28 Apr 2016

MIONGONI mwa wahadhiri walionifundisha nilipokuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ni Mmarekani mmoja aliyependa sana kufundisha kwa kutumia mifano halisi. Moja ya mada ambazo zilizonigusa sana ni kuhusu ‘undugunaizesheni.’ Alieleza kuwa hata Marekani kuna tabia hiyo, ambapo mara nyingi watu wenye nyadhifa muhimu hupenda kufanya kazi na watu wanaowafahamu au hata ndugu zao. 

Na kwa vile mfumo wa serikali nchini humo sio kama wetu wa ‘ili mtu ateuliwe kuwa waziri sharti awe mbunge – awe wa kupigiwa kura na wananchi jimboni, wa viti maalumu au wa kuteuliwa na rais. Kwa wenzetu huko, rais anaweza kumteua mtu yeyote kuwa kwenye “kabineti” yake japo baadhi ya nyadhifa zinahusisha mteuliwa kuidhinishwa na mabunge ya nchi hiyo. 

Mhadhiri huyo Mmarekani alitanabaisha kuwa baadhi ya viongozi ‘huwavuta’ ndugu zao wa karibu, jamaa au marafiki sio tu kwa vile ni watu wao wa karibu bali pia kulingana na sifa walizonazo. Lakini la muhimu zaidi ni matarajio kuwa ndugu, jamaa au rafiki anaweza kuwa mtiifu sana kwa aliyemteua, hasa ikizingatiwa kuwa ‘akimwangusha, anajiangusha naye pia.’

Kwa hiyo, si kwamba suala la undugunaizesheni – kufanya upendeleo kwenye maeneo kama vile teuzi za nafasi za uongozi, halipo Afrika, au huko nyumbani pekee bali hata huku kwa hawa wenzetu wanaojigamba kwa kuzingatia taratibu na kanuni. 

Kimsingi, kumteua mtu unayemjua, alimradi ana sifa stahili, sio kuvunja taratibu na kanuni, hususan kama mchanganuo wa kumteua mtu huyo haukuwanyima watu wengine fursa ya kuteuliwa. 

Suala la ‘undugunaizesheni’ limekuwa likinijia akilini kila ninapokutana na habari kuhusu sakata la Lugumi. Lakini pengine kabla ya kuingia kwa undani kujadili sakata hilo ni vema nikaweka bayana msimamo wangu maana ‘wenye nchi’ wamekuwa wakali kweli, ukikosoa kidogo tu unaonekana kuwa wewe ni jipu au mtetezi wa majipu.

Ni kwamba namuunga mkono Rais Dk. John Magufuli, katika jitihada zake kubwa za kutumbua majipu. Hata hivyo, mara kadhaa amekuwa akitusihi Watanzania tumsaidie katika jitihada zake hizo. Na miongoni mwa njia za kumsaidia mtu ni kumshauri au hata kumkosoa pale inapobidi. Binafsi, ninaamini kuwa mtu pekee anayeweza kumaliza sakata la Lugumi ni Rais Magufuli tu, hakuna cha Bunge wala Takukuru. Ni hivi, si mfanyabiashara yeyote tu anayeweza kupewa zabuni nyeti ya kuweka mashine za kuchukua alama za vidole katika mamia ya vituo vya polisi nchini. Mtu anayepewa dhamana kubwa namna hiyo lazima awe ‘mtu fulani.’ 

Mengi yanayozungumzwa kuhusu mmiliki wa kampuni hiyo ya Lugumi yamebaki kuwa tetesi tu, lakini moja linalisikika zaidi ni madai kuwa alikuwa ‘karibu na watawala’ katika Serikali ya Awamu ya Nne. Na kwa jinsi tunavyoelewa nchi yetu ilivyokuwa inajiendesha yenyewe (on autopilot) katika awamu hiyo, hakuna miujiza hapa wala hakuna la ajabu ambalo lisingewezekana. Tuwe wakweli, nchi ilikuwa inaendeshwa kimzaha. 

Tetesi pia zinadai kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga, ambaye sio tu ndiye mwenye dhamana ya kufuatilia kuhusu sakata hilo kwa vile linaihusu wizara yake, lakini pia ni mmoja wa wanaotajwa kuhusika na ufisadi huo kupitia umiliki wa kampuni yake ya Infosys. 

‘Mazingaombwe’ yanayolizunguka sakata hili yanazidi kuendelea. Awali, ilielezwa kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi aliikwepa Kamati husika ya Bunge alipotakiwa kutoa maelezo kuhusu sakata hilo. Baadaye, tukasikia Bunge likitoa taarifa za kujikanganya, ikiwa na pamoja na kituko cha kudai kuwa kamati husika haikuomba mkataba husika bali maelezo tu (kana kwamba kuomba mkataba huo ni kuvunja sheria za nchi). 

Siku chache baadaye, ikaibuka video inayomwonyesha mtendaji mmoja wa kampuni ya Infosys akieleza kuwa Waziri Kitwanga sio mmiliki wa kampuni hiyo, na kwamba aliachana nayo kabla haijaingia mkataba huo wenye utata. 

Baadaye tena, Waziri Kitwanga mwenyewe akajitokeza kuzungumzia suala hilo akidai kuwa wakati suala hilo linatokea, yeye hakuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, na ndio maana hapendi wala hataki kuzungumzia suala hilo. 

Kauli hii inatoka kwa waziri ambaye Jeshi la Polisi lipo chini ya wizara yake. Sawa, hakuwa waziri wakati suala hilo linatokea, lakini sasa ni waziri. Kwa nini basi asipende wala kutaka kuongelea suala ambalo sio tu linaitia doa wizara yake na jeshi la polisi bali pia linaweza kuathiri usalama wa taifa letu? 

Kwa nini kama Waziri Kitwanga anajua vema majukumu yake hakushughulikia suala hilo kabla ya kuibuliwa na Kamati ya Bunge? Na hapo tunaweza kujiuliza, kwa nini Rais Magufuli hakuchukua hatua stahili dhidi ya mtendaji wake huyo, kwa staili ya kutumbua majipu? 

Sarakasi za sakata la Lugumi zimeendelea kwa Bunge kuunda timu maalumu ya kuchunguza suala hilo. Nilidhani kuwa Takukuru wangeweza kufanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi kwa vile sidhani kama wabunge walioteuliwa ni wataalamu wa uchunguzi wa masuala yenye dalili za ufisadi. Labda tuwape muda, huenda wanajua wanachofanya. 

Kichekesho zaidi kimeibuka muda mfupi kabla sijaandaa makala hii, ambapo Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu ameibuka na kudai kuwa kampuni ya Lugumi ilitekeleza mkataba husika, na kukanusha madai ya Kamati husika ya Bunge, na taarifa zilizosambaa mtandaoni na kwenye vyombo vya habari kuwa kampuni hiyo ilishindwa kufunga mashine za kuchukulia alama za vidole kwenye vituo 108 kama ilivyotamkwa kwenye mkataba. 

