Showing posts with label MBOWE. Show all posts
Showing posts with label MBOWE. Show all posts

10 Jan 2018

Image result for magufuli lowassa
Jana Januari 9, 2018, wiki moja na siku mbili baada ya kuanza kwa mwaka huu mpya, duru za siasa za Tanzania zilitikiswa na habari kuhusu kiongozi maarufu wa Chadema, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kukutana na Rais John Magufuli kwa “mazungumzo”, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Baada ya “mazungumzo” hayo Lowassa alimmwagia pongezi Magufuli kwa kile alichokiita “kazi nzuri anayoifanya” na kutaja mafanikio katika sera ya elimu bila malipo, ujenzi wa mradi wa uzalishaji wa umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler’s Gorge), na ujenzi wa viwanda na ujenzi wa reli ya “standard gauge”.

Nimepata faraja sana kuja hapa Ikulu kuonana na Mheshimiwa Rais, tumezungumza nae na nimempongeza kwa kazi nzuri anayoifanya, lazima tukiri anafanya kazi nzuri na anahitaji kutiwa moyo,” alinukuliwa Lowassa aliyejiunga na Chadema miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 baada ya ndoto zake kuwania urais kwa tiketi ya CCM “kuota mbawa.”


Image result for magufuli lowassa

Mwanasiasa huyo ambaye baada ya kujiunga na Chadema alipitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya muungano wa vyama vinne vya upinzani – Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD – uliofahamika kama UKAWA, aliendelea kusema kuwa “Moja kubwa ambalo ni la msingi sana ni la kujenga ajira, katika kuanza ujenzi wa reli ya kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro hapo anajenga ajira, na kwenye nchi yoyote inayoendelea suala muhimu ni kujenga ajira, Stiegler’s Gorge ni kujenga ajira na mingine ya aina hiyo, lazima kuwepo na kipaumbele cha kusema kwamba tunajenga ajira. Jingine ni la elimu, ni muhimu sana, hauwezi kuacha elimu katika mambo yako unayofanya, hili nalo lazima lisemwe vya kutosha, kwa kweli nakushukuru Mheshimiwa Rais, you made my day.

Rais Magufuli kwa upande wake alimpongeza Lowassa kwa kile alichokiita “kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali” na kumtaja Lowassa kama mmoja wa viongozi ambaye kwa wakati wake alitoa mchango wake katika nchi.

Magufuli alimmwagia sifa Lowassa akidai kuwa “ni mwanasiasa mzuri kwani hata wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita ambao naye aligombea kiti cha Urais, hakuwahi kumtukana.”

Mheshimiwa Lowassa ameniomba mara nyingi nikutane nae, na leo nimekutana nae, tumezungumza mambo mengi, ameniambia ya kwake na mimi nimemwambia ya kwangu. Kwa ujumla Mheshimiwa Lowassa ni mwanasiasa mzuri na tuendelee kuwaenzi wazee hawa ambao kwa nyakati fulani walifanya mambo mazuri, na mimi napenda kumpongeza Mhe. Lowassa ambaye kama alivyosema hapa kuwa tumefanya mambo mazuri mengi,” alisema Rais Magufuli

Ametaja miradi mbalimbali tunayotekeleza, ametaja mradi wa Stiegler’s Gorge utakaogharimu zaidi ya Shilingi Trilioni 7, amezungumzia juu ya elimu bure, amezungumzia juu ya maji ambayo kwa bahati nzuri yeye alikuwa Waziri wa Maji na anafahamu sasa tumefikia wapi, amezungumza juu ya umeme tulivyosambaza katika vijiji mbalimbali, elimu bure, huduma za hospitali na mengine” aliongeza Rais Magufuli.

Kwanza, ni muhimu kutambua kuwa kama Mtanzania yeyote yule, Lowassa alikuwa na kila haki ya kukutana na Rais wake. Kadhalika, kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani, isingepaswa kuwa jambo la kushangaza kwa viongozi hao wawili kukutana.

Hata hivyo, Lowassa sio tu amekutana na Magufuli, bali pia ammemwamgia sifa. Je ni dhambi kwa kiongozi wa chama cha upinzani kumwagia sifa Rais aliyepo madarakani? Jibu lingepaswa kuwa “si dhambi,” laiti uhusiano kati ya Rais Magufuli, serikali yake na taasisi zake (kama vile jeshi la polisi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa), watendaji wa serikali (hasa mawaziri na manaibu wao, na wakuu wa mikoa na wilaya), pamoja na chama cha Magufuli yaani CCM, na chama anachotoka Lowassa, yaani Chadema, na Upinzani kwa ujumla, ungekuwa mzuri.

Lakini ukweli ni kwamba japo tangu kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, uhusiano kati ya CCM, serikali zake na taasisi zake, na vyama vya upinzani umekuwa “wa kusuasua,” hali katika miaka miwili tu ya utawala wa Magufuli imekuwa mbaya zaidi hususan kutokana na ukweli kwamba hakuna jitihada za kuficha chuki iliyopo dhidi ya Upinzani.

Kama kiongozi wa ngazi za juu kabisa wa Chadema, na pengine mwanasiasa anayeheshimiwa zaidi ya kiongozi mwingine yoyote ndani ya chama hicho, ni wazi Lowassa anafahamu vema msimamo na mtazamo wa chama chake kuhusu Magufuli na utendaji kazi wake, na serikali yake, na chama chake.

Pengine kwa kuweka picha sawia, inaelezwa kwamba hadi wakati huu, zaidi ya wana-Chadema 400 ikiwa ni pamoja na viongozi na wanachama, aidha wapo jela au wana kesi zinazoendelea mahakamani ambazo takriban zote ni matokeo ya chuki za kisiasa zinazofanywa na Magufuli, serikali yake na chama chake.

Kadhalika, katika utawala wa Magufuli, vyama vya upinzani ikiwemo Chadema ambayo Lowassa ni kiongozi wake wa kitaifa vimepigwa marufuku kufanya shughuli zao za kisiasa ikiwa ni pamoja na mikutano na maandamano. Hayo yanatokea wakati CCM ikiwa huru kufanya mikutano na maandamano itakavyo, mara nyingi ikitumia raslimali za umma.

Sambamba na jitihada za Magufuli kubana fursa ya siasa (political space), utawala wa kiongozi huyo umekuwa mstari wa mbele kuvibana vyombo vya habari na kudhibiti uhuru na haki ya wananchi kutoa mawazo yao kama Katiba inavyowaruhusu.

