Showing posts with label DINI TANZANIA. Show all posts
Showing posts with label DINI TANZANIA. Show all posts

17 Feb 2013


Padre E. Mushi Paroko wa parokia ya Minara Miwili Zanzibar ameuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiofahamika asubuhi hii. 

Ameuawa wakati akijiandaa kuingia kanisani akitokea kwenye gari yake ambapo ghafla ilitokea gari ndogo na waliokuwamo ndani ya gari ile wakamrushia risasi. 

Kwa siku za hivi karibuni kumekuwako na vitisho vya wazi wazi dhidi ya wakristu huko visiwani Zanzibar ambapo inaelezwa kuwa jeshi la polisi halijafanya juhudi yoyote kuzuia tishio hili. Kumekuwapo na vipeperushi vinavyodai kuwa kupigwa risasi kwa padre Ambrose sio mwisho wa mapambano. 

Taarifa hizi zimeripotiwa direct toka Zanzibar


CHANZO: Jamii Forums

15 Nov 2012


Nianze makala hii kwa kujipongeza kutokana na ‘ubashiri wangu sahihi’ kuhusu Uchaguzi wa Rais wa Marekani. Kama mnakumbuka, katika makala ya kwanza kwa mwaka huu nilijaribu kubashiri mwenendo wa masuala mbalimbali kwa ‘mwaka mpya’ 2012, na moja ya ubashiri huo ulikuwa huu:

“Kwa kuzingatia uchambuzi wa watu mbalimbali na kwa kadri ninavyofuatilia siasa za Marekani, dau (bet) langu ni ushindi ‘kiduchu’ kwa Obama dhidi ya Mitt Romney, mgombea ninayetabiri atapitishwa na Republican (iwapo upepo wa kisiasa hautobadilika.)”

Well, Romney alifanikiwa kushinda kuwa mgombea wa Republican na hatimaye kuchuana na Obama kwenye uchaguzi moja ya chaguzi zilizokuwa na ushindani mkali kabisa, na hatimaye Obama akafanikiwa kutetea kiti chake cha Urais (nami nikafarijika kuona ‘utabiri’ wangu umetimia.)

Tukiachana na hilo, makala hii anahitimisha mfululizo wa makala zangu kuhusu vurugu za kidini huko nyumbani. Katika kuhitimisha, nitazungumzia maeneo manne: vikwazo vya ndani ya Uislam kupata ufumbuzi wa manung’uniko yao; baadhi ya migongano ya kiimani kati ya Waislam na Wakristo, na ‘utata’ wa Kikatiba kuhusu migongano hiyo; na mwisho, mapendekezo ya nini kifanyike kukabiliana na vurugu za kidini huko nyumbani.

Vikwazo vya ndani ya Uislam kupata ufumbuzi wa manung’uniko yao:
Maeneo mawili yanayothibitika kitaaluma kuwa ni msingi wa manung’uniko ya Waislamu wengi ni upatikanaji (access) wa nafasi ya elimu na ajira. Sote twatambua kuwa ukimnyima mtu elimu unamnyima fursa ya ajira (angalau kwa ajira zinazohitaji ujuzi.)

Tukiweka kando ‘lawama’ kuhusu ‘mfumo wa kibaguzi, ni muhimu kwa Waislam wenyewe kutambua kuwa lawama pekee haziwezi kuleta ufumbuzi utakaoleta angalau usawa katika fursa za ajira na elimu. Tukumbuke kuwa hata mkoloni hakuamua kutupa uhuru kwa kumchukia au kumlaumu tu.

Kadhalika Nduli Idd Amin (ambaye hivi karibuni baadhi ya ‘Waislam wenye msimamo mkali’ walibadili mtizamo wao na kumwona kama shujaa katika namna ileile ya kifo cha gaidi la Kimataifa Osama bin Laden kiliombolezwa na watu hao kama shujaa wao) hakuondoka kwa vile tulimwita kila aina ya jina baya.
Kama Waislam wanaafikiana kuwa mfumo ‘wa kibaguzi’ uliwanyima fursa ya elimu na hivyo kuwatengenezea mazingira magumu ya kupata ajira zinazohitaji elimu, basi ni muhimu kwao kuwekeza vya kutosha kwenye elimu.

Na moja ya njia bora inaweza kuwa kuziwezesha shule za kidini (pengine kuanzia madrasa) zitoe pia elimu ‘ya kidunia.’ Nilishaeleza huko nyuma kwenye mfululizo wa makala hizi jinsi shule za seminari za Kikristo zilivyochangia kuzalisha wasomi Wakristo.

Huu ni ‘ukweli mchungu’: kama mtoto wa Kikristo akitoka shule anaenda twisheni kuongeza maarifa ya ‘elimu ya kidunia’ ilhali mwenzie wa Kiislam akitoka shule anaenda madrasa kuongeza elimu ya kidini, ni wazi mmoja wao anajitengenezea mazingira mazuri ya kufaulu huku mwingine anajikwaza. Hapa simaanishi watoto wasiende madrasa bali ikiwezekana, shule za kidini (ikibidi hata kuanzia madrasa) zijumuishe pia elimu ya kidunia.

Kwa uelewa wangu, misikiti si mahala pa ibada pekee bali pia sehemu ya kumpatia muumini elimu itakayomwezesha kumtumikia Muumba wake ipasavyo. Pengine kuna umuhimu kwa kasi ya ujenzi wa misikiti kuendana na kasi ya ujenzi/uanzishwaji wa taasisi za kielimu, au ikibidi kutumia misikiti hiyo kama sehemu za ‘mapambano ya kuziba pengo la kielimu linalowakabili Waislam wengi.’

Pendekezo jingine ambalo lipo nje ya uwezo wa Waislamu ni kwa serikali kuangalia uwezekano wa kile kinachofahamika katika lugha ya Kiingereza kama ‘affirmative action’ (yaani upendeleo wenye lengo la kuleta uwiano kwa kundi flani katika jamii katika eneo flani.) Sitaki kuamini kuwa kama takwimu zikiwekwa wazi kuonyesha pengo lililopo kielimu na kiajira kati ya Wakristo na Waislamu, kisha serikali ikaridhia kutaka kupunguza pengo hilo kwa njia za uwazi, Wakristo watapinga hatua hiyo. Cha muhimu ni kufanya jitihada hizo kwa uwazi. Affirmative action imeweza kufanikiwa kwa kiasi fulani katika nchi za Magharibi kuleta uwiano kati ya, kwa mfano, ‘wazungu’ (Whites) na makundi madogo katika jamii (minorities), kwa mfano Watu Weusi (Blacks).

Baadhi ya migongano ya kiimani kati ya Waislamu na Wakristo, na utata wa Kikatiba unaotokana na migongano hiyo:
Kuna migongano kadhaa ya kiimani kati ya Waislamu na Wakristo lakini nafsi hainiruhusu kuitaja/kuizungumzia yote. Hapa nitazungumzia eneo moja tu, ambalo binafsi ninalitafsiri kama ‘nyeti’ zaidi.
Kwa Wakristo, Yesu ni Mungu na pia mwana wa Mungu (yaani Utatu Mtakatifu wa Mungu.) Kwa Waislamu, ile kusema tu Mungu ana mtoto (achilia mbali mtoto huyo ni Nabii Issa bin Mariam, yaani Yesu) ni kufr. Hakuna njia ya mkato katika migongano huu, hasa kwa vile dini hizi mbili zinaongozwa na Maandiko Matukufu/Matakatifu tofauti, yaani Kuran Tukufu kwa Waislam na Biblia Takatifu kwa Wakristo. Laiti Waislam wangekuwa wanatumia Biblia kuchunguza imani ya Wakristo kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, na laiti Wakristo wangekuwa wanatumia Kuran kuchunguza kwanini kusema Mungu ana mtoto ni kufr, labda kungepatikana mwafaka wa namna flani.

Lakini kama ilivyo kwa sie wanafunzi wa stadi za siasa kuwekea mkazo zaidi kwenye siasa na sio Fizikia, ndivyo ambavyo Waislam wanawekea mkazo kwenye Kuran na Wakristo kwenye Biblia. Na huo ni wajibu kwa kila muumini.

Hata hivyo, kama ambavyo sie wanafunzi wa siasa kuna nyakati tunalazimika kuyaelewa maeneo mengine ya kitaaluma in relation to siasa, ndivyo ambavyo baadhi ya Waislam wanafanya jitihada ya kuuelewa Ukristo in relation to Uislam, na baadhi ya Wakristo kuuelewa Uislam in relation to Ukristo. Hata hivyo hao ni wachache.

Na kwa bahati mbaya (au makusudi), jitihada hizo za kusaka uelewa wa dini nyingine ‘zimetekwa’ na dhamira ‘mbaya’ ya ‘kutaka kumwelewa adui vizuri ili kumkabili vizuri pia.’ Kwa wanaofuatilia mihadhara ya ‘kashfa’ ya kidini watakuwa wameshuhudia namna wengi wa wahubiri wanavyotumia Biblia au Kuran kuonyesha kwanini Ukristo au Uislam sio dini sahihi.

Lakini ili kuepusha ‘overgeneralization’ (kuhitimisha mambo jumla jumla) ni muhimu kufahamisha kuwa wapo wanazuoni wachache wa Kiislamu wanaoisoma Biblia kwa minajili ya uelewa tu wa kidini (na si kupambana na Ukristo).Kadhalika, katika stadi za kidini za Kikristo kuna wachache wanaoisoma Kuran kwa minajili ya uelewa tu wa kidini.

