Showing posts with label Mgomo wa Madaktari. Show all posts
Showing posts with label Mgomo wa Madaktari. Show all posts

10 Mar 2012


FRIDAY, MARCH 9, 2012

Mamlaka ya Urais yawezeshe uwajibikaji kumaliza mgogoro wa Serikali na Madaktari


Jana tarehe 8 Machi 2012 asubuhi nilitoa tamko kwa niaba ya CHADEMA la kutaka kauli ya haraka ya Rais Jakaya Kikwete ya kutengua uteuzi wa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk. Hadji Mponda na Naibu Waziri wa wizara husika Dk. Lucy Nkya kutokana na udhaifu wao mkubwa wa kiongozi waliouonyesha katika kushughulikia mgogoro wa madaktari ambao umedumu kwa muda wa takribani miezi miwili. 

Nilieleza kusitikitishwa na ukweli kwamba Rais Kikwete toka mgogoro utokee hajatumia ipasavyo mamlaka yake ya kikatiba kwa mujibu wa ibara ya 34 na 35 na tarehe 5 Februari 2012 aliahidi kwamba atazungumzia kwa kina suala la mgomo wa madaktari lakini badala yake akalizungumza kwa ufupi tarehe 29 Februari 2012 katika hotuba yake kwa taifa bila kuchukua hatua za msingi hali inayoashiria ombwe la uongozi. 

Nilieleza kuwa iwapo Rais Kikwete haitatoa kauli viongozi wakuu wa CHADEMA wataeleza hatua za ziada ambazo chama kitachukua kuiwajibisha serikali. Jioni Serikali ilieleza kuwa leo Rais angezungumza na wazee wa Dar es salaam, na leo imetolewa taarifa kuwa atazungumza nao kesho.

Jana usiku na leo asubuhi masuala kadhaa yameendelea kuhusu mgogoro huu, mosi; hukumu ya mahakama ya kazi, pili; uamuzi wa serikali na wadau wake kufanya propaganda dhidi ya madaktari tatu; uamuzi wa serikali kufanya mawasiliano na uongozi wa madaktari.

Mkakati wa kufanya propaganda hautaisaidia Serikali badala yake iwekeze katika mawasiliano na uongozi wa madaktari kabla ya Rais kuzungumza ili Rais atoe kauli baada ya kuchukua hatua za msingi ikiwemo za kuwezesha uwajibikaji wa viongozi waliotajwa na pia kuanza kushughulikia madai ya madaktari na yale yanayohitaji kuingizwa kwenye bajeti kuwe na makubaliano ya utekelezaji. 

Izingatiwe kwamba matatizo ya Wizara ya Afya pamoja na udhaifu wa kiutendaji yalichangiwa pia na ufinyu wa bajeti, na bajeti husika iliandaliwa na serikali na kupitia kwenye baraza la mawaziri ambalo Rais ni mwenyekiti wake kabla ya kuletwa bungeni na wengine tuliipinga tukitaka fedha zitoke kwenye matumizi mengine ya anasa na kuelekezwa kwenye huduma muhimu za kijamii. 

Pia; kutokana na matatizo katika serikali kwenye wizara mbalimbali yenye madhara ya kiuchumi, kisiasa na kijamii katika taifa tunasisitiza umuhimu wa Rais Kikwete kulivunja baraza la mawaziri ili kufanya mabadiliko ya kimsingi ya kuongeza uwajibikaji kama ilivyoazimiwa pia na kamati kuu ya CHADEMA katika mkutano wake wa tarehe 3 na 4 Machi 2012.

Tarehe 7 na 8 Machi 2012 Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa mara nyingine tena alitoa taarifa kinyume na kauli za awali za tarehe 9 Februari 2012 ambazo badala ya kushughulikia vyanzo vya mgogoro vimeendeleza mgogoro na kusababisha mgomo mwingine wa madaktari wenye athari kubwa kwa wananchi.

Ndio maana nikatoa kauli ya kumtaka Waziri Mkuu kuweka wazi kwa umma taarifa ya uchunguzi uliofanywa na serikali kuhusu tuhuma dhidi ya viongozi wakuu na watendaji waandamizi wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, na kushughulikia madai ya msingi ya madaktari. 

Aidha, pamoja na kuunganisha nguvu za pamoja kuhakikisha mgomo unakwisha ili kuepusha athari zaidi kwa umma, ni muhimu hatimaye tathmini huru ikafanyika kuhusu matokeo ya mgogoro na mgomo toka ulipoanza mpaka sasa ikiwemo kueleza wazi idadi ya vifo vilivyotokea na madhara yaliyojitokeza katika hospitali za umma tofauti na kauli potofu iliyotolewa bungeni tarehe 3 Februari 2012 na Waziri husika.

