Showing posts with label ELIMU TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label ELIMU TANZANIA. Show all posts

2 Mar 2013


MIONGONI mwa habari ambazo zinatawala kwenye vyombo mbalimbali vya habari nchini mwetu, ni matokeo ya kutisha ya mitihani ya kuhitimu kidato cha nne, ambapo zaidi ya asilimia 60 ya watahiniwa wamefeli.
Ingawa matokeo hayo yamewashitua wengi, lakini kimsingi halikuwa jambo lisilotarajiwa. Kwa muda mrefu, sekta ya elimu imekuwa ikipewa kipaumbele kwa kauli zaidi kuliko vitendo vya dhati. Wakati chama tawala, CCM, ambacho kwa vyovyote vile hakiwezi kukwepa lawama kuhusu matokeo hayo mabovu, kimekuwa mahiri kuonyesha kuwa kinathamini sana umuhimu wa elimu, na hivyo kuipigia mstari katika kila manifesto zake za chaguzi kuu zilizopita, ukweli unabaki kuwa sekta ya elimu imekuwa ikipuuzwa.
Pengine, huwezi kuelewa mazingira mabovu yanayozikabili shule mbalimbaliza msingi na sekondari mpaka utoke nje ya miji. Kimsingi, wanafunzi wengi katika maeneo ya vijijini wanasoma katika mazingira magumu sana, na kitu pekee kinachowasukuma wazazi kupeleka watoto wao shuleni ni ukweli kuwa bado wanaamini kuwa elimu ni ufunguo wa maisha, hata kama ufunguo huo umepotea au haupo kabisa!
Binafsi, nadhani moja ya sababu kubwa za matokeo hayo mabaya ni mgogoro wa muda mrefu kati ya Serikali na walimu. Kilio kikubwa cha walimu kimekuwa ni kuitaka Serikali iboreshe mazingira ya utoaji na upatikanaji wa elimu, hususan kwenye maeneo ya mishahara na makazi ya walimu, pamoja na vitendea kazi vyao, sambamba na nyenzo muhimu kwa wanafunzi kama vile madarasa na madawati.
Hata hivyo, kama ilivyozoeleka kila inapojitokeza migogoro kati ya Serikali na watumishi wake, ubabe ulitawala kuliko busara. Pasi kujali busara kuwa ‘unaweza kumpeleka punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji,’ walimu walipoonyesha dalili ya kuchoshwa na ‘kupuuzwa kwao’ na kufanya migomo ya hapa na pale, walishurutishwa kurejea mashuleni kufundisha.
Pengine walimu wanaweza kulaumiwa kwa matokeo hayo mabaya, na tayari kuna taarifa kuwa watachunguzwa na Serikali, lakini ni muhimu kabla ya kuwalaumu tukaelewa kwa undani mazingira ya kazi ya walimu wetu.
Binafsi, ni mhanga wa kumomonyoka kwa mfumo wetu wa elimu, ingawa si kwa kiasi kikubwa. Nilikuwa miongoni mwa wanafunzi wa kwanza wa shule ya sekondari ya Kilombero, kule Ifakara, mkoani Morogoro, ilipoanzishwa mwaka 1986.
Pamoja na kufanikiwa kuwa mmoja wa wanafunzi wanne waliopata daraja la kwanza miaka minne baadaye, lakini ukiachilia mbali masomo ya sanaa (arts), tulisoma masomo ya sayansi kama vile Kemia, Fizikia na Baiolojia kwa nadharia tu kwani maabara yetu ilikuwa ya kufikirika zaidi kuliko uhalisia.
Nilipokwenda kidato cha tano katika shule ya sekondari ya Wavulana Tabora (Tabora Boys’), nikakumbana na tatizo la ukosefu wa mwalimu wa somo la Jiografia, ambapo ilitulazimu kwenda shule ya jirani ya Sekondari ya Wasichana Tabora (Tabora Girls’) kumfuata mwalimu wa somo hilo. Na japo nilifanya vizuri kwenye mitihani ya kuhitimu kidato cha sita, uzoefu niliopata unanikumbusha mengi kuhusu sekta ya elimu huko nyumbani.
Lakini angalau wakati huo nilipokuwa mwanafunzi kulikuwa hakuna vitu vinavyoweza ‘kumpa faraja feki mwanafunzi.’ Hapa ninazungumzia maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano ambapo tunakutana na vitu kama Facebook,YoutTube, BBM na kadhalika.