IGP Mangu alidai kushangazwa na habari hizo na kueleza kuwa kampuni ya Lugumi ilitekeleza mkataba husika kama ilivyokubaliana na serikali. 

“Siyo kweli, watu wana ugomvi wao, lakini nakueleza wazi kwamba, tembelea vituo vyote tulivyokubaliana, utakuta mashine zipo. Inawezekana zingine hazifanyi kazi kwa sababu ya kukosekana kwa intaneti,” alisema mkuu huyo wa jeshi la polisi. 

Ni akina nani hao “wenye ugomvi wao” ambao jeshi la polisi linashindwa sio tu kuwachukulia hatua bali hata kuwataja majina hasa ikizingatiwa kuwa kashfa hiyo inachafua taswira ya taasisi hiyo ya dola? 

Na kama huo ndio ukweli, kwa nini basi IGP Mangu hakujitokeza kwenye kikao cha Kamati ya Bunge iliyokutana kufuatilia suala hilo? Si angeenda tu na kuwaeleza kama anavyosema sasa kuwa suala hilo linatokana na “ugomvi” wa watu fulani? 

Lakini utetezi wake ungekuwa na maana tu kama angeweza kubainisha ni vituo vingapi na vipi ambavyo mashine hizo zilifungwa, na vingapi na vipi ambavyo mashine zinafanya kazi au hazifanyi kazi. 

Na kuhusu uwezekano wa kuwepo mashine zisizofanya kazi kutokana na kutokuwepo kwa Intaneti, basi ni uzembe wa wazi wa IGP na Waziri wake Kitwanga kwa sababu hilo ni jipu lililopaswa kutambuliwa mapema kabla ya kuibuliwa na kamati ya Bunge. Je, huduma ya Intaneti ilikatwa kwa kutolipiwa kwa vile Jeshi la Polisi lilinyimwa fungu husika au ni habari zile zile wa ‘watumishi hewa’? 

Nilianza makala hii kwa kuzungumzia suala la undugunaizesheni. Kuna hisia kuwa uteuzi wa Waziri Kitwanga ulitokana na ukaribu alionao na Rais Magufuli. Hilo sio kosa. Lakini ni jukumu la mteuliwa kuhakikisha hamwangushi aliyemteua. Na katika sakata hili la Lugumi, yayumkinika kuhisi kuwa Waziri Kitwanga anamwangusha Rais Magufuli. 

Wengi tuna imani na Dk. Magufuli, lakini ni ukweli usiofichika kuwa moja ya mitihani mikubwa inayomkabili ni pamoja na uwezekano wa kuangushwa na ‘maswahiba zake,’ watu anaowaamini lakini wasioitendea haki imani hiyo, shinikizo ndani ya chama chake CCM, na kubwa zaidi, ‘madudu’ yaliyofanyika katika awamu iliyopita hususan yale ambayo akiyagusa tu, nchi itatikisika (rejea kauli ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyowahi kuitoa bungeni kuhusu sakata moja la ufisadi ambapo aliwaambia bayana wabunge wamsulubu tu lakini asingeweza kuongelea suala husika). 

Nimalizie makala hii kwa kumsihi Rais Magufuli kuwa uungwaji mkono anaohitaji zaidi ni kutoka kwa Watanzania wa kawaida, waliompigia kura na hata waliomnyima kura. Hawa hawatomwangusha kwa sababu wanamhitaji, na hadi sasa amewathibitishia hivyo. Baadhi ya watendaji wake wapo kwa maslahi yao binafsi, na hawa watamwangusha asipokuwa makini. Ni muhimu kwa Rais wetu kukumbuka kuwa utumbuaji majipu halisi unamtengenezea maadui lukuki, ambao wanaweza kuunganisha nguvu na kumyooshea kidole pale yanapojitokeza mambo kama haya ya kina Lugumi. 


Mpendwa Rais Magufuli, chukua hatua moja tu na sakata hili la Lugumi litamalizika (kwa maslahi ya Watanzania) 

21 Apr 2016


MAJUZI nilibandika habari mbili kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook zilizohusu ufisadi na umasikini. Habari moja ilihusu taarifa za vyombo vya habari kwamba wabunge wameshtushwa na ripoti inayoonyesha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetumia shilingi bilioni 18 kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha.

Niliambatanisha habari hiyo na nyingine iliyoonyesha ‘shule ya kipekee’ ambayo madarasa matatu yanalazimika kutumia jengo moja, kitu ambacho kinaweza kuiingiza shule hiyo katika rekodi ya miujiza ya Guinness.

Lengo lilikuwa kuonyesha kuwa wakati TCRA ikitumia mabilioni hayo kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha, kuna wanafunzi wanaosoma katika mazingira magumu kwa kulazimika ‘kuchangia’ jengo la darasa.

Watumiaji wengi wa mtandao huo wa kijamii waliguswa na habari hiyo, lakini kilijitokeza kikundi kidogo kilichoitetea TCRA kwa nguvu zote. Hoja yao kuu ni kuwa majukumu ya taasisi hayo ni muhimu na teknolojia inabadilika kwa kasi, kwa hiyo ni sahihi kutumia fedha nyingi kuiwezesha taasisi hiyo kwenda na wakati.

Kilichonisikitisha zaidi ni pale wanahabari wawili wakongwe (mmoja wa gazeti hili) ‘walipomvuta’ kiongozi mmoja wa TCRA, sio kwa minajili ya kumbana kuhusu taarifa hiyo bali kuvilaumu vyombo vya habari vilivyoripoti habari hiyo, sambamba na kutetea matumizi hayo ya mabilioni kwa mafunzo, semina na warsha.

Nilikerwa mno na utetezi wa wanahabari hao kwa sababu laiti wangerejea ripoti za nyuma kuhusu matumizi ya taasisi hiyo wangetambua tukio hilo sio la mara ya kwanza. Mwaka 2011, Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ilikagua hesabu za TCRA na kugundua madudu ya kutisha, ikiwa ni pamoja na mamlaka hiyo kusomesha nje wafanyakazi wake watatu kwa gharama ya shilingi bilioni 2.2

Na hata kama TCRA ingekuwa haijawahi kuingia matatizoni kutokana na matumizi hayo makubwa ya fedha za umma, bado isingehalalisha taasisi hiyo kutumia shilingi bilioni 18 kwa ajili ya mafunzo, semina na warsha. Sio kwa Tanzania yetu hii ambayo ni moja ya nchi masikini kabisa duniani.