Mgongano wa kiimani kati ya Waislam na Wakristo kuhusu “Yesu ni Mungu na pia Mwana wa Mungu” ulijidhihirisha zaidi katika kesi iliyomkabili mhadhiri mmoja wa Kiislam, Ustaadh Khamis Dibagula, ambaye mwaka 2000 alihukumiwa kwenda jela huko Morogoro kwa ‘kashfa’ ya kudai “Yesu si Mungu” kama wanavyoamini Wakristo.

Kipengele cha 19 cha Katiba yetu kinatoa uhuru wa kuamini dini yoyote (japo kinakumbushia umuhimu wa kufanya hivyo bila kuathiri sheria za nchi). Na kipengele cha 18 kinatoa uhuru wa kutoa maoni (pasipo kuathiri sheria za nchi.) Kwahiyo basi Kipengele cha 19 cha Katiba kilimruhusu Dibagula kuamini “Yesu si Mungu/Mwana wa Mungu”, na kipengele cha 18 kilimruhusu kueleza imani yake hiyo waziwazi.

Kwahiyo, kwa upande mmoja Katiba iliruhusu kutoa maoni ambayo kwa upande mwingine ni kashfa. Hili ni eneo hatari ambalo ninachelea kuingia kwa undani zaidi kwani hata huo migongano wa kisheria uliopelekea Dibagula kufungwa na hatimaye kuachiwa huru ni suala ambalo Waingereza wanaliita legal minefield (yaani uwanja wa kisheria uliotegwa mabomu).

Kwa kifupi, ufanisi wa Katiba katika suala hilo unategemea zaidi busara za waumini, hususan utashi kuwa “nikasema hili-japo ni sahihi katika imani yangu-nitakuwa ninamkwaza flani.” Lakini, kusema ni jambo moja na kuamini ni jambo jingine. Katiba inaweza kuzuwia kusema hadharani kuwa “Yesu si Mungu/Mwana wa Mungu” lakini haiwezi kuzuwia wanaoamini kuwa “Yesu si Mungu/Mwana wa Mungu.”

Na kwa vile sheria zinazotokana na Katiba yetu ndizo zilizomfunga Dibagula kwa ‘kashfa’ lakini baadaye zikamwachia huru, hatua hiyo inajenga taswira gani kuhusu Katiba yetu kama chombo kinachopaswa kulinda uhuru wa kuabudu na wa maoni?
Nini kifanyike?
  1. Tuukabili ukweli kuwa tuna matatizo. Badala ya kuwa na sensa zinazokwepa kutupa ufahamu wa uwiano wa kielimu na ajira kati ya Wakristo na Waislam, ni muhimu kuwa na njia za wazi za kufahamu ukubwa wa tatizo la inequality katika maeneo mbalimbali, na hili si kwa Waislam pekee bali hata makundi mengine ya jamii.
  2. Jitihada za makusudi zinahitajika kushughulikia matatizo hayo. Ugonjwa hauponi kwa kujidanganya kuwa haupo. Badala ya kuruhusu wanasiasa watumie manung’uniko ya Waislam kama mtaji wao wa kura (mfano ahadi feki za CCM kwa Waislamu kuhusu Mahakama za Kadhi na kujiunga na OIC), harakati za kiraia zikiongozwa na wanazuoni na wanataaluma wenye mtizamo wa kuleta maelewano badala ya mifarakano ziimarishwe.
  3. Jitihada za ndani na nje ya Uislam zinahitajika katika kuhamasisha maendeleo ya kielimu kwa Waislam. Malalamiko pekee hayawezi kuleta ufumbuzi. Kadhalika, ushirikiano kati ya Waislam na serikali na taasisi nyingine za kidini na kijamii ni muhimu iwapo itakubalika kuwa na affirmative action.
Mwisho, ninatambua tofauti zetu za kiimani. Busara inahitajika katika kudumisha imani zetu na wakati huo kutoa fursa kwa wenzetu kubaki na imani zao. Tuliweza huko nyuma, na tunaweza sasa na hata milele kuwa Watanzania kwanza kisha ndio tuangalie huyu Muislam au Mkristo, Mchagga au Mndamba, mwanamke au mwanaume, nk.

Adui yetu mkubwa ni umasikini unaotishia uhai wa nchi yetu bila kujali huyu ni Hamisi na yule ni John. Mafisadi wanaotafuna raslimali zetu na kuficha mabilioni huko Uswisi, visiwa vya Jersey, nk hawafanyi hivyo kwa vile wanawapenda Wakristo na kuwachukia Waislam (au kinyume chake), bali wanamnyonga kila Mtanzania pasi kujali dini yake.

Kama ambavyo umasikini wetu ni mtaji mzuri kwa maharamia wa kisiasa kununua kura ndivyo ambavyo utengano wetu wa kidini unavyokuwa turufu kubwa kwa wanasiasa mufilisi ambao kimsingi dini zao si Uislam au Ukristo bali ulafi wa kuifilisi nchi yetu hadi tone la mwisho.
UMOJA NI NGUVU UTENGANO NI UDHAIFU

