13 Oct 2013


NIANZE makala hii kwa pongezi zangu za dhati kwa Ubalozi wetu nchini Kenya ambao juzi ulitangaza kuwa umejiunga na mtandao wa kijamii wa Twitter. Kadhalika, naushukuru ubalozi huo kwa heshima waliyonipatia kwa ‘kunitwiti’ kuhusu habari hiyo njema.
Lilipotokea shambulio la kigaidi nchini Kenya hivi karibuni, nilihoji kama Ubalozi huo unatumia mtandao wa Twitter kuwafahamisha Watanzania waliopo nchini humo au/na huko nyumbani kuhusu usalama wao au wa ndugu, jamaa au marafiki zao.
Kwa nchi nyingi duniani, hususan za Magharibi, balozi zao na hata Wizara zao za Mambo ya Nje, hujihangaisha sana kwenye mitandao ya jamii na tovuti zao kuwafahamisha wananchi kuhusu hali ya usalama, na hasa wakati wa majanga kama tukio la ugaidi jijini Nairobi.
Ni matumaini yangu kuwa balozi zetu nyingine zitaiga mfano wa ubalozi wetu wa Kenya na kuanza kutumia vyombo mbalimbali vya habari, na hasa mitandao ya kijamii kusambaza na kurahisisha mawasiliano.
Baada ya pongezi hizo, nibaki huko huko Twitter kwa ajili ya mfano unaohusiana na mada yangu wiki hii. Majuzi nilikuwa na maongezi ya utani na mbunge mmoja wa Bunge la Afrika Mashariki, Abdullah Mwinyi (mtoto wa Rais wa Awamu ya Pili, Mzee Ali Hassan Mwinyi).
Pasi kuingia kiundani kuhusu maongezi yetu hayo, mbunge huyo alinieleza (kwa utani) kwamba namnukuu: “Chahali, you are very cynical...” (akimaanisha mie ni mtu mwenye kuyaangalia mambo kwa mashaka, kwa tafsiri isiyo rasmi).
Ninapenda kukiri kuwa mara nyingi mtizamo wangu kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu mustakabali wa taifa letu, umetawaliwa na mashaka. Pengine tabia hiyo, ni matokeo ya kujihusisha na fani moja huko nyuma ambayo inasisitiza kuliangalia kila jambo kwa mashaka, sambamba na dhana kuwa imani itapelekea mauti yako (trust will get you killed).
Ni katika hali hiyo, mtizamo wangu kuhusu mchakato mzima wa kuelekea kupata Katiba Mpya, umetawaliwa na mashaka. Na huenda nikieleza sababu zinazonipa mashaka hayo, wasomaji wangu wanaweza kushawishika kukubaliana nami kwamba japo ni vema kuwa na matarajio mema, lakini ni muhimu matarajio hayo yakatokana na misingi imara na ya kuleta matumaini.
Kwa wanaofuatilia kwa karibu suala la Katiba Mpya, watakuwa wanafahamu kuwa kimsingi ajenda hiyo iliasisiwa na chama cha upinzani cha CHADEMA, kabla ya kuporwa na CCM.
Lakini, jambo la msingi si nani aliyeasisi hoja hiyo au nani aliipora, bali umuhimu wake kwa taifa letu. Hata hivyo, ukweli kwamba awali CCM ilionyesha upinzani dhidi ya wazo hilo la CHADEMA kuhusu Katiba mpya, unaweza kutupa mwanga kuhusu sokomoko linaloendelea katika mchakato wa kupata Katiba Mpya.
Kwa wanaofuatilia makala zangu kwa karibu, wanaweza kubaini kwamba sijalitilia maanani sana suala la Katiba mpya. Kwanini? Jibu langu ni jepesi tu, ambalo pengine linachangiwa na kile alichokieleza Mmbunge Mwinyi kuwa ninayaangalia mambo mengi kwa mashaka, ni kwamba ninapata shida sana kuamini kwamba CCM ipo tayari kujitundika kitanzi kwa kuruhusu Katiba Mpya yenye maslahi ya wananchi, badala ya utaratibu uliozoeleka miaka nenda rudi, wa kuweka mbele maslahi ya kibinafsi na/au kiitikadi.
Kwamba CCM iruhusu nchi iongezwe na Katiba badala ya Chama kushika hatamu (hata kama tupo kwenye mfumo wa vyama vingi)? Ninapata shida kuamini hilo, kama ambavyo siamini kuwa chama hicho tawala kitaruhusu kundi lolote lile, iwe ni Tume ya Warioba, wawakilishi wa makundi mbalimbali ya kijamii na kadhalika, kuongoza mchakato huo badala ya CCM yenyewe.
Ni hivi; kwa viongozi wengi wa CCM, kila suala linaloihusu nchi yetu, lipo chini ya hakimiliki yake. Ukiwasikiliza viongozi mbalimbali wa chama hicho wanapozungumzia masuala yanayohusu nchi yetu, unaweza kudhani wanazungumzia kitu wanachokimiliki binafsi na si cha umma.
