5 Apr 2014

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.


KATIKA  taifa la ‘nani-anajali?’ (a who-cares nation) ajali zimeanza kuzoeleka kama mgao wa umeme,” ni ujumbe nilioandika juzi katika mtandao fulani wa kijamii baada ya kusoma habari kwamba matukio mawili ya ajali yamegharimu maisha ya Watanzania wenzetu 33.
Ujumbe huo ulibeba mambo mawili ya msingi. Kwanza, ni kasumba inayozidi kushamiri miongoni mwa Watanzania ya kupuuzia masuala ya muhimu kwao binafsi na kwa taifa lao. Mifano ni mingi lakini hapa nitabainisha michache.
Kama kuna vitu viwili vinavyonikera mno katika mitandao ya kijamii ni malalamiko yasiyoisha ya watumia huduma mbalimbali huko nyumbani. Maeneo mawili yanayozalisha walalamikaji wengi ni mgao wa umeme na huduma duni za baadhi ya kampuni za simu za mkononi.
Katika tatizo la mgao wa umeme, wengi wa walalamikaji hutumia lugha kali na hata matusi dhidi ya Tanesco, kana kwamba kwa kufanya hivyo shirika hilo la umeme litaona aibu na kuacha tabia inayoelekea kuwa ya kudumu sasa ya kukata umeme mara kwa mara, wakati mwingine mara kadhaa ndani ya siku moja.
Huwa najiuliza, hivi kitu pekee wananchi hawa wanachoweza kufanya ni kuitukana tu Tanesco? Lakini pengine kundi linaloweza pia kubebeshwa lawama licha ya wananchi hao ‘walalamishi’ ni wanasheria na wanaharakati wa haki za watumia huduma (consumer rights).
Kundi hili linajumuisha watu wanaojua sheria zinazomlinda mlaji (consumer), na laiti wangeguswa na tabia hii ya Tanesco basi ni dhahiri wangeweza kufungua kesi zinazofahamika kisheria kama class action. Kesi za aina hii ambazo ni maarufu zaidi nchini Marekani hufunguliwa na kundi kubwa la watu wanaowakilishwa na mwanasheria mmoja au kundi la wanasheria, dhidi ya mtu au taasisi.
Kwa mfano, mwaka 2008 wateja kadhaa wa kampuni moja ya huduma za mawasiliano nchini Marekani, AT&T, walifungua kesi dhidi ya Shirika la Ushushushu la nchi hiyo (NSA) wakilituhumu kwa vitendo vya kunasa mawasiliano na kufuatiliaji nyendo zao (surveillance).
Japo walalamikaji katika kesi hiyo walishindwa mahakamani, lakini mfano huo umelenga kuonyesha jinsi watumia huduma huko kwa wenzetu wanavyosaka haki zao. Japo mimi si mtaalamu wa sheria, je hakuna uwezekano wa kufungua kesi kama ya aina hiyo (class action) dhidi ya wahusika wote wa mgao wa umeme?
Kwa wanaolalamika kuhusu huduma zisizoridhisha za baadhi ya makampuni ya simu (hivi kuna hata moja isiyolalamikiwa?), wala haihitaji class action bali uamuzi tu kwamba “ninaachana nanyi kwa sababu mnaniona kama mteja nisiye na thamani kwenu.”
Hiyo ikizua kitu kinachojulikana kama domino effect (yaani kama goroli zikiwa kwenye mstari, ukiipiga moja inaisukuma nyingine, na nyingine, na kadhalika) hatimaye kampuni husika itabaini kwamba uhai wake upo hatarini laiti isipojirekebisha.
Kichekesho ni kwamba ‘domino effect’ iliyopo huko nyumbani miongoni mwa wateja wasioridhishwa na huduma za baadhi ya makampuni ya simu ni mtu mmoja kuitukana kampuni husika, na mwingine kufanya hivyo, na kadhalika.  Na wasichotaka kujifunza kwa watangulizi wao ni ukweli kwamba hasira hayajawahi kuleta ufumbuzi wa tatizo lolote mahali popote pale.
Lakini kama nilivyoeleza mwanzoni mwa makala hii, mada ya wiki hii ni kuhusu kukithiri kwa ajali na mwamko mdogo miongoni mwa Watanzania kukabiliana na janga hilo ambalo kwa kiasi kikubwa linazuilika. Ndiyo, wanasema ‘ajali haina kinga’ lakini pindi ukiruhusu basi la abiria ambalo si tu linatumia injini ya ‘kibajaji’ lakini injini hiyo pia imechakachuliwa, ni wazi pindi basi hilo likipata ajali hatuwezi kudai kwamba ‘ajali haina kinga.’
