24 Jan 2017

Mazingira yote yalikuwa 'yameiva' kwa vyama vya upinzani kufanya vizuri kwenye chaguzi za madiwani. Angalau kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Zanzibar, vyama vya upinzani 'vya Bara' (Chadema, ACT- Wazalendo, nk, isipokuwa CUF) vinaweza kuwa na 'kisingizio' kuwa upinzani huko, kwa maana ya CUF pekee, umepaganyika mno na isingekuwa rahisi kuchukua jimbo la Dimani. 

Lakini vyama vyetu vya upinzani haviwezi kuwa na excuse ya maana kutokana na matokeo mabaya kabisa waliyopata katika chaguzi hizo. 

Mwaka juzi, wakati Tanzania yetu inakwenda kwenye uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, uchaguzi ambao mie binafsi nililazimika kumpigia debe mgombea wa CCM, Dkt John Magufuli, baada ya 'Chadema kutusaliti' kwa kumpokea aliyekuwa kada maarufu wa CCM, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, niliwakumbusha mara kwa mara ndugu zangu wa UKAWA kwamba, kwanza, ni ukosefu wa busara kutegemea vyama vya upinzani kufanya vema katika mazingira yaleyale yaliyowafanya wafanye vibaya katika chaguzi zilizotangulia.

Vyama vya upizani vilivyoshiriki katika chaguzi hizo za madiwani viliingia vikiwa katika mazingira yaleyale yaliyovifanywa vibwagwe na CCM katika uchaguzi mkuu wa 2015.

Kibaya zaidi, hadi leo, si Chadema, NCCR Mageuzi, CUF au ACT-Wazalendo waliofanya 'post-mortem' (taarifa ya uchunguzi inayoeleza chanzo cha kifo) ya kwanini vyama husika vilifeli. Badala ya kufanya tathmini ya kina kuhusu sababu zilizovikwamisha vyama hivyo mwaka 2015, kumekuwa na mwendelezo wa porojo kuwa "njia ya Ikulu 2020 ni nyeupe."

save image


Kama kuna chama ambacho kinapaswa 'kusikia maumivu zaidi' kutokana na matokeo ya chaguzi hizo basi ni Chadema, kwa sababu wafuasi wa chama hicho - na kidogo ACT-Wazalendo - ndio pekee miongoni mwa vyma vyote vya upinzani nchini Tanzania, kuendeleza harakati za siasa, licha ya zuwio la serikali ya Rais Magufuli.

Kwamba, zuio hilo halijaathiri wafuasi wa Chadema kutumia teknolojia ya  mitandao ya kijamii, kuanzia Twitter, Whatsapp, Facebook, Jamii Forums, nk kuiban a mfululizoCCM na serikali yake. 

Lakini hapohapo kuna walakini. Ndio, ni wajibu wa vyama vya upinzani kuikosoa CCM na serikali yake. Hata hivyo, kukosoa tu hakutoshi hasa pale ambapo panapohitajika ufumbuzi.

Mifano ni mingi, lakini tuchukulie tishio la baa la njaa. Wakati serikali ya Rais Magufuli na CCM wakisisitiza kuwa hakuna tishio hilo, vyama vya upinzani vikiongozwa na Chadema vimekuwa mstari wa mbele kuonyesha kuwa tatizo hilo lipo.

Lakini kuonyesha tatizo tu bila kujaribu kutafuta ufumbuzi sio busara sana. Na baadhi yetu tulipomsikia Lowassa akisema, namnukuu "Serikali imesema haitoi chakula, mimi nimejadiliana na chama changu tumeona tufanye mpango wa kuwatafutia chakula Watanzania.”

Hicho chakula kiko wapi? Kuwapa wananchi matumaini kisha kutotekeleza ahadi husika ni hadaa. Lakini kuna wanaoshangaa eti "mbona licha ya 'kiburi cha serikali ya CCM kuhusu tishio la njaa' badi chama hicho kimeibuka kidedea kwenye chaguzi za madiwani?"

Jibu jepesi ni kwamba CCM "is the devil they know," kwamba pamoja na mapungufu yake, inaweza kutoa mifano hai ya ilivyowahi kuwasaidia wananchi siku za nyuma. Na hata kama inafanya 'kiburi' kuhusu tishio la njaa, angalau "haijatoa ahadi hewa" kama hiyo ya Bwana Lowassa.

Hebu pata picha: siku chache kabla ya chaguzi hizo, CCM 'yajipiga bao yenyewe' kwa kushikilia msimamo kuwa hakuna njaa na hata ikiwepo hakutokuwa na chakula cha msaada. Chadema kwa kushushiwa bahati hiyo, wanachangamka, wanakusanya misaada ya chakula, na kufanya harambee ya kuwasaidia watu wenye uhaba wa chakula. Naam, pengine serikali ingetaka kuingilia, lakini ninaamini nguvu ya umma ingekuwa upande mmoja na Chadema katika dhamira yao hiyo nzuri. Kwa bahati mbaya imebaki kuwa nzuri tu, na haijatekelezwa.

