Showing posts with label NAPE NNAUYE. Show all posts
Showing posts with label NAPE NNAUYE. Show all posts

25 Mar 2017


Kuna wanaotusimanga tuliompigia kampeni Rais John Magufuli wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 2015. Kwamba sie ndo tumemleta Magufuli. Kwamba bila sie kumnadi, Tanzania isingeshuhudia kipindi hiki cha 'maajabu' ambapo kwa mara ya kwanza tumeshuhudia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam'anayebebwa na Magufuli' akiwa na uhuru wa kuvunja sheria, na yeyote atakayemkemea atakuwa amenunua ugomvi na Magufuli.

Wanaotusimanga wanasahau kitu kimoja. Laiti Upinzani ungekuwa na mgombea imara katika uchaguzi mkuu uliopita, kazi ya kuiangusha CCM ilikuwa rahisi kuliko wakati mwingine wowote ule.

Nakumbuka kada mmoja mwandamizi wa CCM alinieleza wakati wa kampeni kuwa "laiti Wapinzani walivyoungana na kumsimamisha mtu asiye na rekodi yenye mawaa, kwa mfano Dokta Slaa hivi, basi uchaguzi huu ungekuwa mgumu sana kwetu." Alieleza kuwa UKAWA uliirahisishia CCM kampeni ya kumnadi mgombea wake kwa vile, pamoja na sababu nyingine, mgombea wa UKAWA -Lowassa- alikuwa akijulikana vizuri mno huko CCM, kitu kilichowarahisishia kumshinda 'kirahisi.'

Kwahiyo, kabla ya kuachana na suala la lawama hizo, niseme hivi: sie tuliomnadi Magufuli hatukujua kuwa angekuja kubadilika kiasi hiki, lakini laiti Upinzani ungesimamisha mgombea bora, sie wengine wala tusingekimbia, tungefanya kampeni kama mwaka 2010, na kwa vile kwa kiasi kikubwa Upinzani auliamia kuweka kando tofauti zao, basi uwezekano wa kuiangusha CCM ulikuwa mkubwa. Ila hayo yameshapita sasa, tugange yaliyopo na yajayo.

Na yaliyopo tunayaganga vipi? Ni kwamba wakati tunaendelea kukuna vichwa kufahamu kitu gani kilichomsibu Rais Magufuli, aliyeingia kwa kishindo kikubwa sio Tanzania tu bali kimataifa pia, na hadi kutawala dunia na alama ya reli #WhatWouldMagufuliDo hadi kufikia hatua aliyofikia sasa ya kutawala kwa vitisho, jazba, ubabe na kutetea waziwazi uvunjifu wa sheria uliofanywa na RC Makonda, ni vema basi tujipange imara kuzuwia jitihada zozote za kiongozi huyu kuwa wa kutumia mabavu tu.

Kuna mwanafalsafa mmoja aliusia huko nyuma kuwa "ili maovu yashamiri, yahitaji tu watu wema kutofanya lolote." Wenye uwezo wa kupiga sauti dhidi ya maovu tukikaa kimya, labda kwa vile tu tuliwahi kumpigia kampeni Magufuli, au kwa vile "yatapita tu," kuna kila dalili kuwa tunakoelekea sio kuzuri.

Moja ya mambo yanayotatiza sana kuhusu Rais Magufuli ni kile kinachoonekana kama kupenda ugomvi usio wa muhimu. Hilo nimelieleza kwa kirefu katika makala ninayoiambatanisha hapo chini ambayo ilipaswa kuchapishwa na gazeti la Raia Mwema toleo la wiki hii lakini ninahisi haikuchapishwa (njia pekee ya mie kufahamu imechapishwa au la ni kuona makala husika kwenye tovuti ya gazeti hilo, na wiki hii haipo).

Kati ya nilipoandika makala hiyo na leo, kuna matukio makubwa manne yaliyojitokeza. Kwanza ni Waziri wa Habari (na masuala mengine)  Bwana Nape Nnauye kusimamia vema wajibu wake kama waziri husika, kufuatilia uvamizi uliofanywa na RC Makonda kwenye kituo cha redio na televisheni cha Clouds. Nape alipokea ripoti ya Tume aliyounda, na licha ya msimamo wa Magufulikujulikana mapema kuwa "anambeba Makonda," Nape alionyesha ujasiri na kuiweka hadharani ripoti hiyo ambayo awali baadhi yetu tulidhani ingekuwa 'changa la macho.'