Ingawa kwa maeneo ya vijijini upatikanaji wa teknolojia hiyo bado ni wa kubahatisha, ni rahisi kwa wanafunzi wa mijini ‘kumalizia hasira zao za shuleni’ kwa ku-chat kwenye Facebook, kutumiana meseji kupitia BBM au kuangalia video huko YouTube!
Na ni wazi kuwa mwanafunzi anayetumia muda mwingi kwenye vitu kama hivyo, anajinyima nafasi ya kujisomea na hivyo kujitengenezea mazingira mazuri ya kufeli. Lakini wakati ni rahisi kukilaumu ‘kizazi cha Facebook’ ni vema tukatambua pia ili mwanafunzi aweze kujisomea, sharti awe na kitu cha kusoma.
Ukichanganya ufundishaji wa walimu ‘wanaofunika kombe ili mwanaharamu apite’ (wanatimiza tu wajibu wao) na uhaba wa vitabu vya kiada, hata mwanafunzi mwenye kiu ya kujisomea binafsi anakuwa na wakati mgumu kufanya hivyo.
Tukiweka kando lawama, ni vigumu japo kufikiria jinsi taifa letu linavyoweza kuirejesha elimu kwenye viwango kama vile vya zama za Ujamaa. Ninasema ni vigumu kwa vile kinachohitajika zaidi si kauli za porojo, bali uwekezaji wa kutosha katika sekta ya elimu.
Na ili uwekezaji huo uwezekano, inalazimu kuwapo na fedha. Sasa wakati Tanzania yetu inakabiliwa na deni la ndani na nje lenye thamani ya matrilioni ya Shilingi, na huku watawala wakigoma kuelewa kuwa sisi ni masikini na tunapaswa kupunguza matumizi ya anasa zisizo za lazima, tutakuwa tunajidanganya tukidhani kuwa uwekezaji huo katika sekta ya elimu utawezekana.
Vipaumbele vya watawala wetu vipo katika kuboresha maslahi ya wabunge badala ya kuboresha walau mazingira tu ya shule zetu, achilia mbali maslahi ya walimu. Ni busara gani iliyotumika kuongeza posho na mishahara ya wabunge wetu hadi kufikia zaidi ya Shilingi milioni 10 kwa kila mmoja ilhali shule kadhaa hazina madawati na majengo yake ni ya ‘mbavu za mbwa?’
Kuwaruhusu wanafunzi waliofeli warudie mitihani ilhali watajiandaa na mitihani hiyo katika mazingira yaleyale yaliyowafelisha mwanzoni, ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu. Kuwachunguza walimu ilhali sababu zilizopelekea matokeo mabaya zinajulikana, ni kutafuta mchawi asiyekuwapo.
Lakini tunaweza kwenda mbali zaidi na kuihoji Serikali kama kweli inathamini sekta ya elimu. Hivi kama Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo, anaamini kuwa Muungano wa Tanzania ni matokeo ya Muungano wa visiwa vya Zimbabwe na Pemba, tutarajie nini kwa mwanafunzi wa kawaida?
Na Waziri Mulugo anataka Serikali isilaumiwe, bali wadau wote wa elimu waangalie uwajibikaji katika nafasi zao. Kwanini asionyeshe mfano kwa kuwajibika yeye kwanza, kisha adai wengine waige mfano wake? Kimsingi, huyu mtu hakustahili kuendelea kushika wadhifa huo baada ya ‘mchemsho’ wake wa Muungano. ‘He is a pretty bad influence.’
Nimalizie makala haya kwa kuikumbusha Serikali kuwa mpango wake kabambe wa maendeleo ambao unaojumuisha hatua kama kuwawajibisha mawaziri walioshindwa kazi, hauwezi kufanikiwa kwa stahili hii inayoonekana katika picha hii. Badala ya kusubiri mawaziri waboronge, ingekuwa vema mpango huo ukaanza kwa mifano hai na kumwajibisha Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, ambaye ameshatamka kuwa hatojiuzulu, na Naibu wake Mulugo, ambaye ameshaliaibisha taifa vya kutosha.



