14 May 2010

Kuna wakati najiuliza kwanini sie masikini wa kutupwa ni hodari sana kwenye matumizi ya ovyo ovyo.Moja ya kumbukumbu za serikali ya awamu ya nne ilikuwa kuongeza mishahara ya wabunge licha ya hali yetu mbovu kabisa ya uchumi.Sambamba na hilo ni utitiri wa magari ya kifahari ambayo kimsingi si miongoni mwa vipaumbele kwa taifa masikini kama letu.

Wakati sie tunaendeleza matumizi ya kutapanya huku tukitembeza bakuli kwa wafadhili,serikali mpya ya hapa Uingereza chini ya David Cameron imetangaza kuwa mishahara ya mawaziri itapunguzwa kwa asilimia 5 na hakutakuwa na nyongeza katika mishahara hiyo (pay freeze) kwa miaka mitano.Mshahara wa sasa wa Waziri Mkuu Cameron utakuwa pungufu ukilinganisha na mishahara wanayolipwa meya wa manispaa mbalimbali 61 (kila manispaa hapa inajipangia kiwango cha mishahara ya viongozi wao kulingana na uwezo wa manispaa husika.Kukupa picha nzuri,alichofanya Cameron ni kama JK angeamua alipwe mshahara pungufu kulinganisha na meya wa manispaa ya Temeke au Kinondoni...ah,naota tu.Afanye hivyo achekwe!!!?)



Yah,unaweza kusema hizi ni mbwembwe tu za serikali mpya,au manjonjo tu,lakini ukweli ni kwamba serikali makini ni ile inayoonyesha kwa vitendo kuwa inatambua hali inayolikabili taifa.Cameron ameingia madarakani wakati Uingereza ikiwa kwenye msukosuko wa uchumi,na moja ya vipaumbele vya serikali yake ni kurekebisha uchumi mapema iwezekanavyo.

Kwa mujibu wa gazeti la The Sun la hapa,mshahara wa Waziri Mkuu Cameron umepunguzwa kwa pauni 7,500 na kubaki pauni 142,500.Mishahara ya Naibu Waziri Mkuu Nick Clegg na mawaziri wengine waandamizi itakatwa pauni 7,082 na kubaki pauni 134,565 huku mawaziri wa kawaida wakikatwa pauni 5,197 na kubaki pauni 98,740.Mishahara ya mawaziri 'wadogo' itakatwa pauni 4,707 na kubaki 89,435.Hatua hiyo ya kukata mishahara kwa asilimia 5 itaokoa pauni milioni 3.

Wakati hayo yanatokea,gazeti la Mwananchi lina habari kuwa nchi wahisani wanaochangia bajeti ya serikali yetu wameamua kuunguza mchango wao kwenye bajeti ya serikali kwa mwaka 2010/2011 kwa sababu mbalimbali, ikiwamo ni pamoja na kasi ndogo ya serikali katika kutekeleza mageuzi kwenye sekta za umma.

Taarifa ya wahisani hao iliyotolewa jijini Dar es Salaam juzi, inaeleza kuwa mwaka huo wa fedha, watatoa dola za Marekani 534 milioni sawa na Sh721bilioni, ambazo ni pungufu kwa Dola za Marekani 220 milioni sawa na Sh297 bilioni walizotoa mwaka 2009/2010.

Wahisani wa bajeti ya serikali ni Benki ya Maendeleo Afrika (ADB), Canada, Denmark, Jumuiya ya Ulaya (EU), Finland, Ujerumani, Ireland, Japan, Uholanzi, Norway, Sweden, Uswisi, Uingereza na Benki ya Dunia (WB) mwaka jana walichangia Sh1.9 trilioni katika bajeti ya serikali kupitia miradi ya maendeleo na mifuko ya kisekta.

Taarifa hiyo ilitaja maeneo ambayo serikali ilishindwa kufikia malengo kuwa ni mabadiliko ya haraka katika menejimenti ya sekta ya fedha za umma, mategemeo ya kuboreka kwa hali ya mazingira ya uwekezaji na uboreshaji wa huduma kwa kutoka sekta za umma.

Hii ni mara ya nne kwa wahisani hao kuiwekea ngumu serikali katika kuchangia bajeti yake kila inapofikia mwisho wa mwaka, kwa kushindwa kutekeleza mambo wanayofikiria wao kuwa ni muhimu zaidi katika maendeleo ya nchi.