Lakini jingine ambalo Chadema ni mhanga mkubwa, kada maarufu wa chama hicho Ben Saanane “alipotea” Novemba mwaka jana na hadi leo hajapatikana.

Na ni wakati ninaandika makala hii nimebaini kuwa Lowassa hajawahi kuongelea suala la kada huyo (naomba nikosolewe kama nimekosea).
Kubwa zaidi linaloweza kuhalalisha hasira za Chadema kwa utawala wa Magufuli ni tukio la hivi karibuni ambapo Mbunge wake maarufu, ambaye pia alikuwa mpinzani maarufu dhidi ya Magufuli, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, kunusurika kuuawa baada ya shambulio la risasi kadhaa huko Dodoma. Kwa sasa Lissu yupo nchini Ubelgiji kwa matibabu, lakini japo Lowassa alimtembelea alipokuwa hospitalini Nairobi, Magufuli hakuwahi kutia mguu kumjulia hali mwanasiasa huyo ambaye pia ni mnadhimu mkuu wa upinzani bungeni na Rais wa Tanganyika Law Society (TLS).

Kwahiyo japo pongezi za Lowassa kwa Magufuli zinaweza kuwa na uzito, mapungufu ya utawala wa rais huyo wa awamu ya tano, hususan kuhusiana na chuki na uonevu dhidi ya vyama vya upinzani, hususan Chadema, yalipaswa “kumzuwia” kada huyo wa zamani wa CCM kumwaga pongezi hizo.

Kibaya zaidi, imebainika kuwa Lowassa alishawahi kumwomba Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amsaidie kukutana na Magufuli. Hata hivyo, Gambo alipotamka hilo hadharani, Lowassa “aliruka kimanga.”


Hata hivyo, jana Magufuli alitamka bayana kuwa Lowassa aliomba mara kadhaa kukutana naye. Kwahiyo, alichosema Gambo kilikuwa kweli, na Lowassa hakuwa mkweli alipokana kuwa hajaomba kukutana na Magufuli.

Tukio hilo la Lowassa kukutana na Magufuli na kumwagia pongezi limepokelewa kwa hisia tofauti. Wakati kuna kundi dogo la wana-Chadema waliopongeza hatua hiyo, kwa mfano “kada” mmoja wa chama hicho Yericko Nyerere, wengi ikiwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wamepingana waziwazi na Lowassa.

Wakati Yericko aliandika haya


Mbunge maarufu wa Chadema, Godbless Lema alikuwa wa kwanza kueleza bayana kutoafikiana na pongezi za Lowassa kwa Magufuli.


Baadaye, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, naye alieleza kuwa kauli za Lowassa ni zake binafsi na sio msimamo wa chama hicho.

Kadhalika, Mbowe alionekana kumkumbusha Lowassa kuhusu matukio mbalimbali yasiyopendeza katika utawala wa Magufuli

Lakini pengine aliyeeleza kwa kirefu kuhusu suala hilo ni Lissu, ambaye akiwa hospitalini huko Ubelgiji, alitoa waraka huu hapa chini.



Waheshimiwa habari za Tanzania na poleni kwa yote.
Naomba na mimi niseme kwa uchache kuhusu suala hili. Samahani kama 'uchache' wangu utakuwa mrefu kidogo.
Baada ya Mwenyekiti kuzungumzia jambo hili, inaelekea kuwa wazi kwamba Mheshimiwa Lowassa hakumshirikisha Mwenyekiti kabla ya kukubali au kuamua kwenda Ikulu kukutana na Rais Magufuli.
Na juzi tu wakubwa wetu hawa wawili walikuwa pamoja hospitalini kumsalimia Mzee Ngombale Mwiru.
Je, inawezekana Mheshimiwa Lowassa hakuwa anajua tayari kwamba ana appointment Ikulu?
Kama alikuwa anajua, kutokumshirikisha Mwenyekiti wake kuna tafsiri gani hasa?
Katika mazingira ya sasa ya Tanzania ya Magufuli, uamuzi wowote wa kufanya nae mazungumzo, hata kwa nia njema yoyote ile, bila kushauriana au kuwashirikisha viongozi wa juu wa chama, ni uamuzi usio sahihi na mgumu kukubalika.
Vile vile, kauli za aina ambayo tumeisikia leo kutoka kwa Mheshimiwa Lowassa, zina athari kubwa kisiasa.
Sio tu zinachanganya wanachama na wafuasi wetu, lakini pia zinawapa mtaji wa kisiasa maadui zetu.
Kuanzia sasa tutegemee sana kuwasikia maCCM yakishangilia 'busara' za Mheshimiwa Lowassa.
Masuala ya ukiukwaji haki za binadamu, uvunjwaji wa Katiba na mengine mengi sasa yatajibiwa kwa namna moja: Lowassa amemkubali Magufuli nyie wengine mnapiga kelele za nini.
Huu ni mtaji wa bure kwa Magufuli. Ukweli, ambao umesemwa sana humu, ni kwamba amefeli karibu katika kila jambo.
Hata hiyo reli anayosifiwa nayo na Lowassa bado ni ndoto tu: nani ajuaye itajengwa kwa hela za nani???
Za Wachina kama tulivyoambiwa mwanzoni; au za Waturuki kama tulivyoambiwa baadae; au za Afrika Kusini kama alivyosema mwenyewe anaenda kumwomba Zuma???
Kama chama hatujawahi kukataa mazungumzo na Rais au kiongozi mwingine yeyote wa serikali.
Na hatukatai kuzungumza na Magufuli kuhusu matatizo mengi na makubwa yanayoikabili nchi yetu.
Lakini ni muhimu na lazima viongozi wakuu wa chama washirikishane na washauriane kabla ya mazungumzo hayo.
Na baada ya mazungumzo, ni lazima viongozi wakubaliane juu ya kauli za kutoa hadharani kwa umma ili wote tuwe kwenye ukurasa mmoja.
Katika mazingira ya sasa, ambako viongozi na wanachama wetu wanashambuliwa hadharani kwa mapanga na hata kwa risasi, kumsifia Rais ni kumuunga mkono yeye na matendo yake.
Katika mazingira ya kesi nyingi za kutunga dhidi yetu, 'kazi nzuri' inayofanywa na Magufuli ina maana gani hasa, kama sio kuhalalisha ukandamizaji tunaofanyiwa.
Katika mazingira ambapo hata jumuiya ya kimataifa imeanza kuhoji mwenendo wa Rais Magufuli, kutoa kauli kwamba 'anafanya kazi nzuri' ni 'kumtupia taulo' la propaganda litakalomfichia madhambi mengi aliyowafanyia Watanzania katika miaka hii miwili.
Kwa vyovyote vile, kitendo cha Mheshimiwa Lowassa sio cha kunyamaziwa au kuhalalishwa kwa hoja nyepesi nyepesi.
TUNDU LISSU(MB).
Top of Form

Kadhalika, kada maarufu wa kike wa chama hicho, Hilda Newton nae alieleza masikitiko yake kutokana na kauli za Lowassa.



