10 Jan 2018

Image result for magufuli lowassa
Jana Januari 9, 2018, wiki moja na siku mbili baada ya kuanza kwa mwaka huu mpya, duru za siasa za Tanzania zilitikiswa na habari kuhusu kiongozi maarufu wa Chadema, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kukutana na Rais John Magufuli kwa “mazungumzo”, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Baada ya “mazungumzo” hayo Lowassa alimmwagia pongezi Magufuli kwa kile alichokiita “kazi nzuri anayoifanya” na kutaja mafanikio katika sera ya elimu bila malipo, ujenzi wa mradi wa uzalishaji wa umeme katika maporomoko ya mto Rufiji (Stiegler’s Gorge), na ujenzi wa viwanda na ujenzi wa reli ya “standard gauge”.

Nimepata faraja sana kuja hapa Ikulu kuonana na Mheshimiwa Rais, tumezungumza nae na nimempongeza kwa kazi nzuri anayoifanya, lazima tukiri anafanya kazi nzuri na anahitaji kutiwa moyo,” alinukuliwa Lowassa aliyejiunga na Chadema miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 baada ya ndoto zake kuwania urais kwa tiketi ya CCM “kuota mbawa.”


Image result for magufuli lowassa

Mwanasiasa huyo ambaye baada ya kujiunga na Chadema alipitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya muungano wa vyama vinne vya upinzani – Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD – uliofahamika kama UKAWA, aliendelea kusema kuwa “Moja kubwa ambalo ni la msingi sana ni la kujenga ajira, katika kuanza ujenzi wa reli ya kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro hapo anajenga ajira, na kwenye nchi yoyote inayoendelea suala muhimu ni kujenga ajira, Stiegler’s Gorge ni kujenga ajira na mingine ya aina hiyo, lazima kuwepo na kipaumbele cha kusema kwamba tunajenga ajira. Jingine ni la elimu, ni muhimu sana, hauwezi kuacha elimu katika mambo yako unayofanya, hili nalo lazima lisemwe vya kutosha, kwa kweli nakushukuru Mheshimiwa Rais, you made my day.

Rais Magufuli kwa upande wake alimpongeza Lowassa kwa kile alichokiita “kutambua kazi kubwa inayofanywa na Serikali” na kumtaja Lowassa kama mmoja wa viongozi ambaye kwa wakati wake alitoa mchango wake katika nchi.

Magufuli alimmwagia sifa Lowassa akidai kuwa “ni mwanasiasa mzuri kwani hata wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita ambao naye aligombea kiti cha Urais, hakuwahi kumtukana.”

Mheshimiwa Lowassa ameniomba mara nyingi nikutane nae, na leo nimekutana nae, tumezungumza mambo mengi, ameniambia ya kwake na mimi nimemwambia ya kwangu. Kwa ujumla Mheshimiwa Lowassa ni mwanasiasa mzuri na tuendelee kuwaenzi wazee hawa ambao kwa nyakati fulani walifanya mambo mazuri, na mimi napenda kumpongeza Mhe. Lowassa ambaye kama alivyosema hapa kuwa tumefanya mambo mazuri mengi,” alisema Rais Magufuli

Ametaja miradi mbalimbali tunayotekeleza, ametaja mradi wa Stiegler’s Gorge utakaogharimu zaidi ya Shilingi Trilioni 7, amezungumzia juu ya elimu bure, amezungumzia juu ya maji ambayo kwa bahati nzuri yeye alikuwa Waziri wa Maji na anafahamu sasa tumefikia wapi, amezungumza juu ya umeme tulivyosambaza katika vijiji mbalimbali, elimu bure, huduma za hospitali na mengine” aliongeza Rais Magufuli.

Kwanza, ni muhimu kutambua kuwa kama Mtanzania yeyote yule, Lowassa alikuwa na kila haki ya kukutana na Rais wake. Kadhalika, kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani, isingepaswa kuwa jambo la kushangaza kwa viongozi hao wawili kukutana.

Hata hivyo, Lowassa sio tu amekutana na Magufuli, bali pia ammemwamgia sifa. Je ni dhambi kwa kiongozi wa chama cha upinzani kumwagia sifa Rais aliyepo madarakani? Jibu lingepaswa kuwa “si dhambi,” laiti uhusiano kati ya Rais Magufuli, serikali yake na taasisi zake (kama vile jeshi la polisi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa), watendaji wa serikali (hasa mawaziri na manaibu wao, na wakuu wa mikoa na wilaya), pamoja na chama cha Magufuli yaani CCM, na chama anachotoka Lowassa, yaani Chadema, na Upinzani kwa ujumla, ungekuwa mzuri.

Lakini ukweli ni kwamba japo tangu kuruhusiwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, uhusiano kati ya CCM, serikali zake na taasisi zake, na vyama vya upinzani umekuwa “wa kusuasua,” hali katika miaka miwili tu ya utawala wa Magufuli imekuwa mbaya zaidi hususan kutokana na ukweli kwamba hakuna jitihada za kuficha chuki iliyopo dhidi ya Upinzani.

Kama kiongozi wa ngazi za juu kabisa wa Chadema, na pengine mwanasiasa anayeheshimiwa zaidi ya kiongozi mwingine yoyote ndani ya chama hicho, ni wazi Lowassa anafahamu vema msimamo na mtazamo wa chama chake kuhusu Magufuli na utendaji kazi wake, na serikali yake, na chama chake.

Pengine kwa kuweka picha sawia, inaelezwa kwamba hadi wakati huu, zaidi ya wana-Chadema 400 ikiwa ni pamoja na viongozi na wanachama, aidha wapo jela au wana kesi zinazoendelea mahakamani ambazo takriban zote ni matokeo ya chuki za kisiasa zinazofanywa na Magufuli, serikali yake na chama chake.

Kadhalika, katika utawala wa Magufuli, vyama vya upinzani ikiwemo Chadema ambayo Lowassa ni kiongozi wake wa kitaifa vimepigwa marufuku kufanya shughuli zao za kisiasa ikiwa ni pamoja na mikutano na maandamano. Hayo yanatokea wakati CCM ikiwa huru kufanya mikutano na maandamano itakavyo, mara nyingi ikitumia raslimali za umma.

Sambamba na jitihada za Magufuli kubana fursa ya siasa (political space), utawala wa kiongozi huyo umekuwa mstari wa mbele kuvibana vyombo vya habari na kudhibiti uhuru na haki ya wananchi kutoa mawazo yao kama Katiba inavyowaruhusu.

Lakini jingine ambalo Chadema ni mhanga mkubwa, kada maarufu wa chama hicho Ben Saanane “alipotea” Novemba mwaka jana na hadi leo hajapatikana.

Na ni wakati ninaandika makala hii nimebaini kuwa Lowassa hajawahi kuongelea suala la kada huyo (naomba nikosolewe kama nimekosea).
Kubwa zaidi linaloweza kuhalalisha hasira za Chadema kwa utawala wa Magufuli ni tukio la hivi karibuni ambapo Mbunge wake maarufu, ambaye pia alikuwa mpinzani maarufu dhidi ya Magufuli, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, kunusurika kuuawa baada ya shambulio la risasi kadhaa huko Dodoma. Kwa sasa Lissu yupo nchini Ubelgiji kwa matibabu, lakini japo Lowassa alimtembelea alipokuwa hospitalini Nairobi, Magufuli hakuwahi kutia mguu kumjulia hali mwanasiasa huyo ambaye pia ni mnadhimu mkuu wa upinzani bungeni na Rais wa Tanganyika Law Society (TLS).

Kwahiyo japo pongezi za Lowassa kwa Magufuli zinaweza kuwa na uzito, mapungufu ya utawala wa rais huyo wa awamu ya tano, hususan kuhusiana na chuki na uonevu dhidi ya vyama vya upinzani, hususan Chadema, yalipaswa “kumzuwia” kada huyo wa zamani wa CCM kumwaga pongezi hizo.

Kibaya zaidi, imebainika kuwa Lowassa alishawahi kumwomba Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amsaidie kukutana na Magufuli. Hata hivyo, Gambo alipotamka hilo hadharani, Lowassa “aliruka kimanga.”


Hata hivyo, jana Magufuli alitamka bayana kuwa Lowassa aliomba mara kadhaa kukutana naye. Kwahiyo, alichosema Gambo kilikuwa kweli, na Lowassa hakuwa mkweli alipokana kuwa hajaomba kukutana na Magufuli.

Tukio hilo la Lowassa kukutana na Magufuli na kumwagia pongezi limepokelewa kwa hisia tofauti. Wakati kuna kundi dogo la wana-Chadema waliopongeza hatua hiyo, kwa mfano “kada” mmoja wa chama hicho Yericko Nyerere, wengi ikiwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wamepingana waziwazi na Lowassa.

Wakati Yericko aliandika haya


Mbunge maarufu wa Chadema, Godbless Lema alikuwa wa kwanza kueleza bayana kutoafikiana na pongezi za Lowassa kwa Magufuli.


Baadaye, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, naye alieleza kuwa kauli za Lowassa ni zake binafsi na sio msimamo wa chama hicho.