Mwaka juzi wahisani hao waligoma kutoa fedha baada ya serikali kusuasua kuchukua hatua dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi wakiwemo wa fedha za EPA mpaka zilipofunguliwa kesi kadhaa ambazo mpaka sasa zinanguruma mahakamani.

Tatizo la viongozi wetu sie ni porojo nyingi na ulaghai mwingi wa kisiasa.Majukwaani wanahubiri kama watu wenye uchungu kweli na nchi yetu,lakini matendo yao tofauti kama kiza na mwanga.Tunapenda kuishi kifahari wakati uwezo wetu ni duni kabisa.Yani kuna wakati naangalia msafara wa Waziri Mkuu hapa,kisha nikikumbuka misafara ya viongozi wetu wakuu nabaki na maswali mengi kuliko majibu.Hebu angalia video hii hapo chini inayoonyesha msafara wa Gordon Brown siku alipokwenda makazi ya Malkia Elizabeth (Buckingham Palace) kuwasilisha ombi lake la kujiuzulu.

13 May 2010

Ndoa ya Mkeka.Haya ni mambo ya pwani zaidi kuliko 'bara'.Kule kwetu Ifakara hakuna vitu kama hivyo,lakini maeneo kama Tanga,Dar,Bagamoyo,nk ndoa za mkeka 'zinakula sahani moja' kwa umaarufu kama ndoa 'za kawaida'.Actually,ilikuwa almanusra 'nipigwe ndoa ya mkeka' wakati nilipoishi Tanga kwa takriban miaka 15 ilopita.Unajua tena mambo ya ujana...ukiyaangalia wakati huu wa utu uzima inabaki kichekesho.Anyway,kwa kifupi ndoa ya mkeka ni mithili ya fumanizi kati ya wanaovunja amri ya sita pasipo minajili ya kuwa wanandoa,na 'katika kuwapa one-stop fundisho na ufumbuzi' wanafungishwa ndoa ya chap-chap.It's like "si mnapenda kuvunja amri ya sita kisirisiri?Okay,sasa tunawahalalishia mtende manyotenda for the rest of your lives"...lol!Tatizo ni kwamba ni nadra kwa ndoa za mkeka kudumu kwa vile huwa ni'za kulazimisha'.Yani hazina tofauti na stori kama binti 'anayejiachia' na kupata ujauzito ili aolewe na mpenziwe.It rarely works!


Well,makala hii inazungumzia 'ndoa ya mkeka ya kisiasa' kati ya chama cha wahafidhina (Conservatives) na kile cha Waliberali (Liberal Democrats) ambao kwa pamoja wameunda serikali ya mseto hapa Uingereza. 

Uamuzi wa kiongozi wa Conservatives kuunda serikali ya mseto na Liberal Democrats umepokelewa kwa hisia tofauti huku watu wengi wakitabiri kuwa mseto huo hauna maisha marefu.Kikubwa kinachopelekea utabiri huo ni itikadi za vyama husika sambamba na tofauti zao katika sera zao.Japo tumeambiwa kuwa moja ya sababu zilizopelekea kufanikiwa kwa mseto huo ni kwa kila chama "kukubali matokeo" kwa aidha kuelegeza au kuachana kabisa na baadhi ya misimamo yao,hiyo haimaanishi kuwa misimamo hiyo imepotea 'vichwani' mwa wafuasi wa vyama hivyo.

Wakati wahafidhina wanafahamika kwa mrengo wao wa kulia na kati-kulia (right wing or centre-right politics) waliberali ni maarufu zaidi kwa mrengo wa kushoto na kidogo kati-kushoto (left wing or centre-left politics).Pengine hili sio rahisi sana kueleweka kama tukichukulia siasa zetu huko nyumbani kama mfano,kwani nadhani tunaweza kukubaliana kwamba nafasi ya mrengo katika siasa zetu huko Afrika ni ndogo sana.Yayumkinika kabisa kusema kuwa fedha za kukiwezesha chama au mgombea kununua kura ni muhimu zaidi kwenye siasa zetu kuliko mrengo wa chama au mgombea husika.Na hili ni tatizo kwa vile chama (au mgombea) kisicho na mrengo (au msimamo) ni sawa na bendera inayoweza kuelekea upande wowote ule kulingana na mvumo wa upepo.