Lakini kingine kilichonikera kuhusu matumizi hayo ya ‘anasa’ ya TCRA ni ukweli kwamba mamlaka hiyo kwa kiwango kikubwa imekuwa butu hususan katika eneo la udhibiti dhidi ya makosa ya mtandaoni. Taasisi hiyo ilikuwa mstari wa mbele kutetea muswada wa sheria ya makosa ya mtandao (Cybercrime Bill 2015) hadi ilipopitishwa kuwa sheria kamili.

Binafsi niliunga mkono muswada huo na hatimaye sheria husika kwa sababu, kwa upande mmoja, nilikwishawahi kuwa mhanga wa unyanyasaji mtandaoni, na kwa upande mwingine, nilikuwa nikikerwa mno na matumizi mabaya ya uhuru mtandaoni yaliyojumuisha matusi, picha za utupu na vitendo vingine visivyofaa, hususan katika mtandao wa kijamii wa Instagram.

Sasa, tangu sheria hiyo dhidi ya uhalifu wa mtandaoni ipitishwe imeishia kuungana na lundo la sheria nyingine kali lakini zisizo na ufanisi wowote. Ni kweli kwamba hoja za waliokuwa wakiipinga sheria hiyo zilikuwa na mantiki, hususan hofu kuwa itatumika vibaya, hususan uwezekano wa kutumika kisiasa zaidi kuliko kisheria.

Inatusikitisha baadhi yetu tuliotumia nguvu kubwa kuunadi muswada wa sheria hiyo ambao ulipata upinzani mkali kutoka kila kona ya Tanzania, lakini hatimaye ulifanikiwa na kuwa sheria kamili.

Majuzi, sheria hiyo imeonekana kufanya kazi ‘ghafla.’ Kijana mmoja amekamatwa na kufikishwa mahakamani chini ya ulinzi mkali kabisa, kwa kosa la kumtukana Rais John Magufuli.

Hakuna Mtanzania mwenye akili timamu anayeweza kuunga mkono kuwatusi viongozi wetu, awe Rais au mwenyekiti wa kijiji. Tatizo ni kwamba sheria hiyo dhidi ya uhalifu mtandaoni inaonekana kuwa na meno pale tu ‘wakubwa’ wanapoguswa.

Kwa yeyote anayetaka kuthibitisha jinsi gani sheria hiyo ‘ina upendeleo’ atembelee mtandao wa kijamii unaohusu picha, yaani Instagram, ambapo huko kuna kila aina ya laana: kuna ushoga wa waziwazi, kuna lundo la akaunti zinazobandika picha za utupu, kuna ‘ligi kuu’ ya matusi ambapo kadri watu wanavyoonyesha umahiri wa matusi ndivyo kadri wanavyopata wafuasi wengi.

Hali huko Instagram ni mbaya mno kiasi kwamba ni rahisi kudhani kuwa wanaofanya ‘madudu’ huko wapo katika nchi isiyo na sheria (lawless country). Kwa vile ‘wakongwe’ wa matusi wameendelea kupata umaarufu kwa kutukana pasipo kuchukuliwa hatua zozote, mtandao huo umewavutia hata watu ‘wasio na matusi’ kujaribu fursa ya kujipatia umaarufu wa bure.

Na umaarufu huo una ‘faida’ kwani akaunti zinazosheheni matusi pia hufanya matangazo ya biashara mbalimbali, kuanzia ‘video za ngono’ hadi tiba za ajabu ajabu.

Wakati fulani niliwajulisha watu wa TCRA kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter, lakini ‘bosi’ wa mamlaka hiyo aliishia kutoa ‘darasa’ refu lisilo na maana akidai kuwa ni muhimu Watanzania watambue sheria zilizoianzisha Mamlaka hiyo na shughuli zake kwa ujumla. Alidai kuwa jukumu la udhibiti wa matusi na uchafu mwingine huko Instagram ni la polisi. Kichekesho ni kwamba kesi ya huyo jamaa aliyemtukana Rais inaendeshwa kwa ushirikiano kati ya polisi na TCRA.

Kwa hiyo si kwamba TCRA haina mamlaka ya kupambana na ‘laana’ inayoendelea huko Instagram, lakini kinachoonekana ni kwamba haina muda na adha zinazowakumba wananchi wa kawaida. Uvunjifu huo wa sheria ukimgusa kiongozi, basi mamlaka hiyo na sheria dhidi ya uhalifu wa mtandaoni vinafufuka ghafla. Hii sio sawa hata kidogo.

Nimalizie makala hii kwa kuisihi serikali ifanye jitihada za makusudi kukomesha hali mbaya inayoendelea katika mtandao huo wa kijamii. Haihitajiki kukamata kila mhusika lakini vinara wachache tu wakitiwa nguvuni itasaidia kufikisha ujumbe kwa wenzao.

Suala hili linaweza kuihusu wizara yenye dhamana na masuala ya afya pia, kwa sababu mtandao huo umegeuka kuwa duka lisilo rasmi la dawa za aina mbalimbali, suala ambalo linaziweka afya za Watanzania shakani.

Penye nia pana njia, pasipo na nia pana kisingizio. 

8 Apr 2016

MOJA ya masuala yanayotawala anga za habari na mijadala mbalimbali mtandaoni ni uamuzi wa Bodi ya Taasisi ya Changamoto ya Milenia (Millennium Challenge Corporation - MCC) ya Marekani kusitisha misaada kwa Tanzania.
Sababu kuu mbili zilizotolewa na bodi hiyo kuhusu uamuzi huo ni marudio ya uchaguzi huko Zanzibar Machi 20, mwaka huu, ambao licha ya kususiwa na chama kikuu cha upinzani cha CUF, ulilalamikiwa kwa kiasi kikubwa na baadhi ya nchi wahisani, ikiwa ni pamoja na Marekani.

Sababu ya pili, kwa mujibu wa bodi hiyo, ni uamuzi wa Serikali ya Tanzania kupitisha Sheria Uhalifu wa Mtandaoni (Cybercrime Act) ya mwaka 2015 licha ya upinzani mkali dhidi ya muswada wa sheria hiyo, iliyotafsiriwa kuwa imelenga kukandamiza uhuru wa habari na haki za binadamu.

Kabla ya kuingia katika uchambuzi huu kiundani, nieleze mtazamo wangu kuhusu sababu hizo mbili zilizotolewa na Bodi ya MCC. Kwanza, kwa mtazamo wangu, suala la marudio ya uchaguzi wa Zanzibar ni mzaha wa kidemokrasia. Haihitaji uelewa mkubwa wa siasa za Zanzibar kufahamu kuwa kuna ‘sheria isiyo rasmi’ kuwa ‘kamwe CUF hawapaswi kutawala Zanzibar.’

