Showing posts with label NIMROD MKONO. Show all posts
Showing posts with label NIMROD MKONO. Show all posts

17 Jan 2014

KATIKA hitimisho la makala yangu iliyochapishwa wiki mbili zilizopita, iliyobeba kichwa cha habari ‘Ni mwaka wa siasa za hovyo CCM, CHADEMA, niliahidi kuendeleza utabiri wa mwaka huu 2014, kwa kuangalia anga za kimataifa.
Kwa bahati nzuri, siku nne tu baada ya kuchapishwa makala hiyo, moja ya mambo niliyotabiri - kuendelea kwa mgogoro wa CHADEMA na uwezekano wa migogoro ndani ya vyama vya upinzani kuwa ya hadharani - limetokea.
Ninaomba niweke bayana kuwa masikitiko yangu kuhusu maendeleo mapya katika mgogoro wa CHADEMA ni makubwa zaidi ya furaha yangu kuona nilichotabiri wiki iliyopita kweli kimetokea. Nitakuwa mbinafsi na mnafiki ‘kusherehekea usahihi wa utabiri wangu’ katika jambo lisilopendeza. Laiti ingekuwa ni chaguo langu basi ningetamani mabaya yote niliyotabiri yasitokee, lakini kwa bahati mbaya hali halisi haikwepeki.
Takriban wiki mbili zilizopita, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) Zitto Kabwe alirusha ‘bomu zito’ ambapo alitoa tuhuma kubwa na hatari dhidi ya Mwenyekiti wake taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe, na chama hicho kwa ujumla. Pengine ili kuleta ladha halisi ya alichosema Zitto ni vema nikanuu ‘waraka’ mzima kama ifuatavyo:
"Lissu anasema nimepewa magari 2 na Mzee Mkono. Anasema kaambiwa na Mkono. Naamini Mkono alimwambia pia mwaka 2005 alimpa Freeman Aikaeli Mbowe tshs 40m ili Mbowe asifanye kampeni Musoma Vijijini.
“Nadhani alimwambia pia mwaka 2008 (baada ya orodha ya mafisadi kutangazwa 2007) Mkono alimpa Freeman tshs 20m za uchaguzi wa Tarime na Freeman akasema kwenye chama ametoa mkopo na akalipwa. Nadhani alimwambia pia kuwa mwaka 2010 Mkono alimpa Mbowe tshs 200m za kampeni ya Slaa.
“Pia hakusahau kumwambia kuwa Rostam Aziz alimpa Mbowe tshs 100m za kampeni. Lissu anajua kuwa gazeti la Tanzania Daima limeanzishwa na fedha za chama kutoka Conservative Party?
“Nimefanya internship yangu kwa Mkono and Company Advocates kuhusu masuala ya mikataba. Mzee Mkono ni Mzee wangu na alisaini petition ya kumtoa Waziri Mkuu Pinda. Lissu awaambie waliyemtuma wamwambie ukweli wote. Lissu ajue yeye ni kifaranga tu, Mimi namtaka mama wa kifaranga ajitokeze. Aeleze aliingia deal gani na Kinana na Sumaye mwaka 2005 kufuatia deni lake NSSF. Aweke wazi mkataba kati yake na NHC kuhusu nyumba ya umma ilipo Club Bilicanas.
“They must know I am not a push over. Chacha died, I won't. Mtu ambaye hawezi kuheshimu mke wake aliyemzalia watoto hawezi kunyooshea mtu kidole kuhusu maadili."
Zitto alibandika waraka huo katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook, lakini kwa sababu anazojua yeye pekee, baadaye aliuhariri na kutojumuisha tuhuma hizo. Aidha kwa kutofahamu au makusudi, uhariri uliofanywa na mwanasiasa huyo katika waraka huo haukuzuia kusambaa kwa kasi mtandaoni.
Niliposoma waraka huo nilipatwa na mshtuko mkubwa, nikabaki ninajiuliza iwapo Zitto alikuwa ‘mzima’ wakati anaandika alichoandika.  Japo inawezekana alifanya hivyo kwa kuzingatia kile kinachofahamika mtaani kama ‘umemwaga ugali na mie namwaga mboga...bora tukose wote,” ukweli ni kwamba bandiko hilo lina madhara makubwa, kwa Zitto binafsi na kwa pengine ustawi wa CHADEMA kwa ujumla.
