Showing posts with label WAISLAM. Show all posts
Showing posts with label WAISLAM. Show all posts

11 Nov 2012


KATIKA matoleo mawili yaliyopita ya jarida hili maridhawa, safu hii imekuwa ikijadili vurugu za kidini zilizojitokeza hivi karibuni nchini.
Katika makala hii, nitaanza sehemu ya kwanza ya kuhitimisha mjadala huo (na sehemu ya pili ya hitimisho itakuwa katika toleo lijalo).Ni matarajio yangu kuwa mfululizo huu wa makala hizi utafungua mjadala mpana zaidi kuhusu hali ya dini nchini Tanzania, nafasi ya dini katika kujenga au kubomoa amani, na hatimaye mapendekezo ya nini kifanyike kudumisha umoja, upendo, amani na mshikamano miongoni mwetu.
Mwamko ulioonyeshwa na makundi mbalimbali ya kijamii katika kulaani na kuzungumzia suala hili unatoa picha chanya kuwa wengi wetu tunatamani kuiona Tanzania yetu ikiendelea kuwa “kisiwa cha amani” (japo neno ‘amani’ lina tafsiri pana, na linaweza kuzua mjadala mwingine mpya. Lakini kwa minajili ya mada hii, tuitafsiri amani kama hali ya utulivu na maelewano miongoni mwa jamii).
Katika makala zilizotangulia, nilijikita zaidi kubainisha sababu ambazo kwa uelewa wangu zilichangia kuleta vurugu hizo za kidini. Nimejaribu kurejea historia ya nchi yetu, kabla na baada ya uhuru, na kuonyesha sababu zilizozalisha manung’uniko ya Waislam, hususan katika maeneo makuu mawili ya upatikanaji (access) wa fursa ya elimu na ajira.
Kwa kuangalia michango mbalimbali ya wanajamii katika mjadala kuhusu vurugu hizo, moja ya hoja inayoonekana kupewa uzito mkubwa ni ile inayodai kuwa chanzo cha vurugu hizo si dini.
Naomba niweke bayana msimamo wangu kuwa binafsi ninazitafsiri vurugu hizo ZINA SABABU ZA KIDINI japokuwa si DINI PEKEE bali pia kuna mwingiliano wa sababu nyingine.
Ninachomaanisha hapa ni kwamba si kweli kuwa vurugu hizo hazihusiani kabisa na dini bali dini ni moja ya sababu za vurugu hizo.
Kwa kuwa katika makala zilizotangulia nimeelemea zaidi katika sababu hizo ‘zisizo za kidini kwa asilimia 100,’ katika makala hii ya mwanzo wa hitimisho nitajaribu kujadili ‘eneo hatari’ la dini kama moja ya chanzo cha vurugu hizo.
Ninasema ‘eneo hatari’ kwa sababu yayumkinika kuhisi kuwa baadhi ya wasomaji hawatopendezwa na uthibitisho nitakaoweka wazi, na ambazo ni lazima tuziongelee ili si tu tuweze kuwa na mjadala wa maana kuhusu suala hili, bali pia tuweze kuwa katika nafasi ya kusaka ufumbuzi.
Kama ilivyo mahala kwingineko (kwa maana ya si Tanzania pekee), uchambuzi kuhusu dini si tu unaweza kuzua hisia hasi (kama vile kuhisi mwandishi Mkristo haruhusiwi kukosoa Uislam, au kinyume chake), lakini pia unakabiliwa na tatizo la msingi la vigezo vingine vinavyoathiri dini husika, kama vile tofauti kati ya mjini na vijijini, idadi ya wakazi katika sehemu husika, historia ya sehemu husika, nk.
Kwa kifupi-na huu ni mfano tu-inaweza kuwa na ugumu wa namna fulani kuuchambua Ukristo kwa kutumia mikoa miwili ya Kilimanjaro na Kaskazini Pemba kama maeneo ya kupata takwimu za kuwezesha uchambuzi husika.
Wakati Kilimanjaro ina idadi kubwa ya Wakristo, Kaskazini Pemba ina idadi kubwa ya Waislamu. Tofauti hizo ‘zisipolindwa vema kwa kuzingatia kanuni za tafiti’ zinaweza kuzua matokeo ‘fyongo.’