Tukio la pili ni uamuzi wa Rais Magufuli kumfukuza kazi Nape kwa kufanya mabadiliko kwenye kabineti yake, na nafasi ya Nape kukabidhiwa Dkt Harrison Mwakyembe, ambaye majuzi tu 'alilikoroga' kwa kupiga marufuku kufunga ndoa bila cheti cha kuzaliwa. Amri hiyo ya kizembe ilitenguliwa na Magufuli siku chache baadaye.

Tukio la tatu ni mkutano wa Nape na waandishi wa habari, ambao tukiweka kando aliyoyasema mwanasiasa huyo, kubwa zaidi lilikuwa kitendo cha afisa mmoja wa usalama (haijulikani kwa hakika kama alikuwa polisi au taasisi nyingine ya dola) kumtolea bastola Nape hadharani. Tukio hilo la kutisha, na lile na Makonda kuvamia Clouds, yatabaki kuwa historia isiyopendeza kwa taifa letu kwani hayajawahi kutokea...labda zama za ukoloni.

Tukio la nne ni 'mafuriko' ya maneno yasiyopendeza kutoka kwa Rais Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa jana wakati anawaapisha Mwakyemba na Profesa Kabudi, aliyerithi nafasi ya Mwakyembe. 

Sitaki kurudia vitisho alivyotoa Rais Magufuli lakini nachoweza kutahadharisha ni kuwa tunakoelekea sio kuzuri. Unapoona Rais anakerwa kwa vile habari zinazomhusu hazijapewa kipaumbele kwenye vyombo vya habari vingi, basi ujue tuna tatizo kubwa. Unapoona Rais anaamini kuwa habari za maandamano ya wafugaji na wakulima kuhusu migogoro ya ardhi ni "habari mbaya mbaya" basi ni wazi huyu si yule tuliyedhani ni tetezi wa wanyonge.

Tulipasw akuona dalili hizo mapema, kupitia baadhi ya kauli zake kama "I wish I could be Jaji Mkuu" na "I wish I could be IGP." Ukiona Rais anatamani madaraka zaidi ya aliyonayo, hiyo ni hali ya hatari.

Nihitimishe makala hii kwa kumshauri Rais Magufuli asikilize ushauri anaopewa na "wataalamu kuhusu hali ilivyo huko mtaani." Kadhalika, ninamsihi Rais wangu apunguze jazba. Hazitamfikisha popote. Aache kasumba ya kutafuta 'mabifu' yasiyo na msingi. Lakini jingine ni ukweli kwamba hatoweza 'kumbeba Makonda' milele, na kuendelea kumkumbatia kijana huyo kunaweza kumgharimu yeye Magufuli binafsi. 

SOMA MAKALA ILIYOPASWA KUTOKA KATIKA RAIA MWEMA TOLEO LA WIKI HII (JUMATANO 23/03/2017) LAKINI HAIKUTOKA (KWA SABABU WANAZOJUA WAMILIKI WA GAZETI HILO)


MAKALA YA RAIA MWEMA TOLEO LA MACHI 22, 2017

Disemba 31 mwaka juzi, siku ya mkesha wa ‘mwaka mpya 2016, nilichapisha kitabu cha kielektroniki kilichobeba jina “Dokta John Magufuli: Safari ya Urais, Mafanikio na Changamoto Katika Urais Wake.”

Pamoja na watu wengi waliokisoma kitabu hicho kukipongeza, wapo pia walionikosoa, hoja yao kuu ikiwa “ni mapema mno kutathmini Urais wa Magufuli katika muda huu mfupi aliokaa madarakani.”
Kwa wakati huo, sikuafikiana na ukosoaji huo, hasa kwa vile tathmini ya uongozi ni kama maadhimisho ya siku ya kuzaliwa: yanaweza kufanywa siku 40 baada ya kuzaliwa, kila mwezi, na kila mwaka kama wote tunavyofanya.

Kwahiyo, sikuona tatizo katika kufanya tathmini ya urais wa Dokta Magufuli, hasa ikizingatiwa kuwa aliingia na “kasi ya kutisha.” Kati ya siku aliyopishwa, Novemba 5, 2015 hadi nilipochapisha kitabu hicho – takriban miezi miwili hivi – Rais Magufuli alimudu kukonga nyoyo, sio za Watanzania tu, bali dunia nzima kwa ujumla kutokana na msimamo wake mkali dhidi ya uzembe, rushwa, ufisadi, sambamba na ari yake kubwa ya kubana matumizi.

Naamini sote tunakumbuka alama ya reli (hashtag) ‘iliyotikisa’ dunia nzima ya #WhatWouldMagufuliDo ambayo watumiaji mbalimbali wa mtandao wa kijamii wa Twitter katika kila kona ya dunia walijaribu kuonyesha jinsi gani Dokta Magufuli alivyo bora zaidi ya viongozi wengine duniani.