11 Nov 2012


KATIKA matoleo mawili yaliyopita ya jarida hili maridhawa, safu hii imekuwa ikijadili vurugu za kidini zilizojitokeza hivi karibuni nchini.
Katika makala hii, nitaanza sehemu ya kwanza ya kuhitimisha mjadala huo (na sehemu ya pili ya hitimisho itakuwa katika toleo lijalo).Ni matarajio yangu kuwa mfululizo huu wa makala hizi utafungua mjadala mpana zaidi kuhusu hali ya dini nchini Tanzania, nafasi ya dini katika kujenga au kubomoa amani, na hatimaye mapendekezo ya nini kifanyike kudumisha umoja, upendo, amani na mshikamano miongoni mwetu.
Mwamko ulioonyeshwa na makundi mbalimbali ya kijamii katika kulaani na kuzungumzia suala hili unatoa picha chanya kuwa wengi wetu tunatamani kuiona Tanzania yetu ikiendelea kuwa “kisiwa cha amani” (japo neno ‘amani’ lina tafsiri pana, na linaweza kuzua mjadala mwingine mpya. Lakini kwa minajili ya mada hii, tuitafsiri amani kama hali ya utulivu na maelewano miongoni mwa jamii).
Katika makala zilizotangulia, nilijikita zaidi kubainisha sababu ambazo kwa uelewa wangu zilichangia kuleta vurugu hizo za kidini. Nimejaribu kurejea historia ya nchi yetu, kabla na baada ya uhuru, na kuonyesha sababu zilizozalisha manung’uniko ya Waislam, hususan katika maeneo makuu mawili ya upatikanaji (access) wa fursa ya elimu na ajira.
Kwa kuangalia michango mbalimbali ya wanajamii katika mjadala kuhusu vurugu hizo, moja ya hoja inayoonekana kupewa uzito mkubwa ni ile inayodai kuwa chanzo cha vurugu hizo si dini.
Naomba niweke bayana msimamo wangu kuwa binafsi ninazitafsiri vurugu hizo ZINA SABABU ZA KIDINI japokuwa si DINI PEKEE bali pia kuna mwingiliano wa sababu nyingine.
Ninachomaanisha hapa ni kwamba si kweli kuwa vurugu hizo hazihusiani kabisa na dini bali dini ni moja ya sababu za vurugu hizo.
Kwa kuwa katika makala zilizotangulia nimeelemea zaidi katika sababu hizo ‘zisizo za kidini kwa asilimia 100,’ katika makala hii ya mwanzo wa hitimisho nitajaribu kujadili ‘eneo hatari’ la dini kama moja ya chanzo cha vurugu hizo.
Ninasema ‘eneo hatari’ kwa sababu yayumkinika kuhisi kuwa baadhi ya wasomaji hawatopendezwa na uthibitisho nitakaoweka wazi, na ambazo ni lazima tuziongelee ili si tu tuweze kuwa na mjadala wa maana kuhusu suala hili, bali pia tuweze kuwa katika nafasi ya kusaka ufumbuzi.
Kama ilivyo mahala kwingineko (kwa maana ya si Tanzania pekee), uchambuzi kuhusu dini si tu unaweza kuzua hisia hasi (kama vile kuhisi mwandishi Mkristo haruhusiwi kukosoa Uislam, au kinyume chake), lakini pia unakabiliwa na tatizo la msingi la vigezo vingine vinavyoathiri dini husika, kama vile tofauti kati ya mjini na vijijini, idadi ya wakazi katika sehemu husika, historia ya sehemu husika, nk.
Kwa kifupi-na huu ni mfano tu-inaweza kuwa na ugumu wa namna fulani kuuchambua Ukristo kwa kutumia mikoa miwili ya Kilimanjaro na Kaskazini Pemba kama maeneo ya kupata takwimu za kuwezesha uchambuzi husika.
Wakati Kilimanjaro ina idadi kubwa ya Wakristo, Kaskazini Pemba ina idadi kubwa ya Waislamu. Tofauti hizo ‘zisipolindwa vema kwa kuzingatia kanuni za tafiti’ zinaweza kuzua matokeo ‘fyongo.’
Na suala hili la ‘vigezo vingine’ ni moja ya mambo yaliyojitokeza katika utafiti wangu kuhusu harakati za vikundi vya Kiislamu huko nyumbani.
Kwa mfano, baadhi ya wahojiwa wa Kiislamu katika jiji la Dar es Salaam walionekana kuwa na hamasa kubwa kuzungumzia ‘ubaguzi wanaofanyiwa na kile walichokieleza kama Mfumo Kristo,’ wengi wa wahojiwa katika ‘maeneo yasiyo ya mijini (rural areas) walionekana kuelemea zaidi kwenye kero zinazowakabili kila siku katika nyanja kama za afya, elimu na kilimo.
Hata mwanazuoni mmoja wa Kiislamu niliyefanya naye mahojiano alikiri kwamba, (namnukuu) “…kwa huko vijijini haya masuala ya udini hayana uzito kulinganisha na adha zinazowakabili wananchi katika maeneo hayo ambazo kimsingi hazibagui kuwa huyu ni Juma au Petro…”
Tukiweka kando ‘kikwazo’ hicho kinacholeta ugumu fulani katika kuchambua dini, moja ya mifumo (models) ya kuchambua vurugu (ziwe za kidini, kikabila, kisiasa, nk) unaonyesha hali hii (kwa mchanganuo wa jumla): ubaguzi huzua manung’uniko; manung’uniko huzua hamasa; hamasa huzua upinzani ambao waweza kuzua vurugu.
Na moja ya sababu za msingi zinazoelezwa katika model hiyo kuwa zinaweza kujenga hisia ya kubaguliwa ni kupotea kwa hali ya kujiendeshea mambo pasi kuingiliwa (autonomy).
Kufutwa kwa Mahakama za Kadhi kunaweza kuwa mfano mwafaka.
Japo mahakama hizo zilikuwa za kidini lakini kimsingi zilijitosheleza kushughulikia ‘kesi za kidini’ miongoni mwa Waislamu (yaani masuala kama mirathi, nk).
Lakini eneo jingine linaloweza kuingia katika kundi hili ni ushiriki wa baadhi ya Waislamu katika harakati za uhuru. Ushiriki huo haukuwa wa kisiasa tu bali wa kidini kwani moja ya mafundisho ya Uislamu katika kushughulikia jambo baya (kama udhalimu wa mfumo wa ukoloni) ni “kulikemea, kulichukia au kuliondoa” jambo hilo.
Kwa kutafsiri ushiriki wa Waislamu hao ulikuwa na msingi wa kidini (licha ya siasa), kujumuika kwao kuliwapa autonomy ya aina fulani, yaani kuweza kuitumia imani yao ya kidini kukabiliana na jambo baya (ukoloni).
Kama nilivyobainisha katika makala zilizotangulia, hisia kuwa “tulikuwa mstari wa mbele kupambana na mkoloni lakini uhuru ulipopatikana tumeishia kuwa chini ya wenzetu waliomsapoti mkoloni (kwa maana ya ukaribu kati ya ukoloni na Kanisa/ Ukristo)” zinaweza kutafsiriwa kama kupoteza autonomy hiyo.
Lakini pia ni muhimu kuelewa kuwa Uislamu si suala la imani pekee bali ni mfumo kamili wa maisha. Stadi zinaonyesha kuwa pindi mfumo wa kimaisha unapoonekana kuwa hatarini (kwa sababu moja au nyingine) inaweza kuleta mwamko wa kukabili tishio husika.
Kimsingi, dini hutoa mwongozo kwa muumini kuhusu maisha yake kibinafsi na katika jamii. Sasa tukiafikiana kuwa Uislamu kama dini na kama mfumo kamili wa maisha hauridhii aina yoyote ya uonevu, ni wazi hisia kuwa “Waislamu wanabaguliwa” zinaweza kufuata ile model ya ubaguzi – manung’uniko – hamasa – upinzani.
Pengine hili halitowapendeza baadhi ya wasomaji: katika utafiti wangu (na katika baadhi ya stadi nyingine) kuna uthibitisho wa kuwapo kwa vikundi vya Kiislamu vyenye mrengo mkali wa kiimani (Islamic extremists). Naomba ieleweke kuwa uwepo wa vikundi hivyo katika Uislamu haimaanishi kuwa mrengo mkali katika dini ni kwa Uislamu pekee.
Israel kuna Wayahudi wenye mrengo mkali kabisa ambao hawataki kabisa kusikia lolote kuhusu Wapalestina. Huko Marekani kuna Wakristo wenye msimamo mkali kabisa ambao kwa kiasi fulani wanachangia ‘uhasama’ kati ya taifa hilo na Waislamu na Uislamu kwa ujumla (kwa mfano Pasta Terry Jones aliyezua sokomoko duniani kwa kuchoma Kuran Tukufu).
Sasa kwa huko nyumbani, vikundi hivyo vya Waislam wenye msimamo mkali si tu ‘wameteka’ ajenda ya msingi ya manung’uniko (tunayoweza kuafikiana kuwa ni halali) ya Waislamu bali pia wamegeuza ajenda hiyo kuwa nguzo muhimu ya kupambana na wale wote wasioafikiana na mtizamo wao.
Wahanga wa ‘wana-msimamo mkali’ hawa si Wakristo pekee bali hata Waislamu wenzao wanaoonekana ‘kutokuwa na msimamo kama wao.’
Uthibitisho wa hii ni pamoja na vurugu zilizojitokeza nyakati fulani za uporaji wa misikiti. Japo wateka misikiti hao walidai kuwa wanairejesha kwa Waislamu misikiti iliyokuwa chini ya BAKWATA, kuna uthibitisho kuwa lengo lilikuwa kuigeuza misikiti hiyo kuwa ya ‘msimamo mkali.’
Badala ya hoja ya msingi inayohusu manung’uniko ya Waislamu dhidi ya mfumo wanauona kuwa unawakandamiza, vikundi vya Kiislamu vyenye msimamo mkali vinakwenda mbali zaidi kiasi cha kutaka kulazimisha kila mtu afuate imani yao (pasipo kujali ni Muislamu au la).
Uchambuzi wa wasifu wa baadhi ya viongozi wa vikundi hivyo unatoa picha ya waumini ambao ‘si washika dini kihivyo’ lakini ‘wenye hasira kali dhidi ya yeyote asiyeshika dini inavyostahili.’
Kwao, ‘kafir’ si asiye Muislamu tu bali hata Muislamu anayeshirikiana na wasio Waislamu (hata pale ambapo ushirikiano huo hauna madhara kwa Waislamu na dini yao).
Kuna tatizo jingine la msingi. Wakati kumekuwa na jitihada kubwa kwa Wakristo kutafsiri Biblia Takatifu kwa Kiswahili, yayumkinika kusema kuwa jitihada za kuitafsiri Kuran Tukufu kwa Kiswahili hazijaendelezwa vya kutosha.
Sasa, kwa vile ni rahisi kutumia Maandiko Matukufu/Matakatifu kuhalalisha au kuharamisha kitu fulani, kutoa fursa kwa watu wasio na uelewa wa kutosha wa maandiko hayo kuwa viongozi wa dini kunaweza kuwa na madhara.
Kwa uelewa wangu, ijtihad ni jukumu la wanazuoni wa Kiislamu, lakini kuna uthibitisho wa kitaaluma kuwa baadhi ya viongozi wa vikundi vya Kiislamu vyenye msimamo mkali wamejipachika jukumu hilo na kufanya tafsir (exegesis au tafsiri) katika minajili inayoendana na ajenda/matakwa yao (ya ‘msimamo mkali.’)
Japo katika Uislamu ni vigumu kuchora mstari unaotenganisha dini na siasa, tofauti na kwenye siasa ambapo mwananchi yeyote yule anaweza kuwa mwanasiasa, kwenye dini ni tofauti, kwani uelewa wa dini (kwa maana ya maandiko, sheria, nk) ni kigezo muhimu cha kuwa na mamlaka ya kuwaongoza waumini wengine.
Katika toleo lijalo, makala ya mwisho wa mfululizo huu itaangalia vikwazo vya ndani ya Uislamu kupata ufumbuzi wa manung’uniko yao; baadhi ya migongano ya kiimani kati ya Waislamu na Wakristo, na ‘utata’ katika Katiba kuhusu migongano hiyo; mapendekezo ya nini kifanyike kukabiliana na vurugu za kidini huko nyumbani.
ITAENDELEA