Na suala hili la ‘vigezo vingine’ ni moja ya mambo yaliyojitokeza katika utafiti wangu kuhusu harakati za vikundi vya Kiislamu huko nyumbani.
Kwa mfano, baadhi ya wahojiwa wa Kiislamu katika jiji la Dar es Salaam walionekana kuwa na hamasa kubwa kuzungumzia ‘ubaguzi wanaofanyiwa na kile walichokieleza kama Mfumo Kristo,’ wengi wa wahojiwa katika ‘maeneo yasiyo ya mijini (rural areas) walionekana kuelemea zaidi kwenye kero zinazowakabili kila siku katika nyanja kama za afya, elimu na kilimo.
Hata mwanazuoni mmoja wa Kiislamu niliyefanya naye mahojiano alikiri kwamba, (namnukuu) “…kwa huko vijijini haya masuala ya udini hayana uzito kulinganisha na adha zinazowakabili wananchi katika maeneo hayo ambazo kimsingi hazibagui kuwa huyu ni Juma au Petro…”
Tukiweka kando ‘kikwazo’ hicho kinacholeta ugumu fulani katika kuchambua dini, moja ya mifumo (models) ya kuchambua vurugu (ziwe za kidini, kikabila, kisiasa, nk) unaonyesha hali hii (kwa mchanganuo wa jumla): ubaguzi huzua manung’uniko; manung’uniko huzua hamasa; hamasa huzua upinzani ambao waweza kuzua vurugu.
Na moja ya sababu za msingi zinazoelezwa katika model hiyo kuwa zinaweza kujenga hisia ya kubaguliwa ni kupotea kwa hali ya kujiendeshea mambo pasi kuingiliwa (autonomy).
Kufutwa kwa Mahakama za Kadhi kunaweza kuwa mfano mwafaka.
Japo mahakama hizo zilikuwa za kidini lakini kimsingi zilijitosheleza kushughulikia ‘kesi za kidini’ miongoni mwa Waislamu (yaani masuala kama mirathi, nk).
Lakini eneo jingine linaloweza kuingia katika kundi hili ni ushiriki wa baadhi ya Waislamu katika harakati za uhuru. Ushiriki huo haukuwa wa kisiasa tu bali wa kidini kwani moja ya mafundisho ya Uislamu katika kushughulikia jambo baya (kama udhalimu wa mfumo wa ukoloni) ni “kulikemea, kulichukia au kuliondoa” jambo hilo.
Kwa kutafsiri ushiriki wa Waislamu hao ulikuwa na msingi wa kidini (licha ya siasa), kujumuika kwao kuliwapa autonomy ya aina fulani, yaani kuweza kuitumia imani yao ya kidini kukabiliana na jambo baya (ukoloni).
Kama nilivyobainisha katika makala zilizotangulia, hisia kuwa “tulikuwa mstari wa mbele kupambana na mkoloni lakini uhuru ulipopatikana tumeishia kuwa chini ya wenzetu waliomsapoti mkoloni (kwa maana ya ukaribu kati ya ukoloni na Kanisa/ Ukristo)” zinaweza kutafsiriwa kama kupoteza autonomy hiyo.
Lakini pia ni muhimu kuelewa kuwa Uislamu si suala la imani pekee bali ni mfumo kamili wa maisha. Stadi zinaonyesha kuwa pindi mfumo wa kimaisha unapoonekana kuwa hatarini (kwa sababu moja au nyingine) inaweza kuleta mwamko wa kukabili tishio husika.
Kimsingi, dini hutoa mwongozo kwa muumini kuhusu maisha yake kibinafsi na katika jamii. Sasa tukiafikiana kuwa Uislamu kama dini na kama mfumo kamili wa maisha hauridhii aina yoyote ya uonevu, ni wazi hisia kuwa “Waislamu wanabaguliwa” zinaweza kufuata ile model ya ubaguzi – manung’uniko – hamasa – upinzani.
Pengine hili halitowapendeza baadhi ya wasomaji: katika utafiti wangu (na katika baadhi ya stadi nyingine) kuna uthibitisho wa kuwapo kwa vikundi vya Kiislamu vyenye mrengo mkali wa kiimani (Islamic extremists). Naomba ieleweke kuwa uwepo wa vikundi hivyo katika Uislamu haimaanishi kuwa mrengo mkali katika dini ni kwa Uislamu pekee.