Kadhalika, Mbowe alionekana kumkumbusha Lowassa kuhusu matukio mbalimbali yasiyopendeza katika utawala wa Magufuli

Lakini pengine aliyeeleza kwa kirefu kuhusu suala hilo ni Lissu, ambaye akiwa hospitalini huko Ubelgiji, alitoa waraka huu hapa chini.



Waheshimiwa habari za Tanzania na poleni kwa yote.
Naomba na mimi niseme kwa uchache kuhusu suala hili. Samahani kama 'uchache' wangu utakuwa mrefu kidogo.
Baada ya Mwenyekiti kuzungumzia jambo hili, inaelekea kuwa wazi kwamba Mheshimiwa Lowassa hakumshirikisha Mwenyekiti kabla ya kukubali au kuamua kwenda Ikulu kukutana na Rais Magufuli.
Na juzi tu wakubwa wetu hawa wawili walikuwa pamoja hospitalini kumsalimia Mzee Ngombale Mwiru.
Je, inawezekana Mheshimiwa Lowassa hakuwa anajua tayari kwamba ana appointment Ikulu?
Kama alikuwa anajua, kutokumshirikisha Mwenyekiti wake kuna tafsiri gani hasa?
Katika mazingira ya sasa ya Tanzania ya Magufuli, uamuzi wowote wa kufanya nae mazungumzo, hata kwa nia njema yoyote ile, bila kushauriana au kuwashirikisha viongozi wa juu wa chama, ni uamuzi usio sahihi na mgumu kukubalika.
Vile vile, kauli za aina ambayo tumeisikia leo kutoka kwa Mheshimiwa Lowassa, zina athari kubwa kisiasa.
Sio tu zinachanganya wanachama na wafuasi wetu, lakini pia zinawapa mtaji wa kisiasa maadui zetu.
Kuanzia sasa tutegemee sana kuwasikia maCCM yakishangilia 'busara' za Mheshimiwa Lowassa.
Masuala ya ukiukwaji haki za binadamu, uvunjwaji wa Katiba na mengine mengi sasa yatajibiwa kwa namna moja: Lowassa amemkubali Magufuli nyie wengine mnapiga kelele za nini.
Huu ni mtaji wa bure kwa Magufuli. Ukweli, ambao umesemwa sana humu, ni kwamba amefeli karibu katika kila jambo.
Hata hiyo reli anayosifiwa nayo na Lowassa bado ni ndoto tu: nani ajuaye itajengwa kwa hela za nani???
Za Wachina kama tulivyoambiwa mwanzoni; au za Waturuki kama tulivyoambiwa baadae; au za Afrika Kusini kama alivyosema mwenyewe anaenda kumwomba Zuma???
Kama chama hatujawahi kukataa mazungumzo na Rais au kiongozi mwingine yeyote wa serikali.
Na hatukatai kuzungumza na Magufuli kuhusu matatizo mengi na makubwa yanayoikabili nchi yetu.
Lakini ni muhimu na lazima viongozi wakuu wa chama washirikishane na washauriane kabla ya mazungumzo hayo.
Na baada ya mazungumzo, ni lazima viongozi wakubaliane juu ya kauli za kutoa hadharani kwa umma ili wote tuwe kwenye ukurasa mmoja.
Katika mazingira ya sasa, ambako viongozi na wanachama wetu wanashambuliwa hadharani kwa mapanga na hata kwa risasi, kumsifia Rais ni kumuunga mkono yeye na matendo yake.
Katika mazingira ya kesi nyingi za kutunga dhidi yetu, 'kazi nzuri' inayofanywa na Magufuli ina maana gani hasa, kama sio kuhalalisha ukandamizaji tunaofanyiwa.
Katika mazingira ambapo hata jumuiya ya kimataifa imeanza kuhoji mwenendo wa Rais Magufuli, kutoa kauli kwamba 'anafanya kazi nzuri' ni 'kumtupia taulo' la propaganda litakalomfichia madhambi mengi aliyowafanyia Watanzania katika miaka hii miwili.
Kwa vyovyote vile, kitendo cha Mheshimiwa Lowassa sio cha kunyamaziwa au kuhalalishwa kwa hoja nyepesi nyepesi.
TUNDU LISSU(MB).
Top of Form

Kadhalika, kada maarufu wa kike wa chama hicho, Hilda Newton nae alieleza masikitiko yake kutokana na kauli za Lowassa.



Kama alivyotahadharisha Lissu, ni wazi kwamba CCM watakuwa wamepewa “silaha” mpya katika “kumpamba” Magufuli na “kuwapenda” wapinzani, kwamba “hata Lowassa wenu anamkubali Magufuli.” Na ni rahisi kwa CCM kuonekana wana mantiki katika hoja hiyo, kwa kudai “kama mtu muhimu kabisa kwenye chama chenu (yaani Lowassa) ambaye ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Magufuli kwenye uchaguzi mkuu uliopita, anamkubali mkuu huyo wa nchi, ninyi ni akina nani kumpinga?”

Wakati ni wazi kwamba uamuzi wa Lowassa kukutana na Magufuli, na kumwagia pongezi, umezua “sintofahamu” huko Chadema, kuna masuala kadhaa ya muhimu yanayopaswa kuangaliwa kwa makini kwa ajili ya mustakabali wa chama hicho.

Kwanza, ni muhimu kwa viongozi na wanachama wa Chadema kutambua nafasi ya Lowassa katika chama hicho. Wakati baadhi ya wachambuzi wa siasa – mie nikiwa mmoja wao – wanaamini kuwa ujio wa Lowassa katika chama hicho ulikuwa na hasara zaidi kuliko faida, jitihada zilizofanywa na chama hicho kumpigania mwanasiasa huyo zimemjengea hadhi ambayo haipo kwa mwanasiasa mwingine yoyote ndani na nje ya chama hicho.

Ikumbukwe kuwa hadi wakati jina lake lilipokatwa na vikao vya CCM katika mchakato wa kusaka mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho tawala, Lowassa alikuwa ndiye mwanasiasa maarufu kuliko wote Tanzania. Yayumkinika kusema alikuwa mtu wa pili kwa umaarufu baada ya marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Licha ya kulazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008 kutokana na kashfa ya Richmond, Lowassa aliendelea kuwa mwanasiasa maarufu na mwenye nguvu kuliko yeyote yule ndani ya CCM, hata zaidi ya Rais na mwenyekiti wa taifa wa chama hicho wakati huo, Jakaya Kikwete.

Na japo kukatwa kwa jina la Lowassa huko CCM kulimpunguzia kidogo umaarufu wake kwa siasa za Tanzania – ilikuwa kama miujiza kuona CCM ilikuwa na ujasiri wa kukata jina la mwanasiasa huyo- alihamia Chadema akiwa na sapoti ya kutosha kiasi japo si kubwa kama ilivyotarajiwa.

Japo kuna “tuliopishana nae mlangoni” – kwa maana yeye alipoingia, sie tukatoka – ujio wake ulipelekea kuwa mwanasiasa maarufu zaidi ya wote wa Upinzani. Na ndio maana haikuwa vigumu kwake kupitishwa kuwa mgombea urais kwa tiketi ya UKAWA.

Nimeeleza kuwa baadhi yetu “tulipishana nae mlangoni” kwa sababu mie binafsi nilikuwa naiunga mkono Chadema, si kama mwanachama bali ukweli kwamba kwa muda mrefu nimekuwa nikijihusisha na harakati za mapambano dhidi ya ufisadi, na chama hicho kilijitokeza kuwa championi wa mapambano hayo. Kwahiyo, “naturally” nilijikuita nikikiunga mkono.

Hata hivyo, ujio wa Lowassa katika chama hicho ulinikimbiza. Sababu kuu ni binafsi zaidi, na nisingependa kuongelea hapa, lakini sababu nyingine ni kile nilichotafsiri kama usaliti wa Chadema. Ikumbukwe kuwa tangu mwaka 2006, chama hicho “kilimkalia kooni” Lowassa kumtuhumu kuwa ni fisadi, na ndicho kilichofanya jitihada kubwa zilizopelekea mwanasiasa huyo kujiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008.

Sasa bila hata kutumia jitihada kidogo tu za busara, chama kilichomwandama Lowassa kuwa ni fisadi, kwa miaka 9 mfululizo, yaani 2006 hadi 2015, kilionekana kituko kwa baadhi yetu tuliokuwa tukikiamini, kwa sababu, pamoja na mengine, isingewezekana kutumia miezi mitatu (Julai 2015 Lowassa alipojiunga na chama hicho hadi Oktoba wakati wa uchaguzi mkuu) kumsafisha vya kutosha.

Na gharama ya ujio wa Lowassa ilikuwa kubwa. Moja kubwa zaidi ilikuwa lazima kwa Chadema “kuitosa” turufu yake muhimu, ajenda ya vita dhidi ya ufisadi. Ililazimika kufanya hivyo kwa sababu kuzungumzia ufisadi ilhali chama hicho kimemkumbatia mwanasiasa kiliyemwita “baba wa ufisadi” kwa miaka 9 mfululizo ingeonekana kioja.

Kadhalika, kwa kumpokea Lowassa, Chadema ilikuwa haina jinsi ya kukwepa tuhuma kutoka CCM kuwa chama hicho upinzani ni cha kifisadi kwa sababu ya kumkumbatia mwanasiasa ambaye kilikuwa kikimuita fisadi. Jitihada za Chadema kujibu mashambulizi kuwa “kama Lowassa ni fisadi mbona hajachukuliwa hatua,” zilikuwa hazina mashiko.