Na japo ni rahisi kuwalaumu kwa ubinafsi huo, lakini tutarajie nini kutoka kwa wanasiasa ambao wengi wao wametumia mamilioni ya fedha kuingia kwenye nyadhifa walizonazo sasa?
Kwa watu wa aina hiyo, siasa ni zaidi ya ajira; ni njia ya mkato ya kujinufaisha na hata kupata utajiri wa haraka, kama si kinga kwenye matendo yaliyo kinyume cha sheria.
Lakini, hata kama CCM ingekuwa chama ‘kisafi’ bado kinakabiliwa na tatizo moja kubwa la haiba ya viongozi wakuu wa chama hicho. Tangu ‘utotoni,’ chama hicho kilitegemea sana nguvu na busara za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ingawa wengine wanatafsiri kuwa alikuwa mbabe, ambapo alimudu kwa asilimia kubwa kukipa dira na mwongozo chama hicho tawala.
Kila anayeifahamu CCM ya sasa anajua fika kuwa japo Rais Jakaya Kikwete anapewa heshima zake kama Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, lakini yayumkinika kuhitimisha kuwa kuna wanasiasa wawili-watatu wenye nguvu kubwa zaidi yake ndani ya chama hicho.
Tetesi kadhaa zinaeleza kuwa hata hali ya sintofahamu au upinzani katika masuala kadhaa yanayohusiana na mchakato wa Katiba hiyo mpya, vinachangiwa na kiongozi mmoja ‘mwenye nguvu za ajabu’ ndani ya CCM, ambaye inaelekea ameapa kuwa lazima aingie Ikulu mwaka 2015 ‘no matter what’ (iwe, isiwe).
Inaelezwa kwamba mwanasiasa huyo, ambaye sihitaji kumtaja jina, amekuwa akiongoza CCM kwa namna anavyotaka, pengine kutokana na habari kwamba ametumia fedha zake nyingi kuwaingiza madarakani viongozi mbalimbali wa chama hicho, ikiwa ni pamoja na wale waliopo ngazi za juu.
Kwa hiyo, ingawa ningetamani kuandika maneno tofauti na haya, binafsi sidhani kwamba tutaishia kupata Katiba tunayoitamani. Ninashindwa kabisa kuamini kuwa ‘walafi’ ndani ya CCM, wataruhusu mwanya unaoweza kupunguza uwezekano wao wa ‘kuifakamia keki ya taifa.’
Naam, mengi ya mapendekezo yaliyomo katika Katiba hiyo yanaweza angalau kupunguza mianya ya ufisadi, matumizi mabaya ya madaraka na ukandamizwaji wa haki.
Ingawa ninatamani sana kuona nchi yetu inapata Katiba yenye kujali maslahi ya kila Mtanzania na taifa letu kwa ujumla, historia na uzoefu wangu binafsi, vinanikwaza kuamini kwamba chama tawala, hususan genge la wanasiasa wanaoendekeza maslahi binafsi, kitaruhusu tufikie ndoto hiyo.
Na pia, ninaomba kuwa mkweli, hata kama ukweli wenyewe ni mchungu, Rais Kikwete anaweza kuwa na nia nzuri kwa taifa letu kuhusiana na suala hili la Katiba mpya, lakini amezungukwa na wanasiasa wabinafsi na wenye nguvu kubwa, ambao kwa namna moja au nyingine, wanaweza kumzidi kete na hatimaye tukaishia kuwa na Katiba iliyo mpya, si kwa kilichomo ndani yake, bali mpya kwa mwaka ilipopitishwa rasmi.
Labda, mimi ni ‘cynical’ kama alivyotania Mbunge Mwinyi, lakini labda hii ndiyo hali halisi tunayopaswa kujiandaa nayo kisaikolojia. Lakini kinachonisumbua zaidi, ni kukosekana kwa njia bora. Waingereza wanasema ‘foolproof’ itakayozuia uwezekano wa mchakato huu wa Katiba mpya kuishia kuwa zoezi la gharama kubwa, kifedha na kimatumaini, litakaloishia kuwa sehemu ya historia isiyo na manufaa kwa mwananchi wa kawaida.
Nihitimishe makala hii kwa ushauri unaoweza kuonekana hauna maana. Imani zetu za kidini kwa asilimia kubwa zimekuwa sehemu muhimu ya maisha yetu.
Na kwa vile dua na sala zina umuhimu wa kipekee, na hasa katika mazingira yanayokatisha tamaa, basi pengine ni vema tukiwekeza nguvu zetu katika dua/sala kumwomba Mola aangamize vikwazo vya kila mwenye malengo mabaya dhidi ya Katiba Mpya, sambamba na kuwajaalia ujasiri wale wote wanaopigania kupatikana kwa tunu hiyo muhimu kwa taifa letu. Katika Mungu, yote yanawezekana!
- See more at: http://raiamwema.co.tz/tujiandae-kisaikolojia-kupata-katiba-mpya#sthash.dTZXvHqP.dpuf