Madhara kwa Zitto ni ya kisheria zaidi. Tayari Mbowe ameonyesha nia ya kumburuza Zitto mahakamani kuthibitisha tuhuma hizo nzito. Bila kujali kuwa tuhuma hizo zina ukweli au la, mtu yeyote mwenye uelewa wa ‘dili za siri’ atafahamu kuwa ni vigumu kuzithibitisha kisheria, yayumkinika kuhisi kuwa Zitto atakuwa na kazi ya ziada katika ‘kesi’ hiyo (iwapo itafunguliwa).
Iwe ni tuhuma za Nimrod Mkono kumpa Mbowe shilingi milioni 260 katika mazingira ambayo si tatanishi tu bali pia kwa namna fulani ni hujuma dhidi ya CHADEMA, au Rostam Aziz kumpatia Mbowe shilingi milioni 100, au ‘dili’ kati ya Mbowe na Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na Katibu Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana, sidhani kama Zitto anaweza kuthibitisha tuhuma hizo iwapo Mbowe atatimiza azma yake ya kufungua kesi. 
Je, inawezekana kuwa kwa kutambua ‘kosa hilo la kisheria’ ndio maana muda mfupi baadaye Zitto alihariri ‘post’ hiyo? Wakati jibu analo Zitto mwenyewe, ukweli unabaki kuwa tuhuma hizo ni nzito mno, na iwapo ni za kweli basi zinapoteza kabisa hadhi ya CHADEMA.
Ikumbukwe kuwa katika waraka uliopelekea Zitto kuvuliwa nyadhifa zake mbalimbali ndani ya CHADEMA, walioandika waraka huo waligusia walichokiita ‘udhaifu wa wanayemtaka’ (wakimaanisha Zitto), na kudai, “Maneno yake mara nyingine hayazingatii anayazungumza katika mazingira gani na hivyo kuwasha masikio ya wanataasisi jambo linalompunguzia kukubalika kwake taratibu.” 
Kadhalika, walieleza kuwa; “Kuna wakati tunayemtaka (Zitto) hujibu kwa taharuki kubwa dhidi ya mashambulizi yanayoelekezwa kwake jambo linalomfanya achukue maamuzi yasiyo sahihi kwa wakati huo. Kwa kifupi kuna wakati tunayemtaka (Zitto) huonekana kufanya maamuzi kwa hisia zaidi badala ya kutulia kwanza na kutafakari kwa kina ikiwa ni pamoja na kutafuta ushauri kwa wenzake kabla ya kujibu.”
Ndugu msomaji, huhitaji kuwa mwanasaikolojia kuhisi kuwa huenda kilichomsukuma Zitto kuandika ‘waraka’ huo kwenye ukurasa wake wa Facebook ni kile Waingereza wanakiita “putting emotions in front of common sense”, yaani kwa tafsiri isiyo rasmi, kuweka mbele jazba badala ya busara.
Kwa kujaribu kuonyesha kuwa Mbowe si mwadilifu (kwa maana ya kupokea misaada kutoka kwa ‘wanasiasa kama Mkono na Rostam waliowahi kutajwa na CHADEMA kuwa ni mafisadi’), linakuja swali la msingi, kwanini Zitto alikalia kimya tuhuma hizo nzito kwa takriban miaka minane hadi sasa baada ya kuvuliwa madaraka? Hivi kuna neno stahili kuelezea hali hiyo zaidi ya unafiki?
Tukiamini tuhuma hizo za Zitto, je naye si sehemu ya ‘uhuni wa CHADEMA’ wa kukemea mafisadi hadharani ilhali pembeni wanapokea misaada ya watu hao hao wanaowatuhumu? Ninasema hivyo kwa sababu Zitto hakuwa katibu wa shina bali Naibu Katibu Mkuu (taifa)  wa chama hicho, na mbunge, na kwa vyovyote vile naye ni mnufaika wa fedha hizo ‘za mafisadi.’