Bila kuuma maneno, hiyo ndiyo sababu pekee ya kufutwa kwa uchaguzi wa awali (ambao inadaiwa mgombea wa CUF, Seif Shariff Hamad, alishinda) na kuamriwa uchaguzi huo urudiwe huku CCM ikiwekeza nguvu zake zote kuhakikisha inashinda. Hata kama CUF wasingesusia uchaguzi huo, bado CCM wangeshinda kwa sababu ‘ni lazima iwe hivyo,’ kwa ‘kanuni’ zao.

Je, MCC ipo sahihi kutumia kigezo cha Zanzibar kusitisha misaada yao? Kwa upande mmoja, wapo sahihi. Kwa sababu, hata katika uhusiano wetu wa kawaida tu kibinadamu, anayekupa msaada anapata ruhusa pia ya ‘kukutawala’ kwa kukupa masharti ambayo ukiyakiuka, yanaweza kuathiri uhusiano kati ya mtoa msaada na mpokea msaada. Miongoni mwa masharti ya MCC ni pamoja na masuala ya demokrasia, na haihitaji kukuna kichwa sana kubaini kuwa marejeo ya uchaguzi wa Zanzibar, ambayo binafsi ninayaona kuwa ni mzaha wa kidemokrasia, yamewapa MCC ‘kisingizio chepesi’ hata kama hawangekuwa na sababu nyingine.

Mgogoro wa muda mrefu wa kisiasa huko Zanzibar ni zaidi ya jipu. Ni kansa ambayo imeshachafua sura ya Tanzania huko nyuma ambapo kwa mara ya kwanza tulizalisha wakimbizi baada ya vurugu za Uchaguzi mkuu mwaka wa 2000.

Ni kansa ambayo sasa imewapa MCC kisingizio cha kutunyima misaada yao. Kwa bahati mbaya au makusudi, hakuna utashi wa kisiasa wa kusaka ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro huo. Kila kiongozi wa CCM, kwa upande wa Bara, anaogopa suala hilo kwa kuhofia kuvunjikiwa na Muungano mikononi mwake.

Baadhi ya wanasiasa wa Zanzibar sio tu wanaufahamu udhaifu huo bali pia wanautumia vema. Wanaendesha siasa za chuki na uhasama watakavyo wakifahamu kuwa hakuna mwana-CCM wa Bara mwenye jeuri ya kuwaingilia.

Sina hakika Zanzibar itaathirika vipi kwa uamuzi wa MCC kukata misaada, lakini kinachowapa kiburi viongozi wa huko ni kwamba ‘Tanganyika’ haina jeuri ya kuisusa Zanzibar au kuinyooshea kidole katika mwendelezo wa siasa za chuki na ubaguzi.

Lakini kwa upande wa pili, hao MCC ni wanafiki tu. Huhitaji kuwa na uelewa mkubwa wa siasa za kimataifa kutambua unafiki wa Marekani linapokuja suala la demokrasia. Nchi hiyo ni mshirika mkubwa wa tawala za kidikteta kama vile huko Misri, Saudi Arabia na kwingineko. Sawa, labda Zanzibar wamefanya mzaha wa kidemokrasia lakini vipi kuhusu demokrasia isiyopo kabisa huko Saudi? Jibu rahisi ni kwamba Zanzibar na Tanzania sio muhimu sana kwa Marekani ilhali taifa hilo linazitegemea mno tawala za kibabe za nchi kama Misri au Saudi, hususan katika masuala ya ushushushu au mapambano dhidi ya ugaidi wa kimataifa.

Kuhusu suala la Sheria ya Uhalifu wa Mtandao, hapa kumesheheni unafiki, na upo wa aina mbili. Kwanza, Wamarekani na pili ni Watanzania wenyewe. Binafsi ni mfuatiliaji wa karibu wa masuala ya usalama mtandaoni, ambao kwa namna moja au nyingine unahusiana na hiyo masuala ya Cybercrime Act.
Kwa kifupi tu, Marekani ina sheria kandamizi mno dhidi ya uhuru wa raia mtandaoni. Naamini umekwishasikia kuhusu jamaa anayeitwa Edward Snowden. Huyu bwana alikuwa mtumishi katika Shirika la Kijasusi la Marekani linalohusika na kunasa mawasiliano mbalimbali (NSA – National Security Agency) na baadaye nafsi yake ilimsuta, akaamua ‘kuingia mitini’ na kumwaga siri lukuki kuhusu jinsi NSA inavyohujumu haki za raia kimawasiliano. Hawa jamaa wamekuwa wakinasa mawasiliano ya takriban kila mtu, wakishirikiana kwa karibu na mashushushu wenzao wa hapa Uingereza, GCHQ, taasisi ya kishushushu inayohusika na kunasa mawasiliano.
Lakini hata tukiweka kando suala la NSA kunasa mawasiliano mbalimbali (waliwahi kuzua kasheshe kubwa baada ya mashushushu wa Ujerumani kubaini kuwa NSA walikuwa wakinasa kwa siri mawasiliano ya Kansela Angela Markel hadi waliposhtukiwa), mashambulizi ya kigaidi nchini humo mwaka 2001 yalisababisha kuundwa kwa sheria kali kabisa dhidi ya uhuru wa habari na haki za kibinadamu kwa kisingizio cha usalama wa taifa. Kwa hiyo, kwa kifupi, ni uhuni tu wa Marekani kudai Sheria ya Makosa ya Mtandaoni inakiuka uhuru wa Watanzania. Sheria zao za wazi na za kificho ni mbaya mara milioni zaidi yetu.

Hata hivyo, katika suala hili la Cybercrime Act, tuna wanafiki kadhaa huko nyumbani. Kwa kumbukumbu tu, nilikuwa mtetezi mkubwa wa muswada uliozaa sheria hiyo, yaani Cybercrime Bill, na niliunga mkono kwa nguvu zote jitihada za aliyekuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, kuhusu muswada huo.

Hata hivyo, baadhi ya watu ambao sasa wanailaumu Marekani na wafadhili wengine kuhusu suala la Tanzania kukatiwa misaada, walikuwa mstari wa mbele wakati huo kuziomba nchi wahisani ziingilie kati kuibana serikali ili muswada huo usipitishwe kuwa sheria. Sasa kama uamuzi huo wa Marekani umechangiwa na ‘kelele’ zao hizo, kwa nini leo wanalalamika?

Ninakerwa kuona kundi la wanafiki hawa likiilaumu MCC au Marekani au nchi nyingine wahisani kuhusu suala la kutukatia misaada, kwa sababu wao walikuwa mstari wa mbele kuhamasisha nchi wahisani zichukue hatua, na ‘hatua maarufu’ ya wahisani huwa ni kukata misaada. Badala ya kulalamika, wanafiki hawa wanapaswa kufanya sherehe maana dua zao zimetimia.

