22 Dec 2016

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
IJUMAA iliyopita, kulijitokeza tukio ambalo hadi wakati ninaandika makala hii limezua utata. Usiku wa siku hiyo, Rais Dk. John Magufuli alitengua wadhifa wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Maradhi ya Binadamu (NIMR), Dk. Mwele Malecela.
Siku moja kabla, Dk. Mwele alizungumza na waandishi wa habari kuwaeleza kuhusu matokeo ya utafiti wa takriban mwaka mzima kati ya NIMR na Chuo Kikuu cha Bugando kuhusu ugonjwa huo na ilibainika kuwa kati ya sampuli za damu 533, 88 zilikutwa na virusi vya ugonjwa wa zika.
Hata hivyo, siku iliyofuata, serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto ilitoa taarifa kuwa ugonjwa huo haujaingia nchini, kana kwamba taarifa ya Dk. Mwele ilizungumzia kuingia kwa ugonjwa huo.
Pengine kabla ya kuingia kwa undani katika kujadili suala hili, ni vema niweke bayana ukweli kuwa Dk. Mwele ni dada-rafiki yangu, na nimesikitishwa sana na tukio hilo, hususan jinsi wadhifa wake ulivyotenguliwa.
Ni kwamba, wakati taarifa ya wadhifa wake kutenguliwa ilitolewa usiku wa Ijumaa iliyopita, saa chache baadaye, Jumamosi asubuhi, kukatangazwa uteuzi wa Profesa Yunus Mgaya kuchukua wadhifa ulioachwa wazi na Dk. Mwele.
Kama nilivyoeleza awali, hadi wakati ninaandika makala hii kuna utata unaoendelea kuhusu suala hilo. Hiyo imetokana na vitu kadhaa. Kwanza, taarifa ya Ikulu kuhusu uamuzi wa Rais Magufuli kutengua ukurugenzi wa Dk. Mwele haikueleza kwa nini rais alichukua uamuzi huo, tena usiku.
Kadhalika, utata huo unachangiwa na hisia kuwa huenda ‘siku za Dk. Mwele zilikuwa zinahesabika,’ kwani katika mazingira ya kawaida, sio rahisi mkurugenzi wa taasisi nyeti kama NIMR kuondolewa madarakani usiku kisha mbadala wake akapatikana asubuhi.
Hisia hizo zinachangiwa pia na ukweli kuwa Dk. Mwele ni mtoto wa Waziri Mkuu wa zamani, mzee John Malecela. Miezi minane iliyopita, familia ya mwanasiasa huyo mkongwe ilikumbwa na ‘balaa’ kama hili, ambapo Rais Magufuli alimwondoa madarakani mke wa mzee Malecela, mama Anne Kilango, aliyekuwa mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Tofauti na wadhifa wa Dk. Mwele ulivyotenguliwa bila maelezo, tukio la mama Kilango liliambatana na maelezo kwamba alitangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mkoa wake hauna watumishi hewa jambo ambalo lilisababisha Ikulu kufanya uchunguzi wake na kubaini wafanyakazi hewa 45 katika awamu ya kwanza huku awamu ya pili ya uchunguzi bado ukiendelea.
Katika mazingira ya kawaida, huwezi kumlaumu mtu anayeweza kuhoji “tatizo lilikuwa utendaji kazi wa mama Kilango na Dk. Mwele au ‘mlengwa’ ni mzee Malecela?”
Wasomi kadhaa waliozungumzia hatua ya rais dhidi ya Dk. Mwele wameonyesha kushangazwa kwao, hasa ikizingatiwa kuwa rais naye ni miongoni mwa wasomi. Kwamba, alichofanya Dk. Mwele ni kuripoti tu matokeo ya utafiti husika, lakini kukajitokeza mkanganyiko katika tafsiri ya ripoti ya matokeo hayo.
Laiti busara ingetumika, basi Dk. Mwele angefahamishwa tu kuwa taarifa yake imezua mkanganyiko, na angeitisha mkutano na waandishi wa habari kutoa ufafanuzi. Ikumbukwe kuwa dada huyo ni mmoja wa wanasayansi wachache kabisa kutoka Afrika na hususan Tanzania wanaoheshimika mno kimataifa.
Japo sijapata idhini yake ‘kutoa siri hii,’ mwishoni mwa mwaka jana alinieleza kuwa anahitajiwa na taasisi moja ya kimataifa inayohusiana na masuala ya afya duniani, lakini akasema hayupo tayari kuacha kuwatumikia Watanzania wenzake. Binafsi nilimshauri akubali tu nafasi hiyo kwa vile atakapoitumikia dunia, atakuwa akiitumikia Tanzania pia. Hata hivyo, Dk. Mwele alikataa nafasi hiyo.
Vile vile, baada ya jina lake kutopitishwa kuwania kuteuliwa katika nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM mwaka jana, Dk. Mwele alielekeza nguvu zake kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa, Dk. Magufuli na kila jioni alitumia muda wake baada ya kazi kufanya ‘majukumu ya kisomi’ katika kampeni za chama chake. Na licha ya kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, baadhi ya vijana aliowakabidhi majukumu ya kampeni za Dk. Magufuli hawajalipwa stahili zao hadi leo (licha ya Dk. Mwele kufuatilia suala hilo kwa zaidi ya mwaka sasa). Linganisha hilo na makada ‘waliozawadiwa’ nafasi mbalimbali licha ya kampeni zao ndani au nje ya chama dhidi ya Dk. Magufuli alipokuwa mgombea.
Mwaka jana nilipata fursa ya kuandika wasifu wake kwenye blogu yangu. Pamoja na mengineyo mengi, alieleza kuwa tangu alipokuwa binti mdogo alikuwa na ndoto ya kuwa mtafiti wa maradhi. Na licha ya kuwa mtoto wa waziri mkuu, ambapo alikuwa na fursa ya ‘kufanya chochote atakacho,’ alifuata ndoto yake ya kitaaluma na kitaalamu, akatumia muda mwingi ‘vichakani na misituni’ kujifunza kuhusu maradhi mbalimbali ya binadamu. Kwa hakika, safari yake tangu utotoni hadi kupata shahada ya uzamivu na hatimaye kuwa mkurugenzi mkuu wa kwanza wa kike wa NIMR, inatoa hamasa kubwa.
Kuna wanaoona kuvuliwa madaraka kwa Dk. Mwele ni kama mwendelezo wa kile kilichomkumba aliyekuwa Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru, ambaye kutenguliwa kwa wadhifa wake hivi karibuni kunatafsiriwa kama matokeo ya yeye kutoa maoni yake ya kitaalamu kuhusu suala fedha za taasisi za serikali kuwekwa kwenye akaunti za muda maalumu (fixed deposits).
Nihitimishe makala hii kwa kumpa pole Dk. Mwele huku nikiamini kuwa muda si mrefu ataipatia fahari Tanzania kama mwanasayansi wa kimataifa. Kadhalika, inasikitisha kuona tukio hili ilhali majuzi tumeshuhudia teuzi za baadhi ya mabalozi zikifanywa kwa kigezo cha ukada