Lakini jingine lililoipa jeuri CCM ni ukweli kwamba kwa chama hicho, Lowassa alikuwa ni “makapi” sambamba na wanasiasa wengine waliomfuata huko Chadema. Hiyo ilikipa chama hicho tawala “jeuri” ya namna flani. Na waliitumia vema kwenye kampeni, kwamba “hawa jamaa si lolote si chochote. Yani wameshindwa hata kutafuta mgombea wao wenyewe mpaka wakasubiri makapi kutoka kwetu ndo wakapata mgombea urais.” Na pamoja na maneno hayo kuwa machungu, ndo ukweli ulivyokuwa.

Chadema na UKAWA kwa ujumla walikuwa na takriban mwaka mzima wa kujipanga; kuafikiana kuhusu mgombea urais kwa tiketi ya umoja huo, na kumnadi, huku wakitumia “advantage” ya “vita vya wenyewe kwa wenyewe” kati ya zaidi ya makada 40 waliokuwa wakichuana kuteuliwa na CCM.

Badala yake, kumbe tayari kulikuwa na makubaliano ya siri kati ya uongozi wa baadhi ya viongozi wa juu wa Chadema kwamba wasubiri kutangaza mgombea wao hadi baada ya mchakato wa CCM kupata mgombea wake, ka maana ya “kumhifadhia nafasi Lowassa endapo jina lake litakatwa huko CCM.”

Kabla ya kwenda mbali na makala hii ningependa nishauri Chadema irejee suala hilo la Lowassa kuandaliwa nafasi ya kuwania urais japo wakati huo alikuwa CCM. Hatua stahili zinapaswa kuchuliwa dhidi ya wote waliohusika na mpango huo.

Na ujio wa Lowassa ulipelekea Chadema kumpelekea mmoja wa magwiji wa siasa za upinzani, Dokta Willbrord Slaa. Umahiri wa Dokta Slaa haukuwa tu katika kuchukia ufisadi kwa dhati bali umahiri wake mkubwa katika kujenga hoja kisomi. Kadhalika, alikuwa akiaminiwa na watu mbalimbali muhimu ndani ya serikali, kiasi kwamba baadhi yao walihatarisha ajira zao kwa kumpatia mwanasiasa huyo nyaraka muhimu zilizoiwezesha Chadema kuwa na ushahidi mbalimbali katika vita yake dhidi ya ufisadi.

Na kuonyesha kuwa alikuwa na msimamo imara, Dokta Slaa aliamua kujiweka kando katika uongozi kupinga Lowassa kupewa ugombea urais wa UKAWA. Lakini jambo la kusikitisha mno, kiongozi huyo aliyekifanyia mengi chama hicho alidhalilishwa na kutukanwa kupita kiasi.
Na “akina sie” tulishindwa kustahimili ujio wa Lowassa, na kwa vile kwa baadhi yetu ilikuwa muhimu kumzuwia asiingie Ikulu, na hivyo kulazimika kumpigia kampeni mpinzani wake yaani Magufuli, tulitukanwa kila aina ya matusi. Sijui watu hawa waliojitoa ufahamu wataweka wapi sura zao pindi Lowassa “akirejea nyumbani” CCM.

Wakati anajiweka kando na uongozi wa Chadema, Dokta Slaa alikitahadharisha chama hicho kuwa ili kuleta mabadiliko ya kweli (badala ya hayo “ya kisanii” aliyokuwa akiyanadi Lowassa) chama hicho kinahitaji mkakati makini utakaoongozwa na watu makini. Na kwa hakika, tangu wakati huo, Chadema imekuwa kama kundi la wanaharakati wa kudandia hoja kuliko chama cha siasa chenye ajenda ya kueleweka. Uamuzi wa kuitelekeza ajenda ya vita dhidi ya ufisadi ulipelekea chama hicho kutokuwa na ajenda moja ya maana, huku CCM “wakipora” kiurahisi ajenda ya vita dhidi ya ufisadi.

Je mustakabali wa Chadema ukoje? Japo sio rahisi sana kubashiri kwa uhakika kuhusu hatma ya chama hicho, binafsi – kwa kutumia uzoefu wangu na uelewa wa kutosha wa siasa za Tanzania, sambamba na kuwa na fursa ya kufahamu “yanayojiri nyuma ya pazia” la siasa za nchi yetu – ninadhani kuwa kuna uwezekano mkubwa tu kwa Lowassa kurudi CCM kama sio kuachana kabisa na siasa.

Kwanini Lowassa anaweza kurudi CCM? Kuna sababu kuu mbili. Moja ni dalili za wazi kuwa ndoto zake za urais kupitia chama hicho ni kama zimeyeyuka. Umaarufu wake umegubikwa na kuibuka na kuimarika kwa umaarufu wa Lissu. Ni dhahiri kwamba ikipigwa kura ya maoni kuwa nani kati ya Lowassa na Lissu awe mgombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020, Lissu ataibuka mshindi. Na Lowassa anafahamu kuwa hakuna njia ya mkato kwa yeye “kulazimisha” awe mgombea katika uchaguzi mkuu huo ujao, licha ya ukweli kwamba alishatangaza kuwa atagombea.

Sababu nyingine ni binafsi zaidi. Lowassa ni mmoja wa matajiri wakubwa nchini Tanzania. Kama utajiri huo ulipatikana kihalali au kifisadi, si lengo la makala hii kujiingiza katika mjadala huo. Lililo wazi ni ukweli kwamba licha ya kuwa mwanasiasa, yeye pia ni mfanyabiashara. Na kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, serikali ya Magufuli imefanikiwa kutumia nyenzo yake muhimu dhidi ya wapinzani ambao pia ni wafanyabiashara, KODI.

Inaelezwa pia kwamba mali mbalimbali za mwanasiasa huyo zipo hatarini kutokana na uwepo wake huko Upinzani. Inadaiwa kuwa hata jengo la Tanesco Ubungo ambalo serikali imetangaza kulivunja, linamilikiwa na Lowassa, na tishio la kulivunja lilikuwa kama kufikisha ujumbe kwake.

Katika hili, Lowassa hatoonekana mtu wa ajabu akiamua kurudi CCM ili asibughudhiwe kuhusu biashara na mali zake. Ni nani kati yetu anayeweza kujitoa mhanga kwa ajili tu ya imani yake ya siasa? Si kama hawapo ila ni adimu mnooo! Na kibaya zaidi, hata akiamua kung’ang’ania huko Chadema, hatma yake na ya chama hicho haieleweki kwa sababu hadi muda huu – na hii ni licha ya zuwio la Magufuli dhidi ya vyama vya upinzani kufanya shughuli zao za siasa – chama hicho kikuu cha upinzani “kipo kipo” tu. Hakina ajenda moja ya kueleweka zaidi ya kudandia kila tukio linalojiri.

Iwapo Lowassa ataamua kubaki Chadema, hiyo itakuwa fursa mwafaka kwa chama hicho kumpumzisha. Naamini kuwa wana-Chadema wakiweka kando ushabiki wa kisiasa, wanafahamu fika kuwa mwanasiasa huyo hana nguvu, uwezo wala mvuto wa kukabiliana na siasa hatari zinazoendelea muda huu huko nyumbani.

Kwa upande mwingine, tukio la Lowassa kukutana na Magufuli Ikulu linaweza pia kuhusishwa na tamko la hivi karibuni la Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad, ambaye kama Lowassa, alimmwagia sifa Magufuli.

Nimefanya uchambuzi kuhusu kauli za wanasiasa hao wawili hapa, lakini ninachoweza kugusia hapa ni haja ya kutambua kuwa wanasiasa hao bado wanatunzwa na serikali kutokana na nyadhifa walizowahi kushika huko nyuma. Haihitaji uelewa mkubwa kuhusu "siasa za kibabe" kuhisi kwamba huenda "malezi" wanayopewa na serikali yametumika kama "chambo" cha kuwavuta karibu na Magufuli.

Kuhusu matatizo yanayoikabili Chadema muda huu,ukweli ni kwamba ni zaidi ya uwepo wa Lowassa ndani ya chama hicho. Japo huu ni ukweli mchungu usioruhusiwa kabisa kusikika ndani ya chama hicho, licha ya kazi nzuri ya kuifikisha Chadema ilipo leo, mwenyekiti wa taifa Mbowe anapaswa kutoa fursa kwa wana-Chadema wengine kusukuma gurudumu la chama hicho. Na hatua hiyo wala haihusiani na mchango wake mkubwa wa kumleta Lowassa ndani ya chama hicho na “kumpa” ugombea urais wa UKAWA.

Kirefu cha Chadema ni Chama cha DEMOKRASIA na Maendeleo. Sasa ni demokrasia gani hiyo ambayo inaruhusu mwenyekiti mmoja kuwa madarakani milele? What if “uenyekiti wa milele” ni miongoni mwa vikwazo kwa maendeleo ya chama hicho?