Kama alivyotahadharisha Lissu, ni wazi kwamba CCM watakuwa wamepewa “silaha” mpya katika “kumpamba” Magufuli na “kuwapenda” wapinzani, kwamba “hata Lowassa wenu anamkubali Magufuli.” Na ni rahisi kwa CCM kuonekana wana mantiki katika hoja hiyo, kwa kudai “kama mtu muhimu kabisa kwenye chama chenu (yaani Lowassa) ambaye ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Magufuli kwenye uchaguzi mkuu uliopita, anamkubali mkuu huyo wa nchi, ninyi ni akina nani kumpinga?”

Wakati ni wazi kwamba uamuzi wa Lowassa kukutana na Magufuli, na kumwagia pongezi, umezua “sintofahamu” huko Chadema, kuna masuala kadhaa ya muhimu yanayopaswa kuangaliwa kwa makini kwa ajili ya mustakabali wa chama hicho.

Kwanza, ni muhimu kwa viongozi na wanachama wa Chadema kutambua nafasi ya Lowassa katika chama hicho. Wakati baadhi ya wachambuzi wa siasa – mie nikiwa mmoja wao – wanaamini kuwa ujio wa Lowassa katika chama hicho ulikuwa na hasara zaidi kuliko faida, jitihada zilizofanywa na chama hicho kumpigania mwanasiasa huyo zimemjengea hadhi ambayo haipo kwa mwanasiasa mwingine yoyote ndani na nje ya chama hicho.

Ikumbukwe kuwa hadi wakati jina lake lilipokatwa na vikao vya CCM katika mchakato wa kusaka mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho tawala, Lowassa alikuwa ndiye mwanasiasa maarufu kuliko wote Tanzania. Yayumkinika kusema alikuwa mtu wa pili kwa umaarufu baada ya marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Licha ya kulazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008 kutokana na kashfa ya Richmond, Lowassa aliendelea kuwa mwanasiasa maarufu na mwenye nguvu kuliko yeyote yule ndani ya CCM, hata zaidi ya Rais na mwenyekiti wa taifa wa chama hicho wakati huo, Jakaya Kikwete.

Na japo kukatwa kwa jina la Lowassa huko CCM kulimpunguzia kidogo umaarufu wake kwa siasa za Tanzania – ilikuwa kama miujiza kuona CCM ilikuwa na ujasiri wa kukata jina la mwanasiasa huyo- alihamia Chadema akiwa na sapoti ya kutosha kiasi japo si kubwa kama ilivyotarajiwa.

Japo kuna “tuliopishana nae mlangoni” – kwa maana yeye alipoingia, sie tukatoka – ujio wake ulipelekea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi ya wote wa Upinzani. Na ndio maana haikuwa vigumu kwake kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA.

Nimeeleza kuwa baadhi yetu “tulipishana nae mlangoni” kwa sababu mie binafsi nilikuwa naiunga mkono Chadema, si kama mwanachama bali ukweli kwamba kwa muda mrefu nimekuwa nikijihusisha na harakati za mapambano dhidi ya ufisadi, na chama hicho kilijitokeza kuwa championi wa mapambano hayo. Kwahiyo, “naturally” nilijikuita nikikiunga mkono.

Hata hivyo, ujio wa Lowassa katika chama hicho ulinikimbiza. Sababu kuu ni binafsi zaidi, na nisingependa kuongelea hapa, lakini sababu nyingine ni kile nilichotafsiri kama usaliti wa Chadema. Ikumbukwe kuwa tangu mwaka 2006, chama hicho “kilimkalia kooni” Lowassa kumtuhumu kuwa ni fisadi, na ndicho kilichofanya jitihada kubwa zilizopelekea mwanasiasa huyo kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.

Sasa bila hata kutumia jitihada kidogo tu za busara, chama kilichomwandama Lowassa kuwa ni fisadi, kwa miaka 9 mfululizo, yaani 2006 hadi 2015, kilionekana kituko kwa baadhi yetu tuliokuwa tukikiamini, kwa sababu, pamoja na mengine, isingewezekana kutumia miezi mitatu (Julai 2015 Lowassa alipojiunga na chama hicho hadi Oktoba wakati wa uchaguzi mkuu) kumsafisha vya kutosha.

Na gharama ya ujio wa Lowassa ilikuwa kubwa. Moja kubwa zaidi ilikuwa lazima kwa Chadema “kuitosa” turufu yake muhimu, ajenda ya vita dhidi ya ufisadi. Ililazimika kufanya hivyo kwa sababu kuzungumzia ufisadi ilhali chama hicho kimemkumbatia mwanasiasa kiliyemwita “baba wa ufisadi” kwa miaka 9 mfululizo ingeonekana kioja.

Kadhalika, kwa kumpokea Lowassa, Chadema ilikuwa haina jinsi ya kukwepa tuhuma kutoka CCM kuwa chama hicho upinzani ni cha kifisadi kwa sababu ya kumkumbatia mwanasiasa ambaye kilikuwa kikimuita fisadi. Jitihada za Chadema kujibu mashambulizi kuwa “kama Lowassa ni fisadi mbona hajachukuliwa hatua,” zilikuwa hazina mashiko.

Lakini jingine lililoipa jeuri CCM ni ukweli kwamba kwa chama hicho, Lowassa alikuwa ni “makapi” sambamba na wanasiasa wengine waliomfuata huko Chadema. Hiyo ilikipa chama hicho tawala “jeuri” ya namna flani. Na waliitumia vema kwenye kampeni, kwamba “hawa jamaa si lolote si chochote. Yani wameshindwa hata kutafuta mgombea wao wenyewe mpaka wakasubiri makapi kutoka kwetu ndo wakapata mgombea urais.” Na pamoja na maneno hayo kuwa machungu, ndo ukweli ulivyokuwa.