28 Oct 2012


KABLA ya kuingia kwa undani katika makala hii ambayo ni mwendelezo wa makala iliyochapishwa katika toleo la wiki iliyopita, naomba niwasimulie wasomaji mkasa ambao unaweza kuwa “funga kazi” katika utitiri wa vimbwanga vya watawala wetu.
Wiki iliyopita, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo, aliwatia aibu Watanzania akiwa Afrika Kusini alipodai kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaundwa kwa Muungano kati ya kisiwa cha Bahari ya Hindi cha Pemba na Zimbabwe. Ukidhani ninamsingizia, basi angalia video hii kupitia kiunganishi hiki; http://goo.gl/uW6H2
Na licha ya kufanya madudu hayo, Mulugo ‘alilikoroga’ zaidi alipodai kuwa Muungano huo wa ‘Zimbabwe na Pemba’
ulitokea mwaka, (namnukuu) “one nineteen sixty-four.” Mwaka huo hauleti maana yoyote, iwe kwa Kiingereza au kwa Kiswahili, kwani 1-19-64 inaweza tu kuleta maana kwa mfumo wa tarehe wa Marekani (yaani tarehe 19 mwezi wa kwanza mwaka 64).
Ninaomba nitamke bayana kuwa Naibu Waziri Mulugo ni mzembe wa hali ya juu. Yawezekana aliandaliwa hotuba hiyo, lakini haihitaji busara japo kidogo kuwa huwezi kukurupuka kutoa hotuba kabla hujaipitia. Sijui Rais Jakaya Kikwete alijisikiaje baada ya kuona video hiyo yenye hotuba ya Mulugo, lakini kwa kosa hilo la ajabu kabisa, Naibu Waziri Mulugo sio tu anapaswa kutuomba radhi Watanzania kwa kupotosha historia ya taifa letu bali pia ingefaa aondolewe katika wadhifa wake unaoshughulikia elimu (elimu gani hiyo ambayo wakati Tanzania ‘haijamalizana’ na Malawi kuhusu mpaka kwenye Ziwa Nyasa, yeye ‘anaihamasisha Zimbabwe ‘idai Pemba ni sehemu ya nchi hiyo?’)
Nisiongelee sana suala hilo bali ninawaachiwa Watanzania wenzangu kuhitimisha wenyewe kuhusu madudu haya ‘ya karne.’
Kama nilivyoahidi katika toleo lililopita, wiki hii ninaendelea na mjadala kuhusu vurugu za kidini ambazo kwa siku za karibuni zinaonekana kushika kasi.
Katika makala iliyopita, nilijaribu kuonyesha sababu zilizojenga msingi wa manung’uniko ya Waislamu katika masuala ya elimu na ajira. Mwishoni mwa makala hiyo niliuliza maswali yafuatayo (ninajinukuu)
“Je; kilichotokea Mbagala ni hasira tu za baadhi ya Waislamu waliochukizwa na kitendo cha ‘mtoto wa Kikristo’ kukojolea Kuran Tukufu?
Je; udini ni tatizo kubwa katika Tanzania yetu ingawa halizingumzwi vya kutosha? Binafsi, ninaamini jibu la swali hilo, ni ndiyo. Kama ni ndiyo, kwa nini tunalikwepa tatizo hili?
Je; yawezekana udini ni turufu muhimu kwa baadhi ya wanasiasa mufilisi?”
Kwa swali la kwanza, nilishabainisha kwenye makala hiyo kuwa kwa mtizamo wangu, vurugu hizo za Mbagala zilisababishwa na zaidi ya hasira za baadhi ya Waislamu waliokasirishwa na kitendo cha mtoto kuikojolea Kuran Tukufu.
Yayumkinika kusema kuwa hasira za baadhi (na pengine ni wengi) ya Waislamu huko nyumbani (Tanzania) ni dhidi ya kile kinachotajwa kama ‘Mfumo Kristo.’ Kwa kifupi, wanaoamini hivyo wanauona mfumo huo unawapendelea Wakristo sambamba na kuwabagua Waislamu, hususan katika sekta za elimu na ajira, ambazo kimsingi zinahusiana kwa karibu.
Japo, kama nilivyobainisha katika makala yangu iliyopita kuwa Ukristo kwa kushirikiana na ukoloni ulichangia kutengeneza hali ya kutokuwa na usawa katika elimu na ajira, haimaanishi moja kwa moja kuwa Wakristo wanawabagua Waislamu. Naomba nieleweke hapa: kuna tofauti kati ya mfumo na watu wanaonufaika au kuathiriwa na mfumo huo.
Ninasema hivyo kwa sababu, wakati hoja ya kuwa Wakristo wanawabagua Waislamu ingeweza kuwa na mashiko wakati wa utawala wa Awamu ya Kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, na Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa, ambao wote ni Wakristo, ni vigumu kwa hoja hiyo kuwa na uzito kwenye Awamu ya Pili na hii ya sasa (ya Nne) za marais Waislamu Ali Hassan Mwinyi na Jakaya Kikwete.
Hata hivyo, kwa mtizamo wangu, viongozi hao wote wanne, hawawezi kukwepa lawama kuwa kwa kiasi kikubwa hawajafanikiwa sio tu kuyatupia macho kwa makini malalamiko ya Waislamu bali pia wamekuwa wakikwepa kuyashughulikia kwa uzito unaostahili.
Angalau kwa upande wa Baba wa Taifa tunaweza kukubaliana kuwa sio tu kwamba alishakiri kuwa kukosekana kwa usawa katika elimu na ajira kwa Waislamu ni tatizo, lakini pia alikwenda mbali zaidi na kujaribu kuukarabati mfumo wa elimu ili uweze kutoa fursa kwa Watanzania wote bila kujali imani zao.
Ni muhimu kukumbuka kuwa licha ya ukweli kuwa Mwalimu alikuwa Mkristo na mshika dini, mafanikio yake katika harakati za kupigania uhuru yalichangiwa zaidi na Waislamu.
Lawama ‘kubwa’ inayoweza kuelekezwa kwa Mwalimu ni jinsi serikali yake ilivyoshughulikia suala ‘nyeti’ la uundwaji Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na kupigwa marufuku Jumuiya ya Ustawi wa Waislamu wa Afrika Mashariki (East African Muslim Welfare Society- EAMWS).
Kwa kifupi, tangu kuundwa kwake, kwa kiasi kikubwa BAKWATA imeshindwa kujitenganisha na serikali, na pia imeshindwa kufuta hisia kuwa ‘ni chombo kinachotumiwa na serikali kuwagawanya na kuwakandamiza Waislamu.’
Japo EAMWS ilikuwa taasisi ya kidini lakini ilionekana kama ‘mkombozi wa Waislamu’ hususan kwenye sekta ya elimu, na yayumkinika kusema kuwa laiti kuundwa kwa BAKWATA kungeibua taasisi yenye ufanisi kama EAMWS, basi pengine pengo lililopo kwenye maeneo ya elimu na ajira kati ya Waislamu na Wakristo lingekuwa limepungua kwa kiasi kikubwa.