Wenye hofu kuhusu 'ndoa ya mkeka' kati ya wahafidhina na waliberali wana sababu za msingi kwa vile mseto kati ya siasa za mrengo wa kulia na zile za mrengo wa kushoto hauko mbali sana na jitihada za kuchanganya maji na mafuta.Wakati chama cha Conservatives kinafahamika zaidi kwa siasa zake za kuwakumbatia matajiri huku zikiwakalia kooni 'walalahoi' kwa kudi kubwa (tayari kuna taarifa za 'kiama' cha kodi) waliberali wanafahamika zaidi kwa siasa za kuwa karibu na jamii huku vitu kama haki za binadamu,uvumulivu na ushirikiano vikiwa na umuhimu mkubwa.

Wakati Liberal Democrats walikuwa na sera ya msamaha (amnesty) kwa wahamiaji 'haramu' (illegal immigrants) huku wakisisitiza kuwa hatua kali dhidi ya wahamiaji hao si ufumbuzi kwa vile 'zinazidi kuwaficha msituni',chama cha Conservative kiliweka bayana msimamo wake wa kupunguza idadi ya wahamiaji kwa kuweka ukomo (cap) katika idadi ya wanaoingia/kuhamia Uingereza,sambamba na sheria kali za uhamiaji.Na katika hatua inayoweza kuwagharimu Liberal Democrats,chama hicho kimekubali kuachana na sera yake ya msamaha kwa 'wahamiaji haramu' na badala yake kimeafiki hatua ya Conservatives kuweka ukomo kwenye idadi ya wahamiaji wanaoingia nchini hapa.

Kuna tofauti ya kimtizamo kuhusu umoja na ushirikiano wa Ulaya.Wahafidhina wanasifika kwa upinzani wao dhidi ya suala hilo huku waliberali wakipendelea kuona ushirikiano huo ukisambaa zaidi ikiwa ni pamoja na wazo la Uingereza kutumia sarafu ya Euro badala ya Pound Sterling.Katika kufanikisha 'ndoa' yao,Liberal Democrats wamekubali kusitisha mipango yao kuhusu kukuza ushiriakiano wa Ulaya,jambo linaloweza kuwaudhi waumini wa siasa za chama hicho.

Lakini tayari kuna dalili za mpasuko kwenye 'ndoa hiyo ya mkeka' baada ya taarifa kwenye baadhi ya magazeti ya hapa kwamba 'Waziri' mpya wa fedha ((Kansela) George Osborne (wa Conservatives) amepinga vikali wazo kwamba 'Waziri' wa biashara (Business Secretary) Vince Cable (wa chama cha Liberal Democrats) ndiye atakayekuwa na dhamana ya kufanya mabadiiko kwenye mfumo wa mabenki (kwa minajili ya kudhibiti na kuzuwia uwezekano wa mtikisiko wa kifedha/kiuchumi kutokana na 'uzembe' wa mabenki katika utekelezaji wa sheria za fedha).Badala yake,hazina chini ya Osborne ndio itakayoshikilia dhamana ya utekelezaji wa sera ya mabenki na sekta ya fedha kwa ujumla.


Taarifa zaidi zinaeleza kuwa kuna hofu kuwa chama cha Liberal Democrats kitakimbiwa na idadi kubwa tu ya wafuasi wake kufuatia uamuzi wake wa kushirikiana na Conservatives.Hali hiyo sio tofauti sana kwa upande wa wahafidhina kwani kuna idadi kubwa tu miongoni mwao wanaoona 'ndoa hiyo ya mkeka' kuwa jambo lisilofaa.Pengine tatizo kubwa kwa vyama vyote viwili ni wale walio 'mwisho wa upande' wa mrengo wa vyama hivyo,yaani wenye mrengo wa kulia kabisa kwa upande wa Conservatives na wa mrengo wa kushoto kabisa kwa upande wa waliberali.Hawa ni watu wanaoongozwa na imani na itikadi,na haiwaingii akilini kuona mambo hayo ya msingi yakiwekwa rehani kwa minajili tu ya kuunda serikali.

Lakini kuna wanaoona kuwa 'ndoa hii ya mkeka' kati ya David Cameron na Nick Clegg inaweza kudumu kwa vile kimsingi viongozi hao wawili wana mambo kadhaa yanayoshabihiana.Wote walisoma shule 'za bei mbaya',wanatoka familia zenye uwezo mkubwa kifedha na,kimsingi, wanaishi katika tabaka tawala.Kwa minajili hii,baadhi ya wachambuzi wanatabiri kuwa mfanano wa haiba za Cameron na Clegg,na sio tofauti katika itikadi zao,utafanikisha kudumu kwa serikali hiyo ya 'ajabu' kati chama chenye siasa za mrengo wa kulia (conservatives) na kile cha mrengo wa kushoto (Liberal Democrats).