Huo ni mfano wa kufikirika tu lakini ukweli unaochukiza ni kwamba asilimia kubwa ya vyombo vya usafiri wa abiria havipaswi japo kubeba majani ya kulisha mifugo au hata takataka. Sasa kwanini vyombo hivyo vya usafiri vinaruhusiwa kuwa barabarani?
Majibu mawili makuu ni aidha vinamilikiwa na vigogo ambao askari wa usalama barabarani hawawezi kuomba rushwa au kama mmiliki ni ‘mtu wa kawaida’ basi ni halali kwa askari kudai rushwa na kisha kuviruhusu viendelee na safari.
Wanasema ‘rushwa ni adui wa haki’ lakini kisichosemwa sana ni kwamba rushwa ni janga hatari kama ukimwi au ugaidi, vyote vyaweza kugharimu maisha ya watu wasio na hatia.
Na hata pale chombo cha usafiri kinapokuwa imara (kwa maana kinaweza kumudu kusafirisha abiria bila matatizo), tatizo jingine ni madereva. Katika mazingira ya kawaida tu, mtu akikesha baa kisha akaamka na mabaki ya pombe ya jana kichwani, anaweza kuwa na wakati mgumu kutembea kwa miguu achilia mbali kumudu kuendesha usafiri mwepesi kama pikipiki au hata baiskeli. Sasa dereva wa basi la abiria anaporuhusiwa kuendelea na safari huku ana ‘faida kichwani’ ni wazi kwamba hatma ya safari hiyo ni kama bahati nasibu.
Kwa nini madereva wasiostahili kuwao barabarani (maana hata mwendesha guta au bajaji akiwa na uwezo wa kuhonga trafiki ataruhusiwa kuendesha basi la abiria, hata kama hana leseni wala ujuzi stahili) wanaruhusiwa? Jibu ni lilelile: aidha chombo cha usafiri anachoendesha ni cha kigogo hivyo trafiki hawawezi kumdai rushwa au dereva anamudu kuwapatia trafiki haki yao ya rushwa.
Lakini kwa upande mwingine ni abiria wenyewe kutolipatia kipaumbele suala la usalama barabarani. Ni jambo la kawaida kusikia abiria wakipiga mayowe kwenye basi pindi dereva wa basi, kwa mfano, anapolikosakosa gari jingine barabarani, lakini hakuna ‘nguvu ya umma’ (kwa maana ya abiria kwa umoja wao ndani ya basi hilo) itakayotumika kumdhibiti dereva huyu. Na si kwamba abiria hao wanasafirishwa bure kiasi cha kuhofia kuwa “tukimbana dereva aendeshe kwa umakini atatushusha njiani.”
Kilichoniuma zaidi baada ya kusoma habari hiyo kuhusu wenzetu 33 waliopoteza maisha kutokana na ajali ni jinsi habari yenyewe ilivyoonekana ya kawaida miongoni mwa Watanzania wengi. Hata kwenye vyombo vya habari, magazeti mengi yalitawaliwa na habari kuhusu vituko vinavyoendelea kwenye Bunge Maalumu la Katiba huko Dodoma badala ya kulipa uzito janga hilo la kitaifa.
Katika salamu zake za rambirambi kwa wahanga wa moja ya ajali hiyo, Rais Jakaya Kikwete alieleza kwamba “vifo hivyo si vya lazima” na “ameshtushwa na kusikitishwa.” Lakini je inatosha tu kushtushwa na kusikitishwa ilhali, Mungu aepushie mbali, tuendelee kutarajia ajali zaidi hadi hapo hatua madhubuti zitakapochukuliwa ikiwa pamoja na kulifanya tatizo la ajali ‘zinazoepukika’ kuwa janga la kitaifa?
Lakini wakati Rais Kikwete anastahili pongezi kwa angalau kutoa salamu hizo za rambirambi, Watanzania wengine ukiachilia mbali wahanga wa ajali hizo, walifanya nini? Pitia pitia yangu kwenye mitandao ya jamii ilionyesha kuwa janga hilo lilikamata hisia za watu wachache sana ukilinganisha na, kwa mfano, klabu ya Liverpool ya hapa Uingereza kufanikiwa kushikilia usukani wa Ligi Kuu, au kimuhemuhe cha mpambano wa Ligi ya Mabingwa wa soka wa Ulaya kati ya Manchester United ya hapa na Bayern Munich ya Ujerumani  jana.
Inasikitisha kuona Tanzania yetu inazidi kuwa taifa la ‘who cares?’ (nani ajali?). Na kwa kiasi kikubwa tatizo hili linaanzia kulekule kwenye kutokujali haki au stahili zetu binafsi. Ni wazi kuwa familia isiyojali inaweza ‘kuzaa’ ukoo usiojali, na hatimaye uwezekano wa kabila lisilojali, na hadi kufikia hapa tulipo: taifa lisilojali.
INAWEZEKANA, TIMIZA WAJIBU WAKO