Ufinyu wa nafasi unaninyima fursa ya kuingia kwa undani kujadili hoja za kuifungia EAMWS na hatimaye kuanzisha BAKWATA, lakini ukweli kwamba serikali hiyo hiyo iliyoipiga marufuku EAMWS ilishiriki kikamilifu katika uundwaji wa BAKWATA umechangia kudumu kwa hisia kuwa ‘BAKWATA iliundwa kama chombo cha serikali dhidi ya Waislamu.’
Na katika utafiti wangu, matokeo ya awali yanaonyesha Waislamu wengi hawaridhishwi na mwenendo wa BAKWATA katika kutetea maslahi yao. Kimsingi, moja ya jambo lilionekana ‘kuwaunganisha’ wahojiwa wangu wa Kiislamu (ambao nilieleza katika makala iliyopita kuwa niliwagawanya katika makundi mawili ya ‘walio na msimamo mkali’ na ‘wa kawaida’- kwa minajili ya kiutafiti- ni suala hilo la BAKWATA.
Sasa katika mazingira haya ambacho chombo pekee kikuu kinachotarajiwa kuwaunganisha Waislamu kinaonekana kuwa kinawakandamiza, na-kuwanukuu baadhi ya wahojiwa- ni sehemu ya ‘Mfumo Kristo’ ni wazi kuwa baadhi (na pengine wengi) ya Waislamu wanajiona kama ‘mateka wa mfumo,’ kwa maana ya hisia za kubaguliwa na Wakristo na kubaguliwa na chombo kinachopaswa kutetea maslahi yao (BAKWATA).
Kwa mtizamo wangu, kuwa ‘mateka wa mfumo usiokubalika’ kunasababisha kuuchukia, na kama tujuavyo, chuki huzaa hasira. Hasira hizo zinasubiri mazingira ‘mwafaka’ ili zichomoze hadharani. Na tukio kama la Mbagala lilitoa ‘fursa mwafaka’ kwa hasira hizo.
Na ‘hasira’ hizo zinatoa jibu la swali la pili kuhusu udini. Kwamba Waislamu wanawachukia Wakristo, sitaki kuamini hivyo. Kwamba Waislamu (baadhi au wengi) wanachukizwa na mfumo wanauona kuwa unawabagua na kuwapendelea Wakristo, binafsi jibu langu ni ndio.
Na kwa vile ni vigumu kutofautisha ‘Mfumo Kristo’ na Wakristo kama waumini wa dini, ni muhimu kutambua kuwa kwa namna fulani-kubwa au ndogo- kuna uhasama wa kisaikolojia au kihisia kati ya madhehebu haya mawili. Kinachosaidia ‘kuficha’ uhasama huo ni misingi iliyojengwa huko nyuma ambayo ilisisitiza zaidi Utanzania wetu kuliko Uislamu au Ukristo wetu.
Kwa bahati mbaya-au makusudi-misingi hiyo inavunjwa kwa nguvu na wanasiasa waliokuja baada ya Mwalimu Nyerere. Kwa kifupi, wakati siasa ya Ujamaa na Kujitegemea ilijenga misingi ya kutuunganisha Watanzania tuwe kitu kimoja, ‘ubabaishaji’ uliofuatwa-kwa mfano kinachoitwa Azimio la Zanzibar- umechangia sana kukuza ombwe lililotokana na ‘kifo cha Ujamaa,’ na wakati huo huo kutoa fursa kwa wenye ‘hasira’ zao kuziweka hadharani.
Kama nilivyowahi kuandika katika makala moja huko nyuma kuhusu unafiki wetu kuhusu suala la ushoga (hoja kubwa ikiwa ni imani zetu za kidini na mila na desturi zetu), kuna unafiki unaoendelea katika sio tu kuzungumzia suala la udini kwa uwazi zaidi bali pia hakuna utashi wa kisiasa (na hata kijamii) kukabili tatizo hili.
Ni nani asiyejua kuwa wakati wa utawala wa Mwinyi kulikuwa na baadhi ya Wakristo waliokuwa wakinung’unika chini chini kuwa teuzi za Mwinyi zilikuwa zinapendelea Waislamu? Ni nani pia asiyejua kuwa alipokuja Mkapa lawama kama hizo ziliendelea kuwapo chini chini kuwa Mkapa alikuwa akiwapendelea Wakristo? Na ni nani atakayejifanya hajui kuwa utawala wa Rais Kikwete umekuwa ukilaumiwa chini chini kuwa unawapendelea Waislamu?
Ninafahamu kuna watakaosema hizi ni hisia zangu tu. Hawa ndio ninaowaita wanafiki. Na unafiki huu ndio miongoni mwa vikwazo vikubwa vya kujadili tatizo la udini, na vurugu zinazohusishwa na tatizo hilo, kwa hofu ya kuitwa mdini. Niseme hivi, bora niitwe mdini kwa kujitoa mhanga kuanzisha mjadala wa suala hili kuliko ‘nionekane mwema’ ilhali tunalipeleka taifa letu mahali kusikofaa.
Nitajitahidi kuhitimisha mfululizo wa makala hizi kuhusu vurugu za kidini kwenye toleo lijalo, au pengine makala mbili zijazo. Hata hivyo, nihitimishe makala hii kwa jibu fupi kwa swali la tatu kuhusu udini unavyotumiwa na wanasiasa mufilisi kwa minajili yao binafsi.
Ninaamini sote tunakumbuka jinsi kampeni za uchaguzi mkuu uliopita zilivyogubikwa na tuhuma za udini. Na hapa nisiume maneno: chama tawala CCM kilifanya kila jitihada kuufanya ‘upadri’ wa mgombea wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, kuwa turufu muhimu ya kumnyima kura za Waislamu. Hili nitalijadili kwa kirefu katika makala ijayo, lakini kwa namna fulani, CCM haiwezi kukwepa lawama kuwa ni miongoni mwa vyanzo vya vurugu za kidini tunazoshuhudia hivi sasa.
Chama cha siasa kinapoamua kwa makusudi kuwagawa wapiga kura kwa misingi ya imani zao za kidini, kinaandaa ‘viungo’ kwa ajili ya vurugu za kidini. Na ikumbukwe kuwa ni CCM hii hii iliyowahadaa Waislamu kuhusu kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi (huku ikitambua kuwa haina dhamira ya dhati ya utekelezaji wa ahadi hiyo) na hadi sasa inaendelea kucheza danadana katika suala hilo.
Nimalizie makala hii kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa tuna kila kitu cha kupoteza (everything to lose) kwa kutengana kwa misingi ya kidini na hatuna cha kupoteza (nothing to lose) tukiendelea kuwa wamoja, kama majeruhi wa ufisadi, umasikini, magonjwa na dhahma nyingine zinazotukabili ambazo hazijali imani zetu za kidini. Ili Tanzania yetu ifike mahala tunapotamani ifike, au inapostahili kuwa, ni lazima tuwe kitu kimoja. Tukumbuke, UMOJA NI NGUVU NA UTENGANO NI UDHAIFU
Makala hii itaendelea toleo lijalo