Chadema na UKAWA kwa ujumla walikuwa na takriban mwaka mzima wa kujipanga; kuafikiana kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo, na kumnadi, huku wakitumia “advantage” ya “vita vya wenyewe kwa wenyewe” kati ya zaidi ya makada 40 waliokuwa wakichuana kuteuliwa na CCM.

Badala yake, kumbe tayari kulikuwa na makubaliano ya siri kati ya uongozi wa baadhi ya viongozi wa juu wa Chadema kwamba wasubiri kutangaza mgombea wao hadi baada ya mchakato wa CCM kupata mgombea wake, ka maana ya “kumhifadhia nafasi Lowassa endapo jina lake litakatwa huko CCM.”

Kabla ya kwenda mbali na makala hii ningependa nishauri Chadema irejee suala hilo la Lowassa kuandaliwa nafasi ya kuwania urais japo wakati huo alikuwa CCM. Hatua stahili zinapaswa kuchuliwa dhidi ya wote waliohusika na mpango huo.

Na ujio wa Lowassa ulipelekea Chadema kumpelekea mmoja wa magwiji wa siasa za upinzani, Dokta Willbrord Slaa. Umahiri wa Dokta Slaa haukuwa tu katika kuchukia ufisadi kwa dhati bali umahiri wake mkubwa katika kujenga hoja kisomi. Kadhalika, alikuwa akiaminiwa na watu mbalimbali muhimu ndani ya serikali, kiasi kwamba baadhi yao walihatarisha ajira zao kwa kumpatia mwanasiasa huyo nyaraka muhimu zilizoiwezesha Chadema kuwa na ushahidi mbalimbali katika vita yake dhidi ya ufisadi.

Na kuonyesha kuwa alikuwa na msimamo imara, Dokta Slaa aliamua kujiweka kando katika uongozi kupinga Lowassa kupewa ugombea urais wa UKAWA. Lakini jambo la kusikitisha mno, kiongozi huyo aliyekifanyia mengi chama hicho alidhalilishwa na kutukanwa kupita kiasi.
Na “akina sie” tulishindwa kustahimili ujio wa Lowassa, na kwa vile kwa baadhi yetu ilikuwa muhimu kumzuwia asiingie Ikulu, na hivyo kulazimika kumpigia kampeni mpinzani wake yaani Magufuli, tulitukanwa kila aina ya matusi. Sijui watu hawa waliojitoa ufahamu wataweka wapi sura zao pindi Lowassa “akirejea nyumbani” CCM.

Wakati anajiweka kando na uongozi wa Chadema, Dokta Slaa alikitahadharisha chama hicho kuwa ili kuleta mabadiliko ya kweli (badala ya hayo “ya kisanii” aliyokuwa akiyanadi Lowassa) chama hicho kinahitaji mkakati makini utakaoongozwa na watu makini. Na kwa hakika, tangu wakati huo, Chadema imekuwa kama kundi la wanaharakati wa kudandia hoja kuliko chama cha siasa chenye ajenda ya kueleweka. Uamuzi wa kuitelekeza ajenda ya vita dhidi ya ufisadi ulipelekea chama hicho kutokuwa na ajenda moja ya maana, huku CCM “wakipora” kiurahisi ajenda ya vita dhidi ya ufisadi.

Je mustakabali wa Chadema ukoje? Japo sio rahisi sana kubashiri kwa uhakika kuhusu hatma ya chama hicho, binafsi – kwa kutumia uzoefu wangu na uelewa wa kutosha wa siasa za Tanzania, sambamba na kuwa na fursa ya kufahamu “yanayojiri nyuma ya pazia” la siasa za nchi yetu – ninadhani kuwa kuna uwezekano mkubwa tu kwa Lowassa kurudi CCM kama sio kuachana kabisa na siasa.

Kwanini Lowassa anaweza kurudi CCM? Kuna sababu kuu mbili. Moja ni dalili za wazi kuwa ndoto zake za urais kupitia chama hicho ni kama zimeyeyuka. Umaarufu wake umegubikwa na kuibuka na kuimarika kwa umaarufu wa Lissu. Ni dhahiri kwamba ikipigwa kura ya maoni kuwa nani kati ya Lowassa na Lissu awe mgombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020, Lissu ataibuka mshindi. Na Lowassa anafahamu kuwa hakuna njia ya mkato kwa yeye “kulazimisha” awe mgombea katika uchaguzi mkuu huo ujao, licha ya ukweli kwamba alishatangaza kuwa atagombea.

Sababu nyingine ni binafsi zaidi. Lowassa ni mmoja wa matajiri wakubwa nchini Tanzania. Kama utajiri huo ulipatikana kihalali au kifisadi, si lengo la makala hii kujiingiza katika mjadala huo. Lililo wazi ni ukweli kwamba licha ya kuwa mwanasiasa, yeye pia ni mfanyabiashara. Na kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, serikali ya Magufuli imefanikiwa kutumia nyenzo yake muhimu dhidi ya wapinzani ambao pia ni wafanyabiashara, KODI.

Inaelezwa pia kwamba mali mbalimbali za mwanasiasa huyo zipo hatarini kutokana na uwepo wake huko Upinzani. Inadaiwa kuwa hata jengo la Tanesco Ubungo ambalo serikali imetangaza kulivunja, linamilikiwa na Lowassa, na tishio la kulivunja lilikuwa kama kufikisha ujumbe kwake.

Katika hili, Lowassa hatoonekana mtu wa ajabu akiamua kurudi CCM ili asibughudhiwe kuhusu biashara na mali zake. Ni nani kati yetu anayeweza kujitoa mhanga kwa ajili tu ya imani yake ya siasa? Si kama hawapo ila ni adimu mnooo! Na kibaya zaidi, hata akiamua kung’ang’ania huko Chadema, hatma yake na ya chama hicho haieleweki kwa sababu hadi muda huu – na hii ni licha ya zuwio la Magufuli dhidi ya vyama vya upinzani kufanya shughuli zao za siasa – chama hicho kikuu cha upinzani “kipo kipo” tu. Hakina ajenda moja ya kueleweka zaidi ya kudandia kila tukio linalojiri.