2 Apr 2014

 
 
Habari Njema kwa wadauzii wangu na pia wateja kwa ujumla, tunayo furaha kuwaambia tumehama sehemu tuliyokuwa awali, na kwa sasa tupo Msasani road opp NMB Branch, hii yote ni kukushukuru weye unaye tu support katika shughuli zetu ndio maana tumefika hapa tulipo 

Kwahio kuanzia leo 2nd April 2014 hatutakuwepo tena Sinza, tunapatikana Msasani road opp NMB Bank, na duka linafunguliwa rasmi jumamosi hii, tupo katika marekebisho ya hapa na pale, nawashukuru sana tena sana wadau wa hii blog kwa kunitangaza hukooo, 

wadau wangu wa mikoani pamoja na hapa kitovu cha Nchi Dsm city, kama unakwama sehemu kindly call me  0652 112071 ila ni kwa kibiashara tuuuu, umbea na story za hapa na pale mwiko we busy making money.......

mzigo mpya umewasili na kipindi cha toba kinaisha njoo uanze ku shop na swagga tamu za harusi, accesories, shoes nk 

Ukifika NMB kwa upande wako mwingine wa barabara, utaona bango kubwa limeandikwa Sintah's Wedding Lounge ndipo tulipo

mwambie na rafiki mwambie na yule 

Mungu ni Mwema sana 

1 Apr 2014

Rais Kikwete akihutubia mamia ya Watanzania wanaoishi hapa Uingereza
Baada ya sokomoko lilodumu kwa siku kadhaa sasa kuhusu mchakato wa kupata Katiba mpya, hatimaye Rais Jakaya Kikwete ametangza kulivunja Bunge hilo akibainisha kwamba ni vigumu kwa mazingira yaliyopo kufikiwa mwafaka wowote ule, sambamba na dhamira ya kuokoa fedha za umma.

Rais aliyasema hayo alipoongea na Watanzania wanaoishi hapa Uingereza, ambapo yupo kwa ziara ya kidola ya siku tatu. Kwa maelezo kamili bofya HAPA

31 Mar 2014

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.