Pamoja na yote hayo,siasa ni mchezo usiotabirika.Siku chache zilizopita ingekuwa jambo lisilofikirika kwa wahafidhana na waliberali kushirikiana katika uongozi wa serikali,lakini leo hii 'habari ndio hiyo'.Basi kwa minajili hiyohiyo,haitokuwa ajabu kwa 'ndoa hii ya mkeka' kudumu muda mrefu kuliko inavyotarajiwa.

Muda utatanabaisha (time will tell).

11 May 2010




Gordon Brown has just announced on live tv that he is stepping down as the Prime Minister.It's now clear that the next PM shall be David Cameron.

. http://goo.gl/5bKK.

Shamsi Vuai Nahodha.Huyu ni Waziri Kiongozi huko Zanzibar.Naomba kukiri hadharani kuwa kwa muda mrefu nimekuwa nikimuona mwanasiasa huyu kama 'yupo yupo' tu.Unajua kuwa mwanasiasa au kiongozi kunapaswa kuendana na mchango wa namna flani kifikra au kimatendo.Nyerere hakumbukwi kwa vile tu alikuwa mwanasiasa au kiongozi bali jitihada na mchango wake kwa umma,hata kama baadhi ya maeneo alikosea (hiyo ni makala nyingine: ALIPOKOSEA NYERERE).
Pasipo kutarajia,Nahodha kanipa 'surprise ya nguvu'.Ameongea maneno ya busara sana kuhusu fikra potofu zilizotawala akilini mwa viongozi wengi wa CCM kuwa chama hicho kitatawala milele.Japo si dhambi kwa chama kutawala milele (kama inawezekana na kama kinakidhi matakwa ya kinaowaongoza),ni uzembe wa tafakuri kuamini kuwa CCM itatawala daima hasa kutokana na uswahiba wake na ufisadi,kauli za kibabe hata kwenye mwaka wa uchaguzi na kupuuza watu waliokiweka chama hicho madarakani.Sasa,Waziri Kiongozi Nahodha amewatahadharisha wana-CCM wenzake kwamba KUNA SIKU CCM ITANG'OLEWA.Hebu msome hapa chini
Nahodha: Iko siku CCM itang'olewa


• AKUMBUSHA WAJIBU WA VIONGOZI KWA WANANCHI
na Mwandishi Maalum, Mererani
WAZIRI KIONGOZI wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha amewataka wana CCM kuacha kujidanganya kwamba chama chao kitaendelea kutawala milele.
Nahodha, mmoja wa viongozi wa juu wa CCM na serikali alitoa kauli hiyo jana wakati akiwahutubia wananchi katika kituo cha kulelea watoto yatima cha Rafiki Child Care kilichoko Mererani wilayani Simanjiro mkoani Manyara.

Kiongozi huyo ambaye kimamlaka ni wa pili baada ya Rais Amani Karume katika SMZ aliwataka wana CCM kuachana na dhana kwamba chama chao hakiwezi kuondolewa madarakani na vyama vya upinzani.

“Ninatofautiana kimtazamo na watu wanaosema kwamba CCM itaendelea kutawala milele na milele, hapa kama hatutajipanga vizuri ipo siku chama chetu kitang’olewa madarakani…tusibweteke,” alisema Nahodha.

Waziri Kiongozi alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Katibu wa CCM wilaya ya Simanjiro, aliyetajwa kwa jina moja la Mujungu kuhutubia na kutamka kuwa, CCM haiwezi kuondolewa madarakani na vyama vya upinzani.

“Wapo wana CCM ambao kimtazamo wanaona sisi ndiyo wenyewe, kumbe wenye chama ni wananchi wanaowatawala. Tuna kila sababu ya kuwa makini katika utelezaji wa majukumu yetu… jambo hili nawaambia si kweli,” alisema Nahodha.

Akitoa mfano, Nahodha aliwataka wana CCM kujifunza kutoka katika nchi jirani ambako baadhi ya vyama vilivyopigania uhuru kama ilivyo CCM vimeng’olewa madarakani.

Alikitaja chama cha Kenya African National Union (KANU) ambacho kilipigania uhuru wa Kenya kuwa mmoja wa vyama vilivyopata kung’olewa madarakani.

“Kumbukeni namna ambavyo KANU ilisambaratika kule Kenya… leo hii imesahaulika kabisa. Lakini si huko tu, kule Zambia (UNIP) na Malawi (MCP) vyama tawala vilibwagwa vibaya na sasa vimesahaulika masikioni mwa wananchi,” alionya Nahodha.