14 Feb 2013


Walimu wote waliopewa ajira ya Ualimu Serikalini ambao majina yao yametangazwa katika tovuti za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na Ofisi ya Waziri Mkuu- TAMISEMI, wanatakiwa kuripoti tarehe 01 Machi 2013 kwenye Ofisi za Wakurugenzi wa Halmashauri walikopangiwa kwa ajili ya kupangiwa Vituo vya kazi. HAKUNA MABADILIKO YA VITUO VYA KAZI YATAKAYOFANYWA. Mwalimu anatakiwa kwenda na vyeti vyake halisi vya taaluma na cheti cha kuzaliwa pamoja na nakala zake. Mwalimu ambaye hataripoti ifikapo tarehe 9 Machi 2013 atapoteza nafasi hiyo.

NB: WALIMU WALIOKWISHA AJIRIWA WARUDI KWA WAAJIRI WAO



19 Jan 2012



Kwanza Tunapenda wasalimu wakubwa wetu Shikamoo na vijana wenzetu Mambo vipi..  Tunatambua kuwa Wanavyuo wenzetu walimu walikuwa hawana kazi kwa muda mrefu Jambo ambalo liliwafanya wengi kuwa na wasi wasi na mwajiri wao. Tunapenda kuwapa tarifa kupitia mtandao wenu wa Matukio na wanavyuo (www.tzwanavyuo.blogspot.com)  kuwa, Walimu wahitimu wote  Jana usiku majira ya sa saba Nafasi hizo zilitangazwa Rasmi, Pia sisi Tunapenda kuwasilisha majina ya wanafunzi ambao wamechaguliwa Tunaomba mchukue Muda wenu kutazama kwa umakini majina yenu yote yapo hapa. Hongereni sana.


Imeandaliwa na,
Matukio na Wanavyuo Crew 

19 Sept 2011

 
SALAM,
Habari zenu wadau wote popote Duniani Tunapenda kuwasalimu wakubwa Shikamoo na tulio Umri sawa Mambo zenu!, Baada ya salamu hizi tunapenda kuwaletea habari njema sana kwa wazazi na wanafunzi ambao walikuwa wamefanya mtihani kidato cha sita lakini hawakufanikiwa kuyaona majina yao wakati wa Selection ya kwanza, Lakini muda sio mrefu sana yametoka majina mapya ya Second Selection ambapo utaweza Bahatika kuliona jina lako, la ndugu yako, rafiki ama mwanao. Tunawaomba mkipata taarifa hii muwape na wengine pia ili wapate kutazama majina hayo. mwisho tunawapa hongera sana wale walio chaguliwa kwa mala ya kwanza na hawa ambao mmechaguliwa kwa mala ya pili. Web site ya Matukio na wanavyuo itaendelea kuwaletea habari zaidi za vyuo mbali mbali Tanzania. 

Nyongeza: Tunaomba sana ushirikiano wenu uongozi wa vyuo mbali mbali Tanzania, ikiwa ni kututumia matukio mbali mbali ambayo yanatokea katika vyuo vyenu, mfano mikutano,mahafari na mambo kama hayo, pia kama mna applications za kutaka wanafunzi wajiunge na vyuo vyenu pia tunakaribisha sana na matangazo mengine. Kwa wanafunzi wa vyuo mbali mbali Tanzania pia tunawaomba ushirikiono wenu wa ukaribu wa kututumia matukio mbali mbali sisi ni wasimamizi tuu wa kupost habari lakini mshiriki mkuu ni wewe msomaji na mtumaji wa matukio. Lengo ni kuwaunganisha wanafunzi wote wa vyuo Tanzania. Pamoja tunaweza 

Matukio yote ama kitu chochote tutumieni kupitia Barua pepe: [email protected]
Asanteni sana
Matukio na wanavyuo Crew


BOFYA HAPA CHINI KUONA MAJINA HAYO
 

6 Oct 2010





Kwa hisani ya SUBI

4 Jun 2009

Nimekumbana na picha hii katika tovuti ya IPPMEDIA.Tujiulize:Taifa la kesho (kama wanavyopenda kusema wanasiasa) linaloandaliwa katika mazingira ya aina hii litatengeneza Watanzania wa aina gani?Yayumkinika kusema CHUKI,HASIRA,LAWAMA,na vitu kama hivyo ndio vinavyotawala vichwani mwa madogo hawa na vitaendelea kutawala.Je haya ndio maisha bora waliyotuahidi CCM 2005?


21 Apr 2009


Baraza la Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) limepitisha uamuzi wa kuishirikisha Tume ya Uchaguzi Tanzania (NEC) kuhakiki vyeti vya wote wanaoomba kuwania nafasi za kisiasa ili sifa zao kielimu zitambulike.

Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Mayunga Nkunya, aliwaambia waandishi wa habari jana Dar es Salaam, TCU imewasiliana na NEC kwa barua, ili utaratibu huo uanze kutumika katika uchaguzi mkuu ujao mwakani.

Nkunya alitoa taarifa hiyo wakati akizungumzia maonyesho ya vyuo vikuu yaliyoandaliwa na TCU yatakayoanza kesho hadi Aprili 24, mwaka huu. “Baraza letu limepitisha uamuzi ili watu wanaotaka kugombea nafasi za kisiasa, vyeti vyao vihakikiwe, ili akipita sifa ijulikane rasmi kama ni daktari basi awe daktari na si daktari feki,” alisema Profesa Nkunya.

Hatua hiyo ya tume inatokana na kilichoelezwa na Nkunya kuwa ni kukithiri kwa vyuo na vyeti bandia nchini, jambo ambalo alisema wamejipanga kulivalia njuga kwa kushirikiana na wadau ili kuhakikisha Tanzania haiangamii kitaalamu na kitaaluma.

Alisema orodha ya vyuo visivyotambulika vya nje ambavyo Watanzania wengi wakiwamo mawaziri na wabunge wamesoma, ni ya kweli na kwamba kama kuna mtu anahisi kuonewa ruhusa kwenda mahakamani...ENDELEA

CHANZO: Habarileo.

TAMKO ZURI LAKINI LINALOSTAHILI UMAKINI KATIKA KULIAMINI.HAWA TCU WAKATI WANAZUNGUMZIA UCHAGUZI WA 2010,WANATAKA KUTUMBIA HAWAKUWEPO 2005?AU WATAPATA NGUVU HIYO 2010?JE KAMA SASA WANASHINDWA KUWASHUGHULIKIA HAO "MADAKTARI WA FALSAFA" WALIOKWAA SHAHADA ZAO MTANDAONI TUTAAMINI VIPI KUWA WATAWEZA HIYO 2010?
TATIZO LA NCHI YETU SIO SHERIA,KWANI ZIMEKUWEPO TANGU TUNAKABIDHIWA UHURU NA MKOLONI.TATIZO NI UTEKELEZAJI WA SHERIA HIZO.KUNA MBUNGE ALIKUWA NA TUHUMA ZA KUFOJI ELIMU (SIO YA CHUO KIKUU) BALI YA SEKONDARI.CHA AJABU HADI LEO "ANAPETA".JE HII HAILETI USHAWISHI KWA VIHIYO WENGINE KUJARIBU BAHATI ZAO?

TATIZO LA PILI LA NCHI YETU SIO SHERIA BALI UTEKELEZAJI WAKE UNAOELEMEA ZAIDI AINA YA MKOSAJI.YALEYALE YA ANAEIBA KUKU KWA NJAA KUITWA MWIZI LAKINI ANAYEFUJA MABILIONI ANAOTWA M-BADHIRIFU (NA SANASANA BADALA YA KWENDA JELA ATAHAMISHWA KITUO CHA KAZI).KUNA SHERIA KWA AJILI YA VIGOGO (KAMA AKINA CHEYO WANAOUA KWENYE AJALI LAKINI WANAUNDIWA TUME BADALA YA SHERIA KUCHUKUA MKONDO WAKE) NA SHERIA NYINGINE NI KWA AJILI YA MAKABWELA.

26 Feb 2009


MKUU wa wilaya ya Maswa, James Yamungu, amempongeza aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Bukoba mkoani Kagera, Albert Mnali, akimwita kuwa ni shujaa kutokana na kitendo chake cha kuchapa viboko walimu wa shule tatu za msingi na kusababisha atimuliwe kazi na Rais Jakaya Kikwete.

Mnali, ambaye hakujutia kitendo chake cha kuchapa walimu akisema alikuwa tayari kwa uamuzi wowote toka juu, aliwachapa viboko walimu wa shule za Kansenene, Katerero na Kanazi kwa madai ya utoro kazini, kuchelewa na uzembe na kusababisha kushuka kwa kiwango cha elimu kwenye wilaya hiyo. Kitendo chake kililaaniwa na wadau mbalimbali, ikiwa ni pamoja na serikali na kufuatiwa na uamuzi wa Rais Kikwete kumvua ukuu wa wilaya.