19 Oct 2012
























































Picha zote kwa hisani ya Blogu ya AUDIFACE JACKSON

18 Oct 2012


KWA mara nyingine, wiki iliyopita Tanzania imeshuhudia ‘sura mbaya’ (ugly face) ya imani ya kidini. Kwa mujibu wa taarifa zenyewe, kilichoanza kama mchezo wa watoto kilisababisha vurugu kubwa zilizopelekea makanisa zaidi ya matano kuchomwa moto, sambamba na uharibifu wa mali kadhaa.
Inaelezwa kwamba chanzo cha vurugu hizo ni kitendo cha mtoto mmoja kuikojolea Kuran Tukufu baada ya ‘mabishano ya kitoto’ na mtoto mwenzie. Habari zinasema mtoto aliyefanya kitendo hicho alitaka kuthibitisha ukweli wa ‘tishio’ alilopewa na mtoto mwenzie kuwa iwapo atakikojolea Kitabu hicho Kitukufu, basi atageuka nyoka!
Sote tuliwahi kuwa watoto katika hatua za mwanzo za maisha yetu, na kwa kutumia uzoefu huo kama ‘watoto wa zamani’ tunaweza kukumbuka vitu vya ajabu, vya kukera, vya kuchekesha, na vya kila aina ambavyo twaweza kuvihitimisha kwa msemo huu wa Waingereza: ‘kids will always be kids’ (watoto wataendelea kuwa watoto).
Kwamba binadamu, pasipo kujali umri wake, anaweza kukojolea Kitabu Kitukufu cha dini fulani, ni jambo lisilopendeza hata kidogo. Na kwa hakika, kitendo cha aina hiyo, kitamchukiza kila muumini wa dini husika. Lakini kama ilivyo katika maeneo mengine ya maisha ambapo umri unaangaliwa kama kigezo muhimu cha kuhukumu tendo, ukweli kwamba aliyekojolea Kuran Tukufu ni mtoto wa miaka 14, ulipaswa kupewa uzito na baadhi ya waumini wa dini ya Kiislam ambao waliamua kuchukua sheria mkononi kwa kufanya vurugu kubwa ikiwa ni pamoja na kuchoma moto makanisa.
Licha ya kuguswa na tukio hilo la kusikitisha kama Mtanzania na Mkristo, lakini pia nimeguswa kwa vile linahusiana na eneo ambalo nimekuwa nikihangaika nalo kitaaluma kitambo sasa. Miaka michache iliyopita, nilikuja huko nyumbani kukusanya data kwa ajili ya utafiti wa kitaaluma kuhusu harakati za vikundi vya Kiislam nchini Tanzania. Kwa sababu zilizo nje ya uwezo wangu, utafiti huo bado haujakamilika japo katika hatua niliyofikia unaweza kutoa majibu fulani kuhusu kinachoendelea huko nyumbani hivi sasa.
Nilipata fursa ya kuzungumza na makundi makuu mawili ya waumini wa dini ya Kiislam. Wale tunaoweza kuwaita ‘wenye msimamo mkali’ na wale wa ‘wenye msimamo wa kawaida.’ Naomba nisisitize kuwa matumizi ya maneno ‘msimamo mkali’ na ‘kawaida’ ni kwa minajili ya mjadala tu. Ninatoa tahadhari hii mapema kwa kuchelea uwezekano wa shutuma kuwa ninawagawa Waislam katika makundi, ambayo kama ilivyothibitika katika utafiti wangu, wengi wao hawapendi mgawanyo wa aina hiyo kwani wanaamini wote ni Waislam.
Moja ya mambo yaliyojitokeza katika mahojiano yangu na ‘makundi’ yote mawili ni manung’uniko (grievances) ambayo yamedumu kwa muda mrefu. Manung’uniko hayo yameshamiri zaidi kwenye suala la usawa katika elimu na ajira. Wahojiwa wengi walionyesha kuwa na hisia ya kubaguliwa kati yao na Wakristo katika upatikanaji wa fursa za elimu na ajira. Kimsingi, ukimnyima mtu fursa ya elimu, unatengeneza mazingira ‘mazuri’ ya kumkwaza kupata ajira.
Takwimu mbalimbali nilizokusanya katika utafiti huo, zinaweza kusapoti madai hayo. Lakini la muhimu zaidi hapa si sapoti ya takwimu hizo, bali mazingira yaliyopelekea uwepo wa hali hiyo. Kutokana na ufinyu wa nafasi ninalazimika kutoa maelezo ya jumla kwani kupitia kipengele kimoja hadi kingine kunahitaji zaidi ya makala moja.
Kwa kifupi, moja ya sababu zilizopelekea ‘ubaguzi’ katika upatikanaji wa fursa za elimu na ajira kati ya Waislamu na wasio Waislam (hususan Wakristo) ni mfumo wa utawala wa kikoloni. Kama tunavyofahamu, wakoloni walikuwa Wakristo, na tunafundishwa kwenye somo la historia kuwa miongoni mwa ‘watangulizi wa ukoloni’ walikuwa wamisionari wa Kikristo.
Moja ya mbinu zilizotumiwa na wamisionari kutengeneza mazingira mazuri ya kutawala jamii za Kiafrika ni ‘kusilimisha,’ japo neno hilo lina maana zaidi kwenye Uislam. Ninalitumia hapa kwa maana ya kuwatoa watu kutoka katika imani yao ya awali na kuwaingiza katika imani mpya.
Lakini historia inatufundisha kuwa Uislam ulifika huko nyumbani karne kadhaa kabla ya Ukristo. Kwa bahati mbaya au makusudi, walioleta Uislam walikuwa wafanyabiashara kutoka Arabuni na Mashariki ya Mbali, na hawakuwekea mkazo sana kusambaza dini yao.
Yayumkinika kuhitimisha kwamba kushindwa kwa watangulizi hao wa Uislam kueneza dini hiyo miaka kadhaa kabla ya ujio wa Wamisionari na hatimaye wakoloni, kulichangia kurahisisha kusambaa kwa Ukristo kwa ama ‘kusilimisha’ Wapagani (ninatumia neno hili kumaanisha dini za asili za Kiafrika) na Waislam.
Tukifupisha historia, mkoloni alitumia Ukristo kama moja ya njia za kuzitawala jamii zetu. Ni katika mazingira hayo, stadi mbalimbali zinaonyesha kuwa kwa namna fulani baadhi ya Wakristo walichelea kuunga mkono mapambano dhidi ya mkoloni kudai uhuru wetu hasa kwa vile wakoloni walifanikiwa kwa kiasi fulani kuulinganisha ukoloni na Ukristo (yaani kumpinga mkoloni ni sawa na kumpinga Yesu/Mungu).
Kwa kutumia Ukristo kama njia ya kurahisisha utawala wao, wakoloni pia walitumia dini hiyo kama chombo cha kuwatenganisha watawaliwa. Kimsingi, kuna aina ya mwafaka wa kitaaluma kuwa si kwamba wakoloni waliwathamini sana Wakristo wa Kiafrika, bali waliwaona kama nguzo muhimu katika kuigawa jamii, na hivyo kuwarahisishia kiutawala jamii husika.
Ingawa kuna wamisionari waliokuja Afrika kwa minajili ya kidini halisi, wengi wao waliendelea kushirikiana na utawala wa kikoloni katika maeneo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na utoaji elimu. ‘Ushirika’ huu wa wamisionari na wakoloni katika utoaji elimu, unaweza kuelezewa kama mwanzo wa ujenzi wa tabaka la Wakristo wenye elimu na ‘wasio Wakristo’ (hususan Waislam) wasio na elimu.
Kadhalika, baadhi ya Waislam walichelea kujiunga na taasisi za elimu za wamisionari/wakoloni kwa kuhofia kuingizwa katika dini hiyo (Ukristo). Tukiweka hali ilivyokuwa kabla ya uhuru, mazingira yaliyojitokeza baada ya kuondoka mkoloni, yameendelea kwa kiasi fulani kurutubisha ‘ubaguzi’ huo wa elimu na ajira.
Baada ya kupata uhuru, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alikiri hadharani kuwa kuna umuhimu wa kurekebisha hali ya kutokuwapo usawa wa kielimu kati ya Wakristo na Waislam. Licha ya jitihada zake kubwa, hadi anaondoka madarakani ‘usawa’ huo haukuweza kufikiwa kwa kiwango cha kuridhisha.
Kuna maelezo mengine hapa. Shule za seminari za Wakristo ambazo kimsingi ni maalum kwa ajili ya ‘kuzalisha’ viongozi wa makanisa, zilikuwa ‘zikizalisha’ kundi la wasomi wa Kikristo ambao kwa sababu moja au nyingine, hawakuishia kuwa viongozi wa kanisa, bali wakachukua ajira serikalini au kwenye taasisi nyingine. Kwa upande mwingine, shule za kidini za Waislam ziliegemea zaidi kwenye utoaji elimu ya kidini, na katika mazingira hayo, tofauti na ilivyo kwa seminari, ‘hazikuzalisha’ wasomi wa kutosha kuingia kwenye ajira serikalini (naomba nieleweke kwa makini hapa).
Kwamba utawala wa Mwalimu Nyerere uliwapendelea Wakristo na kuwabagua Waislam, ni jambo ambalo halijathibitika kitaaluma. Hoja hiyo ni miongoni mwa masuala yanayojenga manung’uniko kwa baadhi ya Waislam. Kwamba baadhi ya Wakristo, hususan waliotoka seminari na kujiunga na ajira serikalini, waliwabagua Waislam na kuwapendelea Wakristo, ni jambo ambalo halijathibitika kitaaluma ingawa linawezekana kinadharia na kimantiki.
Kimsingi, tatizo si ubaguzi wa msomi/mwajiri Mkristo dhidi ya mwanafunzi/msaka ajira Muislam, bali mfumo ambao ulijengeka wakati wa ukoloni na umeendelea kuwepo. Unatoa nafasi (on merit) kwa Wakristo zaidi ya Waislam. Kama mwajiri anataka kujaza nafasi kwenye ofisi yake, anapaswa kuangalia, pamoja na mambo mengine, sifa za kitaaluma za waomba kazi. Sasa kwa vile mfumo wa elimu tuliorithi kwa mkoloni, na kama nilivyobainisha hapo juu, unatengeneza wasomi wengi wa Kikristo kuliko wa Kiislam, ni dhahiri kutarajia ‘ubaguzi’ wa nafasi za ajira.
Majuzi tumefanya sensa. Watawala wetu wamegoma kujumuisha kipengele cha dini kwa madai mbalimbali. Lakini kwa kufanya hivyo, watawala wanajinyima fursa ya kuelewa, kwa mfano uwiano wa ajira kati ya Wakristo na Waislam. Na cha muhimu hapo si kuelewa tu, bali pia kutafuta namna ya kurekebisha hali hiyo. Na hili ni tatizo la msingi linalofanya ‘tatizo la dini’ kuendelea kuwapo. Kuna hisia kwamba kwa kujaribu kulizungumzia suala hili kwa uwazi, kutazua tafrani kubwa kuliko mwafaka. Lakini sote tunajua kuwa ugonjwa hautibiki kwa kujidanganya kuwa haupo mwilini!
Je; kilichotokea Mbagala ni hasira tu za baadhi ya Waislam waliochukizwa na kitendo cha ‘mtoto wa Kikristo’ kukojolea Kuran Tukufu? Binafsi, naamini kuna sababu za ndani zaidi ya ‘hasira’ hizo na zinazosababisha ‘hasira’ hizo. Je; udini ni tatizo kubwa katika Tanzania yetu ingawa halizingumzwi vya kutosha? Binafsi, ninaamini jibu la swali ilo, ni ndiyo. Kama ni ndiyo, kwanini tunalikwepa tatizo hili?
Jibu linaweza kupatikana kwenye tatizo jingine ‘lisilozungumzika’ la kero za Muungano wa ‘Tanganyika’ na Zanzibar. Kwa kifupi, hadi sasa hakuna utashi wa kisiasa na kijamii kulikabili tatizo hili. Kwenye Muungano, kila Rais anachelea kuvunjikiwa na Muungano, ambao Baba wa Taifa ‘alishatoa radhi’ kwa atakayeuvunja. Kwenye hili la udini, viongozi wetu wanakwepa kulikabili kwa kuchelea kuonekana wadini. Kibaya, baadhi yao walitumia udini kwenye kampeni za uchaguzi mkuu uliopita. Je; yawezekana udini ni turufu muhimu kwa baadhi ya wanasiasa mufilisi?
Makala hii itaendelea wiki ijayo.




