa zinazoletwa Kigamboni kutoka sokoni kama Kariakoo kwa kutumia maguta zimepanda. Mtu mwenye gari anapadishiwa bei chini ya mwenye guta, vigezo gani hivi? Baada ya kuona hivyo, niliwasiliana na Waziri Mkuu Ijumaa (Desemba 30, mwaka jana) na jana Mkuu wa Mkoa akanipa jibu kwamba Waziri Mkuu kasema nauli hizo zisipandishwe kwanza. Kwa hiyo mimi na wananchi wangu tunajua hivyo,” alisema na kuongeza:

“Hili ni jambo la ajabu sana. Yaani Waziri Mkuu anasema hivi halafu waziri wake anafanya vingine! Uko wapi sasa utendaji kazi wa pamoja wa Serikali?”


Baadhi ya wananchi wamelaani kauli hiyo za Dk Magufuli wakisema haikupaswa kutolewa na waziri ambaye ana dhamana ya kuhakikisha matatizo ya wananchi yanatatuliwa. Mmoja wa wakazi wa Kigamboni aliyejitambulisha kwa jina la Hamis Bwamkuu alisema: “Waziri anatoa kauli za kejeli namna hii! Ametusikitisha sana na kwa kweli tunamuomba Rais Jakaya Kikwete amchukulie hatua za kinidhamu.”

Pia wananchi hao wamemshutumu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Dk Hurbet Mrango na Temesa kwa kushindwa kuwashirikisha na pia kumshauri vibaya waziri katika jambo hilo. 

"Katibu Mkuu ndiye mtendaji na Temesa wao ndiyo wakala lakini hawakumwambia kwamba wananchi hawakujua na hata mbunge wetu. Kwa hiyo hawa ni sehemu ya tatizo na hii si mara ya kwanza.”

1 Jan 2012


31 Dec 2011


Kikwete's smile says it all
Vyombo mbalimbali vya habari leo vimebeba picha ya Rais Jakaya Kikwete akiwa na Katibu Mkuu Kiongozi mpya,Balozi Ombeni Sefue na mtangulizi wake Philemon Luhanjo ambaye amestaafu.Sidhani kama kuna Mtanzania asiyefahamu uhusika wa Luhanjo katika sakata la ufisadi uliofanywa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini,David Jairo.Bunge lilishamshauri Kikwete awawajibishe wahusika wote wa ufisadi huo,ikiwa ni pamoja na Jairo na Luhanjo.

Lakini kama ilivyokuwa katika sakata la ufisadi wa Richmond ambapo Bunge lilishauri wahusika wachukuliwe hatua,lakini tukaishia kuona watu kama aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Johnstone Mwanyika walistaafu kwa heshima (bila kusahau marupurupu ya kustaafu),Kikwete amerejea tena udhaifu wake kwa kumwogopa Luhanjo na hatimaye kumwokoa kwa kumruhusu astaafu badala ya kumwadhibu kwa ufisadi wake na Jairo.

Kwa vile leo ni siku ya mwisho kwa mwaka huu 2011,picha ya Kikwete na Luhanjo ni kama kuwakumbusha Watanzania jinsi Rais wao alivyo dhaifu na mbabaishaji wa hali ya juu katika kushughulikia ufisadi.Na japo wengi wenu mtajipa matimaini kuwa mwaka 2012 utakuwa wa matumaini,ukweli mchungu ni kwamba kwa mwenendo huu wa Kikwete kuwaogopa na kuwalea mafisadi,viumbe hao hatari watazidi kuzaliana kwani wanajua fika hakuna wa kuwadhibiti au kuwaadhibu.

Samahani Mheshimiwa Rais,lakini uzembe wako katika kuwashughulikia mafisadi ni sawa na tusi kwa taasisi takatifu ya Urais.Ni lini utaamka na kuyatumia madaraka yako ipasavyo kupambana na ufisadi?

Salama zangu za mwaka mpya kwako si za kupendeza kwani namwomba Mungu aharakishe siku ili umalize muhula wako na ubaki historia isiyo na manufaa kwa Watanzania.Can't wait to see you gone!