Rais Kikwete alipaswa kabisa kuchukua hatua kuiongoza serikali kufanya maamuzi ya msingi mara baada ya matokeo ya kikao kati ya ujumbe wa Serikali ulioongozwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda na wanataaluma wa kada ya afya sanjari na mkutano kati ya madaktari na wawakilishi wa kada nyingine za sekta ya afya katika utumishi wa umma vilivyofanyika tarehe 9 Februari 2012; kwa kuzingatia pia ushauri tuliotoa tarehe 10 Februari 2012.

Kwa upande mwingine, jana nilirudia kutoa mwito tuliotoa tarehe 30 Januari 2012 kwa TUGHE, MAT na kamati ya muda ya madaktari kuendelea kutoa ushirikiano unaostahili kwa chama, kambi rasmi ya upinzani na wadau wengine ili kuweza kuunganisha nguvu ya pamoja katika kushughulikia madai ya msingi ya madaktari yenye kuathiri sekta ya afya nchini na maisha ya wananchi kwa ujumla. 

Naendelea kuwashukuru wanaharakati kwa kuunganisha nguvu katika kutaka uwajibikaji wa viongozi wa serikali katika kushughulikia mgogoro na madaktari na kinaitaka Serikali kuacha vitisho na matumizi makubwa ya vyombo vya dola kwa madaktari na makundi mengine katika jamii yanapotumia uhuru wa kikatiba kwa kukusanyika, kujadiliana na kuhoji kuhusu uwajibikaji wa serikali na viongozi wake kwa kuzingatia ibara za 8, 18 na 20 za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Rais Kikwete anapaswa baada ya mawasiliano yanayoendelea kutoa hotuba yenye kuleta matumaini badala ya kurudia tena maelezo yasiyoridhika kama yale yaliyotolewa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda tarehe 9 Februari 2012 na 7 na 8 Machi 2012 kuhusu namna ambavyo imeshughulikia mgogoro huu na madai ya madaktari, watumishi wengine wa umma katika sekta ya afya nchini pamoja na uboreshaji wa huduma katika hospitali, zahanati na vituo vya afya nchini.

Narudia kutoa rai kwa wananchi kuendelea kuunga mkono madai ya msingi ya madaktari ili kuhakikisha kwamba hospitali za umma nchini zinakuwa mahali salama kwenye huduma bora za kulinda maisha ya wananchi hususan wasio na uwezo wa kudumu gharama za matibabu katika hospitali binafsi za ndani na nje ya nchi. 

Pamoja na madai ya maslahi ya madaktari ambayo ni kwa maslahi ya umma, madaktari wanataka pia serikali ichukue hatua za kuboresha huduma za afya. Serikali inaingia gharama kubwa kupeleka baadhi ya watanzania wengi wao wakiwa viongozi kwenda kutibiwa nje ya nchi huduma katika hospitali za umma zinazidi kuzorota kutokana na ukosefu wa madawa, vifaa tiba na wataalamu wa kutosha katika hospitali za umma. 

Aidha, serikali inashindwa kuipa kipaumbele sekta ya afya kwa kisingizio cha kutokuwa na uwezo wakati ambapo inafanya matumizi mengine ya anasa kwa kiwango kikubwa kama ilivyokuwa katika maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru. Serikali inachelewa kushughulikia madai ya posho za madaktari kama nyongeza ya posho ya kulala kazini (on call allowance) na posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi (risk allowance) wakati huo huo serikali hiyo hiyo inazungumzia nyongeza ya fedha katika matumizi mengine ya serikali yasiyokuwa ya lazima. Serikali ishughulikie vyanzo vya migogoro ya kijamii badala ya matokeo.

MTEMBELEE MHESHIMIWA MNYIKA KATIKA BLOGU YAKE INAYOPATIKANA http://mnyika.blogspoti.com.PIA UNAWEZA KUMFUATA TWITTER www.twitter.com/jjmnyika NA UKURASA WAKE WA FACEBOOK NI http://www.facebook.com/pages/John-Mnyika/113913842009362

11 Feb 2012



Taarifa Kwa Umma Na Madaktari Wote Nchini Juu Ya Maamuzi Yaliyofikiwa Leo February 9

7 Feb 2012


WAFANYAKAZI WA HAZINA, TANESCO NA WIZARA YA NISHATI WAHUSIKA, NGELEJA ATHIBITISHA UCHUNGUZI KUFANYWA
Mwandishi Wetu
SERIKALI inawachunguza baadhi ya maofisa wake waandamizi kwa tuhuma za wizi wa dola50 milioni za Marekani sawa na Sh86 bilioni, zilizotengwa kwa ajili ya ununuzi wa mafuta mazito ya kuzalishia umeme kwa Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), katika kipindi hiki nchi inapokabiliana na tatizo la uhaba wa nishati hiyo.

