18 Oct 2012


KWA mara nyingine, wiki iliyopita Tanzania imeshuhudia ‘sura mbaya’ (ugly face) ya imani ya kidini. Kwa mujibu wa taarifa zenyewe, kilichoanza kama mchezo wa watoto kilisababisha vurugu kubwa zilizopelekea makanisa zaidi ya matano kuchomwa moto, sambamba na uharibifu wa mali kadhaa.
Inaelezwa kwamba chanzo cha vurugu hizo ni kitendo cha mtoto mmoja kuikojolea Kuran Tukufu baada ya ‘mabishano ya kitoto’ na mtoto mwenzie. Habari zinasema mtoto aliyefanya kitendo hicho alitaka kuthibitisha ukweli wa ‘tishio’ alilopewa na mtoto mwenzie kuwa iwapo atakikojolea Kitabu hicho Kitukufu, basi atageuka nyoka!
Sote tuliwahi kuwa watoto katika hatua za mwanzo za maisha yetu, na kwa kutumia uzoefu huo kama ‘watoto wa zamani’ tunaweza kukumbuka vitu vya ajabu, vya kukera, vya kuchekesha, na vya kila aina ambavyo twaweza kuvihitimisha kwa msemo huu wa Waingereza: ‘kids will always be kids’ (watoto wataendelea kuwa watoto).
Kwamba binadamu, pasipo kujali umri wake, anaweza kukojolea Kitabu Kitukufu cha dini fulani, ni jambo lisilopendeza hata kidogo. Na kwa hakika, kitendo cha aina hiyo, kitamchukiza kila muumini wa dini husika. Lakini kama ilivyo katika maeneo mengine ya maisha ambapo umri unaangaliwa kama kigezo muhimu cha kuhukumu tendo, ukweli kwamba aliyekojolea Kuran Tukufu ni mtoto wa miaka 14, ulipaswa kupewa uzito na baadhi ya waumini wa dini ya Kiislam ambao waliamua kuchukua sheria mkononi kwa kufanya vurugu kubwa ikiwa ni pamoja na kuchoma moto makanisa.
Licha ya kuguswa na tukio hilo la kusikitisha kama Mtanzania na Mkristo, lakini pia nimeguswa kwa vile linahusiana na eneo ambalo nimekuwa nikihangaika nalo kitaaluma kitambo sasa. Miaka michache iliyopita, nilikuja huko nyumbani kukusanya data kwa ajili ya utafiti wa kitaaluma kuhusu harakati za vikundi vya Kiislam nchini Tanzania. Kwa sababu zilizo nje ya uwezo wangu, utafiti huo bado haujakamilika japo katika hatua niliyofikia unaweza kutoa majibu fulani kuhusu kinachoendelea huko nyumbani hivi sasa.
Nilipata fursa ya kuzungumza na makundi makuu mawili ya waumini wa dini ya Kiislam. Wale tunaoweza kuwaita ‘wenye msimamo mkali’ na wale wa ‘wenye msimamo wa kawaida.’ Naomba nisisitize kuwa matumizi ya maneno ‘msimamo mkali’ na ‘kawaida’ ni kwa minajili ya mjadala tu. Ninatoa tahadhari hii mapema kwa kuchelea uwezekano wa shutuma kuwa ninawagawa Waislam katika makundi, ambayo kama ilivyothibitika katika utafiti wangu, wengi wao hawapendi mgawanyo wa aina hiyo kwani wanaamini wote ni Waislam.
Moja ya mambo yaliyojitokeza katika mahojiano yangu na ‘makundi’ yote mawili ni manung’uniko (grievances) ambayo yamedumu kwa muda mrefu. Manung’uniko hayo yameshamiri zaidi kwenye suala la usawa katika elimu na ajira. Wahojiwa wengi walionyesha kuwa na hisia ya kubaguliwa kati yao na Wakristo katika upatikanaji wa fursa za elimu na ajira. Kimsingi, ukimnyima mtu fursa ya elimu, unatengeneza mazingira ‘mazuri’ ya kumkwaza kupata ajira.
Takwimu mbalimbali nilizokusanya katika utafiti huo, zinaweza kusapoti madai hayo. Lakini la muhimu zaidi hapa si sapoti ya takwimu hizo, bali mazingira yaliyopelekea uwepo wa hali hiyo. Kutokana na ufinyu wa nafasi ninalazimika kutoa maelezo ya jumla kwani kupitia kipengele kimoja hadi kingine kunahitaji zaidi ya makala moja.
Kwa kifupi, moja ya sababu zilizopelekea ‘ubaguzi’ katika upatikanaji wa fursa za elimu na ajira kati ya Waislamu na wasio Waislam (hususan Wakristo) ni mfumo wa utawala wa kikoloni. Kama tunavyofahamu, wakoloni walikuwa Wakristo, na tunafundishwa kwenye somo la historia kuwa miongoni mwa ‘watangulizi wa ukoloni’ walikuwa wamisionari wa Kikristo.
Moja ya mbinu zilizotumiwa na wamisionari kutengeneza mazingira mazuri ya kutawala jamii za Kiafrika ni ‘kusilimisha,’ japo neno hilo lina maana zaidi kwenye Uislam. Ninalitumia hapa kwa maana ya kuwatoa watu kutoka katika imani yao ya awali na kuwaingiza katika imani mpya.
Lakini historia inatufundisha kuwa Uislam ulifika huko nyumbani karne kadhaa kabla ya Ukristo. Kwa bahati mbaya au makusudi, walioleta Uislam walikuwa wafanyabiashara kutoka Arabuni na Mashariki ya Mbali, na hawakuwekea mkazo sana kusambaza dini yao.
Yayumkinika kuhitimisha kwamba kushindwa kwa watangulizi hao wa Uislam kueneza dini hiyo miaka kadhaa kabla ya ujio wa Wamisionari na hatimaye wakoloni, kulichangia kurahisisha kusambaa kwa Ukristo kwa ama ‘kusilimisha’ Wapagani (ninatumia neno hili kumaanisha dini za asili za Kiafrika) na Waislam.
Tukifupisha historia, mkoloni alitumia Ukristo kama moja ya njia za kuzitawala jamii zetu. Ni katika mazingira hayo, stadi mbalimbali zinaonyesha kuwa kwa namna fulani baadhi ya Wakristo walichelea kuunga mkono mapambano dhidi ya mkoloni kudai uhuru wetu hasa kwa vile wakoloni walifanikiwa kwa kiasi fulani kuulinganisha ukoloni na Ukristo (yaani kumpinga mkoloni ni sawa na kumpinga Yesu/Mungu).
Kwa kutumia Ukristo kama njia ya kurahisisha utawala wao, wakoloni pia walitumia dini hiyo kama chombo cha kuwatenganisha watawaliwa. Kimsingi, kuna aina ya mwafaka wa kitaaluma kuwa si kwamba wakoloni waliwathamini sana Wakristo wa Kiafrika, bali waliwaona kama nguzo muhimu katika kuigawa jamii, na hivyo kuwarahisishia kiutawala jamii husika.
Ingawa kuna wamisionari waliokuja Afrika kwa minajili ya kidini halisi, wengi wao waliendelea kushirikiana na utawala wa kikoloni katika maeneo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na utoaji elimu. ‘Ushirika’ huu wa wamisionari na wakoloni katika utoaji elimu, unaweza kuelezewa kama mwanzo wa ujenzi wa tabaka la Wakristo wenye elimu na ‘wasio Wakristo’ (hususan Waislam) wasio na elimu.
Kadhalika, baadhi ya Waislam walichelea kujiunga na taasisi za elimu za wamisionari/wakoloni kwa kuhofia kuingizwa katika dini hiyo (Ukristo). Tukiweka hali ilivyokuwa kabla ya uhuru, mazingira yaliyojitokeza baada ya kuondoka mkoloni, yameendelea kwa kiasi fulani kurutubisha ‘ubaguzi’ huo wa elimu na ajira.
Baada ya kupata uhuru, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alikiri hadharani kuwa kuna umuhimu wa kurekebisha hali ya kutokuwapo usawa wa kielimu kati ya Wakristo na Waislam. Licha ya jitihada zake kubwa, hadi anaondoka madarakani ‘usawa’ huo haukuweza kufikiwa kwa kiwango cha kuridhisha.
Kuna maelezo mengine hapa. Shule za seminari za Wakristo ambazo kimsingi ni maalum kwa ajili ya ‘kuzalisha’ viongozi wa makanisa, zilikuwa ‘zikizalisha’ kundi la wasomi wa Kikristo ambao kwa sababu moja au nyingine, hawakuishia kuwa viongozi wa kanisa, bali wakachukua ajira serikalini au kwenye taasisi nyingine. Kwa upande mwingine, shule za kidini za Waislam ziliegemea zaidi kwenye utoaji elimu ya kidini, na katika mazingira hayo, tofauti na ilivyo kwa seminari, ‘hazikuzalisha’ wasomi wa kutosha kuingia kwenye ajira serikalini (naomba nieleweke kwa makini hapa).
Kwamba utawala wa Mwalimu Nyerere uliwapendelea Wakristo na kuwabagua Waislam, ni jambo ambalo halijathibitika kitaaluma. Hoja hiyo ni miongoni mwa masuala yanayojenga manung’uniko kwa baadhi ya Waislam. Kwamba baadhi ya Wakristo, hususan waliotoka seminari na kujiunga na ajira serikalini, waliwabagua Waislam na kuwapendelea Wakristo, ni jambo ambalo halijathibitika kitaaluma ingawa linawezekana kinadharia na kimantiki.
Kimsingi, tatizo si ubaguzi wa msomi/mwajiri Mkristo dhidi ya mwanafunzi/msaka ajira Muislam, bali mfumo ambao ulijengeka wakati wa ukoloni na umeendelea kuwepo. Unatoa nafasi (on merit) kwa Wakristo zaidi ya Waislam. Kama mwajiri anataka kujaza nafasi kwenye ofisi yake, anapaswa kuangalia, pamoja na mambo mengine, sifa za kitaaluma za waomba kazi. Sasa kwa vile mfumo wa elimu tuliorithi kwa mkoloni, na kama nilivyobainisha hapo juu, unatengeneza wasomi wengi wa Kikristo kuliko wa Kiislam, ni dhahiri kutarajia ‘ubaguzi’ wa nafasi za ajira.
Majuzi tumefanya sensa. Watawala wetu wamegoma kujumuisha kipengele cha dini kwa madai mbalimbali. Lakini kwa kufanya hivyo, watawala wanajinyima fursa ya kuelewa, kwa mfano uwiano wa ajira kati ya Wakristo na Waislam. Na cha muhimu hapo si kuelewa tu, bali pia kutafuta namna ya kurekebisha hali hiyo. Na hili ni tatizo la msingi linalofanya ‘tatizo la dini’ kuendelea kuwapo. Kuna hisia kwamba kwa kujaribu kulizungumzia suala hili kwa uwazi, kutazua tafrani kubwa kuliko mwafaka. Lakini sote tunajua kuwa ugonjwa hautibiki kwa kujidanganya kuwa haupo mwilini!
Je; kilichotokea Mbagala ni hasira tu za baadhi ya Waislam waliochukizwa na kitendo cha ‘mtoto wa Kikristo’ kukojolea Kuran Tukufu? Binafsi, naamini kuna sababu za ndani zaidi ya ‘hasira’ hizo na zinazosababisha ‘hasira’ hizo. Je; udini ni tatizo kubwa katika Tanzania yetu ingawa halizingumzwi vya kutosha? Binafsi, ninaamini jibu la swali ilo, ni ndiyo. Kama ni ndiyo, kwanini tunalikwepa tatizo hili?
Jibu linaweza kupatikana kwenye tatizo jingine ‘lisilozungumzika’ la kero za Muungano wa ‘Tanganyika’ na Zanzibar. Kwa kifupi, hadi sasa hakuna utashi wa kisiasa na kijamii kulikabili tatizo hili. Kwenye Muungano, kila Rais anachelea kuvunjikiwa na Muungano, ambao Baba wa Taifa ‘alishatoa radhi’ kwa atakayeuvunja. Kwenye hili la udini, viongozi wetu wanakwepa kulikabili kwa kuchelea kuonekana wadini. Kibaya, baadhi yao walitumia udini kwenye kampeni za uchaguzi mkuu uliopita. Je; yawezekana udini ni turufu muhimu kwa baadhi ya wanasiasa mufilisi?
Makala hii itaendelea wiki ijayo.