Lakini sababu nyingine ya kuandika kitabu hicho ilikuwa ushiriki wangu binafsi kwenye kampeni za kumnadi Dokta Magufuli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Pamoja na sababu nyingine, niliamua kumnadi kutokana na sababu zangu binafsi dhidi ya mpinzani wake mkuu.

Na haikuwa kazi rahisi kumnadi mwanasiasa huyu, kwa sababu baadhi ya watu walishindwa kabisa kunielewa, huku wengine wakihoji “kwanini unaweza kutusaliti wapinzani na kumpigia debe mgombea wa chama tawala, ambacho wewe binafsi ni mhanga wa unyanyasaji unaofanywa na serikali yake dhidi ya wanaoikosoa?” Na kilichoambatana na kauli hizo ni matusi mazito, udhalilishaji usiomithilika, na mengineyo yasiyostahili kukumbukwa.

Takriban miaka miwili baadaye, nimeshikwa na bumbuwazi baada ya kumsikia Rais Magufuli “akimkingia kifua” Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ambaye majuzi ameandika historia ya matukio ya kisiasa nchini Tanzania kwa kuvamia ofisi za kituo cha habari cha Clouds, akiambatana na askari wenye silaha nzito.

Niweke rekodi sahihi. Awali nilimtetea RC Makonda katika nilichoamini kuwa ni jitihada zake dhidi ya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Niliamini kuwa suala la ‘utata wa elimu yake’ ni sehemu tu ya mikakati za kumwondoa kwenye ajenda hiyo muhimu.

Hata hivyo, baada ya mawasiliano na “wenye uelewa wa yanayojiri nyuma ya pazia la siasa za Tanzania,” nilithibitishiwa kuwa tuhuma dhidi ya kiongozi huyo zina ukweli, na nikaelezwa kuwa “hata Dokta Magufuli anafahamu hilo.” Na kimsingi, awali nilipanga makala hii iwe ya ushauri kwa Rais kuchukua hatua stahili dhidi ya mteuliwa wake huyo “ili kuwatendea haki wanaomshauri.”

Lakini kabla sijawasilisha makala hiyo, ambayo ililenga zaidi kwenye kusisitiza haja kwa viongozi wetu kuzingatia ushauri wa kitaalamu badala ya kuendekeza ajenda binafsi, kukajitokeza tukio la RC Makonda kuvamia huko Clouds.

Nitumie fursa hii kuupongeza uongozi wa kampuni ya Clouds, hususan Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga, kuwa kufanya kile kilichotamaniwa na Watanzania wengi waliokuwa wakisubiri tamko la kampuni hiyo kuhusu tukio hilo la uvamizi wa Makonda, kwamba wasimamie ukweli.

Na kwa hakika, Ruge na Kusaga hawakuwaangusha watumishi wenzao wa Clouds na Watanzania kwa ujumla, wakaeleza “A hadi Z” ya kilichotokea wakati wa uvamizi huo ambao, kwa kumbukum bu zangu, ni wa kwanza kabisa kutokea nchini mwetu.

Ingeweza kuwa rahisi tu kwa viongozi hao wa Clouds “kuweka mbele maslahi yao binafsi” na kubadili maelezo, hasa ikizingatiwa kuwa lolote ambalo wangesema lingeweza kuaminika, lakini wakaamua kuhatarisha uhusiano wao na Makonda pamoja na shabiki mkubwa wa kituo hicho, yaani Rais Magufuli mwenyewe.

Akiongea kwenye uzinduzi wa mradi wa ujenzi wa barabara za juu, pamoja na mambo mengine Rais Magufuli aliwaomba Watanzania kujielekeza kwenye vitu vya maendeleo badala ya kujielekeza zaidi kwenye udaku. Ikumbukwe kuwa siku chache tu zilizopita, Rais alipiga simu kwenye kituo cha televisheni cha Clouds na kueleza kuwa yeye pia ni shabiki wa kipindi cha Shilawadu, ambacho ni cha “udaku” huo huo anaokemea Rais.

Suala hapa sio tu “kama ni sahihi kwa Rais kuwa shabiki wa kipindi cha udaku, basi isiwe dhambi kwa wananchi kupenda udaku” bali “kitendo cha Makonda kuvamia Clouds sio kujielekeza kwenye maendeleo.”

