Showing posts with label Kassim Majaliwa. Show all posts
Showing posts with label Kassim Majaliwa. Show all posts

20 May 2016


WIKI iliyopita yaweza kubaki kwa muda mrefu kwenye kumbukumbu za Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Kwa upande mmoja, wiki hiyo ilimalizika kwa mkutano kati ya baadhi yao na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, na kwa upande mwingine wiki hiyo ilitawaliwa na mizengwe ya ‘kuzuia’ fursa kwa wengi kukutana na Waziri Mkuu.

Awali, zilipatikana tetesi kwamba Rais John Magufuli angefanya ziara ya kikazi hapa Uingereza, lakini baadaye ikafahamika kuwa Waziri Mkuu Majaliwa ndiye angemwakilisha.

Hatimaye Waziri Mkuu aliwasili hapa kwa mara ya kwanza tangu ashike wadhifa huo, na pia kuwa kiongozi wa kwanza wa kitaifa kuzuru nchini hapa tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani.

Wengi wa Watanzania wanaoishi nchini hapa walionyesha kiu kubwa ya kukutana na kiongozi huyo mpya, hususan kusikiliza visheni ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa Tanzania na Watanzania, ikiwa ni pamoja na tunaoishi nje ya nchi yetu.

Hata hivyo, kiu hiyo ilikumbana na kikwazo kutoka Ubalozi wa Tanzania hapa Uingereza, haukujali kutoa taarifa yoyote kwa Watanzania wanaoishi hapa kuhusu ujio wa kiongozi huyo wa kitaifa wala kueleza iwapo angekutana nao kwa maongezi.
Baadaye zikasikika tetesi kuwa Ubalozi huo (aidha kama ofisi au baadhi ya maofisa wake) ulitoa mwaliko kwa takriban watu arobaini hivi kuhudhuria ‘kikao’ na Waziri Mkuu. Tetesi hizo hazikueleza jinsi gani ‘wawakilishi’ hao walivyopatikana, lakini kilichoonekana bayana ni suala hilo kuzingirwa na usiri mkubwa.

Binafsi, nilianzisha jitihada za kuutaka Ubalozi uangalie umuhimu wa kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anayeishi hapa anapatiwa fursa ya kuhudhuria mkutano huo. Awali niliweka ujumbe kwenye kundi la ‘Whatsapp’ la Watanzania wanaoishi hapa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha.

Baadaye nilichukua jukumu la kuandika makala katika blogu yangu baada ya kuzungumza na Watanzania kadhaa wanaoishi hapa, na ambao walionyesha bayana kutoridhishwa na jinsi Ubalozi wetu ulivyoonekana ‘kuhujumu’ uwezekano wa Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa kukutana na kiongozi wao.

Kwa bahati nzuri, ‘kelele’ za makala hiyo na ‘kilio’ kilichofikishwa kwenye kituo kimoja cha radio huko nyumbani na baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa, zilizaa matunda. Hatimaye, Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa tamko kuwa Waziri Mkuu angekutana na Watanzania wanaoishi hapa.

Ofisi ya Waziri Mkuu pia ilijaribu kujitetea kuwa haikuhusika na maandalizi ya mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa, japo haikuwahi kulaumiwa na mtu yeyote kwa sababu utaratibu uliozoeleka ni kwa Ubalozi (sio Wizara au ofisi za huko nyumbani) kufanya maandalizi ya mikutano ya viongozi wa kitaifa na Watanzania wanaoishi hapa.

Kwa upande mwingine taarifa hiyo ilikuwa kama inakanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalumu waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa. Hata hivyo, kulikuwa na uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kwa kundi la watu kadhaa tu kukutana ‘kwa faragha’ na Waziri Mkuu.

Uthibitisho huo ulisikika baada ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu hapa kujirekodi na kuweka ujumbe wa sauti (voice note) kwenye kundi la Whatsapp (la Watanzania wanaoishi hapa) ambapo pamoja na mambo mengine alikebehi jitihada za kutaka Watanzania wengi zaidi wanaoishi hapa wapate fursa ya kukutana na Waziri Mkuu. Alidai kuwa “hata Rais anapoongea na wazee jijini Dar haimaanishi basi wazee wote wa Dar wataalikwa kwenye mkutano huo.” Alidai kuwa hakuna ubaya kuteua watu wachache tu kuzungumza na Waziri Mkuu, na kuongeza kuwa ‘Watanzania wamezoea kuja wengi japo walioalikwa wachache tu.’