Israel kuna Wayahudi wenye mrengo mkali kabisa ambao hawataki kabisa kusikia lolote kuhusu Wapalestina. Huko Marekani kuna Wakristo wenye msimamo mkali kabisa ambao kwa kiasi fulani wanachangia ‘uhasama’ kati ya taifa hilo na Waislamu na Uislamu kwa ujumla (kwa mfano Pasta Terry Jones aliyezua sokomoko duniani kwa kuchoma Kuran Tukufu).
Sasa kwa huko nyumbani, vikundi hivyo vya Waislam wenye msimamo mkali si tu ‘wameteka’ ajenda ya msingi ya manung’uniko (tunayoweza kuafikiana kuwa ni halali) ya Waislamu bali pia wamegeuza ajenda hiyo kuwa nguzo muhimu ya kupambana na wale wote wasioafikiana na mtizamo wao.
Wahanga wa ‘wana-msimamo mkali’ hawa si Wakristo pekee bali hata Waislamu wenzao wanaoonekana ‘kutokuwa na msimamo kama wao.’
Uthibitisho wa hii ni pamoja na vurugu zilizojitokeza nyakati fulani za uporaji wa misikiti. Japo wateka misikiti hao walidai kuwa wanairejesha kwa Waislamu misikiti iliyokuwa chini ya BAKWATA, kuna uthibitisho kuwa lengo lilikuwa kuigeuza misikiti hiyo kuwa ya ‘msimamo mkali.’
Badala ya hoja ya msingi inayohusu manung’uniko ya Waislamu dhidi ya mfumo wanauona kuwa unawakandamiza, vikundi vya Kiislamu vyenye msimamo mkali vinakwenda mbali zaidi kiasi cha kutaka kulazimisha kila mtu afuate imani yao (pasipo kujali ni Muislamu au la).
Uchambuzi wa wasifu wa baadhi ya viongozi wa vikundi hivyo unatoa picha ya waumini ambao ‘si washika dini kihivyo’ lakini ‘wenye hasira kali dhidi ya yeyote asiyeshika dini inavyostahili.’
Kwao, ‘kafir’ si asiye Muislamu tu bali hata Muislamu anayeshirikiana na wasio Waislamu (hata pale ambapo ushirikiano huo hauna madhara kwa Waislamu na dini yao).
Kuna tatizo jingine la msingi. Wakati kumekuwa na jitihada kubwa kwa Wakristo kutafsiri Biblia Takatifu kwa Kiswahili, yayumkinika kusema kuwa jitihada za kuitafsiri Kuran Tukufu kwa Kiswahili hazijaendelezwa vya kutosha.
Sasa, kwa vile ni rahisi kutumia Maandiko Matukufu/Matakatifu kuhalalisha au kuharamisha kitu fulani, kutoa fursa kwa watu wasio na uelewa wa kutosha wa maandiko hayo kuwa viongozi wa dini kunaweza kuwa na madhara.
Kwa uelewa wangu, ijtihad ni jukumu la wanazuoni wa Kiislamu, lakini kuna uthibitisho wa kitaaluma kuwa baadhi ya viongozi wa vikundi vya Kiislamu vyenye msimamo mkali wamejipachika jukumu hilo na kufanya tafsir (exegesis au tafsiri) katika minajili inayoendana na ajenda/matakwa yao (ya ‘msimamo mkali.’)
Japo katika Uislamu ni vigumu kuchora mstari unaotenganisha dini na siasa, tofauti na kwenye siasa ambapo mwananchi yeyote yule anaweza kuwa mwanasiasa, kwenye dini ni tofauti, kwani uelewa wa dini (kwa maana ya maandiko, sheria, nk) ni kigezo muhimu cha kuwa na mamlaka ya kuwaongoza waumini wengine.
Katika toleo lijalo, makala ya mwisho wa mfululizo huu itaangalia vikwazo vya ndani ya Uislamu kupata ufumbuzi wa manung’uniko yao; baadhi ya migongano ya kiimani kati ya Waislamu na Wakristo, na ‘utata’ katika Katiba kuhusu migongano hiyo; mapendekezo ya nini kifanyike kukabiliana na vurugu za kidini huko nyumbani.
ITAENDELEA