12 Oct 2012


MIONGONI mwa faida ninazopata kutokana na uandishi wa makala katika jarida hili maridhawa, ni mawasiliano ya kila wiki na baadhi ya Watanzania wenzangu. Wengi wa ninaowasiliana nao, ni wasomaji ambao kwa namna moja au nyingine huwa wameguswa na mada ninazoongelea. Kuguswa huko hufuatiwa na ama pongezi au kukosolewa. Wakati mara nyingi pongezi huandamana na maneno ambayo si tu yananipa moyo na ujasiri zaidi wa kuendelea na uandishi wa makala hizi, mara nyingi kukosolewa huambatana na maneno yasiyopendeza kuyasoma au kuyasikia popote pale.
Baadhi ya wanaopongeza safu hii hudiriki kwenda mbali zaidi na kushauri labda nifikirie kuingia kwenye siasa. Mara zote jibu langu huwa lile lile. Najisikia fahari kuwatumikia Watanzania wenzangu kupitia uandishi wa makala, huku nikiamini kuwa si lazima kuwa mwanasiasa ili uweze kutekeleza jukumu hilo ipasavyo.
Lakini kwa upande mwingine, baadhi ya wanaonikosoa huenda mbali zaidi na kunituhumu kuwa uandishi wangu umeelemea kwenye chuki binafsi, husda na vitu kama hivyo. Jamaa mmoja alifikia hatua ya kudai kuwa makala zangu ni sehemu tu ya mikakati wa dini yangu dhidi ya utawala unaoongozwa na mtu anayetoka dini tofauti na yangu.
Kama ambavyo ninaridhishwa na pongezi kuhusu safu hii, huwa ninajifunza jambo moja au jingine kutoka kwa wakosoaji wangu (wengi wao hupenda kuhifadhi majina yao halisi). Kukosolewa huko, kunanisaidia kwa kiasi fulani, na hasa tukizingatia ukweli kwamba ukiona unamwagiwa sifa tu pasipo kuelezwa japo kasoro kidogo, basi yayumkinika kuhisi kuwa kuna mushkeli mahala fulani.
Nimelazimika kuandika hayo kutokana na ukweli kwamba makala yangu katika toleo lililopita ambayo pamoja na mambo mengine ilimzungumzia mbunge wa Kigoma Kaskazini kupitia CHADEMA, Zitto Zuberi Kabwe, imetafsiriwa na baadhi ya wasomaji wangu kama sehemu ya kampeni zangu za kumkwamisha kuingia ‘Ikulu.’
Nimeshaeleza mara kadhaa katika baadhi ya makala zangu zilizopita kuwa mimi si mwanachama wa chama chochote kile cha siasa, na nimekuwa hivyo kwa miaka kadhaa, tangu nikiwa huko nyumbani. Wakati, kwa kiasi kikubwa nilipokuwa huko nyumbani sheria ilikuwa inanikataza kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa, kwa sasa uamuzi wangu wa kuwa neutral unachangiwa zaidi na imani yangu kuwa itikadi bora zaidi kwa mwananchi ni uzalendo na kuitumikia jamii kwa hali na mali.
Moja ya sifa kuu za sheria, ni kwamba iwe mbaya au nzuri, inabaki kuwa sheria hadi itakaporekebishwa au kuondolewa. Kuna nyakati tunalazimika kufuata sheria zinazokinzana na haki zetu (kimsingi sheria inapaswa kuendana na uwiano kati ya haki na wajibu), lakini tunalazimika kuzifuata kwa vile ndizo sheria zinazotawala.
Ni kwa mantiki hiyo, ninarejea tena kutofautiana na Zitto katika dhamira yake ya kutaka kuwa Rais wa Tanzania, kwa sababu kwa mujibu wa sheria tulizonazo, hatokuwa na sifa ya urais hapo mwaka 2015 kutokana na kuwa na umri pungufu ya ule unaotajwa kwenye sheria mama ya nchi, yaani Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninaafikiana na Zitto kwamba sheria hii ni ya kionevu kwa sababu kama inawezekana kwa mtu wa miaka 40 kuwa Rais kwanini ishindikane kwa mtu mwenye miaka 39?
Hata hivyo, napenda kumfahamisha kuwa hadi hapo sheria hiyo itakaporekebishwa au kubadilishwa, pamoja na ‘ubaguzi’ inaoubeba, itaendelea kuwa sheria inayopaswa kufuatwa. Na kwa vile kwa mazingira ya kawaida tu inatarajiwa Rais kuwa miongoni mwa vinara wa si tu kufuata sheria, bali pia kuzilinda, itakuwa ni ‘utani mbaya’ kwa mtu anayetaka kuwa Rais kudhamiria kuvunja sheria kama hiyo inayokataza walio chini ya miaka 40 kugombea urais.
Nimesema ninamuunga mkono Zitto kwamba sheria hiyo ni ya kibaguzi. Lakini kama tunachukia ubaguzi kwenye sheria, basi pia tunapaswa kuchukia ubaguzi kwenye kila eneo, iwe kwenye jinsia, imani, asili, rangi na hata kundi la mtu katika jamii. Siku chache zilizopita, kulikuwa na taarifa za kwamba Zitto aliongea na kituo kimoja cha redio jijini Dar es Salaam na kutamka maneno yafuatayo:
“Wazee wetu walitusaidia sana kutupatia maendeleo ya kisiasa, sasa ni jukumu letu kuleta maendeleo ya kiuchumi. Ila naomba nisisitize kuwa jukumu hilo haliwezi kutekelezwa na mtu yeyote aliyezaliwa kabla ya uhuru, na ninatangaza nitagombea urais mwaka 2015.”
Binafsi, ninahitimisha kuwa kauli hiyo ni ya ubaguzi wa mchana kweupe. Lakini pia, licha ya ubaguzi, inaonekana kichekesho kwani imetoka kwa mwanasiasa (Zitto) ambaye hajawahi kuficha hisia zake dhidi ya ubaguzi wa watu kwa vigezo vya umri. Tukiweka kando taratibu za ndani ya CHADEMA kupata mgombea wake, moja ya sababu kuu zinazoonekana kama kikwazo kwa dhamira ya Zitto kuwa Rais, ni hiyo tuliyoiongelea hapo juu ya kutotimiza umri wa miaka 40 mwaka 2015 kama inavyotajwa kwenye Katiba.
Tunaomsapoti Zitto katika hoja yake hiyo, tunazingatia ukweli kwamba japo nchi haiwezi kuongozwa na mtoto wa miaka mitano, kwa mfano, mtu yeyote mzima (kiumri) anaweza kuiongoza nchi yetu pasipo umri wake kuathiri utendaji kazi wake. Utu-uzima si umri maalumu bali masafa (range) ya umri. Utu-uzima unaendana zaidi na uwezo wa mtu kutambua wajibu wake na kumudu kuutekeleza.
Wajibu huo unaweza kuwa katika ngazi ya familia (kama vile kuoa/kuolewa) au katika jamii pana, kama vile kushika dhamana ya uongozi.
Kwa hiyo, kimsingi, kama Zitto amemudu kuwatumikia wapigakura wa jimbo la Kigoma Kaskazini kwa mihula miwili sasa, sambamba na kulitumikia taifa kupitia uenyekiti wake kwenye Kamati ya Bunge, basi hakuna sababu ya msingi kwa umri wake kuwa kigezo cha kumzuwia kugombea urais mwaka 2015 hata kama atakuwa hajatimiza miaka 40. Ndiyo. Katiba inazuwia, lakini ukweli ni kuwa inazuwia kiuonevu!
Sasa wakati tunaafikiana na Zitto kupingana na uonevu huo wa Katiba, inakuwaje tena anatumia kigezo cha umri kuwabagua ‘wazee’ anaodai hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi? Busara ndogo tu ingeweza kumfahamisha Zitto-kama msomi-kuwa siasa na uchumi ni maeneo yanayotegemeana. Kama wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru walimudu kutuletea maendeleo ya kisiasa, kwanini washindwe kwenye maendeleo ya kiuchumi?
Kama yeye aliyezaliwa baada ya Uhuru ameweza kufanya kazi nzuri kabisa katika uongozi wake wab kisiasa, ni kigezo kipi anachotumia kuwaona wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru kuwa hawatoweza harakati za kuleta maendeleo yetu? Kwa hakika kabisa, huu ni ubaguzi, na kamwe mtu mwenye hisia za ubaguzi hapaswi japo kufikiriwa kuongoza nchi yetu.
Ninasema hivyo kwa sababu kama alivyotuusia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ubaguzi huzaa ubaguzi. Leo itakuwa “wazee waaliozaliwa kabla ya Uhuru hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi,” kesho itakuwa “Wakristo/Waislamu hawawezi kufanya hili,” “Wapogoro hawawezi kufanya lile,” au “wanawake hawawezi jukumu Fulani na kadhalika.
Naomba nimpe darasa dogo tu Mheshimiwa Zitto kuhusu kikwazo halisi cha maendeleo yetu. Uhaba unaozidi kukua katika uzalendo wa Mtanzania. Uzalendo hauna umri. Historia inatufundisha mengi tu kuhusu mchango wa wazee katika maendeleo ya sehemu zao husika. Mwalimu Nyerere, Nelson Mandela, Mahatma Ghandhi na kadhalika.
Binafsi, niliwahi kupishana kimtizamo na Zitto kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, ambapo katika hali ya kuchokoza mjadala, nilitamka kuwa muundo wa Tume ya Kuratibu Maoni ya Katiba haukuzingatia uwiano kati ya Wakristo na Waislam. Zitto alikerwa sana na hoja yangu hiyo aliyoiita ya kibaguzi. Alisisitiza kuwa tunapaswa kuangalia wasifu wa wajumbe kwa kigezo cha uwezo na uzoefu wao na si imani zao za kidini.
Cha kushangaza, ndani ya miezi michache tu, mtu huyo huyo aliyekemea vikali virusi vya ubaguzi (wa dini), amegeuka mfuasi wa ubaguzi wa umri. Kama tunapojadili teuzi mbalimbali tunapaswa kuangalia uwezo na uzoefu wa mteuliwa, kwanini basi wazee waliozaliwa kabla ya Uhuru wasitizamwe kwa uwezo na uzoefu wao kutuletea maendeleo ya kiuchumi, badala ya kuwahukumu kwa umri wao?
Ninaibua changamoto kama hiyo ya ‘ubaguzi’ kwa minajili, si ya kukwaza dhamira ya Zitto kuingia Ikulu mwaka 2015, bali kumsaidia kuamsha tafakuri yake iwapo utekelezaji wa dhamira hiyo utakuwa na manufaa kwake na kwa chama chake, au utaishia kuwa njia ya mkato kwa CCM kurejea madarakani huku CHADEMA ikiishia kuonekana chama cha mapambano kati ya vijana na wazee kukimbilia Ikulu.
Nimalizie makala haya kwa kukumbushia tena kauli ya Baba wa Taifa, ya kwamba yatupasa kuwaogopa kama ukoma wale wote wanaokimbilia Ikulu. Kama sisi wengine tunaweza kuitumikia nchi yetu kupitia makala zetu, huku wanasiasa kama Zitto wakimudu kututumikia kama wabunge, kisa cha kukimbilia Ikulu ambako Mwalimu alituasa kuwa anayefanya hivyo aogopwe kama ukoma, ni cha nini?
Simshawishi Zitto aachane na ndoto zake za urais kwani ninatambua hiyo ni haki yake ya kidemokrasia. Hata hivyo, ni muhimu kwa mwanasiasa huyo kijana kutambua kuwa wapenda mabadiliko ya kweli watamwona kama msaliti pindi ndoto zake hizo zitakapoishia kuwa kikwazo kwa CHADEMA kuing’oa CCM madarakani. Japo busara zinatueleza kuwa na ndoto pekee haitoshi, bali ni muhimu kutekeleza ndoto hizo kwa vitendo, ukiota unakata kuti unalokalia, na ukiamka ukaamua kulikata, sote tunajua matokeo yake.