29 Dec 2011




Tatizo Serikali au wanaoishi mabondeni?

Maafa ya mafuriko Dar
Mafuriko Dar es Salaam
Mafuriko Dar es Salaam
NIANZE kwa kutoa pole kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kutokana na janga la mafuriko ya wiki iliyopita. Inasikitisha kuona tunamaliza mwaka 2011 kwa majonzi, badala ya furaha (hata kama tuna vitu vichache vya kufurahia).
Kwa hakika si jambo jema kutumia janga kama hili kunyoosheana vidole, hususan katika kipindi hiki ambacho hata hatujafahamu kiwango cha athari kilichosababishwa na mafuriko hayo.
Hata hivyo, tunaweza kuendelea kusononeka na kuomboleza milele lakini pasipo kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha kuwa huko mbele tunajiandaa ipasavyo kukabiliana na majanga kama haya basi ni dhahiri tunaweza kujikuta tena katika hali kama hii inayotukabili sasa.
Ni ukweli usiofichika kuwa nchi yetu inaendeshwa kwa mtindo wa zimamoto. Tunasubiri litokee balaa kisha watawala wetu wapite huku na kule wakijifanya kuguswa na kusononeshwa na maafa yaliyowakumba watawaliwa.
Jiji la Dar es Salaam kama yalivyo maeneo mengine ya nchi yetu ni kama bomu linalosubiri kulipuka. Japo mafuriko ni janga la asili kwa maana hakuna namna ya kuyazuwia, kwa hakika kuna njia kadhaa za kujiandaa kukabiliana nayo na hata kupunguza madhara yake.
Kimsingi haya si mafuriko ya kwanza kuwakumba wakazi wa Jiji la Dar es Salaam au kusababisha madhara katika sehemu nyingine nchini.
Tofauti na mafuriko yaliyotangulia ni kiwango cha madhara ambacho yayumkinika kuhisi kwamba inaweza kuwa vigumu kufahamu kutokana na uzembe, ubabaishaji na kutowajibika ipasavyo kwa wahusika.
Janga hili la mafuriko jijini Dar es Salaam limeibua tena mjadala wa miaka nenda miaka rudi kuhusu makazi ya mabondeni. Swali ambalo limejitokeza katika mijadala mbalimbali ni nani alaumiwe kati ya Serikali na wakazi wa mabondeni.
Pengine cha muhimu si lawama bali kuangalia chanzo na utatuzi wa tatizo hili ambalo likiachwa liendelee litasababisha vilio vingine huko mbele (hata kama tunaombea isiwe hivyo).
Ni rahisi kuwalaumu wakazi wa mabondeni kwa hoja dhaifu kama “nani awalazimishe kuhama mabondeni kama wenyewe hawataki au hawajali maisha yao?”
Unaweza kutoa lawama hizo kirahisi kama hujui ugumu wa kupata sehemu ya kuishi jijini Dar es Salaam, achilia mbali ugumu wa kupata kiwanja cha kujenga nyumba mpya.
Ripoti kadhaa kuhusu utawala bora zimekuwa zikizitaja mamlaka za ardhi kama kiongozi wa muda mrefu katika rushwa. Na kama inavyoeleweka, waathirika wakubwa wa rushwa ni walalahoi wasio na uwezo wa kuhonga. Sitaki kabisa kuamini kuwa wakazi wa mabondeni wanaendelea kuhatarisha maisha yao katika maeneo hayo kwa vile wanapenda iwe hivyo.
Nani asiyeogopa kifo? Nani anayetaka kuishi sehemu ambayo kufikika kwake hata wakati wa kiangazi ni kwa shida? Nani anayependa kukaa eneo ambalo mvua kidogo tu ikinyesha basi inaweza kusababisha wakazi wa eneo husika kujifungia ndani kutwa nzima au usiku kucha kwa vile kila eneo limejaa maji?