Sasa niangalie upande wa athari za uamuzi huo wa MCC kukata misaada. Tuwe wakweli, kwa watu masikini kama sisi, hatua yoyote ile ya kutupunguzia msaada wa aina yoyote ile itatuathiri. Hilo halihitaji uelewa wa jinsi gani misaada inavyofanya kazi au jinsi gani nchi yetu ilivyo “mtegemezi mzoefu wa misaada”.

Tatizo kubwa hapa kuhusu kukatiwa misaada kutatuathiri au hakutatuathiri ni tofauti zetu za kiitikadi. Kwa kiasi kikubwa, suala hilo linaangaliwa katika lensi ya u-CCM na u-Ukawa /Upinzani. Kwa wana-CCM, ni mwendo wa ‘kiburi’ kwenda mbele, kwamba “waende tu na misaada yao,” au “hela yenyewe ilikuwa ya mradi wa kifisadi wa Symbion,” mara “ah misaada gani hiyo yenye masharti kibao.” Wanamhadaa nani? Kama misaada hiyo haikuwa na umuhimu, kwa nini basi tuliiomba?

Kwa upande wa wana-Ukawa /Wapinzani, bila kujali kuwa wao kama Watanzania ni waathirika watarajiwa wa uamuzi huo wa nchi yetu kukatiwa misaada, wanakenua meno yote 32 kwa furaha, huku wakiwazodoa wenzao wa CCM kwa vijembe kama “...ndio matunda ya ubabe wenu huko Zanzibar, tuone sasa…” au “mtaisoma namba” au “mtakula jeuri yenu…”
Ulemavu huu wa kifikra unaosababishwa na kuliangalia suala la kiuchumi kwa mtizamo fyongo wa itikadi za kisiasa. Naam, suala la Zanzibar ni la kisiasa, lakini athari za uamuzi wa Marekani (MCC) wahisani ni la kiuchumi.


Mimi si mchumi lakini naelewa fika kuwa uchumi wetu umekuwa tegemezi tangu tupate uhuru. Kabla ya kuipa kisogo siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, tulikuwa tukipata misaada kutoka kwa marafiki zetu wa mrengo wa Ukomunisti. Baada ya kuzika Ujamaa, tumekuwa kama puto linaloyumbishwa na upepo, tupo radhi kumpigia magoti yeyote anayeweza kutusaidia. Kimsingi, tuna ombwe la kiitikadi: majukwaani, CCM wanasema sisi ni Wajamaa, vitendo vyetu havipo kwenye Ujamaa wala Ubepari, tupo tupo tu. Huo ndio ukweli mchungu kuhusu ubabaishaji wetu.

Kwa hiyo, tuache kudanganyana kuwa kukatiwa misaada hakutotuathiri. Huko ni kujipa jeuri tu. Tunachoweza kukubaliana ni kwamba suala hilo limekwishakutokea, tumekwishakatiwa misaada, na si ajabu wahisani wengine wakaamua kufuata mkumbo na kufanya hivyo pia.

Jukumu letu kubwa kwa sasa sio kuendelea kunyoosheana vidole bali tuwe kitu kimoja kama taifa bila kujali nani hasa aliyetusababishia tatizo hili. Ni tatizo la Watanzania wote bila kujali itikadi zao. Uamuzi wa wahisani kukata misaada utawaathiri wana-CCM wanaodai hautowaathiri kama ambavyo utawaathiri wana-CUF au Chadema wanaokenua meno yote 32 kufurahia hatua hiyo. Na utatuathiri (angalau kisaikolojia) hata sisi ambao itikadi yetu pekee ni Tanzania yetu. Huo ni ukweli usiopingika (we are all in this together).

Kuna mambo mawili ya kupigiwa mstari. Kwanza, kwa miaka mingi tumekuwa tukiishi kifahari mno kuliko uwezo wetu. Na kimsingi, uwezo wetu duni haukupaswa kuwepo kwani sisi si masikini hata kidogo. Tuna kila aina ya utajiri lakini kuna majambazi walioigeuza Tanzania yetu kuwa kitu cha kufisadiwa kila kukicha. Kila mwenye uelewa anafahamu kilichojiri katika takriban miaka 30 iliyopita. Tanzania yetu ilikuwa shamba la bibi, watu wanafisadi wapendavyo kiasi kwamba kuwa na uchungu na nchi ilionekana kama uwendawazimu.

Kwa bahati nzuri, Mwenyezi Mungu amesikia kilio cha baadhi yetu na sasa tumempata Rais, Dk John Magufuli, ambaye anaonekana amedhamiria kurekebisha mwenendo wa mambo. Kikwazo chetu kikubwa kilikuwa ufisadi, lakini sasa Magufuli ameamua kuvalia njuga kupambana na ufisadi kwa nguvu zote. Mwanzo ni mgumu lakini angalau dalili za mafanikio zimeanza kujionyesha. Tumuunge mkono, tuchukie ufisadi, tuongeze uzalendo, tuikwamue Tanzania yetu, tujikwamue nasi wenyewe, tuache kutafuta njia za mkato za mafanikio, tufanye kazi, tuache majungu na kusaka sifa za kijinga mitandaoni, tuwajibike.
Tunahitaji kujifunga mikanda. Haiwezekani wafadhili wetu waishi kimasikini ilhali sisi wafadhiliwa tunaishi kama matajiri. Viongozi wetu waache kuchuana na wauza unga kushindana jinsi ya kuishi kitajiri, wawabane wauza unga hao, majangili na maharamia wengine ili tuiokoe Tanzania yetu.

Je, tunaweza kujitegemea? Naam, lakini tusidanganyane kuwa tunaweza kufanya hivyo ghafla. Tukumbuke, mtoto hazaliwi na kisha akatembea. Tumekuwa wategemezi mno wa misaada kiasi kwamba tumesahau kuwa tunapaswa kujitegemea. Tunahitaji kuchukua na kukubali uamuzi mgumu wa kutuwezesha kujitegemea.

Jambo jingine, kwa hisia zangu, japo suala la Zanzibar na Cybercrime Act zinatajwa kama sababu za uamuzi wa kutunyima misaada, ninashawishika kuamini kuwa baadhi ya nchi wahisani hawapendezwi na kasi ya Rais Magufuli kuziba mianya ambayo kimsingi licha ya kuwanufaisha mafisadi wa ndani, ilikuwa pia inanufaisha taasisi za kifisadi za kimataifa

Wengi wa majambazi waliokuwa wakitupora fedha zetu walikuwa hawahifadhi fedha zao katika benki zetu bali zilizopo katika nchi za wahisani hao. Wanaweza kudhani huu ni utani mbaya, lakini jiulize, je kama unamfadhili mtu pesa za kumsaidia yeye na familia yake, lakini anatumia fedha hizo kufanya matumizi ya anasa, kwa nini usichukue hatua?
Mfano huo unamaanisha hivi: kwa nini wahisani wetu walionekana kutokerwa na jinsi pesa walizokuwa wanatupatia zikifisadiwa kila kukicha lakini wakaendelea kutumwagia misaada? Na kwa nini sasa, tumempata Magufuli ambaye amepania kwa dhati kupambana na ufisadi, wahisani wanaanza kuvaa sura ya ubabaishaji.