Dokta Magufuli alikumbusha pia kuwa “kampeni zimekwisha, ulie lakini Rais ni Magufuli, mimi kwangu hapa ni kazi tu, maendeleo.” Hivi kweli Rais anaamini kelele za kutaka Makonda achukuliwe hatua kutokana na uvamizi huko Clouds ni mwendelezo wa kampeni? Au ni “kelele za wasiojua kuwa Rais ni Magufuli”? Na sitaki kabisa kuamini kuwa Rais anaamini kitendo cha uvamizi wa Makonda huko Clouds ni sehemu ya “hapa ni kazi tu.”

Kilichonisikitisha zaidi ni kauli ya Dokta Magufuli kwamba “mnahangaika na viposti vyenu mara hili mara lile, mpaka wengine wanaingilia uhuru wangu kwamba nifanye hivi, ukiniingilia ndio unapoteza kabisa.”

Kwangu binafsi, nimeoiona kauli hiyo ya Rais kuwa kama dhihaka dhidi ya baadhi yetu tulioshiriki kikamilifu kumpigia kampeni mwaka 2015 kwa kutumia “viposti” hivyo hivyo anavyovidharau. Na sio sahihi kwa Rais kudai tunamwingililia uhuru wake. Yeye ni mtumishi wetu, na tuna haki ya kumweleza matakwa yetu. Huko sio kumwingilia uhuru wake bali kudai stahili yetu kutoka kwake.

Rais alitukumbusha pia kuwa yeye hapangiwi mambo, anajiamini, na ndio maana siku ya kuchukua fomu alikwenda peke yake. Kumtaka amwajibishe mteule wake aliyevamia kituo cha habari sio kumpangia mambo bali kumkumbusha wajibu wake kama kiongozi. Na kupangiwa mambo kama “mwajiriwa wa Watanzania” sio kosa, isipokuwa tu pale “kumpangia mambo” huko kunalenga kuidhuru nchi yetu.

Sawa, Dokta Magufuli alikwenda peke yake kuchukua fomu za kuwania urais, lakini hakufanya kampeni peke yake. Na kwenda kwake pepe yake kuchukua fomu hakumpi ruhusa ya kutuongoza peke yake, bali kwa ushirikiano kati yetu waongozwa na yeye kiongozi. Hivi, sio Dokta Magufuli huyuhuyu ambaye kila mara anatusihi tumwombee, lakini leo anatuona tunamwingilia?

Kadhalika, Rais alimuunga mkono RC Makonda kwa kumwambia kuwa yeye (Rais) ndio anayepanga nani akae wapi na afanye nini…kwahiyo RC Paul Makonda achape kazi. Hivi Rais amesahau kuwa sio yeye kama Magufuli bali taasisi ya Urais ndiyo inayompa nguvu kufanya maamuzi kwa maslahi ya Watanzania wote?

Na je Dokta Magufuli anataka kutuaminisha kuwa ameridhia kitendo cha Makonda kuvamia kituo cha habari akiwa na askari wenye silaha, kiasi cha kumtaka Mkuu huyo wa mkoa “aendelee tu kuchapa kazi”? Je hiyo haitompa jeuri Makonda, na hata wengineo, kufanya “abuse of power” kwa vile “Rais kuruhusu”?

Nimalizie makala hii kwa ushauri huu kwa Dokta Magufuli: kwanza, hakuna tija katika kusaka ugomvi usio na umuhimu (picking up cheap fights). Uamuzi wa kuzuwia kurushwa matangazo ya bunge mubashara, kuzuwia mikutano ya vyama vya siasa vya upinzani, kuwaambia wahanga wa tetemeko Kagera kuwa “serikali haikuleta tetemeko hilo” na “kila mtu abebe msalaba wake mwenyewe”, kuwaambia wananchi wanaolalamikia njaa kuwa “wewe Rais huwezi kuwapikia,” nk sio tu ni “kusaka ugomvi usio wa lazima” lakini haziendani na matarajio ya Watanzania kwako Rais wetu.

Vilevile ninaomba sana kumshauri Rais kuzingatia ushauri wa kitaalamu anaopatiwa na wasaidizi wake. Ni vigumu kufafanua katika hili, lakini ninaamini “nimeeleweka.” Taifa litakuwa katika hali mbaya itapofika mahala “washauri watakapotumia njia mbadala kukufikishia ujumbe.” Na ndicho kinachotokea kuhusu “viposti.”