Kwa upande mmoja ninaipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ‘kusoma alama za nyakati’ na kuruhusu mkutano kati ya Waziri Mkuu na Watanzania wanaoishi hapa kuwa wa wazi. Kwa upande mwingine ninaikosoa kwa sababu tamko lake kuwa mkutano huo utakuwa wa wazi sio tu lilitolewa Ijumaa - siku moja kabla ya mkutano – lakini pia haikubainisha muda wala sehemu kutapofanyika mkutano huo. Pengine ni mazoea tu ya huko nyumbani, lakini maisha ya hapa kwa kiasi kikubwa yanaambatana na ‘ratiba kali,’ na taarifa ya muda mfupi na isiyojitosheleza kimaelezo (kama hiyo ya Ofisi ya Waziri Mkuu) inaweza kuwa iliwanyima fursa watu wengi zaidi kuhudhuria mkutano huo.

Kwa upande wa Ubalozi wetu hapa, hadi wakati ninaandika makala hii haujafanya jitihada za kuwaomba radhi Watanzania wanaoishi hapa kwa ‘mpango wake fyongo’ ambao laiti ungefanikiwa, basi mkutano huo wa Waziri Mkuu ungekuwa ni kati yake na ‘wateule wachache’ tu. Kadhalika, ofisa ubalozi aliyejirekodi na kukebehi harakati zetu kudai fursa kwa wote kuhudhuria mkutano huo angeomba radhi kwa kauli zake zisizoendana na wadhifa wake wala ustaarabu wetu Kitanzania.

Pengine utata huo ungeweza kuepukika laiti pande mbili zinazohusika na ziara za viongozi wa kitaifa zingewajibika ipasavyo. Kwanza, ubalozi wetu hapa ungeweza kutengeneza mazingira mazuri ya mawasiliano na Watanzania wanaoishi hapa kwa kutumia mitandao ya kijamii au njia nyingine mwafaka. Hisia ni kwamba ‘ukimya’ uliojitokeza kuhusu ziara hiyo ulikuwa wa makusudi (yaani mkutano huo ulipaswa kuwa ‘shughuli ya wateule wachache’).

Pili, idara yetu ya masuala ya usalama imekuwa na utaratibu wa kutanguliza maafisa wake eneo ambalo kiongozi wa kitaifa atatembelea, kitu kinachofahamika kiintelijensia kama ‘advance party.’ Na moja ya majukumu ya waliomo kwenye ‘msafara’ huo ni kubaini yanayoweza kujitokeza wakati wa ziara husika. Kwa hiyo, laiti wangetupia macho ‘sehemu’ za maongezi ya Watanzania wanaoishi hapa (kwa mfano kundi lao la ‘Whatsapp’) basi wangeweza kubaini mapema kuwa kuna kiu ya mkutano na Waziri Mkuu sambamba na shutuma kuwa ubalozi unakandamiza kiu hiyo.

Nimalizie makala hii kwa kutoa wito kwa ofisi zetu za ubalozi popote zilipo ziwe kiunganishi kati ya Watanzania wanaoishi nchi hizo na nchi yetu, sio kwa masuala yanayohusu hati za kusafiria tu na masuala ya kidiplomasia bali kudumisha Utanzania wetu kwa upendo, umoja na mshikamano. Balozi zetu kadhaa zimekuwa zikilaumiwa kwa ‘kutokuwa na msaada,’ sambamba na kauli za jeuri/kiburi kwa baadhi ya maofisa wetu wa ubalozi, hali inayodhaniwa inatokana na baadhi yao kukaa huku nje muda mrefu mno kiasi cha ‘kuwadharau Watanzania wenzao.’

Mwisho, iwe ni kwa busara zake binafsi au ofisi yake, shukrani za pekee kwa Waziri Mkuu Majaliwa kuweza kuongea na Watanzania wanaoishi hapa Uingereza. Takriban kila aliyehudhuria mkutano huo ameridhishwa na hotuba ya Waziri Mkuu ambayo imetoa matumaini makubwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuiboresha Tanzania yetu katika kila eneo.

16 May 2016

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akihutubia Watanzania wanaoishi hapa Uingereza



Sehemu ya hotuba ya Waziri Mkuu Majaliwa


Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo na Waziri Mkuu Majaliwa



Sehemu ya hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje Balozi Mahiga

Waziri Mkuu Majaliwa na Balozi Mahiga 

Baadhi ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza wakiwa katika mkutano huo




Waziri Mkuu Majaliwa akiwa na Kaimu Balozi Mr Marwa (wa kwanza kushoto), Balozi Mahiga na Jaji Mkuu Chande (kulia)

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubua


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Valentino Mlowola akiongea kwenye mkutano huo


Jaji Mkuu Chande akiongea


Jaji Mkuu Chande akiongea. Kushoto kabisa ni Balozi Mahiga na kulia ni Kamanda Mlowola

Waziri Mkuu Majaliwa akihutubia


Meza kuu


Sehemu ya Watanzania waliohudhuria Mkutano huo uliofanyika kwenye ubalozi wa Tanzania jijini London hapo jumamosi Mei 14, 2016

14 May 2016


Jana nilibandika makala kuhusu manung'uniko ya Watanzania wengi wanaoishi hapa Uingereza ambao walikuwa hatarini kukosa fursa ya kuhudhuria mkutano na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye yupo nchini hapa kikazi.