Kuna tunaodhani kuwa hao wahisani wanataka tuendelee kuwa wategemezi wao milele. Kwa upande mmoja utegemezi wetu unawapa uhuru wa kukwapua kila rasilimali tuliyonayo, na kwa upande mwingine, wananeemesha taasisi zao za fedha kwa vile mafisadi wetu wa ndani wanahifadhi fedha zao kwenye taasisi hizo.


Mwisho, tuache porojo, tuache unafiki, tuwe kitu kimoja, athari za kukatiwa misaada zipo, tukishikamana tutaweza kukabiliana nazo japo mwanzoni itakuwa ngumu. Yawezekana uamuzi huo wa Wamarekani ukawa ‘blessing in disguise’ kwa maana ya kutupa ‘wake-up call’ tuanze kujitegemea kwa lazima badala ya kutembeza bakuli letu huko na kule, kisha kile kidogo kinachopatikana kikaishia kwenye ujenzi wa mahekalu ya mafisadi, ongezeko la magari yao ya kifahari, na kutanua ukubwa wa nyumba ndogo zao.

Mungu ibariki Tanzania

1 Apr 2016

Moja ya masuala yanayotawala anga za habari na mijadala mbalimbali mtandaoni ni uamuzi wa bodi ya taasisi ya Changamoto ya Milenia (Millennium Challenge Corporation) ya Marekani kusitisha misaada kwa Tanzania. Sababu kuu mbili zilizotolewa na bodi hiyo kuhusu uamuzi huo ni marudio ya uchaguzi huko Zanzibar Machi 20, mwaka huu, ambao licha ya kususiwa na chama kikuu cha upinzani cha CUF, ulilalamikiwa kwa kiasi kikubwa na nchi wahisani, ikiwa ni pamoja na Marekani.

Sababu ya pili, kwa mujibu wa bodi hiyo, ni uamuzi wa serikali ya Tanzania kupitisha Sheria Uhalifu wa Mtandaoni (Cybercrime Act) ya mwaka 2015 licha ya upinzani mkali dhidi ya muswada wa sheria hiyo, iliyotafsiriwa kuwa imemlenga kukandamiza uhuru wa habari na haki za binadamu.

Kabla ya kuingia katika uchambuzi huu kiundani, nieleze mtazamo wangu kuhusu sababu hizo mbili zilizotolewa na bodi ya MCC. Kwanza, kwa mtazamo wangu, suala la marudio ya uchaguzi wa Zanzibar ni mzaha wa kidemokrasia, na ni jeraha la kisiasa ambalo historia inaweza kutuhukumu huko mbeleni. Haihitaji uelewa mkubwa wa siasa za Zanzibar kufahamu kuwa kuna ‘sheria isiyo rasmi’ kuwa ‘kamwe CUF hawapaswi kutawala Zanzibar.’ Bila kuuma maneno, hiyo ndo sababu pekee ya kufutwa kwa uchaguzi wa awali (ambao inadaiwa mgombea wa CUF, Seif Shariff Hamad, alishinda), na kuamiriwa uchaguzi huo urudiwe huku CCM ikiwekeza nguvu zake zote kuhakikisha inashinda. Hata kama CUF wasingesusia uchaguzi huo, bado CCM wangeshinda kwa sababu ‘ni lazima iwe hivyo,’ kwa ‘kanuni’ zao.

Je MCC ipo sahihi kutumia kigezo cha Zanzibar kusitisha misaada yao? Kwa upande mmoja, wapo sahihi. Kwanini? Kwa sababu, hata katika mahusiano yetu ya kawaida tu kibinadamu, anayekupa msaada anapata ruhusa pia ya ‘kukutawala’ kwa kukupa masharti ambayo ukiyakiuka, yanaweza kuathiri mahusiano katika ya mtoa msaada na mpokea msaada. Miongoni mwa masharti ya MCC ni pamoja na masuala ya demokrasia, na haihitaji kukuna kichwa sana kubaini kuwa marejeo ya uchaguzi wa Zanzibar, ambayo binafsi ninayaona kuwa ni mzaha wa kidemokrasia, yamewapa MCC ‘kisingizio chepesi’ hata kama hawangekuwa na sababu nyingine.

Mgogoro wa muda mrefu wa kisiasa huko Zanzibar ni zaidi ya jipu. Ni kansa ambayo imeshachafua sura ya Tanzania huko nyuma ambapo kwa mara ya kwanza tulizalisha wakimbizi baada ya vurugu za uchaguzi mkuu mwaka wa 2000. Ni kansa ambayo sasa imewapa MCC kisingizio cha kutunyima misaada yao. Kwa bahati mbaya, au makusudi, hakuna utashi wa kisiasa wa kusaka ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro huo. Kila kiongozi wa CCM, kwa upande wa Bara, anaogopa suala hilo kwa kuhofia ‘kuvunjikiwa na Muungano mikononi mwake.’

Wanasiasa wa Zanzibar sio tu wanaufahamu udhaifu huo bali pia wanautumia vema. Wanaendesha siasa zao cha chuki na uhasama watakavyo wakifahamu fika kuwa hakuna mwana-CCM wa Bara mwenye jeuri ya kuwaingilia.

Sina hakika Zanzibar itaathirika vipi kwa maamuzi ya MCC kukata misaada, lakini kinachowapa kiburi viongozi wa huko ni kwamba ‘Tanganyika’ haina jeuri ya kuisusa Zanzibar, au kuinyooshea kidole katika mwendelezo wa siasa za chuki na ubaguzi.

Lakini kwa upande wa pili, hao MCC ni wanafiki tu. Huhitaji kuwa na uelewa mkubwa wa siasa za kimataifa kutambua unafiki wa Marekani linapokuja suala la demokrasia. Nchi hiyo ni mshirika mkubwa wa tawala za kidikteta kama vile huko Misri, Saudi Arabia na kwingineko. Sawa, labda Zanzibar wamefanya mzaha wa kidemokrasia lakini vipi kuhusu demokrasia isiyopo kabisa huko Saudi? Well, jibu rahisi ni kwamba Zanzibar na Tanzania sio muhimu ‘kihivyo’ kwa Marekani ilhali taifa hilo linazitegemea mno tawala za kibabe za nchi kama Misri au Saudi, hususan katika masuala ya ushushushu/mapambano dhidi ya ugaidi wa kimataifa.

