Showing posts with label MAJIRA. Show all posts
Showing posts with label MAJIRA. Show all posts

29 Mar 2009

(Picha kwa hisani ya KENNEDY)

Gazeti la Majira limepotea mtandaoni kwa muda mrefu sasa,na kwa akina sie tunaotegemea habari za nyumbani kupitia nakala za kielektroniki za magazeti husika mkombozi wetu mkuu amebaki Mr Kennedy.Na ni kwa kupitia tovuti yake ndipo nilikutana na version isiyopendeza ya habari kuhusu ajali iliyomhusisha Mzee wa Vijisenti,Andrew Chenge,na kupelekea vifo vya akinadada wawili.

Gazeti la Majira lilidai kuwa marehemu hao ni "machangudoa waliokuwa wanatokea Maisha Club".Sijui vyanzo (sources) vyao vya habari husika ni vipi lakini mwandishi yeyote mwenye busara angepaswa kujiridhisha kuhusu identity halisi ya marehemu hasa kwa vile tunazungumzia watu waliopoteza maisha.Hivi mwandishi huyo atajisikiaje iwapo baada ya uchunguzi itagundulika kuwa marehemu hao hawakuwa machangudoa?In fact,magazeti kadhaa yameripoti maelezo ya ndugu za marehemu yanayoeleza kwamba mmoja wao alikuwa mfanyabishara na mwingine mfanyakazi wa hoteli jijini Mwanza.

Pengine haikuwa nia ya mwandishi kuwa-describe marehemu hao kama changudoa (labda kutokana na haraka ya kuwahisha habari kwa mhariri) lakini taswira ya haraka iliyopatikana kutoka katika habari hiyo ni ujenzi wa matabaka:kigogo (mzee wa vijisenti) kagonga fukara (changudoa).By the way,hata hata kama hao mabinti wangekuwa machangudoa as suggested by the Majira reporter bado haiondoi haki yao ya kuwa hai muda huu!

Kingine ambacho hakihusiani na uandishi japo kinahusu tukio hilo la kusikitisha ni namna Jeshi la Polisi linavyoonekana "kubabaika" katika kushughulikia ajali hiyo.Kwa mujibu wa vyombo vya habari,Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam,Suleiman Kova,ameunda TUME MAALUM ya kuchunguza ajali hiyo eti kwa "kuzingatia uzito wa tukio hilo".Chenge ni Mtanzania kama mie na wewe,na kama amehusika na ajali basi sheria za uslama barabarani zifanye kazi yake.Sijui ni madereva wangapi walalahoi wanaopata "bahati" kama ya Chenge ya kuundiwa tume!

Kamanda Kova anadai kuwa tume hiyo imeundwa ili "kusiwepo mwanya wowote ,taratibu zote zitafuatwa bila kujali nani na wala nafasi aliyonayo....na kuleta uwazi na utawala bora" (kwa mujibu wa gazeti la Majira) na pia amenukuliwa na gazeti la Mwananchi akisema kuwa "hapa bwana hakuna mchezo wala hakuna kuangalia vyeo wala nani ni nani...".Hivi matamshi kama hayo (iwapo kesi itapelekwa mahakamini) hayawezi kutumiwa na wakili wa Chenge kudai "ameonewa kwa vile Kamanda Kova alishadai hawataangalia vyeo-which directly points to Chenge ambaye licha ya kuwa ex-minister,pia ni munge na kigogo wa CCM?"

Kama nilivyoandika jana,tuendelee kuwapa polisi benefit of doubt kwa matarajio kwamba wanafahamu bayana kuwa tukio hilo linaangaliwa na Watanzania wengi kama kipimo cha haki sawa kwa wote (huku wakiwa na kumbukumbu ya kesi ya marehemu Ditto).

23 Sept 2008



Mgomo wa NMB nchi nzima-Mishahara kuchelewa

Na Waandishi Wetu 

ZAIDI ya wafanyakazi 5,000 nchini wanaochukua mishahara yao kupitia Benki ya National Microfinance Bank (NMB) watalazimika kutolipwa wiki hii kutokana na mgomo wa nchi nzima wa wafanyakazi wa benki hiyo ulioanza jana. 

Wafanyakazi hao waligoma wakiishinikiza Serikali kuwalipa mafao na kupewa asilimia tano ya hisa zilizotengwa kwa ajili yao wakati Serikali ilipoamua kuuza hisa zake. 

Mgomo huo umekuja baada ya Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (TUICO), kutoa notisi ya saa 48, Septemba 19 mwaka huu ikieleza kusudio la kugoma. 

Akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam jana kuhusu mgomo huo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo, Bw. Ben Christiaanse, alisema hatua iliyochukuliwa na wafanyakazi hao katika matawi 121 nchini, ni kubwa kuliko tatizo lililopo. 

Aliulaumu uongozi wa TUICO kwa kile alichodai mbali ya kusababisha matatizo mengine, umekiuka amri ya mahakama kwa kuwa suala la wafanyakazi hao bado lilikuwa linashughulikiwa na kusisitiza, kwamba mgomo huo umesababisha matatizo makubwa kwa mamilioni ya Watanzania. 

Akizungumza kwenye mkutano huo, Mwanasheria wa NMB, Bw. Rosan Mbwambo, alisema jana asubuhi benki hiyo iliwasilisha ombi rasmi mahakamani la kukiukwa amri hiyo iliyotolewa Januari 21 mwaka huu na kutaka wahusika kuchukuliwa hatua za kijinai. 