28 Mar 2014

 
 “HIVI ujumbe aliotoa Rais Jakaya Kikwete alipohutubia Bunge la Katiba Ijumaa ulikuwa wa Rais? Mwenyekiti wa CCM? Mtanganyika au Mtanzania wa kawaida?”,  niliuliza swali hili katika mtandao mmoja wa kijamii baada ya kuchanganywa na hotuba hiyo.
Lakini siku chache baadaye, Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Ikulu, Salva Rweyemamu, ‘alijibu’ swali hilo kwa namna fulani. Akizungumza na moja ya magazeti ya huko nyumbani, Salva aliushutumu Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kwa kile alichoeleza kuwa ni kuendeleza propaganda, na kubainisha kuwa “Rais kama Mtanzania ana haki ya kutoa maoni yake.
Wakati ninakubaliana na maelezo hayo, sote tunafahamu kuwa shughuli iliyompeleka Rais Kikwete katika Bunge hilo la Katiba ni kulizindua, si kutoa maoni yake. Ninaamini kwamba kama ilivyokuwa kwa Watanzania wengine, Rais alikwishakupewa nafasi ya kutoa maoni yake huko nyuma, na hakukuwa na haja ya kutumia tukio hilo la uzinduzi wa Bunge la Katiba ‘kutoa tena’ maoni yake.
Kwa upande mwingine, binafsi sikushangazwa na msimamo wa Rais Kikwete hususan kwenye hoja ya muundo wa Muungano. Kwa wenye kumbukumbu nzuri watakumbuka kwamba wakati wa maadhimisho ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Mbeya, Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho tawala aliweka bayana msimamo wa CCM kuwa ni muundo wa Muungano wa serikali mbili.
Sasa kwanini ilitarajiwa kwamba angebadili msimamo siku ya uzinduzi wa Bunge Maalumu la Katiba?  Ni muhimu pia kukumbuka kwamba wazo lenyewe la mabadiliko ya Katiba halikuanzia CCM (angalau kipindi hiki, na tukiweka kando harakati za ndani ya CCM kama zile za kundi la G55) bali kwa vyama vya upinzani hususan, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Kuna baadhi ya wachambuzi wanaokwenda mbali zaidi na kubainisha kuwa hata huko kwa wapinzani kulikoanzia wazo hilo la Katiba mpya, msukumo ulikuwa zaidi katika mazingira ya chaguzi, hususan Uchaguzi Mkuu, baada ya kuonekana bayana kwamba Katiba iliyopo inatengeneza mazingira magumu ya ushindani halisi wa kisiasa (au kwa lugha nyingine, ni vigumu mno kukiondoa chama tawala madarakani katika mazingira ya Katiba iliyopo).
Mara kadhaa huko nyuma nimebainisha msimamo wangu kuhusu suala la Katiba mpya. Japo ninaafiki kwamba Katiba tuliyonayo ina mapungufu ya kutosha na kuna umuhimu mkubwa wa kuibadilisha, ninapata shida sana kuona jinsi kuja kwa Katiba mpya kutakavyoweza kumsaidia Mtanzania wa kawaida anayeandamwa na umasikini unaochangiwa kwa kiasi kikubwa na ufisadi.
Tatizo jingine linaloninyima shauku ya kuona Katiba mpya inapatikana ni ukweli mchungu kwamba kwa kiasi kikubwa tatizo linaloikabili nchi yetu si ukosefu wa sheria bali usimamizi na utekelezaji wake. Hivi tumewahi kujiuliza kwamba kama sheria zilizomo kwenye Katiba iliyopo (na ni muhimu kutambua kuwa Katiba ni ‘sheria mama’) hazisimamiwi ipasavyo na kupuuzwa mara kadhaa, kuna mwamana (guarantee) gani kwamba sheria zitakazokuwemo katika Katiba mpya zitaheshimiwa?
Kati ya sababu za msingi zinazochangia kero za Muungano ni hiyohiyo ya kupuuza sheria. Wakati Rais Kikwete anahubiri faida za Muungano wa serikali mbili, alishindwa kabisa kukemea uvunjifu wa sheria (Katiba) ulioruhusu Zanzibar kujipa hadhi ya nchi ndani ya nchi. Kwa makusudi, mjadala kuhusu muundo wa Muungano unakwepa kujadili Marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 2010 ambayo hayakuingizwa kwenye Katiba ya Muungano.
Uvunjifu huo wa Katiba kwa maana ya kuruhusu kuundwa kwa nchi yenye Rais wake, bendera yake, wimbo wake wa Taifa, Katiba yake, nk (Zanzibar) ndani ya nchi nyingine (Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania) ulifanyika wakati wa utawala wa Rais huyuhuyu tuliyenae sasa (Jakaya Kikwete), na si yeye wala washauri wake, kwa mfano ‘wakereketwa wa Muungano kama Mzee Kingunge Ngombale Mwiru, waliodiriki kukemea jambo hilo.