15 Sept 2011



Raia Mwema Ughaibuni
Rais Kikwete na ‘usanii’ wa Mahakama ya Kadhi!
Evarist Chahali
Uskochi
14 Sep 2011
Toleo na 203
NIANZE makala hii kwa kutoa salamu zangu za rambirambi kwa wafiwa waliopoteza ndugu na/au jamaa zao katika ajali ya boti ilivyotokea usiku wa kuamkia Jumamosi iliyopita kwenye Bahari ya Hindi kati ya Nungwi na Pemba.
Kwa mara nyingine tena Watanzania tunashuhudia wenzetu wakipoteza maisha katika ajali ambayo, kwa namna moja au nyingine, ingeweza kuepukika.
Japo hadi wakati naandaa makala hii hakujatolewa taarifa rasmi ya chanzo cha ajali hiyo, lakini kwa mujibu wa abiria walionusurika katika ajali hiyo inadaiwa kuwa chanzo inaweza kuwa boti husika kuelemewa na wingi wa abiria na mizigo.
Kwa nini ninasema ajali hiyo ingeweza kuepukika? Ni wazi kuwa laiti mamlaka zinazohusika zingeweka mbele uhai wa abiria na kuzingatia sheria zinazotawala usafiri wa majini, ni wazi kuwa chombo hicho cha usafiri kisingezidisha shehena zaidi ya uwezo wake.
Lakini kwa kuwa kipindi hiki ni cha maombolezo, naomba nisiingie kiundani zaidi kuhusu namna taifa linavyoweza kuepusha matukio ya kusikitisha kama hili kutokea tena. Kwa sasa tuelekeze nguvu zetu katika kuwasaidia majeruhi na kuwafariji wafiwa.
Nielekee kwenye dhima ya makala hii. Katika maadhimisho ya hivi karibuni ya sherehe za Idd, Rais Jakaya Kikwete alitoa hotuba iliyoelekea kuwagusa wengi ambapo, pamoja na mengine, alizungumzia suala la kurejesha (na si kuanzisha) Mahakama ya Kadhi.
Nasema kurejesha kwa vile mahakama hiyo ilikuwepo huko nyuma kabla ya kufutwa.Kwahiyo,iwapo itafanikiwa kuwepo tena itakuwa si kwa mara ya kwanza; bali mwendelezo tu wa ile iliyokuwepo awali.
Bila kuuma maneno, napenda kumwaga shutuma kwa Rais Kikwete mwenyewe kama sehemu ya tatizo la uanzishwaji wa mahakama hiyo. Ikumbukwe kuwa Chama cha Mapinduzi katika Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2005 kiliahidi kushughulikia uanzishwaji wa mahakama hiyo.
Kimsingi, hakukuwa na shinikizo lolote kwa chama hicho kuja na ahadi hiyo hewa, lakini baadaye kukatokea kurushiana mpira kati ya watendaji wa serikali na wale wa CCM.
Kama ambavyo Watanzania wengine ‘walivyoingizwa mkenge’ na ahadi hewa za kuletewa maisha bora (na badala yake kuishia kushuhudia maisha bora kwa mfisadi pekee),CCM ilitumia ahadi hiyo ya kurejesha Mahakama ya Kadhi kwa minajili tu ya kupata kura za Waislam.
Kwa bahati mbaya,Waislam hawakuibana CCM wakati huo kuhoji kwa undani namna ahadi hiyo ingetekelezwa. Kwa mfano, hawakujihangaisha kukibana chama hicho kiwape ratiba kamili ya utekelezaji wa ahadi hiyo.
Lakini haikuwachukua muda mrefu kubaini kuwa ahadi hiyo ilikuwa ni ‘changa la macho’ na ya kisiasa zaidi kuliko yenye nia ya kusikiliza kilio chao cha muda mrefu.
Binafsi, licha ya kuwa Mkristo, sina tatizo na uanzishwaji wa mahakama hiyo alimradi sheria na taratibu zikizingatiwa. Msimamo wangu huo unatokana na ukweli kwamba kihistoria huko nyuma hakukuwa na tatizo lolote lililotokana na uwepo wa mahakama hiyo.
Ni muhimu kwetu kutambua kuwa, kwa muda mrefu tofauti zetu za kidini zimefunikwa na Utanzania wetu; japokuwa baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakifanya kila wawezalo kupanda mbegu za udini kwa maslahi yao binafsi.
Siamini kabisa kuwa iwapo Mahakama ya Kadhi ikirejeshwa itawaathiri wasio Waislam kwa vile lengo kuu la chombo hicho ni kuwahudumiwa Waislam pekee.
Na jingine zuri ni kwamba mahakama hiyo inaweza kusaidia kupambana na maovu katika jamii; hususan suala la ufisadi.
Kwa nini ninamlaumu Kikwete kuhusu sakata hilo la Mahakama ya Kadhi? Licha ya utetezi wake wakati fulani kuwa si yeye aliyeandika Ilani ya Uchaguzi ya chama chake mwaka 2005, ukweli ni kwamba aliitumia ilani hiyo kugombea kura takriban nchi nzima.
Ni wazi kuwa aliona mahala fulani kwenye ilani hiyo ikieleza kwamba chama anachokitumikia na kukitumia kugombea urais kimeahidi jambo ambalo, kimsingi, yeye mwenyewe linamgusa (kwa maana naye ni Muislam).
Lakini katika ubabaishaji uliozoeleka wa wanasiasa wetu, ‘maji yalipozidi unga’, Kikwete alifikia hatua ya kudai aliyeanzisha wazo la kurejeshwa Mahakama ya Kadhi ni Augustine Mrema, na sio yeye (Kikwete).
Huku ni kukwepa wajibu; kwani hata kama wazo hilo lingekuwa kweli limeanzishwa na Mrema, lakini lina umuhimu kwa sehemu fulani ya jamii, basi, la msingi sio aliyenazisha wazo; bali kulitekeleza katika namna inayostahili.
Katika hotuba hiyo,Kikwete alizungumzia pia suala la udini na kuonya viongozi wa dini kutotumia nafasi zao kuchochea chokochoko za kidini.
Ninaamini wakati Kikwete anazungumza hayo, alikuwa anafahamu fika kuwa siasa sio jambo haramu kuingizwa kwenye dini; hasa ikizingatiwa michango ya dini katika harakati za uhuru wa nchi yetu.
Kauli za kuhamasisha kutenganisha dini na siasa hazina mashiko makubwa kwa vile hazina tofauti na kauli zilizokuwa zikitolewa na mkoloni kwa minajili ya kukwaza jitihada zetu za kupata uhuru.
Kwa wanaofahamu historia za mapambano ya ukombozi wetu kutoka himaya ya mkoloni, watakumbuka fika namna misikiti ilivyokuwa sehemu muhimu ya harakati hizo.
Mkoloni alijaribu kuharamisha dini kwenye siasa kwa vile alifahamu kuwa dini inagusa imani na inawaunganisha wanajamii/waumini kirahisi zaidi kufikia lengo wanalokusudia.
Wanasiasa wa zama za Kikwete wanarejea kauli kama hizo za mkoloni si kwa minajili ya hofu ya vurugu; bali kwa vile wanafahamu kuwa pindi wananchi watakapounganishwa na imani zao kupambana na siasa za kibabaishaji, basi, watawala watakuwa katika nafasi ileile iliyomkuta mkoloni enzi za kupigani uhuru.
Katika hotuba hiyo, Kikwete aliwataka viongozi wa dini kuhubiri amani ili kuepusha waumini wao kujihusisha na mambo yasiyokubalika. Kwa maana nyingine, alikuwa anawahamasisha kuhubiri dhidi ya maovu kama ufisadi na mengine yanayoshabihiana nayo.
Sasa, watumishi wa Mungu watawezaje kuepuka kuzungumzia siasa iwapo baadhi (kama si wengi) ya mafisadi, ni wanasiasa?
Naomba unielewe hapo.Utawezaje kuzungumzia mwanasoka, kwa mfano, pasipo kuzungumzia soka?
Kimsingi, Kikwete na wanasiasa wengi wa Tanzania wanapaswa kuwashukuru sana viongozi wa dini; kwani viongozi hao wamechangia sana kuwawezesha wanasiasa wasiofaa kuchaguliwa au kuendelea kuwepo madarakani.
Ni wazi Rais anakumbuka kuwa wakati anagombea urais kwa mara ya kwanza, baadhi ya viongozi wa dini walimtakasa na kudai yeye ni ‘chaguo la Mungu.’
Kwa nini basi hakuwakemea wakati huo kuwa wanachanganya dini na siasa? Lakini kibaya zaidi ni namna baadhi ya watu wa karibu wa timu ya kampeni ya Kikwete kwenye uchaguzi mkuu uliopita walivyofanya kila waliloweza kupandikiza mbegu za udini.
Kila aliyefuatilia kampeni hizo kwa makini atakumbuka namna mgombea wa tiketi ya urais kupitia CHADEMA, Dkt Willibrod Slaa ‘alivyochorwa’ taswira ya ‘mgombea wa Kanisa Katoliki’ huku baadhi ya vyombo vya habari vinavyomilikiwa na serikali vikidiriki kumwita padre licha ya ukweli kuwa Dk. Slaa hakuwa padre wakati huo.
Pamoja na lawama hizo kwa Kikwete, naungana naye mkono katika maelezo yake kwa Waislam kuwa adui wao katika azma yao ya kurejeshewa Mahakama ya Kadhi si kanisa au maaskofu.
Ni kweli kwamba kanisa na maaskofu wameonyesha hofu yao (si upinzani) pengine kwa kuwa kumekuwa na jitihada duni kwa Waislam wenyewe kukazani kwenye elimu ya uraia (kwa Waislam na wasio Waislam) kuhusu namna mahakama hiyo zitakavyofanya kazi.
Kama alivyosema Kikwete, Mahakama ya Kadhi haitashughulikia kesi za jinai, na hivyo wanaohofia adhabu za kukatwa mikono au kuuawa kwa mawe hawapaswi kuwa na hofu hiyo. Kinachohitajika hapo ni elimu ya kutosha kwa umma.
Nimalizie kwa kurejesha lawama tena kwa Kikwete; kwani japo aliwahakikishia Waislam kuwa kikwazo cha urejeshwaji wa Mahakama ya kadhi si Kanisa au maaskofu, hakuwaeleza ukweli kwamba kikwazo kikubwa ni walaghai wa CCM ambao mwaka 2005 walitoa ahadi hiyo kwa minajili ya kupata kura za Waislam pasipo dhamira ya dhati ya kushughulikia suala hilo.
Kabla ya kuahidi kuwa suala hilo linashughulikiwa, Kikwete alipaswa kuwaomba radhi Waislam kwa ‘usanii uliofanywa na CCM kuingiza hoja hiyo kwenye ilani yake ya uchaguzi mwaka 2005’ lakini hadi sasa imeendelea kuwa ahadi tu - kama zilivyo ahadi nyingine lukuki zinazoendelea kutolewa kila kukicha.

Wasomaji

200
Wasiliana


12 Sept 2011

JUMUIYA ya Taasisi za Kisilamu, imesema utatumia maandamano ya usiku na mchana, kushinikiza kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi na kwamba hatua hiyo inakuja baada ya kushindikana kwa njia ya kidiplomasia, kuhusu kuanzishwa kwa mahakama hiyo.

Hayo yalibainishwa jana na Katibu Mkuu wa Shura ya Maimamu Tanzania, Shehe Issa Ponda, alipokuwa akisoma tamko la msimamo wa Taasisi za Kisilamu kufuatia kauli ya Rais Kikwete katika Baraza la Idd el Fitri, lililofanyika Septembe mosi mwaka huu mjini Dodoma, kuhusu kuanzishwa kwa mahakama hiyo.

Shehe Ponda alizitaja taasisi zilizokutana na kuazimia kutoa tamko hilo kuwa ni pamoja na Baraza Kuu, Jopo la Mashehe, Baraza la Vijana wa Kiislamu na Basuta.

Alisema, baada ya kukutana wameamua kutoa tamko la kupinga hotuba ya Rais Kikwete na kwamba hatua hiyo imetokana na kutokubaliana na baadhi ya vipengele vilivyomo katika hotuba yake kuhusu kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi.

“Moja ya vipengele vilikuwamo katika hotuba yake (Rais Kikwete) ni kwamba Serikali haitaanzisha Mahakama ya Kadhi na kwamba badala yake Waislamu wenyewe ndiyo waanzishe mahakama hiyo. Hii moja inonyesha kutokukubaliana juu ya kuanzishwa kwa mahakama hiyo,” alisema Shehe Ponda.