Mwisho, siku zote Rais wetu umekuwa ukimtanguliza Mungu katika hotuba zako mbalimbali na kuwasihi Watanzania wakuombee. Wewe ni Mkristo, na hii ni Kwaresma. Ni kipindi cha maungamo, kusamehe waliotukosea, kuangalia tulikotoka, tulipo na tuendako. Penye Mungu pana upendo, na penye upendo pana haki. Japo hupangiwi cha kufanya, naomba kukushauri uwapatie haki Watanzania kwa kumwajibisha RC Makonda kwa kuvunja haki za Clouds kutokana na uvamizi aliofanya.
Mungu Ibariki Tanzania


Baruapepe: [email protected] Tovuti: www.chahali.com Twitter: @cha



15 May 2011


11 May 2011

Mwangalie huyo kijana (well,may be mzee.You can't tell the difference,can you?) wa kwanza kulia.Sidhani kama anayoongea Nape yanamwingia akilini.Na wa tatu kutoka kulia,mwanamama aliyeshika tama,ni kama aliamrishwa kuhudhuria mkutano huo.Sio kashfa au dharau,lakini ni wazi kuwa sura za wahudhuriaji zinatia huzuni.Zimejaa mawazo,hazionyeshi matumaini....yet wamehudhuria.Ukiwaangalia akinamama hao hapo chini,japo kuna kijitabasabu cha kujipa matumaini,lakini hizo flana za njano na khanga zimeficha mengi...ngozi zao zinaonyesha waziwazi namna maisha yao ya kila siku yalivyo magumu katika harakati za kupeleka mkono kinywani.


Lakini bado wanahudhuria mikutano ya porojo.Wanajua wanadanganywa,kwani huhitaji kwenda shule kujua una njaa ilhali anayepiga porojo ameshiba.Mng'aro tu wa ngozi ya Nape as opposed to msinyao wa ngozi za wasikilizaji wake unaelezea mengi.Wanaambiwa kuwa CCM imejivua magamba,sasa itaendeshwa kisayansi,sijui imekuwa mpya...lakini hawaambiwi ni kwa namna gani ugumu wa maisha ya walalahoi hao utapungua...ni lini nao watapata fursa ya kunawiri kama akina Nape....

Lakini bado wanahudhuria mikutano hii ya porojo.Ndio maana katika kichwa cha habari nimehoji: WAMEROGWA?

Picha kwa hisani ya Jamii Forums

23 Mar 2009


KADA maarufu wa Chama cha Mapinduzi, Nape Nnauye, amesema malumbano yanayoendelea sasa nchini ni ishara kwamba mafisadi wamejipanga kuifanya nchi isitawalike.

Nape alitoa kauli hiyo jana alipotakiwa kutoa maoni yake kuhusu hali ya kisiasa nchini, hususani malumbano yanayoendelea sasa kati ya Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz na Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe.

Bila kutaja majina ya watu, Nape alisema chimbuko la malumbano hayo aliyoyaita ya kipuuzi ni kashfa nzima ya kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Richmond, iliyosababisha aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi na aliyekuwa Waziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk. Ibrahim Msabaha, kujiuzulu.

Huku akiwa makini kuchangua maneno ya kuzungumza, Nape alisema malumbano hayo yanaonyesha kuna baadhi ya watu hawakuridhika na taarifa ya Kamati Teule ya Bunge iliyoongozwa na Dk. Mwakyembe, hivyo kuna ulazima wa hoja hiyo kurudishwa tena bungeni ili kukata mzizi wa fitna.

“Kuna kila dalili kuwa mafisadi wamejipanga kuhakikisha nchi haitawaliki, ndiyo maana mijadala isiyo na kichwa wala miguu inaibuka kila kukicha hata kwa mambo ambayo yamekwishaamuliwa na chombo kikubwa kama Bunge,” alisema.

Katika kuthibitisha kauli yake, Nape alisema ana taarifa za siri kuwa kuna baadhi ya mafisadi wamekuwa wakifanya mikutano ya faragha ambapo pamoja na mambo mengine, wamepanga kuhakikisha nchi haitawaliki kwa kuibua hoja na mijadala kupitia baadhi ya vyombo vyao vya habari.

“Tunakoenda ni kubaya, ila naamini serikali iko imara na CCM kama chama tawala, tutaomba tulizungumze kwenye vikao vyetu kwa nia njema ya kuliokoa taifa linalovurugwa na watu wachache wenye fedha,” alisema Nape.

Nape alisema ili kuhakikisha Tanzania haiyumbishwi, aliwataka wananchi kupuuzia mjadala wa sasa kwa madai kuwa hauna tija na una lengo la kuhatarisha amani na utulivu uliopo nchini.

Kuhusu mjadala wa ununuzi wa mitambo ya kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Dowans iliyorithi kutoka Kampuni ya Richmond, kada huyo wa CCM alisema anashangazwa na uamuzi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), kuomba kibali cha Bunge au kamati zake.