Laiti angekuwa haridhii vitendo hivyo basi aidha angejitoa mhanga na kuweka ukweli hadharani wakati huo (na hiyo ingeweza kuzuia kurejea kwa vitendo kama hivyo) au angeweza kujiuzulu kwa kuona ‘chama chake kinashirikiana na watuhumiwa wa ufisadi. Kwa nini hakufanya hivyo? Jibu jepesi ni hilo nililoandika hapo juu: alikuwa mnufaika wa vitendo hivyo (iwapo kweli vilitokea, maana tayari baadhi ya aliowataja wamekanusha ‘kumpa msaada’ Mbowe).
Binafsi, ninadhani moja ya matatizo yanayomkabili Zitto ni wanaojiita au kujitambulisha kama wafuasi wake. Wengi kati yao ni wenye mapenzi na CCM, na ushabiki wao kwa Zitto ni wa kirafiki (kimaslahi?) zaidi. Ndio, tofauti za kiitikadi hazimaanishi uadui, lakini wengi wetu tunaufahamu msemo ‘nionyeshe marafiki zako na nitakwambia wewe ni nani,’ yaani mara nyingi watu wanaotuzunguka hutoa picha fulani kuhusu sisi wenyewe.
Lakini tatizo jingine kuhusu ‘wafuasi na marafiki hao wa Zitto’ ni kutokuwa washauri wazuri kwake. Ukisoma mengi ya wanayoandika, hususan huko kwenye mitandao ya twitter, utabaini kuwa kimsingi wanachofanya ni ‘kumvimbisha kichwa Zitto’ bila kutoa ushauri unaoweza kusaidia ustawi wa kisiasa wa mwanasiasa huyo kijana.
Na mfano wa hivi karibuni ni baada ya Zitto kubandika waraka huo wenye tuhuma nzito huko Facebook. Wengi wa wafuasi wake walionekana kuchekelea ‘Mbowe alivyoumbuka’ bila kujali athari za kisheria kwa Zitto na ustawi wa CHADEMA kwa ujumla (kwanini wajali ilhali wengi wao ni wanaCCM)?
Kwa wafuasi wa Zitto, mwanasiasa huyo ni majeruhi wa siasa za chuki na mizengwe ndani ya CHADEMA. Lakini kwa wengine, Zitto anaonekana kama mtu anayeendeshwa na ‘ego’ kubwa inayomfanya kujiona yeye ndiye-au zaidi ya- CHADEMA.
Ni vigumu kubashiri hatma ya maisha ya kisiasa ya Zitto lakini kwa hali ilivyo ni vigumu mno kuona mustakabali wake ndani ya chama hicho. Ninakumbuka mwanasafu mmoja wa gazeti hili alimshauri mwanasiasa huyo hivi karibuni kuwa suluhisho la busara kwake kwa sasa ni kutosubiri kuvuliwa uanachama, ajiondoe mwenyewe huko CHADEMA, na kuitaka Mahakama isiingilie kazi ya chama.
Mwisho, bado ninaamini kuwa Zitto ni mwanasiasa mzuri lakini pengine kwa upungufu wa kibinadamu au makusudi, washauri wabovu au sababu nyinginezo, hazingatii umuhimu wa busara hizi tatu katika medani ya siasa: moja, waweke marafiki zako karibu lakini waweke maadui zako karibu zaidi, na pili, hakuna marafiki au maadui wa kudumu katika siasa, na tatu, hakuna mwanasiasa anayeweza kuwa mbadala wa chama (hasa katika mazingira ya siasa zetu ambapo kwa kiasi kikubwa chombo pekee cha uongozi wa kisiasa ni chama cha siasa. Bila chama, mwanasiasa hata awe maarufu kiasi gani anabaki kuwa raia wa kawaida tu).
Katika waraka wake, Zitto aliandika, “They must know I am not a push over. Chacha died, I won't” (lazima wafahamu mie sio mtu wa ‘kupelekeshwa.’ Chacha (Wangwe?) alikufa, mimi sitokufa). Hiki ni kiburi, utoto au? Ni mwanadamu mwenye uhakika wa kutokufa? Nihitimishe kwa kumshauri kwamba labda kweli ana uhakika wa kuishi milele lakini kwa kutanguliza hisia badala ya busara, yayumkinika kubashiri kuwa anaweza kuwa anajiua mwenyewe kisiasa (committing political suicide).