Kutekelezwa kwa ahadi hiyo kungeweza kutafsiriwa na CCM kama rushwa kwa wapigakura lakini mwenye njaa anachojali ni mkono kwenda kinywani na wala sio amepewa chakula kama msaada au rushwa. Ninaamini kabisa kuwa laiti ahadi ya Lowassa na Chadema yake kuhusu kuwasaidia wananchi wanaokabiliwa na baa la njaa ingetimizwa, basi pengine muda huu chama hicho kingekuwa kinachelekea ushindi.

Tukiweka kando suala hilo, ndugu zangu wa Upinzani, hususan Chadema wameendelea kuwa na imani fyongo kuwa "CCM inachukiwa mno," na "chuki hiyo dhidi ya CCM itapelekea kura kwa Wapinzani." Wanachopuuza ndugu zangu hawa ni ukweli kwamba udhaifu wa CCM sio uimara wa Upinzani. 

Ikumbukwe kuwa wakati CCM inaweza kusubiri hadi mwaka 2020 ili ianze kampeni za kubaki madarakani, Wapinzani wanapaswa kutumia muda huu kuwaonyesha Watanzania kuwa wao wanaweza kuwa mbadala wa kweli wa CCM. Lakini tunachoshuhudia ni Upinzani kuwa 'bize zaidi' kuiongelea CCM badala ya kutenda vitu vitakavyowapa matumaini Watanzania kuwa vyama hivyo ni mbadala sawia.

Ndugu zangu wa Chadema wana mtihani mkubwa zaidi. Pengo lililoachwa na Dokta Slaa limeshindwa kuzibika. Katibu Mkuu aliyepo madarakani anaweza kukisaidia sana chama hicho akiamua kuachia ngazi kwa hiari yake mwenyewe. Ninaamini mtu kama Godlisten Malisa, kada mwenye uwezo mkubwa, anaweza kushika wadhifa huo na akaibadili Chadema. 

Kwa upande mwingine, Mwenyekiti wa chama hicho Bwana Freeman Mbowe, yupo kwenye wakati mgumu mno pengine kuliko muda wowote ule wa maisha yake ya kisiasa. Mbowe anaandamwa na madeni yanayoweza kuathiri mno biashara zake. Japo deni sio jinai, kiongozi wa upinzani kuandamwa na madeni au kutolipa kodi kwa miaka kadhaa ni kitu kinachotoa taswira mbaya kwa wananchi.

Kuna lawama kadhaa zinazorushwa kwa Rais Magufuli kuwa anazitumia taasisi za serikali kama  vile TRA na NHC "kumwandama" Mbowe, lakini ukweli ni kwamba dawa ya deni ni kulipa. Na Chadema inaweza kuingia matatani ikitetea "ukwepaji kodi wa Mbowe" kwa sababu sote twajua kuwa hilo ni kosa (japo si la jinai).

Halafu kuna hizi 'drama' zinazoweza kuwavunja moyo watu wasio na chama lakini wanatafuta chama cha kukiunga mkono. Suala la 'kupotea' kwa kada wa Chadema, Ben Saanane, limeacha doa kubwa kwa chama hicho. Kwa upande mmoja, ilichukua wiki tatu tangu kada huyo adaiwe kupotea kabla ya uongozi wa chama hicho kutoa tamko rasmi. Lawama zaidi zaweza kwenda kwa Mbowe kwa vile Ben alikuwa msaidizi wake binafsi. 

Na Chadema walipotoa tamko rasmi kukfuatiwa na mkanganyiko mkubwa zaidi: huku Mbowe anadai Ben katekwa, kule Tundu Lissu anadai vyombo vya dola vinajua kada huyo yuko wapi, na pale, gazeti la Mwanahalisi la mbunge wa chama hicho Saed Kubenea likaeleza kuwa "Ben yupo, amekuwa akionekana kwenye vijiwe vya chama hicho." Na baada ya jithada fupi mtandaoni zilizoambatana na alama ya reli #BringBenBackAlive na kuchapishwa fulana, suala hilo limekufa kifo cha asili. Huu ni uhuni wa kisiasa maana hatutegemea chama makini kinachojitanabaisha kuwa mbadala wa CCM kuendesha mambo yake kienyeji hivyo.

Kuna tatizo jingine ambalo Chadema wamekataa katakata kulishughulikia. Kabla ya kumpokea Lowassa, ajenda kuu ya Chadema ilikuwa vita dhidi ya ufisadi. Ujio wa Waziri Mkuu huyo wa zamani ulikilazimisha chama hicho kuachana na ajenda hiyo ambayo kwa kiasi kikubwa sana ndio iliyokiwezesha chama hicho kuwa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania.

Na kwa vile Rais Magufuli amejaribu kuifanya vita dhidi ya ufisadi kuwa moja ya ajenda zake kuu, Chadema kwa muda huu haina ajenda kuu yenye mvuto kwa wananchi. Chama hicho kimegeuka kuwa cha kusubiri matukio kisha kuyadandia. Sawa, ni kazi ya vyama vya upinzani kukikosoa chama tawala/kuikosoa serikali, lakini hiyo sio kazi pekee. Na kwa kusubiri matukio, Chadema inakuwa kama "inaendeshwa na CCM."

Niliandika kwa kirefu katika vitabu vyangu viwili kuhusu uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, kimoja kabla ya uchaguzi huo na kingine baada, kwamba asilimia kubwa ya wapigakura nchini Tanzania sio wanachama wa CCM au vyama vya upinzani. Kwamba mtaji  mkubwa kwa chama chochote kinachotaka kushinda uchaguzi ni ku-win hearts and minds za hao wasio na chama chochote. Kundi hili ndilo lililompa ushindi Magufuli mwaka 2015.