6 Oct 2013

Taasisi za usalama nchini Kenya zitaendelea kusuasua kuepusha umwagaji damu kama uliotokea mwezi uliopita kwenye shambulizi kwenye eneo la  maduka ya Westgate, iwapo watendaji wa kada za chini wa vyombo hivyo wataendelea kuwa wanahongeka kirahisi na endapo uhasama baina ya vyombo hivyo utaendelea kuathiri ushirikiano wa kupashana habari za kiusalama.

Shambulio la kigaidi  lililofanywa Septemba 21 mwaka huu na kupelekea zaidi ya vifo 67, na kudumu kwa siku kadhaa, limeishtua nchi hiyo inayojivunia wanausalama wenye uzoefu mkubwa katika kupambana na ugaidi.

Lakini wakati uchunguzi unaendelea katika eneo la tukio ili kuwatambua wahusika na mbinu walizotumia, changamoto mbalimbali kwa taifa hilo lililo mshirika muhimu wa nchi za Magharibi katika kupambana na magaidi wa Kiislam zinaanza kujitokeza.

Maafisa Usalama wa zamani na wa sasa, wanadiplomasia na wataalam wanaelezea vyombo vya usalama vinavyotumia isivyo ujuzi uliopatikana kwa msaada wa Marekani na Uingereza na wakufunzi wengine kwa vile watuhumiwa wanaweza kuhonga na kuepuka kukaguliwa na polisi, huku ushirikiano duni kati ya vymbo vya usalama ukimaanisha ni vigumu kukamilisha taarifa za kiusalama.

Pia wanaharakati wanasema kuwa vyombo vya dola vimeingizwa mno kwenye siasa za ndani ya nchi hiyo badala ya kuweka mkazo kwenye majukumu yao ya kiusalama.

Hakuna anayetarajia kuwa Kenya itaweza kuzwia kila shambulio la kigaidi, na kwa hakika wanadiplomasia wa nchi za Magharibi wanazipongeza taasisi za usalama za nchi hiyo kwa kufanikiwa kuzuwia mashambulizi kadhaa kabla ya hilo la Westgate.

Lakini, kikundi cha kigaidi cha Al-Shabaab,ambacho kimekiri kuhusika na shambulio hilo,  kimedhirisha kuwa Somalia itaendelea kuwa kiota cha kuanzishia mashambulizi ya kigaidi kama hayo.Kenya kama jirani wa Somalia haiwezi kumudu kupuuza mapengo yanayosababishwa na mapungufu ya kitaasisi na utumishi.

"Hata kama utawekeza nguvu kiasi gani katika taasisi za usalama, ruhswa bado itaathiri malengo yako," anasema Meja Jenerali Mstaafu Charles Mwanzia, ambaye alikuwa mkuu wa idara ya usalama jeshini hadi mwaka 2005.

"Ni fundisho chungu na wito wa kuamka ili kuboresha usalama wa nchi hii katika maeneo ya kukusanya na usimamizi wa taarifa za usalama" anasema Jenerali huyo kuhusiana na shambuliz la Westgate.

Dalili za uhasama miongoni mwa vyombo vya dola vya nchi hiyo zilionekana wakati wa mapambano kati ya wanasualama na magaidi katika eneo hilo la maduka jijini Nairobi.

Afisa upelelezi mmoja, ambaye kama wengine, aliongea  na Shirika la Habari la Reuters kwa masharti ya kutotajwa jina, alieleza jinsi kikosi maalum cha jeshi na polisi (General Service Unit) kilichokuwa cha kwanza kufika eneo la tukio kilivyosukumwa kando baada ya askari wa Jeshi la Ulinzi (KDF) kuwasili.

MAADUI DHIDI YA URAFIKI

Kutokuwepo ushirikiano wakati wanajeshi hao wa KDF wanaingilia kati mapambano hayo kulitoa fursa kwa magaidi kujipanga upya, na pengine hiyo ilichangia kurefusha harakati za kuwadhibiti magaidi hao (zilzodumu kwa angalau siku 4). "Maafisa wa ngazi za juu wa GSU na KDF hawakuwa na ushirikiano wa kutoa mwongozo," anaeleza afisa upelelezi huyo.