“Kwani TANESCO wanapoenda kununua transfoma na vifaa vingine, wanaomba kibali cha Bunge? Kama si hivyo, kwa nini wanataka kuhalalisha ununuzi wa mitambo ya Dowans kupitia kamati za Bunge? Hata hivyo, Bunge lilishatoa msimamo wake juu ya hilo, kama kuna mtu hakuridhika, alirudishe bungeni na si kuwagawa Watanzania kwa mijadala isiyoisha na vitisho,” alisema Nape.

Mwanasiasa huyo machachari aliwataka mafisadi kutambua kuwa hata wakiibua mijadala ya kuwagawa Watanzania kama ilivyo sasa, hakutabadili ukweli kwamba Richmond na hata mrithi wake Dowans, ndio waliolifikisha taifa hapa lilipo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa, John Shibuda, alisema malumbano yanayoendelea sasa kati ya Dk. Mwakyembe na Rostam kumetokana na upepo wa kisiasa ambao wakati mwingine huleta tija katika kukuza demokrasia.

Hata hivyo, Shibuda ambaye hupenda kuzungumza kwa mafumbo, alisema mjadala huo umejikita kwenye hila na visa vya kufunika mema na mazuri ya mtu.

“Mimi naona hayo ni mapepo ya kisiasa na mtenguko wa fikra ambao umeleta mng’atuko dhidi ya dhulma, lakini ni mjadala wa heri kwa maana kuwa unawafanya watu kutoa manung’uniko yao, bila hivyo hali ingekuwa mbaya siku moja, kwa hiyo naona mjadala uendelee,” alisema Shibuda.

Mbunge wa zamani wa Morogoro Vijijini, Semindu Pawa (CCM), aliiambia Tanzania Daima jana kuwa, mjadala huo sasa umechacha na kuwataka waandishi wa habari kuachana nao.

“Mimi sitaki kusema nani yuko sahihi, lakini nasema mjadala huo umechacha, umepitwa na wakati, wanahabari mkiacha tu, hautausikia tena, lakini naweza kusema wanahabari ndio mnaoukuza, waacheni,” alisema Semindu Pawa.

Mwishoni mwa wiki, Dk. Mwakyembe alijibu tuhuma zinazomhusisha na kumiliki kampuni binafsi ya kuzalisha umeme kuwa ni kazi mahususi inayofanywa na majeruhi wa vita ya ufisadi, ambao waliumizwa na matokeo ya kazi ya Kamati Teule ya Bunge ya kuchunguza mkataba wa Kampuni ya Richmond, ambayo yeye alikuwa mwenyekiti wake.


Hatua ya Mwakyembe kujibu tuhuma hizo, ilikuja baada ya magazeti mawili ya kila siku, (si Tanzania Daima) kuchapisha habari zinazomhusisha yeye na umiliki wa hisa 1,000,000 zenye thamani ya jumla ya sh bilioni 1.5 katika Kampuni ya Power Pool East Africa Ltd.

Mbali ya habari hizo kuandikwa katika magazeti hayo mawili; moja la binafsi na jingine la serikali, nyaraka kadhaa zinazomhusisha Mwakyembe na kampuni hiyo, zimesambazwa katika mtandao wa intaneti.

Taarifa hizo pia zinamtaja Mbunge wa Lupa, Victor Mwambalaswa ambaye ni Mjumbe wa Bodi ya TANESCO, kuwa miongoni mwa wanahisa wa kampuni hiyo binafsi ambayo wakati fulani Mwakyembe alipata kuwa mtendaji mkuu wake.

Taarifa hizo zinajaribu kujenga hoja zinazojaribu kumuondolea Mwakyembe uhalali wa kuendelea kudai kupambana na ufisadi ndani na nje ya Bunge ilhali yeye mwenyewe akionekana kuwa na ukwasi mkubwa unaotiliwa shaka.

Pia zinaonyesha kuwa, Mwakyembe licha ya kuwa na hisa nyingi katika kampuni hiyo, ameisaidia katika mambo mbalimbali ambayo hata hivyo hayakufafanuliwa, wakati akiwa katika wadhifa wa mtendaji mkuu.

Kwa mujibu wa uchunguzi wetu, lengo kuu la kusambaza nyaraka hizo ni kujaribu kumnyoshea kidole Mwakyembe na kujaribu kumuondolea uhalali wa kuendelea kupigania sekta ya nishati ilhali yeye mwenyewe akijua kuwa na maslahi.

Mwakyembe ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alisema kuwa katika Kampuni ya Power Pool East Africa Ltd, hakuwezi kukamsababishia akaingia katika mgogoro wowote wa kimaslahi kutokana na ukweli kwamba, kampuni hiyo iliyosajiliwa kwa Wakala wa Usajili wa Makampuni (BRELA), bado ipo katika hatua ya awali ya mradi ambao bado haujaanza kuzalisha.