Katika hilo, tatizo kubwa la vyama vyetu vya upinzani ni 'kudanganganyana wao kwa wao kuhusu mshikamano, umoja na wingi wao.' Badala ya kufanya jtihada za ku-reach out kudni la watu wasio na vyama, wao wapo bize kuhamasishana wenyewe kwa wenyewe. Basi angalau kuhamasishana huko kungeendana na kuwavuta watu wasio na vyama, ambao ni turufu muhimu kwenye chaguzi zetu.

Nilwahi kuandika huko Facebook, kuwa 'hasira sio mkakati (wa kisiasa)' kwa kimombo "anger is not a strategy.' Sio siri kuwa wafuasi wa upinzani wana hasira, ni hii sio dhambi wala kosa, lakini wanakosea kudhani kuwa hasira hiyo itawaletea mafaniko ya kisiasa. Hawataki kujifunza kwenye mifano hai ya hasira ambazo zimebaki kuwa hasira tu: hasira dhidi ya Tanesko zimeshindwa kuifanya taasisi hiyo iache uhuni wa mgao wa umeme wa milele; hasira dhidi ya huduma mbovu zinazotolewa na baadhi ya makampuni ya simu hazijaziathiri kwa namna yoyote ile; hasira dhidi ya TFF haijaweza kuifanya Taifa Stars iache kuwa kichwa cha mwendawazimu.

Hasira ili iwe na manufaa shurti iambatane na programu makini ya kuleta mabadiliko kusudiwa. Na hili liliusiwa na Dkt Slaa, kwamba mabadiliko ya kweli yatapatikana tu kwa kuwa na programu makini zitakazohusisha watu makini.

Pengine wapinzani watajitetea kuwa zuio la Dkt Magufuli linalokataza mikutano na maandamano ya vyama vya siasa (isipokuwa CCM) limewaathiri kwa kiasi kikubwa katika kujitengenezes mazingira bora ya ushindi kwenye chaguzi hizo. Mie siafikia kabisa zuio hilo la Rasi Magufuli, lakini wapinzani wangeweza kulitumia 'kumpiga bao yeye na CCM' kwa kulitekeleza kwa kuelekeza nguvu zao 'mtaani,' kuwatumikia wananchi zaidi ya 'wanavyoangushwa na CCM/Serikali.'

Nihitimishe makala hii kwa kutoa wito kwa vyama vya upinzani kukaa chini na kufanya post-mortem ya chaguzi za madiwani, na kutengeneza programu makini (sio hizo operesheni zisizo na kichwa wala miguu) zitakazosimamiwa na kutekelezwa na watu makini. Na wafuasi wa vyama hivyo waache kupoteza muda mwingi kwenye kukosoa tu CCM na serikali huku wakikwepa kuelekea focus yao kwenye vyama vyao. Ni hivi, kama vyama vya upinzani vimeweza kumng'oa moja wa madikteta hatari duniani huko Gambia, Yahya Jammeh, basi hakuna sehemu ambapo upinzani hauwezi kukiong'oa chama tawala madarakani. Lakini hilo halitotokea kwa kujidanganya kuwa "CCM inachukiwa sana." Kuchukiwa kwa CCM sio kupendwa kwa Chadema, au Cuf, au chama kingine cha upinzani. 

ANGALIZO: Mada husika ilikuwa kwa ajili ya makala kwenye gazeti la Raia Mwema lakini nimechukua mapumziko ya uandishi wa makala kwenye gazeti hilo wakati nikisubiri marekebisho flani kutoka kwao.