Akiendelea, alisema ni wazi ipo siku wananchi wanaweza kukichoka CCM na kukibwaga iwapo viongozi watashindwa kutimiza ndoto za wananchi za kuwaletea maendeleo.

“Kuna mwanafalsafa mmoja mmoja anasema, msitafute uzuri wetu kwa kuangalia jinsi tulivyo, bali kwa kuangalia yale mema tuliofanya,” alisisitiza Nahodha.

Alisema uwajibikaji wa baadhi ya viongozi wanatokana na CCM ndani ya CCM unatia shaka inayoweza kuwafanya wananchi kukichukia chama hicho.

Alisema jukumu kubwa la viongozi wanaotokana na CCM ni kutekeleza majukumu yao kwa Watanzania kwa kuyafanya maisha yao yawe bora zaidi.

“Yuko mwanafalsafa mmoja wa zamani, aliwahi kusema maneno haya: ‘Tutakapokufa msitutafute katika makaburi yetu yaliyotengenezwa vizuri kwa chokaa bali mtutafute katika nyoyo za watu tuliowasaidia’. Ninawashauri viongozi wenzangu wa serikali na chama tuitumie sana busara ya mwana falsafa huyo,” alionya Vuai.

Katika hatua nyingine, Nahodha alieleza kusikitishwa na kuibuka kwa malumbano ya kisiasa miongoni mwa viongozi katika mkoa wa Manyara akisema hali hiyo haina faida kwa wananchi wanaowaongoza.

Kauli hiyo ya Nahodha iliyoonekana kuzungumzia na kukerwa na malumbano yaliyoibuka wiki iliyopita kati ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Henry Shekifu na Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka


Inaelekea habari kwamba raia mmoja wa India ameweza kuishi kimiujiza kwa kwa kutokula au kunywa chochote kwa miaka 70 sio fiksi bali ni kweli kabisa.Prahlad Jani ameimshangaza timu ya wanajeshi waliokuwa wakimchunguza kwa wiki 2 sasa kuthibitisha madai hayo.

Mtu huyo amekuwa chini ya uangalizi katika hospitali moja katika jimbo la Gujarat huku madaktari wakifuatilia kila jambo kwa kutumia kamera na CCTV.Kwa muda wote huo,hajawahi kula au kunywa chochote wala kwenda msalani.

"Bado hatufahamu ni namna gani anaweza kustahimili",anasema mtaalam wa mfumo wa fahamu Sudhir Shah alipoongea na waandishi wa habari baada ya uchunguzi huo."Bado ni muujiza usioweza kuelezeka kisayansi".

Prahlad,mwana-Yoga (Yogi) mwenye nywele ndefu na madevu aliwekwa hospitalini ili kuchunguzwa na taasisi ya utafiti na maendeleo ya ulinzi ya India (DRDO),ambapo ilitarajiwa kuwa matokeo ya uchunguzi huo yanaweza kusaidia kuwasaidia wanajeshi kumudu kuishi bila kula au kunywa chochote (kwa mfano wanapokuwa vitani),wanaanga na hata kuokoa maisha ya wengi yanapotokea majanga ya asili.

"Muda pekee Jani aligusa kimiminika ni wakati anasukutua na kuoga kwa vipindi maalum wakati wa uchunguzi huo",anasema G. Ilazavahagan,mkurugenzi wa taasisi ya ulinzi ya saikolojia na stadi shiriki (DIPAS).

Mtu huyo sasa amerejea kijijini kwake Ambaji,kaskazini mwa Gujarat,ambako ataendelea na taratibu zake za Yoga na uwazo (meditation).Anasema alipata karama alizonazo udogoni  kutoka kwa 'mungu wa kike' na tangu wakati huo amekuwa na uwezo wa ajabu.

Katika uchunguzi huo wa siku 15 uliohitimishwa Alhamisi iliyopita,madaktari walichukua vipimo (scans) vya viungo,ubongo na mishipa ya damu pamoja na vipimo (tests) vya moyo,mapafu na uwezo wake wa kufikiri.Matokeo zaidi ya uchunguzi wa vinasaba (DNA analysis),molekyuli za kibiolojia na vipimo vya homoni zake,enzymes na uzalishaji nishati mwilini (energy metabolism)  utatolewa hapo baadaye.

"Kama Jani hazalishi nishati ya mwili kutoka kwenye chakula na maji basi anapata nishati hiyo kutoka vyanzo vingine vinavyomzunguka kama vile mwanga wa jua",anaeleza Shah."Kama wataalam wa utabibu hatuwezi kufumbia macho uwezekano wa kuwepo vyanzo vingine vya nishati ya mwili zaidi ya kalori".