15 Dec 2016


KATIKA toleo la Oktoba 20, 2016 la gazeti hili niliandika makala iliyokemea madai ya uongo yaliyokuwa yakisambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu elimu ya Rais Dk. John Magufuli. Kwa mujibu wa madai hayo, shahada ya uzamifu ya kiongozi huyo ilikuwa feki, na kama sio feki basi athibitishe hadharani.
Binafsi nilikerwa sana na madai hayo. Nilijaribu kuyakemea huko kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook, kwa kuwashauri wenye kuhitaji uthibitisho wa elimu ya Dk. Magufuli waende Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, taasisi ambayo ndiyo ilimtunuku shahada hiyo kiongozi huyo.
Hata hivyo, ushauri huo haukupokelewa vema na kada wa Chadema, Ben Saanane, aliyekuwa mstari wa mbele kumtaka Dk. Magufuli ahakiki PhD yake. Badala ya kuzingatia ushauri kuwa kuna njia rahisi ya kusaka ukweli kuhusu suala hilo, kijana huyo alitumia lugha isiyopendeza dhidi yangu.
Baada ya kuona suala hilo linazidi kupamba moto hasa huko Facebook, nikaamua kuandika makala katika gazeti hili toleo la Oktoba 20 mwaka huu. Katika makala hiyo, niliepuka kutaja jina la mhusika mkuu katika madai hayo ya uongo dhidi ya elimu ya rais wetu.
Katika toleo la wiki iliyofuata (Oktoba 27, 2016), kada maarufu wa Chadema Ben Saanane alijitokeza kujibu makala hiyo, huku akidai kuwa ni haki kuhoji elimu ya Dk. Magufuli. Licha ya kutumia mifano mingi ya watu mbalimbali maarufu ‘waliofeki’ taaluma zao, Saanane hakuweza kuthibitisha madai yake kuwa PhD ya Magufuli ni feki pia.
Japo mara zote nimekuwa nikikwepa kujibishana na wasomaji wa makala zangu, ilinilazimu kujibu makala ya Saanane kwa vile ilinitaja moja kwa moja. Nilifanya hivyo katika toleo la gazeti hili la Novemba 3, 2016. Katika makala hiyo nilieleza bayana kuwa tatizo la madai ya kada huyo wa Chadema na wenzake sio kuhoji kuhusu elimu ya Rais bali kumtuhumu Rais kuwa PhD yake ni feki. Basi angalau yeye na wenzake wangejihangaisha kuonyesha ‘ukweli’ wa tuhuma zao badala ya kumtaka Rais athibitishe kuwa ‘tuhuma hizo dhidi yake ni za uongo.’
Wiki iliyopita, zilipatikana taarifa kuwa kada huyo ‘hajulikani alipo kwa zaidi ya wiki tatu sasa.’ Hadi wakati ninaandika makala hii, jitihada zilikuwa zinaendelea kumtafuta kada huyo. Hata hivyo, pengine kwa vile Saanane ‘alishikia bango’ tuhuma kuwa PhD ya Dk. Magufuli ni feki, tayari ‘kupotea’ kwake kunahusishwa na tuhuma zake hizo.
Wakati ninaungana na familia ya Saanane na makada wenzake wa Chadema kumwombea awe salama, kuna vitu viwili muhimu vya kuzingatia. Kwanza, wakati Saanane ‘alipojipa uhuru wa kudhalilisha elimu ya Rais,’ makada wenzake hawakuona haja ya japo kumsihi apunguze ukali wa lugha yake dhidi ya kiongozi mkuu wa nchi. Badala yake walimmwagia sifa, huku wakimshambulia kila aliyejaribu kumsihi kada huyo asitumie lugha isiyofaa.
Hili ni tatizo sugu katika mitandao ya kijamii. Kuna wenzetu wakiwa mtandaoni wanajiona kama majabali fulani, wenye uhuru wa kudhalilisha watu, kutukana watu, kunyanyasa watu na tabia mbaya kama hizo. Watu hawa hutumia kisingizio cha ‘uhuru wa kujieleza’ huku wakipuuza haki ya kila mtu kuheshimiwa. Uhuru wa kufanya jambo bila kujali kuwa linakiuka haki za wengine ni uhuni.
Pili, kuna mkanganyiko mkubwa kuhusu ‘kupotea’ kwa kada huyo. Inaelezwa kuwa ‘alipotea’ katikati ya mwezi uliopita, lakini taarifa kuhusu ‘kupotea’ kwake zimeibuka zaidi ya wiki tatu baadaye. Licha ya wadhifa wa Mkuu wa Sera na Utafiti wa Chadema, Saanane alikuwa pia ‘msaidizi binafsi’ (Personal Assistant) wa mwenyekiti wa taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe. Hadi wakati ninaandika makala hii, si Mbowe au kiongozi yeyote wa ngazi za juu wa chama hicho aliyetoa tamko kuongelea suala hilo.
Kuna wanaohoji, hivi inawezekana kweli msaidizi binafsi wa mwenyekiti wa taifa wa chama kikuu cha upinzani ‘apotee kwa zaidi ya wiki tatu’ lakini kiongozi husika asionekane kuguswa na tukio hilo? Kwa nini ‘wanaomtafuta’ Saanane wasiubane uongozi wa juu wa Chadema, ambao ‘ukimya’ wake katika suala hilo ni kama unaashiria kufahamu alipo kada huyo?
Nihitimishe makala hii, kwanza, kwa kuutaka uongozi wa Chadema kitaifa kujitokeza kuongelea suala hili (kama lina uzito stahili kwao), sambamba na Jeshi la Polisi kusaidiana na wahusika kumsaka kada huyo

9 Dec 2016

Leo ni siku ya Uhuru wa nchi yetu, tunatimiza miaka 55 kama taifa huru. Siku kama ya leo, miaka 55 iliyopita, Tanganyika ilikabidhiwa uhuru wake kutoka kwa Mwingereza. Japo kuna wanaohoji iwapo tupo huru kweli, kwa leo tusherehekee tukio hilo la mkoloni kutukabidhi nchi yetu.

Pia siku ya leo ni siku yangu ya kuzaliwa. Ninamshukuru Mungu kwa kila kitu. 


Ninawashukuru pia wazazi wangu ambao japo ni marehemu kwa sasa, kiroho nipo nao siku zote: marehemu baba Mzee Philemon Chahali na marehemu mama Adelina Mapango. Bwana Mungu awajalie pumziko la milele na mwanga wa milele awaangazie mpumzike kwa amni. Amen. Naishukuru familia yangu hasa dadangu Sr Maria-Solana Chahali na wadogo zangu mapacha Peter (Kulwa) na Paul (Doto). Naomba Bwana Mungu atujalie maisha marefu zaidi, afya njema na mafanikio katika shughuli zetu za kila siku.

Katika maadhimisho haya ya siku yangu ya kuzaliwa, ninatoa zawadi ya kopi za bure za kitabu changu hicho pichani chini.



BONYEZA HAPA kuki-download BURE

8 Dec 2016


KESHOKUTWA, Desemba 9, Tanzania itatimiza miaka 55 tangu ipate uhuru. Siku hiyo hiyo, nami nitatimiza miaka kadhaa tangu nizaliwe. Naam, mimi na nchi yangu ‘tulizaliwa tarehe inayofanana’ japo katika miaka tofauti.
Nijiongelee mwenyewe kwanza. Wakati kwa watu wengi, siku zao za kuzaliwa huandamana na sherehe na chereko mbalimbali, maadhimisho ya siku yangu ya kuzaliwa huwa ni ibada – kumshukuru Mungu kwa kuniweka hai na baraka nyingine anazonijalia – na kufanya tafakuri ya wapi nimetoka, nilipo na ninapoelekea.
Moja ya mafanikio makubwa kwangu kwa mwaka huu ni uamuzi niliouchukua Aprili Mosi kuachana na moja ya tabia hatari kabisa maishani ya uvutaji wa sigara. Hadi nilipochukua uamuzi huo, tabia hiyo hatari kiafya na kiuchumi ilikuwa na ‘umri’ wa miaka ishirini na ushee.
Katika kusherehekea siku yangu ya kuzaliwa, nimeamua kugawa bure kitabu changu cha kielektroniki, kinachoitwa “Mwongozo wa Kitabibu wa Jinsi ya Kuacha Sigara na Ushauri wa Mvutaji Mstaafu.” Ni mwendelezo wa utamaduni mpya, ambapo zamani tulizoea kuona wanaosherehekea siku za kuzaliwa wakizawadiwa, lakini sasa namna maarufu ya kuadhimisha sherehe hiyo ni kutoa zawadi.