19 Oct 2012
























































Picha zote kwa hisani ya Blogu ya AUDIFACE JACKSON

11 Mar 2009


Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi amepigwa kofi na mmoja wa watu waliohudhuria Baraza la Maulid wakati akihutubia katika ukumbi wa Diamond Jubilee Dar es Salaam jana.Mwinyi, ambaye alimwakilisha Rais Jakaya Kikwete katika Baraza hilo, alikutwa na masaibu hayo baada ya kijana aliyefahamika kwa jina la Ibrahim Said (26) kwenda jukwaani akajifanya fundi na kumpiga kofi la nguvu Rais mstaafu.

Kijana huyo aliyekuwa miongoni mwa umati uliohudhuria baraza hilo, aliinuka wakati Rais mstaafu akizungumzia masuala ya Ukimwi na kwenda hadi jukwaani na kujifanya anarekebisha vyombo vya kupaza sauti vikiwemo na vya televisheni alivyokuwa akitumia kuhutubia.Kijana huyo ambaye alikuwa amevalia suruali ya khaki na shati jeupe, alitumia sekunde kadhaa kujifanya kutengeneza vifaa hivyo akiwa mbele ya Mwinyi na ghafla alimzaba kibao. Kitendo hicho kilisababisha viongozi waliokuwa jukwaani, kusimama ghafla na wanausalama kuingilia kati na kumkata mtama kijana huyo katika juhudi za kumdhibiti asiendelee kuleta madhara.

Miongoni mwa watu waliokuwa katika jukwaa kuu ni pamoja Sheikh Mkuu Mufti Issa Shaaban Simba, Kaimu Mufti Suleiman Gorogosi na Waziri Mkuu mstaafu, Rashidi Kawawa ambao wote walibaki katika mshangao. Baada ya wanausalama kumdhibiti kijana huyo waumini walimwagika na kuanza kumtwanga kwa ngumi na mateke na hivyo wanausalama ikabidi wabadili majukumu na kuanza kumhami. Kutokana na hekaheka hizo shughuli za hotuba zilisimama kwa dakika kama nne.

Pamoja na vurumai hizo, wanausalama walifanikiwa kumuingiza kijana huyo katika gari aina Land Cruiser yenye namba za usajili T 531 AUB na kuondolewa katika viwanja vya Diamond Jubilee na kufikishwa Kituo cha Polisi cha Selander Bridge. Kwa mujibu wa Polisi ambaye hakutaka kutaja jina lake kituoni hapo, alisema katika kumhoji, kijana huyo (Said) alijitambulisha kuwa ni mkazi wa Mabibo Farasi, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa hizo zilizopatikana kituoni hapo, Said ni mzaliwa wa Mkoa wa Dar es Salaam aliyehitimu kidato cha Sita mwaka juzi katika Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora. Kijana huyo katika maelezo yake, amejitambulisha kuwa ni Mwalimu wa masomo ya ziada katika Kituo cha Ngome Kongwe, kilichoko Mabibo. Hata hivyo, haikuweza kufahamika sababu za kijana huyo kufanya kitendo hicho kutokana na waandishi kushindwa kupata nafasi ya kuzungumza naye.

Awali, kabla ya kijana huyo kumpiga kofi kiongozi huyo mstaafu wa kitaifa, Mwinyi alikuwa akiwaasa Waislamu kuepukana na ngono zembe zinazochangia ongezeko la Ukimwi. Alisisitiza kwamba ugonjwa huu umekaa mahali pabaya na kuwasihi waumini kuwa ni jukumu la kila mmoja kujilinda. Akizungumza na waandishi wa habari, Kaimu Mufti Gorogosi, alisema amekuwa akimuona kijana huyo katika mikutano ya dini.