Iwapo Lowassa ataamua kubaki Chadema, hiyo itakuwa fursa mwafaka kwa chama hicho kumpumzisha. Naamini kuwa wana-Chadema wakiweka kando ushabiki wa kisiasa, wanafahamu fika kuwa mwanasiasa huyo hana nguvu, uwezo wala mvuto wa kukabiliana na siasa hatari zinazoendelea muda huu huko nyumbani.

Kwa upande mwingine, tukio la Lowassa kukutana na Magufuli Ikulu linaweza pia kuhusishwa na tamko la hivi karibuni la Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad, ambaye kama Lowassa, alimmwagia sifa Magufuli.

Nimefanya uchambuzi kuhusu kauli za wanasiasa hao wawili hapa, lakini ninachoweza kugusia hapa ni haja ya kutambua kuwa wanasiasa hao bado wanatunzwa na serikali kutokana na nyadhifa walizowahi kushika huko nyuma. Haihitaji uelewa mkubwa kuhusu "siasa za kibabe" kuhisi kwamba huenda "malezi" wanayopewa na serikali yametumika kama "chambo" cha kuwavuta karibu na Magufuli.

Kuhusu matatizo yanayoikabili Chadema muda huu,ukweli ni kwamba ni zaidi ya uwepo wa Lowassa ndani ya chama hicho. Japo huu ni ukweli mchungu usioruhusiwa kabisa kusikika ndani ya chama hicho, licha ya kazi nzuri ya kuifikisha Chadema ilipo leo, mwenyekiti wa taifa Mbowe anapaswa kutoa fursa kwa wana-Chadema wengine kusukuma gurudumu la chama hicho. Na hatua hiyo wala haihusiani na mchango wake mkubwa wa kumleta Lowassa ndani ya chama hicho na “kumpa” ugombea urais wa UKAWA.

Kirefu cha Chadema ni Chama cha DEMOKRASIA na Maendeleo. Sasa ni demokrasia gani hiyo ambayo inaruhusu mwenyekiti mmoja kuwa madarakani milele? What if “uenyekiti wa milele” ni miongoni mwa vikwazo kwa maendeleo ya chama hicho?

Lakini hata kama “muda wa Mbowe kutoka madarakani haujafika,” busara tu inapaswa kumfahamisha kiongozi huyo kuwa ni vema kuzingatia busara za akina Nyerere waliojing’atua wakiwa bado wanahitajika. Sipendi kubashiri hili, lakini laiti Mbowe asipohamasisha mageuzi kwenye medani ya uongozi wa chama hicho, haitokuwa jambo la ajabu akiishia kung’olewa kwa nguvu.

Na kwa bahati mbaya kwake, hili “songombingo” alilolianzisha Lowassa jana linaweza kuwa kama mnyororo mrefu ambao mahala flani yupo Mbowe. Ndiye aliyemkaribisha Lowassa.

Moja ya mapungufu makubwa mno yanayoitafuna Chadema muda huu ni pamoja na kulipuuza kundi muhimu linalokisaidia mno chama hicho, lundo la vijana wanaoshinda na kukesha katika mitandao ya kijamii wakijaribu kukinadi chama hicho angalau kwa kuikemea serikali ya Magufuli au CCM kwa ujumla.

Laiti chama hicho kingekuwa na ajenda ya kueleweka, basi jeshi hili la vijana lingekuwa nyenzo muhimu mno. Ni rahisi kuwalaumu vijana hawa kuwa “kazi yao kubwa ni kudandia hoja tu,” lakini ukweli ni kwamba chama chao hakiwapatii ajenda ya/za kueleweka. Kibaya zaidi, hata pale wanapojaribu kutengeneza ajenda wao wenyewe – kwa mfano jitihada za kumsaka Ben Saanane – hawapati sapoti ya kutosha kutoka uongozi wa juu wa chama hicho.

Ni hivi, wengi wa hawa vijana wanahatarisha maisha yao kwa kuwa tu “upande usiotakiwa” na serikali ya Magufuli. Hawategemei malipo yoyote zaidi ya kuamini kuwa siku moja wanaweza kukiingiza chama chao madarakani. Hakuna jitihada za makusudi za uongozi wa juu wa chama hicho kuwa karibu na kundi hili muhimu.

Ukiwa UVCCM una uhakika wa angalau “kuhongwa na Bashite” au kualikwa kwenye “mnuso” sehemu flani. Lakini ukiwa kijana wa upinzani, “zawadi” kubwa yaweza kuwa kusumbuliwa na vyombo vya dola na kuishi maisha ya wasiwasi. Kwahiyo vijana wa upinzani wana kila sababu ya kuichukia siasa, kwa sababu inahatarisha maisha yao, lakini mapenzi yao katika imani ya chama inawalazimisha kung’ang’ania hivyo hivyo.

Niionye Chadema kuwa katika zama hizi za “ununuzi wa binadamu kama zama za utumwa,” chama hicho kisishangae pindi wengi wa vijana hawa watakapoamua kubwaga manyanga na kukubali “kununuliwa.” Kwanini waendelee kuhatarisha maisha yao ilhali uongozi wa juu wa chama hicho hauna muda nao?

Akina Hilda Newton, Ben Malisa, Bob Wangwe, Ndehani Mwenda, Noel Shao, Gift Nanyaro ni miongoni mwa vijana wanaofanya kazi kubwa kwa ajili ya Chadema, bila ya matarajio ya malipo au fadhila flani, zaidi ya kuhatarisha maisha yao. Kama ilivyo kawaida ya mwanadamu yeyote yule, inaweza kufika mahala mtu akarudi nyuma na kujiuliza, “is it worth it?” Na japo sitarajii kuona makada hao vijana wakiamua kuipa kisogo Chadema, lakini sintoshangaa baadhi yao wakiamua kuipa kisogo siasa, hasa kama tasnia hiyo itaendelea kuwa “yenye manufaa kwa genge flani tu.”

Nihitimishe makala hii kwa kukuhamasisha msomaji kujipatia nakala yako ya kitabu changu kipya cha kielektroniki kinachochambua kwa kina miaka miwili ya utawala wa Magufuli. 