Lakini hata kama “muda wa Mbowe kutoka madarakani haujafika,” busara tu inapaswa kumfahamisha kiongozi huyo kuwa ni vema kuzingatia busara za akina Nyerere waliojing’atua wakiwa bado wanahitajika. Sipendi kubashiri hili, lakini laiti Mbowe asipohamasisha mageuzi kwenye medani ya uongozi wa chama hicho, haitokuwa jambo la ajabu akiishia kung’olewa kwa nguvu.

Na kwa bahati mbaya kwake, hili “songombingo” alilolianzisha Lowassa jana linaweza kuwa kama mnyororo mrefu ambao mahala flani yupo Mbowe. Ndiye aliyemkaribisha Lowassa.

Moja ya mapungufu makubwa mno yanayoitafuna Chadema muda huu ni pamoja na kulipuuza kundi muhimu linalokisaidia mno chama hicho, lundo la vijana wanaoshinda na kukesha katika mitandao ya kijamii wakijaribu kukinadi chama hicho angalau kwa kuikemea serikali ya Magufuli au CCM kwa ujumla.

Laiti chama hicho kingekuwa na ajenda ya kueleweka, basi jeshi hili la vijana lingekuwa nyenzo muhimu mno. Ni rahisi kuwalaumu vijana hawa kuwa “kazi yao kubwa ni kudandia hoja tu,” lakini ukweli ni kwamba chama chao hakiwapatii ajenda ya/za kueleweka. Kibaya zaidi, hata pale wanapojaribu kutengeneza ajenda wao wenyewe – kwa mfano jitihada za kumsaka Ben Saanane – hawapati sapoti ya kutosha kutoka uongozi wa juu wa chama hicho.

Ni hivi, wengi wa hawa vijana wanahatarisha maisha yao kwa kuwa tu “upande usiotakiwa” na serikali ya Magufuli. Hawategemei malipo yoyote zaidi ya kuamini kuwa siku moja wanaweza kukiingiza chama chao madarakani. Hakuna jitihada za makusudi za uongozi wa juu wa chama hicho kuwa karibu na kundi hili muhimu.

Ukiwa UVCCM una uhakika wa angalau “kuhongwa na Bashite” au kualikwa kwenye “mnuso” sehemu flani. Lakini ukiwa kijana wa upinzani, “zawadi” kubwa yaweza kuwa kusumbuliwa na vyombo vya dola na kuishi maisha ya wasiwasi. Kwahiyo vijana wa upinzani wana kila sababu ya kuichukia siasa, kwa sababu inahatarisha maisha yao, lakini mapenzi yao katika imani ya chama inawalazimisha kung’ang’ania hivyo hivyo.

Niionye Chadema kuwa katika zama hizi za “ununuzi wa binadamu kama zama za utumwa,” chama hicho kisishangae pindi wengi wa vijana hawa watakapoamua kubwaga manyanga na kukubali “kununuliwa.” Kwanini waendelee kuhatarisha maisha yao ilhali uongozi wa juu wa chama hicho hauna muda nao?

Akina Hilda Newton, Ben Malisa, Bob Wangwe, Ndehani Mwenda, Noel Shao, Gift Nanyaro ni miongoni mwa vijana wanaofanya kazi kubwa kwa ajili ya Chadema, bila ya matarajio ya malipo au fadhila flani, zaidi ya kuhatarisha maisha yao. Kama ilivyo kawaida ya mwanadamu yeyote yule, inaweza kufika mahala mtu akarudi nyuma na kujiuliza, “is it worth it?” Na japo sitarajii kuona makada hao vijana wakiamua kuipa kisogo Chadema, lakini sintoshangaa baadhi yao wakiamua kuipa kisogo siasa, hasa kama tasnia hiyo itaendelea kuwa “yenye manufaa kwa genge flani tu.”

Nihitimishe makala hii kwa kukuhamasisha msomaji kujipatia nakala yako ya kitabu changu kipya cha kielektroniki kinachochambua kwa kina miaka miwili ya utawala wa Magufuli. 




Baadhi ya niliyaoyazungumzia kwenye makala hii yamezungumwa kwa kirefu katika kitabu hicho ambacho hakielemei upande wowote. Kitabu hicho kwa sasa kinasubiri uzinduzi rasmi utakaokiwezesha kununulika kwa “mobile money” kama m-pesa, tigopesa,nk. Nitawataarifu. Ila kwa wasiohitaji kusubiri, waweza kukinunua HAPA

31 Oct 2017



Pasipo kutarajiwa, jana, Jumatatu ya Oktoba 30, 2017, anga za habari huko nyumbani Tanzania zilitawaliwa na habari moja nzito: mmoja wa wana-CCM maarufu, Mbunge kwa tiketi ya chama hicho tawala anayewakilisha jimbo la Singida Kaskazini, na Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bwana Lazaro Nyalandu, alitangaza kujivua uanachama wa CCM na kuomba kujiunga na chama kikuu cha upinzani cha Chadema.


Tukio hilo lilileta mshangao mkubwa kwa sababu kadhaa. Kwanza, licha ya matamshi ya hivi karibuni ya Nyalandu kuhusu haja ya kurejeshwa mchakato wa Katiba mpya, sambamba na kuwasihi wabunge wenzie wa CCM kupinga kwa nguvu zote jaribio la kurefusha muda wa Rais madarakani, hakukuwa na dalili kubwa na za waziwazi iwapo kuna ‘kutofautiana’ kati ya Nyalandu na chama chake.


Na hata kama kungekuwa na dalili hizo – kwa kificho au wazi – bado wananchi wengi wangepokea habari hizo kwa mshtuko mkubwa.

Sababu ya pili ya mshangao kuhusu tukio hilo ni ukweli kwamba mwanasiasa wa chama tawala kuamua kujiunga na upinzani, tena miaka mitatu hivi kabla ya uchaguzi mkuu, ni suala ambalo licha ya kuhitaji ujasiri mkubwa pia linaacha maswali kadhaa ambayo pengine sio rahisi kuyapatia majibu.

Hadi wakati ninaandika uchambuzi huu, kilicho bayana kuhusu sababu za Nyalandu kuchukua uamuzi huo ni sababu alizotanabaisha mwenyewe katika tamko lake kwa umma.

Akizungumza jana, mwanasiasa huyo alidai sababu ya kuchukua uamuzi huo ni kutokuridhishwa na mwenendo wa hali ya kisiasa nchini ikiwa ni pamoja na ukiukwaji wa haki za kibinadamu, ongezeko la vitendo vya dhuluma wanavyofanyiwa Watanzania na kutokuwepo kwa mipaka ya wazi ya mihimili ya dola yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

Lakini hata kabla ya kuchukua uamuzi huo jana, Nyalandu alishaonyesha dalili ya kutofautiana na wana-CCM wenzie, hasa kwa uamuzi wake wa kumtembelea Mbunge Tundu Lissu wa Chadema aliyelazwa huko Nairobi, Kenya kufuatia jaribio la kumuua. Hadi sasa, Nyalandu anabaki kuwa kiongozi wa ngazi za juu wa CCM kumtembelea Lissu huko Kenya.


Huku kukiwa na tetesi kwamba uongozi wa juu wa CCM umewapiga marufuku viongozi wake kujihusisha na suala la Lissu, uamuzi wa Nyalandu kwenye Kenya ‘kinyume na maagizo ya chama chake’ ulihisiwa kuwa ungemwingiza matatizoni.

Dalili nyingine kuwa mwanasiasa huyo hakuwa akipendezwa na baadhi ya mienendo ndani ya CCM ni pale alipoibuka kuhamasisha haja ya kuanzisha upya mchakato wa kupatikana Katiba mpya, sambamba na kuhamasisha wana-CCM wenzake dhidi ya jitihada za chini chini kuongeza muda wa Rais madarakani.

Masuala yote hayo mawili yalitarajiwa ‘kumsababishia matatizo’ mwanasiasa huyo.

Hata hivyo, kuna ‘sababu mbadala’ kuhusu uamuzi wa Nyalandu kujiuzulu. Kuna taarifa kwamba kuna uchunguzi unaofanyika dhidi ya mwanasiasa huyo kuhusiana na utumishi wake kama Waziri wa zamani wa Maliasi na Utalii. Taarifa hizo ambazo bado ni tetesi hadi muda huu, zinaweza kupewa uzito zaidi na ‘screenshot’ inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, ikidaiwa kuwa ni ya mazungumzo ya kundi la Whatsapp la viongozi wanawake wa CCM.

Katika ‘chat’ husika, mmoja wa makada wa kike wa CCM anadai kuwa kuna uchunguzi unaofanyika dhidi ya Nyalandu alipokuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, na kwamba uamuzi wa kujiondoa CCM na kuomba kujiunga na Chadema una lengo la kugeuza suala hilo kuwa la kisiasa pindi akichukuliwa hatua.

Pengine swali muhimu linaloendelea kutawala vichwa ni “kwanini HASWA Nyalandu amejiuzulu?” Kuna sababu alizotoa yeye mwenyewe, ambazo kwa kiasi kikubwa zinaleta mantiki, lakini pia kuna hiyo tetesi kuwa amechukua uamuzi huo kama tahadhari pindi akianzishiwa tuhuma za ufisadi.