25 Aug 2010


Takukuru yakamata mgombea aliyejitoa
Adaiwa kuwa alishawishiwa kwa fedha
Awekwa chini ya ulinzi Makao Makuu Dar

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Makao Makuu jijini Dar es Salaam, imemkamata na kumhoji aliyekuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) katika Jimbo la Musoma Vijijini, Michael Makenji, kwa tuhuma za kupokea rushwa.

Makenji anadaiwa kupokea Euro 1,000 (Sh. 1,850,000) kisha kujitoa katika kinyang’anyiro hicho.
Habari zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa Makenji alihojiwa na maofisa wa Takukuru juzi jioni kuhusiana na tuhuma hizo na kwamba hadi jana alikuwa akiendelea kushikiliwa kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Makenji ni miongoni mwa wanachama wa Chadema waliochukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea katika jimbo hilo, lakini hakurejesha fomu kwa msimamizi wa uchaguzi hivyo jimbo hilo kubaki na mgombea pekee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nimrod Mkono (pichani mwenye kibandiko).

Habari zinaeleza kuwa Makenji baada ya kutorejesha fomu kwa msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Musoma Vijijini, alikwenda katika ofisi za Makao Makuu ya Chadema jijini Dar es Salaam, lakini baadaye baadhi ya wanaChadema walimtilia shaka kutokana na mawasiliano kati yake na baadhi ya watu.

Chanzo chetu cha uhakika kimebainisha kuwa, baada ya wanaChadema kumtilia shaka, walimuweka chini ya ulinzi na kukuta taarifa mbalimbali alizokuwa anatumiana na watu hao kupitia ujumbe mfupi wa simu.Taarifa za ndani ya Chadema zinasema kwamba baada ya mgombea huyo kuhojiwa na kupekua kwenye simu yake ya mkononi, alipatikana na ujumbe kadhaa zilizoashiria kwamba kulikuwa na mkono wa mtu katika kujitoa kwenye kinyang’anyiro cha ubunge.

Miongoni mwa jumbe hizo (sms) ambazo ziko sehemu ya zilizotumwa zilisema:
“Mzee ameshanikatia tiketi ya kwenda Dar sasa muhimize amalizie kiasi kilichobaki maana hali yangu ya kiuchumi si nzuri.”
Nyingine ilisomeka: “Tumeshamaliza kama tulivyokubaliana.” Na mwingine ukisema: “Niko Makao Makuu ya Chama niko chini ya ulinzi.” Ujumbe huo ulionekana kujibiwa hivi: “Nani kakwambia uende huko watakuua. Siwezi kuja huko kukutetea.” Simu iliyotuma ujumbe huo unadaiwa ni ya kiongozi mmoja mwandamizi wa chama hicho.

Chadema baada ya kuona hali imekuwa hivyo, waliamua kuwasiliana na Takukuru na baada ya muda mfupi, maofisa wa taasisi hiyo walifika na kumchukua Makenji.Hata hivyo, Takukuru haikuwa tayari kuthibitisha tukio hilo licha ya jitihada za NIPASHE kuwatafuta maofisa wake tangu juzi jioni.

Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah, juzi jioni alisema alikuwa katika mkutano mjini Arusha na kuahidi kuwa angepiga simu baadaye kutoa ufafanuzi. Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni hakufanya hivyo.

Ofisa Uhusiano wa Takukuru, Doreen Kapwaya, jana alisema kuwa maofisa wa Makao Makuu wangeweza kulizungumzia, lakini mwandishi wetu alipokwenda katika ofisi hizo, aliambiwa kuwa ofisa anayeshughulikia kesi hiyo alikuwa katika kikao.

Hata hivyo, ofisa huyo aliyetambulika kwa jina moja la Kassim, alipoulizwa baadaye jioni, alisema: “Sina comment (sina la kusema) katika hilo, labda kama ungefuata zile taratibu zetu za kila siku kwa kupitia kwa ofisa Uhusiano wetu hadi kwa Mkurugenzi Mkuu.”

Dk. Hoseah alizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu majira ya saa 18:20 jana jioni, alisema: “Sina taarifa, kwa sasa nipo nje ya Dar es Salaam, nani amekuambia hayo.”

Uongozi wa Chadema ulipoulizwa kuhusiana na taarifa hizo, ulithibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kueleza kwamba mtuhumiwa (Makenja) alikiri kupewa kiasi hicho cha pesa.

“Kimsingi ni kwamba Idara yetu ya Ulinzi na Usalama ilimhoji mgombea wetu na akakiri kupewa fedha hizo, tena kwa maandishi ndipo tukawasiliana na Takukuru kwa hatua zaidi…lakini tunawasiliana na mamlaka mbalimbali ili kuona hatua stahili za kumchukulia kwa sababu amekiuka kanuni na sheria za uchaguzi,” alisema Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika.

Kufuatia hali hiyo, Mnyika alisema chama hicho kimelazimika kuwaandikia barua wagombea wake ambao hawakurudisha fomu ili kujua tatizo lililokwamisha kufanya hivyo.Alisema chama kimeamua kuchukua hatua hiyo ili kubaini kama kinafanyiwa hujuma na kwamba watakaobainika kutorudisha fomu makusudi, kitawachukulia hatua kwa mujibu wa sheria za uchaguzi.

CHANZO: Nipashe

Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.