Lakini jana, mkuu wa wilaya ya Maswa alionekana kuchukulia kitendo hicho kuwa sahihi na kumuita Mnali kuwa ni shujaa. Akizungumza wakati akifungua mkutano mkuu wa tatu wa chama cha kuweka na kukopa cha Nyalikungu uliofanyika kwenye ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo, kapteni huyo mstaafu wa jeshi alisema kuwa Mnali ni shujaa ambaye alikuwa akiwatetea Watanzania licha ya kitendo chake kusababisha atimuliwe. ..
ENDELEA


CHANZO: Mwananchi


YAYUMKINIKA KUAMINI KWAMBA KUNA TATIZO KATIKA UTEUZI WA BAADHI YA WATENDAJI WA SERIKALI HASA KATIKA NGAZI ZA MIKOA NA WILAYA.SIJUI NI KUJISAHAU,SIJUI NI KULEWA MADARAKA,AU SIJUI NDIO ILE "MIE NDIO RAIS WA WILAYA,KIJIJI,NK" INAYOWAPA BAADHI YA MA-RC,MA-DC,NA VIONGOZI WENGINEO KATIKA NGAZI MBALIMBALI KUJIONA WAKO JUU YA SHERIA,WAKO SAHIHI KATIKA KILA WAFANYACHO,NA PENGINE KUJIONA WAKO SAHIHI KULIKO HUYO ALIYEWATEUA (RAIS).HIVI HUYU DC ANAYEMWITA MWENZIE ALIEFUKUZWA NA RAIS KUWA NI SHUJAA HAFANYI DHIHAKA KWA RAIS?SI VIGUMU KUJUA WANAPATA WAPI JEURI HII....

17 Nov 2008

Picha (ni kielelezo tu,haihusiani na habari) kwa hisani ya MJENGWA

WALIMU wanaofundisha katika shule zilizopo wilayani Monduli mkoani Arusha ambao waliajiriwa toka Julai mwaka huu, wapo katika hali mbaya kimaisha kiasi cha kufikia hatua ya kufanya kazi za kugonga kokoto ili kujikimu kimaisha.

Hali hiyo imetokana na walimu hao kutolipwa mishahara yao ya miezi zaidi ya minne toka waajiriwe, licha ya kusaini mkataba wa miaka mitano.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na Tanzania Daima, umebaini kuwa walimu walioathirika kwa kiasi na hali hiyo ni waliopo katika maeneo ya Loolkisare, Moita, Meserani Juu, Mto wa Mbu, Losomingo na Lepulko ambapo inadaiwa walimu hawana hata nauli ya kuwafikisha katika Halmashauri ya Wilaya ya Monduli.

Akizungumza na Tanzania Daima, mmoja wa walimu hao, Goodluck Namoyo, alisema hali zao ni mbaya kifedha na wanajiandaa kukutana leo ili kujadili hatma yao.

Katika maeneo mengine ya Loolkisare na shule zilizopo vijiji vya mbali walimu wanaingia darasani kwa muda mfupi na muda mwingi wanatumia kufanya kazi za vibarua kwa kugonga kokoto ili kuwawezesha kupata angalau fedha za kujikimu.

Kaimu Afisa Elimu wa wilaya ya Monduli Emanueli Maundi, alikiri kuwepo kwa hali hiyo na kuongeza kuwa walimu 40 hawajalipwa mishahara yao mpaka sasa na wao kama idara ya elimu, wamefanya jitihada kunusuru hali hiyo.

''Ndugu yangu mwandishi hivi tunavyoongea licha ya mweka hazina kuwasilisha majina ya walimu hao wizarani kwa muda mrefu sasa, hali bado ni tete na imemlazimu afisa elimu hiyo kwenda jijini Dar- es- salaam kushughulikia mishahara ya walimu hao kwani wana hali mbaya sana hivi sasa,'' alisema Maundi.

Naye katibu wa chama cha walimu wilaya za Monduli na Longido Godwin Mushi, alisema hali ya walimu hao inadhihirisha ni jinsi gani walimu hawathaminiwi kwani toka waajiriwe, hawajalipwa.

''Sidhani kama mwalimu huyo anaweza kumshauri ndugu yake yoyote apende kuwa mwalimu kutokana na hali aliyokumbana nayo yeye hivi sasa na hali hiyo ni hatari zaidi kwa siku za baadaye juu ya mustakabali wa elimu nchini, ''alisema Mushi.

Akizungumzia hali hiyo Mkaguzi wa Elimu wa Wilaya ya Monduli, Ernest Mwende, alisema kazi ya walimu kwa sasa ni ngumu kutokana na kupungua kwa thamani ya mwalimu.
CHANZO: Tanzania Daima

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.