Baadhi ya niliyaoyazungumzia kwenye makala hii yamezungumwa kwa kirefu katika kitabu hicho ambacho hakielemei upande wowote. Kitabu hicho kwa sasa kinasubiri uzinduzi rasmi utakaokiwezesha kununulika kwa “mobile money” kama m-pesa, tigopesa,nk. Nitawataarifu. Ila kwa wasiohitaji kusubiri, waweza kukinunua HAPA

17 Jan 2014

KATIKA hitimisho la makala yangu iliyochapishwa wiki mbili zilizopita, iliyobeba kichwa cha habari ‘Ni mwaka wa siasa za hovyo CCM, CHADEMA, niliahidi kuendeleza utabiri wa mwaka huu 2014, kwa kuangalia anga za kimataifa.
Kwa bahati nzuri, siku nne tu baada ya kuchapishwa makala hiyo, moja ya mambo niliyotabiri - kuendelea kwa mgogoro wa CHADEMA na uwezekano wa migogoro ndani ya vyama vya upinzani kuwa ya hadharani - limetokea.
Ninaomba niweke bayana kuwa masikitiko yangu kuhusu maendeleo mapya katika mgogoro wa CHADEMA ni makubwa zaidi ya furaha yangu kuona nilichotabiri wiki iliyopita kweli kimetokea. Nitakuwa mbinafsi na mnafiki ‘kusherehekea usahihi wa utabiri wangu’ katika jambo lisilopendeza. Laiti ingekuwa ni chaguo langu basi ningetamani mabaya yote niliyotabiri yasitokee, lakini kwa bahati mbaya hali halisi haikwepeki.
Takriban wiki mbili zilizopita, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe alirusha ‘bomu zito’ ambapo alitoa tuhuma kubwa na hatari dhidi ya Mwenyekiti wake taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe, na chama hicho kwa ujumla. Pengine ili kuleta ladha halisi ya alichosema Zitto ni vema nikanuu ‘waraka’ mzima kama ifuatavyo:
"Lissu anasema nimepewa magari 2 na Mzee Mkono. Anasema kaambiwa na Mkono. Naamini Mkono alimwambia pia mwaka 2005 alimpa Freeman Aikaeli Mbowe tshs 40m ili Mbowe asifanye kampeni Musoma Vijijini.
“Nadhani alimwambia pia mwaka 2008 (baada ya orodha ya mafisadi kutangazwa 2007) Mkono alimpa Freeman tshs 20m za uchaguzi wa Tarime na Freeman akasema kwenye chama ametoa mkopo na akalipwa. Nadhani alimwambia pia kuwa mwaka 2010 Mkono alimpa Mbowe tshs 200m za kampeni ya Slaa.
“Pia hakusahau kumwambia kuwa Rostam Aziz alimpa Mbowe tshs 100m za kampeni. Lissu anajua kuwa gazeti la Tanzania Daima limeanzishwa na fedha za chama kutoka Conservative Party?
“Nimefanya internship yangu kwa Mkono and Company Advocates kuhusu masuala ya mikataba. Mzee Mkono ni Mzee wangu na alisaini petition ya kumtoa Waziri Mkuu Pinda. Lissu awaambie waliyemtuma wamwambie ukweli wote. Lissu ajue yeye ni kifaranga tu, Mimi namtaka mama wa kifaranga ajitokeze. Aeleze aliingia deal gani na Kinana na Sumaye mwaka 2005 kufuatia deni lake NSSF. Aweke wazi mkataba kati yake na NHC kuhusu nyumba ya umma ilipo Club Bilicanas.
“They must know I am not a push over. Chacha died, I won't. Mtu ambaye hawezi kuheshimu mke wake aliyemzalia watoto hawezi kunyooshea mtu kidole kuhusu maadili."
Zitto alibandika waraka huo katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook, lakini kwa sababu anazojua yeye pekee, baadaye aliuhariri na kutojumuisha tuhuma hizo. Aidha kwa kutofahamu au makusudi, uhariri uliofanywa na mwanasiasa huyo katika waraka huo haukuzuia kusambaa kwa kasi mtandaoni.
Niliposoma waraka huo nilipatwa na mshtuko mkubwa, nikabaki ninajiuliza iwapo Zitto alikuwa ‘mzima’ wakati anaandika alichoandika.  Japo inawezekana alifanya hivyo kwa kuzingatia kile kinachofahamika mtaani kama ‘umemwaga ugali na mie namwaga mboga...bora tukose wote,” ukweli ni kwamba bandiko hilo lina madhara makubwa, kwa Zitto binafsi na kwa pengine ustawi wa CHADEMA kwa ujumla.
Madhara kwa Zitto ni ya kisheria zaidi. Tayari Mbowe ameonyesha nia ya kumburuza Zitto mahakamani kuthibitisha tuhuma hizo nzito. Bila kujali kuwa tuhuma hizo zina ukweli au la, mtu yeyote mwenye uelewa wa ‘dili za siri’ atafahamu kuwa ni vigumu kuzithibitisha kisheria, yayumkinika kuhisi kuwa Zitto atakuwa na kazi ya ziada katika ‘kesi’ hiyo (iwapo itafunguliwa).
Iwe ni tuhuma za Nimrod Mkono kumpa Mbowe shilingi milioni 260 katika mazingira ambayo si tatanishi tu bali pia kwa namna fulani ni hujuma dhidi ya CHADEMA, au Rostam Aziz kumpatia Mbowe shilingi milioni 100, au ‘dili’ kati ya Mbowe na Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na Katibu Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana, sidhani kama Zitto anaweza kuthibitisha tuhuma hizo iwapo Mbowe atatimiza azma yake ya kufungua kesi. 
Je, inawezekana kuwa kwa kutambua ‘kosa hilo la kisheria’ ndio maana muda mfupi baadaye Zitto alihariri ‘post’ hiyo? Wakati jibu analo Zitto mwenyewe, ukweli unabaki kuwa tuhuma hizo ni nzito mno, na iwapo ni za kweli basi zinapoteza kabisa hadhi ya CHADEMA.