Serikali ya Kenya ilidai kuwa operesheni ya kukabiliana na magaidi hao iliendeshwa kwa ushirikiano wa vymbo mbalimbali vya dola vikifanya kazi kwa ushirikiano. KDF imejitetea kuwa jeshi la polisi ndilo lililoongoza operesheni hiyo.KDF pia imesema itachunguza tuhuma kuwa baadhi ya askari wake walishiriki kupora mali katika maduka mbalimbali ya Westgate wakati wa operesheni hiyo.

Pamoja na kukoselewa huko, wataalam wa usalama na wanadiplomasia wa nchi za Magharibi walieleza kuwa chombo chochote cha usalama kingekuwa na wakati mgumu kupambana na magaidi hao wenye mafunzo na uwezo wa hali ya juu, katika eneo kubwa kama maduka ya Westgate.

Hata hivyo, wanaona mapungufu katika hatua za kujiandaa na operesheni hiyo dhidi ya magaidi. Wanasema kuwa taasisi za usalama za Kenya hufanya kazi kama maadui baina yao badala ya kushirikiana, hukataa kujumuisha taarifa za kiusalama pamoja, kiasi kwamba tetesi za matishio ya kiusalama zinaweza kutoonekana na pia dondoo zinazopatikana kwenye ufuatiliaji wa washukiwa (surveillance) zinakuwa vigumu kuunda picha ya kuwezesha kfanya maamuzi stahili.

"Ni wazuri katika wanachofanya, hususan katika ukusanyaji wa taarifa za kiusalama...lakini hawajui nini cha kufanya na wanachokipata, na jinsi ya kutengeneza picha kubwa (putting together the big picture)," alisema mtaalam mmoja wa usalama ambaye amefanya kazi na majeshi na idara za usalama za Afrika Mashariki kwa miaka kadhaa.

"Nina hakika hawana mawasiliano kati yao,"alisema kuhusu Idara ya Usalama wa Taifa, kitengo cha usalama wa taifa jeshini na idara za upelelezi na ushushushu za jeshi la polisi.

Wanasiasa wa Kenya na wanahabari wameeleza viokezo mbalimbali ambavyo havikuonwa mapema.Taarifa moja ya kiusalama iliyochapishwa kwenye magazeti, ambayo hata hivyo haikuweza kuthibitishwa rasmi, iliorodhesha nyendo za waliodhaniwa kuwa memba wa Al-Shabaab nchi humo, sambamba na dalili kwamba kuna uwezekano wa shambulizi la kigaidi katika maduka ya Westgate au kanisa.

Wakongwe wa usalama na wanadiplomasia wanaeleza pia kuwa taasisi za kishushushu za nchi za Magharibi nazo zilitetereka katika kuzuia shambulio hilo, kutokana na mawasiliano hafifu miongoni mwao, lakini tatizo hilo ni la dharura zaidi nchini Kenya.

Uratibu hafifu unaweza kuathiri utajiri mkubwa wa Kenya katika uwezo wake kuwafuatilia magaidi, kutoka kwenye mashushushu, majeshi yake nchini Somalia hadi vikosi vya kupambana na ugaidi, ambao hupokea misaada ya vifaa na mafunzo kutoka Marekani, Uingereza na nchi nyingine za Magharibi.

Israeli pia ilitoa msaada wa mafunzo ya kiintelijensia na ilipeleka 'washauri wa usalama' wakati wa tukio la Westgate.

Lakini hata kama intelijensia ingekuwa imara, bado rushwa ingeathiri ufuatiliaji wa watuhumiwa.Kwa fedha zenye thamani ya dola mia kadhaa tu, mtuhumiwa anaweza kununua passport, kupita vikwazo vya upekuzi wa polisi (police checkpoints) pasi kupekuliwa, na kununua silaha, wanaeleza maafisa na wataalam wa usalama.

Hiyo inamaanisha hata kama kuna nyenzo za kisasa kabisa za ufuatiliaji, bado washukiwa wanaweza 'kupotea kwenye rada' na kulazimisha ufuatiliaji usiwe na faida.

KUFIKIA ENEO KUSUDIWA (TARGET)

"Kenya inakabiliwa na tatizo kubwa katika safu ya kati,kwa sababu rushwa imetawala mno kwa polisi wa nchi hiyo" anaeleza mwanadiplomasia mmoja wa nchi ya Magharibi.

"Wamekuwa na mafanikio sana kuwazuwia Al-Shabaab...lakini kitu kisichoweza kukubalika ni jinsi magaidi walivyoweza kuingia nchini na kufikia eneo kusudiwa (target)" anasema mwanadiplomasia huyo.

Hiyo inafanya vigumu kujipenyeza ndani ya vikundi vya kigaidi, jambo ambalo ni muhimu katika kuvidhibiti.