Tuchambue sababu zote mbili, yaani alizotoa mwenyewe na hizo tetesi. Kwa vile hatuna maelezo yenye uhakika yaliyo kinyume na sababu alizotoa Nyalandu, nadhani kwa kuzingatia busara tu, itakuwa sio sahihi kudhani anaongopa. Unapopinga kauli ya mtu basi shurti uwe na kauli mbadala yenye uthibitisho. Kwahiyo, angalau kwa muda huu, hakuna sababu za msingi za kupinga sababu alizotoa mwanasiasa huyo.

Kuhusu tetesi za kuwepo kwa mchakato wa ‘kumshughulikia kutokana na tuhuma za ufisadi,’ kuna mantiki kwa mbali, na utata kwa mbali pia. Sio siri kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii ilikuwa kama ‘makao makuu’ ya ufisadi. Wizara hiyo ilikuwa kama ile ya Nishati na Madini, ambapo mawaziri lukuki walihamishwa au kuondolewa madarakani kutokana na tuhuma za ufisadi.

Kwamba Nyalandu alipokuwa Waziri wa Maliasili na Utalii kulikuwa na tuhuma za ufisadi, hilo halina mjadala. Lakini kwa kuzingatia kanuni ya asili ya haki, tuhuma hizo zinabaki tuhuma tu mpaka zitakapothibitishwa.

Kwahiyo, hadi hapa, mantiki ya mbali kuhusu uwezekano wa uchunguzi wa tuhuma za ufisadi dhidi ya Nyalandu ipo. Hata hivyo, utata wa mbali ni kwamba katika mazingira ya kawaida tu, na tukijifanya kuamini (angalau kwa minajili ya uchambuzi huu) kwa Nyalandu anafahamu kuhusu uchunguzi huo, je isingekuwa mwafaka kwa yeye kupambana na suala hilo akiwa CCM kuliko nje ya chama hicho tawala?

Sawa, kuna hiyo hoja ya “amehama CCM na anataka kuhamia Chadema ili pindi akichukuliwa hatua, suala hilo lionekane la kisiasa,” lakini ikumbukwe kuwa suala la muhimu sio “suala lionekane la kisiasa” bali “lisitokee kabisa.” Na katika mazingira ya kawaida, huo uamuzi wa tu Nyalandu kuhama CCM na kuikosoa hadharani unatosha kuipa serikali ya chama hicho tawala na taasisi zake “hasira” dhidi ya mwanasiasa huyo. Na hapo hatujagusia uwezekano wa mwanasiasa huyo kujiunga na “adui nambari moja wa CCM” yaani Chadema.

Kwa mtazamo wangu, kama ni kweli kuna uchunguzi unaoendelea au unaotarajiwa kufanyika kuhusu Nyalandu basi yayumkinika kuhisi kwamba ingekuwa rahisi zaidi kwa yeye kupambana na suala hilo akiwa ndani ya CCM kuliko nje ya chama hicho chenye historia ya siasa za kinyongo, visasi na majitaka.

Lakini kuna ‘angle’ kubwa zaidi katika uamuzi huo wa Nyalandu. Yawezekana amesoma vema upepo wa kisiasa huko nyumbani chini ya utawala wa Rais Magufuli, na kubaini vitu kadhaa. Moja laweza kuwa kinachoonekana kama wananchi wengi kutoridhishwa na utawala wa Magufuli, ndani na nje ya CCM. Keyword hapa ni ‘kinachoonekana,’ nikimaanisha pengine ni hisia tu kuwa kuna wananchi wengi wasioridhishwa ilhali ukweli ni kinyume na hisia hiyo.

Kwa minajili ya uchambuzi huu, tufanye kuwa hisia hizo zipo kweli. Kwahiyo, kwa vile Nyalandu alikuwa miongoni mwa makada wa CCM walioomba ridhaa ya chama hicho kuwa wagombea wa urais mwaka 2015 lakini haukufanikiwa, basi pengine anataka kutupa kete yake kupitia upande wa upinzani.

Lakini sio tu kusukumwa na nia ya kuwania urais, lakini yayumkinika kuhisi kuwa mazingira yaliyopo muda huu yanampatia mwana-CCM yeyote nafasi nzuri ya kukikimbia chama hicho. Sio siri kuwa hisia kwamba Magufuli ana dalili za udikteta zinazidi kushika hatamu. Kwa maana hiyo, hata mtu mwenye sababu zake binafsi akikurupuka na kutamka “ninahama CCM kwa sababu utawala wa Magufuli ni wa kidikteta” ataeleweka kirahisi, na anaweza kuungwa mkono kirahisi pia.

Kwamba Nyalandu anaweza “kuruka kutoka kwenye ngalawa na kuingia majini kwenye bahari yenye papa na nyangumi” sio suala dogo. Kama kuikosoa CCM ukiwa ndani ya chama hicho ni hatari, sote twafahamu nini kinachoweza kumkumba anayediriki sio kukosoa tu bali pia kuhama chama hicho tawala. Kwa mantiki hiyo, kwa sababu yoyote ile – iwe hizo alizotaja mwenyewe au tetesi za uchunguzi wa ufisadi – mwanasiasa huyo amefanya maamuzi magumu, na yayumkinika kuamini kuwa amejiridhisha vya kutosha kabla ya kuchukua uamuzi huo.

Kuna mambo matatu yanayoweza kutoa mwangaza kidogo. Kwanza, hivi karibuni, Waziri mpya wa Maliasili na Utalii, Dokta Hamis Kigwangallah alinukuliwa akisema kwamba anayo orodha ya watu mashuhuri, viongozi wastaafu na wabunge wanaojihusisha na ujangili, na atahakikisha anawashughulikia.

Pili, jana katika hotuba yake akiwa huko Mwanza, Rais Magufuli alikumbushia kuhusu Mahakama Maalum ya Ufisadi, ambayo pasi kuuma maneno, imekuwa kama kichekesho kutokana na kukosa kesi. Rais kuitaja mahakama hiyo ‘isiyo na ufanisi angalau hadi sasa’ inaweza kumaanisha kilekile alichokigusia Waziri Kigwangallah kuhusu ujangili.

Na tatu, ‘vijana wa Lumumba’ (makada wa CCM kwenye mitandao ya kijamii) walishaanza kuzungumzia ‘ufisadi wa Nyalandu’ mara tu alipoenda Nairobi kumjulia hali Lissu. Na kasi yao ya mashambulizi dhidi ya Nyalandu imepamba moto zaidi jana baada ya mwanasiasa huyo kutangaza kujiondoa katika chama hicho tawala.

Lakini pia kuna tamko la Humprey Polepole, ‘katibu Mwenezi’ wa CCM kuhusu uamuzi huo wa Nyalandu. Binafsi nilitarajia tamko kali na pengine lililosheheni kebehi kama sio kashfa (na Polepole ni hodari sana kwenye maeneo hayo), lakini reaction ya msemaji huyo wa CCM imekuwa ‘muted.’ Sana sana ameishia kudai kuwa Nyalandu amejiondoa kwa sababu ameshindwa kuendana na kasi ya awamu ya tano. Pia amejaribu kuonyesha kuwa mwanasiasa huyo sio ‘mtu mkubwa’ ndani ya chama hicho tawala. Huyu si Polepole tunayemfahamu kwa umahiri wake wa ‘kusema ovyo.’ Huenda ‘upole’ wake una sababu flani.

Japo kauli ya Kigwangallah na ya Rais Magufuli, sambamba na ‘vijana wa Lumumba’ kumwandama Nyalandu, na ‘upole’ wa Polepole yanaweza kuwa mambo ya kawaida tu, lakini pia yanaweza kutoa mwangaza kuhusu uamuzi huo wa Nyalandu. Hata hivyo, kama nilivyotanabaisha awali, sidhani kama mazingira hayo yangetosha kumfanya Nyalandu kuchukua uamuzi huo mzito.

Kwamba Nyalandu ataandamwa baada ya kuchukua uamuzi huo, hilo halina mjadala. Kama asipoandamwa na ngazi za juu za CCM au kupitia taasisi za dola/umma basi ‘vijana wa Lumumba’ watakesha mitandaoni kumchafua. Pamoja na ukongwe wake katika siasa si Tanzania tu bali barani Afrika kwa ujumla, kwa kiasi kikubwa CCM inaendekeza mno siasa za kisasi, kinyongo na adui mkubwa wa ukweli. Kuikosoa CCM au serikali yake ni kama kusaini ruhusa ya kusumbuliwa kwa kila namna.



Na ni muhimu kutambua kuwa Nyalandu alikuwa akifahamu kuhusu ‘mabalaa’ yanayomsubiri baada ya kuchukua uamuzi huo mzito. Angalia yanayomsibu Yusuph Manji, mtu aliyemwaga mamilioni ya fedha kuifadhili CCM lakini amebaki kuwa ‘kielelezo cha hasira za CCM.’

Je CCM wakiamua kulipa kisasi kwa Nyalandu watafanikiwa? Inategemea sana busara za Magufuli. Yote yanayoelezwa kuwa ‘ufisadi wa Nyalandu’ yailikuwa na baraka za mtangulizi wa Magufuli, yaani Rais Kikwete. Kwahiyo, kama ambavyo jitihada zozote za kumbana Lowassa zilivyoshindikana kwa vile zingeishia kumchafua pia Kikwete, ndivyo jaribio la ‘kulipiza kisasi kwa Nyalandu’ linavyoweza kumtia matatani JK.