IPTL inayozalisha megawati 100 za umeme iliingia mkataba na Shirika la Umeme Tanzania(Tanesco), lakini utendaji wake umekuwa na mkanganyiko.Chanzo kutoka serikalini kililiambia gazeti dada la The East African la Februari 12, kwamba kuna ushahidi wa kutosha kwamba baadhi ya maafisa kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Hazina na Tanesco, wanahusika katika mpango huo wa wizi.

Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja alipoulizwa alijibu, “Ndiyo naweza kuthibitisha upo uchunguzi unaoendelea, lakini ndiyo kwanza upo katika hatua za awali.” Tayari taarifa za awali za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG), zinaonyesha kumekuwa na maelezo yaliyokiuka utaratibu wa fedha zilizolipwa na Serikali kwa ajili ya usambazaji wa mafuta mazito kutoka kampuni za ndani.

Ukosefu wa nishati ya umeme unaoikabili nchi kwa sasa unaifanya Tanesco kulipa IPTL dola12 milioni za Marekani sawa na Sh19.2 bilioni kila mwezi, kwa uzalishaji wa megawati 60 badala ya megawati 100.

Mwaka 1995, Tanesco iliingia mkataba na IPTL, mkataba ambao uliihusisha kampuni ya nchini Malaysia , Mechmar Corporation na wawekezaji wa ndani, na VIP Engineering and Marketing Company kwa ajili ya kuzalisha megawati 100 kwa kutumia mitambo inayotumia dizeli kwa miaka 20.Katika mkataba huo, VIP ina hisa ya asilimia 30 na ile ya Mechmar ya Malaysia ikiwa na hisa ya asilimia 70.Serikali ilikubali kulipa kwa ajili ya uzalishaji huo kwa kuwa haikuwa na njia nyingine.

Mpango wa kuifilisi IPTLTayari hivi karibuni Mahakama iliamua IPTL ifiilisiwe na jukumu hilo lilikabidhiwa kwa Wakala wa Ufilisi, Vizazi na Vifo (Rita).Hata hivyo, baadhi ya benki zinazoidai IPTL ziliweka zuio mahakamani zikitaka kwanza kulipwa fedha zao ambazo kampuni hiyo ilikopa.IPTL inakadiriwa kuwa na Sh200 bilioni zilizopo Benki Kuu (BoT) ambazo kama ikifilisiwa zingeangukia mikononi mwa Serikali. Kampuni hiyo imekuwa ikiitafuna Tanesco mabilioni ya shilingi tangu kuingia mkataba huo ambao umekuwa ukitajwa kama wa kifisadi, kuliko hata wa Richmond.


Wakati fedha za umma zikitafunwa bila huruma,mgomo wa madaktari unaoendelea kwa siku kadhaa sasa umeingia katika hatua mpya baada ya madaktari bingwa nao kujiunga na mgomo huo,kama inavyoripotiwa hapa chini:

Geofrey Nyang’oro na Florence Majani
WAKATI Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii ikianza kazi ya kuzungumza na madaktari walio kwenye mgomo, madaktari bingwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na walio katika Taasisi ya Mifupa (MOI) wamegoma. Mgomo huo wa jana ulihusisha vitengo vyote huku wagonjwa waliokuwa wamelazwa hospitalini hapo wakipewa taarifa za kuondoka katika wodi walimolazwa.

Azimio la mgomo huo lilifikiwa katika kikao cha dharura kilichoitishwa na jopo la madaktari bingwa wakiongozwa na Dk James Rwehabura ambaye ni daktari bingwa wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Binadamu.

Habari za ndani kutoka katika kikao cha dharura cha wanataaluma hao, zilisema uamuzi huo ulifikiwa kwenye kikao cha madaktari hao kilichoanza mapema asubuhi jana na kumalizika saa 6:00 mchana. “Kwa pamoja tumekubaliana kuweka vifaa chini, hii ni kutokana na ukweli kuwa hali ya utoaji huduma katika hospitali hii ni mbaya huku taarifa za Serikali zikiwa siyo za kweli,” alidokeza mmoja wa madaktari bingwa.