"Inahitaji polisi mmoja tu mlarushwa kuwezesha ukiukwaji mkubwa wa kiusalama, kupita mpakani isivyostahili, kwa shilingi kutumbukizwa mfukoni na mtu kufanikiwa kuvuka mpaka," anaeleza mtaalam mwingine.

Jeshi la polisi linadai linauhamasisha umma kuripoti rushwa na kuchukua hatua stahili za kinidhamu.

"Hatuwezi kusema hakuna rushwa," alikiri Msemaji wa Polisi, Gatiria Mboroki, lakini akaongeza kuwa "Ukisharipoti, tukio hilo huchunguzwa."

Afisa mmoja wa zamani wa usalama wa taifa anaeleza kuwa wakati flani alijaribu kuwathibitishia wenzake jinsi rushwa ilivyo sugu, ambapo aliweza kuwaingiza nchini humo watoa habari wake kutoka Somalia baada ya kununua passport kwa dola 300 kila moja.

"Nikwenda mbali kuthibitisha kuwa udhibiti katika mipaka yetu ni dhaifu," alisema.

Mageuzi kwa jeshi la polisi yalikuwa moja ya vipaumbele vya Katiba mpya ya Kenya ya mwaka 2010. Lakini ukiweka kando uteuzi wa maafisa waandamizi, mageuzi kwa polisi hayajaleta chochote cha maana.

"Wanasema lakini hawafanyi lolote kuhusu hicho wanachosema. Haihitaji fedha.Inahitaji mabadiliko ya mtazamo," anasema mpigania haki Maina Kiai. "Mashushushu wanapaswa kufahamu kuwa kazi yao sio ya kisiasa, ni ya kiusalama."

Kauli hiyo iliungwa mkono na afisa wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa ambaye alieleza kuwa wanausalama walivurugwa na Uchaguzi Mkuu uliopita. "Usalama wote umeelekezwa kwenye usalama wa kisiasa badala ya usalama wa taifa," alisema.

Ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi mkuu uliopita ulionyesha kuwa ukabila bado ulikuwa na nafasi muhimu kwa wapiga kura, suala ambalo pia linaathiri teuzi za watendaji mbalimbali katika taasisi za usalama.

Serikali imedai kuwa teuzi hufanywa kwa kuzingatia uwezo, sio asili ya mteuliwa. Msemaji wa Polisi Mboroki kuwa jeshi la polisi haliyumbishwi na wanasiasa kwani ni taasisi ya umma.

Hata hivyo, wanaharakati na wataalam wanasema hatua zaidi zinahitajika.

"Pasipo mfumo wa kuwawajibisha kwa matendo yao na kuondoa rushwa," anasema mataalam wa usalama, "hakuna chochote kitakachobadilika."

Imetafsiriwa kutoka wavuti ya Reuters






Kuanzia sasa , blogu hii itakuwa ikiwaletea makala muhimu za mtaalam wa afya, Dokta Joachim Mabula. Makala hizo pia hupatikana katika tovuti ya Fikra Pevu, na unaweza kufuatilia mada mbalimbali kutoka kwa Dkt Mabula kwa kum-follow huko Twitter, ambapo anatumia handle @DrMabula au Google+ +Joachim Mabula au Facebook https://www.facebook.com/DrMabula

Makala yake ya leo inazungumzia ugonjwa wa saratani ya matiti (breast cancer): chanzo, dalili na matibabu. Ungana nae hapa chini


Kansa ya matiti ni aina ya kansa inayojitokeza toka tishu za matiti hasa mirija myembamba inayopitisha maziwa. Ugonjwa huu (Saratani ya matiti) hutokea kwa binadamu na mamalia wengine. Idadi ya wanaume wanaopatwa na kansa ya matiti ni ndogo sana ikilinganishwa na ya wanawake. 
Ulimwenguni pote, kansa ya matiti hubeba asilimia 29 nukta tisa ya kansa zote kwa wanawake. 
Licha ya maendeleo ya kitiba, bado kansa ya matiti ndiyo kansa inayosababisha vifo vingi zaidi vya wanawake. 
Nchi zilizoendelea za Amerika Kaskazini na Ulaya Magharibi ndizo zenye idadi kubwa zaidi ya watu walio na kansa, lakini idadi ya wanawake walio na kansa ya matiti inaongezeka katika bara la Asia na Afrika ambako kwa kawaida kumekuwa na idadi ndogo kiukweli. 
Idadi ya wanaokufa kati ya wale wanaogundulika kuwa na ugonjwa huo huko Asia na Afrika ni ya juu kwasababu kansa hiyo haigunduliwi mapema. Wagonjwa wengi huja ikiwa tayari imeenea sana. 
Kansa ya matiti huanza wakati ambapo chembe moja inajigawanya haraka sana isivyo kawaida na bila utaratibu, na hatua kwa hatua inafanyiza uvimbe. 
Uvimbe unakuwa kansa wakati chembe zake zinapovamia tishu nyingine. Uvimbe fulani unaweza kuchukua miaka kumi hivi kabla ya kugunduliwa. 
VIHATARISHI/VISABABISHI