Licha ya kuelezwa kuwa Nyalandu alikuwa mmoja wa watu wa karibu wa JK, pia ni muhimu kutambua kuwa mmoja wa watu wake wa karibu ni mke wa Rais mstaafu Benjamin Mkapa, Mama Anna. Mara baada ya kurejea Tanzania kutoka Marekani, Nyalandu alikuwa miongoni mwa washauri Mama Anna Mkapa, katika uendeshaji wa taasisi ya Mfuko wa Fursa Sawa kwa Wote (EOTF).

Kwa maana hiyo, jaribio lolote la ‘kumwandama Nyalandu’ linaweza kuzua kile Waingereza wanaita ‘unintended consequences,’ au ‘matokeo yasiyokusudiwa kwa Kiswahili.

Pia ni muhimu kutambua u-kimataifa wa Nyalandu. Mwanasiasa huyo ana mahusiano mazuri na wanasiasa wenye nguvu kubwa hususan nchini Marekani. Japo ‘nguvu’ zao zinaweza kutofua dafu kwa Magufuli, lakini sote twafahamu kuwa ni vigumu kwa Tanzania yetu kuwa na ‘jeuri’ katika umasikini wetu.


Hatma ya Nyalandu akifanikiwa kuhamia Chadema ikoje? Binafsi, ninahisi mambo makuu mawili. Kwanza, ujio wake katika chama hicho kikuu cha upinzani unaweza kuamsha msisimko mpya wa siasa za ndani na nje ya chama hicho, na Tanzania kwa ujumla.

Kwa upande mmoja, anaweza kuendeleza hoja zake kama hiyo ya kudai kurejeshwa kwa mchakato wa Katiba mpya, suala ambalo Chadema na washirika wake wa UKAWA ni kama wamelitelekeza.

Lakini pengine kubwa zaidi ni uwezekano mkubwa wa Nyalandu kuwa mmoja wa wagombea wa Urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi mkuu ujao mwaka 2020. Kwamba amejiondoa CCM kwa hiari yake (angalau kwa mujibu tunachofahamu hadi muda huu) na kujiunga na Chadema kwa hiari yake, anaweza kuwa na faida ya ziada kuliko majina mengine mawili yanayotajwa kuhusu urais mwaka 2020 kupitia Chadema, Mawaziri Wakuu wa zamani, Lowassa na Sumaye.


Kwamba Nyalandu ni ‘mwana-CCM pekee aliyemjali Lissu kwa kumtembelea huko Nairobi,’ na ukweli kuwa yeye na Lissu wanatoka mkoa mmoja, wanaweza kujenga ‘dream team’ inayoweza kuirejesha Chadema enzi za kina Dkt Slaa, Zitto na Mbowe.

Lakini pia katika mazingira yaliyopo sasa, Chadema imekuwa kama haina mpango wa kushiriki uchaguzi mkuu ujao. Maandalizi yanayopaswa kufanyika sasa – miezi 36 tu kabla ya uchaguzi huo – ni kama hayapo. Ndiyo, Magufuli kapiga marufuku shughuli za kisiasa, lakini ni lini Rais kutoka CCM aliwahi kuridhika shughuli za wapinzani?

Kwa maana hiyo, ujio wa Nyalandu unaweza kuamsha matumaini kwa chama hicho kikuu cha upinzani kuhusu nafasi yake katika uchaguzi mkuu ujao.

Hata hivyo, kuna vikwazo vikuu viwili. Cha kwanza, ni lile lililojiri baada ya Lowassa kujiunga na CCM, Kwa minajili ya kumbukumbu tu, Chadema ilimwandama Lowassa kuwa ni ‘baba wa ufisadi’ kwa takriban miaka 9 mfululizo, kisha ghafla wakampokea na kumfanya mgombea wao wa Urais katika uchaguzi mkuu uliopita. Kwa busara za kawaida tu, huwezi kumchafua mtu kwa muda wote huo kisha ukategemea kumsafisha ndani ya miezi mitatu. Japo makada wa chama hicho hawataafiki, athari za kumpokea Lowassa na kumfanya mgombea wao zinaendelea kukisumbua chama hicho.

Kama ilivyokuwa kwa Lowassa, baadhi ya viongozi wa Chadema walishawahi ‘kumpaka’ Nyalandu wakimwita fisadi, hali inayoweza kutumiwa na CCM kudai kuwa ‘Chadema ni kimbilio la mafisadi.’ Hata hivyo ni rahisi kwa chama hicho cha upinzani kuwauliza CCM, “mpaka mwanasiasa awakimbie na kujiunga nasi ndio mnaanza kumwita fisadi?” Ni hoja inayoingilia akilini.


Je Nyalandu atapata mapokezi mazuri huko Chadema? Kama kauli ya Lowassa jana kuwa Chadema itakuwa ‘imelamba dume’ pindi Nyalandu akijiunga na chama hicho inaashiria chochote basi kuna uwezekano mkubwa wa mafanikio makubwa kwa mwanasiasa huyo.

Hata hivyo, ukweli kwamba Nyalandu ni miongoni mwa watu wenye sifa na uwezo wa kuwa wagombea urais kwa tiketi ya Chadema mwaka 2020 unaweza kupelekea mgongano dhidi yake na majina mengine yanayotarajiwa kuwemo kwenye kinyang’anyiro hicho, yaani Lowassa, Sumaye na Lissu.

Hili sio tatizo kubwa sana iwapo maslahi ya Chadema – badala ya maslahi ya mtu au kikundi binafsi – yakiwekwa mbele. Kwamba kufanyike tathmini ya kutosha kufahamu nani anayeweza kukiwezesha chama hicho kuing’oa CCM madarakani hapo mwaka 2020.

Kwamba Nyalandu anaweza kuleta hamasa kwa wana-CCM wengine (Membe?) kujiunga na Chadema, na kama ujio wake huko Chadema utaleta matokeo chanya, ni suala la muda. Lililo bayana hadi muda huu, uamuzi wake huo wa ghafla umetushtua wengi ikiwa ni pamoja na CCM na makada wake. Na yayumkinika kuamini kuwa uamuzi huo utaleta msisimko mpya katika siasa za Tanzania.

Mwisho, uchambuzi huu umetokana na uelewa wangu wa siasa za Tanzania, na unaweza kuwa sio sahihi kulingana na mitazamo tofauti. Jiskie huru kuchangia maoni, kunikosoa au hata pongezi zinaruhusiwa. Siku zote ninajitahidi kwenda mbali zaidi ya kuripoti tu matukio badala ya kuyachambua kwa undani zaidi. Asanteni na siku njema



30 Sept 2017

Mara baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka juzi nilipata ujumbe kutoka kwa watu kadhaa wakinieleza kuwa kwa namna moja au nyingine niliwasaidia kufanya maamuzi ya kumpigia kura aliyekuwa mgombea wa CCM, John Magufuli.

Unajua, moja ya makosa makubwa waliofanya wana-UKAWA kwenye kampeni za uchaguzi huo ni kutojihangaisha kulifikia kundi muhimu la wapigakura nchini Tanzania: wananchi wasiofungamana na chama chochote.

Ili kulielewa vema kundi hili, inabidi kuangalia idadi ya wanachama wa CCM na UKAWA (kwa kuzingatia uchaguzi wa mwaka 2015). Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa CCM ina wanachama milioni 8. Makadirio ya idadi ya wanachama wa UKAWA ni angalau milioni 5. Kwahiyo makadirio ya jumla ya wapigakura wenye kufungamana na vyama vya siasa ni takriban milioni 13. Tanzania ina watu zaidi ya milioni 50, tukitoa hao milioni 13 tunabakiwa na watu milioni 37. Tukienda kwenye idadi ya waliojiandikisha kupiga kura walikuwa milioni 23 hivi. Kwahiyo, kimahesabu, takriban watu milioni 10 (milioni 23 waliojiandikisha kutoa milioni 13 wenye ufuasi wa vyama vya siasa) walikuwa wapigakura wasiojihusisha na chama chochote.

Tofauti na UKAWA ambayo viongozi na wanachama wake walielemea zaidi kuhamasishana wao kwa wao, wenzao wa CCM waliwalenga hao takriban milioni 10 wasiofungamana na chama chochote.

Na kimsingi, mie japo sikuwa mpigakura, nilikuwa katika kundi la watu wasio na vyama. Mara ya mwisho kuwa mwanachama wa chama cha siasa ilikuwa mwaka 2005, na takriban miaka 15 baadae, sheria ilinizuwia kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Mwaka 2006 nilianza kufuatilia skandali ya Richmond iliyokuwa ikimhusisha aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa. Naweza kwa uhakika kuwa nilikuwa bloga pekee niliyevalia njua suala hilo, sambamba na kuliandikia makala mbalimbali katika magazeti ya ‘Kulikoni’ na baadaye ‘Mtanzania’ na hatimaye Raia Mwema. Ufuatiliaji huo ulinigharimu mno lakini hilo si la muhimu kwa sasa.

Kutokana na bughudha niliyopata kuanzia mwaka 2006 na kuendelea, haikuwa ajabu kwa mie kuunga mkono harakati za Chadema kupambana na ufisadi. Na mwaka 2010 nilishiriki kikamilifu kumnadi mgombea urais wa Chadema, Dkt Wilbrord Slaa. Hata baada ya uchaguzi huo, niliendelea kuunga mkono sera hiyo ya ufisadi ya Chadema. Hata hivyo, sikuwahi kuwa mwanachama wa chama hicho.