Ikumbukwe kuwa katika waraka uliopelekea Zitto kuvuliwa nyadhifa zake mbalimbali ndani ya CHADEMA, walioandika waraka huo waligusia walichokiita ‘udhaifu wa wanayemtaka’ (wakimaanisha Zitto), na kudai, “Maneno yake mara nyingine hayazingatii anayazungumza katika mazingira gani na hivyo kuwasha masikio ya wanataasisi jambo linalompunguzia kukubalika kwake taratibu.” 
Kadhalika, walieleza kuwa; “Kuna wakati tunayemtaka (Zitto) hujibu kwa taharuki kubwa dhidi ya mashambulizi yanayoelekezwa kwake jambo linalomfanya achukue maamuzi yasiyo sahihi kwa wakati huo. Kwa kifupi kuna wakati tunayemtaka (Zitto) huonekana kufanya maamuzi kwa hisia zaidi badala ya kutulia kwanza na kutafakari kwa kina ikiwa ni pamoja na kutafuta ushauri kwa wenzake kabla ya kujibu.”
Ndugu msomaji, huhitaji kuwa mwanasaikolojia kuhisi kuwa huenda kilichomsukuma Zitto kuandika ‘waraka’ huo kwenye ukurasa wake wa Facebook ni kile Waingereza wanakiita “putting emotions in front of common sense”, yaani kwa tafsiri isiyo rasmi, kuweka mbele jazba badala ya busara.
Kwa kujaribu kuonyesha kuwa Mbowe si mwadilifu (kwa maana ya kupokea misaada kutoka kwa ‘wanasiasa kama Mkono na Rostam waliowahi kutajwa na CHADEMA kuwa ni mafisadi’), linakuja swali la msingi, kwanini Zitto alikalia kimya tuhuma hizo nzito kwa takriban miaka minane hadi sasa baada ya kuvuliwa madaraka? Hivi kuna neno stahili kuelezea hali hiyo zaidi ya unafiki?
Tukiamini tuhuma hizo za Zitto, je naye si sehemu ya ‘uhuni wa CHADEMA’ wa kukemea mafisadi hadharani ilhali pembeni wanapokea misaada ya watu hao hao wanaowatuhumu? Ninasema hivyo kwa sababu Zitto hakuwa katibu wa shina bali Naibu Katibu Mkuu (taifa)  wa chama hicho, na mbunge, na kwa vyovyote vile naye ni mnufaika wa fedha hizo ‘za mafisadi.’
Laiti angekuwa haridhii vitendo hivyo basi aidha angejitoa mhanga na kuweka ukweli hadharani wakati huo (na hiyo ingeweza kuzuia kurejea kwa vitendo kama hivyo) au angeweza kujiuzulu kwa kuona ‘chama chake kinashirikiana na watuhumiwa wa ufisadi. Kwa nini hakufanya hivyo? Jibu jepesi ni hilo nililoandika hapo juu: alikuwa mnufaika wa vitendo hivyo (iwapo kweli vilitokea, maana tayari baadhi ya aliowataja wamekanusha ‘kumpa msaada’ Mbowe).
Binafsi, ninadhani moja ya matatizo yanayomkabili Zitto ni wanaojiita au kujitambulisha kama wafuasi wake. Wengi kati yao ni wenye mapenzi na CCM, na ushabiki wao kwa Zitto ni wa kirafiki (kimaslahi?) zaidi. Ndio, tofauti za kiitikadi hazimaanishi uadui, lakini wengi wetu tunaufahamu msemo ‘nionyeshe marafiki zako na nitakwambia wewe ni nani,’ yaani mara nyingi watu wanaotuzunguka hutoa picha fulani kuhusu sisi wenyewe.
Lakini tatizo jingine kuhusu ‘wafuasi na marafiki hao wa Zitto’ ni kutokuwa washauri wazuri kwake. Ukisoma mengi ya wanayoandika, hususan huko kwenye mitandao ya twitter, utabaini kuwa kimsingi wanachofanya ni ‘kumvimbisha kichwa Zitto’ bila kutoa ushauri unaoweza kusaidia ustawi wa kisiasa wa mwanasiasa huyo kijana.
Na mfano wa hivi karibuni ni baada ya Zitto kubandika waraka huo wenye tuhuma nzito huko Facebook. Wengi wa wafuasi wake walionekana kuchekelea ‘Mbowe alivyoumbuka’ bila kujali athari za kisheria kwa Zitto na ustawi wa CHADEMA kwa ujumla (kwanini wajali ilhali wengi wao ni wanaCCM)?
Kwa wafuasi wa Zitto, mwanasiasa huyo ni majeruhi wa siasa za chuki na mizengwe ndani ya CHADEMA. Lakini kwa wengine, Zitto anaonekana kama mtu anayeendeshwa na ‘ego’ kubwa inayomfanya kujiona yeye ndiye-au zaidi ya- CHADEMA.
Ni vigumu kubashiri hatma ya maisha ya kisiasa ya Zitto lakini kwa hali ilivyo ni vigumu mno kuona mustakabali wake ndani ya chama hicho. Ninakumbuka mwanasafu mmoja wa gazeti hili alimshauri mwanasiasa huyo hivi karibuni kuwa suluhisho la busara kwake kwa sasa ni kutosubiri kuvuliwa uanachama, ajiondoe mwenyewe huko CHADEMA, na kuitaka Mahakama isiingilie kazi ya chama.
Mwisho, bado ninaamini kuwa Zitto ni mwanasiasa mzuri lakini pengine kwa upungufu wa kibinadamu au makusudi, washauri wabovu au sababu nyinginezo, hazingatii umuhimu wa busara hizi tatu katika medani ya siasa: moja, waweke marafiki zako karibu lakini waweke maadui zako karibu zaidi, na pili, hakuna marafiki au maadui wa kudumu katika siasa, na tatu, hakuna mwanasiasa anayeweza kuwa mbadala wa chama (hasa katika mazingira ya siasa zetu ambapo kwa kiasi kikubwa chombo pekee cha uongozi wa kisiasa ni chama cha siasa. Bila chama, mwanasiasa hata awe maarufu kiasi gani anabaki kuwa raia wa kawaida tu).
Katika waraka wake, Zitto aliandika, “They must know I am not a push over. Chacha died, I won't” (lazima wafahamu mie sio mtu wa ‘kupelekeshwa.’ Chacha (Wangwe?) alikufa, mimi sitokufa). Hiki ni kiburi, utoto au? Ni mwanadamu mwenye uhakika wa kutokufa? Nihitimishe kwa kumshauri kwamba labda kweli ana uhakika wa kuishi milele lakini kwa kutanguliza hisia badala ya busara, yayumkinika kubashiri kuwa anaweza kuwa anajiua mwenyewe kisiasa (committing political suicide).