Habari hii imetafsiriwa kutoka AFP.

10 May 2010










Picha kwa Hisani ya Daily Mail

The British Prime Minister Gordon Brown has made a brief statement that he will stand down as Labour leader,and urged his party to start a process of electing his replacement.That means if the Conservative-Liberal Democrats power discussions on a possibility of  sharing deal bear no fruits,and the Liberal Democrats then agrees with Labour to form a a coalition government,the next PM might not be Gordon Brown,or David Cameron,for that matter.

Jambo moja nililojifunza kutoka kwa hawa wenzetu wa nchi zilizoendelea ni kile kinachoelezeka vizuri kwa kimombo kama not settling for less.Yaani,kwa tafsiri isiyo rasmi,ni kutokubali kuridhishwa na pungufu ya matarajio kamili.Kama ni mwanasiasa na wananachi wanaona 'unawazingua' basi usitarajie kuwa wataendelea 'kukulea'.Kama ni kwenye soka,wenye timu hawatarajii pungufu ya ushindi.

Baada ya matokeo yasiyoridhisha kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Alhamisi iliyopita,tayari 'bundi' mbaya ameshaanza kukiandama chama cha Labour.Baadhi ya wanasiasa ndani ya chama hicho wamejitokeza hadharani kutaka Gordon Brown atoswe kwa madai kuwa yeye ndio hasa chanzo cha matokeo mabaya kwenye uchaguzi huo ambapo Labour iliambulia nafasi ya pili nyuma ya chama cha wahafidhina (Conservative Party).

Japo hadi sasa Brown hajatamka kama ataachia ngazi uongozi wa chama hicho lakini dalili ni kwamba presha ikiendelea kuongezeka hatokuwa na jinsi zaidi ya kujiuzulu.Hapa sizungumzii u-waziri mkuu bali hali ya mambo ndani ya chama cha Labour.

Kukurejesha nyuma kidogo,Labour imekuwa na makundi mawili 'yasiyoiva' kwa kitambo kirefu sasa.Kwa upande mmoja ni wale wanaofahamika kama Blairites,ambao wanamhusudu Waziri Mkuu wa zamani Tony Blair,na kwa upande mwingine ni Brownites,ambao wanamhusudu Gordon Brown.Inasemekana kuwepo kwa makundi hayo kumechangia kwa kiasi flani matokeo mabaya ya chama hicho katika uchaguzi uliopita.Inadaiwa kwamba mmoja ya watu wenye nguvu kubwa ndani ya Labour,Lord Mandelson,alitumia kampeni za Brown na Labour kumuimarisha David Miliband,'Waziri' wa Mambo ya Nje wa Uingereza na chaguo la Blairites kumrithi Brown.Inaelezwa kwamba wakati Labour wanazindua kampeni zao kwa ajili ya uchaguzi huo,Mandelson (maarufu kama Malaika wa Giza-Angel of Darkness-ndani ya Labour)alifanikisha safari ya Miliband kwenda Marekani kwa mazungumzo na Rais Obama,fursa ambayo wachambuzi wa siasa wanaamini ingemwezesha Brown kuonekana kama kiongozi mwenye nguvu katika siasa za kimataifa.

Inadaiwa pia kuwa kampeni ya Brown iligeuzwa na Mandelson kuwa 'makao makuu ya Miliband' kwa maana kuwa ilikuwa ikitumika kwa namna flani kumpromoti mwanasiasa huyo (Miliband) ambaye bado ana ukaribu mkubwa na Blair.Hata meya wa zamani wa jiji la London,Ken Livingstone ameligusia hilo katika makala yake aliyoandika kwenye gazeti moja la Daily Mail.

Kwa sasa,harakati zinazoendelea chini chini ndani ya Labour ni za kumrithi Brown.Yani imekuwa kama ndugu za mgonjwa wanapoanza kugombania urithi kabla mgonjwa huyo hajaaaga dunia.Alosema siasa ni mchezo mchafu hakukosea.Baadhi ya majina yanayohusishwa na mpambano huo ni pamoja na akina Miliband,yaani David na mdogo wake Ed,ambaye ni waziri wa mazingira,Ed Ball- 'waziri' wa elimu na 'waziri' wa mambo ya ndani Alan Johnson.