Mwanzoni mwa mwaka 2015 nilikuwa miongoni mwa watu waliopiga kelele kwenye mitandao ya kijamii kuwataka UKAWA watangaze mgombea wao wa kiti cha urais mapema hasa ikizingatiwa kuwa CCM walikuwa na safari ndefu ya ‘kung’oana macho’ kugombea kuteuliwa na chama chao kuwania urais. Hata hivyo, kelele hizo hazikuzaa matunda, na utetezi mkubwa ulikuwa “UKAWA inajibidiisha kushughulikia daftari la wapigakura sambamba na kuhamasisha wapigakura watarajiwa kujiandikisha.” Hatimaye tulikuja kufahamu kuwa mbinu hiyo ya “kununua muda” ililenga kumwandalia nafasi Bwana Lowassa endapo asingepitishwa huko CCM. Muungano wa vyama makini vinne vya upinzani unasubiri ‘kapi’ kutoka chama tawala!

Kufupisha stori, mara baada ya UKAWA kumtangaza Lowassa kuwa mgombea wao, kwa sie wengine ilikuwa haiwezekani tena kuunga mkono umoja huo uliojumuisha vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.

Kwa vile wagombea wakuu katika uchaguzi huo walikuwa Lowassa na Magufuli, ilikuwa vigumu kumpinga Lowassa bila kumsapoti Magufuli. Kwahiyo japo awali nilijaribu kuepuka kumnadi mgombea wa CCM, Magufuli, mazingira yaliyokuwepo – pamoja na mkataba wa kutoa huduma ya usadi (consultancy) – ilipelekea nami nianze kumnadi Magufuli. Haukuwa uamuzi rahisi hasa kwa kuzingatia serikali ya CCM ilivyonitenda kuanzia mwaka 2006 nilipoanza kufuatilia skandali ya Richmond.

Ushiriki wangu kwenye kampeni haukuwa rahisi. Katika maisha yangu yote sikuwahi kutukanwa kiasi nilichotukanwa katika kampeni za uchaguzi huo. Jitihada zangu za kuwaelewesha watu kwanini nimelazimika kumuunga mkono Magufuli hazikusaidia kitu. Pengine kibaya zaidi ni kwamba wakati wa kuelekea uchaguzi huo nilifiwa na baba yangu, marehemu Mzee Philemon Chahali. Baadhi ya watu bila utu walitumia msiba huo kuingiza uhasama wa kisiasa.

Pamoja na mvua ya matusi ya kila aina, niliendelea na jukumu la kumnadi Bwana Magufuli. Nadhani mchango wangu mkubwa zaidi ulikuwa kwa wapigakura waliokuwa hawajafungama na chama chochote. Na nilifahamu kuhusu hilo baada ya uchaguzi ambapo baadhi yao walinieleza bayana kuwa ushawishi wangu kwao ulipelekea kufanya uamuzi wa kumpigia kura mgombea huyo wa CCM.

Lakini tukiweka kando ‘sababu zangu binafsi,’ Magufuli alionekana kama mgombea bora zaidi ya mpinzani wake Lowassa. Pamoja na sababu nyingine, wakati Magufuli alikuwa ‘mgombea wa CCM kutoka CCM,’ Lowassa alikuwa mgombea wa UKAWA kutoka CCM.

Hatimaye uchaguzi ukafanyika na Magufuli akaibuka mshindi. Kama kuna kitu kilichonipa matumaini sana kuhusu urais wa Magufuli ni hotuba yake aliyoitoa wakati wa uzinduzi wa bunge la Jamhuri ya Muungano. Katika hotuba hiyo, Magufuli alionyesha kuwa mtu anayezielewa vema shida za Watanzania hususan janga la rushwa na ufisadi, na akaapa kushughulikia kwa nguvu zake zote. Na alipoomba Watanzania wamwombee katika vita hiyo ngumu, naamini hata miongoni mwa wale ambao hawakumpigia kura waliitikia wito huo wa kumfanyia maombi.

Kisha zikaja ziara ya kushtukiza na taratibu tukaanza kuingiwa na matumaini mapya ya “mrithi halisi wa Nyerere/Sokoine.” Na dunia pia ikaungana nasi kusherehekea kiongozi huyo adimu, na ikaibuka alama ya reli #WhatWouldMagufuli Do iliyotamba kila kona ya dunia. Na haikupita wiki bila kushuhudia “tumbua majipu.”

Kwa kufurahishwa na kuridhishwa na utendaji wake, mie ‘nikajipinda’ na kuandika kitabu cha tathmini ya urais wa Magufuli, siku 55 tu baada ya yeye kuapishwa kuwa Rais wa tano wa Tanzania. Watu kadhaa walinikosoa kwamba haikuwa sahihi kwangu kufanya tathmini hiyo mapema kiasi hicho. 


Kwa wakati huo niliona walionikosoa kuhusu suala hilo kama watu wenye chuki binafsi dhidi ya ‘mkombozi’ Magufuli.

Dalili ya kwanza kwamba huenda kuna walakini katika utawala wa Magufuli ni pale alipotangaza baraza lake la mawaziri ambalo ilituchukua wiki kadhaa kulisubiri. Lilipotangazwa, sio tu lilikuwa kubwa kuliko ahadi yake kuwa angeunda serikali ndogo tu ili kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali, bali pia lilijumuisha baadhi ya sura ‘zenye utata.’ Miongoni mwa sura hizo ni Profesa Muhongo, ambaye alilazimika kujiuzulu katika serikali ya Awamu ya Nne kutokana na kuhusishwa na skandali ya Tegeta Escrow.

Kuna tuliouona uteuzi wa mtu kama Nape Nnauye kuwa ni wa kisiasa zaidi, huku sura kama Simbachawene, Lukuvi na Profesa Maghembe zikijenga ishara kuwa huenda mambo hayajabadilika kama tulivyotarajia.

Kisha kukafanyika uteuzi wa mabalozi ambao ulionekana bayana kama kutumia nafasi hizo nyeti kuwaondoa watu flani kwenye nyadhifa zao huko CCM. Baadhi yetu tukaanza kujiuliza, “hivi hatujayashuhudia haya huko nyuma?” Lakini tukaendelea kuwa na matumaini.

Dalili ya kwanza kabisa kuwa pamoja na mazuri yake yaliyowavutia Watanzania wengi na kona mbalimbali duniani, Bwana Magufuli ana mapungufu yake ni pale serikali yake kupitia ‘shujaa wa sasa’ Nape Nnauye ilipozuwia haki ya mamilioni ya Watanzania kusikiliza matangazo ya moja kwa moja ya Bunge. Niwe mkweli, wanaomwona Nape shujaa huwa siwaelewi kabisa. Ningemwona shujaa laiti angetumia ukongwe wake ndani ya CCM kumweleza bosi wake Magufuli kuwa wazo la kuzuwia matangazo ya bunge live ni fyongo, na laiti Magufuli angemomea basi angejiuzulu kishujaa badala ya kusubiri kufukuzwauwaziri kwa kupambana na ‘kimeo kingine cha Magufuli’ yaani Daudi Albert Bashite.

Baadaye likaja zuwio dhidi ya mikutano na maandamano ya vyama ya siasa. Awali baadhi yetu tulijipa matumaini kwamba “ah huu ni muda wa kuchapa kazi. Hayo maandamano na mikutano ni ya nini muda huu?” Kwahiyo kwa wakati huo ili-make sense.

Mara tukakumbwa na janga la tetemeko la ardhi huko Kagera. Ikategemewa Rais angekwenda kuwafariji wahanga hasa ikizingatiwa kuwa anatoka Kanda ya Ziwa. Hakwenda hadi baadaye. Na alipokwenda akatoa hotuba isiyopendeza kuisikiliza. Maneno kama “serikali haikuleta tetemeko la ardhi” sio ya busara hata kidogo. Pia akaongopa kwa kudai hakuna serikali duniani inayotoa misaada kwa wahanga wa majanga ya asili. Sijui muda huu anajisikiaje akiona kwenye runinga jinsi serikali ya Marekani inavyowahudumia wahanga wa vimbunga.

Baadaye kukusikika taarifa mbalimbali za tishio la uhaba wa chakula, lakini badala ya kuwafariji wananchi, Magufuli akawaropokea kwamba serikali yake haitotoa chakula kwa vile serikali haina shamba.
Na wakati mmoja alipita sijui Nzega au Urambo, mwananchi mmoja akamwambia “njaa Mheshimiwa.” Hilo jibu alilotoa utadhani ugomvi. Pamoja na majibu mengine ya ngebe akasema “njaa, kwani mnataka niingie jikoni kuwapikia?” Ovyo kabisa.

Likatokea tukio la maaskari polisi wanane kuuawa huko Kibiti lakini Amiri Jeshi Mkuu akaenda kufungua mabweni chuo kikuu cha Dar es Salaama badala ya kwenda kuaga miili ya askari hao.