Hatari ya kupatwa na kansa hiyo huongezeka dadiri umri unavyosonga. Asilimia 80 hivi ya wanawake wenye kansa ya matiti wana umri unaozidi miaka 50. 
Lakini jambo linalofariji ni kwamba kansa ya matiti ni mojawapo ya kansa zinazoweza kutibiwa kwa urahisi. 
Watakao tibiwa kabla ya kansa hiyo kuenea wanaweza kuishi muda mrefu kwa ukawaida. 
Visababishi vya kansa ya matiti bado ni fumbo. 
Baadhi ya wanasayansi wanaamini kwamba kansa ya matiti hutokana na hatua nyingi tata ambazo huanza wakati ambapo chembe fulani ya urithi yenye kasoro inapofanya chembe zitende kwa njia isiyo ya kawaida, yaani, zigawanyike kwa kasi sana, zishambulie tishu nyingine na kuepuka kuharibiwa na mfumo wa kinga, kisha pole pole chembe hizo zinashambulia na kuharibu viungo muhimu vya mwili. 
Jambo lingine linalohusishwa na kansa ya matiti ni homoni ya estrojeni ambayo huenda inachochea aina fulani za kansa hiyo. 
Kwa hiyo, mwanamke anaweza kupatwa na kansa hiyo ikiwa alianza kupata hedhi mapema maishani au ikiwa aliacha kupata hedhi akiwa amechelewa isivyo kawaida, ikiwa alipata mimba ya kwanza umri wake ukiwa umesonga au ikiwa hakuwahi kupata mimba, au ikiwa alipata matibabu ya kurudisha homoni fulani mwilini. 
Kwa kuwa chembe za mafuta hutokeza estrojeni, huenda wanawake walionenepa kupita kiasi waliofika umri wa kuacha kupata hedhi na hivyo ovari zao hazitokezi tena homoni, wakawa katika hatari ya kupatwa na kansa hiyo. 
Pia watu walio na viwango vya juu vya insulini na watu walio na viwango vya chini vya homoni ya usingizi inayoitwa melatonia kama vile watu wanaofanya kazi usiku, wako pia katika hatari ya kupatwa na kansa hiyo. 
Uvutaji wa tumbaku umeonekana kuongeza hatari zaidi ya kupata saratani ya matiti, kiwango kikubwa cha tumbaku iliyovutwa na kuanza kuvuta tumbaku katika umri mdogo hufanya hatari kuongezeka zaidi. 
Mionzi na kemikali za viwandani huongeza hatari ya kansa ya matiti. Kemikali kama polychlorinated biphenyls, polycyclic aromatic hydrocarbons na dawa za kuulia wadudu huchangia kutokea saratani hiyo. 
DALILI

- Uvimbe wowote au kuongezeka kwa unene wa ngozi kwenye makwapa au titi. 
- Umajimaji wowote unaotoka kwenye chuchu ambao si maziwa. 
- Mabadiriko yoyote ya rangi au ngozi ya titi. 
- Chuchu iliyodidimia kwa njia isiyo ya kawaida au inayowasha. 
UCHUNGUZI KUJUA KAMA NI KANSA

Ili kuchunguza ikiwa uvimbe una kansa sindano nyembamba hutumiwa kutoa tishu kutoka kwenye uvimbe huo na kufanyiwa uchunguzi. 
MATIBABU

Uvimbe ukiwa na kansa hufanyiwa upasuaji ili kuondoa uvimbe huo na tishu zinazozunguka titi. Upasuaji husaidia kuonyesha uvimbe ulipofikia (ukubwa, aina na kuenea kwake) na kuchunguza uvimbe unakua upesi kadiri gani. 
Chembe zenye kansa zinaweza kutoka kwenye uvimbe na kusafiri kupitia mfumo wa damu au mfumo wa limfu na kuanza kukua tena mahali pengine mwilini. 
Kuenea kwa kansa hadi kwenye viungo na tishu muhimu kama vile ubongo, ini, uboho wa mfupa au mapafu ndio hufanya ugonjwa huo uwe hatari. 
Hivyo baada ya upasuaji, wagonjwa wengi hupata matibabu mengine ambayo yatazuia kansa isirudi na kuenea. 
Kwasababu ya maendeleo katika matibabu ya kansa ya matiti, kumekuwa na matibabu mbalimbali ikitegemea umri, afya historia ya kansa katika familia, na aina ya kansa. 
Wanasayansi wanajifunza mambo mengine kuhusu kansa kutia ndani kuelewa ni kwa nini kansa huenea, kudhibiti chembe za kansa ambazo haziharibiwi kupitia matibabu ya kemikali, kuzuia kugawanyika kwa chembe na kutibu kila uvimbe kwa njia hususa.