Hiyo ni kwa upande wangu. Sijui ‘mwenzangu’ Tanzania atakuwa na ‘zawadi’ gani ya kutupatia katika maadhimisho yake ya siku ya kuzaliwa. Hata hivyo, siku chache kabla ya siku hizo, kuna jambo moja ambalo linaonekana kugusa hisia za wengi. Nalo ni uteuzi wa mabalozi wapya ulifanywa na Rais Dk. John Magufuli wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa baadhi ya vyombo vya habari, uteuzi wa makada waandamizi wa chama tawala CCM umetafsiriwa kuwa ni ‘hesabu za kisiasa.’ Sina hakika hesabu hizo zina malengo gani, lakini nahisi labda ni Magufuli analenga kujiimarisha katika uongozi wake kama Mwenyekiti wa Taifa wa CCM.
Kama hilo ni kweli, basi uteuzi huo wa makada sio habari njema kwetu sisi wenye matarajio ya kuona teuzi mbalimbali zikifanywa kulingana na uwezo wa kutekeleza majukumu au uchapakazi na sio ukada.
Pengine nitumie fursa hii kukumbusha kuwa kuna wimbi kubwa la mabadiliko linaloendelea duniani, hususan huku nchi za Magharibi. Muda mfupi kabla sijaanza kuandika makala hii, Austria imenusurika kuwa taifa la kwanza kurejea kuwa chini ya utawala wa mrengo mkali kabisa wa kulia. Hofu kuwa mgombea urais Norbert Hofer wa chama chenye mrengo mkali wa kulia cha Freedom Party angeshinda ilipotea baada ya mchakato wa kupiga kura kumalizika, na mgombea binafsi Alexander Van der Bellen kushinda kwa asilimia 53. Lakini muda mfupi baada ya habari hiyo njema kutoka Austria, mambo hayakwenda vizuri nchini Italia, ambapo Waziri Mkuu Matteo Renzi alishindwa kwenye kura ya maoni ya mabadiliko ya katiba ya nchi hiyo, na kulazimika kujiuzulu. Wapinzani wake katika kura hiyo walikuwa ni pamoja na chama chenye mrengo mkali wa kulia cha Northern League na kile cha upinzani wa tabaka tawala (anti-establishment) cha Five Star Movement (F5S).
Sasa macho yanaelekezwa huko Ufaransa na baadaye Ujerumani na Uholanzi ambako kwa nyakati tofauti watakabiliwa na kazi ya upigaji kura. Mtihani mkubwa katika nchi hizo ni jinsi ya kukabiliana na wimbi linalozidi kukua la upinzani dhidi ya tabaka tawala na mfumo wa utawala unaoonekana kutosikiliza sauti za wananchi wa kawaida. Kwa bahati mbaya, wimbi hilo lipo mikononi mwa vyama vya siasa za mrengo mkali wa kulia na vya kibaguzi.
Katika mazingira kama hayo tunahitaji mabalozi wanaoelewa kwa nini wametumwa kutuwakilisha huko nje, na sio wanaojua wameteuliwa kutokana na nafasi zao za kisiasa nchini.
Na wiki chache kabla ya maadhimisho ya miaka 55 ya uhuru wetu, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Serikali ya Mapinduzi Dk Mohammed Ali Shein alisaini sheria inayofanya masuala ya mafuta na gesi ya Zanzibar kuwa sio suala la Muungano, hatua ambayo ni uvunjifu wa Katiba mchana kweupe. Hilo limefanyika kwa vile Shein na SMZ wanajua hakuna mwanasiasa kutoka Bara mwenye jeuri ya kugusia suala hilo, ikiwa ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk. Magufuli.
Lakini pamoja na hayo, Tanzania yetu itasherehekea miaka 55 ya kuzaliwa kwake ikiwa nchi yenye amani, angalau amani kwa maana ya kutokuwa vitani au kwenye machafuko. Kazi kubwa kwa watawala wetu ni kutumia nguvu zao zote kuhakikisha kuwa amani hiyo inadumishwa kwa nguvu zote.
Happy birthday Tanzania.

7 Dec 2016

ANGALIZO: Makala hii ilipaswa kuchapishwa katika toleo la wiki iliyopita la gazeti la Raia Mwema lakini haikuchapishwa kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu.

Mwanzoni mwa mwezi huu, Rais Dokta John Magufuli alitimiza mwaka kamili tangu aapishwe kuwa Rais wa tano wa nchi yetu. Nyingi ya tathmini mbalimbali zilizofanyika kuhusu mwaka wake mmoja wa urais zilionyesha anafanya kazi nzuri.

Hata hivyo, tukifuatilia kwa karibu utendaji kazi wa Rais, twaweza kubaini kuwa baadhi ya mawaziri wake hawaendani na kasi yake. Katika mazingira ya kawaida, Rais angelazimika kuchukua hatua pale tu hatua stahili zisingewezekana kufanywa na mawaziri wake.

Japo wanachohitaji wananchi ni kuona serikali inachukua hatua stahili, lakini suala la mtendaji gani wa serikali anayechukua hatua husika linaweza kueleza kiwango cha ushirikiano na uchapakazi kwa pamoja.

Na kwa ‘kusubiri hadi Rais achukue hatua’ kuna uwezekano wa kujengeka taswira kuwa ‘Rais anaingilia kazi za watendaji wake,’ au mbaya zaidi ni pale maagizo yake yatapokutana na upinzani wa namna flani.

Mfano mzuri ni hatua ya majuzi ambapo Rais aliitumbua Bodi ya Mamlaka ya Mapato (TRA).  Baadaye alieleza kuwa Bodi hiyo iliyokuwa na watendaji hao wakuu wa idara na taasisi za Serikali ilifanya dhambi ya kuidhinisha uamuzi wa menejimenti kuweka mabilioni ya shilingi katika benki za binafsi.

Juzi hapa tumekuta Sh26 bilioni zilizokuwa zimetolewa TRA kwa ajili ya matumizi ya TRA zikapelekwa kwenye mabenki matatu kama ‘fixed deposit account’ na bodi ikapitisha. Ndiyo maana nilipozipata hizo hela; hela nikazichukua na bodi kwaheri,” Rais alikaririwa

Swali hadi hapo ni je Waziri husika na wasaidizi wake walikuwa wapi wakati hayo yanatokea? Je inawezekana maamuzi hayo ya menejimenti na Bodi ya TRA yalikuwa na baraka za Waziri husika, na ndio maana hakuna hatua zilizochukuliwa hadi Rais alipoingilia kati?

Miongoni mwa wajumbe wa Bodi iliyotumbuliwa ni Gavana wa Benki Kuu, Profesa Benno Ndulu, ambaye wiki iliyopita alinukuliwa akitoa kauli inayokinzana na msimamo wa Rais. Gavana Ndulu alidai kuwa TRA kuweka fedha kwenye fixed accounts sio kosa kisheria, na hakuna hasara kiuchumi kuweka fedha kwenye akaunti ya aina hiyo.

Kwa tunaojua ‘kusoma katikati ya mistari’ Tunaelewa bayana kuwa Gavana Ndulu alikuwa anamjibu Rais Magufuli. Na pengine sio kumjibu tu bali kumkosoa. Na hii si mara ya kwanza kwa ‘kiongozi huyo wa benki kuu kupishana lugha na Rais.’ Mwezi Machi mwaka huu Dkt Magufuli alifanya ziara ya kushtukiza huko Benki Kuu, ambapo pamoja na mambo mengine, alitoa agizo kwa Gavana Ndulu kupitia upya orodha ya wafanyakazi wa Benki hiyo, na kuwaondoa mara moja wale wote ambao hawana ulazima wa kuwa wafanyakazi katika benki hiyo.

Siku chache baadaye, Gavana huyo alinukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa orodha yenye majina 14 ya ‘watoto wa vigogo’ iliyokuwa ikisambaa kwenye mitandao ya kijamii ‘haina jipya.’ Hata hivyo alieleza kuwa agizo la Rais kuhusu kupunguza wafanyakazi lingejadiliwa kwenye vikao vya taasisi hiyo na taarifa rasmi ingetolewa. Kwa kumbukumbu zangu, hadi leo hakujatolewa taarifa yoyote.

Wakati akieleza kuhusu sababu zilizopelekea kuvunja Bodi ya TRA, Rais pia aliionya Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwamba imepewa zaidi ya shilingi bilioni 30 na “badala ya kuzipeleka kwenye miradi ya elimu kama kujengea madarasa na kusaidia masuala mengine ya elimu nchini lakini wameamua kuweka kwenye fixed account wakati kuna miradi ya elimu imesimama kwa kukosa pesa.

Na hapa tena tunapaswa kujiuliza, Waziri husika (na wasaidizi wake) yupo wapi? Au hapa pia, uamuzi huo wa Mamlaka hiyo una baraka za Waziri husika ndio maana haikuchukua hatua hadi Rais alipoingilia kati?

Tukiweka kando hilo la ‘kila jambo kusubiri hadi Rais achukue hatua,’ maamuzi ya baadhi ya mawaziri yanaweza ‘kumgombanisha’ kiongozi huyo mkuu wa nchi na sie wananchi anaotuongoza. 

Wiki mbili  zilizopita, Waziri wa Sheria na Katiba, Dokta Harrison Mwakyembe, ‘alilipuka’ kwa kutangaza kuwa serikali ina mpango wa kuwatimua kazi mahakimu wote wa mahakama ya mwanzo wenye elimu ya cheti na diploma. Waziri huyo ambaye ni mwanasheria kitaaluma, alisema, “Tunahitaji mahakimu wenye uwezo wa sheria ambao wamehitimu shahada ya kwanza, hivyo serikali itawafuta kazi mahakimu wote wenye elimu ya cheti na diploma.”

Tungetegemea kuwa kiongozi msomi kama Dkt Mwakyembe angetambua bayana athari za tamko hilo kwa ari na tija wa mahakimu wa mahakama za mwanzo, wengi wao wakiwa wanafanya kazi katika mazingira magumu na hatarishi. Tamko hilo la Mwakyembe linaweza kupelekea mahakimu kuamua “serikali inataka kumwaga ugali, basi nasi tutamwaga mboga.”