"Hata jana (juzi) katika Maulid usiku alikuwepo, hivyo nashindwa kuelewa kama ana akili nzuri au la," alisema Gorogosi. Alimwomba Rais mstaafu awasamehe Waislamu kwa tukio hilo. Wakati huo huo, Joseph Lugendo anaripoti kwamba Mwinyi amewataka viongozi wa dini nchini kujenga daraja la upendo, baina ya waumini wa dini tofauti badala ya kugeuka kuwa kuta zenye kuwagawa Watanzania katika misingi ya dini.

Aliwataka viongozi hao, wakiwamo masheikh na mapadri, kujenga daraja la upendo na masikilizano baina ya waumini wa dini mbalimbali, ili kuendeleza amani na mshikamano uliopo nchini. Akihutubia mkesha wa Maulid ya kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (SAW) usiku wa kuamkia jana Dar es Salaam, Mwinyi alionya viongozi hao wasigeuke kuwa kuta zisizopenyeka zitakazogawa Watanzania kwa misingi ya dini zao.

"Tupo hapa Waislamu na wasio Waislamu kwa kuwa ushirikiano Tanzania ni jadi na mila yetu, sisi huungana kusherehekea siku zote, Waislamu husherehekea na Wakristo siku ya Pasaka na Krismasi na wao hutuunga mkono kwenye Idd zote."Hili ni jambo jema linaloondoa chuki baina ya dini na kuleta mshikamano, mimi napendezwa sana na mwenendo huu na ninatoa mwito kwa mapadri na masheikh kuliendeleza," alisema Mwinyi.

Alisema hawezi kuisemea dini ya Kikristo kwa kuwa haifahamu, lakini miongoni mwa mafunzo yao ni kuwa na subira na kusamehe na kuongeza kwamba mafundisho yao (Wakristo), yamewataka anayepigwa kofi shavu moja ageuze na lingine lipokee kofi la pili. "Huu ni mfano wa kuepusha shari. Lakini na sisi Waislamu pia Mungu katutaka kuwatendea mema na uadilifu ambao hawakupigana nasi wala hawakututoa majumbani kwetu, hakika Mungu huwapenda waadilifu," alisema Mzee Mwinyi huku akinukuu baadhi ya aya kuongeza nguvu katika hoja yake hiyo.

Alisema msingi wa kuishi kwa amani, huanzia katika kaya mpaka jamii na ndio uliosababisha Tanzania kuwa kisiwa cha amani kilichozungukwa na nchi zenye vurugu na kutaja kuwa dini zimechangia kuunda msingi huo. Hata hivyo, alisema kauli hiyo haina maana kuwa nchi zisizo na amani hazina dini, bali malezi ya Watanzania yaliyotekelezwa na viongozi waliotangulia, pia yamechangia sehemu ya amani iliyopo. "Wazee wetu walitandika zulia la utamaduni wa kuishi kwa amani, upendo na utulivu ... katika hali hii ya utu uzima wangu, inanituma kuwausia vijana, tutunze utulivu huu.

"Katu tusiruhusu uondoke tusiwape wenzetu sababu ya kutupa majina mabaya, ya mjahidina na magaidi, vijana nakuusieni tena tusitoe mwanya huo, tumekuwa tukipewa majina na maadui wa nje. "Wanasema dini yetu ni ya fujo, ni wakati wa kushikamana na si wa kulumbana na kama mnajadiliana si mbaya ila kuwepo na staha, heshima na pasiwepo kejeli, ubabe wala dharau dhidi ya dini nyingine," alisema Mwinyi.