19 Jan 2017

WAKATI Marekani ikijiandaa kwa sherehe ya kuapishwa kwa Rais Mteule Donald Trump hapo keshokutwa, rais huyo mteule amejikuta kwenye ‘kitimoto’ baada ya kumshambulia mjumbe wa Congress (bunge ‘dogo’ la nchi hiyo),mmoja wa wanasiasa wakongwe na mpinzani wa muda mrefu wa ubaguzi wa rangi, John Lewis.
Kama ilivyozoeleka, Trump alitumia akaunti yake katika mtandao wa kijamii wa Twitter kufanya mashambulizi hayo baada ya Lewis, ambaye anaheshimika mno nchini humo kwa kushirikiana na nguli wa haki za watu weusi, marehemu Dk. Martin Luther King, Junior, kueleza bayana kuwa hamwoni Trump kama rais halali wa Marekani. Pia alieleza kuwa itakuwa sio sahihi kukalia kimya ‘mambo yasiyopendeza’ ya Trump.
Kadhalika, Lewis alieleza bayana kuwa kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 30 hatohudhuria sherehe za kumwapisha rais mpya, na anasusia kuapishwa kwa Trump kama njia ya kuonyesha upinzani wake kwa rais huyo mpya.
Trump alimshambulia Lewis katika ‘tweets’ zake ambapo alidai kuwa mwana Congress huyo anapaswa kutumia muda mwingi zaidi kushughulikia eneo analoliwakilisha, ambalo kwa mujibu wa Trump, lipo katika hali mbaya na limegubikwa na uhalifu.
Tweets za Trump dhidi ya Lewis zilizosababisha watumiaji kadhaa wa mtandao huo wa kijamii kumlaani rais huyo mtarajiwa, hasa kwa vile wikiendi iliyopita ilikuwa ya maadhimisho ya kumbukumbu ya Dk. King, siku yenye umuhimu mkubwa kwa Wamarekani weusi.
Hayo yamejiri siku chache tu baada ya Trump kuwa katika ‘vita kubwa ya maneno’ dhidi ya ‘jumuiya ya ushushushu’ (intelligence community), taasisi 16 za ushushushu za nchi hiyo. Sababu kuu ya ‘ugomvi’ kati ya Trump na mashushushu hao ni taarifa iliyowasilishwa kwa Rais Barack Obama, na Trump mwenyewe, kuhusu hujuma za Urusi kwenye uchaguzi mkuu uliopita nchini Marekani.
Taarifa hivyo, ilitanabaisha kuwa Rais wa Urusi, Vladimir Putin ndiye aliyetoa maagizo ya ‘kumsaidia Trump’ na ‘kumuumbua Hillary Cinton, aliyekuwa mpinzani mkuu wa Trump.
Lengo la makala hii sio kujadili siasa za Marekani au vituko vya Trump, bali kutumia matukio hayo kuelezea hali ilivyo sasa huko nyumbani – Tanzania, ambapo kwa kiasi kikubwa suala la uwepo au kutokuwepo kwa baa la njaa linazidi kutawala duru za habari.
Kuna masuala kadhaa yanatokea kwa wakati mmoja. Kubwa zaidi ni kauli ya Rais Dk. John Magufuli sio tu kukanusha taarifa za uwepo wa baa la njaa bali pia kusisitiza kuwa ‘serikali haina shamba’ la kuiwezesha kuwapatia chakula wananchi wanaolalamikia njaa.
Jingine ni tishio kali kutoka kwa Rais Magufuli dhidi ya ‘magazeti mawili’ aliyodai yanaandika habari za uchochezi. Pia aliyashutumu kuwa yamenunuliwa na mfanyabiashara mmoja wa nafaka ili yaandike kuhusu taarifa za uwepo wa baa la njaa, kwa minajili ya mfanyabiashara huyo kuuza nafaka zake.
Binafsi sijashangazwa na tishio la Rais kwa magazeti. Uamuzi wake wa kukaa mwaka mzima bila kuongea na wanahabari ulipaswa kutufahamisha mtazamo wake kwa vyombo vya habari. Ikumbukwe kuwa hata wakati wa kampeni zake za urais mwaka 2015 hakufanya mahojiano na vyombo vingine vya habari, pengine ni kwa bahati tu, alifanya mahojiano na gazeti hili la Raia Mwema tu.
Na hii si mara ya kwanza kwa Rais kuvitupia lawama vyombo vya habari, wiki chache zilizopita alivishutumu kwa kumchonganisha na Rais mstaafu Jakaya Kikwete. Japo haikuwekwa wazi, lawama hizo zilitokana na habari zilizoandikwa na baadhi ya magazeti kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikuwa na mpango wa kupiga mnada mizigo ya taasisi ya WAMA iliyo chini ya mama Salma Kikwete. Kusema magazeti yalizusha habari hiyo ni kuyaonea kwa sababu chanzo cha habari kilikuwa taasisi ya serikali, TRA.
Binafsi nabaki najiuliza, hivi kweli kama kuna magazeti yanalipwa kufanya uchochezi, yangekuwepo huru hadi kufikia hatua ya Rais ‘kuyananga’ bila kuyataja jina? Je, Idara Habari (MAELEZO) na wizara yenye dhamana ya vyombo vya habari, na waziri husika (Nape Nnauye) wamelala usingizi mzito kutojua hayo hadi Rais aliposhtuka na kuweka suala hilo hadharani?
Kwa mtazamo wangu, nadhani tishio la Rais limelenga kutisha vyombo vyote vya habari na sio magazeti hayo mawili tu. Kwamba wanahabari wasiandike kitu kisichompendeza Rais.
Rais hataki kusikia habari kuhusu tishio la baa la njaa. Hata wito wa viongozi wa kidini Wakristo na Waislam kuwataka waumini wao wafanye sala/dua kuombea mvua na kuepushwa na baa la njaa haujamfanya Rais kubadili msimamo wake.
Na muda mfupi kabla ya kuandaa makala hii nimeona video ya mkutano wa Rais huko Magu, ambapo wakati akihutubia, baadhi ya wananchi walisikika wakisema “njaa baba,” na Rais akawajibu “njaa… unataka nikakupikie mimi chakula?”
Binafsi sidhani kama Rais anahitaji ‘kisingizio’ cha kufungia magazeti, yawe mawili au yote. Lakini pia Rais asiwe mkosefu wa shukrani kwa mchango wa magazeti katika kumfikisha Ikulu, kwa kufikisha ujumbe wake binafsi na chama chake wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2015.
Lakini ni muhimu pia Rais atambue kuwa hizi sio zama za Radio Tanzania, Uhuru na Mzalendo, na Daily News na Sunday News pekee. Huu ni mwaka 2017, tupo katika zama za digitali ambapo upashanaji wa habari una njia lukuki, kuanzia Whatsapp hadi mitandao ya kijamii kama Twitter, Facebook, Instagram, nk. Katika zama hizi, kufungia chombo cha habari hakuzui usambazaji wa habari muhimu miongoni mwa wananchi.
Nihitimishe makala hii kwa wito huu kwa Rais wangu, mara kadhaa amekuwa akituomba sisi wananchi tumsaidie katika uongozi wake. Na moja ya misaada ambayo watu wengi wamekuwa wakimpatia ni kumsihi apunguze ukali, ajaribu kutumia lugha ya kidiplomasia, na asiogope kukosolewa.