Lakini hata tukiweka kando athari za tamko hilo kwa ari na tija ya mahakimu wa mahakama za mwanzo, kwanini Mwakyembe na wenzake hawakuzingatia busara kwamba elimu pekee sio kigezo cha ufanisi wa mwajiriwa bali pia uzoefu ni muhimu kwenye utaalamu.

Kwahiyo, serikali yenye busara ingeandaa mazingira ya kuwahamasisha mahakimu hao kujiongezea viwango vya elimu wakiwa kazini, hususan kwa kusaka shahada ya sheria kupitia Chuo Kikuu Huria.

Tukio jingine linaloashiria kuwa baadhi ya watendaji wa Dkt Magufuli 'wanamwangusha' ni sakata kati ya serikali ya jiji la Mwanza na wamachinga. Kwa mara nyingine tena, tumeshuhudia ikilazimu Rais kuingilia kati na kumuru kuwa wamachinga waliokuwa wakibughudhiwa huko Mwanza wasisumbuliwe tena.

Hapa pia waweza kujiuliza kuhusu Waziri husika. Alikuwa usingizini kiasi cha kutofahamu kilichokuwa kinaendelea Mwanza hadi imlazimu Rais kuingilia kati? Au Waziri huyo aliridhia kuhusu unyanyaswaji wa wamachinga na ndio maana hakuchukua hatua stahili?

Kuna suala la kiwanda cha Dangote. Kauli za mawaziri husika na watendaji wengine wa serikali zimekuwa sawa na 'kujiumauma.' Sio ngumu kuhisi kuwa 'kuna namna' katika sakata hilo ambalo miongoni mwa atahri zake ni pamoja na kupotea kwa ajira za Watazania wenzetu zaidi ya 1,000.

Kwa jinsi mazingira yalivyo ambapo 'kila kitu lazima kimsubiri Rais,' yayumkinika kuhisi kuwa ufumbuzi pekee wa sakata hilo a Dangote utapatikana kwa Rais kuingilia kati. 

Wakati watendaji 'wanaomwangusha' hawawezi kuwa na kisingizio zaidi ya aidha uzembe wao au hujuma dhidi ya Rais, kwa uapnde mwingine Rais naye anaweza kubeba lawama kwa kuyavumilia majipu yanayomzunguka.


Nihitimishe makala hii kwa kutarajiwa kuwa Rais Magufuli atawakumbusha watendaji wake majukumu yao ili kuondoa taswira ya ‘kila kitu mpaka aje Rais,’ sambamba na kuwakumbusha kutumia busara hasa pale wanapotoa kauli zinazoweza kujenga chuki kati ya ‘waathirika’ wa kauli hizo na serikali


Barua-pepe: [email protected] Blogu: www.chahali.com Twitter: @chahali  




24 Nov 2016


KAMA nilivyoahidi katika toleo lililopita la gazeti hili, wiki hii ninaendelea na uchambuzi kuhusu uchaguzi wa Rais wa Marekani uliofanyika wiki mbili zilizopita na kushuhudia mgombea wa chama cha Republican, Donald Trump, akiibuka mshindi dhidi ya mpinzani wake mkuu, Hillary Clinton wa Democrat.