Watanidharau, watanicheka, watapambana lakini nitashinda

JOHNSON Mbwambo ameandika katika Gazeti la Raia Mwema la Oktoba 3, mwaka huu, kuhusu dhihaka za Zitto kwa Prof. Muhongo (Waziri wa Nishati na Madini). Nimesoma na nimemuelewa. Kwanza naomba radhi iwapo tafsiri ya taarifa yangu niliyoitoa kwa vyombo vya habari na kuwekwa kwenye blogu yangu (zittokabwe.com) ilikuwa ina dhihaka.
Nimefundishwa kutodhihaki watu na hasa watu wanaonizidi umri na siasa zangu sio za dhihaka bali za masuala (issues). Kupitia kwa ndugu Mbwambo naomba radhi kwa wote walioona kuna dhihaka katika andiko langu. Sikuwa na nia ya kumdhihaki Waziri Muhongo. Nia yangu ni kuonyesha kuwa Waziri Muhongo alichokifanya ni kuwacheza shere Watanzania, kwa kuwaambia maneno ambayo yeye mwenyewe alikuwa anaamini kuwa hayawezekani.
Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara yake, Eliakim Maswi, ilithibitisha kauli yangu siku chache tu baada ya kuitoa. Mbwambo kaandika makala yake kana kwamba hapakuwa na kauli ya kufuta maneno ya Waziri. Ninaamini Mbwambo aliiona kauli ile lakini aliamua kupuuza ili kujifurahisha na imani yake kwa Prof. Muhongo na mawaziri aliowataja kwenye makala yake kwamba ni mawakala wa mabadiliko. Mbwambo anaamini kabisa kwamba ndani ya utawala wa CCM, kuna mawaziri wenye nia ya dhati ya kuleta mabadiliko.
Nieleze wazi kwamba nilishtuka sana kuona toleo moja la Gazeti la Raia Mwema likiwa na makala tatu, zote dhidi ya Zitto Kabwe. Wakati makala ya ndugu Mbwambo ilikuwa inahusu suala nyeti sana la rasilimali za taifa na ni makala nzuri yenye mafundisho, makala mbili nyingine zilikuwa ni za siasa dhidi ya Zitto. Mwandishi Mayage Mayage aliandika makala yenye kichwa cha habari “Zitto, Urais 2015 kwa chama gani?” na Mwanasafu wa gazeti hili la Raia Mwema, Evarist Chahali aliandika makala yenye kichwa cha habari “Rais Kikwete anapofikiri kama Kabwe Zitto.”
Namwambia Mayage akasome vizuri historia ya ujenzi wa CHADEMA. Yeye anadhani CHADEMA imeanza mwaka 2010. CHADEMA kimejengwa na watu, si mtu mmoja. Wanaoamua mgombea wa chama si watu wachache anaowadhani yeye Mayage bali ni wanachama wa CHADEMA kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania, ikiwamo Munanila, mkoani Kigoma anapotoka Mayage.
Huyu Chahali anasema ananijua sana. Inawezekana ananijua kuliko mimi ninavyojijua. Lakini mimi simjui na wala sijawahi kumwona ana kwa ana, nimekuwa nikimwona tu kwenye mitandao ya kijamii akinizushia, kunitukana na kunisema. Sikushangaa kusoma makala yake ya wiki iliyopita. Wote wawili nawakumbusha msemo wa Mahatma Gandhi aliposema; “Kwanza wanakudharau, kisha wanakucheka, kisha wanapambana na wewe, kisha unashinda".
Sasa nirejee kwenye makala ya ndugu Mbwambo. Prof. Muhongo simjui, licha ya kwamba nimekuwa mmoja wa wabunge walioko mstari wa mbele kuhakikisha utajiri wa nchi unatumika kwa manufaa ya nchi, sikuwahi kumsikia Prof. Muhongo mpaka alipoteuliwa kuwa Waziri wa Nishati na Madini.
Sikuwahi kusikia akipaza sauti yake dhidi ya mikataba mibovu ya madini licha ya kwamba yeye ni msomi aliyebobea katika masuala ya miamba. Wakati Bunge la tisa, chini ya Spika Samuel Sitta, likiwa limecharuka kutaka mikataba mibovu ipitiwe na kubadilishwa tulitarajia sana kupata ushauri wa wataalamu wetu lakini hawakuonekana, "walikwina"?
Walikuwa waoga kusema maana wangeharibu uhusiano kati yao na watawala. Tulihangaika wenyewe bila maarifa yoyote kuhusu sekta ya madini. Wengine ilibidi kuacha kazi za ubunge na kwenda masomoni ili kuongeza ujuzi wa masuala ya kisheria na kiuchumi kuhusu sekta ya rasilimali (madini na mafuta).
Wasomi wetu hawakuwa nasi. Walichague kuendelea kufanya kazi za ushauri kwa kampuni za utafutaji madini nchini. Leo Mbwambo anawaona hawa ndiyo mawakala wa mabadiliko. Labda anasema kweli. Ila mimi nimekata tamaa na mabadiliko kuletwa na watu waliomo serikalini, kwa sababu kadhaa.
Moja, kama alivyosema ndugu Mbwambo, nilipigia kelele sana mkataba wa Buzwagi na mikataba mingine ya madini. Niliendelea kupiga kelele mpaka sheria mpya ya madini ilipopitishwa na Bunge. Nimuulize Mbwambo kwamba, licha ya sheria mpya kuandikwa imechukua miaka mingapi kampuni za madini kufanya kazi zao kwa kutumia sheria hiyo mpya? Je, mikataba mingapi iliyopitiwa imerekebishwa au hata kuvunjwa? Pengine niwasaidie kuwakumbusha taarifa kwamba, hakuna kilichofanyika kwa mujibu wa sheria mpya, licha ya kufuatilia kwa kina bungeni kupitia michango na hata maswali bungeni sambamba na makala mbalimbali.
Tangu Waziri Prof. Muhongo na timu yake waingie ofisini ni maneno tu tunayosikia bila matendo. Hata suala la mgawo wa umeme ambalo ndugu Mbwambo analisema kama mfano, yeye anajua namna ambavyo wananchi wanalalamikia umeme kukatika hovyo, tena bila taarifa wala maelezo. Muhongo alifanikiwa sana kuaminisha watu wenye mawazo huru kama Mbwambo wakamwona yupo sahihi kiasi hata cha kufumbia macho mgawo wa umeme usio na maelezo, unaoendelea nchini.
Siwaamini mawaziri kwa sababu wanasema lolote linalowajia midomoni mwao hata kama wanaamini kuwa wanalosema haliwezekani kutekelezwa. Waziri wa Nishati na Madini alisema kuhusu mikataba ya mafuta na gesi ili kufurahisha watu. Huo ni msingi wa kwanza wa kauli yangu ambayo ndugu yangu Mbwambo ameitafsiri kuwa ni dhihaka. Nilikuwa nasema ukweli mchungu kwamba, serikali haiwezi kufanya lolote kuhusu mikataba. Nilitoa changamoto kuwa kama serikali kweli imedhamiria, iweke mikataba hii wazi. Je, wameiweka wazi?