CHANZO: Habari Leo


AJALI HUTOKEA,LAKINI LINAPOKUJA SUALA LA ULINZI WA VIONGOZI AJALI ZINAPASWA KUZUIWA KWA GHARAMA YOYOTE ILE.TULISIKIA YALIYOJIRI MBEYA HIVI KARIBUNI AMBAPO KUNDI LA WANANCHI WALIURUSHIA MAWE MSAFARA WA RAIS JK.KWA MTAZAMO MPANA,TUKIO HILO LINGEWEZA KUTAFSIRIWA KAMA SEHEMU YA MAPUNGUFU KATIKA ENEO ZIMA LA ULINZI WA VIONGOZI WETU.NASEMA HIVYO KWA VILE KUNA WATU WENYE JUKUMU LA KUHAKIKISHA USALAMA WA NJIA AU ENEO ATAKALOPITA KIONGOZI,NA NI KWA UHAKIKA KUTOKA KWAO ONLY,NDIPO MSAFARA AU ZIARA YA KIONGOZI ITAENDELEA KAMA ILIVYOPANGWA.THANKS GOD,HAYO MAWE HAYAKUMDHURU YEYOTE,NA PENGINE LA KUSHUKURU ZAIDI NI KWAMBA YALIKUWA MAWE TU NA SIO SILAHA.
SASA TUNASIKIA MZEE MWINYI NAE AMEKUMBWA NA ZAHAMA KAMA INAVYOELEZWA KATIKA HABARI YA HAPO JUU NA PICHANI HAPO CHINI.INAFAHAMIKA KWAMBA ULINZI WA VIONGOZI HUWA MGUMU ZAIDI KWENYE MIKUSANYIKO AU MIKUTANO YA HADHARA LAKINI KWA KAWAIDA UGUMU HUO UNAPASWA KUWA CHANGAMOTO YA MAFANIKIO YA SHUGHULI NZIMA YA KIONGOZI HUSIKA.TUNAPASWA KUMSHUKURU MUNGU KWAMBA ALICHOPIGWA NACHO MZEE MWINYI NI KIBAO TU,LAKINI KAMA TUKIENDELEA NA "BUSINESS AS USUAL" KUNA SIKU ITAKUWA TINDIKALI AU KITU KINGINE CHENYE MADHARA.KAMA MTU HUYO ALIWEZA KUPIGA KIBAO,NI DHAHIRI KWAMBA ANGEWEZA HATA KUCHOMA KISU AU KURUSHA RISASI.KUMKATA MTAMA MHUSIKA WAKATI AMESHAFANYA MADHARA NI SAWA NA KUSOMA RAMBIRAMBI YENYE MANENO MAZURI WAKATI MTU AMESHAPOTEZA UHAI:INALIWAZA LAKINI HAISAIDII.

(Aliyemzaba kibao Mzee Mwinyi akidhibitiwa baada ya tukio.Wajuzi wa mambo ya ulinzi wa viongozi wanaweza kuafikiana nami-kutokana na picha hii-kwamba kuna mapungufu LUKUKI.Picha ya tukio kwa hisani ya MICHUZI Jr)

NI ISHARA NYINGINE KWAMBA KUNA MAPUNGUFU MAHALA FLANI.YAYUMKINIKA KUHISI KWAMBA MAPUNGUFU HAYO NI MATOKEO YA MAZOWEA.KUNA WATU WANATEKELEZA MAJUKUMU YAO KWA MAZOWEA,KWAMBA KWA VILE JANA ILIFANYIKA HIVI BASI HATA LEO ITAFANYIKA HIVYOHIVYO.DHANA YA "HOPE FOR THE BEST EXPECT THE WORST" INAONEKANA KAMA POROJO TU KWA WANAOENDEKEZA MAZOWEA.

TUSIFIKE MAHALA TUKALEWESHWA NA "AMANI NA UTULIVU".KUNA MENGI YANAYOJIRI HUKO MITAANI YANAYOASHIRIA KWAMBA KIWANGO CHA FRUSTRATIONS KWENYE UMMA KINAONGEZEKA.FOR THAT MATTER,KUNA UMUHIMU MKUBWA WA KUENDESHA MAMBO KULINGANA NA HALI HALISI BADALA YA KUONGOZWA NA HISIA AU IMANI ZISIZOZINGATIA REALITY.

IT CAN BE DONE...BUT IF AND ONLY IF SOMEONE OUT THERE PLAYS THEIR PART.