Hawa ni watu wanaohitaji kusaidiwa. Lakini kwa vile sote tunajua kuwa si Serikali kuu wala mamlaka za Jiji zinazoguswa kwa dhati na tatizo hili, ni muhimu kuwaelimisha wakazi hao kudai haki zao za kibinadamu kuhusu makazi bora na usalama wa maisha yao kwa ujumla.
Mwaka unamalizika na janga hili la mafuriko, na japo nisingependa kuwa “nabii wa majanga” (prophet of doom) yayumkinika kubashiri kuwa safari yetu huko mbele si salama. Ni wazi kuwa laiti yakitokea mafuriko mengine iwe Dar es Salaam au kwingineko nchini, tutarejea katika hali hii ya huzuni na majonzi kwa vile mfumo wa kuzuia na kukabiliana na majanga ni sifuri.
Viongozi wetu ni wepesi kumbebesha Mungu mzigo wa lawama kwa kauli maarufu ya “ni mapenzi ya Mungu.” Kuna nyakati ninatamani Mungu apandwe na hasira na kuwaumbua viongozi wa aina hiyo kwa umma kwa yeye (Mungu) kujivua lawama hizo na kuwafumbua macho watawaliwa waelewe kuwa tatizo ni watu waliopewa jukumu la kuongoza lakini wasiotekeleza jukumu hilo ipasavyo.
Kuna janga jingine kubwa la kiuchumi. Kwa sisi tunaoishi kwenye nchi kama Uingereza ambayo ni miongoni mwa wafadhili wakubwa wa Tanzania tunaona kila dalili kuwa muda si mrefu wanaweza “kubwaga manyanga” kusaidia nchi masikini na kuelekeza nguvu kwenye kujisaidia wao wenyewe.
Hali ya uchumi wa dunia ni mbaya sana lakini pengine kinachoweza kusababisha msione hivyo huko nyumbani ni ukweli kwamba hali huko ni mbaya karibuni kila siku.
Sasa kama hali ni mbaya wakati huu ambapo wafadhili wanaendelea kumwaga misaada yao (huku sehemu kubwa ya misaada hiyo ikiishia kwenye mifuko na akaunti za mafisadi), ni wazi kuwa hali itakuwa mbaya zaidi pindi wafadhili hao wakilazimika kupunguza au kukata kabisa misaada hiyo.
Tofauti na mafuriko ambayo ni janga la asili (natural disaster), tatizo hili la uchumi ni la kibinadamu. Na wakati wenye jukumu la kujiandaa na kukabiliana na majanga ya asili wanaweza kuwa na kisingizio kwamba “sie ni masikini sana kumudu kuwa tayari muda wote kujiandaa na kukabiliana na majanga ya asili,” kwenye tatizo hili la uchumi hakuna kisingizio hasa kwa vile tuna raslimali za kutosha za kujiandaa kukabiliana na mtikisiko wa uchumi wa dunia.
Wanasema “kufa kufaana.” Janga hili la mafuriko linaweza kutoa nafasi nzuri kwa watawala wetu kukwepa kutueleza kwa nini tupo katika hali mbaya kiasi hiki katika kipindi hiki tunachoelekea mwisho wa mwaka huku ikiwa ni siku chache tu baada ya kuadhimisha miaka 50 ya uhuru wetu.
Watawala wamepata kisingizio cha “tupo kwenye kipindi cha majonzi na si vema kuanza kunyoosheana vidole kuhusu masuala mengine.” Na kwa vile Watanzania wengi sio tu ni wepesi wa kusahau lakini pia hawapendi kuunganisha mlolongo wa matukio (chain of events) basi ni wazi kuwa janga hili la mafuriko litawanusuru watawala wetu kutupatia majibu kuhusu matatizo mengine mengi ambayo pasi na shaka tutaingia nayo mwaka ujao 2012.
Sawa, kwa sasa tunapaswa kufanya kila linalowezekana kuwasaidia Watanzania wenzetu walioathirika kwa mafuriko. Lakini wakati tunafanya hivyo ni lazima tutambue kuwa laiti tungepata ufumbuzi wa matatizo yaliyokuwepo kabla ya janga hili la mafuriko ni wazi kuwa pindi wahanga hao wakishasaidiwa hawatakuwa na hofu nyingine za kukabiliana na matatizo hayo “ya kudumu.”