Makala yangu katika toleo la wiki iliyopita ilibeba swali ‘je Trump atabadilika?” Swali hilo lilitokana na ukweli kwamba kauli za Trump na tabia yake kwa ujumla, kabla ya kuwa mgombea, akiwa katika mchakato wa chama chake kupata mgombea, na wakati wa kampeni kama mgombea wa chama chake, zilisheheni kasoro lukuki; ubaguzi dhahiri wa kidini, unyanyasaji wa wanawake na dhihaka kwa walemavu, kupandikiza chuki dhidi ya Wamarekani wasio weupe, chuki dhidi ya wageni, na mengineyo mengi yaliyoibua wachambuzi wa siasa kutodhani kuwa Trump angeweza kushinda katika uchaguzi huo.
Lakini tatizo halikuwa kwa Trump pekee bali pia watu waliomzunguka na baadhi ya makundi ya wafuasi wake. Moja ya kundi muhimu kwa ushindi wa bilionea huyo ni lile linalofahamika kama ‘alt-right’ (kifupi cha ‘alternative right’ yaani mbadala wa wahafidhina/wenye mrengo wa kulia). Kundi hili limekuwa ‘mwiba’ sio kwa waliberali pekee bali pia hata wahafidhina wenye msimamo wa wastani.
Na kundi hilo hatari ndilo analotoka mmoja wa wateule wa awali kabisa wa Trump, Steve Bannon, aliyeteuliwa kuwa mkuu wa mikakati wa Trump. Bannon alikuwa mmoja wa viongozi wa kampeni ya bilionea huyo na kabla ya hapo alikuwa mwenyekiti wa gazeti ‘hatari’ la mtandaoni, Breitbart. Gazeti hatari kwa sababu lengo lake kuu ni kuamsha hisia za makundi fulani kwa kubeza, kulaani na hata kutukana makundi kama vile Wamarekani weusi (gazeti hilo lilidai kuwa kiasili ni wahalifu), Walatino, wahamiaji, Waislam (gazeti hilo limewaita kila jina baya), watetezi wa haki za wanawake ikiwa pamoja na waathirika wa vitendo vya kubakwa, na takriban kila baya usilotarajia kuliona kwenye gazeti maarufu ambalo mwezi uliopita pekee, tovuti yake ilitembelewa na wasomaji zaidi ya milioni 19.
Kwa kumteua Bannon, ni wazi kuwa Trump ameamua kukumbatia makundi yaliyomuunga mkono hata kama yanajenga taswira isiyopendeza kwa urais wake. Tayari makundi mbalimbali ya utetezi wa haki za kiraia Marekani yanamtaka Trump kutengua uteuzi wa Bannon, mtu mwenye ajenda za kibaguzi na muumini wa ‘ukuu wa watu weupe’ (white supremacist).
Lakini taswira ya kuogofya kuhusu aina ya watu ambao Trump atawakumbatia katika urais wake haijaishia kwa Bannon pekee bali pia hata chaguo lake la mshauri wake wa masuala ya usalama wa taifa, Luteni Jenerali (mstaafu) Michael Flynn na Mwanasheria Mkuu, Seneta Jeff Sessions. Wakati Jenerali Flynn alitimuliwa na utawala wa Rais Barack Obama kutokana na kile kinachoelezwa kuwa kasoro za kiuongozi, Sessions ana tuhuma za ubaguzi wa rangi. Kadhalika, msimamo wa Jenerali huyo kuhusu masuala ya ugaidi wa kimataifa unaotajwa kuwa unaweza kuikosanisha Marekani na mataifa ya kiislamu kwa vile anaamini kuwa tatizo la ugaidi linachangiwa na Uislamu na sio magaidi kutumia kisingizio cha Uislamu kuhalalisha unyama wao.
Mteule mwingine wa Trump kushika nafasi ya ukuu wa shirika la ujasusi la nchi hiyo, CIA, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi, Mike Pompeo, naye anatazamwa kama mtu anayeweza kulirejesha shirika hilo katika zama zake za hatari kabisa, hasa kutokana na msimamo wake mkali kupindukia kwenye masuala ya intelijensia na usalama. Ikumbukwe kuwa katika zama zake hatari, CIA ilishiriki katika operesheni chafu kama vile mauaji ya Rais wa zamani iliyokuwa Zaire, Patrice Lumumba.
Tukiweka kando dalili za awali za mwelekeo wa serikali ya Trump, tugeukie kwanza swali muhimu: “..kwa nini Hillary Clinton alishindwa na Trump.” Sababu zinaweza kuwa nyingi, lakini za muhimu zaidi ni pamoja na ukweli kwamba Hillary alikuwa mmoja wa wanasiasa wanaochukiwa mno Marekani, japo chuki dhidi yake ilikuwa pungufu kidogo kulinganisha na Trump.
Kadhalika, kasoro kubwa iliyomwandama Hillary ni kuonekana kama sio mwaminifu hususan kutokana na skandali iliyomwandama muda wote wa kampeni yake kuhusu matumizi ya ‘server’ binafsi kwa mawasiliano ya barua-pepe alipokuwa ‘Waziri wa Mambo ya Nje.’
Vile vile, Hillary alishindwa kuwa na kauli mbiu yenye kueleweka kirahisi, kulinganisha na mpinzani wake, Trump, ya ‘Ifanye Marekani jabali tena’ (Make America Great Again). Sambamba na hilo ni ukweli kwamba ilikuwa vigumu mno kwa Democrat kuendelea kuwa Ikulu baada ya miaka minane ya urais wa Barack Obama. Kwa Marekani, ni ngumu sana kwa chama kilichokuwa madarakani kwa mihula miwili mfululizo kushinda muhula wa tatu.
Kingine kilichomwangusha Hillary ni kuzidiwa kwa kura na Trump miongoni mwa Wamarekani weupe, hususan wale ambao hawana elimu ya chuo. Kuongeza majeraha zaidi, ngome zake kuu, yaani wanawake, Wamarekani weusi na Walatino hawakumpigia kura nyingi kama ilivyotarajiwa huku Trump naye akifanikiwa kupata kura za kutosha katika makundi hayo yaliyotarajiwa kumwangusha.
Pengine kubwa zaidi ni kilichotukumba sote tuliokuwa tunafuatilia kwa karibu uchaguzi huo. Ilionekana kama jambo lisilowezekana kwa Trump kushinda urais. Kauli zake zilikuwa chafu kupita maelezo, hasa ile aliyorekodiwa akiwatusi wanawake na kujigamba kuwa ‘ukiwa mtu maarufu wanawake wanakupapatikia,’ kashfa dhidi ya walemavu, wanawake, Waislamu na Walatino (aliowaita wabakaji), na kila neno chafu ambalo mgombea japo wa ukiranja shule ya msingi, achilia mbali urais wa Marekani, hakupaswa kuropoka.
Ni kwamba, katika mazingira ya kawaida, na kwa kuamini kuwa Wamarekani wana akili timamu, isingewezekana Trump kushinda uchaguzi huo. Na katika kutupatia matumaini zaidi, takriban kura zote za maoni (opinion polls) zilionyesha Hillary akiongoza kati ya asilimia mbili na 14. Japokuwa kulikuwa na tahadhari kuwa kura hizo za maoni zilikuwa na walakini, wengi wetu tuliamini kuwa suala sio iwapo Hillary angeshinda bali angeshinda kwa kiasi gani.
Na hii inaleta swali, kwa nini takriban kura zote za maoni ziliashiria kuwa Hillary angeshinda lakini ikawa kinyume chake? Hali kama hiyo ilitokea kwenye uchaguzi mkuu wa Uingereza, Mei mwaka jana na ikajirudia kwenye kura kuhusu Uingereza kubaki au kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya. Katika kura zote hizo, matokeo yalikuwa tofauti kabisa na ubashiri wa kura za maoni.
Moja ya maelezo kuhusu ‘ubashiri fyongo’ wa kura za maoni, sio kwenye uchaguzi huo wa Marekani tu bali pia kwenye uchaguzi mkuu wa UK mwaka jana na kwenye kura ya ‘Brexit’ Juni mwaka huu, ni kile ambacho Profesa Timur Kuran wa Chuo Kikuu cha Harvard huko Marekani amekieleza katika kitabu chake ‘ukweli faraghani, uongo hadharani’ (Private Truths, Public Lies), katika kanuni (theory) yake inayojulikana kama ‘preference falsification.’ Kwa kifupi, kanuni hiyo inaeleza kuwa baadhi ya watu wanaohojiwa kwenye kura za maoni kuhusu masuala yanayogusa hisia za jamii hutoa majibu wanayoona yanaendana na ‘mtazamo wa jamii’ japo misimamo yao ni kinyume.
Kwa mfano, katika suala la Brexit, kwa kuzingatia kanuni ya Profesa, kulikuwa na hisia kuwa wanaotaka Uingereza ijitoe Umoja wa Ulaya ni wabaguzi wa rangi (racists). Kadhalika, kwa vile Trump alishatoa kauli kadhaa za kibaguzi na makundi mbalimbali ya kibaguzi kama vile KKK yalitangaza kumuunga mkono, ilijengeka picha kuwa ‘wafuasi wa Trump ni wabaguzi.’ Kwa hiyo, baadhi ya waliohojiwa kwa minajili ya opinion pools za Brexit na Trump ‘walibaki na ukweli wao faraghani na kuongea uongo hadharani,’ na katika mazingira hayo, uungwaji mkubwa kutaka UK ijitoe EU na hiyo ya Trmp miongoni mwa wapigakura haikuweza kuonekana kwa waendesha kura za maoni (pollsters).
Kwa upande mwingine, Hillary alikuwa mwathirika wa zama mpya za ‘siasa za uongo,’ wenyewe wanaita ‘post-truth politics,’ ambapo vitu muhimu kwenye mijadala na kampeni za kisiasa, kama vile ukweli na hoja za kitaalamu, vinazidiwa nguvu na kauli za uongo lakini za kugusa hisia na imani za watu. Kampeni ya Brexit hapa Uingereza ilitawaliwa na ‘post-truth politics’ na ikawezesha kambi iliyotaka Uingereza ijitoe ishinde kwenye kura ya maoni, na kwa mara nyingine tena imemwezesha Trump kushinda huko Marekani.
Kama nilivyoandika katika makala yangu kwenye toleo lililopita, tatizo la ‘post-truth politicis’ ni ‘waumini’ wa aina hiyo ya siasa. Takriban wote, angalau kwa kuangalia aina ya watu na vikundi vyao, ni waumini pia wa siasa za kibaguzi za mrengo mkali wa kulia.
Ndio, ‘post-truth politics, ni matokeo ya tabaka tawala, tabaka la wanasiasa, tabaka la wasomi na mfumo wa siasa, uchumi na jamii kushindwa kusikiliza vilio vya wananchi wa kawaida, lakini kwa bahati mbaya au makusudi, viongozi wa siasa hizo ni watu hatari zaidi ya viongozi waliopo kwenye mfumo tulionao sasa, angalau kwa nchi za Magharibi.
Je ‘post-truth politics,’ na ufanisi wake kwa Brexit na ushindi wa Trump ni vitu vinavyoweza kuenea kwa upana zaidi? Hilo ni suala la muda. Kipimo cha kwanza ni uchaguzi mkuu nchini Ufaransa Aprili hadi Juni mwakani, na kura ya maoni/chaguzi nchini Italia, Austria na Ujerumani.
Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wa kisiasa wanadai kuwa ‘siasa za umaarufu’ (populist politics) kama hizo za ‘post-truth’ zina ‘uhai’ (life-span) wa kati ya miaka mitano hadi saba tu. Kwa hiyo wanabashiri kuwa hazitodumu kwa muda mrefu, na pengine hiyo itazifanya zisisambae sehemu kubwa ya dunia.
Kwa huko nyumbani, na pengine Afrika kwa ujumla, ‘siasa za hadaa/uongo’ zimekuwa sehemu muhimu ya siasa zetu za kila siku. Tofauti na kinachojiri huku nchi za Magharibi ni kwamba siasa za uongo zinatumiwa na watu wanaotaka kuondoa mfumo uliopo madarakani ilhali kwa akina ‘siye’ siasa za aina hiyo ndio zimeweka mfumo uliopo madarakani.
Je ‘siasa za hadaa/uongo’ zinaweza kuung’oa mfumo uliowekwa madarakani kwa hadaa/uongo? Mwamuzi ni muda. Hata hivyo, ukweli kuwa kuna vuguvugu la kushinikiza mapinduzi dhidi ya mfumo ulioshindwa kuutumiakia umma unaweza kuwa chachu kwa nchi kama zetu kuwahamasisha kuwa ‘imetosha.’ Na kama Trump licha ya kasoro zake zote ameweza kushinda urais kwa kisingizio cha ‘kupigania haki za wanyonge dhidi ya mfumo uliowatelekeza,’ basi yayumkinika kuhisi kuwa hata akina sie tunaweza kukumbwa na hali hiyo, japo binafsi naona uwezekano huo ni mdogo kwa sasa.
Na pengine ‘post-truth politics’ na wimbi la kudai mapinduzi dhidi ya mfumo ulioshindwa kuhudumia umma vinaweza visiwe na matokeo bora kwa nchi zetu za Afrika kutokana na kushamiri rushwa, siasa za kujuana na uwezo wa mfumo uliopo madarakani kutumia kila aina ya nguvu kusambaratisha jitihada zozote za kuupinga.
Mwisho, moja ya athari tarajiwa za Trump – kama akiendelea na msimamo wake wa kibaguzi – ni pamoja na bara la Afrika kutokuwa kipaumbele cha sera za nje za Marekani, kama ambavyo yawezekana uadui kati ya Marekani na nchi za kiislamu kuzorota maradufu, hususan kutokana na imani fyongo ya Trump na baadhi ya wasaidizi wake kuuhusisha Uislam na ugaidi.
Nihitimishe makala hii kwa upande mmoja kuikumbusha CCM kuwa wimbo wa upinzani dhidi ya mfumo unaoonekana kuwapuuza wananchi wa kawaida unapamba moto, na kwa vile CCM ni sehemu ya mfumo ambao baadhi ya Watanzania wanaona umewatelekeza, basi ni muhimu kujirekebisha. Kwa upande mwingine, Brexit na urais wa Trump ni funzo kwa vyama vya upinzani kuwa kusimama upande wa waliochoshwa na mfumo unaowapuuza kunaweza kusaidia kuleta ushindi kwa chama/mfumo mbadala.
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo, kwa kuangalia athari za urais wa Trump duniani kwa ujumla hususan barani Afrika, kwa nini Hillary ameshindwa na kwa nini kura za maoni zilibashiri matokeo ya uchaguzi huo “ndivyo sivyo” na nini tunaweza kujifunza kutokana na uchaguzi huo