Daktari huyo aliyekataa kutaja jina lake, alisema, “Tumekubaliana kugoma hadi hapo Serikali itakapotoa majibu ya madai yote yaliyowasilishwa na jumuiya ya madaktari inayoongozwa na Dk Stephen Ulimboka kwa Serikali.” Jumuiya hiyo iliwasilisha madai mbalimbali likiwamo la kuitaka Serikali kupeleka vifaa na dawa katika hospitali za Serikali ili madaktari hao waweze kutoa huduma bora kwa jamii.

Pia, madaktari hao walitaka kusitisha safari za vigogo kwenda kutibiwa nje kwa magonjwa yanayotibika ndani kwa kile walichodai, hali hiyo inachangia wao kudharauliwa na pia kuzorotesha jitihada za Serikali katika uboreshaji wa mazingira ya kazi kwa madaktari hao.

Kwa nyakati tofauti, madaktari hao walibainisha sababu ya mgomo wao na kudai kuwa, kikubwa ni mazingira magumu ya kazi. Daktari mwingine ambaye hakupenda jina lake kuandikwa gazetini alisema, licha ya mishahara na posho ndogo, lakini mazingira ya kufanyia kazi yamekuwa magumu mno.

“Tumeshaamua , ‘tools down’ hospitali haina kitu, hata ‘mask’ hakuna badala yake tunavaa gozi tunapofanya upasuaji, acha hiyo, hata nyuzi za kushonea wakati wa upasuaji hakuna,” alisema daktari huyo. Daktari huyo alisema, hawawezi kufanya kazi katika mazingira hayo kwa sababu yatawasababisha kuwa na utendaji mbovu na baadaye taifa kuwalalamikia.

Alisema hapa nchini madaktari bingwa ni wachache, kwa hiyo kitendo cha wao kufanya kazi peke yao bila wasaidizi, yaani madaktari wa mafunzo na wale wanaomaliza, wanaelemewa na mzigo wa kazi. Dk Henry Mwakyoma, Mhadhiri Mkuu wa Chuo cha Udaktari Muhimbili, (MUHAS) ambaye hakuwapo katika kikao hicho cha dharura alidai kuwa, yeye kama mhadhiri hajagoma, lakini alikiri kuwapo kwa mazingira magumu ya kazi.

“Mpaka sasa hatujalipwa mishahara ya mwezi uliopita, halafu kazi yetu ndiyo kama hii tunatakiwa tufanye utafiti, unategemea tutafanya kazi kwa umakini kweli? Tutawafundisha madaktari kwa umakini?” alihoji Dk Mwakyoma.

Mwakyoma alisema, Serikali haiwezi kudai kuwa haina fedha za kutosha wakati imetumia mamilioni ya shilingi katika sherehe za miaka 50 ya Uhuru na uchaguzi wa Igunga. Alisema ni vyema Serikali ikajipanga na kuamua kushughulikia masuala ya madaktari kwa hekima kwani kukaa kimya bila kutoa suluhu ni sawa na kufanya ushindani usio na maana.

Hata hivyo, Ofisa Habari Mwandamizi wa MNH Aminael Aligaesha alisema jana jambo hilo lilikuwa likishughulikiwa kwani vipo vikao vinavyoendelea.

Wagonjwa watimuliwa wodini
Wodi mbalimbali hospitalini hapo zilitawaliwa na vilio kutokana na wagonjwa na ndugu za wagonjwa kupewa taarifa za kuondoka katika eneo hilo mara moja, kutokana na mgomo huo wa madaktari. Mmoja wa wagonjwa waliokuwa wamelazwa katika wodi ya Sewahaji, Sadick Dimoso (35) mkazi wa Morogoro alisema hali sasa MNH ni mbaya.

“Tumeambiwa tuondoke wodini bila ya kuruhusiwa na daktari, hii ni hatari tena wanasema tuondoke tukakae huku hadi wiki mbili ndio turudi kuangalia,” alisema Amina Ramadhani, aliyekuwa akisubiri kufanyiwa upasuaji wa jicho. Alisema hatua ya kutakiwa kuondoka hospitalini hapo imekatisha matarajio yao ya kuendelea kuwa hai na kuitaka Serikali kufanyia kazi madai ya madaktari.

Wakati kundi la watu wengine wakililia huduma hosptalini hapo, baadhi ya ndugu za wagonjwa waliingia katika mgogoro na walinzi wa wodi hiyo ya Sewahaji wakitaka waandishi wa habari kuingia wodini.

Vikao vya Kamati Wakati hayo yakijiri, vikao baina ya madaktari na Kamati ya Kudumu ya Huduma za Bunge, viliendelea jana katika ofisi ndogo za Bunge huku taarifa zake zikiwa ni siri.

CHANZO (Habari zote mbili): Mwananchi

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.