Tunamaliza mwaka huku Ripoti ya Bunge kuhusu sakata la akina Jairo likiwa limenyamaziwa na Rais Jakaya Kikwete. Katibu Mkuu Kiongozi Philemon Luhanjo bado hajachukuliwa hatua kama ilivyo kwa Waziri William Ngeleja na Naibu wake, Adam Malima, sambamba na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovic Utoh.
Hivi Kikwete haelewi kuwa katika mazingira ya kawaida tu uwepo madarakani wa watu hawa unaweza kusababisha madhara makubwa zaidi ya hayo yaliyosabisha Bunge liwachunguze?
Hapa ninamaanisha kuwa kwa vile wahusika hawa wanaweza kujiona wapo “mguu ndani, mguu nje” basi ni bora “wachukue chao mapema” kabla hawajawajibishwa.
Tunamaliza mwaka huku ahadi zilizozoeleka za Rais Kikwete kuhusu utatuzi wa tatizo sugu la umeme zikiendelea kuwa ahadi hewa. Mwaka unaelekea ukingoni lakini ahadi ya Rais kuwa ifikiapo mwezi huu Desemba, mpango wa dharura wa kuongeza nishati ya umeme (megawati 572) katika gridi ya taifa ungekamilika inabaki kuwa ndoto ya alinacha.
Mpango huo wa Serikali uliowasilishwa bungeni mwezi Agosti, mwaka huu ulieleza kuwa kati ya megawati hizo, 150 zilikuwa zizalishwe kupitia makubaliano kati yake na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Mgawanyo wa megawati hizo ulionyesha kungeingizwa megawati 50 kwa kila mwezi, kati ya Septemba na Desemba 2011.
Hadi sasa hakuna hata megawati moja ya umeme iliyozalishwa na NSSF na taarifa zinaonesha kuwa mamilioni ya fedha za umma yamepotea kwa “safari za kutalii” kwenda Marekani na Ufaransa “katika mchakato huo” lakini mgawo wa umeme unazidi kudumisha makali yake.
Nimalizie makala hii kwa kurejea pole zangu kwa waathirika wa mafuriko ya Dar es Salaam, sambamba na kuwatakia wasomaji wote wa Raia Mwema na makala hii heri ya mwaka mpya 2012.
Wakati mwaka huu 2011 unamalizika huku tukiwa na mengi ya kulalamikia kuliko kupongeza au kujidai nayo, ninaomba kutoa wito kwa kila Mtanzania mwenye uchungu na nchi yetu kuukaribisha mwaka mpya kwa kauli ya “Enough is enough”(Imetosha); aidha tuendelee kuwaruhusu viongozi wazembe na mafisadi waipeleke nchi shimoni au tusimame kidete na kudai haki zetu za msingi za kuwa na maisha bora na salama.
Kama alivyowahi kutuasa aliyepata kuwa Waziri wa Fedha wakati wa Awamu ya Pili, Marehemu Profesa Kighoma Ali Malima (namnukuu); “haki haitolewi kama zawadi. Haki hudaiwa, hata kwa nguvu inapobidi.” (Atakayeniita mchochezi kwa nukuu hii lazima atakuwa fisadi asiyetaka kuona Watanzania “wanaamka”).
Mkoloni hakuondoka kwa vile tulikuwa tunanung’unika, Nduli Idi Amin hakuacha uharamia wake kwa vile tulimwita kila jina baya. Kilicholeta mwisho wa udhalimu wa mkoloni na Amin ni harakati za dhati za kukomesha maovu yao.
Manung’uniko na majina mabaya kwa mafisadi na wazembe hayawezi kutuletea “ukombozi” wetu. Kinachohitajika ni mwamko na jitihada za dhati za kukomesha uharamia huo.
Heri ya mwaka mpya  2012.


Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.