7 Jun 2012

Picha ya kwanza inamuonesha Mwenyekiti Freeman Mbowe akikata utepe wa kufungua Ofisi ya CHADEMA Kijiji cha Mkangaula. Ilikuwa ni baada ya Katibu Mkuu, Dkt. Slaa kutoa hotuba ya ufunguzi na John Mnyika kupandisha bendera ya chama nje ya ofisi hiyo, ikiwa ni ishara ya kupiga hatua katika mapambano ya awamu ya pili.

Picha zingine zinamuonesha Mnyika akitoa 'somo' kwa wanakijiji wa vijiji vya Kata ya Lumesule. Mapema kabla alikaribishwa na kuzungumza na Katibu wa Tawi wa CUF, Bi. Zaituni (pichani). Wananchi walimwelewa vyema. Kadi zikauzwa vizuri. Akaacha uongozi wa muda wa tawi lenye wanachama wa 34. Katika Kijiji hicho cha Lumesule, mwananchi mmoja kwa jina la Yasin Mohamed alihoji ilikuwaje CHADEMA wakaachia Dkt. Slaa ashindwe urais, wakati alichaguliwa kwa kura nyingi na wananchi na wao wanajua alishinda uchaguzi huo wa mwaka 2010.





Picha ZIFUATAZO zinamuonesha John Mnyika akiwa katika vijiji vya Kata za Makukwe na Mkwedu, wilayani Newala. Kwa George Mkuchika ambako alikutana na kiashiria cha wazi kuhusu udhaifu wa Waziri Mkuchika (Mbunge wa Newala) katika kusimamia majukumu yake, baada ya wananchi katika Kijiji cha Tengulengu, Kata ya Mkwedu kumlalamikia kuwa Diwani wa Kata hiyo, Juma Dadi hajawahi kufungua ofisi yake zaidi ya mwaka mmoja sasa. Pamoja na kuwasilisha malalamiko yao kwa barua Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Newala na kwa Mbunge wao, Mkuchika, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

Unaweza kuona pia wanawake walivyonogewa na PIPOOOOOOOOOOZ POWER, nao wakaipiga ya nguvu kweli kweli kuonesha umoja na mshikamano katika Falsafa ya Nguvu ya Umma ya CHADEMA, katika kudai uwajibikaji, kupigania haki, uhuru na mabadiliko ya kweli ya mfumo na utawala nchini.

Unaweza pia kumuona Kamanda Alfonsi Mawazo akiendelea kupata uzoefu wa mikikimikiki ya kujenga hoja katika uwanja wa mapambano. Si ofisini.








Picha zifuatazo zinamuonesha John Mnyika akiwa katika vijiji vya Kata za Makukwe na Mkwedu, wilayani Newala. Kwa George Mkuchika ambako alikutana na kiashiria cha wazi kuhusu udhaifu wa Waziri Mkuchika (Mbunge wa Newala) katika kusimamia majukumu yake, baada ya wananchi katika Kijiji cha Tengulengu, Kata ya Mkwedu kumlalamikia kuwa Diwani wa Kata hiyo, Juma Dadi hajawahi kufungua ofisi yake zaidi ya mwaka mmoja sasa. Pamoja na kuwasilisha malalamiko yao kwa barua Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Newala na kwa Mbunge wao, Mkuchika, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

Unaweza kuona pia wanawake walivyonogewa na PIPOOOOOOOOOOZ POWER, nao wakaipiga ya nguvu kweli kweli kuonesha umoja na mshikamano katika Falsafa ya Nguvu ya Umma ya CHADEMA, katika kudai uwajibikaji, kupigania haki, uhuru na mabadiliko ya kweli ya mfumo na utawala nchini.

Unaweza pia kumuona Kamanda Alfonsi Mawazo akiendelea kupata uzoefu wa mikikimikiki ya kujenga hoja katika uwanja wa mapambano. Si ofisini.




Pichani chini ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa Freeman Mbowe akihutubia Masasi




Chini,wananchi wakigombea kadi za Chadema




Picha chini,wananchi wakisikiliza hotuba kwa makini








Picha zote zimetumwa na mdau SAJJO

27 May 2012



Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Dk Wilbrod Slaa akiwahutubia wafuasi wa chama hicho leo katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam kwenye uzinduzi wa kampeni yao ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.




 Mwenyekiti wa Taifa Freeman Mbowe Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA  akiwahutubia wafuasi wa chama hicho leo katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam kwenye uzinduzi wa kampeni yao ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.


Mbunge wa Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Singida Magharibi Mheshimiwa Tundu Lissu akiwahutubia wafuasi wa chama hicho leo katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam kwenye uzinduzi wa kampeni yao ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.


 Mbunge Wa Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Ubungo Mheshimiwa John Mnyika akiwahutubia wafuasi wa chama hicho leo katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam kwenye uzinduzi wa kampeni yao ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.


Mbunge  wa Chama cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Mbeya Mjini Mheshimiwa Joseph Mbilinyi aka Mr II(SUGU) akiwahutubia wafuasi wa chama hicho leo katika viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam kwenye uzinduzi wa kampeni yao ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.


 Viongozi wa chadema wakifurahia kadi nyingi za CCM zilizorudishwa leo jioni kwenye mkutano
Deo Munish Katibu mkuu wa BAVICHA akiteta jambo na mmoja aliyehudhuria mkutano wa CHADEMA Wa uzinduzi wa kampeni ya VUA GAMBA VAA GWANDA ambayo itazunguka mikoa yote ya Tanzania.




  Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe akiwaaga wananchi waliokuwa wamefurika makao makuu ya chama kinondoni walikofika wakitokea jangwani usiku huu
 Mbowe akiwatania wanachama ofini kinondoni baada ya wananchi kuanza kudai chama kimfukuze John Shibuda.Alikuwa akijifanya hasikii wanachosema na hapa anajaribu kuwasikiliza zaidi.hata hivyo Mbowe aliwaondoa wasiwasi na kusisitiza kuwa chama kinao utaratibu wa kushughulika na viongozi wanaokiuka maadili ya chama na kuwaomba wawaamini kama viongozi kuwa wanaouwezo wa kulishughulikia jambo hilo na mengine
 Mh.Mbowe na Mnyika wakiwa wamesimama kwenye gari wakati wa matembezi wakitoka kwenye mkutano
Aliyekua Mbunge wa Arusha Mjini(CHADEMA)Mheshimiwa Godbless Lema akiwa juu ya gari huku akishangiliwa na vijana jioni baada ya mkutano
 Sehemu ya umati uliowasindikiza viongozi wa chadema toka jangwani hadi kinondoni.wamesambaa yapata saa 2 usiku.

PICHA ZOTE NA MAELEZOKWA HISANI YA BLOGU YA MHESHIMIWA HAKI NGOWI

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.