Pili, Waziri wa Nishati na Madini anataka umma umwone kwamba anajua sana masuala ya sekta kuliko Mtanzania mwingine yeyote. Nitatoa mfano mmoja unaonihusu moja kwa moja. Katika mkutano wa Bunge uliopita, Tanzania ilitembelewa na Waziri Mkuu mstaafu wa Urusi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Kirusi iliyonunua leseni ya kutafuta uranium kule Selous. Kampuni ya UraniumOne iliyonunua leseni hii ya Mkuju River Project kutoka Kampuni ya Mantra ya Australia, kwa dola za Marekani milioni 980.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilitaka ilipwe kodi ya ongezeko la mtaji (capital gains tax) kampuni hii ilikataa. TRA wakaenda mahakamani kudai malipo ya kodi yenye thamani ya dola za Marekani milioni 116 ambazo ni sawa na asilimia 20 ya thamani ya mauzo na kesi inaendelea. Kwa mujibu wa sheria zetu kampuni zinapouziana leseni, lazima Waziri wa Nishati na Madini atoe idhini ya mauzo hayo. Mgeni huyo kutoka Urusi alikuja nchini kupigia debe idhini hii, ili itolewe leseni maalumu ya uchimbaji (special mining licence).
Nikasimama kutoa taarifa bungeni kwamba mawaziri wanakutana na huyu Waziri Mkuu mstaafu wa Urusi kuhusu leseni ya Mkuju River Project na kuweka wazi kwamba Kampuni ya UraniumOne hawajalipa kodi ya capital gains. Nilisimama kutoa taarifa baada ya majibu ya Waziri Muhongo kwamba, kilichouzwa si kampuni ya Tanzania bali Australia na hivyo hakuna kodi.
Kwa makusudi kabisa niliacha habari ya kesi ya TRA dhidi ya kampuni hii ili kuona umakini wa mawaziri wetu wapya kabla ya kukutana na lobbyists (washawishi) wa kampuni hizi za madini. Waziri Muhongo aliposimamishwa na Naibu Spika, Job Ndugai, akasema “Sisi tunajua zaidi kuliko Zitto" Kwanza Waziri hakuwa anajua.
Ni makosa kabisa kujadili suala ambalo mamlaka mojawapo ya nchi wamelipeleka mahakamani na linasubiri uamuzi. Lakini suala la Waziri kutokuwa na taarifa lilidhibitishwa na ujio wa Naibu Waziri George Simbachawene, aliponifuata na kuomba "details" kuhusu taarifa niliyotoa. Kulikuwa na haja gani kwa Waziri kusema bungeni yeye anajua zaidi na baadaye kumtuma Naibu wake kutafuta taarifa?
Huu ni udhaifu mkubwa sana wa uongozi. Kutojua si makosa, inawezekana kuwa wengine hatukusomea miamba lakini tumesomea masuala ya kodi kwenye madini na mafuta. Waziri makini anayejali nchi yake anawezaje kukutana na mwekezaji anayekataa kukulipa kodi yako bila wewe hata kuulizia utalipwa lini?
Unaulizwa bungeni unasema "ninajua zaidi" na Mwandishi mahiri kama Mbwambo anasema "mpeni nafasi atende"!
Nilipomsikia Waziri anasema ameagiza TPDC (Shirika la Maendeleo la Mafuta) kupitia mikataba nikajua na hili nalo hajui. Amesema tu ili watu wafurahi kwamba mikataba inapitiwa. Kupitia mikataba bila kuchukua hatua dhidi ya mikataba mibovu ni nini kama sio kutafuta umaarufu tu? Unapitia mikataba ili iwe nini kama huwezi kuchukua hatua?
Kuna mikataba ambayo imeingiwa kwa rushwa, sheria zetu zinasema kuwa mikataba iliyoingiwa kwa rushwa ni sawa na haipo. Hata sheria za kimataifa za mikataba zinatambua hivyo. Waziri anaposema kuwa tunapitia mikataba ili kuhakikisha kuwa mikataba ijayo inakuwa mizuri ni kichekesho. Hivi tunajua vitalu vingapi vimegawiwa na vingapi vimebaki? Hivi sasa kuna mikataba 29 na leseni 26. Vitalu vilivyobaki hivi sasa ni tisa tu.
Wizara inatuambia tunaangalia hii mikataba 29 ili kuboresha 9. Haya si mapitio bali ni kuangalia tu kama nilivyosema katika sentensi iliyotangulia. Mapitio bora zaidi ni uwazi wa mikataba yote tuliyoingia mpaka sasa na kuzuia kabisa mikataba mipya wala kugawa vitalu vipya vya kutafuta mafuta na gesi.
Uporaji wa rasilimali ni wa namna mbili, moja ni watu wachache na kampuni zao kupora kwa kupitia mikataba mibovu na pili ni kizazi kimoja kunyonya rasilimali zote bila kujali kizazi kijacho. Katika maandiko yangu nimeshauri kuwa tusigawe vitalu vipya mpaka tuone mafanikio ya mikataba hii 29 na leseni 26 tulizonazo hivi sasa. Wito wangu ni mmoja tu, uwazi wa mikataba. Kutaka uwazi si dhihaka. Uwazi ni uwajibikaji.
Suala la mapitio ya mikataba kwa jicho la juu juu ni suala la kuunga mkono. Lakini ukitazama historia ya nchi yetu katika masuala haya utabaini kwamba tunapaswa kufanya zaidi ya mapitio ya mikataba.
Tunapaswa kufanya jambo ambalo hatujawahi kulifanya nalo ni kuiweka wazi mikataba hii kwa umma. Hii ndiyo hoja yangu.
Inawezekana kabisa kwamba maneno niliyotumia yameudhi watu fulani lakini ikumbukwe mimi ni Mbunge wa Upinzani na ni wajibu wangu kukosoa serikali kila inapowezekana. Bahati nzuri miaka yangu saba bungeni hivi sasa imetumika kwa kiasi kikubwa sana katika kufuatilia kwa karibu sekta ya madini, mafuta na gesi. Ni rahisi sana mimi kuweza kuona suala linalosemwa na serikali linasemwa tu au serikali inamaanisha? Katika suala la mapitio ya mikataba kwenye sekta ya madini na mafuta kwa kweli serikali haipo makini. Watu wajuvi wa mambo kama kina Mbwambo wanapaswa kwenda zaidi ya mapitio na kutaka mikataba iwekwe wazi na kuchambuliwa kwa uwazi kabisa.
Waziri Muhongo anayo nafasi ya kufanya kazi yake, afanye kazi yake bila bugudha. Mbwambo ajue kuwa Mbunge Zitto pia anayo kazi yake kwa mujibu wa Katiba ibara ya 63 nayo ni "kuisimamia" serikali. Niacheni nami nifanye kazi yangu.
Makala hii iliyoandikwa na Kabwe Zitto, Mbunge wa Kigoma Kaskazini ni majibu kwa makala iliyoandikwa na Mwanasafu wetu, Johnson Mbwambo, katika toleo lililopita la gazeti hili la Raia Mwema, kupitia safu yake ya Tafakuri Jadidi.
MAONI: NI KWELI ZITTO HANIJUI, NA KATIKA MAKALA HUSIKA NILIANDIKA "NAMJUA ZITTO VIZURI" NA SIO "TUNAJUANA VIZURI." NA KIMSINGI, HAKUPASWA KUNIJUA WAKATI NILIPOKUWA NAMJUA (KINYUME CHA HIVYO,JUKUMU ZIMA LA KUMJUA LISINGEKUWA NA MAANA). BY THE WAY, HIVI ZITTO ANAMJUA KILA MPIGA KURA KATIKAJIMBO LAKE, LET ALONE MIE AMBAYE SIKUMPIGIA KURA?