17 Nov 2016

JUMANNE iliyopita inaweza kuingia kwenye vitabu vya kumbukumbu mbaya kutokana na uchaguzi mkuu nchini Marekani ambao mshindi alikuwa mgombea wa chama cha kihafidhina cha Republican, Donald Trump.
Trump – mwongo wa waziwazi, mnyanyasaji wa wanawake, mzinzi, mbaguzi wa rangi, mbaguzi wa kidini na mwasisi wa harakati za kibaguzi dhidi ya uraia wa Rais wa sasa wa nchini hiyo, Barack Obama, alifanikiwa kumshinda mpinzani wake mkuu, mgombea wa chama cha Democrat, Hillary Clinton.
Kibaya zaidi ni kwamba mfumo fyongo wa uchaguzi wa rais wa nchi hiyo ulimwezesha Trump kuwa mshindi licha ya kupata kura pungufu (60,350,241) dhidi ya mpinzani wake Hillary (aliyepata kura 60, 981, 118). Kura hizo zilizopigwa siku ya uchaguzi hujulikana kama popular vote, lakini kura muhimu zaidi na zinazoamua mshindi wa uchaguzi ni zinazofahamika kama electoral votes. Mshindi hutakiwa kupata kura hizi 270 au zaidi.
Inabidi kuelezea kwa kifupi kuhusu mfumo huo unaokanganya. Kimsingi, Wamarekani hawamchagui Rais wao moja kwa moja, badala yake kila jimbo lina watu wanaofahamika kama electors (wachaguzi) ambao hukutana mwezi Desemba mara baada ya kura zilizopigwa na kila aliyejiandikisha kupiga kura Novemba 8 ya mwaka wa uchaguzi.
Kama tulivyoona kwenye matangazo ya runinga, kila jimbo lina idadi yake ya "wachaguzi." Na jumla ya wachaguzi hao kutoka majimbo yote 51 ya Marekani ni 538.
"Wachaguzi" hao nao huchaguliwa na vyama vyao. Kila chama kina kanuni zake za uchaguzi wa "wachaguzi" hao. Uchaguzi wao hufanyika kwa hatua mbili. Kwanza, chama huchagua orodha ya "wachaguzi watarajiwa" na pili, "wachaguzi halisi" huchaguliwa na wapigakura siku ya uchaguzi. Majina ya wanaogombea kuwa “wachaguzi" yanaweza kuonekana katika karatasi ya kura au yasionekane, kutegemea kanuni husika.
Hakuna sheria inayowabana "wachaguzi" kumpigia kura mgombea aliyeshinda popular vote. Na ni katika mazingira haya ndio maana kumekuwa na jitihada za kuwashawishi "wachaguzi" hao kutompigia kura Trump, ili kumkwamisha na hatimaye kumwezesha Hillary achaguliwe. Hata hivyo, uwezekano wa hilo kutokea ni mdogo. Kihistoria, asilimia 99 ya "wachaguzi" hupiga kura kwa mshindi wa "popular vote."
Kila jimbo lina "ikulu" yake (state capitol), na hapo ndipo "wachaguzi" kutoka kila jimbo hukutana Desemba kupiga kura zao. Masanduku ya kura walizopiga hufunguliwa mwezi Januari katika kikao cha "Baraza la Wawakilishi".
Iwapo katika matokeo kutakuwa hakuna mgombea mwenye kura nyingi, au wagombea wawili watakuwa na kura sawa, Baraza la Wawakilishi litamchagua Rais miongoni mwa wagombea watano wenye kura nyingi zaidi.
Kila jimbo hupewa "kura za wachaguzi" (electoral votes) kulingana na jumla ya maseneta na wawakilishi. Kiwango cha chini kwa kila jimbo ni kura tatu. Majimbo makubwa huwa na kura nyingi kwa vile uwakikishi katika Baraza la Wawakilishi hutegemea idadi ya wakazi katika jimbo husika.
Tukirejea kwenye matokeo ya uchaguzi, Trump alipata kura za “wachaguzi” 290 huku Hillary akiambulia 228. “Wachaguzi” katika kila jimbo watakutana Desemba 17 kupiga kura zao, huku matarajio makubwa yakiwa wataheshimu jinsi wingi wa kura za “wachaguzi” alizoshinda Trump.
Kwa hiyo japo kinadharia kuna uwezekano wa “wachaguzi” hao kuamua kumnyima kura Trump na badala yake kumpa kura hizo Hillary, hali itakayosababisha matokeo ya uchaguzi huo kubadilika, uwezekano huo kiuhalisi ni mdogo mno.
Tathmini ya uchaguzi huo inahitaji zaidi ya makala moja, na katika makala hii nitagusia mambo muhimu kwa kifupi tu kwa matarajio ya kuendeleza mada hii katika makala zijazo.
Ushindi wa Trump umetokana na nini? Nchi za Magharibi zinapitia zama mpya ya siasa inayofahamika kama “post-truth politics.” Hii ni aina ya siasa inayotawaliwa na hisia na ushawishi kuliko ukweli au hoja za kitaalamu. Aina hii mpya ya siasa ilikuwa na ufanisi sana hapa Uingereza, katika kampeni za kura ya kuamua iwapo nchi hii iendelee kuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya (EU) au ijitoe. Wanasiasa wa kambi iliyotaka Uingereza ijitoe walishutumiwa mara kadhaa kwa kutumia takwimu za uongo na kujenga hoja za chuki dhidi ya wageni na EU kwa ujumla, huku wakipinga kwa nguvu zote takwimu za kitaalam zilizoonyesha bayana madhara ya nchi hii kujitoa EU.
Tulipopiga kura Juni 23 mwaka huu, kambi hiyo iliyotumia hadaa na hoja za chuki ndiyo iliyoibuka mshindi, japo tayari nchi hii inashuhudia kipindi kigumu kiuchumi kama ambavyo wataalamu mbalimbali walivyoonya wakati wa kampeni.
Ukweli (facts) una sehemu tukufu katika siasa za kidemokrasia za Magharibi. Kila wakati demokrasia ilipokwenda mrama, kila ilipotokea wapigakura kufanyiwa ulaghai au wanasiasa kukwepa maswali, tulikimbilia kwenye ukweli kama mkombozi.
Lakini kwa sasa, ukweli unaonekana kupoteza nafasi yake katika kujenga mwafaka. Tovuti ya kutofautisha ukweli na uongo ya PolitiFact ilibaini kuwa takriban asilimia 70 ya hoja za Donald Trump ziliangukia makundi ya “karibu na uongo” “uongo” and “uongo kabisa." Lakini hiyo haikumzuia kushinda urais wa Marekani
Kadiri siasa zinavyozidi kuwa za uhasama na kutawaliwa na ufanisi wa wahusika kwenye nyenzo za teknolojia kama vile runinga na mitandao ya kijamii, "afya" ya ukweli (facts) kwenye mijadala na midahalo inakuwa tete. Matarajio ya wasikilizaji, watazamaji na wasomaji yanaelemea zaidi kwenye ushawishi wa mtoa hoja hata kama hoja hizo ni za uongo wa waziwazi.
Taratibu, nafasi ya wajuzi, wasomi, wazoefu na makundi mengine tuliyozoea kuyaamini kutupatia mwongozo sahihi inazidi kudidimia na mbadala wake ni hoja za kugusa hisia za watu hata kama zinapanda mbegu za mfarakano, kutumia uongo hata pale unapoonekana waziwazi ilimradi tu unaweza kuvutia kuungwa mkono na sehemu ya hadhira, kupandikiza hasira ili kuipa nguvu hadhira kuchukua hatua hata kama zinapanda athari na kwa ujumla, kutotoa fursa kwa ukweli (facts).
Aina hii mpya ya siasa ni hatari, sio tu kwa sababu unafanya ukweli kuwa uongo na uongo kuwa ukweli, bali pia kwa vile imetokea kuwa chaguo mwafaka la wanasiasa waumini wa siasa za mrengo mkali wa kulia; wabaguzi wa rangi, wabaguzi wa kidini; na viumbe hatari kama hao.
Nitazungumzia zaidi mada hii siku nyingine.
Kwa upande mwingine, ushindi wa kambi iliyotaka Uingereza ijitoe EU (licha ya hoja zao za uongo na kupandikiza chuki) na ushindi wa Trump huko Marekani ni ujio wa mapinduzi ya kimfumo; upinzani wa umma dhidi ya tabaka la wanasiasa, wasomi na taasisi za kisiasa na uchumi. Hii ingepaswa kuwa habari njema lakini tatizo ni kwamba wanaoendesha kampeni ya mapinduzi haya ni wanasiasa hatari kabisa katika nchi zao na kimataifa.
Ushindi wa Trump umepokelewa kwa shangwe kubwa na viongozi wa vyama vya kisiasa vya kibaguzi na vyenye mrengo mkali wa kulia, kama Marine LePen wa Ufaransa, Victor Orban wa Hungary, Frauke Petry wa Ujerumani, Heinz-Christian Strache wa Austria na Geert Wilders wa Uholanzi. Na kwa hapa Uingereza, mwasisi wa harakati za nchi hii kujitoa EU, Nigel Farage, amekuwa mwanasiasa wa kwanza wa nchi hii kukutana na Rais-Mteule, Donald Trump.
Kwa hali ilivyo Marekani hivi sasa ambapo kuna maandamano mbalimbali ya kupinga ushindi wa Trump, mustakabali utategemea zaidi jinsi kiongozi huyo atakavyomudu kubadilika na kuwa kiongozi wa Wamarekani wote na sio kundi la Wamarekani weupe wasio na elimu ya chuo, Wakristo wenye msimamo mkali, na magenge ya wabaguzi wa rangi kama vile kundi la Klu Klux Klan (KKK) pekee.
Je, Trump atabadilika? Kwa jinsi ambavyo kila kitu kuhusu Trump ni vigumu kukibashiri kwa ufasaha (mwenyewe anasema kutotabirika ni siri ya mafanikio), jibu fupi ni kwamba; “…hakuna ajuaye isipokuwa Trump mwenyewe.” Jibu refu ni kwamba awali kauli zake kuwa atachukua mazuri na kuacha mabaya ya mpango wa bima ya afya ya jamii ujulikanao kama Obamacare (ambao Trump aliahidi kuufuta mara moja wakati wa kampeni) ziliashiria dalili za mabadiliko.
Pia taarifa kuwa amezitoa hofu nchi za Japan na Korea Kusini kuhusu msaada wa kijeshi wa Marekani kwa nchi hizo, zilileta dalili ya matumaini kwamba huenda ameanza kubadilika. Japan inakabiliwa na tishio kutoka China, na Korea Kusini inakabiliwa na tishio kutoka Korea Kaskazini, na Jeshi la Marekani ni ngao muhimu kwa mataifa hayo.
Vile vile, tovuti ya kampeni za uchaguzi ya Trump iliondoa tamko lake la kuwazuia Waislamu kuingia nchini humo pindi akishinda urais. Hatua hiyo Ilitafsiriwa kuwa ni dalili za ‘msema ovyo’ huyo kulegeza msimamo.
Hata hivyo, tayari Trump ameeleza kuwa ataanza utekelezaji wa dhamira yake ya kuwatimua wahamiaji haramu wanaokadiriwa kuwa zaidi ya milioni 11 nchini humo, ambapo ametangaza kuwa ataanza kuwatimua ‘wageni haramu’ milioni tatu mara tu baada ya kuapishwa.
Nihitimishe makala hii kwa kugusia vitu viwili. Kwanza, kushamiri kwa wimbi la “post-truth politics” na “mapinduzi dhidi ya tabaka la wanasiasa, wataalam au taasisi za siasa na uchumi” hasa kwa vile mwezi ujao, Italia itakuwa na kura ya maoni kuhusu katiba za nchi hiyo na Austria itakuwa na uchaguzi mkuu, Uholanzi itakuwa na uchaguzi wa bunge mwezi Machi mwakani, Ufaransa itakuwa na uchaguzi mkuu Aprili hadi Juni mwakani, na Ujerumani itakuwa na uchaguzi wa wabunge mwezi Septemba mwakani. Mataifa yote hayo yanakabiliwa na vuguvugu kubwa la upinzani dhidi ya Umoja wa Ulaya na chuki dhidi ya wageni, pamoja na “post-truth politics.”
Pili, moja ya makundi yaliyomsaidia sana Trump kushinda urais ni linalofahamika kama ‘alt-right.’ Kwa lugha rahisi, hawa ni zaidi ya wahafidhina. Ni wabaguzi wa rangi na dini, wapinzani wa harakati za wanawake na wanaosherehesha unyanyasaji wa wanawake, na kwa kifupi, “watu waliofanikiwa kuhamasisha kuwahadaa watafiti wa kura za maoni kuhusu nafasi ya Trump katika uchaguzi wa rais Marekani.”
Nimalizie makala hii kwa kuahidi kuendelea na uchambuzi huu katika toleo lijalo, kwa kuangalia athari za urais wa Trump duniani kwa ujumla hususan barani Afrika, kwa nini Hillary ameshindwa na kwa nini kura za maoni zilibashiri matokeo ya uchaguzi huo “ndivyo sivyo” na nini tunaweza kujifunza kutokana na uchaguzi huo.
ITAENDELEA TOLEO LIJALO