Alisema hakuna mahakama yoyote inayoweza kuanzishwa ikiwa nje ya dola na kwamba vinginevyo mahakama hiyo haitakuwa na nguvu katika kutekeleza majukumu yake.

“Lakini pia Jumuiya ya Taasisi za Kislamu, inapingana na kifungu cha pili na cha tatu cha hotuba kwamba Mahakama ya Kadhi haitowekwa ndani ya katiba, jambo linalomaanisha kwamba haitakuwa na nguvu kama ilivyo kwa mabaraza ya Kiisilamu ambayo yamesajiliwa kwa utaratibu wa kawaida lakini hayana uwezo wa kisheria,”alisema Shekhe.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Jumuiya za Taasisi za Kiislamu, Ramadhani Sanze, alisema njia pekee ya kudai haki ya kutaka kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi hapa nchini ni kufanya maandamano ya usiku na mchana ili kilio cha Waislamu kiweze kusikilizwa.

“Wasilamu hawawezi kukubali kuona haki yao ya msingi ya kutaka kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi haipatiwi majibu sahihi, Kumekuwa na maneno mengi ya kuzungushwa kuhusu undwaji wa chombo hiki muhimu ambacho tunaamini kitasaidia kupunguza matatizo ya Waislamu,” alisema Shehe Sanze.

Alielezea kushangazwa kwake na kauli ya Rais Kikwete kwamba mahakama hiyo, itanzishwa na Wasilamu wenyewe.Alisisitiza kuwa waumini wa dini hiyo, wanaamini kuwa hakuna mahakama yoyote inayoweza kuwa na nguvu kama itakuwa nje ya dola.

“Kauli ya Rais Kikwete inaashiria kwamba hakuna uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi, mahakama yoyote haiwezi kuwa nje ya chombo cha dola vinginevyo, haitakuwa na nguvu za kisheria,” alisema Sanze.

CHANZO: Mwananchi

7 May 2011


Nilipofika hapa Uingereza kwa mara ya kwanza,takriban muongo mmoja uliopita,nilishangazwa na jinsi wengi wa watu hawa waliotuletea dini huko nyumbani wakiwa hawana habari kabisa na dini.Ilinishangaza kuona baadhi ya majengo yaliyokuwa yakitumika kama nyumba za ibada huko nyuma yakiwa yamegeuzwa klabu za usiku au baa.

Kwa ujumla,idadi kubwa ya wanaohudhuria makanisani kwa hapa ni raia wa kigeni au wale wenye asili ya nje ya nchi hii.Hata hivyo,kuna idadi ya wastani ya Waingereza wanaojitambulisha kama wenye imani ya kidini japo haimaanishi kuwa wanakwenda makanisani.

Pamoja na kuzorota kwa dini miongoni mwa wengi,kwa kiasi kikubwa wananchi hapa wana uadilifu mkubwa hususan katika kutoa huduma.Unajua,kibarua sio suala la mshahara tu bali pia kujali yule unayemhudumia.Kadhalika,kutoa au kupokea rushwa sio tu suala la kukosekana kwa sheria madhubuti bali pia ni suala la kiroho,namna nafsi inavyomsuta mtu kutoa,kudai au kupokea rushwa.

Binafsi nadhani dini ya kweli ni upendo.Na hata katika Biblia Takatifu tunafundishwa kuwa ni vigumu mtu kumpenda Mungu ambaye hamuoni ilhali anamchukia jirani yake anayemwona kila mara.

Japo ni muhimu kuhudhuria nyumba za ibada,lakini binafsi naona ni bora kuwa mtu asiyekwenda kanisani au msikitini lakini anaishi katika namna anayompendeza Mungu (na wanadamu wenzie) kuliko hao wasiokosekana makanisani au misikitini lakini ndio wanaodumisha uzinzi,ufisadi,unafiki,na kila aina ya baya.Hapa simaanishi kuwa kila aendaye kanisani au msikitini hafanyi anayopaswa kufanya,bali napigia mstari umuhimu wa matendo mema.

Kwa hapa Uingereza kumekuwa na mfumuko mkubwa wa makanisa "mapya" (new Christian movements).Makanisa haya yanazidi kupata waumini wengi na kukua aidha kwa sababu madhehebu makuu (Katoliki,Waluteri,Waanglika,nk) yameshindwa kukidhi matarajio ya waumini hao wanaokimbilia makanisa mapya,au kwa upande mwingine ni ukweli kuwa licha ya majukumu ya kiroho,makanisa hayo ambayo waumini wake wengi ni wageni (hususan Waafrika) yamekuwa kama sehemu ya watu wanaotoka eneo moja kujumuika.Mnaijeria akienda kanisa la Kinaijeria anajikuta kama yupo nyumbani,na hivyo hivyo kwa Mtanzania akienda kanisa linaloendesha ibada kwa kiswahili.

Lakini,baadhi ya makanisa hayo yamekuwa yakishutumiwa kuwa ni miradi ya kitapeli ya wajanja flani.Kwa mfano,kituo cha runinga cha Channel 4 kiliwahi kuonyesha documentary ya namna baadhi ya makanisa ya Waafrika jijini London yalivyokuwa yakisababisha kuvunjika kwa ndoa (kwa mfano pale mchungaji anapomwambia mume kuwa mkewe ana majini) na hata kupelekea vifo,hususan vya watoto wadogo wanaotuhumiwa kuwa wana majini.Kibaya zaidi,baadhi ya maaskofu wa makanisa hayo walidiriki kudanganya mabinti kuwa matatizo waliyokuwa nayo yalihitaji maombi maalumu nyakati za usiku,na hatimaye mabinti hao wakaishi kufanyiwa tendo la ndoa.

Utafiti mdogo tuliofanya mie na wanafunzi wenzangu Faith Msina,Latifa Almasi (Queen Latifa) na Baraka Msemwa,mwaka 1999 (kama sehemu ya kozi ya Mwaka wa Tatu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika Sosholojia ya Dini) ulionyesha matokeo kwamba wengi wa watu wanaoamua kujiunga na "madhehebu mapya" ni pamoja na wale wenye matatizo ya kibinadamu ambayo "dini kuu" zimeshindwa kuyatatua.Tulifanya utafiti wetu kwenye Kanisa "la Kakobe" (Full Gospel Bible Fellowship),Mwenge jijini Dar,na asilimia kubwa ya wahojiwa walikiri kuwa kilichowavutia kujiunga na kanisa hilo ni "miujiza" mbalimbali,kwa mfano kwenye uponyaji,ajira,nk.

Lakini jambo la kusikitisha ni tabia inayozidi kushamiri ya matapeli kuanzisha makanisa kama ajira.Hawa ni wajanja wanaofahamu fika kuwa masuala ya imani hayahitaji udadisi,na laiti tapeli husika akifanikiwa kutangaza "miujiza yake",basi muda si mrefu kijikanisa chake kitageuka hekalu kubwa la "maombezi na miujiza".Simaanishi kuwa wote wanaoanzisha makanisa ni matapeli,lakini ni ukweli usiopingika kuwa kuna matapeli kadhaa wanaotumia jina la Bwana kutapeli waumini wenye mahitaji ya kimwili na kiroho.

Ni kwa mantiki hiyo basi,siafikiani na msimamo wa baadhi ya wachunga kondoo wanaopinga dhamira ya serikali kukagua mapato na matumizi yao.Pengine ni kukosa ufahamu tu,uamuzi wa serikali kutotoza kodi au kutoangalia mapato na matumizi ya taasisi za dini ni suala la upendeleo (privilege) zaidi kuliko stahili.Kama waumini wa taasisi hizo za kidini wanawajibika kwa mamlaka za mapato,kwanini isiwe kwa viongozi wa dini na/au taasisi zao?

Je wachunga kondoo hao wa Bwana wanahofia nini kuhusu dhamira hiyo nzuri ya serikali?Ieleweke kuwa kama wana kipato juu ya kiwango cha msamaha wa kodi basi ni lazima walipe kodi.Lakini hata kama suala hapa si ulipaji wa kodi,ni muhimu kwa mamlaka za mapato kufahamu mapato na matumizi ya taasisi hizo kama ilivyo kwa taasisi nyingine za umma na za binafsi.Dini si kigezo cha kutofuata sheria,na hata Maandiko Matakatifu yanakumbusha kuwa "ya Musa apewe Musa,na ya Kaizari apewe Kaizari",or something like that.

Enewei,soma habari husika hapa chini

Maaskofu wapinga serikali kudai taarifa za mapato

na Betty Kangonga

BAADHI ya makanisa ya Kipentekoste yamesema si haki kwa serikali kudai taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za makanisa wakati yenyewe haitoi hata ruzuku kwa taasisi hizo za dini.

Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mchungaji wa Kanisa la Maombezi la Ubungo Kibangu (GRC), maarufu kama Mzee wa Upako, Anthony Lusekelo, wakati wa hafla ya chakula cha usiku kwa wachungaji 100 wa makanisa ya Kipentekoste.

“Huu ni uonevu usio na mfano, wachungaji lazima tusimame imara kuhakikisha tunatetea haki zetu, tena tunatakiwa kuacha woga. Kwa nini serikali inahitaji mapato na matumizi wakati hawajui fedha hiyo tunapopata? Tunahitaji serikali ijenge heshima na kazi inayofanywa na viongozi wa dini ndani ya nchi,” alieleza.

CHANZO:Tanzania Daima

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.