SIKUANDIKA KUWA NAMJUA ZITTO VIZURI KWA MINAJILI YA KUSAKA SIFA AU KUJIKOMBA KWAMBA "NINAMFAHAMU VIZURI RAIS MTARAJIWA" BALI NILIANDIKA HIVYO KUPIGIA MSTARI KUWA MWANASIASA NINAYEMZUNGUMZIA NI MTU NINAYEMFAHAMU (KIVIPI,WAPI...NAOMBA NISIZUNGUMZIE HILI KWA MUDA HUU).

SITAKI KUMWITA MHESHIMIWA ZITTO MBABAISHAJI LAKINI MAKALA YAKE HII INANISHAWISHI KUFIKIRIA HIVYO.ZITTO ANAZUNGUMZIA MIE KUMJUA, ANADAI NINAMTUKANA (HIVI RAIS MTARAJIWA HATAMBUA KUWA MTU AKIKUTUKANA KWENYE TWITTER UNAPASWA KUMRIPOTI KWA WAMILIKI WA MTANDAO HUO BADALA YA KULALAMIKA KWENYE MAKALA?).HUYU ANAYEDAI NINAMTUKANA NDIYE SAME PERSON ALIYEANDIKA HAYA  ni upumbavu kufikiri kwa misingi wa kidini. Huna haki kuleta ubaguzi wako wa kidini hapa. 3 out of 15 muslims, unaita ubaguzi? (chanzo: http://goo.gl/8MLDO

Mwanasiasa huyu mbabaishaji alinilaumu kwa "kuleta ubaguzi" lakini yeye si mbaguzi anapodai watu waliozaliwa kabla ya uhuru hawawezi kutuletea maendeleo ya kiuchumi.

NIMALIZIE KWA KUWAACHIA WASOMAJI FURSA YA KUAMUA WENYEWE IWAPO MHESHIMIWA ZITTO AMEJIBU HOJA (NINAZOZIONA) ZA MSINGI KATIKA MAKALA HII