Na akina Miliband  wanazua mvutano ambao unavuka anga za siasa kwa vile wakati David (pichani kushoto) ni Blairite,mdogo wake (kulia) ni Brownite.Inaelezwa kuwa tayari Ed ameshamfahamisha mama yao kuwa anadhamiria kupambana na kaka yake kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Labour.Hata hivyo,inaelezwa pia kuwa bado yuko njia panda kwa vile kwa upande mmoja Brownites wenzie wanamwona kama chaguo mwafaka kwa nafasi hiyo,lakini kwa upande mwingine 'damu ni nzito kuliko maji' na anatafakari kama pengine itakuwa jambo la busara kumsapoti kaka yake.

Tukiachana na mvutano huo wa kifamilia,'vita' kubwa inatarajiwa kuwa kati ya kaka yake (David) na (Ed) Balls.Wakati David anasifika kwa upeo na akili ya hali ya juu (ni Mwingireza mwenye asili ya Kiyahudi huyu) na ufahamu wake wa siasa za kimataifa hasa kutokana na wadhifa alionao sasa,Balls ana sapoti kubwa kwenye vyama vya wafanyakazi ambavyo kimsingi vina nguvu ya kutosha kwenye chama cha Labour.Kadhalika,wakati David anaonekana kama mtu wa 'tabaka la juu' Balls yuko karibu zaidi na wana-Labour wa ngazi za chini.

Tukiweka kando kidogo matatizo yaliyo ndani ya Labour kwa sasa,huko kwa wahafidhina nako mambo si shwari sana.Kuna wanaomuona mgombea wa chama hicho,David Cameron, kama amewaangushwa kwa kushindwa kwake kupata ushindi wa jumla (overall majority).Upinzani wa chini chini dhidi ya Camron haukuanza kwenye uchaguzi huu tu bali tangu alipoweka bayana dhamira yake ya kukibadilisha chama cha Conservative kutoka mwonekano wake kama 'chama kibaya' (nasty party) kwenda chama chenye kujumuisha makundi mbalimbali katika jamii.Kabla ya harakati za Cameron,chama hicho kimekuwa kikitafsiriwa kama 'cha Waingereza Weupe wa tabaka la juu' na kinachokumbatia zaidi mabwanyenye kuliko watu wa kawaida.

Cameron amefanikiwa kwa kiasi flani kubadili taswira hiyo japo si sana.Katika uchaguzi uliopita alihamasisha uteuzi wa baadhi ya wagombea kutoka makundi ambayo kimsingi 'hayamo kwenye akili za chama hicho' kwa mfano wagombea kutoka jamii ndogo za wasio weupe (ethnic minority),shoga na mabinti kadhaa.Japo baadhi ya wagombea hao wameshinda,wengi wao wamefanya vibaya na tayari baadhi ya wahafidhina wanamlaumu Cameron kwa uamuzi huo wa 'kuwapigia debe wageni wa tamaduni za chama hicho'.

Jingine linalomwandama Cameron ni mchango wa kundi dogo la washauri wake wanaofahamika kama 'wana-Eton wa zamani' (ex-Etonian),yaani marafiki zake wa karibu aliosoma nao katika shule ya Eton yenye hadhi ya juu kabisa na chaguo la 'wateule wachache' kwa hapa.Hao ni pamoja na Kansela ('waziri wa fedha') kivuli George Osborne na mwanamikakati anayesifika kwa akili nyingi Oliver Letwin (ambaye pia ni 'waziri' kivuli).Wengine wanaotuhumiwa 'kumshika akili' Cameron ni pamoja na kiongozi wa zamani wa Conservative,William Hague,na Mkurugenzi wa Mawasiliano,Andy Coulson (ambaye kabla ya kuchukua wadhifa huo alikuwa mhariri wa gazeti maarufu kwa udaku la News of The World).Coulson anafahamika kwa uwezo wake katika 'kutengeneza fitna,majungu na kummaliza mtu' (maeneo yanayolipa umaarufu News of the World).