Pia kulijitokeza tukio la ‘kupotea’ kwa kada wa Chadema Ben Saanane ambaye hadi ‘kupotea’ kwake alikuwa akihoji kwa nguvu kubwa kuhusu PhD ya Magufuli. Baadhi tulimsihi awe makini (kwa sababu dalili zilishaanza kujionyesha kuwa Magufuli ni mtu wa aina gani) lakini bahati mbaya hakusikia ushauri wetu. Hadi leo haijulikani nini kimemsibu kijana huyo japo Chadema nao hawawezi kukwepa lawama katika poor handling ya suala hilo. Kumekuwa na kauli zinazokinzana kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho kama ile ya mwenyekiti Mbowe kuwa Ben alitekwa huku Mbunge wa chama hicho Saeid Kubenea akidai kuwa kada huyo anaonekana vijiweni. Kwanini chama hicho hakijawabana viongozi hao kufafanua kauli zao, only God knows!

Lakini kama kuna tukio lililompotezea heshima kubwa Bwana Magufuli ni lile la Mkuu wa Mkoa Paul Makonda kuvamia stesheni ya redio na runinga cha Clouds  akiwa na askari wenye silaha. Siku chache baadaye huku baadhi ya watu wakitarajia angemtimua Makonda, Magufuli akatufanya sote mabwege kwa kumtetea Makonda huku akidai yeye hapangiwi kazi, yeye ndo Rais, na kumwita Makonda mchapakazi. Yaani Mkuu wa Mkoa amevamia kituo cha habari, kitendo ambacho ni kosa la jinai, halafu Rais anamsifu kuwa ni mchapakazi?
Uswahiba wa Magufuli na Makonda umechangia mno ugumu wa kuchunguza tuhuma kuwa mkuu huyo wa mkoa amefoji jina analotumia pamoja na cheti cha kuhitimu kidato cha nne. Laiti Magufuli angekuwa mwajibikaji kama tunavyoamini basi angeamuru uchunguzi kuhusu suala hilo.

Na kwa wanaofahamu yanayoendelea ‘nyuma ya pazia,’ inadaiwa kuwa vetting aliyofanyiwa Bashite ilionyesha bayana mapungufu yanatajwa kumhusu yeye, na ‘Bwana mkubwa’ akashauriwa kuchukua hatua stahili lakini hakufuata ushauri huo.

Hili la Bashite limeendelea kuwakera watu wengi sana, hasa ikizingatiwa kuwa mtu huyo anatumia ipasavyo upendeleo anaopewa na Magufuli, na kufanya dharau za wazi kama ile ya kupigiwa saluti na vingozi wa ngazi za juu wa jeshi la polisi huku amevaa kapelo. Hiyo ni dharau ya hali ya juu kwa vyombo vyetu vya dola.



Na Magufuli ataingia kwenye vitabu vya historia kwa serikali yake kulifungia gazeti la kila wiki la Mwanahalisi kwa miaka mitatu, na siku 10 baadaye akalifungia gazeti jingine la kila wiki la Raia Mwema kwa siku 90. 

Na kama kuna gazeti lilijitahidi mno 'kumnadi' Magufuli ni Raia Mwema. Nakumbuka makala nyingi katika gazeti hilo wakati wa kuelekea kwenye uchaguzi zilisheheni habari 'nzuri' kuhusu Magufuli.

Pengine si vibaya nikitumia fursa hii kueleza kuwa sababu hasa iliyonifanya niache uandishi wa makala katika gazeti hilo ni kwamba lilihojiwa na 'vijana wa Magufuli' kuhusu mie lakini wahusika hawakuona umuhimu wa kunieleza wala kuandika kuhusu habari hiyo.


Na kilichopelekea bwege huyo kudadisi kuhusu mie ni TWEET...Yes, just a tweet, a #FutureTweet to be precise. 

Kanuni muhimu katika chombo cha habari ni kwamba unyanyasaji wa taasisi yoyote ile dhidi ya mwenzenu ni unyanyasaji dhidi yenu nyote. Gazeti hilo lilipaswa kunijulisha kuhusu kilichotokea au kukiandika kama habari gazetini. Lakini bahati nzuri mie mzoefu wa 'dark arts' nikafahamu mapema kilichokuwa kinaendelea.

Hata hivyo, kitendo cha gazeti hilo nilikiona kama usaliti, nikaamua kuachana nao. Hata hivyo, mie sina kinyong'o nao na ndio maana jana nililaani na kupiga kelele kuhusu hatua hiyo ya serikali.

Haya yanatokea wakati Tanzania bado ipo kwenye mshtuko kufuatia jaribio la kumuua mwanasiasa ambaye amekuwa mpinzani mkubwa wa Magufuli, mbunge wa Chadema Tundu Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria cha TLS. Chuki inayopandikizwa dhidi ya wapinzani imepelekea takriban asilimia 99 ya viongozi wa CCM kuogopa kwenda kumjulia hali Lissu huko Nairobi alikolazwa.

Lakini pengine kipimo halisi cha mambo kwenda kinyume na matarajio ya baadhi yetu kuhusu Magufuli ni kwamba tangu aingie madarakani, zaidi ya viongozi na wanachama 400 wa Chadema wamekamatwa na polisi. Imefika mahala, wakuu wa wilaya wanakamata viongozi wa Chadema kila wanapojisikia. Na pengine kibaya zaidi ni ukweli kwamba taratibu jamii inaanza kuzowea kuona viongozi na wanachama wa upinzani – hususan Chadema – wakidhalilishwa na kukamatwa kiholela.

Jambo jingine la kusikitisha kuhusu utawala wa Magufuli ni utitiri wa sheria kandamizi kuhusu uhuru wa habari. Licha ya sheria ya makosa ya mtandao ya mwaka 2015 ambayo ni kazi ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete, tayari kuna sheria ya Huduma za Habari, ambayo ‘shujaa Nape’ alihusika kwa kiasi kikubwa, na sasa kuna kinachoitwa ‘Kanuni za Maudhui ya Mitandao ya Kijamii,’ ambayo laiti zikipitishwa zitakuwa balaa kubwa.

Na huku Chadema ikishuhudia viongozi na wanachama wake wakinyanyaswa ovyo ovyo, kuna kila dalili kuwa mgogoro unaoendelea ndani ya chama cha CUF una mkono wa serikali hasa kwa kuzingatia mwenendo wa ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa (taasisi ya serikali) kuibeba waziwazi kambi ya mwanachama aliyejiuzulu kwa utashi wake Prof Lipumba, ambaye from nowhere alirudi chamani na kudai yeye bado mwenyekiti.

Majuzi, Magufuli katumwagia siri kwamba kuna siku aliombwa ushauri na Spika Ndugai kuhusu uteuzi wa wajumbe wa kamati ya bunge. Hiyo ina maana kuwa bunge limewekwa mfukoni na mhimili wa serikali. Kadhalika, kauli za Jaji Mkuu ‘mpya’  baada ya jaribio la mauaji dhidi ya Tundu Lissu zinajenga taswira ya mhimili wa mahakama nao kuwekwa mfukoni na mhimili wa serikali.

Katika kuhitimisha makala hii ndefu ninarudia swali lililobeba kichwa cha habari: nini kilichomsibu Magufuli hadi kubadilika kiasi hiki? Kauli yake kuwa alisukumwa kuchukua fomu ya urais inazidi kuleta mkanganyiko kwamba labda alikuwa anafahamu fika hana uwezo wa kuongoza taifa letu lakini akakubali tu kutokana na shinikizo hilo, ambalo hata hivyo hatujui limetoka kwa watu gani.

Dalili kwamba ‘Magufuli atabadilika’ (kurejea kuwa yule tuliyemwona ni mkombozi wetu) ni finyu. Kwa vile maamuzi yake mengi yanamtengenezea maadui zaidi ya waliopo, kuna kila dalili kwamba atazidi kuwa mkali ili ‘kujilinda.’ Tutegemee uhuru wa kujieleza/habari uendelee kubinywa zaidi kadri bwana mkubwa anavyozidi kutukumbusha yeye ndio Rais, asiyeambiwa nini cha kufanya, anayejua siri zote na nchi yetu, na vitu kama hivyo.

Nimalizie kwa kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuhusu rai ya mara kwa mara ya Rais Magufuli kuwataka Watanzania tumwombee. Na tufanye hivyo kwa bidii kubwa ili Mwenyezi Mungu amwonyeshe njia sahihi ya kuliongoza taifa letu kwa kuzingatia haki na usawa. Tumwombee aondokane na 'fear of the unknown,' apate muda wa kupumzika badala ya kukesha macho akihofia 'the unknown.' Aachane na chuki dhidi ya kila anayemkosoa hata kama kukosoa huko ni kwa nia njema. Tumwombee awe na busara ya kutokitumia 'kitengo' kama kampuni yake binafsi. Ajiulize, kwanini licha ya ulinzi wake wa 'kufa mtu' bado siri zinavuja? Jibu jepesi: ukiwafanya watu wazima tena wenye utaalamu nyeti kuwa kama watoto, inakuwa 'mwaga ugali nimwage mboga.' Na asije kukasirishwa na makala hii...

Ni wazi kuwa ndoto za kuikomboa Tanzania yetu kiuchumi haziwezi kufanikiwa katika hali ya sasa ya siasa za vitisho, kunyanyasa wapinzani, “watu wasiojulikana,” na vitu kama hivyo. 

Mungu ibariki Tanzania


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.