8 Oct 2012



NIMEKUWA nikiulizwa swali hili takriban kila wiki baada ya makala zangu kuchapishwa katika jarida hili maridhawa: Hivi kuna wakati unaishiwa na cha kuandika? Na siku zote jibu langu linakuwa lile lile; Tanzania yetu haiishiwi mambo yanayopaswa kujadiliwa-iwe gazetini, mtandaoni, kijiweni au popote pale. Kuweka rekodi sawia, kila ninapoingia mtandaoni huwa ninakumbana na wastani wa angalau habari tano zinazoweza kutengeneza mada za makala zangu.
Wiki hii nitazungumzia matukio mawili makubwa yanayoihusu CCM na CHADEMA. Kwa namna moja au nyingine, matukio yote mawili yanahusiana, na nitajitahidi kuonyesha uhusiano wao mwishoni mwa makala haya.
Tukio la kwanza ni kauli ya Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kwamba CCM haitokufa, na pengine wanaodhani hivyo wanaweza kufa wao kabla ya chama hicho tawala kufa.
Kwa baadhi yetu tunaosoma siasa kama eneo la taaluma, tunatambua ukweli mmoja, kwamba chama cha siasa kinazaliwa, kinakua, na kama ilivyo kwa binadamu, kinaweza kufa. Na tofauti na binadamu ambao hatuna udhibiti mkubwa wa kurefusha au kufupisha maisha yetu (kuna watenda dhambi na wanaotumia kila aina ya ‘sumu’-pombe, dawa za kulevya na kadhalika ama kumkera Muumba au kuharibu afya zao-lakini si tu wapo hai bali pia wana afya za kuridhisha, huku wengine mambo yao yakizidi kuwanyookea, huku upande mwingine kukiwa na wacha Mungu, wanaojali afya zao lakini wanataabika muda huu); Vyama vya siasa vinaweza kurefusha maisha yao kwa kuitumikia jamii kulingana na matarajio ya jamii husika au ikaipuuza jamii hiyo na kujichimbia kaburi.
Pamoja na heshima yangu kubwa kwa Rais Kikwete, ninaomba kutofautiana naye katika kauli hiyo kuwa CCM haitokufa. Si tu kuwa vyama vya siasa hufa, bali pia ninaamini kuwa kila Mtanzania anayefuatilia kwa karibu historia na mwenendo wa chama hicho anaweza kabisa kubashiri kuwa ama mwanzo wa mwisho wake unakaribia au kinaharakisha kifo chake.
Simlaumu Rais Kikwete kwa kauli hiyo kwa sababu kama Mwenyekiti wa Taifa wa Chama anachoongoza ana jukumu kubwa la kuwahakikishia viongozi na wanachama wenzake kuwa ‘mambo si mabaya’ kama inavyoelezwa na wapinzani wao.
Binafsi, nasema kinachoweza kuiua CCM kabla ya wakati wake, ni pamoja na mtizamo huo wa Rais Kikwete wa kwamba ‘chama hicho kipo imara na kinaendelea kupendwa na Watanzania wengi-uthibitisho (kwa mujibu wao) ni idadi ya wana-CCM waliojitokeza kugombea nafasi mbalimbali kwenye chaguzi zinazoendelea ndani ya chama hicho.
Ni kweli kwamba idadi ya waliojitokeza kugombea inaweza kujenga picha kuwa CCM bado kinapendwa na wengi. Lakini haihitaji ufahamu mkubwa wa siasa zetu kumaizi kuwa baadhi ya wanaokimbilia uongozi ndani ya chama hicho wana ajenda zao binafsi. Ikumbukwe kuwa huko nyuma chama hiki kilishaonyesha dhamira ya kutenganisha biashara na siasa, hatua iliyotafsiriwa na wengi kuwa ni kutambua kuwa kuna kundi la wafanyabiashara wanaokimbilia kwenye siasa si kwa minajili ya kuutumikia umma, bali kusaka ‘kinga’ ya kuwalinda katika biashara zao.
Binafsi, nilikuwa miongoni mwa wapinzani wakubwa wa wazo hilo, si tu kwa sababu siafikiani na aina yoyote ya ubaguzi, bali pia sikuona kuwa tatizo ni wafanyabiashara kujihusisha na siasa bali wafanyabiashara ‘wachafu’ kuruhusiwa kujihusisha na siasa. Kwa kuharamisha biashara kwenye siasa kungeweza kuwa na hatari ya kuwakwaza wazalendo wazuri tu ambao walichagua kujihusisha na biashara kabla ya kuingia kwenye siasa.
Na ingekuwa ubaguzi wa wazi kuwazuia wafanyabiashara kujihusisha na siasa, lakini kuwaruhusu askari wastaafu, wasomi na wanajamii wengineo kufanya hivyo. Sawa, wanasema samaki mmoja akioza basi wote wameoza, lakini usemi huu hauzingatii ukweli kwamba binadamu hutofautiana.
Kwa mfano, kwa vile Mndamba wa kwanza kumfahamu ni mie ambaye pengine ninakukera na kwa mtizamo wangu haimaanishi kuwa kila Mndamba utakayekutana nae maishani atakukera. Waingereza wana msemo kuwa “people vary because we differ” yaani watu huwa na tofauti kwa sababu wanatofautiana, na kwa mantiki hiyo hiyo, mfanyabiashara anayeingia kwenye siasa kwa minajili ya kujitengenezea kinga katika ufisadi wake kwa taifa, haimaanishi kuwa kila mfanyabiashara anayeingia kwenye siasa ana malengo hayo.
Ninaamini kilichopelekea CCM kudhamiria kumtenganisha biashara na siasa ni historia na uzoefu iliopata kutoka kwa baadhi ya wafanyabiashara walioingia kwenye siasa. Na wazo lilikuwa zuri, kwamba mfanyabiashara atakayeamua kuingia kwenye siasa achague moja: biashara au siasa.
Tukirejea kwenye tamko la Kikwete kuwa CCM haitokufa, yayumkinika kuamini kuwa kauli hiyo ni ya kujipa matumaini tu na kukwepa ukweli kwamba kwa kiasi kikubwa chama hicho kinaonekana machoni mwa baadhi ya Watanzania kuwa ni chanzo cha matatizo mengi yanayoikabili nchi yetu. Kwa kifupi, kitakachoiua CCM si kauli za hao wanaoikitabiria kifo bali matendo ya chama hicho ambayo kimsingi ndio ‘pumzi’ inayokifanya kiwe hai.
Tukio jingine ambalo kwa namna moja au nyingine linahusiana na uhai wa chama cha siasa (kwa maana ya kuwa hakitokufa au la) ni tamko la Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe (CHADEMA), ya kwamba hatogombea ubunge katika uchaguzi mkuu ujao wa 2015, bali atagombea urais.
Kwanini ninalinganisha tamko la Zitto na kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Kikwete? Jibu fupi ni kwamba matamko yote mawili yanaelekea kupuuza hali halisi ya mwenendo wa siasa za huko nyumbani.
Wakati Mwenyekiti Kikwete anajigamba kuwa CCM haitokufa japo kuna mamia kwa maelfu ya wana-CCM wanaokihama chama hicho kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wake, huku pia baadhi ya viongozi wa chama hicho kama kina Samuel Sitta wakionyesha hadharani ‘maovu’ ya chama hicho, Zitto hataki kujihangaisha kutambua wengi wa Watanzania wanamtaka mwanasiasa gani kutoka chama chake ili kubeba dhamana ya kugombea urais kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Kabla sijaendelea kuijadili kauli ya Zitto, ningependa kuweka bayana masuala matatu ya msingi. Kwanza, Zitto ana kila haki si tu ya kutaka kuwa Rais wa Tanzania, bali pia kutangaza kuwa ana nia hiyo. Ni haki yake ya kidemokrasia, hasa ikizingatiwa kuwa anatoka katika chama cha Demokrasia na Maendeleo.
Pili, ni suala la kukubalika kwa wapiga kura watarajiwa (potential voters). Kila mara ninapomsikia Zitto akielezea dhamira yake ya kutaka kuwa Rais, huwa ninajiuliza swali moja la msingi; ni lini amefanya ‘utafiti’ wa kutambua Watanzania wanamhitaji awe rais wao?
Wenzetu huku Magharibi, kabla mwanasiasa hajakurupuka kutangaza kuwa anataka kuwa rais huwa inamlazimu kujihangaisha ‘kusoma upepo,’ yaani kufahamu iwapo wapigakura wanamhitaji.
Sawa, Tanzania si nchi ya Magharibi, na pengine hakuna umuhimu wa kusaka mtizamo wa wapigakura. Lakini kwa mwanasiasa anayejali maslahi ya chama chake na wananchi kwa ujumla, yayumkinika kuamini kuwa atajihangaisha kufahamu iwapo dhamira yake ya kugombea ni kwa maslahi ya chama chake na umma kwa ujumla au ni kwa ajili ya kutimiza ndoto zake binafsi tu.
Suala la tatu, na ambalo kwangu si tu ni la msingi zaidi bali pia linanishawishi kuamini kuwa dhamira ya Zitto kugombea urais ni sawa na kubariki ushindi wa CCM hapo 2015, ni uadilifu wa mwanasiasa huyo.
Ninamfahamu Zitto vizuri, na si kupitia social media. Ni mmoja wa wanasiasa wachache wenye kipaji cha hali ya juu katika ujenzi wa hoja. Lakini, kama mwanadamu mwingine, mwanasiasa huyo ana mapungufu fulani. Kwa wanaomfahamu kupitia social media (hususan Twitter) wanaweza kuafikiana nami kuwa si mwepesi sana wa kuafikiana na watu wenye mtizamo tofauti na wake.
Ni rahisi kumhukumu kuwa ana jazba (japo sitaki kuamini hivyo) pindi mtu anapotofautiana naye katika anachoamini yeye kuwa ni sahihi. Nafasi haitoshi kutoa mifano halisi, lakini waliotofautiana nae kimtizamo ndani ya Twitter wanaweza kuwa mashahidi wazuri.
Tatizo la msingi kuhusu Zitto ni ‘tuhuma’ zilizowahi kuandikwa na jarida moja la kila wiki kwamba katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu uliopita, jarida hilo lilinasa mawasiliano kati ya mwanasiasa huyo na mmoja wa viongozi wa juu wa Idara ya Usalama wa Taifa.
Katika mazingira ya kawaida, mwanasiasa wa chama cha upinzani kuwa na mawasiliano na mtumishi wa taasisi hiyo nyeti (ambayo ilishutumiwa na CHADEMA-ambayo Zitto ni mbunge wake-kuwa ilikihujumu chama hicho kwenye uchaguzi huo) inazua maswali kadhaa.
Ndio, watumishi wa Idara ya Usalama wa Taifa ni Watanzania wenzetu kama ilivyo kwa wanasiasa wa vyama vya upinzani. Lakini mawasiliano kati ya mwanasiasa wa chama cha upinzani kama Zitto na kiongozi wa idara hiyo, yanaweza kuibua maswali mengi. Kibaya zaidi, Zitto hajawahi kutoa ‘maelezo ya kueleweka’ kuhusu mawasiliano hayo.
Kimsingi, Zitto anatambua bayana hisia zilizojengeka baada ya habari hiyo kuchapishwa. Kuna waliotafsiri kuwa mawasiliano hayo yalilenga kukihujumu chama hicho, na kwa kuzingatia mantiki ya kawaida tu hatuwezi kuwalaumu kwa hisia hizo.
Lakini pengine kubwa zaidi ni kwanini bado kuna idadi kubwa tu ya wafuasi wa CHADEMA wanaotafsiri uamuzi wa Zitto kutaka urais kama ‘tamaa ya madaraka.’ Hivi akiweka kando imani yake kuwa ana uwezo na uadilifu wa kuongoza taifa la Tanzania, Zitto ameshawahi kufikiria kuwashawishi sceptics hawa hata kama hoja zao hazina mashiko?
Kubwa zaidi ni ukweli kwamba matokeo ya uchaguzi mkuu uliopita yanaonyesha bayana jinsi mgombea urais kupitia CHADEMA, Dk Willibrod Slaa, alivyokubalika kwa idadi ya kuridhisha tu wapiga kura. Kama dhamira ya Zitto ni kuona CHADEMA inaingia Ikulu, kwanini asiwekeze jitihada kumsapoti Dk Slaa katika uchaguzi ujao na kusubiri ‘zamu yake’ hasa kwa vile umri bado unamruhusu hata kwa miaka mingine 15 ijayo?
Kwa mujibu wa Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano, mgombea urais sharti awe na miaka 40. Mwaka 2015 Zitto atakuwa na umri pungufu na huo. Hivi kung’ang’ania kuwa anataka kugombea ilhali akijua Katiba haimruhusu si ni dalili ya tamaa ya madaraka?
Nimalizie makala haya kwa kulinganisha matukio mawili haya niliyozungumzia. Kama ambavyo Rais Kikwete hataki kujiuliza kwanini baadhi ya watu wanaitabiria kifo CCM, Zitto hataki kujiuliza kwanini baadhi ya watu wanatafsiri dhamira yake ya kutaka urais mwaka 2015 kama mikakati wa kuirejesha CCM madarakani na kuinyima CHADEMA nafasi hiyo.
Suluhisho katika masuala hayo mawili, linaweza kupatikana katika busara hii ya Waingereza isemayo “never ever put emotions in front of common sense” (kwa tafsiri isiyo rasmi, kamwe usitangulize hisia mbele ya tabasuri/ busara).