ABOUT THE AUTHOR: 
Clinician | Programme Officer & Social Media Manager (Cvs-Tanzania) | Bussinessman
- See more at: http://www.fikrapevu.com/saratani-ya-matiti-breast-cancer-chanzo-dalili-na-matibabu-yake/#sthash.vAwVieVu.dpuf




.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

5 Oct 2013



Mnamo tarehe 9 Desemba 1961, Tanganyika ilipata Uhuru chini ya Waingereza waliokuwa waangalizi wetu tu, 

Ni nyakati hizo ambapo mataifa ya Afrika yalikuwa kwenye vuguvugu la kupata uhuru wao kamili yakiongozwa na Nchi ya Gold Coast iliyojinyakulia uhuru kutoka kwa Uingereza mnamo tarehe 6 Machi 1957, na ikawa taifa la kwanza la Afrika Kusini mwa Sahara (Sub-Saharan Africa) kufanya hivyo japokuwa Gold Coast/Ghana haikuweza kutangaza uhuru wake kamili kutoka kwa Uingereza hadi tarehe 1 Julai 1960 ambapo pia nchi ilianza kujulikana kama Jamhuri ya Ghana.

Nchi ya Gold Coast ilianzishwa na Waigereza, "Gold Coast" ni nchi ya Ghana ya leo, Neno Ghana lina maana ya Shujaa Mfalme na lilikuwa ni jina la heshima walilopewa wafalme wa Himaya ya Ghana nyakati za kale za Afrika Magharibi.

Tangu Tanganyika ipate uhuru 09/12/1961 hadi kifo chake chenye utata 1964, ilitumia KATIBA ya chama cha Ukombozi cha TANU iliyoandikwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, pamoja na mahuisho mengi yaliyopita kama yale ya 1962, 1965, 1977, 1992 bado asili ya katiba hii tuliyonayo leo ni ya MKONO wa Julius Nyerere,

Marekebisho makubwa ya Katiba yalikuwa ni mwaka 1977, lakini asili ya KATIBA ile ya Mkono wa Nyerere imeendelea kuishi na kulitendea haki Taifa na wajihi wake!

Nchi ya Gold Coast ilipopata uhuru chini ya Kwame Nkrumah licha ya kubadili jina la nchi na kuitwa Ghana, bado iliendelea kutumia asili ya katiba ya Chama cha The Convention People's Party (CPP) 

Labda kwa wale wasiojua niwafahamishe kuwa Katiba ya Tanganyika African National Union (TANU) ilinakiliwa kutoka chama rafiki cha The Convention People's Party (CPP)

Ni mashirikiano mema katika makutano ya fikra za kisiasa kati ya vijana wawili wasomi na imara ambao bara la Afrika halijapata kuwa nao kwa karne hivi sasa, si wengine ni Julius Nyerere na Kwame Nkrumah walipobadilishara fikra na kuzaa matunda ya Afrika na dunia tuyatafunayo sasa,

Nimekuwa na mtazamo hasi kabisa juu ya uhuru wa Afrika kwa mda mrefu sana hasa kwa matukio niyaonayo na niyasikiao toka Afrika,

Miaka ya 1955-1975 ni kipindi ambacho Afrika ilijitoa toka mikononi mwa mkoloni, mimi huwa naamini ni kipindi ambacho Afrika haikuwa na sifa za kuwa tayari kujitawala kwa maana ya kujipatia/kupewa UHURU,

1. Afrika haikuwa na Wasomi wakuongoza nchi

2. Waafrika walikuwa kwenye lindi la kutopea kwenye ujinga, hawakuwa tayari kwa kuupokea uhuru huo,

Mfano Tanganyika ilipata Uhuru ikiwa na wasomi wachache wenye ngazi ya shahada ya Uzamili (Masters) ambae ni Julius Nyerere, na Shahada ya Uzamivu (PHd) ni mmoja tu ambaye ni Dr Vedasto Kyaruzi, 

Na hata wale waasisi waliokuwemo kwenye harakati za kupigania Uhuru ndani ya TANU hawakuwa wasomi wa ngazi za juu zaidi ya Julius Nyerere,

Wazee hawa ni Julius Kambarage Nyerere, Ali Sykes, Lameck Makaranga, Gosbert Milinga, Gelmandus Pacha, Joseph Kimalando, Japhet Kirilo, Abubakar Ilanga, Saadan Kandoro, Suleiman Kitwara, Kisunguta Kabara, Tewa Said Tewa, Dosa Aziz, Patrick Kunambi, Joseph Kasela-Bantu, John Rupia, Abdul Wahid Sykes.