Kuhusu suala la Sheria ya Uhalifu wa Mtandao, hapa kumesheheni unafiki, na upo wa aina mbili: wa Wamarekani na wa sie Watanzania wenyewe. Mie ni mfuatiliaji wa karibu wa masuala ya usalama mtandaoni, ambao kwa namna moja au nyingine unahusiana na hiyo ishu ya Cybercrime Act. Kwa kifupi tu, Marekani ina sheria kandamizi mno dhidi ya uhuru wa raia mtandaoni. Naamini ushaskia kuhusu jamaa anayeitwa Edward Snowden (kama hujamsikia, Wasiliana na Google…haha). Huyu bwana alikuwa mtumishi katika shirika la ushushushu la Marekani linalohusika na kunasa mawasiliano mbalimbali (NSA – National Security Agency), na baadaye nafsi yake ilimsuta, akaamua ‘kuingia mitini’ na kumwaga siri lukuki kuhusu jinsi NSA inavyohujumu haki za raia kimawasiliano. Hawa jamaa wamekuwa wakinasa mawasiliano ya takriban kila mtu, wakishirikiana kwa karibu na mashushushu wenzao wa hapa Uingereza, GCHQ, taasisi ya kishushushu inayohusika na kunasa mawasiliano.

Lakini hata tukiweka kando suala la NSA kunasa mawasiliano mbalimbali (waliwahi kuzua kasheshe kubwa baada ya mashushushu wa Ujerumani kubaini kuwa NSA walikuwa wakinasa kwa siri mawasiliano ya Kansela Angela Markel hadi waliposhtukiwa), mashambulizi ya kigaidi nchini humo mwaka 2001 yalipelekea kuundwa kwa sheria kali kabisa dhidi ya uhuru wa habari na haki za kibinadamu kwa kisingizio cha usalama wa taifa. Kwahiyo, kwa kifupi, ni uhuni tu wa Marekani kudai Sheria ya Makosa ya Mtandaoni inakiuka uhuru wa Watanzania. Sheria zao za wazi na za kificho ni mbaya mara milioni zaidi yetu.

Hata hivyo, katika suala hili la Cybercrime Act, tuna wanafiki kadhaa huko nyumbani. Kwa kumbukumbu tu, mie nilikuwa mtetezi mkubwa wa muswada uliozaa sheria hiyo, yaani Cybercrime Bill, na niliunga mkono kwa nguvu zote jitihada za aliyekuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, kuhusu muswada huo.

Hata hivyo, baadhi ya watu wanaoinyooshea kidole Marekani na wafadhili wengine kuhusu suala la Tanzania kukatiwa misaada walikuwa mstari wa mbele kuziomba nchi wahisani ziingilie kati kuibana serikali ili muswada huo usipitishwe kuwa sheria. Sasa kama uamuzi huo wa Marekani umechangiwa na ‘kelele’ zao hizo, kwanini leo wanalalamika?

Mie niliunga mkono muswada na sheria hiyo kwa sababu ikitumiwa vema ni nzuri. Hebu nenda Instagram kaangalie uanaharamu unaoendelea huko, kuanzia picha za uchi, ushoga na kila aina ya laana. Huo sio uhuru wa habari, ni uwendawazimu ambao kwa hakika ulihitaji sheria kali kuudhibiti.

Na watu waliopita huku na kule kudai sheria hiyo ni kandamizi na ililenga kuwabana wananchi wasiwasiliane, hawatuambii kama baada ya sheria hiyo kupitishwa wameshindwa kuwasiliana na watu wengine. Kwa kifupi, kulikuwa na udanganyifu mkubwa katika kambi ya waliopinga muswada na sheria hiyo. Walitumia uelewa mdogo wa wananchi wengi kuhusu masuala ya mtandao, na kuwajenga hofu feki.

Ninakerwa kuona kundi la wanafiki hawa likiilaumu MCC au Marekani au nchi nyingine wahisani kuhusu suala la kutukatia misaada, kwa sababu wao walikuwa mstari wa mbele kuhamasisha nchi wahisani zichukue hatua, na ‘hatua maarufu’ ya wahisani huwa ni kukata misaada. Badala ya kulalamika, wanafiki hawa wanapaswa kufanya sherehe maana wishes zao zimetimia.

Sasa niangalie upande wa athari za uamuzi huo wa MCC kukata misaada. Taarifa nyingine zinaeleza kuwa kuna wahisani wengine nao wamekata misaada japo kuna mkanganyiko kama hatua hiyo ni mwendelezo wa hatua za huko nyuma au ni mpya.

Tuwe wakweli, kwa watu masikini kama sisi, hatua yoyote ile ya kutupunguzia msaada wa aina yoyote ile itatuathiri. Hilo halihitaji uelewa wa jinsi gani misaada inavyofanya kazi au jinsi gani nchi yetu ilivyo mtegemezi mzoefu wa misaada. Tatizo kubwa hapa kuhusu “kukatiwa misaada kutatuathiri au hakutatuathiri” ni tofauti zetu za kiitikadi. Kwa kiasi kikubwa, suala hilo linaangaliwa katika lensi ya u-CCM na u-UKAWA/Upinzani. Kwa wana-CCM, ni mwendo wa ‘kiburi’ kwenda mbele, kwamba “waende tu na misaada yao,” au “hela yenyewe ilikuwa ya mradi wa kifisadi wa Symbion,” mara “ah misaada gani hiyo yenye masharti kibao.” Wanamhadaa nani? Kama misaada hiyo haikuwa na muhimu, kwanini basi tuliiomba in the first place? Hizi hadithi za sungura kusema “sizitaki ndizi hizi” baada ya kushindwa kuzikia mgombani.

Kwa upande wa wana-UKAWA/Wapinzani, bila kujali kuwa wao kama Watanzania ni wahanga watarajiwa wa uamuzi huo wa nchi yetu kukatiwa misaada, wanakenua meno yote 32 kwa furaha, huku wakiwazodoa wenzao wa CCM kwa vijembe kama “ndio matunda ya ubabe wenu huko Zanzibar, tuone sasa…” au “mtaisoma namba” au “mtakula jeuri yenu…”

Ulemavu huu wa kifikra unaosababishwa na kuliangalia suala la kiuchumi kwa mtizamo fyongo wa itikadi za kisiasa. Naam, suala la Zanzibar ni la kisiasa, lakini athari za uamuzi wa Marekani/MCC/wahisani ni la kiuchumi.