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

12 Jan 2017

MIONGONI mwa kauli maarufu zaidi za Rais John Magufuli ni ile ya kuwaomba Watanzania wamwombee na msema kweli ni mpenzi wa Mungu.
Kwa bahati mbaya au pengine kwa makusudi, Rais amekuwa mtu wa kwanza kukiuka kauli hizo au kuziweka katika mazingira magumu kutekelezeka.
Nianze na hiyo kauli ya kuwataka Watanzania wamwombee. Pengine wakati ambao alielezea kwa undani mantiki ya kauli hiyo ni wakati wa uzinduzi wa bunge mwaka jana, ambapo alizungumzia kwa undani ugumu unaoikabili vita dhidi ya rushwa na ufisadi.
Katika hotuba hiyo, aliwafahamisha Watanzania kuwa wanaohusika na rushwa na ufisadi sio watu wadogo, kwa maana kwamba ni watu wenye uwezo mkubwa. Na kwamba licha ya dhamira yake na jitihada zake, angehitaji sio tu ushirikiano wa wananchi bali sala na dua zao pia.
Niwapeleke kando kidogo kabla ya kubainisha kwa nini nimeandika Rais amekuwa mtu wa kwanza kukiuka kali zake mwenyewe. Katika sosholojia, kuna kanuni moja inayofahamika kama ‘Social Exchange.’ Kwa kifupi, pamoja na mambo mengine, kanuni hii inaelezea kuhusu uhusiano (interactions) kati ya watu katika jamii.
Kanuni hiyo inatanabaisha kuwa uhusiano kati yetu katika jamii huongozwa na ‘zawadi’ (rewards) na ‘gharama’ (costs). Na watu wengi huongozwa na kanuni (formula) hii: thamani (ya mtu) = zawadi – gharama. ‘Zawadi’ ni vitu vizuri kama vile pongezi, shukrani, kuombewa dua, nk ilhali gharama ni hasara, mtendewa kutoonyesha shukrani, kupuuzwa, nk.
Mfano rahisi: ukipita mtaani, ukakutana na ombaomba, ukampatia hela kidogo, kisha akanyoosha mikono angani kukushukuru, basi kuna uwezekano mkubwa wa kumsaidia tena siku nyingine. Na si ombaomba tu, bali hata ndugu, jamaa au rafiki au ‘mtu baki’ ambaye anashukuru anaposaidiwa.
Lakini laiti ukimpatia msaada ombaomba, au mtu mwingine, kisha asionyeshe kujali msaada huo, basi uwezekano wa kumsaidia tena ni hafifu. Kwa mujibu wa kanuni yetu ya ‘thamani = zawadi – gharama,’ msaidiwa akionyesha shukrani inakuwa zawadi yenye thamani zaidi ya gharama, ilhali kwa asiyeonyesha shukrani gharama inakuwa kubwa kuliko zawadi. Natumaini hizi ‘hisabati’ hazijakuchanganya ndugu msomaji.
Kimsingi, kanuni hiyo inaambatana na matarajio ya ‘nipe nikupe’ (give and take). Kwamba katika kila tunalofanya, tunakuwa na matarajio fulani. Kwamba tunapokwenda kwenye nyumba za ibada, tuna matarajio ya kumridhisha Mola kwa vile tunafuata anachotarajia kwetu: sala/ibada kwake.
Tunapokuwa watu wa msaada, au wakarimu, au wema, nk tunatarajia wale tunaowafanyia hivyo wathamini tabia zetu hizo nzuri.
Turejee kwa Rais Magufuli. Hivi karibuni, akiwa ziarani mkoani Kagera, aliwaambia wananchi kuwa, ninamnukuu; “Serikali na wananchi kila mmoja abebe msalaba wake mwenyewe.’’ Alitoa kauli hiyo alipozungumzia misaada kwa waathirika wa tetemeko la ardhi lililoyakumba maeneo ya Ukanda wa Ziwa hususan Mkoa wa Kagera.
Mwaka jana nilipokuwa naomba kura kwenu, sikuomba tetemeko la ardhi litokee hapa, hili ni jambo ambalo liko nje ya uwezo wangu, tunaomba kila mmoja aweze kutumia msaada uliotolewa ili kurejesha miundombinu ya makazi yenu” alieleza Dk. Magufuli.
Bila kuingia kiundani kuchambua mantiki ya kauli hiyo ya Rais, yayumkinika kuhitimisha kuwa kama “kila mtu abebe mzigo wake mwenyewe” basi na ombi lake maarufu kwa wananchi la “mniombee” alibebe yeye mwenyewe. Ajiombee.
Naandika hivyo kwa sababu, kiustaarabu tu, kuna baadhi ya maneno hayastahili kusemwa katika mazingira ya maombolezo, misiba, nk. Rais ni kama mzazi. Na japo kila mzazi ana jukumu la kuwa mkweli, anapaswa pia kuwa na busara ya kuchagua maneno yanayoweza kuwasilisha ujumbe bila kuumiza mioyo ya watu.
Hivi Rais angeeleza kwa lugha ya upole kuwa uwezo wa serikali ni mdogo na haitomudu kumjengea nyumba kila mwananchi, lakini itashirikiana na wananchi kadri itakavyoweza, ikiwa ni pamoja na kuendelea kuhamasisha misaada kwa waathirika, asingeeleweka? Au angeonekana sio ‘Rais kamili’?