30 Sept 2012




27 Sept 2012



NINAAMINI takriban kila msomaji wa magazeti ameshawahi kukumbana na sentensi hii inayokera ya “jina linahifadhiwa kwa sasa.”
Kinachokera si tu kuhifadhiwa kwa jina la mhusika mkuu katika habari bali ukweli kwamba mara nyingi habari husika hugeuka kuwa mithili ya mtihani uliojaa mafumbo, na pasipo msomaji “kujumlisha 2 na 2 kupata 4” hakuna uwezekano wa habari hiyo kuleta maana yoyote.
Mifano ni mingi lakini mfano mwafaka ni katika habari ambayo nitaizungumzia pia kwenye makala hii. Kwa siku kadhaa, magazeti mbalimbali yalikuwa yakiripoti taarifa kuhusu mke wa kigogo wa Jeshi la Polisi, ambapo utambulisho wa kigogo huyo na mkewe umebaki kuwa “umehifadhiwa,” akihusishwa na utapeli wa mamilioni ya shilingi kwa ahadi ya kuwapatia watu ajira kwenye vyombo vya dola.
Kabla ya kujadili tukio hilo la utapeli wa aina yake, tuendelee na mjadala wa tabia inayozidi kuota mizizi kwenye magazeti yetu ya “jina limehifadhiwa.” Japo uelewa wangu wa sheria ya kumkashifu mtu/taasisi (Defamation Law) ni wa wastani, siku zote kama mwandishi wa blogu na makala nimekuwa makini kuhakikisha kuwa ninapotaja jina la mtu au taasisi kwenye habari husika, nina uhakika na ushahidi ninao.
Kwa msingi huo, sioni haja ya kutumia sentensi “jina linahifadhiwa kwa sasa” (na mara nyingi hiyo ‘sasa’ hugeuka kuwa ‘milele’) kwa sababu iwapo mtajwa katika andiko husika ataamua kunipeleka mahakamani kwa madai ya kumkashifu, nitapambana naye vilivyo.
Nadhani sababu kubwa ya waandishi wetu kusaka hifadhi ya “jina linahifadhiwa kwa sasa” kwenye kuficha majina ya wahusika katika maandiko yao ni uoga wa kuburuzwa mahakamani kwa madai ya kashfa dhidi ya mtajwa. Na sababu pekee inavyoweza kusababisha uoga huo ni ukosefu wa facts au ushahidi kamili.
Ni wazi kwamba sheria ipo upande wa mwandishi pindi anapoandika habari ambayo imejitosheleza, kwa maana ya kuwa na ushahidi usiopingika kuhusu mtajwa katika habari husika.
Kimsingi, taaluma ya uandishi wa habari inashabihiana kwa kiasi kikubwa na ushushushu katika namna habari inayotafutwa. Katika taaluma zote lengo ni kupata habari kwa minajili ya kuziwasilisha sehemu fulani: kwa msomaji kwa upande wa wanahabari, na kwa mwajiri kwa upande wa mashushushu.
Tofauti za msingi katika utafutaji na matumizi ya habari ni kwamba wakati mara nyingi wanahabari wanapaswa kuwa ‘wazi’ wanaposaka habari (kupata habari kwa udanganyifu kunaweza kuwa kosa la jinai), takriban mara zote mashushushu husaka habari kwa kificho (na kwa mujibu wa sheria, shushushu kujiweka wazi-au kujiumbua-ni kosa).
Kwa upande wa matumizi ya habari zilizopatikana, wanahabari wanatarajiwa kuziwasilisha kwa msomaji (tukiweka kando taratibu za kiuhariri ndani ya chombo habari husika) ilhali kwa mashushushu habari, ambayo wakati huo hugeuka kuwa taarifa, huwasilishwa kwa chombo husika kwa hatua nyinginezo.
Kwa hiyo, tofauti ya kimsingi ya mwanahabari na shushushu ipo zaidi kwenye ‘habari’ na ‘taarifa.’ Wakati habari ni kitu cha wazi na kwa ajili ya matumizi ya umma, taarifa ni kitu cha siri na ni kwa ajili ya matumizi ya taasisi ya kishushushu tu.
Sasa tunachoshuhudia katika uandishi wetu wa “jina limehifadhiwa kwa sasa” ni mithili ya ‘mchanyato wa habari na taarifa,’ kwa maana ya ‘kuwasilisha habari nusu kama mwanahabari lakini pia nusu kama shushushu - nusu wazi nusu siri.’
Ni adhabu kubwa kwa msomaji anapokutana na habari iliyoandikwa kwa mfumo huu “kigogo mmoja (jina linahifadhiwa) wa taasisi moja (jina linahifadhiwa) anadaiwa kulimbikiza fedha zilizopatikana kifisadi katika nchi moja (jina linahifadhiwa).” Kimsingi, habari hii haina umuhimu zaidi ya kuuza gazeti husika na kusumbua ubongo wa msomaji.
Kwa nini mwandishi husika asihakikishe anapata facts zote kuhusu mhusika katika habari hiyo kabla ya kukurupuka kuiripoti nusu nusu? Ninatambua kuwa baadhi ya wanahabari wanaweza kujitetea kuwa wanafanya hivyo kwa minajili ya ‘kumshtua mhusika’ kwamba matendo yake yanafahamika lakini kimsingi hilo si jukumu la chombo cha habari. Kama kuna maovu yasiyoandikika gazetini basi yawasilishwe kwa taasisi za dola badala ya kuwachosa wasomaji na ‘habari za kificho.’
Turejee kwenye sakata la utapeli unaodaiwa kufanywa na mke wa kigogo wa polisi ambao kwa pamoja “majina yao yameendelea kuhifadhiwa” na vyombo vya habari vilivyokuwa vinaripoti habari hiyo.
Awali iliripotiwa kuwa mke wa kigogo huyo alijipatia mamilioni ya shilingi kwa ahadi ya kuwapatia ajira vijana 120 kwenye Jeshi la Polisi, Idara ya Usalama wa Taifa na Taasisi ya Kuzuia na Kudhibiti Rushwa (TAKUKURU).
Habari zaidi zilizeleza kuwa Jeshi la Polisi lilikuwa likimlinda mke huyo wa kigogo (na hii si ajabu kwani yeyote anayefahamu utendaji kazi wa vyombo vyetu vya dola anatambua kuwa viongozi wake na watu wanaowahusu ni miungu-watu wasiopaswa kusumbuliwa kwa aina yoyote ile).
Kwa mantiki hiyo, Polisi kumlinda mke wa kigogo wa jeshi hilo ni jambo la kutarajiwa japo si sahihi.
Baadaye ikaripotiwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa Othman Rashid amelitaka Jeshi la Polisi kumkamata na kumchukulia hatua mwanamke huyo. Katika hatua ya nadra mno, Othman alisema (ninanukuu) “Nimewasiliana na IGP (Said) Mwema ili aweze kunipa ufafanuzi kuhusu mke wa kigogo huyo, lakini nashukuru amenipa ushirikiano na kuniambia kuwa suala hilo wanalishughulikia kisheria zaidi. Watanipa taarifa pindi watakapokuwa wamekamilisha.”
Lakini katika kile unachoweza kudhani ni tamthiliya isiyopendeza machoni, habari hiyo ikageuka sarakasi na kugeuka kuwa (ninanukuu) “Wakazi wawili wa jijini Dar es Salaam, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakikabiliwa na makosa 12 ya kujipatia sh milioni 102 kwa njia ya udanganyifu wa kuwatafutia vijana kazi katika Idara ya Usalama wa Taifa na Jeshi la Polisi.”
Miongoni mwa wanaotajwa ‘kutapeliwa’ ni mke wa Mkuu wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi, Kamishna Paul Chagonja, aliyatajwa kwa jina moja tu la Happyphania, ambaye inadaiwa alitapeliwa shilingi milioni 5 “kwa madai kuwa ni malipo ya maombi ya usajili wa mafunzo ya POLISI (herufi kubwa kwa sababu maalumu), TAKUKURU na Idara ya Usalama wa Taifa.
Swali la kwanza, hivi kweli inaingia mke wa Kamishna wa Mafunzo na Operesheni wa Jeshi la Polisi atoe fedha kwa ‘matapeli’ ili kumpatia nafasi ya usajili wa mafunzo ya Jeshi la Polisi ambako mumewe si tu ni mmoja wa vigogo wa ngazi za juu bali pia ndiye mwenye dhamana ya MAFUNZO kwa wanaojiunga na jeshi hilo?
Swali la pili, tukiamini kuwa watu hao wawili waliokamatwa na kufungulia mashtaka (wote si wanawake), kwanini basi Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa alimtaka IGP kushughulikia suala la “mke wa kigogo wa polisi”? Hivi kweli inaingia akilini “mke wa kigogo wa polisi” awe “hao washtakiwa wawili wa kiume”?
Maswali ni mengi, ikiwa ni pamoja na kitendo cha mke wa Kamanda Chagonja kutoa fedha kwa matapeli hao. Pasi kuuma maneno, hivi kutoa fedha kwa ajili ya kupata huduma inayotolewa bure si rushwa? Kwanini basi waliopokea fedha hizo washtakiwe lakini waliotoa fedha wasishtakiwe kwa kutoa rushwa?
Ninatambua uwezekano wa utetezi wa “waliotoa fedha hizo ni victims (majeruhi) wa utapeli.” Hiyo inaweza kuwa kweli tu kwa watu wasiofahamu utaratibu wa kujiunga na taasisi hizo. Sitaki kabisa kuamini kuwa mke wa Kamishna Chagonja hafahamu utaratibu huo hadi kushawishika kutoa fedha kwa washtakiwe hao.
Katika moja ya habari inayomnukuu kigogo wa polisi ambaye kama kawaida jina lake lilihifadhiwa, alisema “…Hata mke wangu ni mmoja wa waliotapeliwa. Alikusudia kuwapeleka wanafamilia watatu akiwemo mtoto wake, mke wa kaka yake na wifi yake ambaye tunamlea.” Mke wa kigogo wa polisi anatapeliwa kuingiza nduguze kwenye jeshi hilohilo analofanya kazi muwewe? Huu ni utani mbaya kabisa.
Kama ilivyo desturi, habari hiyo ndio imeishiwa hapo. Magazeti yaliyokuwa yakiripoti kuhusu mke (jina limehifadhiwa) wa kigogo wa polisi (jina limehifadhiwa) yamemaliza kazi yao na kumwachia kazi msomaji kujumlisha 2 na 2 apate 4.
Na tabia hii ya kukera ya “jina limehifadhiwa” inachangia kuonyesha ubaguzi wa wazi wa kimatabaka. Sijawahi kuona sentensi ya “jina linahifadhiwa” ikitumika kwa tuhuma zinazowahusu walalahoi bali ni kwa vigogo pekee.Ni kwa vile uwezekano wa walalahoi hao kwenda mahakamani kudai wamekashifiwa na gazeti husika ni mdogo au ni kupuuza tu haki zao za kibinadamu?
Mwisho, wakati nina uhakika kuwa majina ya kigogo wa polisi na mkewe anayedaiwa kutapeli yataendelea kuhifadhiwa ‘milele’ (habari yenyewe ni kama imeshakufa kifo cha asili), harakati za kupigania uhuru wa vyombo vya habari hazitozaa matokeo tarajiwa kama vyombo vya habari vitaendeleza kasumba ya “jina linahifadhiwa” ambayo inainyima jamii uhuru wa kuelewa habari husika.