Mie sio mchumi ila ninachoelewa fika kuwa uchumi wetu umekuwa tegemezi tangu tupate uhuru. Kabla ya kuipa kisogo siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, tulikuwa tukapata misaada kutoka kwa marafiki zetu wa mrengo wa Ukomunisti. Baada ya kuuzika Ujamaa, tumekuwa kama puto linaloyumbishwa na upepo, tupo radhi kumpigia magoti yeyote anayeweza kutusaidia. Kimsingi, tuna ombwe la kiitikadi: majukwaani, CCM wanasema sie ni Wajamaa, vitendo vyetu havipo kwenye Ujamaa wala Ubepari, tupu tupo tu. Huo ndo ukweli mchungu kuhusu ubabaishaji wetu.

Kwahiyo, tuache kudanganyana kuwa kukatiwa misaada hakutotuathiri. Huko ni kujipa jeuri tu. Tunachoweza kukubaliana ni kwamba suala hilo limeshatokea, tumeshakatiwa misaada, na si ajabu wahisani wengine wakaamua kufata mkumbo na kufanya hivyo pia.

Jukumu letu kubwa kwa sasa sio kuendelea kunyoosheana vidole bali tuwe kitu kimoja kama taifa bila kujali nani hasa aliyetusababishia tatizo hili. Ni tatizo la Watanzania wote bila kujali itikadi zao. Uamuzi wa wahisani kukata misaada utawaathiri wana-CCM wanaodai hautowaathiri kama ambavyo utawaathiri wna-CUF au Chadema wanaokenua meno yote 32 kufurahia hatua hiyo. Na utatuathiri (angalau kisaikolojia) hata akina sie ambao itikadi yetu pekee ni Tanzania yetu. Huo ni ukweli usiopingika: we are all in this together.

Kuna mambo mawili ya kupigiwa mstari. Kwanza, kwa miaka mingi tumekuwa tukiishi kifahari mno kuliko uwezo wetu. Na kimsingi, uwezo wetu duni haukupaswa kuwepo kwani sie sio masikini hata kidogo. Tuna kila aina ya utajiri lakini kuna majambazi walioigeuza Tanzania yetu kuwa kitu cha kubakwa kila kukicha. Kila mwenye uelewa anafahamu kilichojiri katika takriban miaka 30 iliyopita. Tanzania yetu ilikuwa shamba la bibi, watu wanafisadi wapendavyo kiasi kwamba kuwa na uchungu na nchi ilionekana kama wendawazimu.

Kwa bahati nzuri, Mwenyezi Mungu amesikia kilio cha baadhi yetu na sasa tumempata Rais, Dkt John Magufuli, ambaye anaonekana amedhamiria kurekebisha mwenendo wa mambo. Kikwazo chetu kikubwa kilikuwa ufisadi, lakini sasa Magufuli ameamua kuvalia njuga kupambana na ufisadi kwa nguvu zote. Mwanzo ni mgumu lakini angalau dalili za mafanikio zimeanza kujionyesha. Tumuunge mkono, tuchukie ufisadi, tuongeze uzalendo, tuikwamue Tanzania yetu, tujikwamue nasi wenyewe, tuache kutafuta njia za mkato za mafanikio, tufanye kazi, tache majungu na kusaka sifa za kijinga mitandaoni, tuwajibike.

Twahitaji kujifunga mikanda. Haiwezekani wafadhili wetu waishi kimasikini ilhali sie wafadhiliwa twaishi kama matajiri. Viongozi wetu waache kuchuana na wauza unga kushindana jinsi ya kuishi kitajiri, wawabane wauza unga hao, majangili na maharamia wengine ili tuiokoe Tanzania yetu.

Je twaweza kujitegemea? Absolutely, lakini tusidanganyane kuwa twaweza kufanya hivyo ghafla ghafla. Tukumbuke, mtoto hazaliwi akatembea. Tumekuwa wategemezi mno wa misaada kiasi kwamba tumesahau kuwa twapaswa kujitegemea. Twahitaji kuchukua na kukubali maamuzi magumu ya kutuwezesha kujitegemea. Ni kama kumlazimisha mtoto anayetambua aanze kutembea kwa nguvu. Sio rahisi, lakini tukimkazania anaweza kusimama mwenyewe na baadaye akaweza hata kukimbia. Hilo linahitaji kujitoka mhanga kwa ajili ya nchi yetu, sambamba na kuweka mbele uzalendo badala ya maslahi binafsi.

Jambo jingine, kwa hisia zangu, japo suala la Zanzibar na Cybercrime Act zinatajwa kama sababu za uamuzi wa kutunyima misaada, ninashawishika kuamini kuwa baadhi ya nchi wahisani hawapendezi na kasi ya Rais Magufuli kuziba mianya ambayo kimsingi licha ya kuwanufaisha mafisadi wa ndani, ilikuwa pia inanufaisha taasisi za kifisadi za kimataifa. Wengi wa majambazi waliokuwa wakitupora fedha zetu mchana kweupe walikuwa hawahifadhi fedha zao katika benki zetu bali zilizopo kwa hao wahisani wetu. Waweza kudhani huu ni utani mbaya, lakini jiulize, je kama unamfadhili mtu pesa za kumsaidia yeye na familia yake, lakini anatumia fedha hizo kununulia bling bling, kuongeza nyumba ndogo, kufanya matumizi ya anasa, nk kwanini usichukue hatua?

Mfano huo unamaanisha hivi: kwanini wahisani wetu walionekana kutokerwa na jinsi pesa walizokuwa wanatupatia zikifisadiwa kila kukicha lakini wakaendelea kutumwagia misaada? Na kwanini sasa, tumempata Magufuli ambaye amepania kwa dhati kupambana na ufisadi, wahisani wanaanza kuleta ‘longolongo’?

Kuna tunaodhani kuwa hao wahisani wanataka tuendelee kuwa wategemezi wao milele. Kwa upande mmoja utegemezi wetu unawapa uhuru wa kukwapua kila raslimali tuliyonayo, na kwa upande mwingine, wananeemesha taasisi zao za fedha kwa vile mafisadi wetu wa ndani wanahifadhi fedha zao kwenye taasisi hizo.

Mwisho, tuache porojo, tuache unafiki, tuwe kitu kimoja, athari za kukatiwa misaada zipo, tukishikamana tutaweza kukabiliana nazo japo mwanzoni itakuwa ngumu. Yawezekana uamuzi huo wa Wamarekani ukawa ‘blessing in disguise’ kwa maana ya kutupa ‘wake-up call’ tuanze kujitegemea kwa lazima badala ya kutembeza bakuli letu huko na kule, kisha kile kidogo kinachopatikana kikaishia kwenye ujenzi wa mahekalu ya mafisadi, ongezeko la magari yao ya kifahari, na kutanua ukubwa wa nyumba ndogo zao.

MUNGU IBARIKI TANZANIA 

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.