Kwa mujibu wa ‘social exchange theory,’ matarajio ya Watanzania wanaaombwa na Rais wao kuwa wamwombee si kumsikia akiwaambia “kila mtu abebe mzigo wake mwenyewe” hususan mbele ya watu wanaoendelea kukabiliana na athari za janga la tetemeko la ardhi.
Lakini kama hilo la “kila mtu atabeba msalaba wake mwenyewe” halitoshi, Rais Dk. Magufuli akakiuka kauli yake maarufu ya “msema kweli mpenzi wa Mungu” kwa kutoa maelezo yasiyo sahihi, kwamba (ninamnukuu) “Kuna nchi kama Japan na Italia, zimekuwa zikikumbwa na matetemeko mengi, haijawahi kutokea serikali yao ikawajengea nyumba upya isipokuwa inarejesha miundombinu ya taasisi za umma kama vituo vya afya, shule na barabara.”
Sio heshima wala nidhamu kusema “Rais amedanganya” lakini alichoongea kina kasoro. Kwa Italia, baada ya tetemeko lililotokea mwezi Agosti mwaka jana, Waziri Mkuu wa zamani Mateo Renzi alishughulikia upitishwaji wa sheria ya kuidhinisha Euro bilioni 4.5 kwa ajili ya waathirika na miundombinu. Euro bilioni 3.5 kwa ajili ya waathirika na euro bilioni kwa ajili ya majengo ya umma.
Kutegemea eneo, sheria iliidhinisha malipo kati ya asilimia 50 hadi 100 kwa wananchi ambao nyumba zao ziliharibiwa na tetemeko hilo.
Huko Japan nako, mara tu baada ya tetemeko kubwa la ardhi la mwaka 2011, serikali ilichukua hatua kadhaa kuwasaidia waathirika ikiwa ni pamoja na fedha za rambirambi kwa kila familia iliyopoteza ndugu katika janga hilo (Yen milioni 5), fedha kwa familia zenye majeruhi (Yen milioni 3), misaada ya fedha kwa kila familia na mikopo yenye masharti nafuu kwa kila familia (Yen milioni 3.5), mikopo maalumu kwa watu/biashara waliokuwa na madeni kabla ya tetemeko,  ahueni ya kodi mbalimbali kwa waathirika wote, malipo kwa waliopoteza ajira (unemployment benefits), mkakati maalumu wa utengenezaji ajira mpya, na hatua nyinginezo.
Kanuni za tawala zetu za kiafrika zipo wazi: “kiongozi huwa hakosei, na akikosea huwa amenukuliwa vibaya, na kama ikithibitika amekosea haina haja ya kumradhi.” Sitarajii kusikia tamko lolote kwamba “Kauli ya Rais kuwa ‘Kuna nchi kama Japan na Italia, zimekuwa zikikumbwa na matetemeko mengi, haijawahi kutokea serikali yao ikawajengea nyumba upya’ haikuwa sahihi. Anaomba radhi.”
Wakati wa kampeni zake za kuwania urais na hata baada ya kushinda urais, Dk. Magufuli amekuwa akituomba mara kwa mara kuwa tumsaidie. Makala hii ni mwitikio wa ombi hilo. Ni mchango wangu wa msaada kwake kumsihi ajaribu kuepuka lugha inayoweza kujenga tafsiri mbaya.
Kadhalika, suala la kusaidia wenzetu waliokumbwa na tatizo sio la kisheria, kisera au ki-kanuni, au kwa vile fulani hakufanya, bali ni suala la utu. Na utu ni kama pale Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba alipomtembelea mzazi wa msanii Chid Benz, kuangalia uwezekano wa kumsaidia msanii huyo aliyeathirika na matumizi ya dawa za kulevya. Ni utu kwa sababu, kisheria, anachofanya msanii huyo (kununua na kutumia mihadarati) ni kosa la jinai (Ibara ya 15 ya Sheria mpya ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya ya mwaka 2015).
Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli kwamba pamoja na dhamira yake nzuri kuitumikia nchi yetu kwa uwezo wake wote, na licha ya Watanzania kuwa na matumaini makubwa kwake, ni muhimu sana ajaribu ‘kupunguza makali’ kwenye lugha yake. Kama nilivyoeleza katika makala yangu iliyopita, ‘lugha ya ukali’ inaweza kujenga nidhamu ya uoga, kitu ambacho kitakwaza jitihada za Rais wetu kuijenga Tanzania tunayostahili. Ninatumaini Rais ataupokea ushauri huu na kutoona kuwa anakosewa heshima kwa kusahihishwa pale alipokosea.
Mungu ibariki Tanzania

Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  

11 Jan 2017

Kwamba Rais wa Russia, Vladimir Putin na watu wake wa karibu, walitaka mgombea urais wa chama cha Republican cha Marekani, Donald Trump, ashinde uchaguzi wa Urais uliofanyika Novemba mwaka jana, wala sio siri. 