22 Aug 2006

KULIKONI UGHAIBUNI-21

Asalam aleykum,

Leo nina jambo muhimu sana kuhusiana na maslahi ya Taifa letu.Nawaomba wasomaji wapendwa tuwe pamoja kwa makini ili tusipoteane njiani na hatimaye kuleta tafsiri potofu ya ninachotaka kuzunguzia.Natanguliza rai-au niite tahadhari-kwa vile mada yangu ya leo ni nyeti,na ni kuhusu suala ambalo mara nyingi limekuwa likikwepwa na watu wengi.Lakini kabla sijaingia kwa undani,nielezee uzoefu wangu mimi mwenyewe katika suala hilo.

Kwa wafuatiliaji wa makala hii watatambua kwamba mara zote huwa naanza na asalam aleykum.Nimezowea sana kuwasalimia ndugu zangu kwa namna hiyo.Pengine ni kwa vile nimewahi kukaa miji ambayo salamu hiyo inatumika sana,au pengine wengi wa marafiki zangu ni Waislam.Robo ya elimu yangu ya msingi niliipata mkoani Kigoma katika kitongoji cha Ujiji.Nakumbuka kuna wakati flani katika darasa nililokuwa nasoma tulikuwa Wakristo watatu tu na waliosalia (nadhani zaidi ya silimia 90) walikuwa Waislam.Niliwahi kufundisha sekondari flani mjini Tanga na takribani robo tatu ya wanafunzi wangu walikuwa Waislam pia.Na nikipiga hesabu ya harakaharaka,katika marafiki zangu kumi bora saba ni Waislam.Hata siku moja,tangu nikiwa Kigoma,Tanga,Dar na kwengineko sikuwahi kujiona nimezungukwa na watu tofauti nami ambaye ni Mkristo Mkatoliki.Wanafunzi wenzangu,wanafunzi niliowafundisha na marafiki zangu walinichukulia kama Mtanzania mwenzao japo tulikuwa tunatoka madhehebu tofauti.Na hivi karibuni nilipokuja huko nyumbani kwa utafiti wa PhD nayosoma,wengi wa niliohojiana nao walikuwa Waislam.Sikuwahi kupata matatizo yoyote hata pale nilipokutana na wanaoitwa mujahidina.Katika levo ya familia,kaka-binamu yangu mmoja ambaye ni Mkatoliki wa kwenda kanisani kila Jumapili ana mke ambaye ni Mwislam wa swala tano.Uzoefu wangu huo mdogo unatoa picha moja muhimu:Watanzania tumekuwa tukijichanganya sana bila kujali tofauti zetu za kidini.Nikisema kujichanganya namaanisha kujumuika pamoja na sio vinginevyo.

Kuanzia kwenye miaka ya 80 kulianza kujitokeza dalili zilizoashiria kwamba mambo si shwari sana katika eneo la dini nchini.Tunakumbuka uvunjaji wa mabucha ya nguruwe,matukio kwenye msikiti wa Mwembechai,mihadhara ya kidini,suala la Ustaadh Dibagula na mengineyo.Wapo waliosema kwamba kulikuwa na kikundi cha watu wachache kilichokuwa kinachochea vurugu za kidini kuganga njaa zao.Wapo pia waliokuwa wanadai kuwa vurugu za kidini zilikuwa na sura ya kisiasa huku mara kadhaa chama cha CUF kikibebeshwa lawama.Yayumkinika kusema kuwa japo viongozi wetu walikuwa wakikemea vurugu hizo hakukuwa na jitihada za makusudi za kubaini chanzo hasa ni nini.Wanataaluma wetu nao kwa namna flani wamekuwa wakilikwepa suala hili pengine kwa vile linagusa hisia za wengi au pengine kutokana na hisia kwamba matokeo ya tafiti zinahusu migogoro ya kidini huweza kuchangia kuleta utata zaidi badala ya ufumbuzi wa matatizo.Mwalimu wangu wa zamani katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,Dr John Sivalon alichapisha kitabu ambacho kilitokana na thesis yake kuhusu mahusiano kati ya Kanisa Katoliki na Serikali ya Tanzania.Bila kuingia kwa undani kujadili kitabu hicho cha mhadhiri huyo wa Kimarekani ambaye pia ni Padre,ukweli ni kwamba kimekuwa ni nyenzo muhimu katika mihadhara na mijadala ya kidini nchini,japo sina hakika kama kimesaidia katika kuwa sehemu ya utatuzi wa matatizo yaliyopo.