Alipotakiwa kueleza ni kwa nini wakati alipoteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge iliyoichunguza Richmond kuanzia Oktoba mwaka juzi na kuwasilisha ripoti yake mwaka jana, hakueleza lolote kuhusu kuwa na kampuni ya kuzalisha umeme, Mwakyembe alisema asingeweza kufanya hivyo wakati mkakati wao wa kikampuni ukiwa katika hatua ya mradi tu.

‘‘Kwa mujibu wa sheria ya makampuni, majina yanakuwapo mpaka hapo kampuni itakapoanza ‘ku-take off’ (kuanza kazi). Sikuweza kuitaja kuwa ni sehemu ya makampuni yangu, kwa kuwa bado ilikuwa katika hatua ya mradi,” alisema Mwakyembe.

Mwanasiasa huyo alikwenda mbele zaidi na kuwaeleza wanahabari hao ambao miongoni mwao walionekana dhahiri kukabiliana naye kwa njia ya malumbano kuwa, hata wakati akiandikisha mali anazomiliki chini ya sheria ya viongozi kutangaza mali wanazomiliki, hakuitaja kampuni hiyo ya Power Pool kwa sababu hizo hizo za kutoanza kwake kazi.

Akifafanua tuhuma hizo dhidi yake, alimgeukia mbunge mwenzake wa CCM, Rostam Aziz na kumtuhumu kuwa nyuma ya habari zote mbaya zinazoandikwa dhidi yake.

Huku akilitaja jina la Rostam mara kadhaa, Mwakyembe alisema ni jambo ambalo haliingii akilini kwa mtu ambaye amechafuka kuamua kutumia maji taka kujisafisha.


WALA TUSINGEFIKA HAPA TULIPO IWAPO SHERIA INGEFUATA MKONDO WAKE.VINARA WALIOTUINGIZA MKENGE KWENYE UTAPELI WA RICHMOND HAWAJACHUKULIWA HATUA BAADA YA KUJIUZULU,NA SASA WAMEPATA JEURI YA KUTAKA KUTULIZA MARA YA PILI KWA KUTUUZIA MITAMBO MITUMBA ILEILE ILE YA RICHMOND a.k.a DOWANS.HUU MTINDO WA KULINDANA UTALIPELEKA TAIFA MAHALA PABAYA.

HOWEVER,LET IT BE KNOW TO MAFISADI AND THOSE WHO SHIELD THEM THAT IF THEY TURN OUR BELOVED COUNTRY INTO ANOTHER MADAGASCAR THEY TOO WOULDNT BE SAFE!

11 Dec 2008

Na Simon Mhina
Kada machachari wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, amesema kauli ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusuf Makamba, kwamba mjadala juu ya mafisadi wa Akauti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ufungwe, inaashiria kuwakumbatia mafisadi. 

Mwanasiasa huyo chipukizi ambaye yupo katika kipindi cha mapambano na makada wenzake ndani ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), kutokana na kuvuliwa uanachama kwa kupinga mradi wa Jengo Jipya la Umoja huo, alisema hatua ya Makamba kuweka mizengwe mapambano dhidi ya ufisadi inawavunja moyo watendaji wa serikali ambao wapo mstari wa mbele kushughulikia tatizo hilo. 

Nape ambaye bado ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), alisema kauli ya Makamba ni sawa na ya mtu anayeogopa kivuli chake. 

Hata hivyo, Nape katika mazungumzo na Nipashe jijini Dar es Salaam jana, alisema kimsingi Makamba hana uwezo wala madaraka ya kuzuia mjadala juu ya mafisadi. 

Nape alisema ingawa hana uhusiano wowote na watu wanaopiga makelele juu ya ufisadi, lakini anafikiri wanafanya hivyo kutokana na machungu makubwa ya umasikini wanayopata Watanzania kutokana na mafisadi. 
Alihoji: ``Hivi Mzee Makamba mafisadi wakisemwa vibaya yeye anakerwa na nini? 

Hivi kinachomkera ni kipi, mafisadi waliopora fedha za wavuja jasho au wavuja jasho wanaopiga makelele juu ya mafisadi kuwaibia?`` 

Alisisitiza kuwa katika hali ya kawaida, hakuna Mtanzania ambaye atanyamazia ufisadi kutokana na uzito wake. 

Nape alihoji tena: ``Ina maana Mzee Makamba anajua idadi ya mafisadi wote nchini?`` 

Akifafanua, alisema kazi ya kuwashughulikia wahalifu hao ipo chini ya serikali na vyombo vyake vya dola na sio jambo la kisiasa. 