16 Nov 2016

Moja ya vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dkt John Magufuli ni ukusanyaji mapato, ikiwa ni pamoja na yale yatokanayo na madeni. Ni katika utekelezaji wa kipaumbele hicho, Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa taasisi za Elimu ya Juu (HESLB) imeanza 'msako mkali' dhidi ya 'wadaiwa sugu.' watu walionufaika na mikopo hiyo lakini hawajaanze kuirejesha.

Kwanza, nianze makala hii kwa kuipongeza serikali kwa hatua hii muhimu ambayo ikifanyika kw aufanisi, itasaidia ukusanyaji wa mapato makubwa yatakayowezesha udhamini wa serikali kwa wanafunzi wengi zaidi. Sote twatambua umasikini wa Tanzania yetu, na ni jukumu letu kuisaidia nchi yetu.

Binafsi, nilisoma kwa mkopo wa serikali kuanzia mwaka 1996 hadi nilipohitimu mwaka 1999. Wakati huo, na hadi ninaondokaTanzania mwaka 2002, hakukuwa na utaratibu wowote wa urejeshaji wa mkopo huo.

Hali hiyo imeendelea hadi mwaka huu 2016, ambapo ghafla serikali kupitia HESLB imeamka usingizini na kuanza kufuatilia fedha inayotudai, lakini sio kistaarabu (kwani sio kosa letu wadaiwa kutotengenezewa mfumo stahili wa kufanya marejesho ya mikopo tuliyopewa, bali kosa la serikali) na tunaitwa WADAIWA SUGU. Mdaiwa sugu ni mtu ambaye amedaiwa zaidi ya mara moja na hajalipa. Si sahihi kumwita mtu 'mdaiwa sugu' wakati hujamwelekeza jinsi ya kulipa deni unalomdai wala hujahangaika kumdai.



Sina hakika kama kuna watu walishawahi kupewa utaratibu wa kurejesha mikopo ya elimu waliyopewa, lakini kwa uelewa wangu na ufuatiliaji wa yanayojiri huko nyumbani, sijawahi kuona hilo.

Hata hivyo, kwa vile lawama hazijengi, na lengo la serikali 'kukurupuka' ni jema (kukusanya mapato), basi ni vema kuweka kando lawama na sote tunaodaiwa kuanza utaratibu wa malipo ya fedha tunazodaiwa.

Kwa upande wangu, nimetuma barua pepe kwa HESLB kuulizia kiwango ninachodaiwa na taratibu za malipo. 


Nimefainya hivyo ili, kwanza, kuunga mkono jitihada za serikali kukusanya mapato ikiwa ni pamoja na malipo ya mikopo tuliyokopeshwa. Pili, dawa ya deni ni kulipa. Ninawahamasisha wadaiwa wenzangu kuhusu umuhimu wa kulipa fedha tunazodaiwa. Na, tatu, ku- preempty jitihada zozote za watakaotaka kutumia suala hili la 'udaiwa sugu' kuchafua jina langu. Ni matarajio yangu kuwa kwa hatua hizi za dhati nilizochukua hakutajitokeza 'mchawi' wa kusema "ah wewe Chahali unajifanya mzalendo kumbe fisadi unadaiwa..." haha. 

Anyway, nitatumia ukumbi wangu huu kuwafahamisha majipu nitakayoletewa na HESLB na mustakabali wa 'udaiwa sugu.' 