Hebu sasa niingie kwenye ishu yenyewe.Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na mijadala inayoendelea kwenye forums mbalimbali za Watanzania kwenye internet.Suala hilo ambalo limegusa hisia zangu ni madai kwamba Rais Jakaya Kikwete amekuwa akiwapendelea Waislam katika teuzi mbalimbali anazoendelea kuzifanya tangu aingie madarakani.Na pengine kinachotajwa zaidi ni ule uteuzi wake wa kwanza wa mabalozi wa mwanzo (akina Adadi na wengineo) ambao kwa mujibu wa majina yao wote ni Waislam.Pengine bila kudadisi sifa za walioteuliwa,wanaolalamika wakaangalia dini zao.Teuzi nyingine nazo zimeendelea kuzua mijadala isiyo rasmi japo sina uhakika kama na huko nyumbani nako hali ni kama hii niliyoiona kwenye mtandao.Ila niliona kwenye mtandao makala mbili tofauti ambazo nadhani zilitolewa kwenye magazeti ya huko nyumbani ambapo mwandishi mmoja mkongwe alikuwa akijibu hoja za mwanasiasa flani ambaye nadhani pia ni kiongozi wa kidini,na mada yenyewe ilikuwa ni hiyohiyo eti Kikwete anawapendelea Waislam.

Mimi siamini kabisa kwamba yeyote kati ya aliyeteuliwa-iwe kwenye uwaziri,unaibu waziri,wakuu wa mikoa,wakurugenzi na kadhalika-wamepewa dhamana zao kutokana na Uislam au Ukristo wao.Unajua kwa miaka mingi sisi tumekuwa Watanzania kwanza halafu ndio vinafuatia vitu kama Ukristo au Undamba wangu.Na ndio maana kule Ujiji,Tanga,Dar na kwingineko nilikokuwa sikuwahi kupata matatizo na waliokuwa karibu nami kwa vile cha muhimu kwetu haikuwa dini au kabila bali urafiki au mahusiano yetu kikazi.Na naamini kabisa kuwa Kikwete ni Mtanzania kwanza,na anaongoza Watanzania kwa misingi ya umoja wao na sio tofauti za kidini,na kwa mantiki hyo hata anapochagua viongozi haangalia dini bali sifa za wateuliwa.

Hata hivyo,kuna matatizo kadhaa yanayohusiana na suala la dini nchini.Tusijidanganye kwamba hatufahamu kuwa kumekuwa na manung’uniko miongoni mwa Waislam kuhusu usawa katika sekta ya elimu na ajira.Iwapo chanzo cha tatizo hilo ni sera za kibaguzi za wakoloni au kuna mbinu za makusudi za kuchochea matatizo hayo,hiyo sio muhimu sana kama ilivyo kwa umuhimu wa serikali,taasisi mbalimbali,wanataaluma na wananchi kwa ujumla kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo.Matokeo ya awali ya utafiti wangu unaohusu harakati za Waislam nchini yanathibitisha kwamba matatizo yapo na yanajulikana ila kinachokosekana ni jitihada za makusudi za kupata ufumbuzi wa kudumu.Habari nzuri ni kwamba,hilo (la kupata ufumbuzi) linawezekana iwapo busara zitatumika na wadau kujumuishwa kwa karibu.Namalizia kwa kusisitiza kwamba wanaoleta madai ya udini wanatumia haki yao ya kikatiba kutoa mawazo yao,japo siafikiani nao.Hivi mtu anapooa au kuolewa na mtu anayetoka naye dini moja anaitwa mdini?Hapana.Kitakachojadiliwa hapo ni sifa za huyo mume au mke.Hivyohivyo,Jakaya hawezi kuitwa mdini pindi akichagua Muislam kama yeye alimradi ana sifa zinazostahili.

Alamsiki

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.