Washauri hao wa Cameron wanatuhumiwa 'kumshauri vibaya' mgombea hasa katika wazo la 'jamii kubwa' (Big Society) ambalo inaelezwa kuwa liliasisiwa na Letwin.Wakosoaji wanadai kuwa wazo hilo halikueleweka kwa wapiga kura na wengine wanakwenda mbali zaidi na kulieleza kama 'wazo muflisi'.Vilevile,inaelezwa kuwa  Lord Ashcroft,'kibopa' aliyemwaga fedha nyingi kwa minajili ya Conservative kushinda uchaguzi huo,hajaridhishwa na matokeo ya uchaguzi huo,sambamba na 'kushindwa' kwa Cameron kusimama kidete kumtetea mhafidhina huyo tajiri (Ashcroft) alipoandamwa na skandali ya 'hadhi ya raia asiyelipa kodi kutokana na ukazi wake nje ya nchi' (non-domicile status).Lord Ashcroft anaamini kuwa suala hilo limechangia kupunguza kura za chama chao na anaamini kuwa Cameron angeweza kumtetea vizuri zaidi ya alivyofanya.Kadhalika,tajiri huyo anadaiwa kutopendezwa na wazo la Cameron kushiriki midahalo ya uchaguzi kwenye runinga,ambapo anaona kuwa ilisaidia kumuimarisha mgombea wa chama cha Waliberali (Liberal Democrats) Nick Clegg na hivyo 'kula' kura za Conservatives.

Nitaendelea kuwahabarisha kinachojiri kwenye anga za siasa za hapa kadri muda utavyoruhusu.

7 May 2010

Matokeo ya Uchaguzi Mkuu hapa Uingereza yametuacha baadhi yetu tukiwa na majonzi baada ya chama tawala cha Labour kuambulia nafasi ya pili (viti 258) huku chama cha wahafidhina (Conservatives) waikibuka mshindi kwa kupata viti 307 (japo ni pungufu ya viti 19 kwa viti 326 vinavyohitajika kuunda serikali ya peke yao).Chama cha kiliberali (Liberal Democrats) kimeshika nafasi ya tatu kwa kuambulia viti 57.

Kila mwenye majonzi kutokana na matokeo mabaya kwa Labour ana sababu zake binafsi.Zangu ni za kibinafsi zaidi (na mambo binafsi yanapaswa kubaki binafsi).Lililo bayana ni kwamba Labour haikushindwa kwa vile ni chama kibaya au kimeboronga wakati wa utawala wake.Hapana.Tofauti kati ya hawa wenzetu na akina sie na CCM yetu ni kwamba haitoshi kuwa umefanya vizuri tu bali watu wanataka vizuri zaidi kama sio vizuri kabisa.Bahati mbaya kwa Labour ni mtikisiko wa uchumi wa dunia ambao kama ulivyoathiri sehemu nyingine ulimwenguni,umepelekea idadi kubwa tu ya Waingereza wakiwa hawana ajira sambamba na ugumu wa wastani wa hali ya maisha.Kwa lugha nyingine,hali hiyo ya uchumi (ambayo kimsingi haikusababishwa na Labour) imechangia chama hicho kuangushwa na wahafidhina.

Hadi dakika hii haijafahamika nani atakuwa Waziri Mkuu kutokana na kanuni na taratibu za uchaguzi za hapa.Tofauti na huko nyumbani ambapo wingi wa kura unatafsiri ushindi wa moja kwa moja kwa chama husika,kwa hapa ili chama kiweze kuunda serikali kinapaswa kushinda viti 326.

Nitachambua zaidi baadaye kuhusu uchaguzi huu na namna Watanzania wanavyopaswa kujifunza kwa ajili ya uchaguzi wetu hapo Oktoba mwaka huu.Ila kuna habari ya 'kuliwaza' inayokihusu chama cha kibaguzi cha BRITISH NATIONAL PARTY (BNP) ambapo mwenyekiti wake Nick Griffin ameshindwa kumuangusha mgombea wa Labour,Margaret Hodge, katika eneo la Barking lililopo mashariki mwa jiji la London.

Habari njema zaidi ni kwamba BNP imepoteza viti vyote 12 ilivyokuwa inashikilia kwenye manispaa ya Barking and Dagenham jijini London.Pengine hili linaweza kutafsiriwa kama tamko la Waingereza dhidi ya siasa za kibaguzi.BNP ilitumia suala la uhamiaji kama ajenda yake kuu kwenye uchaguzi huo lakini ni dhahiri kuwa matokeo hayo yatafikisha ujumbe kwao kuwa watu wenye akili timamu hawaafikiani na ushenzi wa wabaguzi hao.

Mengi,baadaye.Kwa sasa tusubiri matokeo ya majadiliano ya simu katika ya mgombea wa wahafidhina,David Cameron na kiongozi wa waliberali Nick Clegg yanayotarajiwa baadaye leo kuangalia uwezekano wa ushirikianio kati ya vyama hivyo.Wakiafikiana,Cameron atafanikiwa kuwa Waziri Mkuu.Lakini kama Clegg ataamua kushirikiana na Labour basi Gordon Brown ataendelea kushikilia wadhifa wake.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.