Wakati huo huo, Mbunge wa Moshi Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Philimon Ndesamburo, amesema chama chake `kitafunga mdomo` kuhusu ufisadi, iwapo Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, atakamatwa na kufikishwa mahakamani. 

Alisema Mkapa ni hazina kubwa ya mafisadi nchini na siku akifikishwa kortini janga hilo litakuwa limefikia tamati. 

``Chadema hatutaacha kupiga kelele juu ya ufisadi kama anavyosema Makamba hadi hapo Mkapa ambaye ni hazina ya mafisadi atakapopelekwa kortini, mambo yote yaliyofanyika yalikuwa chini ya utawala wake na alikuwa anayajua na alishiriki, lazima akamatwe,``alisema Ndesamburo. 

Mbunge huyo alisema mafisadi ndani ya CCM na serikali yake, hawajamalizika hivyo lazima waendelee kusakwa. 
Alisema asilimia 10 tu ya mafisadi wote nchini ndio wamekamatwa, lakini asilimia 90 akiwemo `baba lao` bado wapo mitaani. 

Ndesamburo alisema japokuwa Makamba amelenga kuwasaidia baadhi ya mafisadi, lakini kwa hili anatakiwa aone aibu. 

``Yaani wakati huu ambao Rais Jakaya Kikwete ameridhia watu waliokuwa mawaziri wafikishwe Mahakamani yeye anasimama kutetea ufisadi, namuomba angalau aone aibu, hata kama amelambishwa asali,`` alisema. 

Kuhusu Operesheni Sangara, Ndesamburo alisema itaendelea kwa nguvu zote licha ya Makamba kuibeza, kwa vile inalenga kuwafumbua macho Watanzania. 

Alisema operesheni hiyo si uchochezi wala nguvu ya soda, bali Makamba ametoa shutuma hizo, baada ya kushindwa kujibu hoja zinazotolewa na Chadema. 

Makamba alinukuliwa katika vyombo vya habari jana akisema kwamba mjadala wa EPA kwa sasa umefungwa kwa kuwa watuhumiwa wote wamefikishwa kortini. 

Hata hivyo, ukweli ni kwamba bado watuhumiwa wengine wakiwamo wamiliki wa Kagoda Agriculture Ltd hawajafikishwa kortini. 

CHANZO: Nipashe

17 Sept 2008

Chama cha siasa huzaliwa,hukua na kinaweza kufa pengine hata kabla hakijakua.Tofauti nachama nchi ikishazaliwa ni lazima iishi milele,tena kwa gharama yoyote ile.Lakini kuna wenzetu wengine hawataki kuelewa ukweli huo.Kwao,chama cha siasa ni kila kitu hata kama kinaipeleka nchi ahera.Angalia mfano huu mwepesi: chama kinapewa dhamana ya kuongoza nchi,lakini kinaendesha mambo yake kihuni na kupeleka nchi mrama.Ni dhahiri kwamba chama cha aina hiyo kinaamsha vurugu ambazo zitalekea mmomonyoko wa amani katika nchi husika.Kwa bahati mbaya au makusudi,kuna wenzetu hawataki kuamini kwamba ni vigumu kujenga na kudumisha amani kuliko kuivunja.Sote tunawajibika kuhakikisha nchi yetu haipelekwi kusikofaa badala ya kunyoosheana vidole tunapotofautiana namna ya kuboresha ustawi wa Tanzania yetu.

Katika toleo la wiki hii la gazeti mahiri la Raia Mwema,pamoja na mkusanyiko wa habari na makala motomoto,kuna hababari kuhusu the man of the moment,Nape Nnauye.Kuna wanaodai kuwa huyu jamaa aanashupalia ishu za ufisadi ndani ya UVCCM kwa minajili ya kutafuta umaarufu utakaopelekea apate nafasi ya juu kwenye jumuiya hiyo.Sina uhakika kuhusu hilo lakini binafsi naamini kwamba hata kama malengo yake ya ni kupata umaarufu au uongozi,jitihada zake kuushikia bango ufisadi ndilo lililo muhimu zaidi kuliko motives zake.Na wanaokemea ufisadi,hata kama kwa njia zisizo sahihi,wanapaswa kuungwa mkono badala ya kunyanyaswa.Enewei,habari ya Nape ni hii HAPA na mambo mengine motomoto yanapatikana ndani ya gazeti hili la RAIA MWEMA.


Categories

Blog Archive

© Evarist Chahali 2006-2022

Search Engine Optimization SEO

Powered by Blogger.