21 Sept 2012


Zitto Kabwe, Let Dr. Muhongo Do His Job


Energy sector has brought to a disgraceful ending some very promising careers. It has sent packing very powerful and prominent figures in the country’s upper echelons of power; Infarct, at one point, it almost brought down the entire government, when the country’s premiere at the time, faced grand corruption allegations, and was forced to resign. It is our economic sector, by far mired by grand corruptions and ineptness. 

Reason behind all these has been nothing more than the bogus contracts. There is therefore, a critical need to review and even terminate some of the existing contracts in the eyes of the public, in order to close the loopholes fleecing the country of its wealth 

The Kigoma North Legislator, Zitto Kabwe, has unleashed in the past few days, some scathing attacks on the Minister of Energy Sospeter Muhongo, for proposing a thorough review of the Gas exploration contracts. Mr. Kabwe described Dr. Muhongo’s statements as irresponsible, publicity stunts and cowboy’s approach at the expense of transparency. What I found rather irresponsible, odd, flawed and vague, was the broad idea of “Transparency” in which Mr. Kabwe is attacking Dr. Muhongo’s premise without providing a practical solution under conventional wisdom

I also found Mr. Kabwe’s idea of shelving gas exploration for ten years as logically, and economically naïve. At best I would describe the proposition as a theory that contravenes the basic and natural economic principles that cannot be implemented in a needy nation like ours. Implementing this thought would be nothing short of economic suicide for a nation whose economy is extremely fragile. 

Mr. Kabwe’s Transparency assertion reveals nothing short of tactical political, intimidation, representation and defense of the unknown interests. I would not go as far as describing the verbal assault as a self serving personal act of vengeance. However, the premise under which Mr. Kabwe’s argument is based, and his pattern of attack, points towards just that.

Mr. Kabwe unambiguously failed to explain how making transparent shoddy contractual agreements, will benefit the country without identifying the loopholes and deficiencies through extensive review. Arguably, lack of legal and technical knowhow to intimately interpret word by word in the existing contracts to weed out the elements tilting the scale on the favor of investors and shadowy forces of corruption, would have lent Mr. Kabwe’s proposition of transparency, some flesh to stand the test in opposition Dr. Muhongo’s hypothesis

Mr. Zitto ought to understand that, major foreign companies operating in Africa have tremendous resources. They have access to some of the best lawyers, and subject matter experts with extensive experience in contractual review, interpretation, negotiations, and writing. A fact which has many a times, led to the creation of lopsided contracts that have benefited investors while fleecing the host country. 

Mr. Kabwe failed to provide a balanced approach to those deficiencies. In my opinion, Dr. Muhongo’s approach is heroic, and nationalistic. The public should, without reservation throw its absolute support behind this man for his position to temporarily suspend and review all the current contracts related to gas exploration and even electricity production

Having worked in the Investment Banking –Capital Markets- Can affirm to the fact that, success or failure of an investment, primarily depends upon how crafty a contract is. Managers across all economic sectors assemble top legal minds and experienced subject matter experts that would pull off successful investments through favorable and well structured contracts. These contracts at the same time have in them, clauses and provisions that provide room for ongoing review and amendments contingent upon the prevailing conditions or circumstances and market situations. 

My only question is why Zitto is up in arms trying to block the review of questionable contacts in the public eyes, what is his fear? Singapore, India, Venezuela, Brazil etc. in recent years, radically modernized and even terminated some contracts with foreign investors in various sectors that were becoming economic liabilities or not equitably representative. This is how things work be it in municipalities, public or private companies, sovereign states and government agencies. Dr. Muhongo as a subject matter expert has suggested just that. Why should he face political interference? 

From my understanding, TPDC, a body tasked with the contractual review is not a political body. It is a professional entity made of subject matter experts –seasoned professionals -. If Mr. Zitto is dissatisfied with TPDC current formation or the capability, he should demand the overhaul of its management team for a more qualified one, which will execute the task –contractual review- diligently, impartially and independently for the interest of the nation. All findings thereafter be made public to satisfy his demand for transparency 

Political meddling, intimidation and personal hostility are not doing the country any good considering the fact that, main victims of bad contracts in the energy sector are the country’s economy, and the public at large. Politics should be kept off professional undertakings. Mr. Kabwe should let Dr. Muhongo do his job. This man has been in the office for a very short period. He has taken bold and risky decisions no other minister has ever taken in the ministry and the energy sector in general. He is stepping on dangerous toes for the best interest of the country, and what he needs the most at this point is our support not interference

Dr. Muhongo’s success or failure is not going to be measured by how many politicians he pleased or displeased, but on what he delivered to the country at the time of need. Soon or later, the public will know whether he was a bluff or a HERO he painted himself to be.  Dr. Muhongo’s approach is the right step in the right direction. Wrong step into the wrong direction is to politically interfere with his work in the name of transparency. Give him a chance to do his Job
 
Mungu Ibariki Tanzania



Forwarded  by Dr Shaban Nzori. "Mzalendo Mtanzania" is Mr Mashaka John.

Jasusi ChatBot

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.