'Kelele' hizo zimezaa matunda, na leo Waziri Mkuu Majaliwa atakutana na Watanzania wote wanaoishi nchini humu wanaoweza kumudu kufika ubalozini London saa kumi alasiri. Awali, maofisa husika katika ubalozi huo walialika kundi dogo tu la Watanzania kuhudhuria mkutano huo, hatua iliyotafsiriwa na wengi kama ubaguzi na pengine jitihada za kuficha majipu yanayoukabili ubalozi huo.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu imeandikwa kidiplomasia, ambapo kwa upande mmoja imejitoa lawama ya kuhusika na maandalizi ya mkutano huo (na hakuna aliyemlaumu Waziri Mkuu au Ofisi yake bali lawama zilielekezwa kwa ubalozi) .



Kwa upande mwingine ni kama imekanusha 'madai ya watu' kuwa kuna watu maalum waliochaguliwa kuhudhuria mkutano huo (badala ya kuwa mkutano wa wazi kwa kila Mtanzania anayeishi hapa). Nimesema ni "lugha ya kidiplomasia" kwa sababu uthibitisho kwamba awali mpango wa ubalozi ulikuwa ni kama ulivyolalamikiwa jana , yaani kundi la watu kadhaa tu ndio wakutane na Waziri Mkuu, na uthibitisho huo unasikika katika audio hii ya mmoja wa maofisa wa ubalozi wetu anayetukebehi kwa kudai haki ya kukutana na Waziri Mkuu. Msikilize kwa kubonyeza play


Ni wazi kuwa laiti afisa ubalozi huyo ndio angekuwa na mamlaka ya mwisho basi ni wazi angebaki na hao watu wachache ambao awali ndio waliteuliwa kuhudhuria mkutano huo kana kwamba ni wa siri.

Badala ya kukiri kwamba ubalozi ulifanya makosa kuteua watu wachache tu, afisa huyo anaelekea kutuona kituko kwa kudai haki ya msingi ya kukutana na viongozi wetu wa kitaifa. Na badala ya kutumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania ratiba ya mkutano huo (tetesi zinasema utafanyika ubalozni mida ya saa 10 jioni) yeye ameamua kutunanga. Madaraka huwafanya baadhi ya wenzetu kujisahau sana.

Tukiweka kando lugha ya kidiplomasia ya Ofisa ya Waziri Mkuu na kebehi za afisa ubalozi, la muhimu ni kwamba sasa Watanzania wote wanaoishi hapa Uingereza wamepewa fursa ya kuhudhuria mkutano huo muhimu na Waziri Mkuu. Binafsi nimefarijika sana kwa sababu nilijitahidi kulipigia kelele suala hilo kwenye kundi la Whatsapp la jumuiya ya Watanzania ambayo ipo katika hatua za awali za kuundwa, japo mapokeo hayakuwa ya kuridhisha (watu wanahimiza umoja lakini walikalia kimya 'ubaguzi' uliotaka kufanywa na baadhi ya maafisa ubalozi wetu hapo London). 

"Kelele" zangu hazikutokana na mie kutopewa mwaliko, kwa sababu hata kama ningekuwa miongoni mwa watu hao takriban 40 walioalikwa bado nisingehudhuria (na leo sintohudhuria...kwa sababu zangu binafsi). Nilipiga kelele kwa maslahi ya walio wengi ambao pengine kwa namna moja au nyingine walishindwa kupiga kelele hizo wao wenyewe. Sie wengine tuna kumbi kama hii ya blogu au makala magazetini ambazo ni rahisi kupiga kelele na watawala kutusikia. Lakini si kila mtu ni blogs au mwandishi wa makala. Ni matumaini yangu kuwa 'kelele' hizi zitawahamasisha wengi kutambua kuwa 'kelele dhidi ya jambo lisilofaa' sio uchizi, kusaka umaarufu au ukorofi. Marehemu Kighoma Ali Malima aliwahi kutuusia kwamba "HAKI HAIPASWI KUOMBWA KAMA ZAWADI. HAKI HUDAIWA...KWA NGUVU IKIBIDI."

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.