Japo binafsi sipingi wala siungi mkono muundo wa Muungano wa serikali mbili au tatu (au hata wa serikali moja) kwa sababu kwangu cha muhimu ni function (kazi) na sio form (muundo), kinachofanyika sasa kwa kung’ang’ania muundo wa serikali mbili uliogubikwa na matatizo yanayoweza kuepukika ni kuahirisha tu tatizo. Ni wazi tatizo hilo litarejea kwani busara zinaeleza kwamba haiwezekani kuua wazo ‘lililoiva’ (you can’t kill an idea whose time has come).
Hatuwezi kutatua tatizo kwa kuficha tatizo jingine. Katika mazingira ya kawaida tu, ilipaswa mjadala kuhusu muundo wa Muungano uambatane na kuwekwa wazi kwa nyaraka zilizounda Muungano huo (Articles of the Union) ambazo zimeendelea kufanywa siri kubwa.
Hata kwa sisi tusiohangaishwa sana na muundo wa Muungano tunadhani kwamba pengine chanzo kikubwa cha ‘kelele zisizoisha’ kuhusu Muungano ni ukweli kwamba waasisi wa Muungano huo, Mwalimu Julius Nyerere na  Sheikh Abeid Karume, walifikia mwafaka wa kuunganisha nchi hizo kana kwamba yalikuwa makubaliano ya watu binafsi na si ya wananchi wote wa nchi hizo mbili. Sina hakika ni Watanganyika na Wazanzibari wangapi waliopewa fursa ya kuafiki au kupinga suala hilo la Muungano.
Na kama alivyofanya Rais Kikwete katika hotuba yake ya uzinduzi wa Bunge Maalumu la Katiba, uhai wa Muungano umeendelea kutegemea zaidi kuogopana, hadaa na vitisho (hususan ile ya takriban kila Rais kudai hayupo tayari Muungano uvunjike mikononi mwake).
Muungano katika muundo wake wa serikali mbili unaweza tu kusalimika iwapo matatizo yanayoukabili yatajadiliwa kwa uwazi pasi kuchelea matokeo ya kufanya hivyo. Iwapo kuujadili Muungano kwa uwazi kutasababisha uvunjike-alimradi kwa amani-basi na iwe hivyo. Iwapo kuujadili kwa uwazi kutauimarisha (na hii ndio njia mwafaka) basi tusipoteze muda na tufanye hivyo sasa.
Ni kichekesho kwa chama tawala CCM chini ya Mwenyekiti wake Rais Kikwete, kujaribu kuuhadaa umma kuhusu utatuzi wa matatizo ya Muungano ilhali kimsingi kinachofanyika ni ‘kuvuta muda’ (buying time) pasipo jitihada zozote za makusudi kufanyika kuimarisha Muungano huo.
Kama tunataka tuwe na Muungano wenye maana halisi ya muungano basi ni muhimu kwa kila raia wa nchi hizi mbili ajisikie huru awapo upande wowote wa Muungano. Vilio vya Watanzania Bara kwamba wanapokuwa Zanzibar wanajiona kama ‘raia wa kigeni’ visipuuzwe, kwa sababu ni vitu kama hivi vinavyoweza kuzua ‘muundo wa lazima’ wa Muungano pasi kujali vitisho vya watawala.
Nihitimishe makala hii kwa kukumbushia kwamba muundo wa Muungano ni kimoja tu kati ya vipengele vingi vilivyomo kwenye Rasimu ya Katiba mpya. Ni muhimu pia kutambua kuwa matatizo ya msingi yanayoikabili nchi yetu- kwa mfano umasikini wa kupindukia na ufisadi unaoshamiri kwa kasi- hayatokani na muundo wa Muungano wa serikali mbili na pengine hata muundo wa Muungano wa serikali tatu hauwezi kuyatatua.
Wakati Watanzania wakitafakari na kujadili hotuba ya Rais Kikwete, baadhi ya magazeti mwanzoni mwa wiki hii yaliripoti taarifa za kigogo mmoja wa Ikulu kufanya jitihada ya kumtoa rumande mmoja wa wafanyabiashara watuhumiwa wakubwa wa madawa ya kulevya anayeshikiliwa na polisi huko Lindi. Je muundo wa Muungano unashughulikia vipi uhuni wa aina hii?
Masuala kama utawala bora, haki za makundi ‘ya wanyonge’ (vulnerable groups), haki za huduma muhimu kama afya, elimu, nishati, na habari yana umuhimu mkubwa pengine zaidi ya aina ya Muungano tunaotaka.
Ndiyo maana nimeeleza hapo juu kwamba la muhimu zaidi kwangu ni function(s) na si form(s) za serikali kama taasisi inayoongoza nchi.
Kuwa na serikali mbili, au serikali tatu, au serikali moja kuna faida tu kwa mwananchi kama kunamwezesha kujipatia mahitaji yake muhimu kwa haki na kumfanya ajione ‘mdau halisi’ wa nchi husika. Vinginevyo, badala ya serikali 2, 3 au 1, kwa mwananchi huyo asiye na uhakika wa mlo wake ujao na ambaye ustawi wake unatarajia kudra za Mwenyezi Mungu, anachoona ni kama kuna serikali 0.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.