Alisema baada ya kuwasilisha ombi hilo, mahakama hiyo iliagiza pande mbili, Benki na Chama cha Wafanyakazi, kufika mahakamani leo asubuhi. 

Aliwataja viongozi wa TUICO wanaotakiwa mahakamani leo kuwa ni Katibu Mkuu wa TUICO, Bw. Boniface Nkakatisi, naibu wake Alquine Senga, Mwenyekiti wa NMB TUICO Tawi na Kamati ya Majadiliano, Bw. Joseph Misana na Katibu wa Tawi la NMB, Bw. Abdallah Kinenekejo. 

Kutoka Tanga, Benedict Kaguo anaripoti kuwa wateja wa Benki ya NMB waliulalamikia uongozi wa benki hiyo kwa kushindwa kusikiliza madai ya watumishi wao hadi kusababisha mgomo mkubwa ulioleta adha kubwa. 

Wakizungumza kwa jazba nje ya ofisi za benki hiyo tawi la Madaraka jana baada ya kukuta tangazo lililowaomba radhi wateja kuwa hakutakuwa na huduma, wateja hao walidai jambo hilo limetokana na kupuuzwa hoja za wafanyakazi hao. 

Walieleza kutofurahishwa na kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo, Bw. Christiaanse kung’ang’ania kuwa mgomo huo ni batili bila kueleza chochote ama ni hatua gani amechukua kutekeleza madai ya wafanyakazi wake. 

“Sisi tunamshangaa huyu Mkurugenzi wa NMB, anaacha kueleza ni nini atawafanyia wafanyakazi hawa ili wasigome, yeye anang’ang’ania kuwa mgomo ni batili haya ni mambo ya ajabu sana,” alisema Mwalimu Deo Temba. 

Alieleza kuwa NMB ni benki kongwe nchini, hivyo kitendo cha kutowajali watumishi wake kinaifedhesha benki hiyo ndani ya jamii. 

Kutoka Shinyanga, Suleiman Abeid anaripoti kuwa mgomo ulichukua sura mpya baada ya wafanyakazi benki hiyo kutishia kuwashawishi na kuwaomba wafanyakazi wa sekta nyingine nao wagome kuishinikiza Serikali ikubali kutekeleza madai yao. 

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini humo jana, wafanyakazi hao wakiongozwa na viongozi wao wa chama chao, ngazi ya tawi na mkoa, walisema watafanya chini juu kuwaomba wafanyakazi wenzao wawaunge mkono, ili Serikali ishughulikie haraka madai yao. 

“Iwapo madai yetu hayatapatiwa ufumbuzi mapema, sisi tutaendelea na mgomo wetu na ni wazi wafanyakazi wenzetu hawataweza kulipwa mishahara yao na hata baadhi ya wafanyabiashara watapata shida, tutawaomba nao wagome katika maeneo yao,” alieleza Bw. Emmanuel Samara Katibu TUCTA mkoani hapa. 

Naye Katibu wa TUICO Shinyanga, Bw. Gabriel Melchior, alisema wafanyakazi wa NMB hawajagoma bali wanaendeleza mgomo ulioanzishwa na Serikali na mwajiri wao. 

Naye Francis Godwin kutoka Iringa anaripoti kuwa mgomo wa wafanyakazi NMB ulikabiliwa na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) baada ya kutanda benki hiyo huku wateja wakiwa wamepanga foleni tangu asubuhi wakisubiri kuchukua fedha zao katika ATM. 

Kutokana mgomo huo baadhi ya wananchi walimtaka Waziri wa Fedha na Uchumi, Bw. Mustafa Mkulo, kuchukua hatua ya kujiuzulu haraka kwa kushindwa kumudu nafasi hiyo. 

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia wateja hao wengi wao wakiwa ni walimu na watumishi wa Serikali wakisubiri milango ya benki hiyo ifunguliwe, kutokana na kutokuwapo tangazo lolote lililoonesha kuwapo mgomo katika benki hizo. Matangazo hayo yalibandikwa saa 5 asubuhi. 

Kutoka Mwanza Jovin Mihambi anaripoti kuwa wafanyakazi katika matawi mawili ya NMB jijini humo walisema wataendelea na mgomo licha ya Menejimenti na Serikali kupuuza mwito wa kuwataka kukutana nao kutatua matatizo yao. 

Wakizungumza na Majira katika ukumbi wa DVN maeneo ya Posta jijini hapa, walisema awali walikubaliana na uongozi wa benki hiyo kupitia kwa Meneja wake, Bw. Methusela Israel, kuwa wangekutana kujua hatma ya nyongeza ya mishahara yao ambayo walisema kuwa ni asilimia tano. 

Katibu wa TUICO Mkoa wa Mwanza, Bw. Renatus Chimola, ambaye aliungana na wafanyakazi wa benki hiyo, alisema kama menejimenti na viongozi wa Serikali hawatatokea katika kikao hicho, mgomo huo utaendelea hadi leo mpaka uongozi huo utakapokutana nao na kujadili matakwa yao. 

Alisema wananchi ambao ni wateja katika matawi hayo watapata usumbufu, yeye na wafanyakazi hao, hawatajali usumbufu huo kwa madai kuwa wanachodai ni maslahi yao ambayo yatawawezesha kutenda kazi yao kwa ufanisi zaidi kama benki zingine nchini

SOURCE:Majira


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.