Ilishafahamika kabla ya uchaguzi huo kuwa Putin na "watu wake" hawakutaka Trump awe rais kwa vile wanampenda bali walikuwa na ajenda na maslahi binafsi. Hata hivyo, hadi muda huu ilikuwa haifahamiki ni kitu gani hasa kilichokuwa kikimfanya Rais huyo wa Russia na mashushushu wake kupigana kufa na kupona kuhakikisha Trump anashinda katika uchaguzi huo, kitu ambacho kwa hakika kilitokea.

Kadhalika, Putin na Russia walishapata ushindi hata kabla ya uchaguzi baada ya duru za kiintelijensia, ndani na nje ya Marekani, kuthibitisha kuwa kiongozi huyo wa Russia na mashushushu wake walikuwa wakihujumu uchaguzi huo. Kiintelijensia, huo ni ushindi hata kama matokeo yake hayakujulikana muda huo.

Kwa 'kumwezesha Trump kushinda,' Putin na mashushushu wake waliibuka na ushindi mkubwa zaidi, pengine wa kihistoria katika 'vita ya muda mrefu ya kijasusi kati ya Russia na Marekani.' Kwa 'macho ya kawaida,' nchi hizo mbili zilionekana kama zina maelewano bora kuliko ilivyokuwa katika zama za Vita Baridi. Lakini 'kizani,' nchi hizo zimekuwa kwenye vita kali ya kijasusi, na ambayo inaelezwa kuwa pengine ni kubwa kuliko ilivyokuwa katika zama za Vita Baridi. Hiyo ni mada ya siku nyingine.

Ijumaa iliyopita, wakuu wa taasisi za ushushushu za Marekani walikutana na Rais Mteule Trump kumfahamisha kuhusu uchunguzi wao uliohitimisha kwamba Russia ilihujumu uchaguzi wa Rais wa Marekani, ambao Trump aliibuka kidedea.


Awali kabla ya mkutano huo nyeti, bosi mkuu wa taasisi za ushushushu za Marekani, Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa (DNI), James Clapper (pichani chini), aliieleza kamati ya bunge la seneti kuwa hujuma zilizofanywa na Russia zipo katika sura nyingi zaidi ya kudukua taarifa za chama cha Democrats, na kumhujumu mpinzani wa Trump, mwanamama Hillary Clinton.

2017-01-05t153806z-1958236086-rc17375221c0-rtrmadp-3-usa-russia-cyber-clapper.jpg

Lakini sasa taarifa zilizopatikana baada ya mkutano wa wakuu hao wa taasisi za ushushushu na Trump zinaeleza kuwa Russia ina kitu kinachofahamika kishushushu kama 'compromising information' kumhusu Trump. Maelezo ya kina kuhusu 'compromising information' yapo katika kitabu changu cha SHUSHUSHU (kinunue hapa), lakini kwa kifupi, ni taarifa ambazo mashushushu wanazo dhidi ya mtu na wanaweza kuzitumia kumshurutisha afanye wanachohitaji wao. Mfano hai, mwanasiasa mmoja huko nyumbani aliwahi kunaswa akifanya 'kitu flani,' kikanukuliwa na 'wahusika,' na amebaki kuwa 'compromised' pengine milele.


Muhtasari wenye kurasa mbili ulioambatana na taarifa ya taasisi hizo za kishushushu za Marekani kuhusu hujuma za Russia ulijumuisha madai kwamba mashushushu wa Rusia wana 'compromosing information' kuhusu Trump. 

Taarifa hiyo imechangiwa na kazi iliyofanywa na jasusi mmoja mstaafu wa Uingereza ambaye kazi zake huko nyuma zinachukuliwa na taasisi za kishushushu za Marekani kuwa ni za kuaminika.

Imefahamika kuwa shirika la ushushushu wa ndani la Marekani, FBI, hivi sasa lipo katika uchunguzi kubaini ukweli kuhusu hizo 'compromising information' kuhusu Trump.

Hata hivyo, inaelezwa kwamba tetesi kwamba Russia 'ina nyeti kuhusu Trump' zimekuwa zikizagaa kitambo japo hazikuwahi kuzungumzwa na taasisi za kishushushu.

Taarifa moja ya kishushushu 'iliyotolewa usiri' (unclassified) iliyowekwa hadharani Ijumaa iliyopita ilitanabaisha kuwa Putin binafsi alitoa amri ya Russia kumsaidia Trump  kwa kumuumbua mpinzani wake, Hillary. 

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa Idara ya ushushushu wa kijeshi ya Russia, GRU, ilikitumia kikundi cha wadukuzi cha WikiLeaks kuvujisha baruapepe mbalimbali kumhusu Hillary na wasaidizi wake wakati wa kampeni za urais zilizomalizika Novemba mwaka jana na Trump kuibuka mshindi.

Endelea kutembelea tovuti hii kwa habari kama hizi kuhusu USHUSHUSHU (bonyeza hapo juu kabisa mwa ukurasa huu palipoandikwa 'intelijensia') na habari nyinginezo.