Nchi ya Gold Coast/Ghana ilipopata uhuru haikuwa na wasomi wengi wa Shahada, Stashada na Shahada ya Uzamivu na uzamili, 

Msomi wa ngazi ya juu alikuwa mmoja tu mwenye shahada ya Uzamili (Master of Science) ndugu Kwame Nkrumah 

Japokuwa usomi wa ngazi ya juu kwa watawala sio tiketi ya uwezo wa kutawala katika nchi, Hili huwa naamini ni kosa la Afrika la 1960-1975 kudai Uhuru na kupewa MAPEMA huku Waafrika hawakuwa tayari kujitawala wenyewe,

Hatua hii hunifanya niamini kuwa Afrika haikuwa imepevuka kujitawala kwa ngazi ya karne ile ya 20, huwa naamini kuwa miaka 1975-1985 ndicho kipindi ambacho Afrika ingekuwa kwenye mapito sahihi ya kujitawala, nikipindi ambacho binadamu wa Afrika angekuwa amepevuka,

Sasa ni karne ya 21, kosa lile la Karne ya 20 linajirudia katika muundo uleule kasoro nadharia tu, nalo ni upatikanaji wa Katiba mpya ya Tanzania,

Hali hii ya uhitaji wa katiba mpya kwa Watanzani ni jambo la kupongezwa na kujivunia kwa kila mtanzania, kwakuwa imedhihirika kuwa sasa Taifa limekuwa kifikra, na zaidi idadi ya wasomi katika nchi imeongezeka maradufu,


Lakini jambo la hatari na lisilokubalika nikuwa Taifa limeaminishwa kuwa Katiba Mpya itapatikana kabla ya 2015, huu ni ulaghai na wendawazimu wa wazi kabisa,

Katiba ya Watanzania haiwezi kupatikana kwa miaka mitano ama mmoja huu uliosalia, Katiba inayohitaji maridhiano, katiba inayopita kwenye misigano ya kitaifa, katiba inayohitaji elimu kwa Watanzania kwanza kamwe haiwezi kupatikana kabla ya 2015, kitakachopatikana kabla ya 2015 kitaitwa katiba ya kisiasa sio katiba ya Watanzania, 

Ninachokiamini nikuwa Watanzania tujipe muda, turuhusu fikra na mijadala huru iendelee juu ya upatikanaji wa Katiba mpya, turuhusu majibizano ya hoja ya endelee, tuyturuhusu Watanzania wote wake kwa waume, Wazee kwa vijana wote watoe ya moyoni bila kuogopa mawazo yao,

Katiba bora ya kiraia yenye matakwa halisi ya Wananchi inaweza kuchukua hata miaka 10 mchakato wake mpaka kuipata, hivyo katiba hii ambayo mchakato wake unaendelea SIO lazima isimamie Uchaguzi wa 2015 kama wanasiasa wanavyotusukuma tuamini hivyo,

Nionavyo muhimu katika kipindi hiki nikuwa, Watanzania, wanaharakati na Wanasiasa waendele kusimamia mchakato uendelee lakini upande wa pili wageuzi fikra zao, uanzishwe mchakato wa marekebisho ya Katiba hii iliyopo ili tuingie nayo kwenye uchaguzi 2015.Kinyume na hapo ni kuwalaghai Watanzania kuwa katika itapatika kabla 2015, 

Ikumbukwe kuwa Jakaya Kikwete ambae sasa ndiye rais wa Tanzania, katika historia ya siasa zake DUNIANI, hajawahi kuhitaji katiba mpya ya Tanzania wala kuizungumzia tu, hata serikali ya Chama chama Mapinduzi ambacho yeye ndiye Mwenyekiti hakijawahi kuhitaji Katiba Mpya ya Tanzania, na zaidi serikali ya Chama cha Mapinduzi iliyodumu kwa miaka 50 sasa haijawahi kuhitaji katiba Mpya ya Tanzania,

Vyama vya upinzani na Wanaharakati wa Tanzania ndio walioasisi mapambano ya kudai Katiba mpya, tena vikipita katika mapito magumu sana yenye kuhatarisha uhai wao,

Ni baada ya uchaguzi mkuu 2010 ndipo mbinyo wakudai katiba mpya ukiongozwa na chama kikuu cha upinzani nchini huku ccm na wahafidhina wake wakipinga katukatu kuwa Taifa halihitaji Katiba mpya,

Lakini KUFUMBA na KUFUMBUA Jakaya Kikwete alilitangazia Taifa kuwa linaanza mchakato wa Katiba, akitumia neno KUHUISHA katiba.

Tafakari Chukua Hatua, Busara ni mwanzo wa kukaribisha Hekima yenye nguvu za maliza tofauti katika nchi na kupata katiba ya kiraia yenye mkono wa Mtanzania

4 Oct 2013


.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.