10 Nov 2016


JUMAMOSI iliyopita ilikuwa siku ya maadhimisho ya mwaka mmoja kamili tangu Dk. John Magufuli aapishwe kuwa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Siku moja kabla ya maadhimisho hayo, Magufuli alifanya mkutano wake wa kwanza na waandishi wa habari.
Mkutano huo umeibua lawama za aina mbili. Kwanza, lawama nyingi dhidi ya wanahabari kwa kutouliza maswali ya msingi na pili, dhidi ya Rais kwa kutotoa majibu ya kuridhisha.
Kuhusu hizo lawama dhidi ya wanahabari, binafsi sikushangazwa maana tunawaelewa vema wanahabari wetu. Wengi wao wamezoea kupewa habari na kuziandika (mara nyingi kwa mujibu wa matakwa ya mtoa habari). Wanahabari wetu wengi ni waoga katika kuuliza maswali magumu.
Kwa mtazamo wangu, chanzo cha tatizo hilo ni kasumba iliyojengeka zama za chama kimoja, ambapo kimsingi viongozi walikuwa waongeaji na wananchi (ikiwa ni pamoja na wanahabari) ni wasikilizaji tu. Huu utaratibu wa kuuliza maswali viongozi (ambao walikuwa kama miungu-watu katika zama za chama kimoja) bado unaonekana kama mgeni na hakuna jitihada za kutosha miongoni wa wanahabari kuondokana na kasumba hiyo.
Malalamiko kwamba Magufuli hakutoa majibu ya kuridhisha kwa maswali aliyoulizwa, yanategemea mtoa malalamiko hayo. Binafsi, ninampongeza Rais sio tu kwa kujibu maswali kwa umahiri na maelezo ya kina bali pia kwa kuwapa wanahabari wetu muda wa kutosha kuuliza maswali yao.
Siku moja kabla ya mkutano huo, baadhi ya wafuasi wa Chadema walisambaza taarifa kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii ikidai kuwa wanahabari watakaohudhuria mkutano wao na Rais wamekwishaandaliwa maswali ya kuuliza. Kwa lugha nyingine walikuwa wanajaribu kupoteza ‘credibility’ ya mkutano huo. Kwa vile njia ya mwongo ni fupi, jinsi wanahabari walivyopewa uhuru mkubwa wa kuuliza maswali ilionyesha bayana kuwa hakuna mwanahabari aliyepewa maswali ya kuuliza kabla ya mkutano huo.
Wengi wa wanaolalamikia majibu ya Rais ni hao hao wenye tofauti za kiitikadi na CCM, chama ambacho Magufuli ni mwenyekiti wake wa taifa. Kwa hiyo, hata kama Rais angejibu vizuri kiasi gani maswali aliyoulizwa, bado wapinzani wake wa kisiasa wangemlaumu. Ndio siasa zetu zilipofikia.
Pamoja na uchaguzi mkuu uliopita kutimiza mwaka mzima sasa tangu umalizike na kutupatia Magufuli kama Rais wetu, bado kuna kundi kubwa tu ambalo, kwa upande mmoja, ni kama haliamini kuwa mpinzani mkuu wa Magufuli kwenye uchaguzi huo, mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa, kweli alishindwa katika uchaguzi huo.
Hali hiyo inaendana na upinzani mkali dhidi ya kila linalofanywa na Rais Magufuli na serikali yake. Nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mwenendo wa chama kikuu cha upinzani cha Chadema baada ya uchaguzi mkuu na yayumkinika kuhitimisha kuwa ajenda kuu ya chama hicho kwa sasa ni kumpinga Dk. Magufuli kwa nguvu zote, hata katika masuala yenye maslahi kwa taifa.
Kwa namna fulani, upinzani huo, ambao sio kosa kisheria, umezaa genge dogo lakini lenye ushawishi mkubwa miongoni mwa wafuasi wa Chadema ambalo kwa ‘anything goes’ (lolote sawa tu) ilimradi urais wa Dk. Magufuli na uongozi wa serikali yake uonekane bomu.
Utekelezaji wa ahadi zake mbalimbali umepokelewa na watu hao kwa mtazamo hasi. Si suala la elimu ya bure au kutumbua majipu, sio kufufua Reli ya Kati au ununuzi wa ndege mbili ili kufufua Air Tanzania kunakowafanya watu hao wathamini jitihada za kiongozi huyo.
Na alipoanzisha operesheni ya kuhakiki vyeti vya elimu kwa watumishi wa umma, ikaibuliwa hoja ya kizandiki kuwa kabla hajaanza kuhakiki vyeti vya watumishi wa umma, aanze na shahada yake ya uzamivu (PhD) ambayo waliituhumu kuwa ni feki.
Na mmoja wa wahubiri wa tuhuma hiyo kuhusu elimu ya Magufuli aliandika makala katika toleo lililopita la gazeti hili akitetea ‘haki ya kuhoji PhD’ ya kiongozi huyo. Tatizo sio kuhoji bali kumtuhumu Rais kuwa shahada yake hiyo ni feki. Na licha ya kutoa mifano mingi ya hadaa mbalimbali za kitaaluma, mtoa lawama alishindwa kuthibitisha tuhuma zake. Unapomtuhumu mtu kuhusu kosa fulani ni jukumu lako mtoa tuhuma kuzithibitisha tuhuma hizo na sio mtuhumiwa. 
Dk. Magufuli hakujipa shahada ya uzamivu, alitunukiwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Yeyote mwenye shaka kuhusu shahada hiyo au mbili zilizotangulia (BSc na MSc) anaweza kuwasiliana na chuo hicho au Kamisheni ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kupata uhakika. Kuhoji sio tatizo. Kutuhumu ni zaidi ya tatizo. Ni uzandiki. Na uzandiki (kumfarakanisha Rais na wananchi anaowaongoza kwa kumtuhumu kuwa ana PhD feki) ni tishio kwa usalama wa taifa.
Lakini tatizo hasa sio ndege mbili za Magufuli au PhD yake au majibu yasiyoridhisha kwenye mkutano kati ya Rais na wanahabari. Tatizo ni hao wenzetu ambao ni kama bado wapo kwenye ‘mode’ ya uchaguzi (election mode), hawataki kukubali kuwa mgombea wa chama chao alishindwa kihalali, na sasa tuna Rais mpya ambaye amekuwa madarakani kwa zaidi ya mwaka sasa. Na wenye nia njema na Tanzania yetu wanaridhishwa mno na utendaji kazi wa Rais huyo, hususan katika mapambano yake dhidi ya rushwa na ufisadi, ajenda iliyokuwa nguzo ya Chadema kabla ya kumpokea Lowassa (mwanasiasa ambaye chama hicho kilimtuhumu kwa miaka tisa mfululizo kuwa ni fisadi, kabla ya kugeuza ‘gia’ angani na kumteua kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho).
Japo kila mgombea anapaswa kuwaaminisha wafuasi wake kuhusu fursa za kushinda katika uchaguzi, binafsi ninaona kama matumaini ambayo Lowassa aliwapatia wafuasi wake yalikuwa ya kina mno kiasi kwamba mwaka mmoja baada ya mwanasiasa huyo kubwagwa kwenye uchaguzi mkuu, bado wafuasi wake wengi hawaamini kilichotokea.
Lakini pia kuna kundi ambalo sio tu liliamini kuwa ushindi wa Lowassa ulikuwa sio wa mwanasiasa huyo pekee bali nao walikuwa na matarajio ya nyadhifa fulani, hususan wale ambao jitihada zao za kuwania nafasi kama ubunge ziliishia kwenye ngazi ya kura za maoni tu. Kwa Lowassa kushindwa kwenye uchaguzi huo ilimaanisha kuwa nao ndoto zao za madaraka ziliota mbawa.
Nimalizie makala hii kwa kumpongeza Dk. Magufuli kwa kutimiza mwaka mmoja wa urais uliosheheni mafanikio lukuki. Amefanikiwa sio tu kuitoa Tanzania yetu kutoka chumba cha wagonjwa mahututi bali pia ameweza kurejesha nidhamu ya kazi na kuondoa dhana kwamba uhalifu (ufisadi, ujangili, kuuza unga, nk) ndio njia halali ya kipato. Wengi wa wanaomlaumu Dk. Magufuli kuwa amefanya maisha kuwa magumu ni watu waliokuwa wakiishi kwa kutegemea ‘dili.’
Na kwa wanaolalamika kuwa Dk. Magufuli ni dikteta, anaminya uhuru wa vyama vya upinzani labda kwanza waanze kudai demokrasia ndani ya vyama vyao ambavyo baadhi vimekuwa kama vya kisultani kwa kuwa na sura zile zile za viongozi wakuu miaka nenda miaka rudi pasi chaguzi kuu.

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.