CHANZO: Habari hii imetokana na vyanzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na HIKI.

9 Jan 2017


Moja ya vipimo kuwa unaitumia vema mitandao ya kijamii ni idadi na aina ya marafiki unaotengeza kupitia mitandao hiyo. Binafsi, nimetengeneza marafiki wengi mno, wanaotoka kada mbalimbali za maisha: wanasiasa, wanataaluma, wasanii, wajasiamali, wakulima, wanafunzi/wanavyuo, na takriban kila kada ya watu.

Ni kwa sababu hiyo ndio maana sio tu ninaiheshimu sana mitandao ya kijamii lakini pia huwa makini kulinda 'hadhi' yangu mtandaoni. Kadri unavyotengeneza marafiki wengi ndivyo unavyokuwa katika nafasi kupata madhara makubwa zaidi iwapo mtu atakuchafua. 

Mmmoja ya watu nilofahamiana kupitia mitandao ya jamii ni Mhadhiri wa chuo kikuu cha London (University of London), katika Shule ya Stadi za Asia na Afrika (School or Oriental and African Studies - SOAS).

Nilifahamiana na Dkt Hannah mwishoni mwa mwaka jana huko kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Na kilichotufanya tufahamiane ni kuvutiwa na mapenzi yake kwa Kiswahili. Kila siku, Dokta Hannah hutwiti 'neno la siku' (word of the day) la Kiswahili, kisha kulielezea kwa Kiingereza.

Awali nilidhani ana asili ya Tanzania au nchi inayoongea Kiswahili, kwa sababu Kiswahili chake ni fasaha kabisa. Ikabidi nimdadisi. Kwa mshangao mkubwa, kumbe mhadhiri huyu ni Mwingereza wa asili, na wala Kiswahili sio lugha yake ya asili. Alijifunza tu wakati anafanya tafiti zake huko Tanzania na katika nchi nyingine za Afrika Mashariki. 

Licha ya kuwa mhadhiri, Dkt Hannah ni 'postdoctoral research fellow' (huu utakuwa mtihani wangu na wake kutafuta neno stahili la Kiswahili). Kwa kifupi, mtu anayefanya 'postdoctoral fellowship' ni mhitimu wa shahada ya uzamifu anayeendelea na tafiti za kitaaluma. 

Eneo lake kuu la utafiti ni jinsi lugha zinavyokutana na zinavyobadilika, mkazo wake ukiwa kwenye lugha za Kibantu katika eneo la Afrika Mashariki.

Kwa sasa anafanya utafiti kuhusu mabadiliko ya kisarufi katika lugha za makabila ya Tanzania na Kenya, yaani Kirangi, ki-Mbugwe, ki-Gusii, Kikurya, ki-Ngoreme, ki-Suba Simbiti.

Habari njema zaidi ni kwamba Dkt Hannah amekubali kushiriki jitihada za kuenzi, kudumisha, kuboresha na kukitangaza Kiswahili kupitia kampeni maarufu ya #ElimikaWikiendi. Taarifa zaidi kuhusu ushiriki wake zitatolewa wakati mwafaka. 

Tovuti binafsi ya Dkt Hannah ipo HAPA na unaweza kum-follow Twitter anatumia @itsthegibson

Orodha ya machapisho yake ya kitaaluma:
 

Book Chapters

Gibson, Hannah and Koumbarou, Andriana and Marten, Lutz and van der Wal, Jenneke (2017) 'Locating the Bantu conjoint/disjoint alternation in a typology of focus marking.' In: van der Wal, Jenneke and Hyman, Larry M., (eds.), The conjoint/disjoint alternation in Bantu. Mouton de Gruyter . (Trends in Linguistics. Studies and Monographs) (Forthcoming)
Gibson, Hannah and Marten, Lutz (2016) 'Variation and grammaticalisation in Bantu complex verbal constructions: The dynamics of information growth in Swahili, Rangi and siSwati.' In: Nash, Léa and Samvelian, Pollet, (eds.), Approaches to Complex Predicates.Leiden: Brill, pp. 70-109. (Syntax and Semantics)

Journal Articles

Gibson, Hannah (2016) 'A unified dynamic account of auxiliary placement in Rangi.' Lingua, 184. pp. 79-103.
Seraku, Tohru and Gibson, Hannah (2016) 'A Dynamic Syntax modelling of Japanese and Rangi clefts: Parsing incrementality and the growth of interpretation.' Language Sciences , 56 (2016). pp. 45-67.
Gibson, Hannah and Wilhelmsen, Vera (2015) 'Cycles of negation in Rangi and Mbugwe.' Africana Linguistica, 21. pp. 233-257.
Marten, Lutz and Gibson, Hannah (2015) 'Structure building and thematic constraints in Bantu inversion constructions.' Journal of Linguistics, 52 (3). pp. 565-607.
Gibson, Hannah (2015) 'The dynamics of structure building in Rangi: At the Syntax-Semantics interface.' Cambridge Occasional Papers in Linguistics, 8. pp. 41-55.
Gibson, Hannah (2013) 'Auxiliary placement in Rangi: A case of contact-induced change?' SOAS Working Papers in Linguistics, 16. pp. 153-166.

Book Reviews



Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.